Showing posts with label #RipotiYaMchanga. Show all posts
Showing posts with label #RipotiYaMchanga. Show all posts

14 Jun 2017





Kwanza, bila kujali ukada wa CCM au Chadema au kutokuwa kada, ni muhimu kutambua kuwa katika Tanzania yetu ya sasa – na pengine katika nchi nyingi za Dunia ya Tatu – alichofanya Rais John Magufuli kinastahili pongezi.

Ofkoz, alichofanya ni kazi yake, tunamlipa mshahara kama Rais wetu ili atutumikie, na uamuzi wa kuunda tume mbili zakufuatilia kuhusu usafirishaji wa mchanga wa madini ni sehemu ya kazi tuliyomwajiri aifanye.

Hata hivyo, uzoefu watuonyesha kuwa katika Dunia ya Tatu, viongozi kuanzia viranja darasani to wakuu wa nchi, hugeukia kuwa viumbe wa ajabu kabisa, na kusahau kabisa watu waliowawezesha kupata madaraka husika.

Sote tumeshuhudia jinsi watu wanavyotumia ovyo madaraka yao, kuanzia viranja shuleni hadi wenyeviti wa vikao vya harusi, kutoka kwa “ma-admini” kwenye Whatsapp groups hadi kwa wazazi kwenye familia, kutoka wajumbe wa nyumba kumi hadi mabosi wetu makazini. Kwahiyo, katika mazingira tunayoishi, ni kama inatarajiwa kuwa “kiongozi atende kinyume na matarajio ya wananchi waliomwajiri kuwatumikia.”

Kwamba tumezowea kushuhudia vituko vya watawala wetu, wapole na wanyenyekevu wakati wanaomba kura, lakini maharamia pindi wakiingia madarakani.

Wakati mwingine tatizo sio viongozi hao as such bali wapambe, viumbe wanaonufaika kwa uwepo wa fulani madarakani. Mfano wa hivi karibuni kuhus hili ni jinsi kundi la “Mtandao” lililokuwa na mchango mkubwa kumwingiza madarakani Rais wa Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete, na likamfanya kuwa kama “mateka wao” kwa takriban miaka yote 10 ya utawala wake.

Kwahiyo, japo Magufuli amefanya kazi tuliyomwajiri kuifanya, anastahili pongezi kwa vile “ameamua tu” kufanya jambo zuri. Twampongeza kwa kuamua kufanya jambo zuri badala ya kufuata “utamaduni uliozoeleka” wa “bora liende.” Na kubwa zaidi, hata angeamua kutofanya lolote, asingeathiriwa na lolote lile. Kwa kiongozi kuamua kufanya kitu asichotegemewa kufanya, na ambacho hata kama asingekifanya kisingemsababishia matatizo yoyote, basi hatuna budi kumpongeza bila kujali itikadi zetu.

Baada ya pongezi hizo, tuelekee kwenye ripoti husika. Kwa vile ninaamini watu wengi wameshazisoma ripoti hizo, sintorudia kueleza yaliyomo kwenye ripoti hizo. Kama hujazisoma, fanya urafiki na Google, andika “ripoti ya mchanga” utakutana nazo.

Makala hii inaangalia maeneo makuu matatu: tulikotoka, tuliko na tuendako. Katika eneo la kwanza, ninawaomba ndugu zangu wa Chama Cha Mapindui CCM waturuhusu tu tuwalaumu kwa makosa yaliyopelekea Tanzania yetu kujikuta katika hali tuliyonayo.

Rafiki yangu Humphrey Polepole, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM amekuwa akiniambia kuwa “nina chuki binafsi” (sijui chuki binafsi na nani, ikizingatiwa nilikuwa na mchango wangu japo kiduchu katika kampeni za Magufuli katika uchaguzi mkuu uliopita mwaka 2015) kila ninapoishutumu CCM kwa mchango wake katika ufisadi kwenye sekta ya madini.

Simalumu Bwana Polepole kwa sababu ajira yake ni Msema Chochote (MC) wa chama tawala. Tunapolumbana nae kwenye mitandao ya kijamii, mnufaika ni yeye maana analipwa “kusema chochote.” Na kama nilivyoeleza hapo awali, madaraka huwabadili watu kuwa viumbe wa ajabu kabisa. Polepole, mmoja wa watu walionnekana kuwa wenye busara mno wakati wa mchakato wa Katiba mpya, leo anadiriki kutoa kauli zinazotubagua Watanzania tunaoishi Ughaibuni, kama kwamba si Watanzania kamili, kwa vile tu baadhi yetu tunaikosoa CCM.

Enewei, makala hii si kumhusu kada huyo. Hoja yangu ni kwamba katika kuangalia tulikotoka, hatuwezi kukwepa kuzungumzia Ilani za uchaguzi za CCM, miswaada mbalimbali ya sheria iliyoungwa mkono na wabunge wa CCM, upinzani mkali wa CCM kupitia kwa marais wake, mawaziri wake, wabunge wake na makada wake mbalimbali dhidi ya mashujaa kutoka kambi ya upinzani – akina Dkt Slaa, Zitto, Tundu Lissu, Lema, nk – waliopigana kufa na kupona kutetea raslimali zetu, na wakaishia kuadhibiwa na uongozi wa Bunge ambao siku zote umekuwa kama muhuri wa kuidhinisha matakwa ya awamu mbalimbali za serikali za CCM.

Kwa vile kwa kupitia Ripoti mbili za mchanga tumeweza kufahamu ni kwa jinsi gani tumefisadiwa, ili tuweze kusonga mbele na jitihada za kujiondoa kwenye ufisadi, hatuwezi kuepuka “kuwajua wabaya wetu.” Huwezi kutibu maradhi kwa kuepuka kuwafahamu bakteria au virusi waliosababisha madhara husika.

Kwahiyo, japo twafahamu inawauma, ndugu zetu wa CCM “wawe wapole tu” wakati Watanzania wanatoa hasira zao dhidi ya viongozi mbalimbali wa CCM walioshiriki kuwezesha ufisadi kwenye sekta ya madini.

Baada ya kuangalia tulikotoka, tunahamia kwenye tuliko muda huu. Ndio, tushasomewa ripoti mbili zinazoeleza jinsi ambavyo tunaibiwa kwenye sekta ya mdani. Lakini sidhani kama kuna Mtanzania anashangazwa na kilichomo kwenye ripoti hizo. Kama mikataba ya madini inafanyiwa usiri kuliko tendo la ndoa, basi ni wazi kuna masuala flani ambayo wananchi wa kawaida hawapaswi kuyajua. Na hawapaswi kuyajua kwa vile yanawapora raslimali zao.

Halafu hapa pia, CCM haiwezi kukwepa lawama kwa sababu kwa kiasi kikubwa – pamoja na mzuri mengi ya chama hicho tawala – kimekuwa kichaka cha ufisadi. Sio siri kwamba Watanzania wengi wanaiangalia CCM kwa jicho la mashaka linapokuja suala la kulinda raslimali za nchi yetu. Rekodi ya chama hicho kwenye ufisadi inatosha kabisa kukipatia OSCAR ya ufisadi: EPA, Kagoda,Richmond, Kiwira, Buzwagi, Escrow…orodha ni ndefu mno.

Lakini sote twajua lawama pekee hazijengi. Sawa, CCM haiwezi kukwepa lawama  kwa kutufikisha hapa, lakini hatuwezi kuendelea kulaumu milele bila kufanya jitihada za kusonga mbele. Na hata tukitaka kuendelea kulaumu, ni muhimu kukumbuka kuwa sio tu Magufuli aliyechukua hatua hizi ni mwana-CCM pia lakini vilevile angetaka kuendeleza kasumba ya CCM, angeweza kabisa kupuuzia suala hilo.

Kwa sasa, tunafahamu kiasi gani tumeibiwa. Hatua za kuchukua ni pamoja na
  • -      Makampuni ya madini ‘kukaliwa kooni’ yarejeshe tunachowaidai.
  • -      Watanzani wenzetu walioshiriki katika ufisadi huo wachukuliwe hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kutaifisha mali zao ili waturejeshee haki yetu
  • -      Tutengeneze mazingira ya kuepusha kujikuta tena katika hali kama hii huko mbeleni. Moja ya solutions ni Katiba Mpya (japo kwa bahati mbaya au makusudi, Rais Magufuli ameonyesha kuwa hiki sio kipaumbele chake)
  • -      Yanapokuja masuala la muhimu kwa nchi yetu, tusiangaliane kwa lesni ya “huyu wa CCM” AU “huyu mpinzani.” Ni wazi kuwa laiti tungesikiliza vilio vya akina Dkt Slaa, Zitto, Lissu, nk basi tusingefika hapa. Tofauti za kiitikadi sio uadui. Na hili pia ni fundisho kwa Bwana Polepole: akina Chahali kuwepo nje ya nchi hakumaanishi wanachopigia kelele kuhusu nchi yao ni “chuki binafsi.”
  • -      Pengine huu ni wakati mwafaka kuangalia uwezekano wa reforms kwa Idara yetu ya Usalama wa Taifa kwani ufisadi wote uliojiri katika sekta ya madini ulifanyika wakati ndugu zangu hao wakiwa ‘macho’ kazini.


Mapendekezo ni mengi lakini angalau kwa sasa tunaweza kuanza na hayo.

Lakini pengine kubwa zaidi ni kwamba kwa wakati huu tunapaswa kuwa kitu kimoja. Ni muhimu tukubaliane kwamba tunapokumbana na mwizi, kila mtu ata-react kwa namna yake. Kuna uwezekano mkubwa kwa wale waliowahi kutuambia “huyu mwizi” tukawapuuza, wakatunyooshe vidole na kutukumbusha “tuliwaambia.” Haina haja ya kuwachukua, Wanatukumbusha na kutuambia ukweli. Kama kina Lissu walinyanyaswa na kubughudhiwa kwa hayahaya tunayoyashangaa leo, kuna dhambi gani kwa wao kutukumbusha kuwa walishatutahadharisha huko nyuma?

Pamoja na pongezi kwa Magufuli kwa kuchukua hatua ya kuanzisha tume ya kuchunguza kuhusu mchanga wa madini, ninamlaumu kwa lugha yake ambayo haiwezi kutusaidia katika kipindi hiki tunachohitaji ushairikiano bila kujali itikadi zetu. Maagizo yake kwa Spika Ndugai (mtu ambaye hapaswi kuongea lolote kuhusu wizi wa madini yetu kwa sababu ‘kila Bunge la CCM’ limekuwa wawezeshaji wa wizi huo) yanajenga mfarakano tu badala ya umoja tunaohitaji kipindi hiki.

Sijui kwanini Rais Magufuli anapenda sana kutengenezea ‘bifu’ zisizo na umuhimu. Hivi akitoa wito kuwa Watanzania wote tushirikiane, na kuwakaribisha wapinzani katika mapambano haya, atapungukiwa nini? Mbona ‘kiongozi mkuu wa upinzani’ Edward Lowassa, kammwagia pongezi Magufuli kwa hatua alizochukua kuhusu suala hilo la madini? Ni muhimu kwa Rais wetu kukumbushwa kuwa siasa za uhasama sio tu hazina fursa katika Tanzania yetu bali pia hazina faida.

Kuhusu jinsi ya kuwashughulikia watu waliohusika katika ufisadi kwenye sekta ya madini, tuna njia mbili tu: aidha, kufumba macho na kumsomba kila aliyehusika, na hii itajumuisha marais wastaafu, au, tuendeshe mambo Kiswahili, tuchukue hatua kwa wale tu ‘wasio na madhara makubwa,’ na kuwastiri ‘watuhumiwa muhimu’ kama vile marais wastaafu.

Tatizo la hiyo approach ya pili ni kwamba hao ‘wasio na mdhara makubwa’ watajitetea kirahisi tu kuwa maamuzi yao yalitokana na ridhaaza ‘watuhumiwa muhimu.’

Je inawezekana suala hili ambalo linanapaswa kushughulikiwa na mkono mrefu wa sheria likafanywa bila kuingiza siasa? Yes, inawezekana lakini sio rahisi kwa Tanzania yetu hii. Ila ni mapema mno kutoa hukumu. Acha muda uongee.

Tunakolekea? Well, Sie kama Watanzania tunapaswa kuacha kuwa ‘wapole’ kupita kiasi. Muda huu tulipaswa kuandamana kulaani waliotuibia, lakini kama kutakuwa na maandamano basi ni ya kisiasa ya kumpongeza Magufuli kutueleza kile ambacho tunakifahamu muda mrefu tu. Ni lini Watanzania wataamka na kudai – kwa amani – haki zao za msingi? Hivi ni lini Watanzania watashinikiza viongozi wetu waweke mbele maslahi ya nchi yetu badala ya maslahi yao binafsi?

Na kufumbukiwa macho suala la mikataba ya madini kuwe mwanzo wa safari ndefu ya “kudai chetu.” Tunataka mikataba ya  gesi na mafuta sio tu iwekwe wazi bali itafsiriwe kwa Kiswahili ili kila Mtanzania aisome.

Tunataka pia mikataba ya ununzi wa Bombadier nayo iwekwe wazi, ili huko mbeleni tusijikute tukilazimika kuunda tume nyingine.

Tunataka mikataba ya utalii, iwekwe hadharani. Tujue nani anatorosha wanyamapori wetu, nani baada ya kupewa Ukatibu Mkuu ghafla biashara ya ujangili nayo ikaanza kupaa, tuambiwe watu waliondoka na magunia ya fedha kwenye utapeli wa Escrow ni akina nani (sio wale tulitajiwa kuhusu ‘benki ya waswahili’ bali Stanbic), tunataka kila kilichofichwa kiwekwe wazi.

Lakini ili hayo yote yawezekana, ni muhimu sote wenye uchungu wa nchi yetu tuwe kitu kimoja. Na nitumie fursa hii kumwomba tena Rais Magufuli ajaribu ku-embrace consensual politics (siasa za kufikia mwafaka) badala ya hizi za mifarakano (conflictual politics). Afterall, Haijalishi mtu ni CCM, Chadema, CUF au hana chama, sote ni Watanzania.


Uchambuzi huu ni endelevu. Kwa leo naomba kuishia hapa. Swaumu njema kwa ndugu zangu Waislamu. Asanteni

26 May 2017



Juzi tumesikia ripoti kuhusu mchanga wenye madini unaosafirishwa nje ya Tanzania yetu (well, kuna jina la kitaalamu lakini sio la muhimu kulinganisha na athari kubwa za usafirishwaji wa mchanga huo).

Kwa baadhi ya wenzetu, taarifa hiyo imewashtua mno, na kuwapandisha hasira kubwa. Ndio Tanzania yetu hiyo, wengi wa raia wake hawana habari kuhusu yanayoisibu nchi yetu. Ukiwauliza watu, "hivi mustakabali wa Tanzania mwakani utakuwaje?" nina hakika watu kadhaa watajiumauma kutoa jibu la kueleweka.

Watanzania wengi aidha hawaelewi au wamesahau nchi yetu ilivyochukua mwelekeo mpya - na usiopendeza - baada ya kung'atuka kwa Baba wa Taifa, marehemu Mwalimu Julius Nyerere. Hatua ya kwanza kabisa ya kubadili mwelekeo ilikuwa kitu kinachofahamika kama Azimio la Zanzibar. Hili lilifanyika katika utawala wa Mzee Ruksa, Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi.

Kimsingi, Azimio la Zanzibar liliua Azimio la Arusha na kulizika mubashara. Ukitafuta nyaraka kuhusu Azimio hilo la Zanzibar hutozipata kirahisi kwa sababu lilifanyika katika mkusanyiko uliokuwa kama "mkutano haramu."

Mzee wetu Mwinyi hakuitwa Mzee Ruksa kama utani. Utawala wake ulitawaliwa na kile Waingereza wanaita 'laissez faire', labda kwa Kiswahili chepesi tuseme 'bora liende' au 'liwalo na liwe.' 

Lakini kumtendea haki 'Mzee Ruksa,' asili hasa ya ufisadi haikuanza katika utawala wake bali ilianza katika utawala uliomtangulia, wa Baba wa Taifa. 

Tofauti kati ya tawala hizo mbili ilikuwa bayana: Wakati baadhi ya waliomzunguka Baba wa Taifa walikuwa 'mafisadi wa chinichini' au 'waliokuwa wakisubiri atokea madarakani ili waanze kutafuna keki ya taifa,' katika utawala wa Rais Mwinyi, ilikuwa ni mwanzo wa 'kula kadri unavyoweza,' Waingereza wanaita 'open season.'

Kwamba labda Baba wa Taifa alifahamu watu hao au walikuwa mahiri kuficha tabia zao, sina jibu la hakika. Lakini huhitaji kuwa mchambuzi mahiri wa siasa kubaini kwamba mara baada ya Nyerere kung'atuka na hatimaye kufariki, ghafla watu walewale waliokuwa wakiimba kuhusu Ujamaa na kulaani Ubepari wakageuka matajiri wa kupindukia, mabepari. Ninachofahamu ni kwamba kulikuwa na idadi kubwa tu ya wanasiasa waliomhadaa Baba wa Taifa kuwa ni waumini wa Ujamaa lakini walimudu kuhifadhi fedha huku nje wakisubiri 'Nyerere aondoke.' 

Kwahiyo, Awamu ya Pili ya Mzee Ruksa ni kama iliyotoa ruksa kwa walafi waliokuwa wakimendea keki ya taifa, lakini walishindwa kuitafuna wakati wa utawala wa Nyerere. Kwa kifupi, utawala wa Mzee Ruksa ulitoa rasmi ruksa kulifisadi taifa letu, hasa kupitia Azimio la Zanzibar. 

Ni muhimu kukumbuka Utawala wa Mzee Ruksa ulikuwa wa Chama Cha Mapenduzi, CCM.

Kuingia kwa Rais Benjamin Mkapa mwaka 1995 kuliingiza zama mpya kuhusiana na ufisadi. Miaka 10 ya Mzee wa Uwazi na Ukweli ilitawaliwa na Watanzania kuhadaiwa kuwa ufumbuzi wa matatizo yao upo mikononi mwa wawekezaji, ilhali wengi wa hao walioitwa wawekezaji walikuwa in fact majambazi waliokuwa wakiwinda raslimali zetu. 

Miaka 10 ya Mkapa ilileta matumaini ya kitakwimu, tukiambiwa kuwa sijui GDP, sijui Pato la Taifa, sijui vipimo gnai vya kiuchumi, kuwa vyote vilionyesha uchumi wa Tanzania ukifanya vizuri. Kama kuna kitu kinanichukiza mno kuhusu hizi takwimu za uchumi ni kuwaangalia watu kama bidhaa au namba na sio binadamu. Haiingii akilini kusema uchumi unakua ilhali watu wanazidi kuwa masikini. Uchumi unakua kimazingaombwe?

Tofauti kati ya utawala wa Mwinyi na Mkapa ni ya wazi: nimeshaeleza kuwa katika zama za Mwinyi ilikuwa 'ruksa' kufanya lolote lile. Zama za Mkapa zilituaminisha kuwa kila kitu kinafanyika kwa uwazi na ukweli, na kwenye uwazi na ukweli hakupaswi kuwa na ufisadi. 

Yaliyojiri katika utawala wa Mwinyi yalikuwa yakionekana mubashara. Hiki kilikuwa kipindi cha mtu tu kuamua kuwa tajiri kwa njia halali au zisizo halali, maana ilikuwa ruksa. Lakini katika zama za 'uwazi na ukweli,' watu pekee walioonekana kuwa na ruksa ya kufanya wapendayo ni wawekezaji.Mkapa aliwathamini wawekezaji kuliko Watanzania wenzake.

Lakini ni baada ya Mkapa kutoka madarakani ndio tukafahamu kilichokuwa kikijiri 'behind the scene.' Kumbe wakati anatuhubiria kuhusu uwazi na ukweli, yeye akaigeuza Ikulu kuwa soko la Kariakoo, akawa anafanya biashara. 

Na Mkapa, mwanafunzi mtiifu wa Mwalimu Nyerere, ni mfano sahihi wa watu ambao Nyerere aliwaamini sana lakini alipoondoka nao wakapuuza misingi aliyoijenga Mwalimu. 

Zama za Mkapa ndio haswa zilizowavutia wawekezaji kujazana nchini mwetu. Wengi wao walikuja na brifukesi tupu, wakaondoka na mamilioni ya dola. Baadhi ya wawekezaji hao, walipoona bado wanahitaji kuchuma wasichopanda, walibadili majina na kuongezewa likizo ya kulipa kodi.

Ni muhimu kukumbuka kuwa Mkapa alikuwa Rais kwa tiketi ya CCM.

Baada ya Mkapa akaingia Kikwete. Ili kuorodhesha madudu yote yaliyofanywa katika utawala wa Kikwete inahitaji kitabu kizima. Wakati mwingine unaweza kupatwa na kizunguzungu kuona sasa Watanzania wengi wanamlilia JK, mwanasiasa ambaye hakuwa makini kabisa kuhusu mustakabali wa Tanzania yetu.

Ni hivi, kuna mengi hayawekwi wazi kuhusu yaliyojiri kati ya 2005 na 2015, na siku yakiwekwa hadharani itakuwa balaa. Bwana Magufuli aliposema 'tusifukue makaburi' alitumia busara tu ili kuepusha aibu ambayo kimsingi isingekuwa kuhusu utawala wa JK tu bali mwendelezo wa CCM kuwa janga kwa taifa letu.

Kutoka EPA hadi Kagoda hadi Richmond hadi Escrow, utawala wa JK ulitawaliwa na skandali mfululizo. Pengine JK hakuwa mwanasiasa mwenye mapungufu lakini kosa lake kubwa lilikuwa maandalizi yake kuwania urais from 1995 to 2005, ambapo alikusanya sapoti ya kila kundi, ikiwa ni pamoja na mafisadi. lipopata urais, JK alikuwa na deni kubwa kwa watu hawa, na hii ilipeleka awaruhusu kutafuna keki ya taifa kama asante yake kwao.

Sihitaji kukumbusha kuwa JK alikuwa Rais kwa tiketi ya CCM.

Magufuli pia ni Rais kwa tiketi ya CCM, lakini wakati tunapongeza jitihada zake binafsi ni muhimu kutambua kuwa chama chake kina mchango mkubwa katika matatizo mengi yanayotukabili leo, ikiwa ni pamoja na hilo la utoroshaji wa mchanga wa dhahabu.

Lakini Magufuli hawezi kukwepa lawama kwa uamuzi wake kumteua Profesa Sospeter Muhongo kuwa Waziri wa Nishati na Madini, nafasi aliyolazimika kujiuzulu katika utawala wa JK kutokana na kashfa ya Escrow. Hivi Magufuli alikuwa anategemea miujiza kutoka kwa Prof Muhongo? 

Kwa waliosoma kitabu changu cha 'Dokta John Magufuli: Sa fari ya Urais, Mafanikio na Changamoto Katika Urais Wake' watakumbuka nilichoandika ukurasa wa 74 kuhusu uamuzi wa Magufuli kumteua Profesa Muhongo. 



Niliandika


Hata hivyo, mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni. Angalau Magufuli amejitahidi kufanya jitihada binafsi kukabiliana na majambazi wanaobaka uchumi wetu. Ile tu kuchukua hatua inapaswa kupongezwa hasa ikizingatiwa kuwa watangulizi wake watatu -Mwinyi,Mkapa na JK - waliishia kutupatia matumaini hewa huku ufisadi ukizidi kushamiri.

Jana nilimwangalia Katibu Mwenezi wa CCM Humphrey Poplepole akitoa maneno mazito kuhusiana na suala la mchanga wa dhahabu. Nikaandika tweet kwamba Bwana Polepole anaongea kana kwamba CCM haihusiki na kuwezesha ujambazi uliopelekea mchanga wa madini kusafirisha. Akaleta uzushi kuwa sijui mie nipo ughaibuni, sijui sina uhalali. Baadhi ya watu wakamshutumu kuwa ni mbaguzi (kuwa ughaibuni  hakuninyimi uhuru wa kuzungumzia mustakabali wa taifa letu) lakini mie siamini kabisa kuwa huyu Polepole ni mbaguzi. Ni siasa tu.

Mwisho, makala hii haitokamilika ipasavyo bila kuwatupia neno ndugu zangu wa kitengo. Hebu fanyeni kuona aibu japo kidogo. Hivi inawezekanaje taifa kuibiwa zaidi ya shilingi trilioni moja ilhali ninyi mkifaidi mishahara minono na posho nzuri inayotakana na jasho la Watanzania masikini lakini mnawaangusha kiasi hicho? Tatizo la kitengo ni vipaumbele fyongo, kuandama watu wasiohusika badala ya kukwekeza nguvu dhidi ya wahalifu halisi/matishi halisi kwa usalama wa taifa letu.

Hata hivyo, kwa vile lawama hazijengi, ni matumaini yangu makubwa kuwa suala hilo la mchanga wa dhahabu litatufungua mcho kama taifa na kukabiliana na ujambazi wa aina hii. Sina uhakika sana kuhusu mbinu mwafaka, lakini pengine kwa kuanzia, CCM hata kama inaona aibu kuwaomba radhi Watanzania kwa kuwa kichaka cha ufisadi, hali iliyowezesha ujambazi wa mchanga huo wenye madini, basi angalau imuunge mkono mwenyekiti wao, si kwa porojo za kina Polepole bali kwa vitendo halisi. Wingi wa wabunge wa chama hicho tawala uwe na faida kwa wananchi na taifa na sio mhuri wa kupitisha kila kitu kama ilivyokuwa kwa miswada iliyopeleka sheria za madini zinazowapa fursa wawekezaji wasio waaminifu kutorosha kila wanachotaka ilhali sie tukizidi kuwa masikini.

Mungu ibariki Tanzania

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.