9 Apr 2010

Takriban nusu karne tangu tupate uhuru tunakutana na takwimu zinazopaswa kuchochea mjadala wa umuhimu wa kumuondoa mkoloni.Kwa mujibu wa gazeti la Mwananchi,zaidi ya asilimia 90 ya uchumi wa Tanzania unamilikiwa na wageni.Kwa bahati mbaya (au makusudi) habari hiyo haikuingia kwa undani kujadili impacts zinazosababishwa na hali hiyo lakini kilicho wazi ni kwamba uhuru wetu uko mashakani.Katika zama hizi ambapo nguvu za kiuchumi zina athari kubwa kwenye siasa,ni dhahiri kuwa hata huo uhuru wetu wa kisiasa unabaki kuwa wa kinadharia zaidi kuliko uhalisia..Habari husika ni hii hapa
Na Ramadhan Semtawa
ZAIDI ya asilimia 90 ya uchumi wa Tanzania unaendelea kumilikiwa watu wenye asili ya Asia na Ulaya, takwimu zinaonyesha.

Takwimu hizo zimetolewa huku kukiwa na kilio kikubwa cha Watanzania wazawa, kutaka wajengewe mazingira mazuri ya uwezeshaji ili kumiliki uchumi wa nchi kupitia migodi mikubwa ya madini na maeneo nyeti ya kiuchumi.

Lakini wakati kilio hicho kikiwa hakijapata ufumbuzi, Taarifa ya Utendaji ya Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, iliyowasilishwa katika kikao cha Kamati ya Bunge ya Fedha na Uchumi jana, ilisema watu wenye asili ya mabara ya nje wanaomiliki uchumi wa Tanzania ni sawa na asilimia moja ya Watanzania.

Takwimu hizo zilifafanua kwamba, asilimia hiyo 90 ya uchumi wa nchi umeshikwa na watu wenye asili ya Asia na Ulaya, wakati asilimia 99 ya Watanzania wazawa, hawana kitu.

Kwa mujibu wa takwimu hizo zilizowasilishwa katika kikao hicho kilichohudhuriwa pia na Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi, Omar Yusuph Mzee, tatizo la Watanzania weupe kumiliki uchumi, lilianza tangu wakati wa ukoloni.

"Wakati wa enzi za ukoloni na hata baada ya uhuru Watanzania wengi hawakuwa wakishiriki kikamilifu katika kumiliki uchumi wa nchi yao. Uchumi wa nchi umeendelea kutawaliwa na wageni wakishirikiana na Watanzania wachache," inasema sehemu ya ripoti hiyo.

Ripoti hiyo inasema "asilimia 99 ya wananchi ni Watanzania weusi na asilimia 1 iliyobaki inajumuisha Waasia na Wazungu ambao wana miliki zaidi ya asilimia 90 ya uchumi wa nchi hii (Msambichaka, 2008).

"Hii ina maana asilimia 99 ya Watanzania halisi wanamiliki asilimia 10 tu ya uchumi wa taifa lao," inasisitiza ripoti.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, serikali imekuwa ikifanya juhudi mbalimbali za kurekebisha kasoro zilizoko, ikiwa ni pamoja na kuanzisha (lililokuwa) Azimio la Arusha, Vijiji vya Ujamaa, Elimu ya Kujitegemea, Serikali za Mitaa, Vyama vya Ushirika, Sera ya Uwekezaji na Sera ya Ubinafsishaji wa Mashirika ya Umma.

Inasema hata hivyo,juhudi hizo hazijazaa matunda yaliyotarajiwa na kwamba na kwamba kushindikana kwa juhudi za kuwawezesha Watanzania kushiriki kikamilifu katika kujenga uchumi wa nchi yao, ndilo chimbuko la kubuniwa kwa mkakati wa kuwawezesha wananchi kiuchumi, katika ilani ya CCM ya mwaka 2000."

CHANZO: Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.