21 Mar 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-55

Asalam aleykum,

Kwanza nianze na pongezi zangu kwa Chama Tawala (CCM) kwa kuibuka kidedea huko Tunduru.Kama ilvyotarajiwa,vyama vya upinzani vilivyoshiriki katika uchaguzi huo mdogo vimekimbilia kulalamikia “mchezo mchafu.”Pengine wanachopaswa kukumbuka ni kukubaliana na wajuzi wa siasa ambao wanaitafsiri siasa kuwa “mchezo mchafu.”Lakini pia wanapaswa kuelewa kuwa wanapouelezea ushindi wa CCM kuwa umetokana na mchezo mchafu wanatakiwa wakumbuke kuwa kimsingi ushindi katika uchaguzi wowote ule hautokani na matakwa ya chama pekee bali maandalizi ya kutosha,ya kisayansi na mbinu ambazo zinakiwezesha chama kutabiri matokeo hata kabla hayajatangazwa.Wote tunafahamu kuwa CCM huwa makini sana linapokuja suala la uchaguzi.Chama hicho hukusanya nguvu zake zote kuhakikisha kuwa ushindi unapatikana.Bila kukusudia kuvivunja nguvu vyama vya upinzani,yayumkinika kusema kwamba CCM itaendelea kushika hatamu kwa miaka mingi sana ijayo.Na kikubwa kitachochangia hilo ni maandalizi mazuri,umoja na mshikamano bila kusahau kuitumia vizuri nafasi ya upinzani dhaifu nchini.Sina budi kusema “CCM Oyee!!!” kama pongezi zangu japo mie sio mwanachama wa chama hicho.

Tukuiachana na habari hizo za uchaguzi,leo nataka kuangalia hali ilivyo nchini Zimbabwe.Mpaka kesho wengi wetu tunakubuka jinsi uhuru wa nchi hiyo ulivyolisismua bara za Afrika na pengine dunia kwa ujumla.Wapenzi wa muziki watakumbuka kuwa sherehe za uhuru wa nchi hiyo zililiwezesha bara letu kupata ugeni mahsusi wa mfalme wa muziki wa reggae hayati Bob Marley.Na licha ya ziara hiyo,Bob na kundi lake la The Wailers waliamua kutunga kibao mahsusi cha “Zimbabwe” ambacho hadi keshokutwa bado kinapendeza ukikisikiliza.Kwa hakika,uhuru wa nchi hiyo ulifungua sura mpya sio tu kwa Wazimbabwe bali kwa wapenda uhuru na amani sehemu nyingi duniani.

Leo hii mambo yako tofauti kabisa katika nchi hiyo.Kwa mtizamo wangu na ujuzi wangu mdogo kama mchambuzi wa siasa (political analyst) nashawishika kumtupia lawama nyingi kiongozi wa nchi hiyo Robert Mugabe.Tatizo kubwa la Mugabe ni uchu wake wa madaraka.Yaani anaiendesha nchi hiyo kama kampuni yake binafsi,anapindisha sheria anavyotaka kuhakikisha kuwa anaendelea kukalia madaraka na anaendelea kuwapa mateso wananchi wake kwa kung’ang’ania sera mufilisi ambazo zimeiacha nchi hiyo masikini wa kutupwa huku maelfu kwa maelfu ya Wazimbabwe wakikimbilia nchi za nje kutafuta hifadhi.

Mwanzoni nilikuwa naafikiana na sera zake za kupora ardhi wazungu na kuwagawia wazawa.Sera ilikuwa nzuri,ila inaelekea ilikuwa ni ya kukurupuka zaidi pasipo kufikiria matokeao yake.Inapaswa kufahamu kuwa nchi nyingi zilizopitia ukoloni haziwezi kufuta moja kwa moja baadhi ya matokeo ya ukoloni.Nachomaanisha hapo ni kwamba hatuwezi kubomoa mashule,barabara,nk kwa vile tu vilitengenzwa na mkoloni.Bahati mbaya baadhi ya wenzetu walijikuta wanapata uhuru huku kukiwa na idadi kubwa kidogo ya wakoloni walioamua kubaki kwenye makoloni hayo huru.Wengi tunafahamu kuwa Kenya iliendelea kubakiwa na idadi kubwa ya wakulima wa kizungu baada ya kupata uhuru kama ambavyo wengi wa makaburu walivyoamua kubakia Afrika Kusini baada ya kung’olewa kwa siasa za kibaguzi.Pamoja na ukweli kwamba bado kuna matatizo ya hapa na pale lakini nchi hizo nilizozitaja na nyinginezo zimefanikiwa kwa kiasi kikubwa kuwajumuisha wakoloni hao katika mifumo yao ya kiuchumi na kisiasa.

Hivi hadi leo Wazimbabwe wamenufaika vipi na mbinde ya Mugabe ya kuwanyang’anya ardhi wazungu?Wapo ambao maisha yao yalikuwa yanategemea mashamba hayo ya wazungu,na kuwatimua hapo pasipo kuwatafutia ajira mbadala ni sawa na ulevi.Yayumkinika kusema kuwa wazungu hao walikuwa na mchango flani katika uchumi wa Zimbabwe.Sasa kilichopaswa kufanyika kabla ya kuwapora ardhi ni kuangalia namna ya kuziba pengo ambalo kwa vyovyote lingejitokeza baada ya kunyofoa kigezo kimoja kinachochangia uchumi wa nchi.

Lakini kinachokera zaidi ni namna Mugabe anavyowapelekesha wapinzani wake.Awali nilikuwa naamini kuwa wapinzani kama Tsavingirai ni vibaraka wa nchi za Magharibi,lakini mtizamo huo ulibadilika baada ya kusikia mawazo ya baadhi ya Wazimbabwe kadhaa niliobahatika kukutana nao hapa.Mugabe anatumia kila nafasi aliyonayo kuhakikisha kuwa anabaki madarakani utadhani yeye ni rais wa maisha.Hilo la kubaki madarakani linaweza kuwa poa iwapo hataendeleza kampeni yake ya mkono wa chuma kuwapondaponda wale wote wanaonekana kuwa na mawazo tofauti na dikteta huyo.

Linalosikitisha zaidi ni namna gani Umoja wa nchi za Afrika (AU) ulivyoshindwa kabisa kuisaidia nchi hiyo isielekee pabaya zaidi.Jitihada zilizofanywa na Rais Kikwete hivi majuzi ni za binafsi na licha ya kupaswa kupongezwa zinapaswa pia kuifanya AU ijisikie aibu kwa namna ambavyo imekuwa kama dude flani ambalo halina uwezo wowote wa kutatua migogoro katika bara letu la Afrika.Wakati naandakaa makala haya nimesmsikia Tony Blair akiongea bungeni kwamba nchi za Afrika zinapaswa kufahamu kwamba matatizo ya mmoja wao yanawaathiri wote kwa namna moja au nyingine.Na hilo ni kweli kwa vile hadi leo sie tunabeba mzigo mkubwa wa wakimbizi kisa ni mamtatizo ndani ya nchi wanazotoka.Kwa AU kuendelea kutoa matamko yasiyo na nguvu huku Somalia inaendelea kuteketea,Darfur inazidi kuwa uwanja wa mauaji,ubakaji na ukiukwaji wa haki za binadamu,na Mugabe anaendelea kuwatumia mkono wa chuma kuipeleka nchi yake kusikoeleweka,ni sawa kabisa na kumpigia mbuzi gitaa:hatacheza.Ndio maana huwa napatwa na usingizi naposikia baadhi ya wanafalsafa wa Kiafrika wanapodai kuwe na taifa moja litakalounganisha nchi zote za Afrika (the united states of Africa).

Ni jukumu la AU kuhakikisha kuwa mambo yanarekebika nchini Zimbabwe.Damu ya wasio Wazimbabwe iliyotumika sambamba na ile ya Wazimbabwe katika harakati za uhuru wa nchi hiyo zisiachwe kupotea bure kwa vile tu mtu mmoja anataka kuwa madarakani milele.Kwa Mugabe,ujumbe kubwa ni kwamba tamaa zake za madaraka zinaendelea kuwatesa wananchi wake.Pia anapaswa kufahamu kuwa ipo siku atatoka madarakani,iwe kwa njia za kidemokrasia au kwa ubabe.Pengine ni vema akafikiria maisha yake ya baadaye yatakuwaje kwa vile hao wanaoteseka kwa ajili yake wanaweza kummeza pindi “ataporejea mtaani.”

Jingine dogo ambalo linanigusa zaidi mie binafsi ni habari kuwa hatimaye mto Kilombero umepata kivuko kipya.Hizo ni habari njema sana kwa wakazi wa Wilaya za Ulanga na Kilombero kwa vile kivuko hicho ni muhimu sana kwa maisha yao ya kila siku.Nitamke bayana kuwa pamoja na kukaa kwangu Ifakara miaka kadhaa sikuwahi kwenda ng’ambo ya pili ya mto Kilombero (upande wa Wilaya ya Ulanga) kwa vile kivuko chenyewe kilitaka ujasiri wa namna flani kabla hujajitosa ndani yake.

Mwisho,ni pongezi zangu kwa watani wetu wa jadi wa mtaa wa Jangwani.Ushindi wao hapo Dar na baadaye huko Angola ni habari za kufurahisha kwa kila Mtanzania asiyependa kuiona nchi yetu ikiwa kichwa cha mwendawazimu.Mechi iliyo mbele yao ni ngumu kwa ni hao Watunisia ni watu waliozowea kushinda kwa gharama yoyote ile.Hata hivyo,hakuna lisilowezekana katika soka.Kwa vile watakapopambana watakuwa 11 kila upande basi ni suala la mbinu na maandalizi tu.Baadhi ya wachezaji wa Yanga waliwastaajabisha hata Wabrazil wakati timu ya Taifa ilipokuwa huko kwa mechi za majaribio.Naamini hao na wengineo ambao hawako timu ya Taifa,pamoja na “uchawi wa Micho” wanaweza kawaondoa Esperance na hata kufika fainali na mwishowe kutuletea kombe.Najiskia kusema “Yanga Oyeee!!!!”

Alamsiki



0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.