10 Jan 2011



Tanzania tuna tatizo kubwa.Hakuna haja ya kunyoosheana vidole as to nani amechangia tatizo hilo bali cha muhimu na haraka ni namna tutakavyoweza kutatua tatizo hili.Nisimung'unye maneno: tatizo kubwa linaloikabili ni kuwa na Rais ambaye takriban miaka sita tangu aingie Ikulu haelewi wajibu wake.

Hivi msomaji mpendwa wa blogu hii utamuelezeaje Jakaya Kikwete,Rais wetu,baada ya kumsikia akijitetea kwa mabalozi wanaowakilisha nchi zao Tanzania kuwa "unyama wa hali ya juu uliofanywa na polisi huko Arusha,na kusababisha vifo vya Watanzania wasio hatia,ni BAHATI MBAYA"!!!

Yani Kikwete aliishiwa kabisa na cha kudanganya mpaka akakurupuka na excuse dhaifu kiasi hiki!Bahati mbaya kwa maana gani?Bahati mbaya IGP Said Mwema kutengua dakika za majeruhi ruhusa ya maandamano iliyotolewa na RPC wa Arusha?Bahati mbaya polisi kuachana na jukumu la kusindikiza maandamano ya amani na badala yake kuanza kuwaadhibu wananchi wasio na hatia ambao "kosa" lao lilikuwa kutumia haki yao ya kikatiba kuandamana kwa amani?Bahati mbaya kupuuza miito kutoka kada mbalimbali juu ya umuhimu wa kutafuta ufumbuzi wa mgogoro wa umeya wa Arusha?Au bahati mbaya kwa risasi kutoka kwenye mitutu ya bunduki na hatimaye kutoa uhai wa Watanzania wasio na hatia?

Au Kikwete alikuwa anamaanisha kwamba unyama wa polisi wake dhidi ya wafuasi wa CUF walipoandamana,au vitendo vya udhalilishaji vya polisi hao dhidi ya wastaafu wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki,au unyanyasaji uliozoeleka dhidi wa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kila wanapoandamana,ni BAHATI NZURI kwa vile hakuna aliyeuawa?

Nashindwa hata kuhisi mabalozi walipatwa na mawazo gani walipomsikia mkuu wa nchi anatoa kauli ya ajabu kiasi hicho.Nahisi kuna waliomhurumia kwa kijibebesha jukumu asiloweza.Hii inanikumbusha wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 (ambazo zilinikuta nikiwa huko nyumbani kwa miezi kadhaa).Kuna baadhi ya wajuzi wa siasa za Tanzania waliniambia kuwa Kikwete anaweza kushinda urais kwa vile ana timu ambayo iko tayari kufanya lolote kuhakikisha anapata ushindi LAKINI urais wake utakuwa kituko.Na kituko amekuwa.

Kuna watakaosema wa kulaumiwa ni washauri wake.Lakini hao watakuwa wamesahau kuwa alipoanguka Mwanza alitanabaisha kuwa huwa anapuuza ushauri wa washauri wake (ambapo tulielezwa walimshauri apumzike kabla ya kukumbwa na zahma hiyo).Sasa inawezekana kabisa kuwa hata kabla ya kuongea na mabalozi hao,washauri wake walimshauri kitu sensible cha kuongea lakini akapuuza.Au pengine waliona hakuna haja ya kumshauri mtu ambaye ni "haambiliki".

Lakini tukiweka kando excuse hiyo ya kitoto iliyotolewa na mtu tuliyemkabidhi jukumu la kutuongoza Watanzania takriban milioni 50,ukweli kwamba Kikwete amediriki kujiumauma kwa mabalozi unapigia mstari ushauri niliotoa kwenye makala yangu iliyopita.Katika makala hiyo niliwashauri Watanzania wanaoishi katika nchi wafadhili wa Tanzania kuwasiliana na wabunge/wawakilishi wao na kuwafahamisha udikteta wa Kikwete,kisha kuwaomba wafikishe kilio cha Watanzania kwa serikali za wafadhili hao.Kikwete amelazimika kuokoteza excuses kwa vile anatambua bayana kuwa ni lazima awapoze wafadhili kwani mchango wa wafadhili hao ni muhimu sana kwa ustawi wa taifa letu.Ni muhimu zaidi kwa ustawi wa Kikwete na serikali yake inayosifika kwa matumizi ya anasa yanayozidi mapato.Wafadhili wakiamua kusitisha misaada,serikali itaanguka within months if not weeks.Lakini idea yangu ya kufikisha ujumbe kwa nchi wafadhili haikulenga kuwashawishi wasitishe misaada bali naamini wao wanaweza kumbana dikteta huyu aanze kuheshimu haki za binadamu.

Na kuthibitisha kuwa Kikwete alikuwa anawazuga mabalozi hao,gazeti la Tanzania Daima lina habari kuwa jeshi la polisi limezuia maandamano ya amani huko Songea yaliyoandaliwa na Chadema kupinga ufisadi katika sekta ya kilimo. Huu ni uthibitisho tosha kuwa unyanyasaji wa raia wasio na hatia na ukiukwaji wa haki za binadamu unaofanywa na polisi sio suala la BAHATI MBAYA kama anavyozuga Kikwete.Ni utekelezaji wa maagizo ya serikali iliyopo madarakani inayoongozwa na Kikwete huyohuyo.

Hivi Kikwete ameshindwa angalau kuwatosa Waziri wa Mambo ya Ndani Shamsi Vuai Nahodha,IGP Mwema na RPC wa Arusha kuwa "mbuzi wa kafara" ali mradi imsaidie kudanganya kuwa yeye hahusiki na maagizo yaliyopeleka polisi kuua.Hawezi kuwatosa kwa vile ni kiongozi anayeendekeza ushkaji.Sasa kama familia haiwezi kuongozwa kishkaji,nchi ikiongozwa kwa mtindo huo inakuwaje?

Na kuna kila dalili kuwa hivi sasa Kikwete anaongoza nchi na CCM yake kwa mtindo wa "bora liende".Hebu angalia jinsi ishu ya fidia kwa Dowans inavyoonyesha mparaganyiko kwenye kabineti ya Kikwete.Wakati Waziri William Ngeleja anatweta kuwakikishia mafisadi wa Dowans kuwa lazima walipwe kwa utapeli wao,Waziri Samuel Sitta anatangaza hadharani kuwa kuwalipa Dowans ni jambo la hatari.Uwajibikaji wa pamoja Kikwete's cabinet style!Huko CCM,Katibu wa chama hicho mkoani Arusha,Mary Chatanda anawawakia viongozi wa dini akiwataka wavue majoho yao wajiunge na siasa badala ya kukemea maovu (mpuuzi huyu anakosa adabu hata kwa Watumishi wa Mungu!).Kwa upande mwingine,Katibu Mkuu wa chama hicho,Yusuph Makamba,anadai kila mtu ana uhuru wa kutoa mawazo yake including viongozi wa dini.Na yote hayo yanatokea huku yakiweka kivuli kwenye tukio la kihistoria la diwani wa CCM kujiunga na Chadema.Tukio hili linapaswa kuchukuliwa kama ugonjwa nyemelezi kwa mwathirika wa ukimwi: linaashiria mwanzo wa mwisho wa CCM.

NIMALIZIE KWA KUKUMBUSHIA WITO WANGU KWA WATANZANIA WENZANGU WANAOISHI NCHI ZA WAFADHILI WA TANZANIA.KUWA MBALI NA NYUMBANI ISIWE SABABU KWETU KUSHINDWA KUSAIDIA UPATIKANAJI WA UHURU WA PILI WA TANZANIA (wa kwanza ulikuwa wa kumwondoa mkoloni,wa pili ni wa kuondoa udhalimu,ufisadi,ubabaishaji,unyanyasaji,ukiukwaji haki za binadamu,udikteta na kila baya unalofahamu).TUWASILIANE NA WABUNGE/WAWAKILISHI KATIKA MAENEO TUNAYOISHI NA KUWAOMBA WATUFIKISHIE KWA SERIKALI ZAO VILIO VYA WATANZANIA WENZETU WANAONYANYASIKA KWA KILA HALI CHINI YA UTAWALA WA KIKWETE NA CCM YAKE

1 comment:

  1. the power allow him to say that coz there is no article which can make him to step down for that words....
    let us be patients as we are always....

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.