Showing posts with label CHADEMA. Show all posts
Showing posts with label CHADEMA. Show all posts

20 Aug 2015

KAMA nilivyoahidi katika makala iliyopita, wiki hii ninaendelea na uchambuzi wangu kuhusu Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25 mwaka huu.
Na kama ilivyokuwa katika makala kadhaa zilizotangulia, uchambuzi wangu utaelemea kwenye kinyang’anyiro cha nafasi ya urais.
Wakati katika makala iliyopita nilijadili fursa na vikwazo kwa wagombea ‘wakuu’ wawili, yaani Dk. John Magufuli wa CCM na Edward Lowassa wa Chadema/UKAWA, wiki hii nitaingia kwa undani zaidi, huku lengo likiwa kuitumia makala hii kufanya uchambuzi kwa mgombea mmoja, na makala ya wiki ijayo itamwangalia mgombea mwingine.
Nianze na Lowassa wa Chadema/UKAWA. Kati ya makala iliyopita na hii, si siri kuwa habari inayotawala zaidi ni kile kinachoitwa ‘mafuriko ya Lowassa’. Shughuli zote zilizomhusisha mwanasiasa huyo katika kipindi hicho kimeandamana na umati mkubwa mno wa watu, kuanzia alipochukua fomu za kuwania urais jijini Dar es Salaam hadi katika mikutano ya kutambulishwa huko Mbeya, Arusha na Mwanza.
Wingi wa watu wanaojitokeza katika shughuli zinazomhusu Lowassa, iwe ni kwa kuandamana au kuhudhuria mikutano, kumewapa matumaini makubwa wafuasi wake kwamba njia ya Waziri Mkuu huyo wa zamani kuelekea Ikulu ni nyeupe.
Sambamba na mahudhurio hayo makubwa, wanachama kadhaa wa CCM wamehama chama hicho tawala na kujiunga na Chadema. Lakini kubwa zaidi ni kuhama kwa baadhi ya viongozi ‘ waliokuwa na majina’ ndani ya CCM.
Kwamba maandamano na mikutano ya Lowaasa inajaza watu wengi mno, hilo halina mjadala. Kwamba matukio yajayo ya mwanasiasa huyo yataendelea kujaza watu pia si suala la mjadala. Kadhalika, kwamba kuna wanachama na viongozi zaidi wa CCM watamfuata Lowassa huko Chadema pia ni jambo la kutarajiwa.
Tusichoweza kuhitimisha kwa uhakika muda huu ni iwapo hamahama hiyo ya baadhi ya wana-CCM na viongozi wao kumfuata Lowaasa huko Chadema itaweza kutafsiriwa katika ushindi katika uchaguzi mkuu ujao hapo Oktoba 25, takribani miezi mawili kutoka sasa.
Licha ya uwepo wa hamasa kubwa kuhusu kujiandikisha katika daftari za wapigakura lililoboreshwa na teknolojia ya kuhifadhi rekodi kwenye kompyuta (Biometric Voter Register kwa kifupi BVR), hadi muda huu Tume ya Taifa ya Uchaguzi haijatoa idadi kamili ya watu waliojiandikisha.

Lakini licha ya hilo, tayari kuna dalili za kasoro katika suala la BVR ambapo zimepatikana taarifa kadhaa za waliojiandikisha kutoyaona majina yao wakati wanaofanya uhakika. Ukubwa au udogo wa kasoro hiyo bado haujafahamika kwa vile Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) haijalitolea ufafanuzi suala hilo.
Hapa nitaunganisha masuala hayo mawili ya hapo juu, yaani idadi kubwa ya watu wanaojitokeza katika shughuli za Lowassa na zoezi la kujiandikisha BVR.
Yayumkinika kuhitimisha kuwa ili wingi wa watu wanaojitokeza katika shughuli za mwanasiasa huyo ziwe na manufaa kwake na chama chake kwa ujumla, basi, kwanza wengi wa watu hao, kama si wote, lazima wawe wamejiandikisha kupiga kura. Bila hivyo wingi wao utabaki kuwa historia tu.
Lakini kwa uzoefu tulionao wengi, kujiandikisha kupiga kura ni suala moja, kufanikiwa kupiga kura ni suala jingine, na kumpigia kura mgombea fulani na kura hiyo kumsaidia ashinde ni suala jingine kabisa.
Nimeshazungumzia katika makala zangu zilizotangulia kuwa moja ya faida kubwa kwa CCM ni mahusiano ya upendeleo kati yake na taasisi mbalimbali za umma. Na ninatarajia wengi wenu ndugu wasomaji mmekuwa mkisikia vilio vya wanasiasa wa upinzani takribani tangu kuanza kwa mfumo wa vyama vingi kwamba wanaohisi kura zao zinahujumiwa na chama tawala kwa kusaidiwa na taasisi za umma ‘zinazokipendelea’ chama hicho.
Japo mara zote tuhuma hizo zimeendelea kubaki kuwa tuhuma tu, ushahidi wa kimazingira unaelekea kuzisapoti tuhuma hizo.
Binafsi, nimekuwa nikifuatilia pilika za uchaguzi mkuu kupitia mtandaoni, hususani kwenye mitandao ya kijamii (social media). Majuzi, niliwatahadharisha mashabiki wa Lowassa kuhusu furaha yao inayotokana na wingi wa wahudhuriaji katika shughuli za hadhara zinazomhusu mwanasiasa huyo.
Niliwakumbusha kuhusu chaguzi zilizopita, hususan ‘kasi ya (Agustino Lyatonga) Mrema,’ aliyekuwa mgombea urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka 1995 kupitia chama cha NCCR-Mageuzi, jinsi alivyokuwa maarufu na kujaza halaiki ya watu kwenye mikutano yake, lakini akaishia kubwagwa na mgombea wa CCM, Benjamin Mkapa.
Niliwakumbusha pia kuhusu wingi wa watu waliojitokeza katika mikutano ya kampeni za Dk. Willibrord Slaa, aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema katika uchaguzi mkuu uliopita, mwaka 2010, lakini akishindwa na mgombea wa CCM, Jakaya Kikwete.
Katika chaguzi zote hizo, pamoja na ule wa mwaka 2000 na 2005, kulikuwa na malalamiko kdhaa kuwa ‘CCM iliiba kura,’ lakini tuhuma hizo zilijifia zenyewe kutokana na kutokuwepo ushahidi halisi, sambamba na vikwazo vya kikatiba kupinga matokeo ya Urais.

Lakini kukumbushia yaliyojiri katika chaguzi hizo kulipelekea mimi kushambuliwa vikali, nikituhumiwa kuwa na ‘chuki binafsi’ dhidi ya Lowassa, huku wengine wakinituhumu kuwa nimenunuliwa na CCM. Na nikakumbushwa kuwa “nenda na wakati, hii ni 2015, achana na habari za 1995”.
Siwezi kuwalaumu watu ambao hawataki kusikikia lolote ‘baya’ kuhusu Lowassa, au jambo linaloweza kuwa kikwazo kwake kupata urais.
Kwa bahati mbaya, ujio wa mwanasiasa huyo huko Chadema unaoonekana kuwabadili wana-Chadema wengi, angalau huko mtandaoni, ambapo watu waliokuwa wakijadili hoja kiungwana, sasa wamekuwa mahiri wa matusi kwa kila anayeelekea kumpinga Lowassa.
Nitawalaumu kwa matumizi ya matusi badala ya kujenga hoja za kistaarabu, lakini sintowalaumu kwa kuwa ‘desperate.’ Wanasema mtu akielemewa na mafuriko basi atang’ang’ania hata unyasi ili ajiokoe.

CCM imewafikisha Watanzania wengi katikia hali hii tunavyoshuhudia. Sapoti kubwa kwa Lowassa sio kwa vile ni mchapakazi au anatarajiwa kuleta ‘miujiza’ bali ni kukata tamaa miongoni mwa Watanzania wengi, Tunasikia watu wakisema “ukiiweka CCM na jini, nitapiga kura yangu kwa jini”.
Lakini wakati kuwa na matumaini yanayotokana na kukata tamaa si tatizo sana, ni muhimu kuzingatia hali halisi. Kuna wanaodai ‘safari hii CCM haiwezi kutuibia kura’ Je kuna tofauti gani ya kimazingira ya uchaguzi katika ya mwaka huu na uchaguzi mkuu wa mwaka 1995,2000,2005 na 2010? Tume ya uchaguzi ni ileile, taasisi mbalimbali za umma zinazoshughulikia uchaguzi huo bado zipo vilevile, na vyombo vyetu vya dola bado vina ‘mentality’ ileile ya kuwaona Wapinzani kama wahaini, na hata Lowassa amekiri kuwa alipokuwa CCM alidhani vyombo vya dola vyalaumiwa bure tu na Wapinzani…hadi alipoonjeshwa ‘jeuri ya polisi’ hivi majuzi.
Lakini tukiweka kando kuhusu tatizo hilo ambalo niliona kama la kimfumo, yaani mfumo unaoipendelea CCM, kuna tatizo jingine ambalo pengine halijawa kubwa sana. Hili ni uwezo mdogo wa Lowassa katika kujieleza.
Unapofanikiwa kukusanya umati wa maelfu ya watu, kisha ukahutubia kwa dakika tano, na katika muda huo mfupi usiseme lolote la maana la kuwafanya waliohudhuria wakumbuke si ukubwa wa umati bali uzito wa hotuba ya aliyewajaza kwa wingi mahala husika, basi hapo kuna tatizo.
Na tatizo hili laweza kuwa turufu kwa mgombea wa CCM, Dk. Magufuli, ambaye anasifika kwa umahiri si tu wa kuongea bali kutoa takwimu nyingi kichwani kana kwamba ni mashine yenye kumbukumbu (memory) kubwa.
Ukizungumzia hilo kwa wana-Chadema/UKAWA, wanasema “nani anataka hotuba? Sisi tunachotaka ni kuondoa CCM tu”. Ninabaki ninajiuliza, “hivi wakifanikiwa ukiondoa CCM, nini kitafuata?” Sipati jibu.
Kwa kifupi, kinachowapa matumaini wana-Chadema/UKAWA na mashabiki wa Lowassa ni hayo ‘mafuriko.’ Iwapo yataweza kujitafsiri katika kura, muda utatupatia jibu (time will tell).
Na iwapo ‘mafuriko’ hayo yatamwezesha Lowassa kuingiza Ikulu, ninadhani hata wana-Chadema/UKAWA wengi hawajui jinsi gani atakavyowezesha kubadili kile kinachowafanya Watanzania wengi wachukizwe kuhusu CCM.

Kwa upande mmoja, kuahidi mabadiliko ni kitu kimoja, kutekeleza ahadi hiyo ni kitu kingine. Kwa upande mwingine, kuwa na nia ya kuleta mabadiliko ni kitu kimoja, uwezo wa kufanikisha nia hiyo ni kitu kingine, na hata pale nafasi ya kuleta mabadiliko inapopatikana, nyenzo na mazingira vyaweza kuwa kikwazo cha kutimiza azma hiyo.
Nihitimishe makala hii kwa kuahidi kuendelea na uchambuzi huu katika toleo lijalo ambapo nitamzungumzia mgombea wa CCM, Dk. Magufuli kama nilivyomjadili Lowassa katika makala hii.

30 Jul 2015


Kama unavyoona hapo pichani juu, mara baada ya kusikia taarifa kwamba Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa anatarajia kujiunga na vyama vinavyounda Muunganowa Katiba ya Wananchi (UKAWA), niliandika tweet hiyo pichani. Kimsingi, binafsi nilishindwa kabisa kuamini kuwa Dkt Willibrord Slaa, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chadema hadi alipotangaza kujiuzulu, angeweza kukaa chama kimoja na Lowassa. Nilishindwa kabisa kupata picha kichwani kumwona Dkt Slaa akiwa jukwaani anamnadi Lowassa. Nilijaribu ku-imagine kwamba labda kwa vile kuingia kwa Lowassa Chadema kunaweza kukiingiza chama hicho na Ukawa Ikulu, na hivy pengine Dkt Slaa angeweza kumsapoti japo kwa shingo upande, lakini nafsini niliona huo sio tu ungekuwa muujiza - na mie si muumini wa miujiza - bali pia ungekuwa usaliti wa hali ya juu.


Siwezi kujisifu kuwa tweet hiyo ya 'kumsuta' Dkt Slaa imesaidia kumfanya achukue uamuzi huo wa kujiuzulu lakini ninachoweza kusema ni kuwa ninamshukuru kwa kufanya maamuzi magumu ya kujiuzulu hasa ikizingatiwa kuwa neno 'KUJIUZULU' halipo katika kamusi ya wengi wa wanasiasa wetu hata pale wakiwa wanaandamwa na kashfa. Lakini pia ninampongeza Dokta Slaa kwa kusimamia anachooamini.

Kwa hakika Dokta Slaa alisimama kidete kupigana kwa nguvu zake zote dhidi ya ufisadi. Na sifa kubwa ya mwanasiasa huyo ilikuwa umakini wake katika kuwasilisha hoja. Hakuwa mtu wa jazba wala mjivuni. Na kwa hakika alikuwa mwenye kuapanga hoja zake na kuziwasilisha kwa umakini mkubwa. Kwa kifupi, Dokta Slaa aliweza kuwasiliana na umma, iwe katika hotuba au maongezi kama DOKTA hasa, maana moja ya sifa ya usomi ni jinsi ya kuwasiliana na jamii kwa ufasaha.

Kuna watakaokuwa wamefurahi kuona Dokta Slaa amechukua hatua ya kujiuzulu, sio furaha ya kuungana naye kwa kuchukua uamuzi huo mgumu bali kwa vile aidha walikerwa na msimamo wake mkali dhidi ya mafisadi na ufisadi, au walimwona kama mmoja ya sababu zilizopokea Zitto Kabwe kung'olewa Chadema. Furaha hiyo ni ya 'kimburula' kwa sababu Dokta Slaa alikuwa mmoja wa wanasiasa wachache kabisa waliosimama kwa dhati na wanyonge kupigania haki zao. Ukimwondoa marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, sioni mwanasiasa mwingine yeyeote yule aliyewajali mno Watanzania kama Dokta Slaa. Na japo nina furaha kutokana na kukataa kushirikiana na Lowassa, na ninampongeza kwa kuwa na msimamo thabiti, kwa upande mwingine nina masikitiko makubwa kuona lulu hiyo ya taifa ikiachana na siasa wakati bado twaihitaji mno.
Dokta Slaa alifanya kazi yake kwa uadilifu mkubwa na kwa hakika kuna idadi kubwa tu ya Watanzania iliyoamini kuwa siku moja angeweza sio tu kuwa Rais wetu bali pia angeweza kuibadili Tanzania yetu. Na kwa kujiuzulu, amethibitisha ni mwasiasa wa aina gani. Badala ya kutanguliza maslahi binafsi na kujiunga na chama kingine cha siasa au kuanzisha chama chake, Dokta Slaa amechukua uamuzi wa kiungwana. Ametambua kuwa tatizo sio CCM pekee bali mfumo mzima wa siasa za Tanzania yetu, kuanzia chama tawala hadi huko Upinzani. Uamuzi wa kujiuzulu utamlindia hadhi yake milele. 

Mimi ni muumini mkubwa wa 48 Laws of Power, na ninaomba nitanabaishe jinsi uamuzi huo wa Dokta Slaa unavyoendana na baadhi ya Laws hizo. Law 34 of Power inasema (ninainukuu)

The way you carry yourself will often determine how you are treated: In the long run, appearing vulgar or common will make people disrespect you. For a king respects himself and inspires the same sentiment in others. By acting regally and confident of your powers, you make yourself seem destined to wear a crown.
Kwa tafsiri ya Kiswahili ni kwamba "Matendo yako ndio yatakavyofanya watu wakuchukuliaje. Katika muda mrefu, kuonekana mtu wa ovyo ovyo kutafanya watu wasikuheshimu. Kwa sababu mfalme hujiheshimu mwenyewe na kuhamasisha watu wengine kujiheshimu na kumheshimu. Kwa matendo makubwa na ya uhakika wa nguvu zako, utaonekana mtu stahili kushika hatamu." 
Na kwa hakika uamuzi wa Dokta Slaa kujiuzulu unamfanya aendelee kuwa sio tu mtu mwenye msimamo bali pia ataendelea kushikilia hadhi na heshima yake kama mtu aliyeuchukia ufisadi kwa dhati hadi kuamua kujiuzulu baada ya fisadi Lowassa kujiunga na UKAWA.
Kuna wanaoweza kumbeza kwa kusema amekimbia vita. Well, Law 36 of Power inatuasa, nanukuu,

...It is sometimes best to leave things alone. If there is something you want but cannot have, show contempt for it...
Kwa tafsiri ya Kiswahili, "Wakati mwingine ni vema kuacha vitu kama vilivyo Kama kuna kitu unakitaka lakini huwezi kukipata, kichukie tu." Na hicho ndicho alichokifanya Dokta Slaa. Alichukia ufisadi na kuwachukia mafisadi kwa dhati. Lakini ghafla akajikuta analetewa fisadi ashirikiane nae kupinga ufisadi. Waingereza wana msemo "You can't put a drug addict in charge of a pharmacy," yaani huwezi kulikabidhi teja liwe msimamizi wa duka la madawa (ambayo kwa kawaida yana madawa baadhi ya madawa kama Heroin ambayo ndio 'chakula' cha mateja). Kwa vyovyote vile, ingekuwa vigumu mno kwa Dokta Slaa kutimiza azma yake ya kupambana na ufisadi akiwa pamoja na Lowassa. Na ndio maana akaamua bora akae kando. Kama ninavyotamka mara kadhaa, huhitaji kuwa kiongozi ili ulete mabadiliko, kuwa raia mwema tu (You don't have to be a leader to bring change. Just be a good citizen).

Law 47 of Power inasema, ninanukuu,

The moment of victory is often the moment of greatest peril. In the heat of victory, arrogance and overconfidence can push you past the goal you had aimed for, and by going too far, you make more enemies than you defeat. Do not allow success to go to your head. There is no substitute for strategy and careful planning. Set a goal, and when you reach it, stop.

Kwa Kiswahili inamaanisha, "Ushindi unapowadia ndio wakati ambao unaweza kuangamia. Katikati ya ushindi, dharau na kujiamini kupita kiasi vyaweza kukusukuma zaidi ya lengo kusudiwa, na kwa kupitiliza lengo hilo, watengeneza maadui zaidi ya uliowashinda. Kamwe usiruhusu mafanikio kupanda kichwani mwako. Hakuna mbadala wa mkakati na mipango makini. Weka lengo, na ukilitimiza, simama."
Hakuna asiyefahamu alichotimiza Dokta Slaa katika mapambano yake dhidi ya ufisadi. Kubwa lilikuwa kuwaamsha Watanzania, na kwa hakika wengi wamefunguka macho dhidi ya ufisadi na wanauchukia kwa dhati. Angeweza kujikaza kisabuni na kusimama pamoja na Lowassa ili aendeleze mapambano dhidi ya ufisadi, lakini sote twafahamu ingekuwa vigumu mno. Na uamuzi wake wa kujiondoa madarakani ni sawa na inavyosema sheria hiyo hapo juu, 'ukitimiza leno, simama.'
Vilevile, Dokta Slaa amefuata vizuri Law 5 of Power inayoonya kuwa "So much dependes on reputation, guard it with your life," yaani "Hadhi ni kitu muhimu sana, ilinde kwa nguvu zote." Sasa, sote tulikuwa tukiitambua Chadema kama kiongozi wa vita dhidi ya ufisadi, lakini ghafla wametusaliti na kumkaribisha papa wa ufisadi katika chama chao. Kwa vile ni mtu makini na msafi, Dokta Slaa ameona kuwa kwa kufanya hivyo, Chadema imejishushia hadhi yake katika uongozi wa mapambano dhidi ya ufisadi, na akaamua kuilinda hadhi yake kwa kujitenga nao. 
Nimalizie makala hii kwa kurudia kumshukuru Dokta Slaa kwa yote aliyoitendea Tanzania yetu. Tunaouchukia ufisadi tutaendelea kumwenzi na kumkumbuka milele. Nitajitahidi huko mbeleni kufanya mawasiliano na Dokta Slaa ili ikiwezekana niweke kumbukumbu ya huduma yake bora kabisa kwa Watanzania kwa kuandika kitabu kinachomhusu. Nitawa-update kuhusu hilo.
MUNGU AKUBARIKI SANA DOKTA SLAA. TANZANIA ISIYO NA UFISADI INAWEZEKANA PASIPO HAJA YA KUWATEGEMEA MAFISADI. 



28 Jul 2015

Ninaipenda siasa...kama stadi  (study, yaani kuisoma), lakini kwa hakika ninapata shida sana na jinsi mengi ya ninayosoma katika stadi za siasa (political studies) yanavyogeuka inapokuja kwenye matendo au shughuli za kisiasa an zinazohusiana na siasa. 

Stori kidogo. Fani niliyotamani sana kuisoma na pengine kubobea ni utabibu. Nilitamani mno kuwa daktari. Lakini ndoto yangu ya udaktari ilipata kikwazo baada ya kupata matokeo ya mtihani wa kumaliza kidato cha nne. Japo nilipata A kwenye Kemia na C kwenye Baiolojia, niliambulia D kwenye Hisabati na kufeli kabisa Fizikia ambapo nilipata F. Na japo nilipata Division One, uwezekano wa kuchukua 'combination ya udaktari' yaani PCB (Fizikia, Kemia na Baiolojia) kidato cha tano uliathiriwa na hiyo F ya Fizikia. Uwezekano pekee ulibaki kwenye kujaribu combination ya CBG (Fizikia, Kemia na Jiografia) ambayo ingeniwezesha kuikwepa Fizikia.

Nilipojiunga na kidato cha tano katika sekondari ya wavulana ya Tabora (Tabora Boys') nikakumbana na vikwazo vingine. Kwanza, Kemia ya kidato cha kwanza mpaka cha nne ni tofauti kwa kiasi kikubwa na ile ya kidato cha tano na cha sita. Kuna kitu inaitwa Physical Chemistry ambayo kimsingi ni kama mchanganyiko wa Kemia, Hisabati na Fizikia. Sasa kama nilivyotanabaisha hapo awali, udhaifu wangu katika Fizikia na Hisabati ulimaanisha kuwa nisingeweza kuimudu Kemia ya High School.

Pili, shule yetu ilikuwa haina mwalimu ya Jiografia, na ilibidi tuwe tunakwenda shule ya jirani ya Tabora Girls' kuhudhuria vipindi vya somo hilo. Angalau Baiolojia haikuwa tatizo japo kiukweli ilihitaji uwezo mkubwa wa kukariri na kuelewa majina ya sampuli za viumbe ambayo mengi yana asili ya Kilatini au Kigiriki. Kwahiyo kwa kifupi, dhamira yangu ya kusoma combination ya CBG ilikufa kifo cha asili.

Hivyo nikaamua kusoma combination yenye masomo ya Historia, Jiografia na Kiingereza. Hii ilikuwa mteremko kwa kiasi kikubwa, lakini ndoto yangu ya kuwa daktari ndio ikayeyuka. Lakini wanasema kile unachotaka sio lazima ndio unachopata (what you wish for is not always what you get).

Sukuma miaka kadhaa baadaye, nikajiunga na chuo kikuu cha Dar es Salaam na hapo nikajikuta nina uchaguzi wa ama kuzamia kwenye sayansi za siasa na utawala wa umma (pilitical science and public administration au sosholijia, elimu inayohusu masuala yya jamii. Mwaka wa pili, nikafanya uamuzi wa kuchukua hiyo choice ya pili, yaani Sosholojia. Kwa hakika niliipenda sana sosholojia. Yaani ilinisaidia mno kuielewa jamii. Miongoni mwa masomo ya kupendeza sana yalikuwa lile lilifundisha kuhusu uhusiano wa jamii, utamaduni na afya; somo la jinsia na uhusiano wa kijinsia, na zaidi ya yote ni sosholojia ya dini ambapo pamoja na mambo mengine tulifundishwa kuhusu Ukristo, Uislamu na Imani za Asili. 

Sukuma miaka kadhaa zaidi mbele, nikapata skolashipu ya kuja hapa Uingereza kusoma Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (Politics and International Relations), mkazo ukiwa kwenye masuala ya usalama. Kwa vile skolashipu ni kama zawadi, mwanafunzi anakuwa hana uchaguzi. Nilitamani sana kuendelea na Sosholojia lakini sikupewa fursa ya kuchagua. Na hivyo ndivyo nilivyojikuta nikiingia kwenye stadi za siasa. Tuishie hapo/

Kwanini nimeelezea stori hiyo? Ni kwa sababu kama nilivyosema awali, ninaipenda siasa kama stadi. Yaani baada ya kutokuwa na choice ya kusoma sosholojia, na 'kulazimishwa' kusoma Siasa, ikabidi niipende tu. Niliipenda pia kwa sababu siasa za kimataifa zina 'raha' yake kuzielewa, ukichanganya na maeneo kama diplomasia, amani na 'ugomvi' (peace and conflicts) na masuala ya usalama wa kimataifa (international security).

Lakini tatizo la siasa kama stadi ni ukweli mchungu kwamba kile unachosoma darasani mara nyingi hakiakisi hali halisi mtaani. Siasa kama fani au stadi sio mbaya, ina mafunzo mengi, inafundisha miongozo mingi na kanuni nyingit muhimu kwa maisha ya mwandamu, lakini mtaani hali ni tofauti.  Sihitaji kuelezea kwa undani kwanini watu wengi wanaichukia siasa. Lakini mfano mwepesi ni kwenye kampeni za uchaguzi ambapo utasikia chama kikitanabaisha sera nzuri kabisa lakini baada ya kuingia madarakani kikaishia kufanya kinyume kabisa na kilichoyaahidi. Na kwa Tanzania yetu tuna mfano hai wa jinsi sera tamu za CCM zinavyoishia kuwanufaisha matajiri na mafisadi huku zikiwadidimiza walalahoi.

Na mfano mchungu zaidi, uliopelekea niandike makala hii, ni jinsi Chadema katika mwavuli wa UKAWA inavyoelekea kuwasaliti mamilioni ya Watanzania kwa uwezekano wa kumpokea fisadi Edward Lowassa kuwa mgombea wa urais.

Jana niliumia mno nilipoona picha kadhaa zinazomwonyesha Lowassa akiwa na viongozi wa UKAWA. Baadaye, mwenyekiti wa NCCR, moja ya vyama vinavyounda UKAWA pamoja na Chadema, CUF na NLD, alitamka bayana kuwa wanamkaribisha Lowassa kujiunga nao.

Lakini baadaye kidogo nikapata ahueni baada ya kupatikana taarifa zilizothibitishwa na akaunti ya Twitter ya Chadema Media kuwa picha zilizokuwa zinamwonyesha Lowassa na viongozi wa UKAWA ni feki, yaani zilikuwa photoshopped. Hata hivyo furaha hiyo haikudumu muda mrefu baada ya Mbatia na wenzake kutangaza bayana kuwa wanamkaribisha Lowassa . Na kuna uwezekano leo Jumanne, aidha UKAWA wakamtangaza Lowassa kuwa mgombea wao wa Urais au Lowassa mwenyewe akatangaza kujiunga nao.
Huu ni usaliti mkubwa mno hasa upande wa Chadema, chama kilichojidhihirisha kuwa kinauchukia ufisadi kwa dhati. Sote twakumbuka jinsi Chadema ilivyojipatia umaarufu kwa kupambana na ufisadi, hasa baada ya kutangaza hadharani 'orodha ya aibu' (list of shame) pale Mwembeyanga jijini Dar ambapo walitaja orodha ya mafisadi akiwemo Lowassa. Kadhalika Chadema ilifanya jitihada kubwa kuibua ufisadi mbalimbali ikiwa ni pamoja na skandali ya Richmond iliyopelekea Lowassa kujiuzulu Uwaziri Mkuu. Vilevile chama hicho kilitufumbua macho kuhusu ufisadi wa EPA, Meremeta, Dowans, Buzwagi, TanGold, Kiwira, nk. Kwa kifupi, ilikuwa haiwezekani kuzungumzia mapambano ya  ufisadi Tanzania bila kuitaja Chadema.

Na katika harakati zake za kupambana na ufisadi, kuna Watanzania wenzetu waliopoteza maisha yao na wengine kujeruhiwa vibaya na kuachiwa ulemavu kwa kukiunga mkono chama hicho. 


Na kwa kuonyesha kuwa Chadema ilikuwa mwarobaini kwa CCM na mafisadi kwa ujumla, chama hicho kilifanyiwa kila aina ya hujuma. Mara kiliitwa chama cha kidini, baadaye kikaitwa cha kikabila, na hadi hivi majuzi kiliitwa chama cha kigaidi. Lakini taratibu Watanzania walifumbuka macho na kubaini kuwa sababu kubwa ya CCM na serikali yake kuiandama Chadema ni kwa vile chama hicho cha upinzani kilichofanya vizuri tu katika uchaguzi mkuu uliopita kinasimamia maslahi ya wanyonge ilhali CCM inatetea mafisadi na ufisadi.
Japo mie binafsi sikuwa mwanachama wa Chadema, nilikiunga mkono kutokana na msimamo wake mkali dhidi ya ufisadi kulingana na msimamo wangu kwenye suala hilo. Nilikuwa nina imani kuwa laiti Chadema ikifanikiwa kuingia Ikulu basi kwa hakika safari ya kuipeleka Tanzania yetu mahali inapostahili kuwa inawezekana. 
Sasa hili la kumpokea Lowassa ni pigo kubwa mno na ni usaliti wa hali ya juu kabisa. Ndio, Lowassa anaweza kuwasaidia Chadema na UKAWA kuingia Ikulu. Lakini kwa kuangalia tu maswahiba wa Lowassa utaweza kujua tutakuwa na serikali ya aina gani. Sipati shida kubashiri kuwa tutaishia kuikumbuka CCM. 

Embedded image permalink

Na huo ndio ubaya wa siasa katika vitendo, tofauti na ilivyo nzuri na mwafaka katika stadi. Kwamba kistadi za siasa, Chadema ilijijenga na kupata umaarufu kwa kuzingatia kanuni ilizojiwekea na ikajitambulisha kama chama kilichopo kwa maslahi ya wanyonge, tofauti na CCM iliyokimbia kanuni zake na kuwakumbatia matajiri na mafisadi. Lakini ghafla bin vup, Chadema inaelekea kwenda kulekule ilipo CCM. 

Nimalizie makala hii kwa kuahidi kufanya uchambuzi wa kina kuhusu suala hili katika makala yangu ya wiki ijayo katika gazeti la Raia Mwema. Spoiler alert, wiki hii katika toleo litakalokuwa mtaani kesho ninamjadili Magufuli. 

Asanteni kwa kuchukua muda wenu kunisoma.

17 Jan 2014

KATIKA hitimisho la makala yangu iliyochapishwa wiki mbili zilizopita, iliyobeba kichwa cha habari ‘Ni mwaka wa siasa za hovyo CCM, CHADEMA, niliahidi kuendeleza utabiri wa mwaka huu 2014, kwa kuangalia anga za kimataifa.
Kwa bahati nzuri, siku nne tu baada ya kuchapishwa makala hiyo, moja ya mambo niliyotabiri - kuendelea kwa mgogoro wa CHADEMA na uwezekano wa migogoro ndani ya vyama vya upinzani kuwa ya hadharani - limetokea.
Ninaomba niweke bayana kuwa masikitiko yangu kuhusu maendeleo mapya katika mgogoro wa CHADEMA ni makubwa zaidi ya furaha yangu kuona nilichotabiri wiki iliyopita kweli kimetokea. Nitakuwa mbinafsi na mnafiki ‘kusherehekea usahihi wa utabiri wangu’ katika jambo lisilopendeza. Laiti ingekuwa ni chaguo langu basi ningetamani mabaya yote niliyotabiri yasitokee, lakini kwa bahati mbaya hali halisi haikwepeki.
Takriban wiki mbili zilizopita, Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA) Zitto Kabwe alirusha ‘bomu zito’ ambapo alitoa tuhuma kubwa na hatari dhidi ya Mwenyekiti wake taifa wa chama hicho, Freeman Mbowe, na chama hicho kwa ujumla. Pengine ili kuleta ladha halisi ya alichosema Zitto ni vema nikanuu ‘waraka’ mzima kama ifuatavyo:
"Lissu anasema nimepewa magari 2 na Mzee Mkono. Anasema kaambiwa na Mkono. Naamini Mkono alimwambia pia mwaka 2005 alimpa Freeman Aikaeli Mbowe tshs 40m ili Mbowe asifanye kampeni Musoma Vijijini.
“Nadhani alimwambia pia mwaka 2008 (baada ya orodha ya mafisadi kutangazwa 2007) Mkono alimpa Freeman tshs 20m za uchaguzi wa Tarime na Freeman akasema kwenye chama ametoa mkopo na akalipwa. Nadhani alimwambia pia kuwa mwaka 2010 Mkono alimpa Mbowe tshs 200m za kampeni ya Slaa.
“Pia hakusahau kumwambia kuwa Rostam Aziz alimpa Mbowe tshs 100m za kampeni. Lissu anajua kuwa gazeti la Tanzania Daima limeanzishwa na fedha za chama kutoka Conservative Party?
“Nimefanya internship yangu kwa Mkono and Company Advocates kuhusu masuala ya mikataba. Mzee Mkono ni Mzee wangu na alisaini petition ya kumtoa Waziri Mkuu Pinda. Lissu awaambie waliyemtuma wamwambie ukweli wote. Lissu ajue yeye ni kifaranga tu, Mimi namtaka mama wa kifaranga ajitokeze. Aeleze aliingia deal gani na Kinana na Sumaye mwaka 2005 kufuatia deni lake NSSF. Aweke wazi mkataba kati yake na NHC kuhusu nyumba ya umma ilipo Club Bilicanas.
“They must know I am not a push over. Chacha died, I won't. Mtu ambaye hawezi kuheshimu mke wake aliyemzalia watoto hawezi kunyooshea mtu kidole kuhusu maadili."
Zitto alibandika waraka huo katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Facebook, lakini kwa sababu anazojua yeye pekee, baadaye aliuhariri na kutojumuisha tuhuma hizo. Aidha kwa kutofahamu au makusudi, uhariri uliofanywa na mwanasiasa huyo katika waraka huo haukuzuia kusambaa kwa kasi mtandaoni.
Niliposoma waraka huo nilipatwa na mshtuko mkubwa, nikabaki ninajiuliza iwapo Zitto alikuwa ‘mzima’ wakati anaandika alichoandika.  Japo inawezekana alifanya hivyo kwa kuzingatia kile kinachofahamika mtaani kama ‘umemwaga ugali na mie namwaga mboga...bora tukose wote,” ukweli ni kwamba bandiko hilo lina madhara makubwa, kwa Zitto binafsi na kwa pengine ustawi wa CHADEMA kwa ujumla.
Madhara kwa Zitto ni ya kisheria zaidi. Tayari Mbowe ameonyesha nia ya kumburuza Zitto mahakamani kuthibitisha tuhuma hizo nzito. Bila kujali kuwa tuhuma hizo zina ukweli au la, mtu yeyote mwenye uelewa wa ‘dili za siri’ atafahamu kuwa ni vigumu kuzithibitisha kisheria, yayumkinika kuhisi kuwa Zitto atakuwa na kazi ya ziada katika ‘kesi’ hiyo (iwapo itafunguliwa).
Iwe ni tuhuma za Nimrod Mkono kumpa Mbowe shilingi milioni 260 katika mazingira ambayo si tatanishi tu bali pia kwa namna fulani ni hujuma dhidi ya CHADEMA, au Rostam Aziz kumpatia Mbowe shilingi milioni 100, au ‘dili’ kati ya Mbowe na Waziri Mkuu wa zamani, Frederick Sumaye na Katibu Mkuu wa CCM Abdulrahman Kinana, sidhani kama Zitto anaweza kuthibitisha tuhuma hizo iwapo Mbowe atatimiza azma yake ya kufungua kesi. 
Je, inawezekana kuwa kwa kutambua ‘kosa hilo la kisheria’ ndio maana muda mfupi baadaye Zitto alihariri ‘post’ hiyo? Wakati jibu analo Zitto mwenyewe, ukweli unabaki kuwa tuhuma hizo ni nzito mno, na iwapo ni za kweli basi zinapoteza kabisa hadhi ya CHADEMA.
Ikumbukwe kuwa katika waraka uliopelekea Zitto kuvuliwa nyadhifa zake mbalimbali ndani ya CHADEMA, walioandika waraka huo waligusia walichokiita ‘udhaifu wa wanayemtaka’ (wakimaanisha Zitto), na kudai, “Maneno yake mara nyingine hayazingatii anayazungumza katika mazingira gani na hivyo kuwasha masikio ya wanataasisi jambo linalompunguzia kukubalika kwake taratibu.” 
Kadhalika, walieleza kuwa; “Kuna wakati tunayemtaka (Zitto) hujibu kwa taharuki kubwa dhidi ya mashambulizi yanayoelekezwa kwake jambo linalomfanya achukue maamuzi yasiyo sahihi kwa wakati huo. Kwa kifupi kuna wakati tunayemtaka (Zitto) huonekana kufanya maamuzi kwa hisia zaidi badala ya kutulia kwanza na kutafakari kwa kina ikiwa ni pamoja na kutafuta ushauri kwa wenzake kabla ya kujibu.”
Ndugu msomaji, huhitaji kuwa mwanasaikolojia kuhisi kuwa huenda kilichomsukuma Zitto kuandika ‘waraka’ huo kwenye ukurasa wake wa Facebook ni kile Waingereza wanakiita “putting emotions in front of common sense”, yaani kwa tafsiri isiyo rasmi, kuweka mbele jazba badala ya busara.
Kwa kujaribu kuonyesha kuwa Mbowe si mwadilifu (kwa maana ya kupokea misaada kutoka kwa ‘wanasiasa kama Mkono na Rostam waliowahi kutajwa na CHADEMA kuwa ni mafisadi’), linakuja swali la msingi, kwanini Zitto alikalia kimya tuhuma hizo nzito kwa takriban miaka minane hadi sasa baada ya kuvuliwa madaraka? Hivi kuna neno stahili kuelezea hali hiyo zaidi ya unafiki?
Tukiamini tuhuma hizo za Zitto, je naye si sehemu ya ‘uhuni wa CHADEMA’ wa kukemea mafisadi hadharani ilhali pembeni wanapokea misaada ya watu hao hao wanaowatuhumu? Ninasema hivyo kwa sababu Zitto hakuwa katibu wa shina bali Naibu Katibu Mkuu (taifa)  wa chama hicho, na mbunge, na kwa vyovyote vile naye ni mnufaika wa fedha hizo ‘za mafisadi.’
Laiti angekuwa haridhii vitendo hivyo basi aidha angejitoa mhanga na kuweka ukweli hadharani wakati huo (na hiyo ingeweza kuzuia kurejea kwa vitendo kama hivyo) au angeweza kujiuzulu kwa kuona ‘chama chake kinashirikiana na watuhumiwa wa ufisadi. Kwa nini hakufanya hivyo? Jibu jepesi ni hilo nililoandika hapo juu: alikuwa mnufaika wa vitendo hivyo (iwapo kweli vilitokea, maana tayari baadhi ya aliowataja wamekanusha ‘kumpa msaada’ Mbowe).
Binafsi, ninadhani moja ya matatizo yanayomkabili Zitto ni wanaojiita au kujitambulisha kama wafuasi wake. Wengi kati yao ni wenye mapenzi na CCM, na ushabiki wao kwa Zitto ni wa kirafiki (kimaslahi?) zaidi. Ndio, tofauti za kiitikadi hazimaanishi uadui, lakini wengi wetu tunaufahamu msemo ‘nionyeshe marafiki zako na nitakwambia wewe ni nani,’ yaani mara nyingi watu wanaotuzunguka hutoa picha fulani kuhusu sisi wenyewe.
Lakini tatizo jingine kuhusu ‘wafuasi na marafiki hao wa Zitto’ ni kutokuwa washauri wazuri kwake. Ukisoma mengi ya wanayoandika, hususan huko kwenye mitandao ya twitter, utabaini kuwa kimsingi wanachofanya ni ‘kumvimbisha kichwa Zitto’ bila kutoa ushauri unaoweza kusaidia ustawi wa kisiasa wa mwanasiasa huyo kijana.
Na mfano wa hivi karibuni ni baada ya Zitto kubandika waraka huo wenye tuhuma nzito huko Facebook. Wengi wa wafuasi wake walionekana kuchekelea ‘Mbowe alivyoumbuka’ bila kujali athari za kisheria kwa Zitto na ustawi wa CHADEMA kwa ujumla (kwanini wajali ilhali wengi wao ni wanaCCM)?
Kwa wafuasi wa Zitto, mwanasiasa huyo ni majeruhi wa siasa za chuki na mizengwe ndani ya CHADEMA. Lakini kwa wengine, Zitto anaonekana kama mtu anayeendeshwa na ‘ego’ kubwa inayomfanya kujiona yeye ndiye-au zaidi ya- CHADEMA.
Ni vigumu kubashiri hatma ya maisha ya kisiasa ya Zitto lakini kwa hali ilivyo ni vigumu mno kuona mustakabali wake ndani ya chama hicho. Ninakumbuka mwanasafu mmoja wa gazeti hili alimshauri mwanasiasa huyo hivi karibuni kuwa suluhisho la busara kwake kwa sasa ni kutosubiri kuvuliwa uanachama, ajiondoe mwenyewe huko CHADEMA, na kuitaka Mahakama isiingilie kazi ya chama.
Mwisho, bado ninaamini kuwa Zitto ni mwanasiasa mzuri lakini pengine kwa upungufu wa kibinadamu au makusudi, washauri wabovu au sababu nyinginezo, hazingatii umuhimu wa busara hizi tatu katika medani ya siasa: moja, waweke marafiki zako karibu lakini waweke maadui zako karibu zaidi, na pili, hakuna marafiki au maadui wa kudumu katika siasa, na tatu, hakuna mwanasiasa anayeweza kuwa mbadala wa chama (hasa katika mazingira ya siasa zetu ambapo kwa kiasi kikubwa chombo pekee cha uongozi wa kisiasa ni chama cha siasa. Bila chama, mwanasiasa hata awe maarufu kiasi gani anabaki kuwa raia wa kawaida tu).
Katika waraka wake, Zitto aliandika, “They must know I am not a push over. Chacha died, I won't” (lazima wafahamu mie sio mtu wa ‘kupelekeshwa.’ Chacha (Wangwe?) alikufa, mimi sitokufa). Hiki ni kiburi, utoto au? Ni mwanadamu mwenye uhakika wa kutokufa? Nihitimishe kwa kumshauri kwamba labda kweli ana uhakika wa kuishi milele lakini kwa kutanguliza hisia badala ya busara, yayumkinika kubashiri kuwa anaweza kuwa anajiua mwenyewe kisiasa (committing political suicide).



28 Nov 2013


MAKALA hii ni mwendelezo wa ile iliyochapishwa katika toleo lililopita la gazeti hili, iliyobeba kichwa cha habari ‘Nani kinara wa CCM urais 2015?’
Lakini kabla sijaingia kiundani, nadhani ni vema nikarejea nilichoandika katika makala iliyopita kuhusu kukua kwa uwezekano wa CCM kubaki madarakani baada ya Uchaguzi Mkuu ujao. Wiki iliyopita ilishuhudia chama kikuu cha upinzani cha CHADEMA, kikiingia katika mtafaruku mkubwa ambao licha ya kutishia uhai wake unazidi ‘kupapalia’ mazingira mwafaka ya ushindi kwa CCM.
Awali, CHADEMA ilitangaza kuwavua madaraka viongozi wake waandamizi watatu, Zitto Kabwe, Dk. Kitila Mkumbo na Samson Mwigamba na kuwapa siku 14 kujieleza kwa nini wasivuliwe uanachama baada ya kupatikana kwa nyaraka inayodaiwa kulenga kukihujumu chama hicho.
Jumapili iliyopita, Zitto na Kitila waliitisha mkutano na waandishi wa habari ambao kimsingi haikusaidia japo kupunguza moto unaozidi ‘kuunguza nyumba ya CHADEMA.’ Kwa kifupi, wanasiasa hao wawili walipinga vikali shutuma zilizoelekezwa kwao na kuhalalisha kile kilichotafsiriwa na uongozi wa chama hicho kama hujuma, huku wao wakibainisha kama matumizi ya demokrasia kwa minajili ya kuiboresha CHADEMA.
Pasi haja ya kuingia kwa undani katika sokomoko hilo, ni wazi kwamba uamuzi wa kuwavua madaraka viongozi hao na msimamo uliotolewa na ‘wahanga’ hao unaendeleza mapambano ya madaraka ndani ya CHADEMA. Kubaki au kuondoka kwa akina Zitto hakuwezi kukirejesha chama hicho katika mahala kilipokuwa. Kibaya zaidi, japo hakuna tathmini yoyote iliyokwishafanywa kuhusu athari za mgogoro huo, ni wazi Watanzania wengi wameanza kupoteza matumaini kwa chama hicho kilichotarajiwa sio tu kutoa upinzani mkubwa kwa CCM bali pia hata kuweza kuingia Ikulu mwaka 2015.
Nihitimishe suala hili la CHADEMA kwa kutanabaisha kuwa japo inafahamika kuwa lolote linawezekana katika siasa, ukweli kwamba tumebakiwa na takriban mwaka na ushee tu kabla ya Uchaguzi Mkuu ujao, sambamba na ukweli kuwa hakuna dalili ya mgogoro huo wa CHADEMA kumalizika hivi karibuni, itakuwa vigumu mno kwa chama hicho kujipanga upya na vyema, kuweza kutoa ushindani wa maana katika Uchaguzi Mkuu ujao. Nitaijadili kwa kirefu hatma ya CHADEMA katika makala zijazo.
Tukiendelea na mada ya urais kwa tiketi ya CCM, niliahidi kuwa wiki hii nitajadili ‘odds’ (uwezekano wa kufanikiwa au la) zinazowakabili wanasiasa wawili ambao tathmini yangu inawaona kama ndio vinara katika mbio za kumpata mrithi wa Rais Jakaya Kikwete kupitia CCM, yaani Edward Lowassa na Bernard Membe.
Pengine hadi siku chache zilizopita, kikwazo kikubwa kwa wote wawili kingeweza kuwa uwezekano wa CCM kubwagwa na CHADEMA katika Uchaguzi Mkuu ujao. Lakini kwa kuzingatia mwenendo ulivyo katika chama hicho kikuu cha upinzani, yayumkinika kuhitimisha kuwa kikwazo hicho ni kama kimekufa kifo cha asili.
Kwa upande wa Lowassa, doa kubwa linaloonekana kuendelea ‘kuchafua’ jina na wasifu wake ni tuhuma za ufisadi wa Richmond. Bila kujali kuwa uamuzi wake wa kujiuzulu uwaziri mkuu kufuatia kashfa hiyo ni ‘kutolewa kafara’ au ‘alivuna alichopanda,’ tafsiri ya haraka kwa wananchi wengi wa kawaida inabaki kuwa ‘ni vigumu kumtenganisha mwanasiasa huyo na moja ya matatizo makubwa kabisa yanayoikabili nchi yetu, yaani ufisadi.’
Ukweli kwamba Tanzania yetu sio tu ni moja ya nchi masikini sana bali pia inazidi kuwa masikini huku ufisadi ukizidi kushamiri, umesababisha kujengeka kwa hisia (pengine zisizopendeza) kuwa kila mwenye uwezo wa kifedha ni fisadi. Hisia hizo hazimsaidii Lowassa ambaye kwa siku za hivi karibuni amekuwa mstari wa mbele katika harambee za kuchangisha mamilioni ya fedha hususan kwenye taasisi za dini. Badala ya ukarimu wake kumjenga kama kiongozi anayejali, kuna wanaotafsiri jitihada zake hizo kama ‘rushwa’ ya kutaka urais mwaka 2015.
Kadhalika, kuna hisia hasi kuwa hata hizo fedha anazotoa kusaidia miradi mbalimbali ‘ni chafu’ kwa maana ya hisia kuwa huenda ni zile zilizotokana na tuhuma za ufisadi. Kibaya zaidi, kutofahamika chanzo cha kinachotajwa kama utajiri mkubwa wa mwanasiasa huyo kunaimarisha hisia hizo za ufisadi.
Vile vile, na hili linawagusa wote-Lowassa na Membe- ukweli kwamba wanasiasa hao wanatajwa kama sehemu muhimu ya ‘mtandao’ uliomwingiza madarakani Rais Kikwete mwaka 2005, unaleta hisia za ‘mvinyo mpya kwenye chupa ya zamani’ (kwa wasiofahamu, thamani ya mvinyo inaelemea sana kwenye ‘ukale’ wake na si upya wake)
Sasa, kama tukiafikiana kuwa mtizamo wa Watanzania wengi ni kuwa utawala wa Kikwete (ambao uliingizwa madarakani na ‘mtandao’ uliowashirikisha Lowassa na Membe) umetawaliwa zaidi na tuhuma za ufisadi huku hali ya maisha ya Mtanzania ikizidi kuwa ngumu, kwa nini basi watu hao wapewe fursa ya kuboronga mambo zaidi?
Faraja kubwa kwa Lowassa (na hata Membe kwa ‘uhusika wake katika mtandao) kuhusu tuhuma za ufisadi ni ukweli mchungu kuwa Watanzania ni wepesi kusahau ‘mabaya.’ Wanasiasa wetu wengi wanafahamu kuhusu udhaifu huo ambao kwa kiasi kikubwa umewasaidia wengi kuendelea kuwapo madarakani licha ya ‘madudu’ yao.
Iwapo ‘kete ya fedha’ niliyobainisha katika makala iliyopita kuwa inamsaidia sana Lowassa itaendelea kutumika, basi kuna uwezekano mkubwa wa mwendelezo wa ‘who cares?’ (nani anajali?) ambapo mahitaji ya muda mfupi kama vile sukari, khanga, mchele na mengine kama hayo yatafunika mahitaji ya muda mrefu kama vile kuondokana na umasikini sambamba, kupambana na ufisadi, na hatma ya taifa letu kwa ujumla.
Kwa upande wa Membe, kikwazo kikubwa kwake ni kutokuwa maarufu ndani na nje ya CCM. Na ukubwa wa kikwazo hicho unatokana na ukweli kwamba ‘mpinzani’ wake, yaani Lowassa, ni mwanasiasa maarufu kuliko wote ndani ya CCM hivi sasa (bila kujali umaarufu huo ni stahili au la). ‘Wajuzi wa mambo’ wanaeleza kuwa inahisiwa Lowassa anaungwa mkono na zaidi ya asilimia 75 ya viongozi wa chama wenye uwezo wa kufanya uamuzi, huku wengi wao wakiwa watu waliofanyiwa fadhila zilizosababisha wawepo madarakani hivi sasa.
Tegemeo pekee kwa Membe dhidi ya Lowassa ni lile nililogusia katika makala iliyopita; nafasi ya Idara ya Usalama wa Taifa katika kumpata mgombea urais ajaye (ndani ya CCM). Kama kuna kitu chochote kinachoweza kumzuia Lowassa kuingia Ikulu, na pengine kumsaidia Membe kupata fursa hiyo, ni pale Idara hiyo itakapoamua ‘kumbeba mwenzao’ (Membe ni shushushu mstaafu). Na hilo si gumu kama inavyoweza kudhaniwa. Moja ya maeneo ambayo mashushushu wetu wanayomudu sana ni hujuma (sabotage) na uzandiki (subversion).
Ni hivi, kwa vile tayari kuna hisia za ‘uchafu’ kuhusu Lowassa (yaani tuhuma za ufisadi) basi haitokuwa vigumu kwa mashushushu kuzikuza na kuziendeleza katika namna ya kile kinachofahamika kama character assassination. Lakini kwa vile Lowassa bado yupo katika ‘himaya’ ya Idara ya Usalama wa Taifa (kama waziri mkuu wa zamani, anapatiwa huduma za ulinzi na Idara hiyo) ni rahisi kwa mashushushu kuibua mengi (ya kweli au hata ya kutunga) dhidi yake, iwapo wataona haja ya kufanya hivyo.
Kwa hiyo, kwa kifupi, kufanikiwa kwa Membe kutategemea kukwama kwa Lowassa. Na pengine katika hatua hii, ni vema nikitanabaisha waziwazi kuwa mwana-CCM anayeongoza katika kinyang’anyiro hicho ni Lowassa akifuatiwa kwa karibu kiasi na Membe.
Nihitimishe makala hii kwa kueleza kuwa mada hii ni endelevu, kwa maana ya kuwa nitaendelea na uchambuzi na mjadala huu kadri tunavyoelekea Uchaguzi Mkuu ujao. Hata hivyo, ninapenda kurejea tena mtizamo wangu kuwa CCM kurejea tena madarakani mwaka 2015 ni janga kwa Watanzania. Chama hicho tawala sio tu kimeishiwa na kila mbinu ya kuongoza nchi lakini pia hakipo kwa ajili ya maslahi ya Watanzania. Na kama uchambuzi huu ulivyoonyesha kuwa uwezekano mkubwa wa aidha Lowassa au Membe kuwa mgombea kwa tiketi ya chama hicho ni kwa aidha fedha au ‘sanaa za giza’, yeyote kati yao atakapopata urais hatokuwa tofauti na utawala uliopo madarakani hivi sasa ambao nao ulitumia mbinu ya ‘mtandao.’
Kwa bahati mbaya au makusudi, watu tuliodhani wangeweza kutusaidia kuiondoa CCM madarakani, yaani CHADEMA, wanaonekana kuwa ‘bize’ kupigana ngwala kugombea madaraka ndani ya chama chao. Sasa kama zoezi dogo tu la kupata uongozi wa chama linasababisha ‘watiane vidole machoni’ kwenye uongozi wa nchi itakuwaje? Ni ukweli mchungu lakini usioepukika na hivyo ni vema kujiandaa kisaikolojia kuendelea kuwa chini ya utawala wa CCM (ninatamani kuwa na suluhisho mbadala lakini sijalipata hadi muda huu)

Soma zaidi kuhusu:

- See more at: http://raiamwema.co.tz/nani-kinara-wa-ccm-urais-wa-2015-ii#sthash.RAQui2j5.dpuf

1 Nov 2013

NIANZE makala hii kwa kuomba radhi kutokana na kuadimika kwangu katika matoleo mawili yaliyopita. Hali hiyo ilitokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu.
Uandishi wa makala katika gazeti hili maridhawa umekuwa sehemu muhimu ya maisha yangu, na pindi ikipita wiki pasi kuandika chochote (kama ilivyokuwa wiki mbili zilizopita) huwa najihisi kupungukiwa kitu fulani maishani mwangu.
Pamoja na kiu yangu kubwa ya kuhamasisha mijadala mbalimbali, kukemea maovu na hata kuhabarishana tu, moja ya hamasa kubwa zinazonifanya niendelee na jukumu hili ni mapokeo ya wasomaji mbalimbali.
Katika wiki hizi mbili, nimepokea lundo la barua-pepe kutoka kwa wasomaji wakihoji kulikoni. Baadhi walikwenda mbali zaidi na kuhoji iwapo “nimenyamazishwa.”  Ni katika mazingira kama haya ambapo ninaendelea kutambua kuwa jukumu hili la uandishi wa makala katika gazeti hili ni muhimu kwa jamii ninayoitumikia.
Katika mazingira ya Tanzania yetu ya sasa, ni rahisi kwa mtu kufika mahala akaamua “kubwaga manyanga,” kwamba hizi “kelele” za kila wiki ni kupoteza muda tu hasa kwa vile mambo yanazidi kwenda mrama badala ya kurekebishika. Lakini Waingereza wana msemo “hope is the last thing to lose” (yaani ‘kamwe usipoteze matumaini) kwa tafsiri isiyo rasmi). Inabidi tuendelee hivyo hivyo licha ya vikwazo tunavyokumbana navyo.
Na katika wiki mbili hizi nimejikuta nikikabiliwa na swali moja la msingi: pamoja na Watanzania wengi kuchoshwa na CCM, je CHADEMA ipo tayari kuiongoza Tanzania? Nimetaja CHADEMA kwa vile kila anayefuatilia kwa karibu siasa za huko nyumbani anatambua kuwa kwa sasa chama hicho ndicho pekee ambacho angalau kinaweza kuing’oa CCM.
Swali hilo limeniijia baada ya kauli ya majuzi ya Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Jakaya Kikwete kwamba CCM inaweza kuanguka kwenye Uchaguzi Mkuu ujao, na mwenendo wa CHADEMA.
Kwamba Mwenyekiti wa Taifa wa CCM ambaye pia ni Rais wa nchi yetu anahisi kuwa chama chake kinaweza kuondoka madarakani si jambo dogo. Lakini kubwa zaidi ni ukweli kwamba kauli hiyo ya Rais Kikwete inaakisi mawazo ya wachambuzi wengi wa siasa wanaoegemea kwenye uhalisia, badala ya hisia au itikadi za kisiasa.
Awali, mmoja wa wanasiasa wakongwe wa CCM, Mzee Peter Kisumo alitoa kauli kama hiyo ya Kikwete kwamba CCM inaweza kung’oka madarakani kutokana na kunyamazia vitendo vya ufisadi na matumizi mabaya ya rasilimali za umma.
Mwanasiasa huyo alitoa onyo hilo wakati wa kumbukumbu ya miaka 14 ya kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere. “Chama kimebaki kuwa cha walalamikaji, kila mtu amekuwa mlalamikaji. Hata Waziri Mkuu amegeuka mlalamikaji. Sijaona watu wanaowajibishwa kwa ufisadi,” alisema Kisumo na kutolea mfano sakata la mabilioni ya fedha za umma zilizotoroshwa na kuhifadhiwa kwenye benki mbalimbali nchini Uswisi.
(CHADEMA) wakijitokeza na kuwataja majina wahusika, wakasema fulani na fulani ndiyo wenye mabilioni haya Uswisi, na serikali ikasita kuwachukilia hatua, wakasema tukiingia madarakani tutawakamata, wananchi wanaweza kuwaamini na kuwachagua,” alisema.
Lakini pengine kwa kutolielewa kwa undani tatizo la ufisadi, Rais Kikwete alitahadharisha uwezekano wa CCM kuanguka katika uchaguzi ujao akisema; “kama rushwa haitakomeshwa ndani ya chama hicho.” Kwa mtizamo wangu, japo ninampongeza Rais Kikwete kwa angalau kuwa na ujasiri wa kutoa tamko hilo, lakini ameendeleza siasa katika suala hili nyeti.
Ni hivi, kitakachoiangusha CCM (si lazima iwe mwaka 2015 japo ni muhimu) sio rushwa ndani ya chama hicho pekee bali katika taifa kwa ujumla. Kuwanyooshea vidole viongozi wa CCM pekee ilhali rushwa ni janga la kitaifa ni moja ya kasoro za kauli hiyo ya Kikwete. Wakati kila Mtanzania anafahamu jinsi rushwa ilivyoshamiri kwenye kila chaguzi za chama hicho tawala, ufisadi mkubwa na wa kutisha unaowahusisha watendaji wa serikali kwa kushirikiana na wafanyabiashara wahalifu wanaolindwa na CCM na taasisi za dola.
Japo kushamiri kwa rushwa ndani ya CCM kumechangia kulea na kukuza ufisadi nchini Tanzania, kuna idadi kubwa tu ya watendaji wa serikali ambao si viongozi wa kisiasa na wanajihusisha na ufisadi. Ningetamani endapo Rais Kikwete angekwenda mbali zaidi na kutangaza ufisadi kuwa ni janga la kitaifa, hasa ikizingatiwa kuwa uhai wa Tanzania sio tu ni muhimu zaidi ya uhai wa CCM, bali pia ukweli kwamba madhara ya rushwa yanamgusa kila Mtanzania bila kujali itikadi yake ya kisiasa.
Lakini angalau kwa Rais Kikwete kuwa na ujasiri wa kulizungumzia suala hilo bayana inaleta matumaini kuwa huenda katika miezi kadhaa iliyosalia kabla ya yeye kumaliza muhula wake wa urais, anaweza kulivalia njuga janga hilo la ufisadi ndani na nje ya CCM.
Hata hivyo, kama CCM itaanguka kwenye Uchaguzi Mkuu ujao na CHADEMA kufanikiwa kushika madaraka, je chama hicho cha upinzani kipo tayari ‘kuikomboa’ Tanzania kutoka katika lindi la umasikini unaochangiwa kwa kiasi kikubwa na ufisadi?
Japo nimekuwa nikiunga mkono harakati za chama hicho (pasi kuwa mwanachama) katika kuiletea nchi yetu ‘ukombozi wa pili’ (wa kwanza ulikuwa kumng’oa mkoloni, wa pili kung’oa mfumo wa kifisadi) bado nina wasiwasi kwamba vita ya chini kwa chini inayoendelea ndani ya CHADEMA inaweza sio tu kukinyima ushindi chama hicho katika Uchaguzi Mkuu ujao, bali pia inaweza kuzalisha ‘CCM-B.’
Ninaandika haya nikitambua hujuma kubwa zinazofanyika dhidi ya chama hicho kutoka nje yake lakini pia kuna hujuma zinazofanyika ndani ya chama hicho, ambazo zinaweza kuwa na madhara makubwa pasipo kuchukuliwa hatua haraka.
Lakini hata tukiweka kando hujuma hizo, kwa mtizamo wangu ninaiona CHADEMA kama imeridhika na uungwaji mkono inaopata kutoka kwa wananchi na kwa namna fulani, wameanza kubweteka. Je, chama hicho hakiwaelewi Watanzania vizuri au ni uzembe tu?
Tujiulize swali hilo tukizingatia ukweli mchungu kwamba, sehemu kubwa ya wapigakura huko nyumbani (Tanzania) ni rahisi mno kughilibiwa kwa vitu vidogo tu (pishi za sukari na mchele, doti za khanga na vitendo vingine kama hivyo).
CHADEMA kinaelekea kutegemea huruma ya umma, kitu ambacho hakipo, kwa tunaozifahamu siasa za Tanzania yetu. Sio kama ninawakashifu Watanzania wenzangu, lakini ukweli ni kwamba kuna wenzetu wengi tu wanaoendeshwa na ‘matukio ya kupita.’ Likitokea jambo kubwa, litashika moto mkubwa kwa saa kadhaa, kisha ‘life goes on.’ Kuna idadi kubwa tu ya Watanzania ambao yayumkinika kuhitimisha kuwa wanaona matatizo yanayoikabili nchi yetu ni hatima yetu na si jambo ‘la kujitakia’ au linaloweza kurekebishika.
Ili CHADEMA iweze kuingia Ikulu inapaswa kujibadili kutoka kikundi cha harakati na kuwa chama kamili kilicho tayari kushika dola. Na sio kushika dola kwa minajili ya kuwa Ikulu tu bali kuhakikisha kuwa sababu zinazowafanya baadhi ya Watanzania kutamani CCM iondoke madarakani haziendelei kuwepo.
Ni rahisi kwa mwananchi anayetaka mabadiliko kuvunjika moyo akishuhudia jinsi harakati za uchaguzi tu ndani ya CHADEMA zikitishia amani na hata hatma ya chama hicho.
Baadhi ya wachambuzi wa siasa wanabashiri kuwa iwapo chama hicho kitaitupa mkono demokrasia ndani yake na kuingia katika Uchaguzi Mkuu katika hali hiyo, basi kisahau ndoto za kwenda Ikulu. Na kana kwamba CHADEMA wapo kwenye majaribio ya siasa, wanapiga danadana kufanya uchaguzi wao mkuu ikiwa ni chini ya mwaka mmoja kabla ya Uchaguzi Mkuu wa nchi. Tufanye tafakari fupi kwa kujiuliza; hao watakaochaguliwa kuongoza chama hicho baada ya uchaguzi, watakuwa na muda wa kutosha kukiingiza chama hicho Ikulu?
Lakini tishio jingine linaloendelea hivi sasa dhidi ya CHADEMA ni mfumuko wa nyaraka kadhaa zinazosambazwa kielektroniki (nimebahatika kuzisoma) zinazomhusu kiongozi mmoja mwandamizi wa chama hicho. Ziwe ni hujuma zinazofanywa na maadui wa nje ya chama hicho au ni sehemu ya vita ya wenyewe kwa wenyewe, au ni tuhuma za kweli, madhara yake yanaweza kuwa makubwa kwa chama hicho kikuu cha upinzani.
Nihitimishe makala hii kwa kubainisha kuwa mjadala huu ni endelevu, nitauendeleza. Kwa sasa, ni muhimu kwa kila Mtanzania anayeitakia mema nchi yetu kutumia muda huu kutafakari kwa makini nafasi yake binafsi katika ‘mapambano ya kupata ukombozi wa pili.’
Tanzania yetu ni muhimu kuliko vyama vya siasa, na wakati vyama vya siasa huzaliwa na kufa, nchi yetu ni lazima ibaki hai kwa gharama yoyote ile.
Inawezekana, timiza wajibu wako.


21 May 2013

Click image for larger version. 

Name: Prof Jay Ajiunga Na Chadema.jpg 
Views: 0 
Size: 47.5 KB 
ID: 94612
 Profesa Jay akipokea kadi ya unachama wa Chadema kutoka kwa Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema) Mh. Joseph Mbilinyi (a.k.a Sugu)
Click image for larger version. 

Name: Prof Jay Na Sugu Na Mnyika.jpg 
Views: 0 
Size: 40.8 KB 
ID: 94613

Profesa Jay akiwa na Mh 'Sugu'  na Mbunge wa Ubungo (Chadema) Mh John Mnyika.

Ni Mtanzania gani kijana (na hata wazee wa kati) asiyemjua Profesa Jay, msanii mahiri wa Bongoflava ambaye jina lake halisi ni Joseph Haule (au Jay wa Mitulinga). Msanii huyo, pengine katika hali ambayo haikutarajiwa kabisa, leo amejiunga na chama cha upinzani cha Chadema.

Uamuzi wa Profesa Jay kujiunga na Chadema unaweza kuwa na manufaa makubwa sana kwa chama hicho hasa kwa vile mabadiliko ya kisiasa huko nyumbani yanategemea zaidi hamasa ya vijana.


Nitaandika zaidi baadaye kuhusu tukio hili muhimu kwa Chadema, muziki wa bongoflava na vijana kwa ujumla, lakini kwa sasa burudika na kibao hiki cha "Nikusaidiaje" cha Profesa Jay akimshirikisha Ferouz

13 Feb 2013



Pichani ni Mwenyekiti wa Taifa wa CCM Rais Jakaya Kikwete, Makamu wake Philip Mangula,na Katibu Mkuu wa Chama hicho Abdulrahman Kinana  wakiwa na Juliana Shonzi na Mwampamba waliohama Chadema na kujiunga na chama tawala.

Umuhimu wa tukio hilo haupo kwenye picha hiyo wala uamuzi wa wanasiasa hao kujiunga na CCM,bali ukweli kwamba katika siku za hivi karibuni, wanasiasa hao wachanga walitokea kuwa chanzo cha sokomoko ndani ya Chadema hasa kwa kutumia mitandao ya kijamii.

Kama wasemavyo waswahili,Mungu hamfichi mnafiki. Wakati Shonzi na Mwampamba walipokuwa wakipita huko na kule kujaribu kuihujumu Chadema kutoka ndani, baadhi yetu tulifahamu kuwa wanasiasa hao walikuwa wakitumiwa na CCM,chama ambacho licha ya ukongwe wake kimekuwa mahiri katika uendeshaji wa hujuma dhidi ya vyama vya upinzani.

Japo uamuzi wa wanasiasa hao kuhama Chadema na kujiunga na CCM ni matumizi ya haki zao za kidemokrasia na kikatiba, lakini kwa kiwango kikubwa kitendo hicho kinasaidia kuipa nafuu Chadema,sio tu kwa maana ya 'kuvuja kwa pakacha ni nafuu ya mchukuzi' bali pia kuuthibitishia umma kuwa kelele za hapa na pale kutoka kwa baadhi wa viongozi wa chama hicho wanaodai kuhujumiwa kwa madai ya 'ukandamizwaji wa demokrasia ndani ya Chadema' ni matokeo ya harakati zisizoisha za CCM kukihujumu chama hicho na vyama vingine vya upinzani.

Wakati Shonzi na Mwampamba wameshapata 'dakika zao 15 za umaarufu' (15 minutes of fame) ni vema wakatambua kuwa kazi waliyotumwa na 'mwajiri' wao huko CCM haikufanikiwa hasa kwa vile jitihada zote walizotumia kuichafua Chadema zimesihia kupuuzwa na watu wengi makini.

Kadhalika, ni muhimu kwao kutambua kuwa licha ya CCM kutumia kila njia-huku nyingi zikiwa ni chafu- lakini kwa hakika chama hicho sio tu kimezeeka bali kina kansa kali ambayo inyeshe mvua liwake jua lazima kitang'oka madarakani.Kama si mwaka keshokutwa 2015 basi miaka michache ijayo.

CCM itakufa kwa sababu itafika mahala Watanzania walio wengi watafikia mwafaka kuwa kuendelea kukiacha chama hicho madarakani ni sawa na ku-fast track kifo cha taifa letu.Haihitaji uelewa wa siasa za huko nyumbani kutambua kuwa vurugu mbalimbali zinazoendela kujitkeza huko nyumbani ni matokeo ya siasa za kihuni za CCM,chama ambacho kipo tayari kufanya lolote hata kama lina madhara kwake au kwa taifa,ilimradi tu kiendelee kubaki madarakani: si kwa minajili ya kutumikia umma bali kuendeleza ujambazi wa mchana kweupe (daylight robbery) kufilisi nchi yetu.

Ni wazi kuwa kuodnoka kwa Shonza na Mwampamba ni good riddance kwa Chadema...watatumika kwa siku mbili tatu kuichafua Chadema na hususan Dkt Slaa lakini mwisho wake ni kama ilivyo kwa kondomu: muhimu kabla na wakati wa tendo la ndoa,lakini uchafu usiovumilika baada ya shughuli hiyo.



Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.