Showing posts with label AFRIKA. Show all posts
Showing posts with label AFRIKA. Show all posts

20 Feb 2008

Makala yangu katika toleo la wiki hii la gazeti la Raia Mwema inazungumzia UHURU.Inaanza kwa kuhabarisha kuhusu tangazo la Uhuru wa Kosovo,kisha inachambua "urafiki mpya" wa Marekani na China kwa Bara la Afrika na kuhitimisha kwamba urafiki huo ni mithili ya Mkutano wa Berlin 1884-5 ulioligawa bara la Afrika miongoni mwa wakoloni.Makala hii inakumbushia pia kwamba kuna uwezekano ziara ya Bush barani Afrika ikabaki kumbukumbu muhimu kwake kutokana na namna alivyonyenyekewa katika kipindi ambacho ni mmoja ya marais wanaochukiwa sana katika sehemu mbalimbali duniani,na very unpopular nyumbani kwake US of A.Kadhalika makala inawashikia bango Mwanyika na Hosea kwamba wajiuzulu haraka sana,sambamba na wale wote waliotajwa kwenye ripoti ya Tume ya Mwakyembe.Pamoja na makala nyingine zilizokwenda shule ya hali ya juu,bingirika na makala hiyo kwa KUBONYEZA HAPA.

24 Jan 2008

Siku chache zilizopita Wamarekani waliadhimisha siku ya Dakta Martin Luther King Jr,mmoja wa wapigania haki za Waamerika Weusi.Historia inamkumbuka Dkt King (aliyezaliwa mwaka 1929 na kuuawa kwa risasi mwaka 1968)kama nguzo muhimu katika kupigania haki za Waamerika Weusi nchini humo.Pengine kilichomfanya wanaharakati huyo akubalike zaidi ni imani yake ya kudai haki kwa njia za amani.

Miaka mitano kabla ya kuuawa,mwaka 1963,Dkt King alitoa hotuba ambayo hadi leo imeendelea kuwa na mvuto mkubwa sio nchini Marekani pekee bali pia sehemu mbalimbali duniani katika mapambano ya kudai usawa.Katika hotuba hiyo iliyopewa jina “I Have a Dream” (“Nina Ndoto”,kwa tafsiri isiyo rasmi),Dkt King alieleza matamanio yake kuona Waamerika Weusi na Weupe wakiishi pamoja kwa amani na usawa.Hotuba hiyo iliyotolewa mbele ya watu zaidi ya laki mbili,inakubalika miongoni mwa wengi kama moja ya hotuba za muhimu kabisa katika historia ya Marekani.Mwaka 1999,hotuba hiyo ilichaguliwa na wasomi kuwa ni hotuba bora kabisa za karne ya 20.

Miongoni mwa nukuu muhimu katika hotuba hiyo ni pamoja na (kwa tafsiri yangu isiyo rasmi) “…nina ndoto kwamba siku moja taifa hili litasimama na kuishi kama inavyotamkwa kwenye imani yake….nina ndoto kwamba siku moja watoto wangu wanne wataishi katika taifa ambalo hawatahukumiwa kutokana na rangi ya ngozi zao bali tabia/utu wao….nina ndoto kwamba siku moja watoto wa waliokuwa watumwa na watoto wa waliokuwa wamiliki watumwa watakaa pamoja katika meza ya undugu…”

Msukumo uliotokana na uongozi wa harakati za Dkt King ulisaidia sana kubadili historia ya Marekani hususan usawa kwa (Wamarekani) Weusi, na kupelekea mabadiliko mbalimbali dhidi ya sheria za kibaguzi.Miongoni mwa sheria hizo ni pamoja na “Civil Rights Act” ya mwaka 1964 iliyoharamisha ubaguzi kwenye sehemu mbalimbali katika jamii.Mwaka uliofuata, “Voting Rights Act” ilipitishwa na kufuta kipengere kilicholazimisha wapiga kura watarajiwa kufanya testi za kupima uwezo wa kusoma na kuandika (wengi wa waathirika wa kipengere hicho walikuwa Wamarekani Weusi ambao walikuwa na maendeleo duni kielimu kutokana na kubaguliwa).

Maadhimisho ya siku ya Dkt King yamekuwa yakitoa changamoto nzuri kwa jamii ya Wamarekani kutafakari mahusiano kati ya Weupe na Weusi.Wengi hujiuliza iwapo ndoto za Dkt King zimetimia kweli,zinaelekea kutimia au hazina dalili ya kutimia kabisa.Ni maswali magumu ambayo yanahitaji uchambuzi wa kina kuyajibu,na pengine hata kwa uchambuzi wa kina bado inaweza kuwa vigumu kupata jawabu moja linalokubalika.Kingine kinacholeta ugumu wa kupata jawabu ni tofauti ya vizazi.Kwa walioishi nyakati za ubaguzi wa rangi na kushuhudia harakati za Dkt King wanaweza kuwa na mtizamo tofauti kuhusu kutimia kwa ndoto za mwanaharakati huyo ukilinganisha na kizazi cha hivi karibuni ambacho kinamwelewa Dkt King kupitia kumbukumbu za historia tu.

Hata hivyo ni rahisi kukubaliana kwamba harakati za Dkt King na wenzie zimesaidia kuleta mabadiliko makubwa ikiwa ni pamoja na hayo ya kisheria niliyotaja awali.Wapo wanaokwenda mbali zaidi na kutoa mifano ya mafanikio ya Waamerika Weusi maarufu kama Jenerali Colin Powell na Condoleeza Rice ambao wameshika nafasi nyeti katika uongozi wa taifa hilo.Lakini mfano mzuri zaidi ni Barack Obama,seneta Mweusi anayewania kuteuliwa kugombea urais wa nchi hiyo kupitia chama cha Democrats.Akiteuliwa kuwa mgombea,ataweka historia ya pekee nchini humo,na akifanikiwa kushinda urais basi hiyo itakuwa zaidi ya kuweka historia (tuite kuandika historia upya).Hata kama atashindwa,mafaniko aliyokwishafikia hadi sasa ni hatua muhimu katika kutimia kwa ndoto za Dkt King.

Afrika nayo imetoa akina Dkt King kadhaa,na kwetu Tanzania tunajivunia Baba wa Taifa marehemu Julius Nyerere ambaye (kama Dkt King) alikuwa na ndoto zake kadhaa ambazo kimsingi zilihusu kuwa jamii yenye usawa.Ndoto za Mwalimu zilivuka mipaka ya Tanzania kuhakikisha kuwa Afrika yote inakuwa huru.Mchango wa Mwalimu katika mapambano ya ukombozi kusini mwa Afrika utaendelea kukumbukwa milele.Na pengine hapo ndipo baadhi yetu tunagundua mabadiliko ya vizazi yanavyochangia kusahaulisha historia.

Mara nyingi napokutana na vijana Waafrika wenzangu (wanaoishi hapa Uingereza) kutoka nchi kama Zimbabwe,Zambia,Angola,Msumbiji,Afrika Kusini,Namibia na Uganda,nabaini kwamba wengi wao aidha wamesahau au wanapuuza mchango wetu katika ukombozi wa nchi zao (kwa Uganda ni kumng’oa Nduli Idi Amini).Angalau Wazimbabwe wanaweza kuwa na kisingizio kwamba kutokana na ubabe wa Mugabe,baadhi yao wanaweza kutoona faida ya kumkimbiza mkoloni na kujipatia uhuru.

Lakini pengine si busara sana kuwalaumu wanaopuuza mchango wa Mwalimu na Tanzania kwa ujumla katika ukombozi wa nchi zao kwani inawezekana kabisa wanafuatilia kinachoendelea nchini mwetu na kugundua kwamba baadhi yetu tumetupilia mbali kabisa jitihada za Baba wa Taifa kuhakikisha tunajenga jamii yenye usawa.Kwa vile dunia ni kama kijiji,katika zama hizi za utandawazi,majirani zetu hao watakuwa wanasoma na kusikia habari kuhusu ufisadi nchi mwetu,na pengine kubaki wanajiuliza “hivi hawa si ndio waliokuwa wanapigania usawa barani Afrika?Mbona wenyewe wako sasa wanafanyiana hivi?”.

Mwalimu alifariki huku baadhi ya ndoto zake zikiwa hazijatimia.Wachambuzi wazuri wa siasa wanadai kwamba baadhi ya ndoto hizo zilishindikana hata kabla hajang’atuka (kwa mfano upinzani wake wa awali dhidi ya ushirikiano na mashirika ya fedha ya kimataifa).Lakini nadhani Mwalimu aliumia zaidi kuona Azimio la Arusha likizikwa hai na Azimio “la kimyakimya” la Zanzibar (naliita hivyo kwani sijawahi kuona “document” yoyote rasmi inayoelezea kilichomo kwenye Azimio hilo).

Wakati Dkt King anaweza kufarijika huko aliko iwapo angeweza kufahamu baadhi ya mambo yanayoendelea sasa nchini Marekani (hususan kuhusu Obama) nashindwa kuhisi ni lipi litakalokuwa linampa furaha Mwalimu huko aliko tukiweka pembeni suala la amani na utulivu.Na hata katika hilo (la amani na utulivu) wapo wanaodai kuwa ni ya kufikirika zaidi kwani ni ukweli usiopingika kwamba masikini ni wengi zaidi kuliko matajiri,na yayumkinika kusema kwamba matumbo ya masikini hao hayana amani wala utulivu.

Kadhalika,kuna wanaodai kwamba kigezo cha amani na utulivu kimekuwa kikitumiwa vizuri zaidi na mafisadi wanaoamini kwamba Watanzania ni wapole sana na hawako tayari kuchezea lulu ya amani na utulivu kwa vile tu flani kakwiba mabilioni ya umma.Pengine mafisadi hao wako sahihi kwani tumekuwa tukishuhudia baadhi ya watu wakiua,wakapewa dhamana za chapchap na kuendela na maisha yao kama kawaida huku hatima ya kesi zao ikisubiri isahaulike akilini mwa watu.Wakati hayo yakitokea,magereza yetu yamejaa wamachinga wanaotafuta ridhiki mitaani na wafungwa wengine ambao inawezekana kabisa walijiingiza kwenye wizi wa nyanya au kuku kwa vile tu hawakuwa na njia nyingine ya kujipatia kipato.Uhalifu ni uhalifu,na kila mhalifu anastahili adhabu lakini inatatiza kuona wahalifu wengine wakiendelea kula raha kana kwamba waliyofanya si kinyume cha sheria.

Tofauti kubwa kati ya ndoto ya Dkt King na Mwalimu ni kwamba wakati Wamarekani Weusi wanafanya kila jitihada kuenzi jitihada za Dkt King kwa kuendeleza mapambano dhidi ya ubaguzi na kupigania usawa,sie tuko kwenye mgawanyiko mkubwa kati ya wachache walionacho wasiosubiri kuongezewa bali wanapora, na wengi wasio nacho ambao hata kile kidogo walicho nacho kinaporwa.Hili ndio tishio kubwa,sio tu kwa ndoto za Mwalimu,bali hata kwa hiyo lulu yetu ya amani na utulivu.

13 Jul 2007

Asalam aleykum,

Baada ya matukio ya hivi karibuni yaliyotuweka matumbo moto kufuatiwa mahayawani flani kuamua kuendesha kampeni yao ya kishetani ya kutaka kulipua mabomu huko London na hapo Glasgow (Waskotishi bado hawaamini kuwa ugaidi umeingia kwenye ardhi yao) sio wazo baya kuanza makala hii kwa habari “nyepesi nyepesi.” Gazeti la Daily Mail la hapa liliripoti hivi karibuni kuhusu matokeo ya utafiti yaliyoonyesha kuwa wanaume wenye aibu wana nafasi kubwa ya kupata magonjwa ya moyo kuliko wale wasio na aibu!Hizi tafiti nyingine…we acha tu.Kwa mujibu wa gazeti hilo,utafiti huo ulifanyika kwa kipindi cha miaka 30 uliwahusisha maelfu ya wanaume ambapo watafiti kutoka chuo kikuu cha Northwestern cha Chicago,Marekani walipokuwa wanafanya ufuatiliaji wa wawaliowahoji kwenye utafiti huo walibaini kuwa asilimia 60 kati yao (waliohojiwa) walikuwa wameshafariki,huku chanzo kikuu cha vifo kikiwa “heart attack” (nadhani kwa Kiswahili sahihi ni msongo wa moyo).Mambo hayo!

Na ukisikia duniani kuna mambo usidhani ni utani.Mzembe mmoja amekamatwa huko New Hampshire (Manchester) baada ya kushindikana kwa jaribio lake la kutaka kufanya uporaji benki huku akiwa amejivika matawi ya miti kama “camouflage” (kificho) yake.Jamaa huyo,James Coldwell,aliingia kwenye tawi la benki ya ushirika ya Citizens,huku akiwa amejivika majani na kuwatisha wahudumu wa benki hiyo kabla ya kufanikiwa kuondoka na kitita cha fedha,lakini alinaswa na polisi muda mfupi baadaye kwani triki yake ya “uninja wa majani” haikumsaidia kwa vile majani hayo hayakufunika sura yake,na wanausalama waliweza kuitambua vizuri kwenye CCTV.

Jumuiya ya Ulaya (EU) nayo ilijikuta kwenye wakati mgumu hivi karibuni baada ya kutoa filamu fupi kwa ajili ya promosheni ya kuhamasisha Jumuiya hiyo ambapo wahusika kwenye filamu hiyo ya sekunde 44 yenye jina “Let’s Come Together” walikuwa wakifanya “ngono nyepesi” (soft porn).Wapinzani wa wazo la Muungano wa nchi za Ulaya waliishambulia EU kwa kupoteza fedha za walipa kodi kwa kutengeneza filamu hiyo waliyoiona kuwa ni mwendelezo wa ubabaishaji wa Jumuiya hiyo.Nilipomtumia rafiki yangu flani habari hiyo kutoka gazetini alitania kwa kusema labda na sie tunahitaji “kampeni chafu” kama hiyo ya EU “kuuza” wazo la Muungano wa Afrika Mashariki ambao unaelekea kuwakera wadau wengi.

Nae mwanamama Amy Beth Ballamura amaepigwa marufuku kutia mguu kwenye pwani yoyote ya Uingereza baada ya kufanya majaribio zaidi ya 50 ya kujiua kwa kurusha baharini.Miongoni mwa sababu zilizopelekea kuchukuliwa kwa hatua ya kumdibiti mwanamama huyo ni pamoja na kuzitia huduma ya uokoji (emergency services) gharama ya zaidi ya pauni milioni 1 (zaidi ya shilingi bilioni mbili za huko nyumbani) kila wanapoitwa kwenda kumuokoa.Lakini pamoja na “tamaa” yake ya kujitoa roho,askari mmoja aliambulia tuzo ya ushujaa mwaka 2003 baada ya kusikia kelele za kuomba msaada kutoka baharini na kuamua kujitosa majini kufuata kelele hizo,ambapo alifanikiwa kumuokoa mwanamama huyo mwenye umri wa miaka 44.Cha kushangaza ni kwamba kama kweli alikuwa na nia ya kujitoa uhai sasa hizo kelele za kuomba msaada zilikuwa za nini?

Enewei,baada ya "nyepesi nyepesi" hizo (zote ni habari za kweli na wala sio kuwa “nawapiga fiksi” wasomaji wangu wapendwa) sasa tuangalie mambo ya muhimu zaidi huko nyumbani.Kwanza niseme siafikiani na hoja za Waziri wa Sheria Mama Nagu kwamba Bunge halipaswi kufanya kazi ya kupitia mikataba kabla ya kutiwa saini ili libaki na uhalali wake wa kuiwajibisha Serikali kwa mujibu wa dhamana ya mgawanyo wa mamlaka, kuchunguzana na kuwajibishana.Siafikiani naye kwa sababu hoja za baadhi ya wabunge kuwa mikataba hiyo ifikishwe kwao kabla ya kusainiwa zilizingatia ukweli kwamba kuna mapungufu makubwa yanayoendelea katika suala zima la kusaini mikataba mbalimbali.Mantiki nyepesi (simple logic) inaweza kutueleza kwamba maslahi ya nchi ni muhimu zaidi ya huo mgawanyiko wa madaraka.Hivi kwa mfano wazo la mikataba kuletwa bungeni lingekubaliwa,halafu nchi inufaike kwa kuingia mikataba yenye maslahi kwa Taifa,tatizo linakuwa wapi?Hivi kipi bora,kulinda mgawanyiko wa madaraka huku mikataba ya ajabu ajabu ikiendelea kuwepo au “kupindisha sheria” kwa kuileta mikataba hiyo bungeni kabla haijasainiwa halafu nchi ikanufaika nayo?

Pia nimesoma kwenye gazeti moja la huko nyumbani kwamba lile tishio la wafugaji huko wilayani Kilombero limerejea tena.Nitamke bayana kuwa hili linanihusu binafsi kwa vile mie ni “mwana wa pakaya” naetokea mitaa ya huko.Hawa wafugaji ni wakorofi,watovu wa nidhamu na wavunja sheria wakubwa.Maagizo kadhaa yameshatolewa kuwataka waheshimu sheria za nchi lakini wameamua kuweka pamba masikio.Mamlaka husika zinapaswa kuliangalia suala hili kwa makini zaidi kwani wanachofanya wafugaji hao sio tu kinahatarisha amani (mifugo yao inakula mazao ya wakulima,na hilo pekee linatosha kuzusha ugomvi) lakini pia hawawatakii mema wakulima kwani kwa kuswaga mifugo yao kwenye mashamba wanamaanisha kuwa wanataka wakulima hao wakose chakula na hela wanazojipatia kwa kuuza akiba ya mavuno yao.Hili ni bomu la wakati (time bomb) kwani japo hakuna bondia wa Kindamba (kama yupo basi samahani kwani sijamsikia) lakini hiyo haimaanishi kuwa mtu atakaeswaga mifugo yake kwenye mashamba ataachwa afanye anavyotaka.Hapo itakuwa kuchukua sheria mkononi,na japo mie ni mpinzani mkubwa wa kuchukua sheria mkononi,natambua dhahiri kuwa mtu “anapoletewa za kuleta” anaweza kabisa kuiweka sheria kando,hususan pale haki yake inapopuuzwa kwa makusudi.Kwa vile mkoa wa Morogoro umebahatika kuwa na RC ambaye ni “mjeshi” mstaafu basi hapana shaka Brigedia Jenerali Kalembo huyo atatumia “mbinu za medani” kuwadhibiti wafugaji hao wenye uhaba wa nidhamu.

Kikao cha Bunge kinaelekea ukingoni na miongoni mwa hoja nilizovutiwa nazo ni ile ya Mheshimiwa Shabiby (wa Gairo) kuhusu ujanja unaofanywa na baadhi ya wamiliki wa mabasi makubwa ya abiria.Alieleza kuwa mengi ya mabasi yanayotumika sasa yamefanyiwa “usanii” kwa kuweka mabodi mapya kwenye “chasis” na injini za malori au za kale.Kuna jina moja tu linalowafaa “wasanii” hawa nalo ni “WAUAJI.” Wanathamini sana kukwepa gharama za kununua mabasi mapya lakini hawajali hata chembe madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na vitendo vyao vya “kuunda mabasi feki.” Kwa upande mwingine tuseme bila kuonekana aibu kwamba mabasi ya namna hiyo yanafahamika hata bila kuwa na ujuzi wa umakanika kwani ulifika pale stendi ya mabasi Ubungo unaweza kukutana na basi ambalo linaonekana dhahiri kuwa bodi yake “imepachikwa” sehemu isiyostahili.Trafiki yeyote aliyehitimu mafunzo yake vyema na mwenye uchungu na maisha ya Watanzania wenzie hawezi kuliruhusu basi “lililovimba mbavuni utadhani lina ujauzito” liendelee na safari,na mabasi ya namna hiyo yako mengi tu.Wanaofanya hivyo wanajua bayana kuwa wanavunja sheria na kuhatarisha maisha ya abiria wao lakini hawajali kwa vile hakuna aliyechukuliwa sheria hadi leo.Si ajabu tukisikia kuwa baadhi ya mabasi hayo yanatumia injini za matrekta au hata za mashine za kusaga….(nashindwa kumalizia,nimekabwa na kicheko japo jambo hili sio la kuchekesha hata chembe.)

Mwisho,wakati Gavana wetu keshatamka bayana kuwa hatojiuzulu (utadhani alijichagua mwenyewe kwenye posti hiyo),sie wapenzi wa Simba tunajipoza kwa kusherehekea ubingwa wetu ambao kidogo umetibuliwa na hizi habari za viongozi kugombea mapato ya mechi huko Morogoro.Wito kwa watani wetu wa jadi Yanga ni huu:Micho akirudi (kama kweli atarudi) ashauriwe kukutana na Twalib Hilal apewe darasa kuwa ukocha sio sawa na ukatibu mwenezi wa klabu: ukocha ni vitendo vingi maneno machache lakini Mserbia Micho kila siku “anachonga” kuhusu hili au lile lakini matunda ya kazi yake kwenye dimba ni haba.Enewei,asilaumiwe sana kwani alishawahi kusema kuwa wachezaji wake hawafundishiki,na katika mechi ya juzi anaweza kuongeza sababu kuwa “lile tumbo la kuendesha” limechangia kukosa ushindi.

Alamsiki






22 Aug 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum,

Naanza makala yangu kwa kuelezea majonzi makubwa niliyonayo kufuatia kifo cha mwanataaluma maarufu huko nyumbani,Profesa Seith Chachage.Majonzi yangu yanachangiwa na ukweli kwamba mimi ni miongoni mwa wanafunzi wake wa zamani hapo Mlimani.Mungu ndiye mtoaji na yeye ndiye mchukuaji kama Maandiko Matakatifu yanavyosema,lakini pengo aliloliacha msomi huyu aliyebobea ni vigumu kuzibika.Nimepitia tovuti mbalimbali na nimegundua kuwa marehemu alikuwa kipenzi cha wengi hasa wale wenye uchungu na Tanzania na bara la Afrika kwa ujumla.Kwa tuliomjua Profesa Chachage tutakumbuka jinsi alivyokuwa akichanganya usomi wake na kauli za utani.Yaani ilikuwa vigumu kuchoka kusikia mhadhara wake.Kwa tunavyowajua wasomi wetu ni nadra kumkuta mmoja wao akipenda vitu kama bongofleva,lakini nimesoma kwenye tovuti moja kwamba marehemu alikuwa anapenda muziki wa kizazi kipya na inasemekana aliweza hata kuimba verses za wimbo maarufu wa TID uitwao Zeze.Mungu ailaze ahali pema roho ya marehemu Profesa Chachage,Amen.

Alhamisi ya tarehe 13/06 mwaka nilisoma kwenye tovuti ya gazeti la Uhuru habari iliyonukuu Rais mstaafu Benjamin Mkapa akisema kwamba “katika baadhi ya mashirkika kama ATC serikali iliingia mikataba bila kuwa na tathmini halisi ya faida ambayo ingepata kwenye mashirika hayo.”Hizi si habari njema hasa ikizingatiwa kwamba serikali haitegemei wataalamu wa njozi kujua kama mkataba flani una manufaa au la bali inapaswa kuwatumia wataalam wake kuhakikisha kuwa kinachofanyika sio bahati nasibu ila ni kitu cha maslahi kwa Taifa.Tunaweza kutomlaumu Chifu MangungO alisaini mikataba feki na akina Karl Peters nyakati za ukoloni kwa sababu enzi hizo hakukuwa na wataalamu wa kupitia mikataba na kujua kama ina manufaa au la.Lakini zama hizi hali ni tofauti.Pale serikali inapoona kwamba jambo flani liko nje ya uwezo wake ina uwezo wa kutafuta na kupata uhakiki flani kutoka nje ya nchi.Yaani hapo namaanisha kwamba yapo makampuni kadhaa ya kimataifa ambayo yanaweza kutoa huduma ya ushauri kwa serikali iwapo itaonekana kwamba wataalam wetu wa ndani wameshindwa kazi hiyo.Hivi inawezekanaje mtu akaingia mkataba bila kujua faida yhalisi ya mkataba huo?Utapangishaje nyumba yako kama huna hakika kuwa kwa kufanya hivyo wewe mwenyewe au familia yako mnaweza kuishia kulala gesti hausi?Na je inapobainika kwamba kuna tu flani,kwa sababu anazozijua yeye,alisaini mkataba usio na faida kwa Taifa,tunafanyaje?Suala hapa sio kunyooshena vidole bali ni kuhakikisha kuwa makosa ya aina hiyo hayajirudii.Na njia nyepesi ya kufanya hivyo ni kuwachukulia hatua wale waliofanya makosa hayo-iwe walifanya kwa makusudi,uzembe au kutojali maslahi ya nchi yetu.

Nilishawahi kuandika huko nyuma kwamba kuna watu hawana uchungu na Taifa letu,na hawa ni pamoja na hao wanaosaini mikataba kama ile ya Chifu Mangungu utadhani wakati wanasaini mikataba hiyo walikuwa bwii(wamelewa) au wamesainishwa wakiwa usingizini.Marehemu Chachage na baadhi ya wasomi wengine wa nchi hii walijikuta wakitengeneza maadui kila walipojitahidi kukemea mambo yanayoendana kinyume na maslahi ya Taifa.Kuna watu hawapendi kuambiwa ukweli hata pale wanapoharibu na si ajabu makala hii ikapata upinzani wao.Lakini hiyo haitatuzuwia sie wenye uchungu na nchi yetu kusema yale yanayotupeleka pabaya.

Nimesikia kuna kampuni ya Kisauzi Afrika imepewa haki za utafutaji mafuta huko nyumbani.Pia kuna tetesi kwamba nchi yetu ina utajiri wa Uranium.Mungu akitujalia,siku moja na sisi tutakuwa na sauti kwenye siasa za kimataifa kwa vile mafuta ni silaha,ukiwa nayo lazima utaheshimika.Lakini bila mipango madhubuti utajiri hio unaweza kuwa kama laana kwa Taifa kama letu lililozowea amani.Huko Nigeria kumekuwa na matukio kadhaa ya vurugu ambazo kimsingi zinatokana na ukweli kwamba wenye ardhi (wananchi) wanaishia kuona tu mabomba ya mafuta na magari ya thamani kwa wale wanaowatumikia wenye makampuni ya mafuta ya kutoka nje,huku walalahoi wakizidi kuwa masikini.Mwanafalsafa Karl Marx aliwahi kusema kuwa masikini hana cha kupoteza anapoamua kupigania haki yake.Watu hawawezi kuendelea kuwa kimya wakati utajiri wao wa asili kwenye nchi yao unawanufaisha wachache kutoka nje na wapambe wao wanaosaini mikataba hewa.

Naomba ieleweke kwamba sizilaumu serikali za awamu zilizotangulia kuwa mikataba yote zilizoingia ilikuwa bomu.Kilio changu hapa ni kwenye hiyo mikataba ya iliyosainiwa ndotoni.Nafahamu kwamba wataalamu wazalendo wanatoa ushauri mzuri tu kabla ya mikataba kusainiwa lakini tatizo linakuja pale maslahi binafsi yanapowekwa mbele ya maslahi ya Taifa.Kwa kuwa mtu ana mamlaka ya kupuuza ushauri wa kitaalamu basi anatumia fursa hiyo kujifanya madudu kana kwamba madhara ya anachokifanya hayatamgusa kwa namna flani.

Naamini serikali ya Awamu ya Nne haitawalea wazembe wanaotaka kutulostisha.Narudia kusema kwamba sisi sio masikini wa namna tulivyo kwa sababu tuna raslimali za kutosha ambazo zinaweza kabisa kutuweka pazuri.Tunachopaswa kuelewa ni kwamba miaka 25 au 50 ijayo vizazi vya wakati huo vinaweza kutushangaa sana pale vitakapokuta kila kitu kimeuzwa na faida ya mauzo hayo haionekani.Inaweza kuwa vigumu sana kwa walimu wa somo la Historia wa wakati huo kuwaelewesha wanafunzi wao kuwa tofauti na mikataba feki ya kina Karl Peters na baadhi ya machifu wetu,mikataba iliyobomoa nchi yao ilifanywa na Watanzania haikuwa ya kilaghai bali ni sababu ya kitu kidogo (sijui wakati huo watakuwa wanatumia msamiati gani kumaanisha rushwa),

Alamsiki

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum,

Kabla sijaenda kwenye mada yangu ya leo ngoja nielezee kichekesho kimoja nilichokisoma kwenye mtandao kuhusu maandalizi ya timu ya Moro United katika majukumu ya kitaifa yanayowakabili.Kiongozi mmoja wa timu hiyo alinukuliwa akisema kwamba timu hiyo imeamua kufuta safari ya kwenda nchini Ufaransa kwa vile wamekosa nafasi ya sehemu ya kufikia “kutokana na hoteli nyingi kujaa kipindi hiki cha summer…”Hiki ni kichekesho kwa sababu Ufaransa ni nchi na sio kijiji au mtaa wenye hoteli moja au mbili.Kilichonisikitisha ni ukweli kwamba mwandishi aliyeripoti habari hiyo hakufanya jitihada yoyote ya kumuuliza kiongozi huyo ni hoteli zipi na katika miji gani ya Ufaransa ambazo timu hiyo ilipanga kufikia,na hapo ingekuwa rahisi kwa mwandishi huyo kuhakiki hoja hiyo kwenye tovuti ya hoteli au sehemu zilizotajwa.Tunaambiwa kuwa badala ya Ufaransa sasa timu hiyo itakwenda Italia,kana kwamba huko Italia sasa ni majira ya baridi au hakuna watalii waoweza kujaza hoteli “kama ilivyokuwa huko Ufaransa.”

Enewei,tuachane na ubabaishaji huo.Majuzi nilipata barua pepe kutoka kwa rafiki yangu mmoja anayesoma siasa kama mimi japo yeye eneo lake la utafiti ni Kusini Mashariki mwa bara la Asia na mimi eneo langu ni Afrika.Katika barua hiyo,niliombwa kutoa mawazo yangu kuhusu kile ambacho rafiki yangu alikiita kukua kwa kasi kwa interests za China katika bara la Afrika.Tangu Januari mwaka huu viongozi wa juu wa nchi hiyo wameshatembelea nchi 15 za Afrika.Wakati Waziri Mkuu Wen Jiabao ametembelea Misri,Ghana,Congo,Angola,Afrika Kusini,Uganda na Tanzania,Rais Hu Jintao ametembelea Morocco,Nigeria na Kenya,huku Waziri wa Mambo ya Nje Li Zhaoxing amezuru Libya,Senegal,Cape Verde,Mali,Liberia na Nigeria.Wafuatiliaji wa siasa za kimataifa wa nchi za Magharibi wanaonekana kuwa na kihoro kwa namna mambo yanavyoonekana kwenda vyema kwa China na marafiki zake wa Afrika.Eti wanadai kuwa tofauti na mapatna wakuu wa biashara wa Bara la Afrika,yaani Marekani na Uingereza,China haijali sana kuhusu masuala ya haki za binadamu na ndio maana baadhi ya misaada ya nchi hiyo imekwenda kwa nchi ambazo rekodi zake katika haki za binadamu sio za kuuridisha sana.Kwa mujibu wa tovuti ya Council for Foreign Relations, China iliipatia Sudan ndege za kivita aina ya Shenyang na silaha vyote vikiwa na thamani ya dola zaidi ya milioni 100,na kati ya 1998 na 2000 ilitoa misaada ya silaha zenye thamani ya dola bilioni 1 kwa Ethiopia na Eritrea wakati nchi hizo zikiwa kwenye vita.Lakini pia wachambuzi hao wanadai kuwa katika kupata mikataba minono China haijali sana wale wanaoomba “teni pasenti” kusaini mikataba yenye utata,na ziadi ni suala la kutumia wataalamu wake badala ya wazawa kwenye nchi inazoshirikiana nazo.

Hata hivyo,pamoja na “longolongo” hizo ukweli unabaki kwamba mchango wa China kwa Afrika ni wa manufaa kwa bara hilo lenye mlolongo wa matatizo.Kwa mfano,mwaka jana uchumi wa Afrika ulikuwa kwa asilimia 5.2 ambayo ni rekodi ya juu kabisa,na miongoni mwa sababu muhimu ni mchango wa China kwenye uchumi wa bara hilo.Pia China ilifuta madeni kwa Afrika yanayofikia takribani dola bilioni 10,mwaka juzi ilichangia askari 1500 kwenye majeshi ya kulinda amani ya Umoja wa Mataifa barani Afrika,na ujenzi wa miundombinu unaofanywa na nchi hiyo ni wa gharama nafuu na unazingatia muda.

Jambo jingine la hivi karibuni ambalo limegusa hisia za duru za kisiasa za nchi za Magharibi ni kikao cha 7 cha Umoja wa Afrika (AU) ambapo Rais wa Iran,Mahmoud Ahmadinejad,na mwenzie wa Venezuela,Hugo Chavez,walihudhuria.Viongozi hao wawili wanaonekana kama “miiba mikali” kwa Marekani na washirika wake.Nchi zote hizo mbili zinajivunia “silaha” zake yaani mafuta,na kwa namna flani Marekani na marafiki zake wanaishia kulalamika tu bila kuchukua hatua yoyote dhidi ya nchi hizo pengine kwa kuhofia madhara kwenye suala nyeti la “wese” (mafuta).

Mara nyingi Afrika inavuta zaidi hisia za siasa za kimataifa kwenye majanga-kama vita,ukimwi,nk-pale inapoonekana kuwa bara hilo linaweza kukumbatiwa na wale wanaoonekana (kwa Marekani na wenzie) kuwa ni nguvu tishio.China ina uchumi unaokuwa kwa kasi ya kutisha,yaani ile shaa kama wanavyosema watoto wa mjini,na ukichanganya na watu wake zaidi ya bilioni moja,wachumi wa nchi za Magharibi wanaiangalia nchi hiyo kwa makini sana.

Enzi za Vita Baridi,washiriki wakuu-nchi za Magharibi chini ya Marekani,na za Mashariki zikiongozwa na Urusi-walipigana vikumbo ndani ya Afrika ili kuliweka mikononi bara hilo.Mbinu chafu sana zilitumika katika kutekeleza azma hiyo ikiwa ni pamoja na mauaji ya wanasiasa kama Patrice Lumumba,na sapoti kwa wanaharamu kama Jonas Savimbi na UNITA yake.Yayumkinika kusema kwamba bara la Afrika halikupata nafasi ya kupumua baada ya mapambano dhidi ya ukoloni kwani mara baada ya uhuru likajikuta limewekwa mtu kati kwenye mapambano kati ya ubepari na ukomunisti.

Ni matarajio yetu kwamba iwapo hao wanaowashwa na kukua kwa mahusiano kati ya China na Afrika wataamua kufanya lolote basi haitokuwa kuligeuza bara letu kuwa uwanja wa mapambano ya kiitikadi.Kwa kuwa hali kwa sasa iko shwari,acha tufaidi ukarimu wa wajukuu wa Mwenyekiti Mao na mwenzie Zhou Enlai (fasheni za zamani zinarudi,je suti za chwenlai nazo zitarudi?).

Alamsiki

18 Jun 2006

KULIKONI UGHAIBUNI

Asalam aleykum.

Hapa Uingereza kuna chama cha siasa kinachoitwa British National Party au kwa kifupi BNP.Hiki ni chama kinachofuata siasa za mrengo wa kulia kabisa,far right kwa “lugha ya mama.”Siasa za namna hiyo ndio zilizokuwa zinahusudiwa na Manazi chini ya Hitler na Mafashisti chini ya Mussolini.Hawa jamaa wa BNP ni wabaguzi waliokithiri.Majuzi wakati wa uchaguzi mdogo huko England mmoja wa watu muhimu katika BNP,Dokta Phill Edwards (jina lake halisi ni Stuart Russell) alizua mjadala mkubwa kuhusu siasa za chama hicho pale alipotoa matamshi ya kuchefua dhidi ya watu weusi.Alirekodiwa kwa siri na kituo cha televisheni cha Sky akisema kuwa watu weusi wana IQ (uwezo wa akili) ndogo,na watoto weusi wakikua sanasana wataishia kukaba watu (vibaka au majambazi).Aliendelea kusema,hapa namnukuu “suala hapa sio kama tunawachukia watu weusi bali ni kama wao ni tishio kwa amani,utulivu na utamaduni wa jamii ya Kiingereza…watoto weusi wakikua watanyonya uchumi wetu na kujaza magereza yetu na pengine kukukaba…huko Afrika kusini mwa jangwa la Sahara hakuna ustaarabu wowote,na hakuna maendeleo ya sayansi…”Kwa kweli ilikuwa inauma kuangalia upuuzi huo kwenye runinga,lakini ni hali tunayoishi nayo hapa kila siku.

Miongoni mwa mambo “halali” yanayowapa nguvu wabaguzi hawa ni vitendo vya baadhi ya wageni na hasa weusi kujihusisha na uhalifu au mambo mengine yasiyofaa katika jamii.Kwa wao,samaki mmoja akioza basi wote wameoza,yaani mtu mmoja mweusi akihusika kwenye uhalifu basi watu wote weusi ni wahalifu.Na kwa BNP sio weusi tu wanaolengwa.Chama hicho kilipata “pumzi” ya kutosha kupinga sera za uhamiaji na ujio wa wageni hapa Uingereza baada ya matukio ya kujilipua mabomu kwa kujitoa mhanga mjini London mwezi Julai mwaka jana. “Vita” ya BNP dhidi ya wageni ikapamba moto na sasa walengwa wakuu wakawa watu wenye asili Asia (hasa Wapakistani).Watatu kati ya waliojilipua mabomu ya muhanga walikuwa Waingereza wenye asili ya Pakistani,na kwa chama hicho cha kibaguzi hiyo ilikuwa sababu tosha ya kuwajumuisha watu wenye asili ya Pakistani na Asia kwa ujumla,na wageni wengine kuwa ni tishio kwa maisha ya Taifa hili.

Huko nyubani moja ya mambo ambayo Watanzania tunajivunia sana ni jinsi “tunavyojichanganya” bila kujali kabila,dini au jinsia.Nikisema “kujichanganya” namaanisha ushirikiano,upendo na maelewano,na sio kukosa msimamo kama maana halisi ya neno ilivyo.Niliwahi kusikia stori flani siku za nyuma inayohusu timu moja ya soka kutoka nchi flani ya jirani.Wachezaji wa timu hiyo walipokuwa wanafanya mazoezi walikuwa wanavuta umati mkubwa wa wakazi wa mji wa Arusha,ambako kulikuwa na michuano ya kimataifa.Kilichokuwa kinawashangaza wachezaji hao ni jinsi watazamaji walivyokuwa “wanajichanganya” kana kwamba ni watu wa kabila moja.Nchi wanayotoka wachezaji,kama zilivyo nchi kadhaa za Afrika,inasifika sana kwa ukabila.Inasemekana katika nchi hiyo ni nadra watu wanaotoka makabila tofauti kuwa marafiki wa dhati.Sasa walipoona baadhi ya watazamaji “wanagongeana sigara” na kutia stori kana kwamba wanaishi nyumba moja,ilikuwa ni jambo la kushangaza sana kwao.Huenda waliondoka Arusha wakiwa na fundisho flani.
Rafiki yangu mmoja,Profesa Tunde Zack-Williams,aliwahi kuniambia kwamba napaswa kujivuna kuwa Mwafrika kutoka Tanzania.Alinieleza kwamba kwa uzoefu wake mwenyewe kama mwanataaluma na Mwafrika,Watanzania ni watu waliojaliwa na “karama” ya mshikamano,upendo na umoja,na wanawaheshimu sana wageni bila kujali wanatoka wapi.Profesa huyo ni mzaliwa wa Sierra Leone,nchi ambayo imeathiriwa sana vita vya wenyewe,na amekuwa akiwasaidia sana kitaaluma vijana wa Kiafrika.Rafiki yangu mwingine anayetoka Sudan aliniambia kwamba alishangaa sana alipofika Tanzania kwa mara ya kwanza,kwa sababu licha ya nchi yetu kuwa na makabila zaidi ya 120 hakuona dalili zozote za watu kubaguana kwa misingi ya kikabila.

Hata hivyo,katika siku za hivi karibuni kumeanza kujitokeza dalili za baadhi ya watu kuchoshwa na “ujiko” huo tulionao ndani na nje ya Afrika.Binafsi,nafanya utafiti unaohusu masuala ya dini na siasa.Sintoongelea sana utafiti huo kwa vile bado “uko jikoni” lakini miongoni mwa matokeo yake ya awali ni dalili kuwa kuna watu au vikundi flani vya jamii vinavyotumia dini kujenga mpasuko katika jamii kwa manufaa yao binafsi.

Kibaya zaidi ni dalili kwamba baadhi ya Watanzania ambao tuna haki ya kuwaita “wageni” wanapoanza kujiingiza kwenye kuleta chokochoko kwenye jamii yetu iliyozowea amani.Siku zote tumekuwa tukiheshimiana na kupendana bila kujali kuwa flani alizaliwa Ifakara au New Delhi.Lakini kama BNP inavyopata “nguvu halali ya kusema ovyo” pindi wageni “wanapoharibu” inaweza kufika mahali Watanzania wazawa wakaanza kujenga chuki dhidi ya wale ambao licha ya “ugeni” wao wanachochea mpasuko katika nchi yetu.Na si “wageni” tu bali hata wale wanaotumia nafasi zao za juu katika jamii kutukoroga.Waasisi wa Taifa letu walifanya kazi kubwa sana kutufikisha hapa tulipo,na nawausia Watanzania wenzangu tusifumbe macho pale wale tulikowakaribisha kwa upendo (na maswahiba zao) wanapoanza kutuletea dharau na chokochoko kwenye nchi yetu.

Alamsiki

KULIKONI UGHAIBUNI

Mambo yakoje huko nyumbani?Natumaini kila mmoja anawajibika kwa namna yake katika ujenzi wa Taifa.

Kuna jamaa mmoja hapa anaitwa David Cameron.Huyu ni kiongozi wa chama cha wahafidhina (Conservative Party).Nia yangu si kuzungumzia wasifu wake,bali nataka nimlinganishe na mwanasiasa nyota wa huko nyumbani kwa muda huu,au kwa lugha ya “kwa mama” tunaweza kumuita “a man of the moment.” (kwa tafsiri ya haraka, “staa wa muda huu”).Nadhani msomaji mpendwa umeshajua ni nani ninayemzungumzia.Lakini hapa namuweka kando kidogo ili nikupashe kuhusu huyo Bwana Cameron na chama chake cha Conservatives (au Torry,kama kinavyojulikana hapa).Kwa tafsiri nyepesi hawa Conservatives ni watu wenye mrengo wa kulia na ndio wapiga kelele wakubwa kuhusu sera za uhamiaji na nyinginezo ambazo zinawagusa makabwela hususan wale ambao si wazawa wa hapa.Pengine jeuri kubwa ya wahafidhina hawa inatokana na uwezo wao wa kifedha.Fedha wakati mwingine huwa na tabia ya kumfanya binadamu asiwafikirie wenzie aliowazidi kiuwezo,na aghalabu anapowafikiria basi huwa ni kwa manufaa yake binafsi.

Kuibuka kwa Cameron kulichochewa zaidi na mwelekeo usioridhisha wa chama chake katika chaguzi mbalimbali.Wachambuzi wengi wa mambo ya siasa walikuwa wanahusisha mwenendo mbaya wa chama hicho na kile kinachoitwa kuwa “out of touch.”Nitafafanua.Chama kilicho “out of touch” ni kile ambacho machoni mwa watu wa kawaida kinaonekana kama hakijihusishi na maslahi ya walio wengi.Kwa mfano,hawa wahafidhina kwa miaka kadhaa wamekuwa wakikumbatia zaidi Waingereza weupe hasa wale wa tabaka la juu na la kati huku wakiwasahau wale wa tabaka la chini pamoja na Waingereza wengine ambao ni “wakuja” (kwa mfano wale wenye asili ya Asia,Caribbean,Afrika,n.k).Pia wamekuwa wakiwaona wageni (ikiwa ni pamoja na wanafunzi wanaochangia mamilioni ya paundi kwenye uchumi wa nchi hii) kama watu wanaokuja kuharibu uchumi,utamaduni na mazingira ya hapa.

Baada ya Waziri Mkuu wa mwisho kutoka Conservative kushika wadhifa huo,John Major,alipoangushwa na Tony Blair mwaka 1997,chama hicho kimebadilisha viongozi kadhaa lakini bila mabadiliko hayo kuwanufaisha kwenye chaguzi mbalimbali.Ndipo katika mchakato huo alipoibuka Bwana Cameron,kijana (ana miaka 40 tu),ana mvuto na haiba ya kutosha.Huyo bwana aliamua kuwapa wenzake kitu “laivu” kwamba chama chao hakina mvuto kwa wapiga kura,kinaonekana kuwa kiko zaidi kwa maslahi ya mabwanyenye kuliko makabwela,na hakizungumzi “lugha ya mtu wa kawaida mtaani.”Kuna mengi ya kumzungumzia huyo bwana lakini kilichonisukuma kuandika makala hii ni jinsi navyomuona anafanana na Jakaya Kikwete.Ukiachilia ukweli kwamba wote ni handsome lugha wanayoongea inafanana:lugha inayomgusha mtu wa kawaida na sio makundi flani tu katika jamii hususan wale wenye nguvu za kiuchumi.

Jakaya amenukuliwa mara kadhaa akiwausia viongozi wenzie kwamba wako madarakani kuwahudumia hao waliowaweka madarakani.Sio dhambi kuwa karibu na matajiri lakini ukaribu huo usiwe kwa ajili ya kuwaumiza wasio nacho.Utajiri sio dhambi,na kuna matajiri kadhaa (mfano Mzee Mengi huko nyumbani au Bill Gates huko Marekani) ambao utajiri wao umekuwa faraja kwa mamilioni ya wale wasio nacho.Matajiri wa aina hii ni muhimu kwao kuwa karibu na viongozi wa serikali,vyama vya siasa na taasisi nyingine kwa vile ni kwa ukaribu huo ndio miradi mbalimbali wanayoifadhilia inaweza kuwa na manufaa kwa wananchi.

Juzijuzi nilimwona Bwana Cameron kwenye luninga akiwa kwenye mtaani wakati wa kampeni za chama chake kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa kwa upande wa England.Jinsi alivyokuwa akijichanganya na watu ilitosha kabisa kumfanya hata mtu aliyekuwa akikichukia chama cha wahafidhina afikirie upya.Siku chache baadae nikasoma kwenye mtandao kuwa Jakaya ameweka historia kuwa Rais wa kwanza wa Tanzania kutembelea wafungwa magerezani.Yalipotokea mauaji ya kutatanisha ya wale wachimba madini wa Mahenge hakukawia kuunda tume,na kinyume ya ilivyozoeleka mara baada ya kupewa ripoti na tume akaweka matokeo hadharani.Aliporejea tu kutoka Kusini mwa Afrika hakukawia kwenda kuwaona majeruhi wa tukio la uporaji wa fedha za NMB pale Ubungo,na kutoa maagizo papo hapo.Lakini si Jakaya pekee bali hata “luteni” wake Lowassa.Ghorofa lilipoanguka Keko hakusubiri kuletewa taarifa bali alikwenda kujionea mwenyewe na kuchukua hatua hapohapo, “mafuriko” yalipoielemea Sinza hakukawia kwenda kushuhudia hali ilivyo na kuwaamuru wahusika wachukue hatua za haraka.

Laiti kasi mpya,ari mpya na nguvu mpya aliyokuja nayo Kikwete itaweza kufikia hatua ya kuigwa na viongozi kuanzia ngazi ya serikali ya mtaa,kata,tarafa,wilaya na mkoa,basi muda si mrefu Bongo itakuwa sehemu ya neema.Na mwenyewe Jakaya amekuwa akisema kuwa Tanzania yenye neema inawezekana.Enyi viongozi mliolala hebu amkeni,msisubiri kuamshwa.Jisikieni aibu pale mnapokwenda kinyume na spidi ya kiongozi wenu mkuu.

Alamsiki

KULIKONI UGHAIBUNI

Asalam aleykum,

Siku za nyuma niliahidi kwamba iko siku nitawaletea stori kuhusu “mateja” wa huku Ughaibuni.Ndio,tatizo la matumizi ya madawa ya kulevya linawaumiza vichwa watu kadhaa huku Ughaibuni.Kuna vijana wadogo kabisa ambao wanashawishika kujiingiza katika kubwia unga.Ni vigumu kutabiri mafanikio ya jitihada za serikali na taasisi mbalimbali katika mapambano yao dhidi ya ulevi huo haramu na hatari.

Hivi karibuni nilipewa habari za kusikitisha sana.Kijana mmoja mwenye umri usiozidi miaka 18 alikutwa amekufa huku sindano aliyoitumia kujidungia adawa ya ulevya ikiwa inaning’inia kwenye mkono wake.Huyo kijana namfahamu vizuri kwa vile siku moja aliwahi kufika hapa ninapoishi akiwa ameongozana na rafiki yangu mmoja mwenye asili ya Afrika Mashariki.Kilichonivutia zaidi kuhusu kijana huyo ni kauli zake ambazo lazima nikiri kuwa mara nyingi kwa hapa zinatolewa na wanasiasa kuliko wananchi wa kawaida.Alikuwa akionyesha kuchukizwa kwake na watu wanaowabagua wenzao kwa vile tu ni wageni au wana rangi tofauti na wao.Kimsingi,alikuwa akilaani suala zima la ubaguzi.Kwa umri wake mdogo,nilimwona kama ni mtu mwenye upeo mkubwa sana.Kwa wakati huo sikujua kabisa kuwa pamoja na busara zake,kijana huyo alikuwa akiweka rehani roho yake kwa kubwia unga.Pengine lishe bora na huduma mbalimbali zinazopatikana kirahisi ndizo zilikuwa zinamsaidia kuficha “uteja” wake,kwani kama tujuavyo wengi si vigumu kumtambua m-bwia unga kwa kumwangalia tu.

Alienisimulia kuhusu mauti yaliyomkumba kijana huyo alinijulisha kwamba aliemletea marehemu madawa hayo ya kulevya alikuwa ni rafiki yake ambae walikuwa wanasoma darasa moja.Kwa lugha nyingine,wawili hao walishirikiana katika kuleta mauti ya mmoja wao.Huo ni ushirika wa mauti,na hilo ndio linanipeleka kwenye mada yangu ya pili kuhusu ujambazi uliotokea hivi karibuni pale Ubungo uliopelekea vifo na majeraha kwa waliosalimika.

Kuonyesha yeye ni kiongozi anaewajali mno wananchi wake,matra baada ya kurejea nchini akitoka ziarani kusini mwa Afrika,Rais Jakaya Kikwete alikwenda kuwajulia hali waliojeruhiwa na majambazi katika tukio hilo la Ubungo.Mheshimiwa Kikwete alinukuliwa na vyombo vya habari akisema kwamba anaamini kuwa kulikuwa na njama ndani ya benki iliyoibiwa fedha hizo kwa vile isingekuwa rahisi kwa majambazi hayo kuvamia tu gari lenye fedha bila kuwa na taarifa sahihi.Wafanyakazi waliohusika kuvujisha taarifa za fedha hizo kwa majambazi watakuwa hawana tofauti na yule kijana aliempelekea unga rafiki yake na hatimaye kumsababisha mauti.Waliovujisha taarifa hizo walikuwa na ushirika wa mauti na majambazi waliofanya unyama huo.Hivi tunapokuwa kazini si huwa tunaunda kitu kama undugu kwa vile muda mwingi tunautumia tukiwa pamoja na pengine kushirikiana katika mambo ya nyumbani kama vile harusi na misiba?Sasa unapotoa taarifa kwa majambazi wenye silaha za moto ili kuwawezesha kuvamia gari ambalo mfanyakazi mwenzio yupo humo si ni kama unamtengenezea mauti mwenzio?Jamani,hivi fedha zinatupeleka kupoteza utu wetu na kutothamini uhai wa wenzetu!Kwa hakika walioshiriki kwa namna yoyote katika kufanikisha uporaji huo wanastahili kusakwa kwa udi na uvumba na hatimaye kupatiwa kibano wanachostahili.Kwa “waliouza ishu” hiyo kwa majambazi wanakuwa wametenda dhambi kuu mbili:kuwasaliti wafanyakazi wenzao ambao aidha waliuawa au kujeruhiwa,na pia walishiriki katika ujambazi huo kwa vile wao ndio hasa waanzilishi wa mpango mzima.Hiyo si kusema kwamba majambazi waliohusika hawana hatia,lakini iwapo waliotoa taarifa hizo wasingewajulisha majambazi kwamba siku flani,muda flani,katika gari flani kutakuwa na shilingi bilioni moja ni dhahiri kwamba tukio hilo lisingetokea.

Kwa upande mwingine,ni muhimu kwa taasisi zetu za fedha kuwa makini zaidi wanaposafirisha fedha kutoka sehemu moja kwenda nyingine.Hivi kweli benki kama NMB inashindwa kununua gari moja ambalo ni maalumu kwa ajili ya kusafirishia fedha?Uzuri wa magari kama hayo ni kwamba licha ya kutoa usalama mkubwa kwa mali inayosafirishwa,maisha ya wanaosafirisha mali hiyo nayo yanakuwa salama zaidi ukilinganisha na magari ya kawaida.Natambua kuwa yapo makampuni binafsi ya ulinzi ambayo yanamiliki magari ya aina hiyo.Lakini siwezi kuilaumu NMB moja kwa moja kwa kutokodi huduma hiyo kwa vile kumbukumbu zinaonyesha kuwa siku za nyuma walinzi wasio waadilifu walishawahi kuingia mitini na mamilioni ya fedha wakiwa katika gari maalumu la kusafirishia fedha.

Hata hivyo,kuwa na gari maalumu la kusafirishia fedha bila kuwa na watumishi waadilifu ni sawa na kulala ukiwa kwenye chandarua chenye dawa lakini kimekufunika kuanzia kichwani hadi kiunoni tu,na hapohapo kuamini kuwa unawadhibiti mbu.Uaminifu,uadilifu na kuthamini maisha ya wenzetu ni vitu muhimu sana na lazima kwa kila Mtanzania.

Alamsiki

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.