20 Sept 2011


Kama ilivyozoeleka,blogu hii inaelemea zaidi katika masuala ya siasa.Lakini kuna nyakati ninajaribu kuangalia nyanja nyingine za maisha katika jamii.Na kwa bahati nzuri kabla ya kuzamia kwenye Siasa kitaaluma nilikuwa mwanafunzi wa Sosholojia (ndio mchepuo niliosoma katika Shahada ya Kwanza hapo Mlimani).

Ninajaribu kuanzisha utaratibu ambapo angalau mara moja kwa wiki nitajadili mada ya kijamii,hususan masuala ambayo ni ya kibinafsi zaidi kama vile mahusiano,mapenzi,nk.Nakaribisha michango na maoni kutoka kwa wasomaji.

Leo ninaanza na jinsi mwanaume anavyoweza kukabiliana na kuvunjika kwa uhusiano kati yake na mwanamke.Karibu sana.

JINSI YA MWANAUME KUDILI NA KUVUNJIKA KWA UHUSIANO NA MWANAMKE

Pointi tatu muhimu za kuzingatia:

  • Kwanza unapaswa kufuta kumbukumbu zote za uhusiano uliovunjika
  • Jaribu kutumia muda mwingi kuwa karibu na watu 'uliowapuuza' wakati ukiwa 'bize' na mwandani wako.Watu hao wanaweza kuwa familia yako,ndugu zako au marafiki zako
  • Kisasi kikubwa dhidi ya aliyekubwaga ni mafanikio.Kwahiyo hamasika kupata mafaniko ili 'ulipe kisasi.'
Hakuna anayeweza kubisha kwamba moja ya mambo magumu kwa manaume yoyote yule (na kwa wanawake pia) ni pale uhusiano na mwenza wako unapovunjika.Mara nyingi wanaume wengi wanapokumbwa na tatizo hilo hujipa matumaini potofu kwamba maisha yataendelea kama kawaida licha ya ukweli kwamba mioyoni mwao wanaumia vya kutosha.Wengi huendelea kujifariji na matumaini 'feki' kuwa wenza waliowabwaga watarejea.

Matokeo ya matumaini hayo 'feki' ni mithili ya mkuki wa kukataliwa wenye makali pande zote (double edged sword of rejection).Kwanza ni maumivu yanayotokana na ukweli kwamba umebwagwa,na kisha ukweli mwingine unaofuatia baadaye kuwa matarajio feki kuwa mwenza atarejea,well,yalikuwa feki.Mwenza wako ndio ameondoka moja kwa moja,na hatorejea (hapa tunazungumzia kubwagana ambako hakuna dalili wala uwezekano wa suluhu).

Lakini maumivu haya yanaweza kufupishwa kwa aliyebwagwa kutambua kuwa hali ndio hiyo-ameshabwagwa na hakuna uwezekano wa kurejea katika hali ilivyokuwa awali.Kuendelea kusubiri na kutarajia miujiza ni sawa na kujifungia kwenye mzunguko wa mateso usio na mwisho (endless circle of turture).

Kwahiyo ili kumudu kuendelea na maisha yako ya kawaida baada ya kubwagwa (au hata kubwagana) jaribu kufuata njia zifuatazo:

ACHA KUJILAUMU

Mara nyingi sie wanaume tumejenga tabia ya kuwa mithili ya watoto wakubwa (big babies) ambapo hatuachi kujilaumu.Kubwagwa ni kama kunaongeza ukubwa wa tabia hii.Kuna wanaochukulia kubwagwa kama mwisho wa dunia,yaani kana kwamba kuondoka kwa mwenza wako maishani mwako ni kama ameondoka na sababu ya wewe kuendelea kuishi.

Lakini ukijaribu kidogo tu kujiuliza "Niliishije kabla sijakutana na huyu aliyenibwaga?" utagundua kuwa ulikuwa ukiishi kama kawaida,na kama binadamu wengine.Kwahiyo,huu ni ushaidi tosha kuwa kama uliwahi kuweza kuishi bila mwenza aliyekubwaga ni dhahiri unaweza kuishi pia baada ya mwenza huyo kuondoka maishani mwako.Acha kujilaumu,jipange upya,na endelea kuishi.

FUTA KUMBUKUMBU

Kama nilivyoandika hapo juu,wengi wa wanaume wanaobwagwa huendelea kuwa na matumaini 'feki' kuwa mwenza aliyeamua kuondoka atarejea.Kwamba labda ni tisha toto tu,au anatikisha kiberiti tu.Mara nyingi wanaume tunapobwagwa hatupendi kukiri hadharani kuwa inatuuma.Wengi wetu hujifanya jasiri mbele ya 'washkaji' zetu tukijigamba kuwa 'ahh yule demu anadhani mimi nitababaika kwa vile tumeachana' (actually huwa tunakwepa kutumia neno 'kanibwaga').

Kiasili,katika mahusiano wanaume wengi wanapenda kuwa ndio walioshika usukani.Kwahiyo hata wanapobwagwa bado watajaribu kudanganya umma kuwa wao ndio waliokuwa wa kwanza kubwaga.Lakini kimsingi huko ni kujidanganya kwa sababu hao unaojaribu kuwaaminisha ujasiri wao hawajali sana (na pengine nao wana ishu zao binafsi zinazowanyima nafasi ya kujihangaisha na ishu zako).

Penigne una picha za mwenza aliyekubwaga,au zawadi mbalimbali alizokupatia wakati wa uhusiano wenu.Licha ya kubwagwa,unaweza kuogopa kuzitupa kwa hofu kuwa labda atarejea na akikuta azawadi alizokupatia hazipo atakasirika na kuondoka tena.Tumia akili yako vizuri.Ameondoka jumla,hatorudi.Usijaze bure nafasi kwenye albamu yako au kwenye sehemu unapoweka zawadi/kumbukumbu zako kwa matarajio hewa.

Uwepo wa kumbukumbu hizo (picha, zawadi,nk) ni sawa na uwepo wa mwenza aliyekubwaga kiroho japo si kimwili.Kila utakapoziona utaendelea kumkumbuka na kutamani awepo au arejee maishani mwako.Ukweli ni kwamba hatorejea.Cha kufanya basi ni kuteketeza kila kumbukumbu ya huyo aliyekubwaga.Hufanyi hivyo kwa ajili ya hasira bali ni kujipa nafasi ya kuendelea na maisha yako kama yalivyokuwa kabla hujakutana naye.Kumbuka,utakapopata mwenza mwingine hutazihitaji kumbukumbu hizo,sio tu kwa vile tayari una mwingine lakini pia itamsaidia mwenza wako mpya kupata uhakika kuwa wewe ni wake peke yake.

JIREJESHE KWA ULIOWATELEKEZA

Wengi wetu tunafahamu jinsi mapenzi motomoto yanavyoweza kutuweka mbali na watu wetu wengine wa karibu.Si kwamba tukiwa kwenye mapenzi tunawasahau watu hao lakini mara nyingi ni maotkeo ya kuweka akili na nguvu zaidi kwenye mahusiano yetu na wenza wetu,na hivyo kupata fursa finyu ya kuwa karibu na watu wetu wa karibu (kwa mfano wanafamilia wenzetu,ndugu,jamaa na marafiki).

Kufanya kosa si kosa bali kurejea kosa.Na alimradi wakati uko na mwenza wako hukuwafanyia dharau watu wako wa karibu basi ni dhahiri utakaporejea kwao (na pengine kuwafahamisha bayana kuwa umebwagwa) watakuwa radhi kukupokea.Kuwa karibu na watu wako wa karibu kutakusaidia sana kukarabati maisha yako,hasa kwa vile walikuwa nawe hata kabla hujakutana na huyo aliyekubwaga.

Kumbuka,mara nyingi hawa ni watu wanaokupenda kwa dhati- aidha kwa vile ninyi ni damu moja au ni watu uliopitia nao kwenye milima na mabonde.Kwa wanafamailia na ndugu,hawa kiasili ni watu ambao tunapaswa kuwa nao kwa vile tofauti na uchaguzi tunaokuwa nao kudeti mtu fulani au la,sheria za kibinadamu hazitupi fursa ya kuchagua nani tuzaliwe naye au atuzae.Ukaribu na watu wako wa karibu utasaidia kukukumbusha nani mwenye umuhimu wa kweli katika maisha yako.

USIKURUPUKE 

Hapa unaonywa usikurupuke kutaka kuanzisha uhusiano mwingine kuziba pengo la yule aliyekubwaga.Uzoefu unaonyesha kuwa mara nyingi jitihada za haraka haraka kutaka kuziba pengo hilo huishi kwenye maumivu/majonzi zaidi kuliko mafanikio.Tatizo kubwa hapa ni kwamba katika papara ya kutaka kuziba pengo hilo,unaweza kukosa muda wa kumwelewa vyema huyo 'unayemfukuzia.' Mara nyingi jitihada hizo huelemea zaidi kwenye kupata 'demu bomba zaidi ya yule aliyenizingua.' Lakini kama wasemavyo waswahili,usione vyaelea vimeundwa.Huyo 'demu bomba' anaweza kuwa na mwenza wake au ana 'pozi nyiiingi' ambazo sana sana zitaishi kukuumiza tu.

Suluhisho ni 'kutuliza boli.' Vuta pumzi.Angalia sababu zilizopelekea ukabwagwa au mkabwagana na mwenza aliyetangulia.Ukishaelewa chanzo/sababu itakupatia nafasi nzuri ya sio tu kuepuka kurejea makosa ya awali bali pia kujenga uwezekano wa kupata mtu aliye bora zaidi ya aliyetangulia.

JIHAMASISHE

Wengi wetu tunapobwagwa tunakuwa mateka wa hasira.Na katika hasira hizo baadhi yetu hujikuta tukifanya vitu vya kitoto,kijinga na visivyo na maana kabisa.Si ajabu kuona mtu akibwagwa akakimbilia kwenye waal ya Facebook profile ya aliyembwaga na kutundika 'madudu' yenye lengo la aidha kumuumiza mhusika au kujaribu kumshawishi arejee.Unaweza kukidhi mahitaji yako kwa dakika au siku chahe lakini mara nyngi matokeo ya 'upuuzi' wa aina hiyo huwa sio mazuri hasa pale utakapobaini kuwa 'kujigonga' kwako hakujafanikiwa kubadili msimamo wake.

Kumbuka,aliyekubwaga anaweza kuwa anafuatilia kwa karibu namna unavyodili na uamuzi wake.Matarajio ya wengi wanaobwaga wenza wao ni kuwa aliyebwagwa ataumia,atakonda,atateseka au,kwa hakika,ataaanza kubembeleza.Hiyo ni attention seeking.Na hakuna dawa mwafaka kwa attention seekers kama kuwapuuza.Kuendelea na maisha yako kana kwamba hakuna lililotokea sio tu itakuwa kama kumwadhibu attention seeker aliyekubwaga (ie kuvunja matumaini yake kuwa amekuumiza na labda utambembeleza) bali pia utakuwa unajisaidia wewe mwenyewe kuendelea na maisha yako kama kawaida.

Kisasi kikubwa kabisa kwa aliyekubwaga ni kwa wewe kupata mafanikio.Yaani badala ya wewe kuonekana umekondeana kwa mawazo ya kubwagwa,siku ya siku unakutana na aliyekubwaga na kukuona ukiwa mwenye furaha na mafanikio.Na kwa vile 'what goes around always comes around' si ajabu aliyekubwaga kwa wakati ho atakuwa anajutia kwanini alichukua uamuzi huo-lakini hawezi kukubembeleza mrejeane kwa sababu yeye ndiye aliyeamua bila kulazimishwa kuwa mwachane.

Pata picha,baada ya kubwaga unaelekeza nguvu zako kwenye kujiendeleza kimaisha (kitaaluma au kikazi),unatumia muda wako kujenga mwili wako kwa mazoezi, na kwa vile Mungu humjalia kila anayejituma,unafikia mafanikio yanayoweza kugeuza shingo za watu (ya kutamanisha).Mafanikio ni sawa na sumaku,lazima yatakusaidia kuongeza nafasi zako za kupata mwenza bora,pengine bora zaidi ya yule aliyekubwaga.Sasa siki ua siku,mwenyewe umenawiri vyema kutokana na kazi inayolipa vyema,na pembeni una mwenza bora,kisha unakutana na aliyekubwaga awali akiwa kachoka kimaisha na pengine akiwa na mwenza wa ovyo ovyo.Anashindwa kujizuia na kujikuta anakuuliza "hey fulani uko wapi siku hizi...naona mambo si mabaya..."Usiwe na haraka ya kujibu bali jitahidi kadri uwezavyo kuachia kicheko cha dharau....na badala ya kujibu swali lake mkebehi kwa kurejea swali lilelile na pigiria msumari kwa "hata wewe naona mambo si mabaya"...na kicheko kingine..Hiyo inaitwa kushinda vita bila kwenda vitani.

AMKA NA ENDELEA NA SAFARI

Vyovyote utakavyofanya huwezi kumzuia mwenza aliyedhamiria kukubwaga.Pengine amepata mtu aliye bora zaidi yako,pengine ameamua tu.Kama binti anatamani kuwa na mtu mwenye uwezo mkubwa kifedha kuliko wewe,kuendelea kumbembeleza mwendelee kuwa pamoja kutakuingiza kwenye vishawishi vya ufisadi,au matendo mengine mabaya ambayo si ajabu badala ya kukusaidia kumridhisha mwenza wako yakaishia kukupeleka jela.Naamini umeshaona au kuskia stori kibao za watu waliolazimika kujiingiza kwenye uhalifu ili kupata fedha za kuwaridhisha wenza wao.

Of course,mwenza wako ana haki ya kutaka kilicho bora.Lakini hiyo sio sababu ya kutaka uurefushe mkono wako zaidi ya uwezo wake.Mwneza wako ana haki ya kukupa changamoto za koboresha maisha yako/yenu lakini sio kwa namna ya kukusukuma uhatarishe maisha yako kwa ajili yake.Kumbuka,kama maisha yake ni muhimu,yako ni muhimu pia.Kama anakupenda kwa dhati atakubaliana na hali yako alimradi isiwe hali yako ni matokeo ya uvivu au uzembe wako au uoga wako kijituma.

Kwa hiyo badala ya kuendelea kuifanya hali ngumu (kubwagwa) kuwa ngumu zaidi,futa machoz yako,amka na endelea na maisha yako.Katika saikolojia kuna imani kwamba mengi ya tunayoyaita matatizo ni matokeo ya fikra zetu tu.Njaa,kwa mfano,si lazima imaanishe mahitaji ya mwili (tumbo) bali ni fikra kuwa tumbo linahitaji kitu fulani.Tamaa ni hali ya kutamani usichokuwa nacho hata kama si cha muhimu.Badala ya kujipa moyo kuwa mwenza wako atarudi aua atajilaumu kukubwaga,kwanini usielekeze fikra zako kwenye masuala mengine ya muhimu katika maisha yako?Kumbuka wewe ndiye nahodha ya maisha yako,kumkabidhi mtu mwingine jukumu hilo sio tu kunaondoka uhuru wako wa kukufikisha unakotaka kwenda bali pia kuna hatari ya kupotezwa.

Kwa leo inatosha!

MAKALA HII IMEANDALIWA KUTOKANA NA VYANZO MBALIMBALI MTANDAONI HUSUSAN MTANDAO WA AskMen 

MAKALA IJAYO ITAZUNGUMZIA IMANI ILIYOJENGEKA MIONGONI MWA MABINTI/WANAWAKE WENGI WA KITANZANIA KUWA WANAUME WA KITANZANIA NI MAHIRI KWA KU-CHEAT,AU KUNUKUU KIUSAHIHI, "OVYO KABISA", "BURE KABISA", "CHU*I MKONONI", NA KAULI KAMA HIZO.KICHANGAMSHA UBONGO: JE TABIA YA MWANAUME (AU MWANAMKE) INA MAHUSIANO YOYOTE NA URAIA WAKE?

HADI MUDA HUO,NAKUTAKIA SIKU NJEMA


1 comment:

  1. Tuko pamoja,maandika mazuri .wanaume mpo? kaka S.

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.