Showing posts with label BUSH. Show all posts
Showing posts with label BUSH. Show all posts

6 Nov 2008


20 Feb 2008

Makala yangu katika toleo la wiki hii la gazeti la Raia Mwema inazungumzia UHURU.Inaanza kwa kuhabarisha kuhusu tangazo la Uhuru wa Kosovo,kisha inachambua "urafiki mpya" wa Marekani na China kwa Bara la Afrika na kuhitimisha kwamba urafiki huo ni mithili ya Mkutano wa Berlin 1884-5 ulioligawa bara la Afrika miongoni mwa wakoloni.Makala hii inakumbushia pia kwamba kuna uwezekano ziara ya Bush barani Afrika ikabaki kumbukumbu muhimu kwake kutokana na namna alivyonyenyekewa katika kipindi ambacho ni mmoja ya marais wanaochukiwa sana katika sehemu mbalimbali duniani,na very unpopular nyumbani kwake US of A.Kadhalika makala inawashikia bango Mwanyika na Hosea kwamba wajiuzulu haraka sana,sambamba na wale wote waliotajwa kwenye ripoti ya Tume ya Mwakyembe.Pamoja na makala nyingine zilizokwenda shule ya hali ya juu,bingirika na makala hiyo kwa KUBONYEZA HAPA.

9 Sept 2007

Asalam aleykum,

Joji W.Bush anafahamika kama rais wa taifa lenye nguvu zaidi ulimwenguni.Lakini Bush ni maarufu pia kwa “kuchapia” maneno.Juzijuzi alimshangaza Malkia Elizabeth alipomshukuru kwa ziara yake ya “mwaka 1776”! kabla hajajikosoa yeye mwenyewe baada ya kugundua kwamba ameboronga.Wiki iliyopita alirudia tena “mchemsho wake” huko Australia.Kwanza alimshukuru John Howard,waziri mkuu wa Australia,pamoja na nchi yake kwa mchango wa jeshi la “Austria” huko Iraki (ni kweli majina ya nchi mbili hizo yanachanganya lakini si vigumu kubaini kwamba moja iko bara la Ulaya na nyingine iko Oceania).Na hakuishia hapo.Alianza hotuba yake moja kwa kumshukuru Howard kwa ukarimu wake na kuwa mwenyeji mzuri wa kikao cha OPEC (ilhali ukweli ni kwamba Australia ilikuwa mwenyeji wa kikao cha APEC).Lakini “machale” yalimcheza na kurekebisha haraka “blunder” hiyo.OPEC ni “Organization of Petroleum Exporting Countries” (ambapo Australia haijawahi kuwa mwanachama) wakati APEC ni kifupi cha “Asia Pacific Economic Co-operation”.Ukidhani ngoma iliishia hapo basi umekosea kwani Bush alijikuta akijiumauma kwenye kutamka jina la kikundi kimoja cha kigaidi cha Jemmiah Islamia.Na katika hotuba yake hiyo alimwacha kiongozi mmoja kutoka ukanda wa Pacific akitabasamu baada ya “kulichapia” jina lake.Huyo ndio Joji Bush!!!

Tukiwa bado kwenye anga hizo,majuzi Osama bin Laden alitoa hotuba yake ya “kuadhimisha” mashambulizi ya kigaidi ya September 11,2001 huko Marekani ambapo takriban watu 3000 walipoteza maisha.Katika hotuba hiyo Osama alikuwa akiongea kama mwanasiasa flani ambapo pamoja na mambo mengine aliwataka Wamarekani kujiunga na Uislam,alizungumzia pia “upinzani” wa baadhi ya wanasiasa wa Marekani katika suala la “global warming” na kugusia baadhi ya matatizo ya ndani ya uchumi wa nchi hiyo.Ikumbukwe kwamba Osama hajawahi kusikika hewani tangu mwaka 2004,na kujitokeza kwake kumezua maswali zaidi kuliko majibu.Nilikuwa naangalia kipindi cha “Late Edition” cha Wolf Blitzer wa CNN ambapo alimdadisi msaidizi mmoja wa White House kwamba je haoni kwamba kwa miaka sita tangu Osama na Al-Qaeda yake wafanye mashambulizi yao huko Marekani bado gaidi huyo sio tu kuwa yuko hai bali pia anajaribu ku-“influence” siasa za Marekani (mfano kwa kuwahubiria kuhusu “madhambi” ya viongozi wao).Wapo wanaodhani kwamba “kosa” la msingi katika msako dhidi ya Osama na kuiteketeza Al-Qaeda lilikuwa katika kuelekeza nguvu nyingi dhidi ya Saddam Hussein (ambaye madai kwamba anashirikiana na Al-Qaeda yalikuja kubainika kuwa sio sahihi) badala ya kukazania kwenye jitihada dhidi ya “adui halisi” Osama na wafuasi wake.Taarifa kutoka huko Afghanistan hazitoi picha nzuri kwani inaelekea kwamba washirika wakuu wa Al-Qaeda,kikundi cha Taliban,wamekuwa wakijiimarisha vizuri na huenda wakawa na nguvu kama walizokuwa nao kabla ya uvamizi dhidi ya Afghanistan uliiongozwa na Marekani.Na moja ya mambo yanayowaumiza vichwa watengeneza sera wa nchi mbalimbali ni hofu ya uwezekano wa Osama,Al-Qaeda,Taliban na vikundi vingine vya kigaidi kupata silaha za maangamizi ya halaiki (kwa mfano za kikemikali au kibaiolojia).Hofu hiyo inachochewa zaidi na ukweli kwamba mbio (kama zile za zama za Vita Baridi ) za kutengeneza na kuongeza uzalishaji wa silaha za nyukilia zimekuwa zikiongezeka kwa kasi.

Ukiachia Mataifa “yenye ruhusa” ya kumiliki nguvu za nyuklia (kwa mfano Marekani na Israel) mataifa mengine yaliyolazimisha “haki hiyo” (kwa mfano Pakistan na India) yanaendeleza kasi ya uzalishaji huku nchi kama Iran ikilazimisha kwa nguvu kujiunga na “klabu hiyo ya nyuklia.” Wajuzi wa mambo wanabashiri kwamba kuna uwezekano mkubwa wa nchi kama Misri na Saudi Arabia nazo kujikuta zinalazimika kuingia kwenye harakati hizo (inaaminika kuwa Saudi Arabia iko mbioni kununua silaha za nyuklia iwapo tishio inaloliona kutoka Iran halitadhibitiwa).Lakini hofu hiyo inaongezeka pia kutokana na taarifa zinazodai kwamba Russia imekuwa ikizidisha uzalishaji wa silaha hizo,na kutokana na mazingira ya kihistoria na sababu za kiuchumi,nchi hiyo inaweza kuuza teknolojia na silaha za nyuklia kwa “mikono isiyostahili” (wrong hands).Je kuna uwezekano kwa nchi kama Iran,China au Russia kuuza uwezo wa kinyuklia kwa kikundi kama Al-Qaeda?Jibu langu ni hapana.Kwanini?Kwa vile naamini nchi hizo zina busara ya kutosha ya kutofanya kosa la aina hiyo ambalo pia linaweza kuwagharimu hata wao.Je kuna uwezekano wa vita vya kinyuklia kati ya taifa moja na jingine?Sidhani kama uwezekano huo ni mkubwa sana japo upo kwa mbali.Je kuna uwezekano wa shambulizi la kikemikali au kibaiolojia litakalofanywa na kikundi cha kigaidi?Jibu la kutisha ni kwamba uwezekano huo upo kwani malengo ya mashambulizi yanayofanywa na vikundi hivyo yamekuwa ni kusababisha vifo vingi,na silaha gani ni bora zaidi katika kuleta madhara ya juu kabisa zaidi ya silaha hizo.Na inajulikana kwamba vikundi vya kigaidi vimekuwa vikihangaika sana kupata teknolojia na silaha za aina hiyo.Hiyo ndio dunia tunayoishi sasa.

Tuangalie mambo yalivyo huko nyumbani.Habari zinazovuma kwa sasa ni madai ya rushwa kwenye mchakato kuelekea kwenye uchaguzi ndani ya CCM.Naamini kuwa wanaofuatilia makala zangu wanafahamu bayana msimamo wangu dhidi ya rushwa na wala rushwa.Lakini niseme bayana kwamba madai ya rushwa kwenye uchaguzi huo hayanishangazi hata kidogo.Nadhani tatizo liko kwenye mkanganyiko wa suala zima la matumizi ya fedha katika harakati za kisiasa.Sidhani kama niko peke yangu katika kuamini kwamba nchi yetu inaimba wimbo wa Ujamaa ilhali staili ya kucheza wimbo huo ni ya Ubepari.Na ukiangalia kwa mfano namna mbio za kuelekea Ikulu ya Marekani hapo mwakani utabaini kwamba matumizi ya fedha ni makubwa sana.Tofauti yao na sisi ni kwamba kuna utaratibu maalumu uliowekwa katika namna gani mtu anaweza kuchangisha fedha,kutoa misaada au zawadi au hata namna ya kutoa fedha kwa ajili ya kujiimarisha kisiasa.Mantiki nyepesi ni hii: ukiwa unahitaji nafasi flani basi yayumkinika kusema kwamba utatumia kila nyenzo uliyonayo kuhakikisha unapata nafasi hiyo.Kinachodhibiti matumizi mabaya ya nyenzo hiyo ni sheria zinazotekelezeka na kufuatiliwa kwa makini.Wanachofanya watoa rushwa katika mchakato huo wa uchaguzi wa CCM ni kutumia “nyenzo” (fedha) walizonazo.Wanaofanya hivyo wanajua bayana kwamba kutumia uwezo sio kosa alimradi kama wanazingatia sheria zinazotawala zoezi zima.Lakini hawajali sana kuhusu kuvunja sheria kwa vile kwa namna flani mazingira yanawapa nafasi ya kufanya hivyo.Rushwa ni kama mmea,unastawi pale tu kwenye ardhi yenye rutuba.Inahitajika busara ya namna flani kuelewa nachomaanisha hapa vinginevyo unaweza kunishangaa kwa kudhani natetea matumizi ya rushwa kwenye jamii yetu.

Mwisho ni habari mbili za kusikitisha zilizojiri mwishoni mwa wiki.Ya kwanza ni matokeo mabaya ya Taifa Stars.Katika hilo naweza kuwafariji Watanzania wenzangu kwamba hata hapa Scotland,ambapo wana kila nyenzo wanayohitaji,timu yao ya taifa imehangaika kweli kufika ilipo sasa.Mafanikio ya Taifa Stars hayawezi kupatikana “overnight.” Tujifunze kwa hawa wenzetu ambao kwao matokeo mabaya ni changamoto ya kujipanga vyema kwa ajili ya mashindano yajayo.Hilo linawezekana kama kutakuwa na subira,uvumilivu na mipango bora.Kutambua ugonjwa,kupata dawa ya ugonjwa huo na kuitumia dawa husika ni hatua tu ya kuelekea kupona,haimaanishi kuwa ugonjwa utaondoka dakika hiyohiyo.Inaweza kufikia wakati ikalazimu kubadili dawa.Tuwe na subira,tutafika.Habari ya pili ni vifo vya Watanzania wenzetu katika ajali huko Mbeya.Hivi maisha ya wenzetu yataendelea kupotea hadi lini?Mbunge Shabbiby aliongea bungeni kuhusu “usanii” unaofanywa na baadhi ya wamiliki wa mabasi ambapo wanapandikiza bodi mpya za mabasi hayo kwenye chasis za zamani au za malori.Simaanishi kuwa basi lililopata ajali ni miongoni mwa yaliyofanyiwa usanii huo lakini kinachosikitisha ni kwamba mamlaka husika bado hazijaanza kufanyia kazi ushauri wa Mbunge huyo.Lakini eneo jingine linalopaswa kurekebishwa kwa haraka ni sheria za usalama barabarani.Semina lukuki na maadhimisho ya kila mwaka ya wiki ya “nenda kwa usalama barabarani” hayawezi kuepusha ajali zinazopoteza maisha takriban kila wiki pasipo kuzisimamia kwa makini sheria zilizopo.Yule “mzalendo” aliyekuja na wazo la “spidi gavana” alikuwa na busara sana lakini sijui mkakati huo umefia wapi!!!Tukiendelea kuamini kuwa spidi gavana bora ni madereva na askari wa trafiki basi, “unfortunately”,habari za kuhudhunisha kuhusu ajali zitaendelea kutusumbua kwa muda mrefu.

Alamsiki

22 Aug 2007

Asalam aleykum,

Nianze na habari “nyepesi nyepesi.” Kwa mujibu wa utafiti ambao matokeo yake yalinukuliwa na gazeti la Daily Mail la hapa Uingereza,kioo kinaweza kuwa na majibu kuhusu hali ya afya ya binadamu.Inaelezwa kwamba “kujishangaa” kwenye kioo kwa muda flani kunaweza kukupatia tetesi kuhusu dalili za matatizo ya kiafya katika mwili wako.Pengine hii itakuwa habari njema zaidi kwa baadhi ya akinamama ambao,kama wengi wetu tujuavyo,huweza kutumia hata nusu saa wakijiangalia kwenye vioo,hususan kabla ya kufanya “mtoko” (kwenda kwenye harusi,kitchen party,ubarikio,nk).Mie ni miongoni mwa “wazembe” ambao naweza kupitisha hata siku tatu bila kujiangalia kwenye kioo (na pengine siko peke yangu).Lakini kwa mujibu wa utafiti huo,kujiangalia kwenye kioo japo kwa muda michache kunaweza kubainisha matatizo ya kiafya kama vile maambukizo ya bacteria,kupanda kwa “cholesterol”, “anaemia”, “arthritis”,upungufu wa Magnesium mwilini,mshtuko wa moyo na hata kubaini ujauzito.Kwa mfano,ukijitazama kwenye kioo na kubaini kuwa macho yamekuwa meupe kuliko kawaida,basi hiyo inaweza kuwa dalili ya kuzidi kwa “cholesterol” mwilini;macho yakiwa yamevimba pasipo sababu inaweza kuwa dalili ya maambukizo ya bacteria au pengine “arthritis”;kope (“eyelids”) zinazoonekana kama zinataka kunyonyoka zinaweza kuashiria dalili za “anaemia”;jicho linalozunguka bila kuzungushwa (“myokymia”) linaweza kuashiria upungufu wa Magnesium;kupauka kwa rangi ya mwili kunaweza kumaanisha dalili za homa ya manjano au matatizo ya maini;fizi zinazotoka damu zinaweza kuashiria “leukaemia” au ujauzito;na mipasuko kwenye “lips” kunaweza kuashiria kisukari.Hata hivyo,kama yalivyo matokeo ya tafiti nyingi,matokeo ya utafiti huu kuhusu “faida za kioo katika kubaini hali ya mwili” hayamaanishi kuwa kila dalili utakayoiona kwenye kioo (kati ya hizo zilizotajwa) basi lazima inaashiria ugonjwa flani.Ni dhahiri kwamba mtu “akilamba” mzinga mzima wa “Mzaramo” (Konyagi) basi siku inayofuatia anaweza kuwa na macho yaliyovimba,na wala si dalili za “arthritis” au maambukizo ya bacteria (sidhani kama bacteria wana jeuri ya kumudu makala ya Konyagi.,,natania tu!).Lakini nadhani licha ya kujiangalia kwenye kioo kwa madhumuni ya kujua kama “reception” (sura) iko maridhawa,kujitazama mwenyewe kwenye kioo kunaweza kukusaidia kujisuta kama umefanya jambo baya,kujipongeza kama umefanya jambo zuri na hata kujishauri pale unapokuwa njia panda kutokana na matatizo au ugumu wa kutoa maamuzi.

Na utafiti mwingine kwa mujibu wa jarida la Saikolojia ya Uchumi (the Journal of Economic Psychology) watu wenye sura nzuri wana uhakika wa kipato kizuri zaidi kushinda wale wenye “sura mbaya.” Wachumi James Andreoni na Ragan Petrie wanaeleza kwamba katika kuangalia mafanikio ya kipato kati ya watu wenye sura nzuri na wale wasio na sura nzuri wamebaini kuwa hata pale watu wa makundi hayo mawili wanapofanya jitihada zinazolingana,wengi wa wenye sura nzuri “wanaibuka kidedea”.Watafiti hao wanaamini kwamba kinachowasaidia wenye sura nzuri kuwa na mafanikio ni ukweli kwamba watu wa aina hiyo huwa na matarajio makubwa ambayo wangependa yawe na matokeo mazuri yatakayoshabihiana na sura zao nzuri.Pia walibaini katika utafiti huo kwamba watu wenye sura nzuri wakizembea “kulinda uzuri wao” (kwa mfano kutojiweka “sopu-sopu” au kuongezeka “nyama za uzembe”) basi wale wanaonekana “wabaya” kwa sura wanapata nafasi ya “kuwapiga bao” (kuchukua nafasi za) hao wenye sura nzuri.Swali nililobaki nalo baada ya kusoma taarifa hizo ni kwamba nani ana mamlaka ya kusema flani mzuri au flani mbaya,pengine kwa kuzingatia msemo wa Kiswahili kwamba “apendae,chongo huona kengeza” au hata pengo kuitwa mwanya.

Pia,siku chache zilizopita wanafunzi kutoka nje ya Uingereza tulipata habari iliyowaacha baadhi ya “wenyeji” wetu wakiwa wamenuna.Kwa mujibu wa Dokta Bernard Lamb,msomi (reader) wa “genetics” kutoka Imperial College London,wengi wa wanafunzi wa kigeni wanaonekana kukimudu vema Kiingereza kuliko wanafunzi wazawa (Waingereza),ambapo wageni hao huwa na makosa machache wanapoandika au kuongea lugha hiyo ulinganisha na hao wenye lugha yao.Dr Lamb alieleza kwamba wanafunzi kutoka nchi za Singapore na Brunnei ndio wanaoongoza kwa ubora wa Kiingereza japokuwa lugha hiyo sio yao ya asili (ni second language).Amesema kwamba sio jambo gani kwa wanafunzi wazawa kuandika kwenye insha zao maneno kama “there” pale inapopaswa kuwa “their” au “bean” pale inapopaswa kuwa “been,” au kutamka “effect” badala ya “affect” na “sun” badala ya “son,” au badala ya wingi (plural) ya “tomato” kuwa “tomatoes” wao wanachapia “tomatos” na badala ya “theories” kama wingi wa “theory” wao wanaibuka na “theorys.” Msomi huyo anadai kuwa udhaifu mkubwa uko kwenye sarufi (grammar) na vituo (punctuation),na sasa anaandaa kitabu cha kuziumbua mamlaka za elimu kwa kuzembea kuweka mkazo kwenye kuboresha somo la Kiingereza mashuleni.

Kadhalika,moja ya mambo yaliyotawala anga za siasa za ndani za Marekani ni tangazo la mpanga-mikakati mkuu (“chief political strategist”) wa rais Bush,Karl Rove,kuwa anajiuzulu mwishoni mwa mwezi huu.Huyu jamaa ana akili sana,tena sana.Tayari wapo wanaodai kuwa hakuna mtu mwenye uwezo wa kuziba pengo lake hapo White House baada ya kuondoka kwake.Inategemea unazungumza na mtu aliye upande gani wa mjadala,kwani kuna watu wanaomtuhumu Rove kwa “kumpotosha” Bush katika maamuzi mbalimbali,na wanadai kuwa kupungua kwa umaarufu wa urais wa Bush (huko Marekani kila baada ya muda flani huwa zinatolewa “ratings” za utendaji kazi wa rais, “congress”,nk na kwa sasa wanaorodhishwa na utendaji kazi wa Bush ni asilimia 32.9 tu huku asilimia 62.4,yaani zaidi ya nusu ya Wamarekani,hawaridhishwi na utendaji kazi wake) kumechangiwa kwa kiasi kikubwa na swahiba huyo wa Bush.Lakini,mpende au mchukie,mwanamikakati huyu ni mtu mwenye kipaji cha hali ya juu katika kuhakikisha ushindi unapatikana kwa kila aina ya mbinu.Na ndio maana haishangzi kuona baadhi ya watu wakijiuliza kama kutatokea mtu mwenye kipaji kama cha Karl Rove.Yayumkinika kusema kuwa kujiuzulu kwake kumekuja wakati mbaya kwani ripoti inayosubiriwa kwa hamu kutoka kwa kamanda wa majeshi ya Marekani huko Irak,Jeneral David Petraeus,kuhusu mwenendo mzima wa vita ya Irak inatarajiwa kuwasilishwa katikati ya mwezi ujao,na wapo wanaodhani kwamba kukosekana kwa Rove katika kipindi hicho muhimu kunaweza kuwa ni tatizo kwa Bush iwapo ripoti hiyo itakuwa siyo nzuri.Rove ambaye anaelezwa kama mtu atakayengia kwenye vitabu vya historia kama kiumbe asiye na huruma (ruthless) linapokuja suala la kufanikisha matakwa ya kisiasa ya bosi wake,na ambaye alipachikwa jina la utani la “the Architect” (msanifu) kutokana na ufanisi wake kwenye sanaa ya kupanga mikakati,alimsaidia Bush kupata ugavana wa jimbo la Texas mwaka 1994,kabla ya lutoa mchango wa hali ya juu katika ushindi wa Bush kwenye chaguzi za urais za mwaka 2000 na 2004.Japo naweza kuwa miongoni mwa wale wanaoamini kuwa kuna maeneo ambayo “alimpotosha” Bush,na ukweli kwamba tofauti na nguli huyo,mrengo wangu kisiasa ni wa kati ya kushoto (Centre-Left),nimetokea kumhusudu sana Karl Rove (na nadiriki kumwita “role model” katika malengo yangu ya mbeleni).Ukipata nafasi ya kusoma kitabu kiitwacho “Boy Genius: Karl Rove, the Brains Behind the Remarkable Political Triumphs of George W Bush” au “Bush's Brain: How Karl Rove Made George W. Bush Presidential” unaweza kuungana nami “kumkubali” huyu jamaa.

Mwisho,napenda kuwapongeza watani wetu wa jadi Yanga kwa kunyakua kombe la Tusker.Nimesikia “rambirambi” zao kwamba fedha inayotolewa na waandaaji wa mashindano hayo haikidhi gharama halisi walizoingia hadi kufikia hatua ya fainali,lakini nadhani walipaswa kutafakari suala hilo kabla ya kuanza mashindano hayo.Licha ya “kuukosa ubingwa” (haituumi kwa vile hatukufungwa bali tulijitoa) wana Msimbazi tunafarijika na hilo “contract” la nguvu la kuitangaza “chata” ya kimataifa ya “ADDIDAS.” Simba ina bahati na wadhamini,pengine kutokana na rekodi yake nzuri kwenye mechi za kimataifa,lakini ni muhimu kwa Kaduguda na wenzie kuhakikisha kuwa udhamini huo unasaidia katika kutimiza ndoto ya Watanzania kuona vikombe vya michuano mikubwa ya vilabu barani Afrika vinatua nchini.

Alamsiki

18 Jun 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum,

Mwaka juzi gazeti maarufu duniani la TIME lilimtangaza George W.Bush kuwa “mtu wa mwaka (2004)” –au “Person of the Year” kwa lugha ya kwa mama.Katika uchambuzi wake kuhusu Bush,gazeti hilo lilimnukuu Rais huyo wa Marekani akisema kwamba “inapotokea kuwa hoja au mawazo yako yanazua mjadala au upinzani basi ni dalili kwamba yana uzito…kwa maana yangekuwa ya kipuuzi wala watu wasingejishughulisha nayo.”Alikuwa anazungumzia upinzani anaokumbana nao katika utendaji wa kazi zake za kila siku.Sio siri kuwa Bush anachukiwa na watu wengi hata ndani ya nchi yake.Lakini japo mie sio shabiki wake,namhusudu kwa jinsi anavyoweza kufanya mawazo yake yakubalike hata kwa wale ambao aidha hawayapendi au hawaafikiani nae.

Mwaka jana wakati nakuja huko nyumba,nilibahatika kukaa kiti kimoja na mama mmoja wa Kimarekani.Ni mtu mwongeaji sana,nami niliitumia nafasi hiyo kumdadisi siasa za Marekani hasa kuhusu mgawanyiko mkubwa wa kiitikadi nchini humo baina ya wale wa mrengo wa kulia(conservatives) na wale wa mrengo wa kushoto (liberals).Mwanamama huyo ambaye alinifahaisha baadaye kuwa ni mwanaharakati wa mazingira,alieleza kuwa kwa kiasi kikubwa mgawanyiko huo unachangiwa na siasa za Bush na maswahiba zake kama Dick Cheney,Donald Rumsfield,Paul Wolfowitz,na wengineo ambao wanajulikana kiitikadi kama “neo-conservatives” (sijui wanaitwaje kwa lugha yetu ya Taifa!).Miongoni mwa imani za hawa jamaa ni kuhakikisha kuwa Marekani inatumia ipasavyo nafasi yake kama Taifa lenye nguvu kabisa duniani.Kwa maana hiyo,ni “haki” yake kutumia “ubabe” wake kikamilifu ikiwa ni pamoja na kuvamia zile nchi zinazoonekana kuwa “korofi”.Ipo siku nitawazungumzia kwa kirefu jamaa hawa ambao takriban wote ni wadau wa taasisi moja isiyo ya kiserikali iitwayo “The Project for The New American Century” (Mradi wa Karne Mpya ya Marekani,kwa tafsiri isiyo rasmi).Turudi kwa yule mama.Basi akanambia kuwa japo yeye binafsi ni mpinzani wa Bush na hao neo-conservatives wenzake kuna wakati huwa “anamzimia sana” kutokana na jinsi anavyoweza kufanya maamuzi yake yatekelezwe hata pale kwenye upinzani mkubwa.Waingereza wana msemo “kama humuwezi unayeshindana nae basi bora uungane nae tu,”na ndio maana hata wale wasioafikiana na Bush mwishowe hujikuta hawana jinsi bali kuendana na mawazo au maamuzi yake.

Muda mfupi uliopita nilipata ujumbe kutoka kwa rafiki yangu flani aliyeko huko nyumbani akinijulisha kuwa kuna mwandishi mmoja ameandika makala katika gazeti flani la kila siku (la hapo Bongo) kupingana nami katika hoja ya makala yangu moja ya hivi ambayo nilimfananisha Rais Jakaya Kikwete na kiongozi wa chama cha Conservatives cha hapa Uingereza,David Cameron.Kwa mujibu wa ujumbe niliopata,mwandishi huyo aliyepingana nami anadai sikuwa sahihi kuwalinganisha wanasiasa hao .Kwa bahati mbaya hadi natayarisha makala hii nilikuwa sijapata hoja zote zilizotolewa kukosoa makala yangu.Kwa mantiki hiyo itakuwa vigumu kujibu hoja baada ya hoja bali nachoweza kusema kwanza ni kwamba makala ya mwandishi huyo ni uthibitisho tosha kuwa gazeti hili la KULIKONI ni kipenzi cha wengi,na ndio maana linazaa hoja na makala katika magazeti mengine.Pili,kama gazeti la TIME lilivyomnukuu Bush naamini makala yangu hiyo ilikuwa na uzito ndio maana ikamsukuma mwandishi huyo kuijadili japo hakuafikiana na nilichokiandika,kwa kuwa laiti ingekuwa ya kipuuzi asingepoteza muda wake kupingana nayo.”

Kwa faida ya mwandishi huyo,Kikwete anashabihiana sana na David Cameron katika maeneo flani.Kwa mfano,wote wawili wako katika vyama ambavyo kabla ya wao kushika hatamu za uongozi kwa kiasi flani vilikuwa vinaonekana kama ni vya “wateule wachache” tu.Ushindi wa tsunami kwa Kikwete ni dalili tosha kuwa hata baadhi ya wanachama wa vyama vya upinzani walimpigia kura kuonyesha kuwa kuteuliwa kwake kuwa mgombea urais kuliiongezea nguvu CCM.Hoja nyingine japo inaweza kuwa si nzito sana ni kwamba wanasiasa hao wana sifa inayofanana ya kuwa handsome,na kwa taarifa yako u-handsome unalipa sana kwenye siasa.Lakini kingine ni lugha zao wanazotumia.Wanaongea lugha za watu wa kawaida wa mtaani,yaani wanajua wananchi wanatarajia nini kwao.Ndio,Cameron anafuata siasa za mrengo wa kulia kuelekea kati (right-centre) na Kikwete kama mwana CCM nadhani atakuwa ni wa siasa za mrengo wa kushoto kuelekea kati (left-centre),na japo Cameron ni Mwingereza na Kikwete ni Mtanzania,la muhimu hapa ni jinsi wananchi wanavyowahusudu kutokana na utendaji wao.Kura za maoni hapa Uingereza zinaonyesha kuwa Cameron amempiku Tony Blair kwa kupendwa na wananchi na naamini kuwa hata kama Watanzania wataamshwa usingizini kupiga kura za maoni,Kikwete ataibuka kidedea kwa sana.Kwenye siasa umaarufu wa mwanasiasa haugemei sana kwenye itikadi zake au chama chake,sehemu aliyozaliwa au umri wake bali kukubalika kwake miongoni mwa wananchi,na hicho ndicho kilichonipelekea kuwafananisha wanasiasa hao.

Mwisho,siamini kuwa mwandishi wa makala hiyo alikuwa anatafuta umaarufu kupitia makala yangu au gazeti hili la KULIKONI,bali alikuwa anatumia haki yake ya kikatiba kutoa mawazo yake.Nampa changamoto aendelee kusoma gazeti hili ilimradi isiwe kwa nia ya kupinga kila kitu hata kama ameishiwa na hoja.Kama alivyoimba Mista Two (Joseph Mbilinyi) kwenye wimbo wake “Sugu” kwamba huwezi kuizuia mvua kunyesha,KULIKONI ni kama jua na mvua,halizuiliki.

Alamsiki.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.