30 Apr 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-60

Asalam aleykum,

Miongoni mwa habari ambazo zinatikisa kwa sasa hapa Uingereza ni dhamira ya mjukuu wa Malkia,Prince Harry,ya kutaka kwenda kwenye uwanja wa vita huko Irak.Harry ambaye kwa sasa ni afisa katika jeshi la nchi hii ameonyesha bayana kuwa lazima aende kushiriki kwenye vita hiyo ambayo tayari imeshagharimu mamia ya maisha ya askari wa Uingereza.Wiki iliyopita kulikuwa na tetesi kwamba Harry “alichimba mkwara” (alitishia) kwamba iwapo hatapelekwa huko Irak basi ataachana kabisa na jeshi.Pia mwishoni mwa wiki kulikuwa na taarifa inayodai kuwa bibi yake Harry,Malkia Elizabeth,angependelea kumwona mjukuu wake akienda vitani hasa kwa vile tukio hilo lingeiletea sifa sana familia hiyo ya kimalkia.Baba mdogo wa Harry,Prince Andrew alishiriki kwenye vita kati ya Uingereza na Argentina kugombea visiwa vya Falklands.Lakini tofauti na hali ilivyokuwa wakati wa vita hiyo,safari hii majeshi ya Uingereza yanakabiliana na adui wa aina tofauti:jeshi lisilo rasmi ambalo miongoni mwa silaha zake kuu ni mashambulizi ya kujitoa mhanga na kuchukua mateka (baadhi ya mateka hao walichinjwa na kuonyeshwa “laivu” kwenye mtandao).

Gazeti moja la mwishoni mwa wiki liliripoti kuwa Waziri wa Ulinzi Des Browne amejivua lawama na kuliacha suala la Harry kwenda Irak kuwa mikononi mwa jeshi la nchi hii.Wachambuzi wa vita vya Irak wanatamka bayana kuwa upo uwezekano wa mjukuu huyo wa Malkia kuishia mikononi mwa vikundi vya wapiganaji (insurgents) kama mateka au kibaya zaidi akaishia kuuwawa,suala ambalo wanadai litakuwa na madhara makubwa sana kwa siasa za Uingereza.Na tayari vikundi vya “insurgents” vimeshatangaza kuwa “Harry ni mlengwa wao namba moja,na ataandaliwa mapokezi rasmi,kabla ya kurudisha mwili wake kwa bibi yake (Malkia) ukiwa hauna masikio.”Tisha toto?Labda,lakini hawa jamaa sio wa kupuuzwa kwani pamoja na Joji Bush kuamua kuongeza wanajeshi wake zaidi ya 20,000 bado wanaendelea kuteketea takriban kila siku.Wiki iliyopita imeshuhudia takriban wanajeshi wa Kimarekani 20 wakiuawa kutokana na mashambulizi yanayofanywa na “insurgents” hao.

Prince Harry anasema kuwa tishio la usalama wa maisha yake huko Irak sio kigezo cha kumzuia yeye kwenda kuitumikia nchi ambayo siku flani katika mahesabu ya kifamilia anaweza kuwa mfalme wake.Anadai kuwa maisha yake hayana thamani tofauti na yale ya askari wengine walioko uwanja wa mapambano au wale waliokwishapoteza maisha yao huko nyuma.Hata hivyo,wapo wanaoona “ushujaa” huo wa Harry ni kitu cha hatari sana kwa vile iwapo kweli “insurgents” wataelekeza nguvu zao zote ili kumteka au kumuua kuna hatari ya askari wengi zaidi kuhatarisha maisha yao kwa ajili ya mtu mmoja (Harry).Kadhalika,ipo hofu kuwa iwapo Harry atatekwa au kuuwawa basi utakuwa ni ushindi mkubwa sana kwa “insurgents” na makundi ya kigaidi kama Al-Qaeda pengine zaidi ya “ushindi” wao wa mashambulizi ya Septemba 11,2001 huko Marekani.

Jingine kwa leo ni changamoto nayoitoa kwa wale wote waliosoma shule ya sekondari ya Tabora Boys.Duniani kote huwa kuna shule,vyuo au taasisi ambazo kwa namna flani haviwezi kutenganishwa na historia ya nchi husika.Mie nilifika hapo mwaka 1990,nikakaribishwa kwa kwata moja kali sana iliyodumu kwa wiki sita.Enzi hizo kulikuwa na mchepuo wa kijeshi,na shule hiyo ilikuwa “maalumu” hasa.Hizo wiki sita za “ngarambe ya ukaribisho” zilipoisha nilijiskia mkakamavu katika kila namna,kimwili na kiakili.Nidhamu ya hapo ilikuwa ni ya kijeshi hasa utadhani uko TMA Monduli,na badala ya yunifomu sie tulikuwa tunavaa kombati za khaki (akinadada wa Tabora Girls nao walikuwa ndani ya kombati kama sie kwani shule yao nayo ilikuwa na mchepuo wa jeshi).

Nilibahatika kuchaguliwa kuwa “Chifu” wa wanafunzi.Kwenye shule za “kiraia” Chifu alikuwa sawa na “Kaka Mkuu” (Head Prefect).Nilikuwa na “mikasi” kadhaa mabegani kuashiria cheo changu kama ilivyokuwa kwa viongozi wengine waliokuwa chini yangu.Najiskia msismko flani nikikumbuka enzi hizo.Hapo kulikuwa hakuna mambo ya “shikamoo mwalimu” au Goodmorning/goodafternoon Sir/madam” bali ni mwendo wa “Jambo afande.”Na sie viongozi tulikuwa tukiitwa maafande pia.Halafu kama nyota ya jaa iliamua kuuwakia ukoo wa Chahali,dada yangu Consolata aliyekuwa mwaka mmoja wa masomo nami alibahatika kuchaguliwa kuwa “Second Chief” huko Tabora Girls,na dada mwingine,Dinna nae alidaka uongozi wa “platuni” (halahala mnaoalikwa kwenye mahojiano Chanel 10,mtu atakaemletea za kuleta anaweza kupigishwa kwata hapohapo studio).Enewei,isijeonekana “tunajifagilia” bure,ngoja nirejee kwenye changamoto nayotaka kuitoa.Sekondari hiyo ya Tabora ina historia ya kipekee nchini.Ni sehemu ambayo Mwalimu alifundisha na viongozi kadhaa wa nchi yetu walipata elimu yao hapo.Nadhani hadi leo ule ubao unaoonyesha viongozi wa wanafunzi tangu “mwaka 47” bado upo (kama upo basi naamini jina langu nalo lipo hapo).Na kwenye ubao huo ndio utamaizi kuwa shule hiyo “imezaa” viongozi lukuki wa nchi yetu.

Niliwahi kusikia kuwa mchepuo wa jeshi umeondolewa shuleni hapo.Hilo ni jambo la kuhudhunisha sana kwa vile ule “ujeshi” ulikuwa ukijenga nidhamu flani ambayo ni adimu sana kuikuta kwenye shule ya kawaida.Wakati wa likizo kundi la wanafunzi lilikuwa likipelekwa msituni kwa ajili ya mafunzo ya kivita.Bila kutia chumvi,napenda kukupasha msomaji wangu mpendwa kuwa kwa kubahatika kupitia Tabora Boys nilifanikiwa kuongoza kikosi kwenye vita.Ofkozi,ilikuwa ni vita ya mfano tu lakini kwa namna maafande walivyokuwa wakiichukulia “siriaz” basi sie “wanajeshi” tulikuwa tunajiskia kama tuko Mtukula tukimwadhibu nduli Idd Amin.Na taaluma hiyo ilikuwa na faida yake tulipokwenda jeshi la kujenga taifa kwa mujibu wa sheria (siku hizooo).Tulijikuta tunapata ki-upendeleo cha namna flani kwa vile kama ni kwata za awali sie tulikuwa tumeshaiva kabla ya kutia mguu kwenye kambi ya JKT.

Sasa naomba kutoa changamoto kwa wale wote waliopitia shule hiyo kuhakikisha kuwa haipotezi sehemu yake katika historia ya taifa letu.Nina wazo ambalo bado nalifanyia kazi la kuunda kitu kama “alumni” ya namna flani (yaani jumuiya ya watu waliosoma mahala hapo).Najua hiyo si kazi rahisi kwa vile baadhi ya waliosoma hapo ni watu wenye majukumu makubwa kitaifa na pengine hawatakuwa na muda wa kujihusisha na jumuiya kama hiyo.Huku ughaibuni,watu hawajali nyadhifa zao linapokuja suala la kuienzi sehemu iliyowafikisha hapo walipo.Si ajabu ukakuta mkutano wa alumni wa taasisi flani ya elimu ikiwakutanisha mawaziri,wafanyabiashara wa kawaida na hata wale ambao mambo hayajawa mambo (majobless.Ndio,huku nako wapo majobless).Nafahamu kuwa kwa Bongo inaweza kuwa vigumu kidogo kwa kigogo kujichanganya na mtu ambaye sanasana jina lake likisikika kwenye chombo cha habari basi atakuwa anakabiliwa na kesi au katajwa kwenye tangazo la kifo,lakini tunaweza kusahau tofauti zetu za kimatabaka na kuangalia namna tunavyoweza kudumisha jina la “Tabora Skuli.”Pengine vuguvugu la namna hiyo linaweza kuhamia na kwenye shule nyingine za kihistoria kama vile sekondari ya Pugu na kwingineko.

Mwisho,nimevutiwa sana na jitihada za mwanamuziki wa kizazi kipya Ambwene Yesaya (AY) ambaye amezindua website yake hivi karibuni.Nilishindwa kujizuia kumpa pongezi zangu nilipoiona kwa mara ya kwanza,na yeye hakufanya “ubishoo” akatoa shukrani zake kwa pongezi na maoni niliyompatia.Website yake inapaswa iwe changamoto wa wasanii wengine hasa kwa vile mtandao ni kitu anbacho kinaweza kumtangaza mtu ulimwengu mzima iwapo mhusika atajituma ipasavyo.Kwa kuwaunga mkono vijana wetu wanaojiajiri wenyewe kwa kutumia vipaji vyao natoa ushauri kwa makampuni ya umma na ya binafsi “kuwapa tafu” wasanii kama AY kwa kuweka matangazo yao kwenye website kama hiyo.Nami ntawaunga mkono kwa kuweka links za websites zao kwenye blogu yangu.Nitumie lugha “ya wenyewe” kwa kusema “nakupa tano mwanangu AY.”

Alamsiki


1 comment:

  1. Mzee katika wasomaji wako, na mimi nimo. Nimekutembela hapa nikukaribishe, na vilevile kujua nyumba yako hii ilivyo. Maoni ntatoa baadae.

    Karibu kwa mikono miwili.

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.