13 Nov 2006

KULIKONI UGHAIBUNI-32


Asalam aleykum,

Kwanza napenda kutoa pole kwa familia za marehemu Walter Mazula na mchumba wake Vonatha Nkya.Kwa namna mazingira ya huku ughaibuni yalivyo,Mtanzania mwenzako popote alipo ni kama sehemu ya familia.Mauaji hayo ya kikatili yamewagusa watu wengi hata kwa sie ambao hatukubahatika kukutana nao wakati wa uhai wao.Kwa mujibu wa wenzetu walio Marekani,kulikuwa na ushirkiano mkubwa na familia ya wafiwa kwa kuwafariji na kuwapatia msaada wa hali na mali,na kwa mara nyingine imeonyesha ni jinsi gani Watanzania tuna moyo wa ushirkiano popte tulipo.Wakati tunaviacha vyombo vya sheria huko Marekani vikiendelea na uchunguzi kuhusu mauaji hayo,tunachoweza kusema kwa sasa ni kuwatakia marehemu pumziko la milele na kuwaombea wafiwa moyo wa uvumilifu na faraja.

Wakati tunazungumzia maisha ya Watanzania hao wawili ambao wamenyang’anywa uhai wao bila chembe ya huruma,pengine ni wakati muafaka pia kuangalia maisha ya Watanzania wengine ambayo yanapotea takribani kila siku huko nyumbani kutokana na ajali za barabarani.Kwa kweli inatia uchungu kusoma habari za ajali kila kukicha huku kukiwa hakuna daliliz zozote kwamba angalau ajali hizo zitapungua.Kuna msemo wa Kiswahili kwamba ajali haina kinga,lakini nyingi ya hizo zinazotokea huko nyumbani zinaweza kuepukika au kupunguzwa iwapo wenye dhamana ya kusimamia usalama barabarani wataongeza jitihada.

Kila mwaka kuna wiki ya “Nenda kwa Usalama Barabarani”.Kama sijakosea,kipindi hiki ndicho ukaguzi wa magari unafanyika japokuwa jukumu la kukagua magari ni la mwaka mzima.Sina tatizo na zoezi hilo kufanyika mara moja kwa mwaka.Ugomvi wangu kwenye zoezi hilo ni jinsi linavyoshindwa kupunguza ajali za barabarani.Lakini ugomvi wangu mkubwa uko kwa wamiliki wa vyombo vya usafiri ambao wameweka mbele tama ya fedha kuliko uhai wa hao wanaowawezesha kupata fedha hizo kwa njia ya nauli (abiria).Laiti wamiliki hao wangekuwa na ubinadamu wa kutambua kuwa magari yao hayako katika hali nzuri ya kubeba abiria,nadhani hata trafiki wasingekuwa na haja ya kuyakamata magari ya aina hiyo.

Wengine wasioweza kukwepa lawama zangu ni madereva wazembe.Hawa wangeweza kukwepa lawama pale tu wanapokabidhiwa magari ambayo wanafahamu fika kuwa ni “vimeo”.Tunafahamu kuwa wanalinda ajira zao kwa vile ni lazima wamepeleka mkono kinywani lakini hata hivyo ridhiki zao zisiwe sababu ya kuleta vilio kwa wenzao.Kwa utaratibu uliozoeleka,wamiliki wa magari kama daladala huwa wanapatia dhamana madereva wa magari hayo kuhakikisha yanafanya kazi kwa namna inavyopaswa.Kwa mantiki hiyo,inaweza kuwa vigumu kwa mmiliki kumsimamia dereva ahakikishe anasima kwenye traffic lights,hafanyi “ovateki” za kizembe,au anazingatia mwendo unaotakiwa katika barabara husika.Majukumu hayo ni yadereva mwenyewe.Kwa bahati mbaya,uhuru huo wanaopatiwa madereva huishia kutumiwa vibaya,na hawa jamaa wakishakuwa kwenye usukani wanajiona kama wanaendesha magari hayo wakiwa peponi.Na napozungumzia madereva wazembe najumuisha madereva wote,wale wa magari ya abiria na yale yasiyo ya abiria.

Labda hapa nitoe mfano mmoja wa sheria za usalama barabarani za hapa Uingereza.Ni “dhambi” isiyosameheka kwa dereva yoyote yule kukutwa anaendesha akiwa amepata kinywaji.Siku za wikiendi utakuta watu wanaacha magari yao nyumbani pindi wanapoamua kwenda kupata kinywaji.Usafiri unaotegemewa wakati wa kurejea majumbani kwa nyakati hizo za usiku ni taksi na mabasi ya usiku pekee.Haina maana hakuna wakorofi wachache wanaojaribu kuwapima nguvu polisi kwa kuendesha huku wamelewa,lakini kwa ujumla madereva wengi wanazingatia sana sheria hiyo.Kingine ni kudhibiti mwendo wa magari.Hilo linasaidiwa sana na teknolojia ambapo kuna kamera za barabarani zinazorekodi magari yanayoendeshwa zaidi ya spidi inayoruhusiwa kwenye barabara husika.

Kundi la tatu ambalo nadhani haliwezi kukwepa lawama kuhusiana na hiz ajali za kila siku ni wenzetu tuliowakabidhi dhamana ya kuhakikisha usalama barabarani.Hapa nawazungumzia polisi wa kitengo cha trafiki.Hawa jamaa wamekuwa wakisifika (au kulaumiwa?) zaidi kwa “kudai kitu kidogo” badala ya kawadhibiti madereva watukutu.Simaanishi kwamba askari trafiki wote ni wala rushwa lakini hatuhitaji digrii ya upelelezi kufahamu kuwa trafiki wengi wanaendekeza zaidi rushwa badala ya kuzingatia majukumu waliyokabidhiwa.Hatuwashuku kuwa ni wala rushwa kwa vile wengi wao wana miili iliyoneemeka licha ya vilio vya askari wetu kuwa mishahara ni kiduchu,bali ni ushahidi ambao sidhani kama kuna dereva au abiria hajawahi kuuona mchana mweupe ambapo trafiki anamshusha dereva au konda wake na kuelekea “mafichoni” kupatiwa mlungula.Hivi huyu mla rushwa anaweza kweli kulizuia gari bovu lisitembee barabarani?Kwa hakika hawezi,kwa sababu akilizuwia ina maana atakosa “maslahi” yake.Nadhani baadhi yao wanasiktika pindi wanapolisimamisha gari na kugundua kuwa halina tatizo na dereva wake hajavunja sheria yoyote.

Serikali yetu nayo haiwezi kukwepa lawama kuhusu kuzidi kwa ajali za barabarani.Kumekuwa na ahadi nyingi zaidi ya vitendo.Baadhi yetu tumeshasahau kuhusu “spidi gavana” na hatujui huyo “tapeli aliyetuingiza mkenge” (tu aliyekuja na wazo hilo) amechukuliwa hatua gani baada ya kubainika kuwa mradi huo ulikuwa feki na haujaleta manufaa yoyote kwa wananchi.Nasema hivi,nyingi ya ajali za huko nyumbani zinaweza kuepukika iwapo serikali itasimamia na kuhakikisha sheria iliyoziweka zinafuatwa bila utani.Na si ajali za barabarani tu lakini hata kwenye vyombo vya majini (hivi lile suala la Mv Nyamangeni limeishia wapi?).Vivuko vyetu vingi ni sawa na majeneza yanayoelea,na kwa vile sie ni watu tuliozowea kuchukua hatua pale tu tatizo linapotokea,maelfu ya Watanzania wanaendelea kutumia pantoni na feri ambazo kwa kiasi kikubwa usalama wake ni wa hatihati.

Mwisho,ifahamike kuwa tatizo la ajali za barabarani halizoeleki.Kuwa na ajali za kila siku haimaananishi kuwa wananchi wanazizowea.Hawana la kufanya ila kusafiri roho mkononi huku wakiomba dua madereva watumie akili zaidi,trafiki watekeleze majukumu yao vizuri na hatimaye wafike salama huko waendako.Tusisubiri hadi gari la kiongozi lipate ajali kwa kugongwa na dereva mzembe na kufumbiwa macho na trafiki aliyepewa rushwa ndio tufumbuke macho kwamba kumbe kweli ajali ni tishio kwa maisha yetu.Sheria zipo na kwa hakika zinatekelezeka,kinachohitajika ni usimamizi na ufuatiliaji tu.

Ramadhan Karim (heri ya mfungo wa Ramadhan…kwa waliouona mwezi)

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.