11 May 2010

Shamsi Vuai Nahodha.Huyu ni Waziri Kiongozi huko Zanzibar.Naomba kukiri hadharani kuwa kwa muda mrefu nimekuwa nikimuona mwanasiasa huyu kama 'yupo yupo' tu.Unajua kuwa mwanasiasa au kiongozi kunapaswa kuendana na mchango wa namna flani kifikra au kimatendo.Nyerere hakumbukwi kwa vile tu alikuwa mwanasiasa au kiongozi bali jitihada na mchango wake kwa umma,hata kama baadhi ya maeneo alikosea (hiyo ni makala nyingine: ALIPOKOSEA NYERERE).
Pasipo kutarajia,Nahodha kanipa 'surprise ya nguvu'.Ameongea maneno ya busara sana kuhusu fikra potofu zilizotawala akilini mwa viongozi wengi wa CCM kuwa chama hicho kitatawala milele.Japo si dhambi kwa chama kutawala milele (kama inawezekana na kama kinakidhi matakwa ya kinaowaongoza),ni uzembe wa tafakuri kuamini kuwa CCM itatawala daima hasa kutokana na uswahiba wake na ufisadi,kauli za kibabe hata kwenye mwaka wa uchaguzi na kupuuza watu waliokiweka chama hicho madarakani.Sasa,Waziri Kiongozi Nahodha amewatahadharisha wana-CCM wenzake kwamba KUNA SIKU CCM ITANG'OLEWA.Hebu msome hapa chini
Nahodha: Iko siku CCM itang'olewa


• AKUMBUSHA WAJIBU WA VIONGOZI KWA WANANCHI
na Mwandishi Maalum, Mererani
WAZIRI KIONGOZI wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Shamsi Vuai Nahodha amewataka wana CCM kuacha kujidanganya kwamba chama chao kitaendelea kutawala milele.
Nahodha, mmoja wa viongozi wa juu wa CCM na serikali alitoa kauli hiyo jana wakati akiwahutubia wananchi katika kituo cha kulelea watoto yatima cha Rafiki Child Care kilichoko Mererani wilayani Simanjiro mkoani Manyara.

Kiongozi huyo ambaye kimamlaka ni wa pili baada ya Rais Amani Karume katika SMZ aliwataka wana CCM kuachana na dhana kwamba chama chao hakiwezi kuondolewa madarakani na vyama vya upinzani.

“Ninatofautiana kimtazamo na watu wanaosema kwamba CCM itaendelea kutawala milele na milele, hapa kama hatutajipanga vizuri ipo siku chama chetu kitang’olewa madarakani…tusibweteke,” alisema Nahodha.

Waziri Kiongozi alitoa kauli hiyo muda mfupi baada ya Katibu wa CCM wilaya ya Simanjiro, aliyetajwa kwa jina moja la Mujungu kuhutubia na kutamka kuwa, CCM haiwezi kuondolewa madarakani na vyama vya upinzani.

“Wapo wana CCM ambao kimtazamo wanaona sisi ndiyo wenyewe, kumbe wenye chama ni wananchi wanaowatawala. Tuna kila sababu ya kuwa makini katika utelezaji wa majukumu yetu… jambo hili nawaambia si kweli,” alisema Nahodha.

Akitoa mfano, Nahodha aliwataka wana CCM kujifunza kutoka katika nchi jirani ambako baadhi ya vyama vilivyopigania uhuru kama ilivyo CCM vimeng’olewa madarakani.

Alikitaja chama cha Kenya African National Union (KANU) ambacho kilipigania uhuru wa Kenya kuwa mmoja wa vyama vilivyopata kung’olewa madarakani.

“Kumbukeni namna ambavyo KANU ilisambaratika kule Kenya… leo hii imesahaulika kabisa. Lakini si huko tu, kule Zambia (UNIP) na Malawi (MCP) vyama tawala vilibwagwa vibaya na sasa vimesahaulika masikioni mwa wananchi,” alionya Nahodha.

Akiendelea, alisema ni wazi ipo siku wananchi wanaweza kukichoka CCM na kukibwaga iwapo viongozi watashindwa kutimiza ndoto za wananchi za kuwaletea maendeleo.

“Kuna mwanafalsafa mmoja mmoja anasema, msitafute uzuri wetu kwa kuangalia jinsi tulivyo, bali kwa kuangalia yale mema tuliofanya,” alisisitiza Nahodha.

Alisema uwajibikaji wa baadhi ya viongozi wanatokana na CCM ndani ya CCM unatia shaka inayoweza kuwafanya wananchi kukichukia chama hicho.

Alisema jukumu kubwa la viongozi wanaotokana na CCM ni kutekeleza majukumu yao kwa Watanzania kwa kuyafanya maisha yao yawe bora zaidi.

“Yuko mwanafalsafa mmoja wa zamani, aliwahi kusema maneno haya: ‘Tutakapokufa msitutafute katika makaburi yetu yaliyotengenezwa vizuri kwa chokaa bali mtutafute katika nyoyo za watu tuliowasaidia’. Ninawashauri viongozi wenzangu wa serikali na chama tuitumie sana busara ya mwana falsafa huyo,” alionya Vuai.

Katika hatua nyingine, Nahodha alieleza kusikitishwa na kuibuka kwa malumbano ya kisiasa miongoni mwa viongozi katika mkoa wa Manyara akisema hali hiyo haina faida kwa wananchi wanaowaongoza.

Kauli hiyo ya Nahodha iliyoonekana kuzungumzia na kukerwa na malumbano yaliyoibuka wiki iliyopita kati ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Henry Shekifu na Mbunge wa Simanjiro, Christopher ole Sendeka


0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.