31 Mar 2010


Mwaka 1996 nikiwa mwanafunzi wa mwaka wa kwanza pale Mlimani nilipata 'somo' moja muhimu kuhusu wanasiasa wa Tanzania.Ilikuwa ni kwenye mhadhara (lecture) ya Dr (Profesa kwa sasa) Max Mmuya katika somo Siasa na Serikali Tanzania na Nchi Nyingine za Afrika Mashariki (PS 102),ambapo mhadhiri huyo alitupatia wasifu wa wagombea urais wanne walioshiriki Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1995.Pasipo kuingia sana kiundani,wagombea hao wote walikuwa 'wawakilishi wa tabaka tawala'.Hakuna mmoja kati yao ambaye tungeweza kumtambua kama 'mlalahoi'.Ni katika minajili hiyo ndipo makala hii inajaribu kuangalia kama ujio wa CCJ utakuwa na lolote jipya kwa 'mlalahoi' (mtu wa kawaida mtaani)Binafsi,tafsiri yangu ya kwanza ya ujio wa CCJ katika kipindi hiki tunachoelekea uchaguzi mkuu hauna tofauti sana na wanasiasa wanaobadili vyama pindi wakiona hawana nafasi ya kupitishwa na vyama vyao kugombea nafasi flani au wale ambao hawakupitishwa na vyama hivyo.Japo hiyo ni haki yao ya kikatiba,jamii inapaswa kuwaangalia wanasiasa hao kwa jicho la shaka pia.Je wanafanya hivyo kwa minajili ya kupata fursa ya kuutumikia umma au ni maslahi binafsi?Historia inaweza kutusaidia katika kupata jibu la swali hili.Mara nyingi tumesikia wanasiasa wakipita huku na kule wakijaribu kutuaminisha kuwa bila wao hatuwezi kupata maendeleo.Cha kuchekesha ni kwamba baadhi ya wanaotueleza hivyo,wamekuwa madarakani miaka nenda miaka rudi na badala ya kusonga mbele maendeleo yetu yanazidi kudorora.

Ni vigumu kuamini kuwa CCJ italeta mabadiliko yoyote ya maana kwa vile kimsingi chama hicho hakina tofauti na CCM,Chadema,CUF au chama kingine cha siasa.Labda tofauti kubwa ni kuwa CCJ si chama tawala,lakini kama ni hilo basi hata Chadema au NCCR Mageuzi navyo si vyama tawala.Labda tofauti nyingine ni upya wake.Lakini historia pia inatuusia kuwa si kila kipya ni kinyemi.Upya wa chama si jambo la muhimu kwa wananchi bali ufanisi wake katika kuwatumikia.Je katika mazingira tuliyonayo,CCJ inaweza kweli kuwa mkombozi wa Watanzania?Jibu linaweza kupatikana kutoka kwa waasisi wa CCJ na sie wananchi wenyewe.Kwa viongozi wa chama hicho,so far hawajatuthibitishia kuwa ujio wa chama chao utaleta lolote jipya zaidi ya maneno mataaaamu just like ilivyo kwenye miongozo mbalimbali ya CCM.Kama nilivyowahi kuandika mara kadhaa,tatizo la Tanzania (na pengine Afrika kwa ujumla) halijawahi kuwa katika kuunda mawazo au mipango mizuri.Siku zote kikwazo chetu ni usimamizi na utekelezaji wa mawazo/mipango hiyo.

Ni katika minajili hiyo ndipo wananchi wanapaswa kuhoji kama CCJ sio CCM kwenye jezi nyingine.Yani mvinyo wa zamani kwenye chupa mpya.Na kibaya zaidi,kwa kuzingati tukio la jana ambapo mmoja wa wabunge wa CCM Fred Mpendazoe ametangaza kujiunga na CCJ,chama hicho kipya kina kila dalili ya kuwa CCM-B.Hilo halina ubaya iwapo wanaotoka CCM na kujiunga na CCJ watakuwa wanasiasa wenye uchungu wa dhati kwa nchi yetu na wenye nia ya kuutumikia umma kwa uadilifu.Lakini miaka arobaini na ushee ya uhuru wetu imeshatupa darasa zuri kuhusu wanasiasa wetu.Wengi wao wametawaliwa na ubinafsi huku wakiamini kuwa ni wao pekee ndio wenye ujuzi,nguvu,mamlaka na haki ya kutuongoza.Kibaya zaidi,kwa kiasi kikubwa wengi wao wamechangia mno kutufikisha hapa tulipo:hohehahe wa kutupwa huku raslimali za nchi yetu zikiibiwa kana kwamba hazina mwenyewe.

Pengine siitendei haki CCJ kwa kuiona kama shati chakavu lililopigwa pasi na kunyunyiziwa uturi.Lakini nina kila sababu ya kuhofia ujio wake.Japo natambua kuwa katika siasa timing is everything,lakini kwa muda huu mchache uliosalia kabla ya uchaguzi mkuu,yayumkinika kuamini kuwa chama hicho kitakuwa washiriki tu badala ya kuwa serious contenders.Hilo si baya sana iwapo matokeo mabaya kwenye uchaguzi ujao hayatopelekea hadithi kama za NCCR Mageuzi mwaka 1995.Tatizo la vyama vinavyofikiria uongozi tu badala ya utumishi kwa umma ni kwamba vikishindwa uchaguzi basi ndio inakuwa mwisho wa safari.Yani vinakuwa kama mapenzi ya pesa,ukiwa nazo utaonekana mfalme,'ukifulia' unabwagwa.

Nimalizie kwa hitimisho lisilopendeza kwa wale wanaotaka kuiona CCM ikidondoka kwenye uchaguzi mkuu ujao.Kinyume na fikra zinazoelekea kupata umaarufu kuwa ujio wa CCJ ni kilio kwa CCM,ukweli ni kwamba chama hicho kimekuja kugawa kura za wapinzani.Hilo linaweza tu kuepukika iwapo CCJ itaamua kushirikiana na chama kingine/vingine kwenye uchaguzi mkuu ujao.Lakini kinachokwaza ushirikiano wa vyama vyetu vya upinzani sio kutofautiana kwa sera zao bali ubinafsi.Wapinzani wataendelea kuwa wapinzani kwa muda mrefu huku CCM 'ikipeta' licha ya kulea ufisadi na kuipeleka nchi kusikoeleweka.Kwa wapiga kura,CCM inabaki kuwa the devil they know.Ni uamuzi mbovu lakini at the end of the day unaendelea kuiweka CM madarakani.

Na nisisahau.CCJ ina kazi ya ziada ya kukabiliana na 'nguvu za giza' zinazotumia pesa za walipa kodi kuhakikisha CCM inatawala milele.Na si ajabu miongoni mwa wanaopigia debe CCJ,au watakaojiunga hivi karibuni, ni wawakilishi wa nguvu hizo za giza.

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.