Showing posts with label BONGOFLEVA. Show all posts
Showing posts with label BONGOFLEVA. Show all posts

5 Mar 2012


ngoma inaitwa AGAIN and AGAIN,
msanii ni SEMY PAGE toka kundi la Macube rymers,akiwa amemshirikisha msanii BIG BOSS
ngoma imetengenezwa kwenye studio za M LAB producer akiwa Kanye Mujwahuki
hii ni nyimbo yake ya kwanza kama solo artist baada ya kutoka na ngoma ya kundi iliyokwenda kwa jina la HIRA.



Picha,Caption na Track kwa hisani ya DJ CHOKA

16 Mar 2009












KIPINDI CHA INSIDE AFRICA CHA CNN WIKI HII KINA SEGMENT KUBWA KUHUSU TANZANIA.MOJA YA YALIYONIVUTIA KATIKA KIPINDI HICHO NI MAHOJIANO KATI YA RIPOTA WA CNN,DAVID MCKENZIE, NA MSANII WETU NAKAAYA SUMARI.MWANADADA ALIJIELEZA CONFIDENTLY.I WISH NINGE-RECORD VIDEO LAKINI KWA SABABU ZILIZOKUWA NJE YA UWEZO WANGU NILIAMBULIA PICHA HIZO HAPO JUU.UKIPATA WASAA UNAWEZA KUCHEKI VIDEO YA SEGMENT HIYO KWENYE TOVUTI YA CNN-INSIDE AFRICA PINDI WATAKAPOIWEKA (HADI MUDA HUU BADO HAIJAWEKWA).PENGINE BAADA YA KUANGALIA SEGMENT NZIMA UNAWEZA KUBAKI NA MASWALI,LIKE I DID, KUHUSU ASSESSMENT YA RIPOTA HUYO WA CNN KUHUSU MWENENDO WA UCHUMI WETU.



19 Jan 2008

Siku chache zilizopita nilizungumzia kuhusu "afya" ya muziki wa Bongofleva.Dhamira ya makala hiyo ilikuwa ni kuwaamsha wahusika na kuwakumbusha kwamba japo ni vizuri kula matunda ya jasho lao,wanapaswa kuwa makini wasije kujikuta wanakata kabisa na mimea inayotoa matunda hayo.

Leo napenda kuzungumzia nafasi ya muziki huo katika kuleta mabadiliko kwenye jamii.Nilisoma mahala flani kuhusu lawama dhidi ya rapa maarufu huko Marekani,Jay-Z,baada ya kutoa albam yake mpya ya American Gangster.Katika makala hiyo,mwandishi alimlaumu Jay-Z kwamba sehemu kubwa ya albam hiyo ilikuwa imetawaliwa na "meseji za kawaida za marapa"...kujisifia kwingi,blings,warembo,nk.Mwandishi huyo alidai kwamba alitegemea,katika nafasi yake kama mmoja ya majina makubwa ya Weusi nchini Marekani, Jay-Z angeelekeza jitihada katika "kuzisaidia 'hoods katika mapambano ya ukombozi wa kweli wa mtu Mweusi".Anyway,sijapata fursa ya kusikia nyimbo zote zilizo katika albam hiyo,kwahiyo siwezi ku-comment lolote katika hoja ya mwandishi huyo.Hata hivyo,alichokisema kina mantiki kuhusiana na muziki wetu huko nyumbani.

Wasanii wa bongofleva na wale wa aina nyingie za muziki (kama taarabu na muziki wa dansi) ni miongoni mwa waathirika wakubwa wa ufisadi.Wengi wao hugeuzwa,ashakum si matusi,mithili ya "kondom za kisiasa".Hapo namaanisha kwamba baadhi ya wanasiasa huwatumia wasanii hawa wakati wa kampeni zao za kusaka uheshimiwa lakini wakishapata madaraka huwapuuza kabisa wasanii hao waliowapigia debe.Ni mithili ya kondom,ambayo kwa kawaida huonekana yenye umuhimu mkubwa (kwa wale wanaojali) kabla ya tendo la ndoa,lakini hugeuka takataka baada ya kutumika.

Wapo watakaodai kwamba wanasiasa wana haki ya "kukatisha" mahusiano na wasanii hao kwa vile huwaalika kwenye kampeni baada ya kuwalipa.Hoja hiyo inaweza kupingwa na ukweli kwamba fedha au malipo sio kila kitu (money isn't everything).Chukulia mfano wa mwalimu.Anapokufundisha anafanya hivyo kwa vile ni mwajiriwa wa taasisi ya elimu,na analipwa kila mwezi kukupatia elimu,achilia mbali uwezekano kwamba unalipia (ada) elimu hiyo.Lakini (pamoja na kupuuzwa kwao) walimu wanaendelea kushikilia nafasi muhimu katika jamii kwani ndio wafunguzi muhimu wa jitihada za binadamu katika kukabiliana na mazingira yake.Mfano mwingine ni wazazi.Wametuzaa,kutulea na kutusapoti katika makuzi yetu.Wapo wanaoweza kudai kuwa huo ni wajibu wao.Lakini tunafahamu kwamba wangetaka,wangeweza kabisa kzuia ujio wetu duniani (kwa baba na mama kuamua kutokuwa na watoto zaidi,kabla sie hatujazaliwa,au hata kutoa mimba zilizosababisha tuzaliwe).Tunaendelea kuwajali wazazi licha ya ukweli kwamba uzazi ulikuwa ni jukumu lao.Mifano hiyo miwili inaweza kulinganishwa na hoja yangu kwamba malipo yoyote yanayofanywa baada ya kutendewa kitu kikubwa hayawezi kulinganishwa na thamani ya matendo hayo.For that matter,fedha yoyote inayotolewa kama malipo kwa wapiga debe kwenye kampeni ya mwanasiasa haiwezi kulingana na mchango wa wapiga debe hao.

Nirejee kwenye kichwa cha habari cha post hii.Wengi wetu tunamfahamu Masudi Kipanya,mchora katuni maarufu huko nyumbani.Katuni zake nyingi huzungumzia matatizo yanayoikabili jamii ya Watanzania,na kwa hakika amekuwa mwiba mkali kwa wanasiasa wababaishaji na mafisadi.Anafanya kazi halisi ya sanaa kwani sanaa ni kioo cha jamii.Kwa bahati mbaya,wasanii wa muziki (hususan bongofleva) wamekuwa "wapole" sana katika mapambano dhidi ya maovu katika jamii yetu.Unakumbuka tungo kama Wauguzi ya Wagosi wa Kaya,au Ndio Mzee ya Profesa Jay?Hizi zilikuwa zina ujumbe mzito ambao kwa hakika ulikuwa unawakilisha kilio cha jamii.Tatizo kubwa la muziki wetu ni kwamba umetawaliwa sana na mada ya mapenzi.Hakuna ubaya kuzungumzia mapenzi,lakini yayumkinika kusema kwamba ili mapenzi yaende vema,shurti kuwe na kitu tumboni,barabara ya kufika kwa mpenzio iwe inafikika kirahisi,ukifika kwao usiku kuwe na mwanga (kwa maana ya upatikanaji wa umeme)....yaani hoja hapa ni kwamba mapenzi yanastawi vema pale huduma muhimu kwa maisha ya binadamu zinapopatikana kwa ufanisi.Ufisadi ni moja ya sababu kuu zinazokwamisha upatikanaji wa huduma hizo,na kwa sababu hiyo,wasanii wenye mahaba na dhima ya mapenzi kwenye tungo zao wana kila sababu ya kupambana nao (ufisadi) kwani vinginevyo wanachokiongelea kitaendelea kuwa ndoto za kujiliwaza tu.

Wapo wasanii ambao wana sababu za ziada za kupambana na mafisadi.Hawa ni pamoja na wale walioporwa wapenzi wao ambao walirubuniwa na nguvu ya fedha za mafisadi.Na kila msanii ana sababu nyingine ya kukabiliana na mafisadi (wadosi) wanaowalipa ujira mdogo ilhali wao (wadosi) wanatengeneza mamilioni ya bure.Ununuzi wa kazi za wasanii zinategemea hali ya kipato cha wateja wao (ikizingatiwa kwamba wengi wenye uwezo wa kiuchumi wako bize sana na masuala yao mengine kuliko kusikiliza tungo za nyumbani,na mafisadi wako bize zaidi na kuimarisha mikakati yao ya kulikamua taifa,kuangalia maendeleo ya miradi yao na kuboresha nyumba zao ndogo),kwa hiyo wasanii wana wajibu wa kushiriki mapambano ya kuboresha maisha ya wateja wao wakuu (wengi wao wakiwa waathirika wakuu wa ufisadi).

Tunahitaji akina (Masudi) Kipanya wengine kwenye bongofleva na miziki mingine kushirikiana na wale wote walio katika mapambano dhidi ya ufisadi huko nyumbani.Kelele za aina yoyote dhidi ya wahalifu (mafisadi) hao zitasaidia angalau kuwakumbusha kwamba tamaa na furaha zao ni kilio kwetu.

Hebu msikie Skinnyman anavyolalamika katika clip hii ya Council Estate of Minds kuhusu hali halisi ya maisha kwenye maghorofa (yaliyosahaulika,na makazi maarufu ya watu wa kipato duni) ya manispaa (Council estates)


22 Aug 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum wasomaji wapendwa wa gazeti hili maridhawa.

Leo nina mada nzito na nakuomba msomaji uifatilie kwa makini kwa manufaa ya Taifa letu.Labda kabla “sijaivaa” mada hiyo nitoe mfano mmoja wa hapa Uingereza.Miongoni mwa matatizo makubwa ya kijamii yanayoikabili nchi hii ni suala la matumizi ya madawa ya kulevya hususan miongoni mwa vijana.Watu wanabwia unga kama hawana akili nzuri.Kipindi hiki cha summer nacho kinasaidia kupata “jeshi jipya la wabwia unga" hasa kwa vile baadhi ya vijana huenda mapumzikoni (summer holiday) nje ya nchi wakiwa mbali na wazazi wao.Ukisimuliwa vituko vinavyotokea pwani za sehemu kama Hispania (kwa mfano Ibiza,Majorca na kwingineko) utabaki mdomo wazi.Hata hivyo,serikali na taasisi nyingine zimekuwa zikifanya jitihada kubwa kupambana na tatizo hilo japokuwa mafanikio si makubwa sana.

Kwa huko nyumbani tatizo naliona kubwa sana zaidi ya kubwia unga ni matumizi ya bangi.Sijui ni kwa vile madhara ya bangi ni ya polepole zaidi ya kubwia unga,au sijui kwa vile bangi imezoeleka sana,ukweli unabaki kuwa hatua madhubuti dhidi ya uvutaji bangi hazijatiliwa mkazo sana na vyombo husika.Kwa bahati mbaya sijaona utafiti wowote rasmi uliofanywa kuonyesha ukubwa wa tatizo hili,lakini naamini pindi utapofanyika matokeo yake yatakuwa ya kutisha.

Kuna kundi maalumu nitalolizungumiza hapa:wasanii hususan wale wa Bongofleva.Nilipokuwa huko nyumbani nilijaribu kufanya utafiti usio rasmi kujua msanii gani anatumia bangi na nani hatumii.Kwa kuwa utafiti huo haukuwa rasmi naomba nisitoe “takwimu” zangu lakini ukweli ni kwamba bangi imekuwa ina wafuasi wengi sana miongoni mwa wasanii wetu.Unajua tatizo mojawapo la uvutaji bangi ni kwamba huwezi kujificha iwapo ni mtumiaji.Kuna vitu flani-flani huwa havifichiki pindi mtu akishapuliza majani hayo haramu.Ilinishtua nilipogundua kuwa karibuni robo tatu ya wasanii wa kundi flani maarufu huwa hawawezi kutumbuiza jukwaani bila kupata misokoto kadhaa ya bangi.Jamani,hii sio hadithi ya kutunga au Isidingo bali ni hali halisi.Kwa bahati mbaya,watu hawajali sana.Na ndio maana hata kwenye tungo za baadhi ya wasanii maarufu wa Bongoflava unasikia bangi ikitajwa kwa namna ya kusifiwa utadhani imekuwa chai.Sintotaja majina ya watu hapa lakini kwa harakaharaka nimesikia nyimbo tatu,mbili kati ya hizo zikiwa zimeimbwa na msanii mmoja ambapo baadhi ya maneno ni kama “mimi nina kijiti cha…na wewe leta kijiti cha …” (kijiti ni bangi,na ukisikia kijiti cha mwanza basi inamaanisha bangi inayotoka mwanza),nyingine kuna maneno “…nitembezee chata…” (kutembeza chata ni kupasiana bangi) na msanii mwingine hakuona aibu kusema waziwazi “…pobe nakunywa,bangi navuta…”Wahusika wanaweza kujitetea kwamba hizo ni nyimbo tu na wao hawatumii kilevi hicho lakini haihitaji PhD kujua kwamba mtu hawezi kusifia kitu kibaya kama hakitumii au kukipenda.

Miongoni mwa hofu zangu kuhusu matumizi ya bangi kwa baadhi ya wasanii ni kwamba mara nyingi (kwa mujibu wa utafiti wangu usio rasmi) baada ya kuvuta bangi na kutumbuiza,msanii husika hujikuta “akizidishiwa ulevi” kwa ofa za pombe kutoka kwa mashabiki au wapambe.Lakini pia kuna watu wanaoitwa “groupies” ambao mara nyingi ni akinadada ambao wanamwandama msanii na wako tayari kufanya lolote kumridhisha msanii huyo.Sasa mtu akishakuwa na “cocktail” ya bangi na pombe,je akipewa ofa ya tendo la ndoa na “groupie” kondom inakumbukwa kweli?Lakini hilo ni tatizo dogo ukilinganisha na lile la “utaahira”.Najua ni vigumu kumshawishi mvuta bangi aamini kuwa bangi inachangia katika kuleta madhara kwenye ubongo,lakini ukweli ndio huo.

Naomba ieleweke kwamba simaanishi kuwa wasanii wote ni wavuta bangi bali pointi yangu ni kwamba ulevi huo haramu umepata wafuasi wengi kwenye fani kama wanavyosema wenyewe.Nawajua wasanii kadhaa ambao wanajiheshimu ambao wanaelewa kuwa licha ya bangi kuwa ni kitu haramu pia ina madhara kwa afya ya mvutaji.Kwenye utafiti wangu “bubu” niligundua kwamba miongoni mwa sababu zinazowafanya baadhi ya vijana kujiingiza kwenye utumiaji wa bangi ni hoja ya kipuuzi kwamba “inaleta kujiamini na hisia za ubabe!!!”Nilidokezwa na rafiki yangu mmoja aliewahi kufanya “shooting” ya video ya tangazo flani lililokuwa limemhusisha msanii mmoja wa “mkoani” kwamba nusura amwombe bosi wake atafute mtu mwingine wa kutokea kwenye tangazo hilo kwa vile msanii huyo alibugia misokoto kama minane hivi siku waliyokuwa wanajiaandaa na shooting hiyo.

Sasa nyie vijana,na hasa baadhi ya wasanii,mnaoendekeza uvutaji bangi mkae mkielewa kwamba mnajitafutia matatizo kwenye maisha yenu.Lakini pia wakati umefika sasa kwa uvutaji bangi kuonekana kama tatizo sugu linalohitaji kutupiwa jicho kali.Wale wanaovuta bangi kwa kisingizio cha “imani zao za kidini” (ndio,wapo wanaodai kuwa wao ni marastafari na bangi ni majani matakatifu) watambue kwamba wanavunja sheria na wakati huohuo wanatuletea uwezekano wa kuwa na mataahira siku za mbeleni.Watambue kuwa nchi yetu ni masikini na wakati huu ambao jitihada zinaelekezwa katika kupambana na majanga kama ya ukimwi wao wanatuongezea mzigo mwingine wa kukabiliana na tatizo la uchizi unaosababishwa na weed (bangi).

Alamsiki

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.