28 Oct 2007

Asalam aleykum,

Kwanza nianze kwa salamu za rambirambi kwa familia,ndugu,jamaa na marafiki wa marehemu Salome Mbatia,aliyetutoka hivi majuzi kutokana na ajali ya gari.Sote ni wasafiri,mwenzetu ametutangulia tu,Bwana ametoa Bwana ametwaa,jina lake lihimidiwe milele.Baada ya rambirambi hizo naomba kuzungumzia suala moja ambalo kwa naona kwa namna flani linaathiri umoja wetu wa kitaifa.Jambo hilo ni kuendekeza itikadi za chama kwenye matukio ambayo kimsingi ni ya kitaifa zaidi kuliko kichama.Katika picha mbalimbali kuhusu msiba wa marehemu Mbatia nimeona “makada” lukuki wa chama tawala wakiwa katika magwanda yao ya kijani na nyeusi.Nikabaki najiuliza,hivi waungwana hao wangevaa mavazi yao ya kawaida wangeonekana hawana majonzi ya msiba huo?Au walivaa mavazi hayo kwa maagizo ya kiongozi flani?Kama ni maagizo kutoka ngazi za juu,mbona viongozi wakuu wa chama hicho walikuwa kwenye mavazi yao ya kawaida tu (hasa suti nyeusi)?JK,Malecela,Karume,Makamba,nk wote walikuwa wamevalia suti nyeusi na wala sio magwanda ya kijani na nyeusi,pengine kwa sababu msiba huo ulikuwa wa kitaifa,na hata jeneza la marehemu halikuvikwa bendera ya CCM bali ya Taifa.

Nafahamu marehemu Mbatia alikuwa mwanachama,kada na kiongozi wa chama dume,lakini marehemu pia alikuwa naibu waziri wa serikali ambayo japo inaongozwa na CCM lakini inawatumikia Watanzania wote bila kujali itikadi zao.Katika utekelezaji wa majukumu yake ya unaibu waziri,marehemu Mbatia alikuwa akigusa maisha ya kila Mtanzania,awe mwanachama wa CUF,TLP,Chadema,au kama sie tusio memba wa chama chochote.Nafahamu waliovaa magwanda ya CCM watasema kuwa walitinga mavazi hayo kutokana na nafasi ya marehemu katika chama,lakini sote tunafahamu kuwa alama za chama (mfano bendera,vipeperushi,mavazi,nk) zina tabia ya kuvuta hisia hasi katika mikusanyiko ya isiyo ya kichama.Nafahamu pia kwamba kila mwombolezaji alikuwa na haki ya kuvaa vyovyote atakavyo lakini pia naamini wengi wetu tunapojiandaa kwenda kwenye misiba huwa tunatafakari nini cha kuvaa,na kuepuka mavazi ambayo yanaweza kuleta hisia tofauti.

Hakuna dhambi kuweka maslahi ya chama mbele ya chama kingine lakini ni dhambi kubwa kuweka maslahi ya chama mbele ya maslahi ya taifa.Chama cha siasa kinaweza kufa lakini taifa lazima liendelee kuwa hai.Mtu anaweza kuamua kuhama chama kimoja na kuingia kingine kadri apendavyo,lakini ni mbinde kwelikweli kuhama utaifa wako na kuchukua mwingine kirahisi namna hiyo.Nafahamu kuna watakaopingana nami,lakini binafsi naamini kwamba kuna wenzetu wamekuwa wakituletea “politiki” hata pale pasipostahili.Yaani matukio kadhaa ya kitaifa yamekuwa yakiporwa na hao wanaotaka kutuonyesha namna gani walivyo wakereketwa kwenye siasa.Na katika hili sio wanachama wa kawaida tu bali hata baadhi ya viongozi wenye nyadhifa serikalini.Kuweka kando mambo ya chama na kuzungumzia masuala ya kitaifa hakumfanyi kiongozi wa serikali kukosa sifa za uongozi.Kuna vikao na mikutano ya chama,na huko ndiko mahala pa kupiga propaganda za vyama.

Kwa kawaida huwa naanza makala zangu na habari za ughaibuni lakini niliona ni vema katika makala hii nikaanza na mada hiyo ya msiba wa marehemu Mbatia,na “kuwananga” wale walioleta mambo ya siasa kwenye msiba huo wa kitaifa.Huku ughaibuni,duru za kisiasa zinaelekea zaidi eneo la Ghuba ambapo kwa upande mmoja hali ya usalama ni ya wasiwasi huko kaskazini mwa Irak kwani majeshi ya Uturuki yameripotiwa kufanya mashambulizi kadhaa dhidi ya Wakurd.Waturuki wanadai kuwa lengo la mashambulizi hayo ni kuwadhibiti wapiganaji wa kikundi cha PKK kinachipigania kuunda kwa taifa huru la Wakurd.Kwa upande mwingine,kuna dalili kwamba Marekani inajiandaa kuivamia Iran.Majuzi,Marekani ilitangaza vikwazo kadhaa dhidi ya Iran,lakini zaidi ya hapo kuna taarifa kwamba jeshi la anga (US air force) limeomba fedha za dharura dola milioni 88 kwa ajili ya kufanya marekebisho kwenye ndege za kivita ziitwazo B2 ili ziweze kuhimili uzito wa mabomu yanayojulikana kama “Big Blu” au “the Mother of All Bombs” (mama wa mabomu yote).Mabomu hayo yana uzito wa takriban tani 13 kila moja,na yana uwezo mkubwa zaidi wa kupenya vizuizi (ardhi,miamba,nk).Inasemekana kuwa majengo ya kituo cha nyuklia cha Iran huko Natanz yapo futi 75 chini ya ardhi,Inaelezwa pia kwamba tayari Marekani imeshatambua “targets” 1000 nchini Iran ambazo zitakuwa za kwanza kushambuliwa pindi mambo yatapokuwa mambo.

Mahesabu ya kisiasa yanaashira pia kwamba wazo la mkutano kati ya Israel na Palestina utakaofanyika hivi karibuni huko Annapolis,Marekani (ambao unatarajiwa “kuzaa” taifa la Palestina) ni miongoni mwa dalili za Marekani kujipanga kuivamia Iran.Yaani mantiki hapo ni kwamba kwa kuunda taifa la Palestina,kelele za mataifa ya Waarabu wa Sunni kama Saudi Arabia na Misri zitakuwa sio kubwa sana pindi Iran itakaposhambuliwa na Marekani.Hata hivyo,wazo la kuishambulia Iran linaangaliwa kwa wasiwasi na baadhi ya wajuzi wa siasa za kimataifa na diplomasia.Kuna wanaodhani kwamba ni vema Marekani ikamaliza kibarua ilichojipachika huko Irak na Afghanistan kabla ya kukimbilia kuivamia Iran.Pia wanaonya kwamba uvamizi dhidi ya Iran unaweza kuzua wimbi kubwa la ugaidi wa kimataifa (pengine kutokana na madai kwamba Iran imekuwa ikivisaidia baadhi ya vikundi vinavyodaiwa kuwa vya kigaidi,mfano Hizbollah),kukongoroa kabisa hali ya usalama nchini Irak na pengine kusababisha bei ya mafuta kupanda zaidi ya dola 100 kwa pipa.

Sababu zinazotolewa na Marekani kuhusu umuhimu wa kuidhibiti Iran ni pamoja na kwamba dunia itakuwa mahala salama zaidi iwapo Iran haitakuwa na uwezo wa kutengeneza au kumiliki silaha za nyuklia (ilishasemwa huko nyuma kuwa dunia itakuwa salama zaidi pindi Saddam Hussein atapong’olewa madarakani).Ukweli ni kwamba Iran yenye uwezo wa kinyuklia ni tishio kwa swahiba mkuu wa Marekani,Israel.Pia kuna wanaotaka Bush aingie kwenye vitabu vya historia kwa “kuiadhibu na kuidhibiti Iran na hivyo kuepusha madhara yanayoweza kutokea pindi nchi hiyo ikiweza kutengeneza na kumiliki silaha za maangamizi”.Waumini wa mawazo haya wanatambua kuwa Bush amebakiwa na muda mchache kabla hajafungasha virago vyake kutoka jengo lilipo namba 1600 Pennsylvania Avenue (makazi ya rais,White House),na wanadhani kwamba asipotumia muda huu kuishikisha adabu Iran,basi inaweza kuwa vigumu mno kufanya hivyo mbeleni hususan iwapo mgombea yoyote wa chama cha Democrats atamrithi Bush.

Nirejee tena huko nyumbani.Hapa nina mawili.Kwanza,katika kikao kilichopita cha Bunge tulisikia namna baadhi ya watendaji katika Wizara ya Maliasili na Utalii wanavyoendeleza ufisadi.Waziri alieleza kuwa ameshakabidhi orodha ya wahusika mahala panapostahili,na akaahidi kuendelea kuwabana mafisadi katika wizara hiyo.Tukio la hivi karibuni ambapo magogo kadhaa yalikamatwa yakiwa tayari kusafirishwa nje,limezuia “mchezo wa kuigiza” ambapo wakati Waziri anasema hivi baadhi ya watendaji wake wanadiriki kumpinga hadharani kwa kusema vinginevyo.Hivi hawa wanaompinga Waziri wanapata jeuri hiyo wapi?Nimeona kwenye gazeti la “Habari Leo” ambapo Waziri Maghembe alieleza kwamba amejipanga vizuri kukabiliana na matatizo yote ndani ya wizara yake,ikiwa ni pamoja na tatizo la ufisadi.Yayumkinika kutabiri kuwa dhamira yake nzuri inaweza isifanikiwe kutokana na kiburi kilichojengwa na baadhi ya anaowaongoza katika wizara hiyo ambapo bila kujali protokali au nidhamu wanadiriki kupinga hadharani na kauli halali ya serikali (kupitia waziri wake).Hivi jeuri,kiburi na kujiamini kwa “wazalendo” hao inatoka wapi?

Mwisho,ni ushindi wa Simba dhidi ya Yanga.Mwenye kununa na anune,lakini ndio hivyo tena,milioni 50 hazikufanikiwa kumaliza uteja wa watani wetu wa mtaa wa Jangwani.Nilishatabiri katika makala za nyuma kuwa atakaefungwa kwenye mapambano wa watani wa jadi ataingia kwenye mgogoro.Mie nadhani kufungwa huko ni sehemu ndogo tu ya tatizo linaloikabili Yanga.Ukiangalia maelezo aliyotoa Mwenyekiti wa klabu hiyo pale mfadhili wao alipojitoa (kwa muda!?) ambapo alieleza kwa undani na kwa kuzingatia vipengele vya sheria kuhusu utata uliopo kwenye suala zima la klabu hiyo kugeuzwa kampuni.He!!muda si mrefu Mwenyekiti huyohuyo alisikika tena akipita huku na kule kuomba radhi.Je ina maana yale maelezo aliyotoa awali hayakuwa sahihi?Mie naamini yalikuwa,bado yako na yataendelea kuwa sahihi kama kweli Yanga (na Simba pia) wanataka wafike sehemu wakajiendesha wenyewe kwa mafanikio na kuachana na utegemezi.Yote yanawekana iwapo kila mmoja atatimiza wajibu wake.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.