16 Nov 2006

KULIKONI UGHAIBUNI-37

Asalam aleykum,

Miongoni mwa mambo ambayo taasisi nyingi za huku ughaibuni zinajitahidi sana kuwa nayo ni hadhi na imani za wananchi kwa taasisi hizo.Na sehemu nzuri ya kuangalia hilo nalozungumzia ni kwenye taasisi za fedha.Kwa hapa Uingereza na nchi nyingine za Magharibi,wateja wa taasisi flani huwa ni kama wameweka “mikataba” na taasisi hizo. Usishangae ukisikia kuwa katika familia flani,tangu enzi za mababu wao wamekuwa wateja wa benki flani,kwa mfano.Na kinachowafanya waing’ang’anie benki hiyo ni jinsi inavyowathamini wao kama wateja na pengine hadhi ambayo benki hiyo imejijengea kwa jamii.Na ili kujenga hadhi hiyo na kuilinda taasisi husika inapaswa kufanya bidii kweli kwa vile kwa kiasi kikubwa hapa watu hawataki usumbufu usio wa lazima.Pia ushindani uliopo kati ya taasisi za kibiashara ni mkali sana,uzembe kidogo tu basi wateja “wanaingia mitini.”

Kwa huko nyumbani hali ni tofauti kwa kiasi kikubwa.Utasikia taasisi flani inatangaza kwamba mteja kwao ni mfalme lakini unaweza kujuta ukitia mguu kwenye majengo ya taasisi hiyo.Na si ajabu ukaishia kudhani kuwa tangazo uliloliona au kulisikia kuhusu taasisi hiyo ikidai kuwa mteja kwao ni mfalme (na pengine malkia) halikuwa tangazo lao.Kuna watumishi wanakuwa wamejisahau kabisa kwamba wanaweza kukosa mishahara pindi hao wateja wanaowadharau wakiwasusa.Pengine wanachoringia ni ukweli kwamba bado kuna ushindani dhaifu kwenye sekta mbalimbali huko nyumbani.Na siku wenye kujua namna ya kuendesha ushindani watakapoamua “kufanya kweli” basi haitoshangaza pale walio wababaishaji wakajiengua wenyewe.Mwaka juzi wakati narinyuu (hivi neno la Kiswahili ni nini hapo…) mkataba wa kiselula changu nilishangaa nilipokabidhiwa DVD Player na DVDs tatu (vyote vya bure) pamoja na simu mpya ya chaguo langu.Japokuwa kampuni iliyotoa zawadi hizo ilikuwa na uhakika wa kurejesha faida yake kadri ntakavyokuwa kwenye mkataba nao,sio siri kwamba nafsi yangu “ilisuuzika” sana.Wanafanya hivyo kwa vile wanafahamu kuwa kuna ushindani sana kwenye biashara ya viselula,na pindi ukimpoteza mteja basi ni vigumu sana kumrejesha.

Moja ya taasisi za huko nyumbani ambazo kwa hakika inaweza kuwa kielelezo kizuri cha mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji wa taasisi za umma ni benki ya CRDB.Zamani ilikuwa inaitwa Benki ya Maendeleo Vijijini lakini baadae ikajitengeneza vema,ikakaribisha watu kununua hisa na sasa benki hiyo inafanya kile ambacho Watanzania wengi wangependa kukiona kwenye taasisi nyingine zilizotolewa kutoka kwenye milki ya serikali pekee.Na miongoni mwa mafanikio makubwa ya huduma za benki hiyo ni ile ya akaunti iitwayo “Tanzanite.”Akaunti hiyo imewalenga zaidi Watanzania walio nje ya nchi ambao wangependa kujiwekea fedha zao kwenye benki ya huko nyumbani.Naomba kukiri kuwa mwanzoni nilihisi kuwa huduma hiyo isingekuwa na mafanikio sana,hasa kwa vile huduma zinazovuka mipaka ya nchi zinahitaji uangalifu na umakini mkubwa.Lakini CRDB wamefanikiwa kwa kiwango kikubwa kuishi kulingana na matarajio ya wateja wao.

Binafsi nimekuwa nikiitumia huduma hii kwa takribani mwaka mzima sasa.Lakini mabadiliko yaliyofanya hivi karibuni yamezidi kunifanya nijiskie “mteja ni mfalme” kwa benki hiyo.Na hapa nadhani nimtaje Meneja mpya wa Uhusiano wa huduma ya Tanzanite aitwaye Jenipher Tondi.Kwa hakika anajituma sana kwa namna ambavyo anashughulikia masuala yanayohusu wateja wa Tanzanite Accounts.Unajua mawasiliano kati ya huduma ya Tanzanite na mteja aliye nje ya nchi yanategemea zaidi barua pepe.Na kama ilivyo kwenye huduma ambazo mawasiliano yanategemea simu,kauli na lugha za mtoa huduma kwa mteja ni kitu chenye umuhimu mkubwa sana.Ukisoma barua pepe kutoka kwa Meneja Tondi kuja kwa mteja unagundua kwa hakika kuwa yeye na benki yake wanakuthamini wewe mteja kwa hali ya juu kabisa.Na pia kasi ya kushughulikia matatizo ya wateja ni kubwa na haikuachi mteja unaomba dua lini utajibiwa au kutatuliwa matatizo yako.Majuzi kadi yangu mpya ya TemboVisa ilinasa kwenye ATM wakati nataka kuangalia balansi ya akaunti yangu.Nikaandika barua pepe kwa CRDB na baada ya muda mfupi tu nikapata majibu kutoka kwa Meneja huyo wa Tanzanite,majibu ambayo licha ya kunipatia ufumbuzi yaliniacha nikiwa nimeridhishwa na jinsi suala langu lilivyoshughulikiwa.Msomaji mpendwa usije ukadhani “nimepewa kidogodogo” (bakshish) kuipigia debe CRDB au Meneja Jenipher,bali ukweli ni kwamba kwa jinsi tunavyoona huduma zinavyotolewa na taasisi nyingi za huku ughaibuni (ukilinganisha na nyingi za huko nyumbani) nitakuwa mchoyo wa shukrani kama sintatoa pongezi kwa benki hiyo.Pongezi hizo zinapaswa kuwa changamoto kwa taasisi nyingine,za umma na za binafsi,kwamba porojo za mteja ni mfalme au malkia hazina maana iwapo mteja huyo anapofika mahala husika ili apatiwe huduma anabaini kuwa badala ya ufalme/umalkia alioahidiwa anaishia kuwa mtumwa (na inauma zaidi unapokuwa mtumwa sehemu ulohifadhi fedha yako mwenyewe).

Kwa mtazamo wangu,wasiwasi wa walio wengi kuhusu ubinafsishaji wa taasisi za umma unatokana zaidi na utendaji wa taasisi hizo baada ya kubinafsishwa na sio kwa vile tu zimebinafsishwa.Hakuna mtu anayejali kama kampuni inaendeshwa na Mpakistani au Mchina badala ya Mtanzania alimradi huduma inayotolewa ni bora kuliko ile ya awali.TBL imekuwa ikitolewa mfano mara kadhaa kuwa ni “success story” ya zoezi la ubinafsishaji.Hilo halina mjadala hata kama TBL iko chini ya Wasauzi Afrika.CRDB iko chini ya uongozi wa Mtanzania,Dr Kimei,na naamini mafaniko yake yamechangiwa na taasisi hiyo kutambua wajibu wake kwa wateja na Taifa kwa ujumla.Tunaweza kabisa kuwa na akina Dr Kimei au Jenipher Tondi wengine kwenye taasisi zetu nyingine iwapo taasisi hizo zitapotekeleza kwa dhati kauli mbiu zao za mteja ni mfalme/malkia.Kwa nyie mnaosuasua kutoa huduma kwa umma mtambue kuwa kuna siku mtajutia nafasi mlizonazo sasa ambapo bado wateja wenu wanaendelea kuwaamini licha ya usumbufu mnaowapatia.Siku watakapowakimbia hamtawaona tena kwenye majengo yenu.Kaulimbiu ya Kikwete na serikali yake ya Awamu ya Nne kuhusu “Maisha Bora kwa kila Mtanzania yanawezekana” inawahusu nanyi pia hasa kwa vile wateja wenu ndio wanawezesha maisha ya taasisi zenu kuwa bora.Kwa mantiki hiyo ni lazima nanyi myafanye yao kuwa bora kwa kuwahudumia kwa nguvu zenu zote.

Alamsiki

Kwa makala zilizopita,tembelea http://chahali.blogspot.com na http://chahali.livejournal.com

1 comment:

  1. Nimepita hapa na kule kwingine asubuhi hii. Poa, noa kalamu!

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.