31 Dec 2011

Kikwete's smile says it all
Vyombo mbalimbali vya habari leo vimebeba picha ya Rais Jakaya Kikwete akiwa na Katibu Mkuu Kiongozi mpya,Balozi Ombeni Sefue na mtangulizi wake Philemon Luhanjo ambaye amestaafu.Sidhani kama kuna Mtanzania asiyefahamu uhusika wa Luhanjo katika sakata la ufisadi uliofanywa na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini,David Jairo.Bunge lilishamshauri Kikwete awawajibishe wahusika wote wa ufisadi huo,ikiwa ni pamoja na Jairo na Luhanjo.

Lakini kama ilivyokuwa katika sakata la ufisadi wa Richmond ambapo Bunge lilishauri wahusika wachukuliwe hatua,lakini tukaishia kuona watu kama aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali Johnstone Mwanyika walistaafu kwa heshima (bila kusahau marupurupu ya kustaafu),Kikwete amerejea tena udhaifu wake kwa kumwogopa Luhanjo na hatimaye kumwokoa kwa kumruhusu astaafu badala ya kumwadhibu kwa ufisadi wake na Jairo.

Kwa vile leo ni siku ya mwisho kwa mwaka huu 2011,picha ya Kikwete na Luhanjo ni kama kuwakumbusha Watanzania jinsi Rais wao alivyo dhaifu na mbabaishaji wa hali ya juu katika kushughulikia ufisadi.Na japo wengi wenu mtajipa matimaini kuwa mwaka 2012 utakuwa wa matumaini,ukweli mchungu ni kwamba kwa mwenendo huu wa Kikwete kuwaogopa na kuwalea mafisadi,viumbe hao hatari watazidi kuzaliana kwani wanajua fika hakuna wa kuwadhibiti au kuwaadhibu.

Samahani Mheshimiwa Rais,lakini uzembe wako katika kuwashughulikia mafisadi ni sawa na tusi kwa taasisi takatifu ya Urais.Ni lini utaamka na kuyatumia madaraka yako ipasavyo kupambana na ufisadi?

Salama zangu za mwaka mpya kwako si za kupendeza kwani namwomba Mungu aharakishe siku ili umalize muhula wako na ubaki historia isiyo na manufaa kwa Watanzania.Can't wait to see you gone!

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.