14 Jun 2017





Kwanza, bila kujali ukada wa CCM au Chadema au kutokuwa kada, ni muhimu kutambua kuwa katika Tanzania yetu ya sasa – na pengine katika nchi nyingi za Dunia ya Tatu – alichofanya Rais John Magufuli kinastahili pongezi.

Ofkoz, alichofanya ni kazi yake, tunamlipa mshahara kama Rais wetu ili atutumikie, na uamuzi wa kuunda tume mbili zakufuatilia kuhusu usafirishaji wa mchanga wa madini ni sehemu ya kazi tuliyomwajiri aifanye.

Hata hivyo, uzoefu watuonyesha kuwa katika Dunia ya Tatu, viongozi kuanzia viranja darasani to wakuu wa nchi, hugeukia kuwa viumbe wa ajabu kabisa, na kusahau kabisa watu waliowawezesha kupata madaraka husika.

Sote tumeshuhudia jinsi watu wanavyotumia ovyo madaraka yao, kuanzia viranja shuleni hadi wenyeviti wa vikao vya harusi, kutoka kwa “ma-admini” kwenye Whatsapp groups hadi kwa wazazi kwenye familia, kutoka wajumbe wa nyumba kumi hadi mabosi wetu makazini. Kwahiyo, katika mazingira tunayoishi, ni kama inatarajiwa kuwa “kiongozi atende kinyume na matarajio ya wananchi waliomwajiri kuwatumikia.”

Kwamba tumezowea kushuhudia vituko vya watawala wetu, wapole na wanyenyekevu wakati wanaomba kura, lakini maharamia pindi wakiingia madarakani.

Wakati mwingine tatizo sio viongozi hao as such bali wapambe, viumbe wanaonufaika kwa uwepo wa fulani madarakani. Mfano wa hivi karibuni kuhus hili ni jinsi kundi la “Mtandao” lililokuwa na mchango mkubwa kumwingiza madarakani Rais wa Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete, na likamfanya kuwa kama “mateka wao” kwa takriban miaka yote 10 ya utawala wake.

Kwahiyo, japo Magufuli amefanya kazi tuliyomwajiri kuifanya, anastahili pongezi kwa vile “ameamua tu” kufanya jambo zuri. Twampongeza kwa kuamua kufanya jambo zuri badala ya kufuata “utamaduni uliozoeleka” wa “bora liende.” Na kubwa zaidi, hata angeamua kutofanya lolote, asingeathiriwa na lolote lile. Kwa kiongozi kuamua kufanya kitu asichotegemewa kufanya, na ambacho hata kama asingekifanya kisingemsababishia matatizo yoyote, basi hatuna budi kumpongeza bila kujali itikadi zetu.

Baada ya pongezi hizo, tuelekee kwenye ripoti husika. Kwa vile ninaamini watu wengi wameshazisoma ripoti hizo, sintorudia kueleza yaliyomo kwenye ripoti hizo. Kama hujazisoma, fanya urafiki na Google, andika “ripoti ya mchanga” utakutana nazo.

Makala hii inaangalia maeneo makuu matatu: tulikotoka, tuliko na tuendako. Katika eneo la kwanza, ninawaomba ndugu zangu wa Chama Cha Mapindui CCM waturuhusu tu tuwalaumu kwa makosa yaliyopelekea Tanzania yetu kujikuta katika hali tuliyonayo.

Rafiki yangu Humphrey Polepole, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM amekuwa akiniambia kuwa “nina chuki binafsi” (sijui chuki binafsi na nani, ikizingatiwa nilikuwa na mchango wangu japo kiduchu katika kampeni za Magufuli katika uchaguzi mkuu uliopita mwaka 2015) kila ninapoishutumu CCM kwa mchango wake katika ufisadi kwenye sekta ya madini.

Simalumu Bwana Polepole kwa sababu ajira yake ni Msema Chochote (MC) wa chama tawala. Tunapolumbana nae kwenye mitandao ya kijamii, mnufaika ni yeye maana analipwa “kusema chochote.” Na kama nilivyoeleza hapo awali, madaraka huwabadili watu kuwa viumbe wa ajabu kabisa. Polepole, mmoja wa watu walionnekana kuwa wenye busara mno wakati wa mchakato wa Katiba mpya, leo anadiriki kutoa kauli zinazotubagua Watanzania tunaoishi Ughaibuni, kama kwamba si Watanzania kamili, kwa vile tu baadhi yetu tunaikosoa CCM.

Enewei, makala hii si kumhusu kada huyo. Hoja yangu ni kwamba katika kuangalia tulikotoka, hatuwezi kukwepa kuzungumzia Ilani za uchaguzi za CCM, miswaada mbalimbali ya sheria iliyoungwa mkono na wabunge wa CCM, upinzani mkali wa CCM kupitia kwa marais wake, mawaziri wake, wabunge wake na makada wake mbalimbali dhidi ya mashujaa kutoka kambi ya upinzani – akina Dkt Slaa, Zitto, Tundu Lissu, Lema, nk – waliopigana kufa na kupona kutetea raslimali zetu, na wakaishia kuadhibiwa na uongozi wa Bunge ambao siku zote umekuwa kama muhuri wa kuidhinisha matakwa ya awamu mbalimbali za serikali za CCM.

Kwa vile kwa kupitia Ripoti mbili za mchanga tumeweza kufahamu ni kwa jinsi gani tumefisadiwa, ili tuweze kusonga mbele na jitihada za kujiondoa kwenye ufisadi, hatuwezi kuepuka “kuwajua wabaya wetu.” Huwezi kutibu maradhi kwa kuepuka kuwafahamu bakteria au virusi waliosababisha madhara husika.

Kwahiyo, japo twafahamu inawauma, ndugu zetu wa CCM “wawe wapole tu” wakati Watanzania wanatoa hasira zao dhidi ya viongozi mbalimbali wa CCM walioshiriki kuwezesha ufisadi kwenye sekta ya madini.

Baada ya kuangalia tulikotoka, tunahamia kwenye tuliko muda huu. Ndio, tushasomewa ripoti mbili zinazoeleza jinsi ambavyo tunaibiwa kwenye sekta ya mdani. Lakini sidhani kama kuna Mtanzania anashangazwa na kilichomo kwenye ripoti hizo. Kama mikataba ya madini inafanyiwa usiri kuliko tendo la ndoa, basi ni wazi kuna masuala flani ambayo wananchi wa kawaida hawapaswi kuyajua. Na hawapaswi kuyajua kwa vile yanawapora raslimali zao.

Halafu hapa pia, CCM haiwezi kukwepa lawama kwa sababu kwa kiasi kikubwa – pamoja na mzuri mengi ya chama hicho tawala – kimekuwa kichaka cha ufisadi. Sio siri kwamba Watanzania wengi wanaiangalia CCM kwa jicho la mashaka linapokuja suala la kulinda raslimali za nchi yetu. Rekodi ya chama hicho kwenye ufisadi inatosha kabisa kukipatia OSCAR ya ufisadi: EPA, Kagoda,Richmond, Kiwira, Buzwagi, Escrow…orodha ni ndefu mno.

Lakini sote twajua lawama pekee hazijengi. Sawa, CCM haiwezi kukwepa lawama  kwa kutufikisha hapa, lakini hatuwezi kuendelea kulaumu milele bila kufanya jitihada za kusonga mbele. Na hata tukitaka kuendelea kulaumu, ni muhimu kukumbuka kuwa sio tu Magufuli aliyechukua hatua hizi ni mwana-CCM pia lakini vilevile angetaka kuendeleza kasumba ya CCM, angeweza kabisa kupuuzia suala hilo.

Kwa sasa, tunafahamu kiasi gani tumeibiwa. Hatua za kuchukua ni pamoja na
  • -      Makampuni ya madini ‘kukaliwa kooni’ yarejeshe tunachowaidai.
  • -      Watanzani wenzetu walioshiriki katika ufisadi huo wachukuliwe hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kutaifisha mali zao ili waturejeshee haki yetu
  • -      Tutengeneze mazingira ya kuepusha kujikuta tena katika hali kama hii huko mbeleni. Moja ya solutions ni Katiba Mpya (japo kwa bahati mbaya au makusudi, Rais Magufuli ameonyesha kuwa hiki sio kipaumbele chake)
  • -      Yanapokuja masuala la muhimu kwa nchi yetu, tusiangaliane kwa lesni ya “huyu wa CCM” AU “huyu mpinzani.” Ni wazi kuwa laiti tungesikiliza vilio vya akina Dkt Slaa, Zitto, Lissu, nk basi tusingefika hapa. Tofauti za kiitikadi sio uadui. Na hili pia ni fundisho kwa Bwana Polepole: akina Chahali kuwepo nje ya nchi hakumaanishi wanachopigia kelele kuhusu nchi yao ni “chuki binafsi.”
  • -      Pengine huu ni wakati mwafaka kuangalia uwezekano wa reforms kwa Idara yetu ya Usalama wa Taifa kwani ufisadi wote uliojiri katika sekta ya madini ulifanyika wakati ndugu zangu hao wakiwa ‘macho’ kazini.


Mapendekezo ni mengi lakini angalau kwa sasa tunaweza kuanza na hayo.

Lakini pengine kubwa zaidi ni kwamba kwa wakati huu tunapaswa kuwa kitu kimoja. Ni muhimu tukubaliane kwamba tunapokumbana na mwizi, kila mtu ata-react kwa namna yake. Kuna uwezekano mkubwa kwa wale waliowahi kutuambia “huyu mwizi” tukawapuuza, wakatunyooshe vidole na kutukumbusha “tuliwaambia.” Haina haja ya kuwachukua, Wanatukumbusha na kutuambia ukweli. Kama kina Lissu walinyanyaswa na kubughudhiwa kwa hayahaya tunayoyashangaa leo, kuna dhambi gani kwa wao kutukumbusha kuwa walishatutahadharisha huko nyuma?

Pamoja na pongezi kwa Magufuli kwa kuchukua hatua ya kuanzisha tume ya kuchunguza kuhusu mchanga wa madini, ninamlaumu kwa lugha yake ambayo haiwezi kutusaidia katika kipindi hiki tunachohitaji ushairikiano bila kujali itikadi zetu. Maagizo yake kwa Spika Ndugai (mtu ambaye hapaswi kuongea lolote kuhusu wizi wa madini yetu kwa sababu ‘kila Bunge la CCM’ limekuwa wawezeshaji wa wizi huo) yanajenga mfarakano tu badala ya umoja tunaohitaji kipindi hiki.

Sijui kwanini Rais Magufuli anapenda sana kutengenezea ‘bifu’ zisizo na umuhimu. Hivi akitoa wito kuwa Watanzania wote tushirikiane, na kuwakaribisha wapinzani katika mapambano haya, atapungukiwa nini? Mbona ‘kiongozi mkuu wa upinzani’ Edward Lowassa, kammwagia pongezi Magufuli kwa hatua alizochukua kuhusu suala hilo la madini? Ni muhimu kwa Rais wetu kukumbushwa kuwa siasa za uhasama sio tu hazina fursa katika Tanzania yetu bali pia hazina faida.

Kuhusu jinsi ya kuwashughulikia watu waliohusika katika ufisadi kwenye sekta ya madini, tuna njia mbili tu: aidha, kufumba macho na kumsomba kila aliyehusika, na hii itajumuisha marais wastaafu, au, tuendeshe mambo Kiswahili, tuchukue hatua kwa wale tu ‘wasio na madhara makubwa,’ na kuwastiri ‘watuhumiwa muhimu’ kama vile marais wastaafu.

Tatizo la hiyo approach ya pili ni kwamba hao ‘wasio na mdhara makubwa’ watajitetea kirahisi tu kuwa maamuzi yao yalitokana na ridhaaza ‘watuhumiwa muhimu.’

Je inawezekana suala hili ambalo linanapaswa kushughulikiwa na mkono mrefu wa sheria likafanywa bila kuingiza siasa? Yes, inawezekana lakini sio rahisi kwa Tanzania yetu hii. Ila ni mapema mno kutoa hukumu. Acha muda uongee.

Tunakolekea? Well, Sie kama Watanzania tunapaswa kuacha kuwa ‘wapole’ kupita kiasi. Muda huu tulipaswa kuandamana kulaani waliotuibia, lakini kama kutakuwa na maandamano basi ni ya kisiasa ya kumpongeza Magufuli kutueleza kile ambacho tunakifahamu muda mrefu tu. Ni lini Watanzania wataamka na kudai – kwa amani – haki zao za msingi? Hivi ni lini Watanzania watashinikiza viongozi wetu waweke mbele maslahi ya nchi yetu badala ya maslahi yao binafsi?

Na kufumbukiwa macho suala la mikataba ya madini kuwe mwanzo wa safari ndefu ya “kudai chetu.” Tunataka mikataba ya  gesi na mafuta sio tu iwekwe wazi bali itafsiriwe kwa Kiswahili ili kila Mtanzania aisome.

Tunataka pia mikataba ya ununzi wa Bombadier nayo iwekwe wazi, ili huko mbeleni tusijikute tukilazimika kuunda tume nyingine.

Tunataka mikataba ya utalii, iwekwe hadharani. Tujue nani anatorosha wanyamapori wetu, nani baada ya kupewa Ukatibu Mkuu ghafla biashara ya ujangili nayo ikaanza kupaa, tuambiwe watu waliondoka na magunia ya fedha kwenye utapeli wa Escrow ni akina nani (sio wale tulitajiwa kuhusu ‘benki ya waswahili’ bali Stanbic), tunataka kila kilichofichwa kiwekwe wazi.

Lakini ili hayo yote yawezekana, ni muhimu sote wenye uchungu wa nchi yetu tuwe kitu kimoja. Na nitumie fursa hii kumwomba tena Rais Magufuli ajaribu ku-embrace consensual politics (siasa za kufikia mwafaka) badala ya hizi za mifarakano (conflictual politics). Afterall, Haijalishi mtu ni CCM, Chadema, CUF au hana chama, sote ni Watanzania.


Uchambuzi huu ni endelevu. Kwa leo naomba kuishia hapa. Swaumu njema kwa ndugu zangu Waislamu. Asanteni

1 comment:

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.