18 May 2007

Asalam aleykum,

Waumini mbalimbali wa dini ya Kihindu hapa Uingereza wametishia kutengeneza “mnyororo wa binadamu” (human chain) ili kulinda maisha ya ng’ombe aitwaye Shambo ambapo kwa imani ya waumini hao ng’ombe ni kiumbe kitakatifu. Ng’ombe huyo ambaye ana umri wa miaka 6 amehifadhiwa kwenye makazi yake huko magharibi ya Wales, na hivi karibuni aligundulika kuwa na kifua kikuu (TB) hali ambayo ilizilazimisha mamlaka zinazohusiana na mifugo kuamuru kuwa ng’ombe huyo achinjwe ili kuzuia kuenea kwa ugonjwa huo. Kinyang’anyiro hicho bado kinaendelea na naahidi kuwajulisha maendeleo yake.

Hilo sio kubwa sana,kilichotawala zaidi kwenye vyombo vya habari ni tangazo rasmi la kung’atuka kwa Waziri Mkuu Tony Blair.Halikuwa jambo la kushtua kwa vile tayari ilikuwa inafahamika bayana kuwa hilo lingetokea hivi karibuni lakini haikujulikana ni lini huyu ndugu ataondoka rasmi hapo nyumba namba 10 Mtaa wa Downing hapo London (makazi ya waziri mkuu).Pia ilikuwa ilishatarajiwa kuwa mrithi wa Blair atakuwa Kansela Gordon Brown,na hilo linaelekea kutimia.Kwa bahati mbaya,au pengine kwa ubishi wake,Blair anaondoka akiwa na doa moja kuu:vita huko Irak.Anaachia madaraka wakati nchi ikiwa katika hali nzuri kwenye nyanja mbalimbali lakini suala la Irak linaonekana kumgubika kabisa.

Blair anaondoka madarakani huku wengi wakiamini kuwa alikuwa kibaraka wa Joji Bushi,kwamba kila alilosema Bushi lilikuwa sahihi kwa Blair japo Bush alionekana kujali zaidi maslahi ya nchi yake kuliko urafiki wake na Blair.Hata hivyo wapo wanaomuona Blair kuwa alikuwa na msimamo thabiti licha ya upinzani mkali kabisa aliokumbana nao katika siasa zake za vita huko Irak.Pengine uimara huo ndio uliomfikisha hapa alipo leo kwani angekuwa legelege pengine angeachia ngazi zamani hizo.

Kuna habari nyingine nyepesi-nyepesi ambayo napenda kushea na wewe msomaji mpendwa.Matokeo ya utafiti mmoja ulofanywa na baadhi ya wanasayansi wa taasisi ya afya ya jamii ya Mailman katika chuo kikuu cha Columbia huko Marekani yameonyesha kuwa katika ndoa kuna uwezekano mkubwa wa mume kutoka nje ya ndoa kuliko mke.Utafiti huo ulikuwa unajaribu kuangalia uthabiti wa taasisi ya ndoa katika mapambano dhidi ya maambukizi ya virusi vya ukimwi.Utafiti huo uliofanywa katika sehemu mbalimbali duniani umetoa ushauri kwamba msisitizo katika kampeni dhidi ya ukimwi kuwataka walio kwenye ndoa “wasitoke nje” unapaswa kuambatana na msisitizo mwingine unaotambua kuwa kuna ushahidi wa kisayansi kwamba walio katika ndoa wanaweza kutoka nje ya ndoa hizo,huku uwezekano wa mume kutoka nje ukiwa mkubwa kuliko wa mke.Watafiti hao wanashauri kwamba kampeni zijumuishe kipengele kinachowataka wanaotaka nje ya ndoa wafanye tendo la ndoa katika njia salama.Yaani hoja hapa sio kubishana kama watu wanatoka nje ya ndoa au la bali ni kuweka msisitizo kwenye nini kinapaswa kufanywa na hao wanaotaka nje ya ndoa.

Wanadai kuwa katika jamii nyingi,kwenye ndoa mume ndio mtafutaji zaidi,na utafutaji huo wakati mwingine hupelekea kuwa mbali na familia yake.Sasa huko aendako anaweza kupata nyumba ndogo au zile wanazoita “hit and run” (mfano mtu anakutana na kimada baa na kesho wanakuwa "hawajuani”).Tatizo ni kwamba katika “mihangaiko hiyo” kuna uwezekano wa kufanya tendo la ndoa lisilo salama.Lakini mume anaporejea nyumbani kwa aibu ya kuulizwa na mama watoto “kulikoni leo unataka tutumie kondomu”,mume anaamua kufanya mapenzi na mkewe bila kondomu japo hana hakika kuwa hajaukwaa huko alokotoka.Hata hivyo, suala la uaminifu sio tatizo kwa wanaume tu bali linaweza kuwepo hata kwa wanawake pia.Kadhalika,sio kwamba hiyo inatokea kwenye kila ndoa na kama zilivyo tafiti nyingine matokeo ya utafiti mmoja hayamaanishi kuwa ndio ukweli katika kila mazingira.Tafiti zina tabia ya kulinganisha matokeo ya sehemu moja na nyingine ilhali sehemu hizo mbili zinaweza kuwa na mila na mazingira tofauti.

Sasa nigeukie mambo ya huko nyumbani.Moja lililonigusa ni habari kwamba uchunguzi unaendelea kuhusiana na watu walimruhusu Braza Ditto atumie mlango wa majaji siku mahakama ilipompatia dhamana.Tatizo sio kuendelea kwa uchunguzi huo bali ni muda uliokwishatumika kwenye uchunguzi huo.Kuna msemo kuwa kuchelewesha haki ni sawa na kunyima haki (justice delayed is justice denied).Wengi wetu tunafahamu kuwa sio kila mshtakiwa anaweza kupewa “upendeleo” wa kupitishwa kwenye mlango wa waheshimiwa,na kwa vile mamlaka husika zilitamka bayana kuwa tendo hilo lilikuwa ni kosa,basi kuna umuhimu wa wahusika kuchukuliwa hatua zinazostahili mapema iwezekanavyo.Mtu anaposema uchunguzi unaendelea anapaswa pia kuelezea kuwa uchunguzi huo unatarajiwa kukamilika lini.Lakini licha ya kutamka hivyo,ni muhimu pia kuushawishi umma kuwa suala hilo linahitaji muda wote huo kulichunguza.Au na hilo linahitaji wataalamu kutoka nje kusaidia kuharakisha uchunguzi huo?

Pia naamini baadhi ya wasomaji wa makala hii wanafahamu msimamo wangu dhidi ya unafiki.Niliwahi kuandika makala moja kuhusu nini kinachotokea ndani ya Kanisa Katoliki,sio huko nyumbani tu bali duniani kote kwa ujumla.Sio siri kwamba kuna utovu wa maadili miongoni mwa baadhi ya watumishi wa Bwana.Bila kupitisha hukumu kwa mtu ambaye hadi sasa anatuhumiwa tu,taarifa kwamba Padri alikuwa na mahusiano na mtoto wa shule,na akamshawishi kutoa mimba kwa njia za kienyeji (hali iliyopelekea kifo cha binti huyo),ni za kusikitisha sana. Tuwe wakweli,tunafahamu baadhi ya viongozi wa dini wanaohubiri tofauti kabisa na wanayotenda katika maisha yao ya kila siku.Isingekuwa ishu kubwa kama kwa kufanya hivyo wanajichumia dhambi (acha mtenda dhambi aende motoni),ni ishu kwa vile wanaokiuka maadili ya uongozi katika kanisa wanatumia fedha zinazotolewa kama sadaka kuendeleza mambo yasiyofaa.Ndio tunajua kuwa wengi wao wana wafadhili walioko nje ya nchi lakini pia tunatambua kuwa sadaka tunazotoa kila Jumapili zinasaidia kuwatunza ili watuhudumie.Na wengine ni wakali kweli kwenye kuweka msisitizo wa “kumchangia Bwana” (kutoa sadaka).

Kuna unafiki wa namna flani kwa vile wakati viongozi wetu wa Kanisa wako makini sana kukemea maovu kwenye mahubiri yao,msisitizo kwenye kujiangalia wao wenyewe ni mdogo.Mie nimetoka katika eneo ambalo kanisa katoliki lina “influence” kubwa miongoni mwa wakazi wa eneo hilo.Bila kuonekana aibu,nafahamu kuna waumini kadhaa wanaojua mapadre wenye watoto au wanaotunza wanawake kana kwamba wako kwenye ndoa.Hivi Kanisa linatutaka tuamini kuwa lilikuwa halijui kabisa namna “mchunga kondoo huyo wa Bwana huko Mbulu” alivyokuwa akivunja amri ya sita hadi kumpa ujauzito binti huyo na hatimaye kumpotezea maisha yake?Au ina maana Kanisa lilikuwa halifahamu kabisa nyendo ya yule fadha alomlawiti mtoto maeneo ya Mlimani (Chuo Kikuu)?Kama Kardinali,maaskofu na maparoko hawajui nyendo za mapadre wao,wanategemea nani afanye kazi hiyo? Na kwa hao wanaoona kuwa hawawezi kuzuia ashki zao, kwanini wasikubali yaishe na kuvua majoho (kuacha utumishi wa Bwana) na kuingia mtaani kisha kuanzisha familia kuliko kuendelea kulitia aibu kanisa?

Maisha wanayoishi watumishi wengi wa Mungu ni tofauti sana na yale ya waumini wao hasa huko vijijini.Wengi wao wanakaa kwenye makazi bora,wanapata huduma zote muhimu na wanapewa heshima kubwa katika jamii wanayoishi,tofauti na baadhi ya waumini wao ambao hawana hata uhakika wa shilingi kumi ya sadaka.Wanapaswa kutotumia vibaya nafasi yao katika jamii bali wawe mfano wa kuigwa miongoni mwao na kwa hao wanaowaongoza.Wanapaswa kutoa kwanza boriti kwenye macho yao ndio wataona vibanzi kwenye macho ya waumini wao.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.