14 Mar 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-54

Asalam aleykum,

Katika makala zangu nyingi nimekuwa nikijitahidi kuwakumbusha Watanzania wenzangu juu ya umuhimu wa kufanya kila liwezekano kuitunza hali ya utulivu na amani tuliyobarikiwa kuwa nayo kwa miongo kadhaa sasa.Na kwa hakika ni jukumu la kila mmoja wetu kuhakikisha kuwa hatutoi fursa kwa mtu yeyote kuichezea lulu hii adimu hasa tukizingatia kuwa takriban majirani wetu wote wanaotuzunguka wako kwenye songombingo moja au nyingine.Hakika,jiografia ya hali ya usalama barani Afrika,hususan eneo la Maziwa Makuu inasapoti kabisa “nickname” yetu ya KISIWA CHA AMANI.Lakini inaelekea kuna wenzetu ambao kwa namna moja au nyingine inaelekea wameshachoshwa na hii amani ya kila siku.Wanataka kufanya majaribio kuona nchi inakuwaje pindi amani ikitoweka.Ni vizuri tukakumbushana kwamba wakati inaweza kuchukua karne kadhaa kujenga amani,amana hiyo adimu inaweza kupotezwa na wazembe wachache kwa siku kadhaa tu.Na kamwe tusiruhusu hilo litokee kwa gharama yoyote ile.

Majuzi,aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora Braza Ditto alipewa dhamana na mahakama katika kesi inayomkabili ya kuua bila kukusudia.Kwamba dhamana ni haki ya kila mshtakiwa,hilo halina mjadala.Kama alivyosema Waziri wa Usalama wa Raia Bakari Mwapachu kwamba ukiwa na mawakili wazuri basi kuna uwezekano wa mshtakiwa kupatiwa dhamana mapema kama ilivyotokea katika kesi ya Braza Ditto.Labda la kujiuliza ni kwamba ni wangapi kati yetu wenye uwezo wa kuajiri mawakili waliobobea ambao kimsingi gharama za huduma zao ziko juu sana.Na kama suala ni la mawakili wazuri au waliobobea,je itakuwaje kwenye kesi za mahakama za mwanzo?Nadhani suala la msingi hapa sio mawakili bali ni kwa mahakama kutoa haki ya dhamana au kusikiliza kesi mapema bila kujali uwezo wa mshtakiwa.

Kesi ya Braza Ditto imekuwa na mvuto wa kipekee.Binafsi,nilishtuka sana niliposikia yaliyomsibu Mkuu huyo wa zamani wa Mkoa wa Tabora.Yayumkinika kusema kuwa wengi tulimuonea huruma mwanasiasa huyo hasa kwa vile ni mtu mcheshi, “mtoto wa mjini” na hutochoka kusikia stori zake.Nadhani wale wanaolalamika kwa hisia kuwa kesi yake imeharakishwa sana hawafanyi hivyo kwa vile hawampendi Ditto bali wangependa kuona kesi zote zinaharakishwa.Binafsi namfananisha Ditto na Makamba.Yaani ni mwanasiasa ambaye ana mvuto wa aina flani.Ditto ni miongoni mwa wanasiasa ambao ungependa kuwasikia muda wote na anajua kuichangamsha hadhira yake.Nitamke bayana kuwa niliposikia yaliyomkuta,hisia yangu ya kwanza ilikuwa kuamini kwamba kila binadamu ana “siku yake mbaya.”Bila kutaka kuingilia uhuru wa mahakama kuhusu kesi yake,nashawishika kuamini kuwa mauaji hayo hayakuwa ya kukusudia kama yalivyobadilishwa na wanasheria wa serikali.Na ukiangalia kwa makini sana matendo ya Ditto tangu akutwe na janga hilo unaweza kukubaliana nami kuwa hajafanya jitihada yoyote ya kutaka kutumia umaarufu wake kisiasa kupindisha mkondo wa sheria.Huwezi kumlaumu yeye kwa kubadilishiwa mashtaka wala kuharakishwa kwa dhamana yake.Ukweli kwamba yeye mwenyewe ndiye aliyewapigia simu polisi kuwajulisha kuhusu mauaji unaeleza jinsi gani alivyokuwa na busara katika kulishughulikia sakata hilo.

Ilianza na kubadilishwa mashtaka yanayomkabili ambapo japo sikuwahi kusikia malalamiko yoyote,mtu mmoja alikurupuka kudai kuwa mashtaka hayo hayakubadilishwa kwa vile Ditto ni mtu maarufu.Ukiona mtu anakimbilia kujitetea kabla hajalaumiwa basi ujue aidha anaogopa balaa flani au kitu flani hakiko sawia kama kinavyoonekana.

Mimi sio mtaalamu wa sheria za mahakama au jela kwa hiyo sijui kama ilikuwa sawa au la wakati tulipokuwa tunasoma kwenye magazeti kuwa mtuhumiwa huyo analetwa mahakamani kwenye gari tofauti na watuhumiwa wengine.Pengine ni suala la mtuhumiwa kuwa na uwezo wa kupata usafiri wake binafsi kumleta mahakamani.Lakini hilo si la msingi sana kwa vile cha muhimu sio usafiri anaojia mtuhumiwa mahakamani bali ukweli kwamba amehudhuria mahakamani hapo.Katika nchi za wenzetu,sio lazima kwa kila mtuhumiwa kuwa rumande wakati anasubiri kuanza kwa kesi yake au hukumu.Wapo watuhumiwa wanaotokea nyumbani kwenda mahakamani japo wana kesi kubwa zinazowakabili.Ila inapaswa kukumbukwa kuwa hawa wenzetu wana teknolojia na utaalam wa kutosha wa kuhakikisha kuwa mtuhumiwa hapotei kiajabuajabu.

Kwa polisi kumpitisha mtuhumiwa kwenye lango linalotumiwa na majaji inaonyesha ni jinsi gani watu tunaowategemea kulinda sheria wanavyoweza kuwa mufilisi wa mawazo pengine sio kwa vile wameelekezwa kufanya bali uoga wao tu.Hakuna uthibitisho wowote kuwa polisi waliofanya madudu hayo walipewa maelekezo ya kufanya hivyo.Kwa mantiki hiyo,ni aidha walikuwa wanajipendekeza au ipo namna flani ambayo mie na wewe hatuwezi kuielewa hivi hivi.Lakini kwa polisi kuwaruhusu wahuni flani kuwafanyia vurugu wanahabari ilhali wao (polisi) wakizubaa tu ni suala ambalo linapaswa kuangaliwa kwa mapana zaidi kwani ni sawa na kupandikiza virusi vyenye sumu kwenye suala zima la usalama na amani kwa raia.Nasema “kuruhusu” kwa vile polisi hawakuchukua hatua yoyote kuzuia uhuni huo.Lakini ukisikia bosi wao anajitetea kuwa eti ilikuwa vigumu kwa polisi kutofautisha ndugu wa Ditto na waandishi wa habari unabaki mdomo wazi.Ina maana hata hao waliokuwa na kamera ya kurekodia picha za televisheni nao walioonekana kuwa ni ndugu za Ditto?Huo ni utetezi dhaifu ambao haukupaswa kutolewa na kwa namna flani umeharibu hata ile samahani iliyotolewa kwa wanahabari waliokumbwa na zahma hiyo.

Lakini pengine watu ambao wanapaswa sio tu kulaumiwa bali pia kuchukuliwa hatua kali ni hao ndugu wa Ditto waliofanya vurugu mahakamani.Wanapaswa kufahamu kuwa baadhi ya maneno waliyokuwa wanasema sio tu yanaweza kuathiri mwenendo mzima wa kesi hiyo bali pia yanachafua majina ya baadhi ya watu ambao hata kama ni marafiki wa Braza Ditto hawakuhusika na uamuzi wa dhamana kwa mshtakiwa huyo.Kujigamba kuwa “wao ndio wenye nchi…” sio kauli nzuri na natumaini hivi karibuni mwenye busara mmoja miongoni mwao atajitahidi kuomba radhi na kurekebisha kauli za kihuni kama hizo.Wakumbuke kuwa moja wa wahusika wakuu wa kesi hiyo ni marehemu,na kifo chake (licha ya kuwa bila ya kukusudia kama tunavyoelezwa) kilisababishwa na mhusika mwingine ambaye yuko hai na huru.Hivi wanadhani wafiwa wanalijisikiaje wakati wao (ndugu za Ditto hapo mahakamani) walipokuwa wanatoa kejeli zao?

Naamini kabisa kuwa Braza Ditto mwenyewe anataka haki itendeke lakini matakwa hayo yanaweza kuathiriwa na jinsi hao wahuni wanaojiita ndugu zake wanavyoendesha mambo yao bila kutumia akili.Ifahamike kuwa kupatikana kwa haki hakumaanishi lazima mtuhumiwa apatikane na makosa,au akipatikana na makosa lazima aende jela.Kanuni muhimu ya kisheria ni sio tu kutendeka kwa haki bali haki ionekane imetendeka.Na ili hilo liwezekane pasipo kinyongo au malalamiko ni lazima pande zote zinazohusika na kesi hiyo ziheshimu utawala wa sheria.Wahuni waliosababisha vurugu mahakamani hapo ndio chanzo halisi cha hii migomo baridi iliyoanzishwa wa mahabusu wanaopinga kesi zao kuendeshwa kwa mwendo wa kinyonga huku ile ya mwenzio imepelekwa kwa kasi ya radi.Wahuni hao wamesababisha kuleta hisia kwamba kwa “wenye nchi” kila kitu kinakwenda “fasta” japo kimsingi uamuzi wa dhamana kwa Ditto umefuata misingi ya sheria kwa vile ni haki yake kwa mujibu wa kesi inayomkabili.Hilo la “kasi ya radi” linaweza kuwa ni matokeo ya kuwa na wanasheria wanaojua wanachokifanya mahakamani.Naungana na kauli ya Jaji Mkuu aliyoitoa huko Tabora kuhusu umuhimu wa kuheshimu sheria (na taasisi za kisheria) na kutowafumbia macho wale wanaotaka kuichezea.Ikumbukwe kuwa pasipo sheria ni vurugu na penye vurugu hao wanaodhani ni “wenye nchi” wanaweza kujikuta hawana pa kufanyia nyodo zao kama walivyofanya pale mahakamani.

Alamsiki


1 comment:

  1. Bonge! huwa napita hapa kimyakimya kama vile unapokuwa ATB-kijiweni kwa chini huku lecture ikiendelea

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.