14 Oct 2010




Siku kama leo,mwaka 1999 Tanzania ilimpoteza muasisi wa taifa,Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.Kilichowaliza Watanzania wengi ni hofu na mashaka kuhusu hatma ya taifa lao.Pamoja na mapungufu yake ya kibinadamu,Mwalimu alijitahidi kadri awezavyo "kuita koleo ni koleo na sio kijiko kikubwa".Ni katika ujasiri huo wa Mwalimu ndipo alisimama kidete mwaka 1995 kukataa jitihada za Jakaya Kikwete na Edward Lowassa kuingia Ikulu.Miaka 10 baadaye,huku Mwalimu akiwa kaburini,Jakaya Kikwete na swahiba wake Lowassa walifanikiwa kuukwaa uongozi wa Taifa letu.

Bahati nzuri,Mungu hamfichi mnafiki.Japo leo hii Mwalimu ni marehemu na hana namna ya kuwalaumu Watanzania kwa kupuuza ushauri wake kuhusu Kikwete na Lowassa,uamuzi wa wanasiasa hao wawili kupuuza ushauri wa Mwalimu na hatimaye kuwania na kushinda uongozi wa juu wa taifa letu umetusaidia kufahamu kwanini Nyerere aliwapinga in the first place.Bahati nzuri zaidi,Lowassa alikuwa majeruhi wa papara zake,na akalazimika kujiuzulu baada ya kuliingiza taifa kwenye mkenge wa kusaini mkataba na kampuni ya briefcase ya Richmond.Bahati mbaya,na kutokana na Katiba yetu kumlinda rais kupita kiasi,Kikwete alisalimika japo haihitaji utafiti wa kichakachuaji wa Redet au Synovate kutambua kuwa Richmond na mrithi wake Kagoda,kama ilivyo kwa skandali za EPA,Meremeta,Tangold,nk ni ishu zilizokuwa na baraka za mkuu wa nchi,yaani Jakaya Mrisho Kikwete.

Miaka mitano ya utawala wa Kikwete inapaswa kuwafumbua macho kwanini Nyerere hakutaka Kikwete awe rais.Na kama tuna imani na Nyerere hadi leo,basi tutazidi kuonekana watu wa ajabu iwapo tutatoa nafasi nyingine kwa Jakaya kulikongoroa taifa letu.Wasiwasi wa Nyerere kwa Kikwete ulielemea zaidi kwenye aina ya watu waliomzunguka mwanasiasa huyu.Kwa bahati mbaya,Nyerere hakuwa hai mwaka 2005 kushuhudia namna Kikwete alivyotumia kila aina ya hila na hujuma kukwaa urais akisaidia na kila aina ya binadamu huku wengi wao wakiwa ni watu hatari kabisa kwa ustawi wa taifa letu.Watu hao ambao hawana tofauti na kundi hatari la Mafia bado wapo na ndio wanaohangaika huku na kule kuhakikisha 'mlinzi' wao-Kikwete-anarejea tena madarakani kwa vile wanafahamu laiti mzalendo kama Dokta Wilbroad Slaa akiingia Ikulu basi makazi ya mafisadi hao yatakuwa Keko kama sio Segerea...

Tuweke kando siasa za haiba.Tuweke kando tabasamu mwanana la Jakaya Kikwete-tabasamu linalowanufaisha zaidi mafisadi kuliko walalahoi.Tuweke kando hayo maji ya bendera ya CCM waliyokunywa wakereketwa.Tuangalie mwelekeo wa taifa letu.Tujiulize hatma ya taifa hili huku tukitambua kuwa hatuna pa kukimbilia pindi Kikwete na watu wake wakituingiza matatizoni zaidi ya ilivyo sasa.

Kampeni zinazoendelea zimeshashuhudia kila aina ya ufisadi unaofanywa na wafuasi wa Kikwete.Wengi wao hawafanyi uhuni huo kwa vile wanampenda Kikwete bali wanalinda nafasi zao na maslahi yao.Hawako tayari kuona Dokta Slaa anaingia Ikulu kwa vile wanafahamu bayana kuwa "watanyang'anywa mapande makubwa ya keki ya taifa" wanayoyafakamia kwa ulafi mkubwa.

Njia bora ya kumwenzi Baba wa Taifa ni kusema HAPANA kwa ufisadi na mafisadi.Na njia ya kufanya hivyo ni kupiga KURA NYINGI ZA HAPANA KWA KIKWETE na CCM yake.Watanzania wasitegemee miujiza kutoka kwa mtu huyu aliyetuthibitishia bayana kuwa hajui chanzo cha umasikini wa nchi yetu,asiyehitaji kura za Wafanyakazi,anayedhani mimba za wanafunzi wa kike ni kimbelembele chao tu,anayeamini kuwa waathirika wa ukimwi wameukwaa ugonjwa huo kwa kimbelembele chao,na asiyetaka kuomba msamaha kwa wimbo la ufisadi lililoshamiri katika miaka yake mitano ya utawala.

Naamini Baba wa Taifa angekuwa hai leo,angesimama hadharani na kumkataa Kikwete kwa vile sababu zilizopelekea amkatae 1995 sio tu bado zipo bali zimethibitika kwa vitendo kati ya 2005-2010.Uhuru uliopiganiwa na Nyerere na wenzake haukumaanisha uhuru wa mafisadi kama mmiliki wa KAGODA ambaye hadi leo anahifadhiwa na Kikwete na wasaidizi wake.

Ewe Mtanzania,unataka Kikwete na CCM wafanye nini zaidi hadi ufikie hatua ya kusema SASA YATOSHA (Enough is enough)?Kama kosa lilishafanywa 2005 kwa kumpa nafasi ya majaribio na amefeli,hakuna haja ya kumpa fursa ya kurejea tena.Na bahati nzuri safari hii tuna Mtanzania mzalendo (Dokta Slaa) ambaye ujasiri wake kama mbunge umefunika utendaji wa Kikwete,Lowassa,Chenge,Rostam Aziz,Karamagi,Kingunge,Msabaha,Marehemu Ballali,Idris Rashid,Basil Mramba,Yona na wababaishaji wengineo.Katika uchaguzi huu hatuna sababu ya kutojikwamua na makucha ya ufisadi kwa vile tuna alternative iliyo bora ambayo ni Dokta Slaa.

NJIA PEKEE YA KUMWENZI MWALIMU NI KUENZI BUSARA ZAKE ZA KUMKATAA KIKWETE MWAKA 1995.TULIPUUZA BUSARA HIZO MWAKA 2005,PENGINE KWA VILE NYERERE HAKUWEPO KUTUONYA.LAKINI MUNGU AMETUSAIDIA KUTONYESHA BAYANA KWANINI NYERERE ALIMKATAA KIKWETE.KWAHIYO,NJIA MWAFAKA YA KUMWENZI BABA WA TAIFA (NA KUMWOMBA MSAMAHA KWA KUPUUZA USHAURI WAKE WA 1995) NI KUMWONDOA KIKWETE MADARAKANI KWA NJIA YA KURA HAPO OKTOBA 31.KUMWONDOA KIKWETE NDIO NJIA MWAFAKA YA KUONDOKANA NA UFISADI.YEYE NDIO SHINA NA HAO WAPAMBE NI MATAWI TU.TUKIONG'OA SHINA LA UFISADI BASI MMEA MZIMA WA UFISADI UTAKUWA HISTORIA.

INAWEZEKANA.TIMIZA WAJIBU WAKO

1 comment:

  1. Katika makala zote ulizoandika kuhusu JK nafikiri hii imenena hasa na kuonyesha uzalendo wako kwa Taifa letu la Tanzania....tunashukuru sana bwana Chahali kwa ufafanuzi wako. Mungu amlaze pema peponi Kipenzi chetu, mzalendo Mwalimu Julius Kambarage Nyerere

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.