Showing posts with label Cyber bullying. Show all posts
Showing posts with label Cyber bullying. Show all posts

1 Apr 2015


Pengine kabla ya kueleza kwanini naunga mkono muswada wa kudhibiti uhalifu wa mtandaoni (The Cyber Crime Bill),ni vema nikaeleza background yangu kidogo ili kutanabaisha sio tu ninavyothamini uhuru wa habari bali pia nilivyonufaika nao.

Nilianza uandishi kwenye vyombo vya habari mwaka 1996,mwaka mmojabaada ya kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.Aliyenishawishi kuingia kwenye fani hiyo ni mwanahabari mkongwe, Albert Memba.Nikiwa mwaka wa pili, na yeye mwaka wa kwanza chuoni hapo, Memba aligundua kuwa 'utani wa busara' niliokuwa nikifanya eneo la 'kijiweni' (nyuma ya ukumbi wa mihadhara ya Sanaa -ATB,mkabala ya Maktaba Kuu ya chuo hicho) ungeweza kunipatia fursa katika gazeti 'lisilo serious.'

Nikafuata ushauri wake na kuanza kuandika 'unajimu wa utani' katika gazeti la 'udaku' la SANIFU lililokuwa linamilikiwa na kampuni ya Business Times, wachapishaji wa gazeti la Majira.Sanifu ni gazeti la kwanza kabisa la udaku Tanzania. Gazeti hilo lilinipa safu (column) niliyoipa jina 'nyota za Ustaadh Bonge.' Nyota hizo licha ya kutumia alama za unajimu kama 'Mshale' (Sagittarius), Ng'e (Scorpio),nk hazikuwa na ukweli wowote zaidi ya burudani. Kwa mfano, ungeweza kukutana na utabiri 'wa kisanii' kama huu: "Wiki hii utakumbwa na nuksi itakayokuletea ulaji mbeleni.Mwanao atagongwa na gari la ubalozi wa Marekani,lakini hatoumia.Ubalozi huo utakufidia kwa kukupatia viza ya kuishi Marekani.Usimzuwie mwanao kucheza barabarani."

Sio siri, watu wengi tu walivutiwa na 'Nyota za Ustaadh Bonge' na hii ilipelekea mie kupewa jina la utani la Ustaadh Bonge kwa muda wote niliokuwa hapo Mlimani (UDSM), na hadi leo, baadhi ya marafiki zangu wananiita Bonge.

Baada ya gazeti la Sanifu 'kufa' nilijiunga na gazeti jingine la udaku la Komesha, na baadaye Kasheshe, magazeti yaliyokuwa yanamilikiwa na kampuni ya IPP. Huko nako niliendeleza safu ya 'Nyota za Ustaadh Bonge.'

Hatimaye niliamua kuachana na magazeti ya udaku na kuhamia kwenye magazeti yenye 'serious news.' Nikafanikiwa kupata safu kwenye gazeti la KULIKONI,na safu hiyo ndio iliyopelekea jina la blogu hii yaani KULIKONI UGHAIBUNI ambalo lilikuwa jina la safu yangu katika gazeti hilo.Lengo la awali la blogu hii niliyoianzisha mwaka 2006 lilikuwa kuwapatia fursa wasomaji wa gazeti la Kulikoni walio nje ya Tanzania kusoma makala zangu kwa vile gazeti hilo halikuwepo mtandaoni.

Ni katika uandishi wa makala katika gazeti la Kulikoni ndipo nilipojitengenezea matatizo makubwa baada ya kuandika makala moja mwishoni mwa mwezi Oktoba 2006 ambapo nilikemea jitihada za aliyekuwa Waziri Mkuu wakati huo, Edward Lowassa, kukwamisha mjadala wa sakata ya Richmond. Makala hiyo ilipelekea Press Secretary wa Lowassa, Said Nguba, kunikaripia vikali hadharani. Mwendelezo wa sakata hilo hatimaye ulipelekea mwisho wa ajira yangu serikalini mwaka 2008.

Baadaye nikapewa safu katika gazeti la MTANZANIA,ambapo safu yangu ilijulikana kama MTANZANIA UGHAIBUNI. Lilipoanzishwa jarida la RAIA MWEMA, nikafanikiwa kupata safu, ambayo niliita RAIA MWEMA UGHAIBUNI, ambayo imedumu kwa miaka kadhaa hadi hivi leo.

Kwahiyo kwa kuangalia background hii utabaini kuwa sio tu nimeutumia vema uhuru wa habari bali pia nimenufaika nao vya kutosha.Nitakuwa mtu wa mwisho kuwa kikwazo cha uhuru huo kwani nami ni mnufaika mkubwa.

Nirejee kwenye mada halisi ya makala hii.Sababu kuu zinazonifanya niunge mkono muswada wa kudhibiti uhalifu wa mtandaoni ni TATU:

Kwanza, KITAALUMA/KITAALAM: Kwa zaidi ya miaka 10 huko nyuma, nilisomea na hatimaye kufanya kazi katika sekta ya usalama. Japo kimsingi kwa sasa si mwajiriwa katika taasisi ya usalama, nina interest kubwa kuhusu stadi na taaluma hiyo, ndani na nje ya Tanzania. Licha ya kujihusisha na usalama kwa maana ya intelijensia, pia nina interest kubwa kuhusu usalama wa mtandaoni hususan uhalifu wa mtandaoni (cybercrime). 

Sambamba na hilo, nimekuwa nikiutumia sana mtandao kwa minajili ya kupashana habari.Licha ya blogu hii, nimekuwa nikiweka mabandiko katika mitandao mingine ya kijamii kama vile Tumblr, Google+, Facebook, Instagram, Pinterest na hata Jamii Forums. Kutokana na uwepo wangu mkubwa mtandaoni, nimelazimika kufuatilia kwa karibu umuhimu wa usalama mtandaoni ikiwa ni pamoja na njia na nyenzo za kujikinga na wahalifu wa mtandaoni, sambamba na kuhabarisha masuala mbalimbali yanayohusiana na suala hilo.

Vilevile, kwa miaka ya hivi karibuni nimepata interest mpya ya software hususan za simu, kwa maana ya maendeleo na matumizi ya apps mbalimbali, pamoja na masuala ya teknolojia kwa ujumla.Katika hilo, nimelazimika pia kufuatilia usalama wa software mbalimbali, za kompyuta na simu.

Kwahiyo, uzoefu wangu mdogo kitaaluma/kitaalam unanituma kuunga mkono umuhimuwa muswada huo hasa kwa vile suala la kompyuta kwa ujumla bado ni geni kwa Watanzania wengi, na hiyo inaota fursa kwa wahalifu wa mtandaoni kufanya hujuma zao kirahisi.Lakini pia hali hiyo inapelekea matumizi yasiyofaa ya teknolojia hiyo ngeni.

Kiintelijensia, kama ilivyosikika hivi karibuni, kuna jitihada za makundi ya kigaidi ya ISIS na Al-Shabaab kufanya hujuma eneo la Afrika Mashariki ikiwamo Tanzania. Kwa bahati mbaya, mtandao umekuwa nyenzo muhimu ya vikundi vya kigaidi, hususan ISIS, katika harakati zao za kidhalimu. Na hivi karibuni tumesikia matukio mbalimbali yanayoelezwa kuwa ya kigaidi huko nyumbani. Hatuwezi kupuuzia taarifa hizi kwa sababu ugaidi, kama ilivyo kifo au tukio la wizi/ujambazi, hausubiri kualikwa.Unatokea tu. Kwahiyo ni muhimu kuchukua hatua za tahadhari ikiwa ni pamoja na kudhibiti matumizi ya kompyuta kwa minajili ya kufanya uhalifu. Naomba kusisitiza kuwa huu ni mtizamo wa kitaalam (kiinteliujensia) zaidi, na pengine si rahisi sana kueleweka.

Pili, KIJAMII: Ni ukweli usiopingika kuwa Tanzania yetu inaweza kuwa inashika nafasi ya juu kabisa katiika matumizi yasiyofaa ya mtandao.Ninaamini kuwa wengi wetu tumeshuhudia utitiri wa blogu za ngono mtandaoni. Ashakum si matusi, uki-Google 'picha za uchi' utakumbana na mlolongo wa mambo yasiyoendana na mila na desturi zetu.

Kama kuna sehemu inayotoa ushahidi mkubwa wa matumizi mabaya ya mtandao kwa Tanzania yetu basi ni INSTAGRAM.Huko imekuwa 'dunia uwanja wa fujo.' Kama si mzoefu wa matusi basi dakika chache tu katika mtandao huo utakutana na kila aina ya matusi. Wenyewe wameanzisha 'timu' za kusapoti au kupinga watu flani maarufu, na kwa hakika lugha inayotumika huko inachefua. Busara pekee hazitoshi kuwadhibiti watu hawa.Dawa pekee ni kuwa na sheria, sio tu ya kuwakumbusha umuhimu wa kuzingatia maadili bali pia kuwazuwia kuendeleza maovu yao.Ifike mahala, kabla mtu hajabandika picha za uchi ajiulize mara mbili iwapo hatochukuliwa sheria.

Matumizi ya simu za kisasa zenye kamera yamechangia 'kumfanya kila mwenye simu kuwa paparazi,' na katika hili, tumekuwa tukishuhudia picha zisizofaa kabisa mitandaoni.Hivi ni mara ngapi tumekwazwa na picha za maiti kwenye mitandao ya kijamii? Ni mara ngapi tumeitaka serikali kuchukua hatua dhidi ya uhuni wa kubandika picha zisizofaa mtandaoni? Naam, serikali imesikia kilio chetu kwa kuleta muswada wa kuzwia uhalifu wa mtandaoni ili kupata sheria itakayosaidia angalau kupunguza kadhia hiyo inayokera wengi.

Pia kuna blog zisizo za picha za ngono lakini zinazosababisha utengano mkubwa katika jamii. Ukimtkana mtu kwa mdomo unaweza kusahau na hata huyo aliyetukanwa anaweza kusahau, lakini mtandao wa kompyuta (internet) hausahau kitu. Uki-Google jina langu, moja ya mambo utakayokutana nayo ni 'ugomvi' wangu wa zamani sana na gazeti moja huko Tanzania uliotokana na mimi kulilaumu kwa kutumia picha za uongo kuhalalisha habari waliyochapiusha.Japo ugomvi huo uliisha miaka mingi iliyopita na wahusika ni marafiki zangu kwa sasa, na tumeshasdahau yaliyopita, lakini internet bado inakumbuka.

Sasa blogu zinazoendekeza matusi, kuchafuana, uzushi na vitu kama hivyo sio tu zinawathiri wahanga kwa muda huo wa tukio lakini zinaweka kumbukumbu ya milele mtandaoni...kwa sababu mtandao hausahau kitu. Tuendelee kuvumilia uhuru huu usio na ukomo wa kumchafua mtu yeyote kwa vile tu mlikorofishana? 

Baba wa Taifa aliwahi kutuusia kuwa "Uhuru bila utii ni ujinga" na "uhuru usio na mipaka ni uwendawazimu." Sasa pasipo sheria ya kudhibiti ujinga na uwendawazimu huu unaotokana na dhana fyongo kuwa 'hakuna anayeniona ninapobandika mabaya mtandaoni' tutaendelea kuumizana.

Tatu, sababu BINAFSI: Japo sitaki kuwa mbinafsi kwa maana ya 'kuunga mokono muswada huu kwa sababu mie pia ni mhanga' lakini pia sitaki kuwa mnafiki kwa kukwepa ukweli kwamba nimeshawahi kuwa mhanga wa matumizi mabaya ya uhuru mtandaoni. Mfano mmoja halisi ni kilipotokea kifo cha binti mmoja aliyekuwa miongoni mwa watumiaji mahiri wa mtandao wa kijamii wa Twitter, Marehemu Betty Ndejembi (Mungu aiweke roho yake mahali pema peponi). Kwa vile kabla ya tukio hilo la kusikitisha nilikuwa nikihamasisha upinziani dhidi ya unyanyasaji mtandaoni, kifo cha marehemu Betty kilinipa changamoto mpya, hasa ikizingatiwa kuwa siku chache kabla ya kukutana na mauti, binti huyo alinyanyaswa vya kutosha huko Twitter. Kwahiyo haikuwa jambo la kushangaza nilipoungana na baadhi ya wanaharakati kutumia hashtag #StopCyberbullying.

Lakini kwa sababu ambazo hadi leo sizielewi, lilijitokeza kundi katika mtandao huo sio tu kupambana na jitihada hizo za kukemea unyanyasaji mtandaoni bali pia kunichafua kwa maana ya jitihada kuonyesha kuwa eti nami ni mnyanyasaji pia huko mtandaoni. Kama kuna kitu kiliniuma na kinaendelea kuniuma hadi leo ni pale mmoja wa watu hao aliponiita MUUAJI. Yaani kuhamasisha mapambano dhidi ya unyanyasaji mtandaoni ni sawa na UUAJI? Ningeweza kumburuza mtu huyo mahakamani kwa kosa la kunidhalilisha (defamation) lakini ukosefu wa sheria halisi inayohusu unyanyasaji mtandaoni (cyberbullying) ungeweza kuniathiri.

Ni rahisi kuzungumzia 'uhuru usio na ukomo' kwa jamii iwapo hujawahi kuwa mhanga wa matumizi ya uhuru huo. Naomba nisieleweke vibaya.Siungi mkono muswada huo kwa vile tu mie ni mhanga huko nyuma, au utakomoa watu flani, lakini pia kuna sababu nyingine muhimu kama nilivyobainisha hapo juu.

MWISHO, japo ninatambua umuhimu wa wananchi kushirikishwa katika utungaji wa sheria zinazowahusu, na pia ninaafikiana na hoja ya kutoharakisha miswada inayohitaji ushirikishwaji wa umma, ninaunga mkono muswada huo kwa sababu UNAHITAJIKA SASA. Na kwa hakika umechelewa sana. Hatuwezi kuendelea kuvumilia matumizi mabaya ya mtandao wa kompyuta kwa kisingizio cha uhuru wa habari. Hatuwezi kuendelea kuvumilia picha za ngono na maiti zikiwekwa hadharani kama mapambo.Jamii yeyote yenye kuzingatia maadili inapaswa kuchukua hatua kali dhidi ya vitendo kama hivyo. Hatuwezi kuwatengenezea mazingira mazuri magaidi kwa kisingizio cha 'umbeya si dhambi.' Madhara ya kutochukua hatua ni makubwa kuliko kuchukua hatua.

Mie ninaweza kuwa mhanga wa sheria hiyo (ikipitishwa) hasa kwa vile ni mtumiaji mkubwa wa mtandao, na pia mkosoaji wa serikali ninapoona inastahili kukosolewa. Ni kweli kwamba sheria hiyo ikipitishwa inaweza kudhuru hata watu wasio na hatia.Lakini katika hili, tatizo si sheria bali CORRUPTION. Tunapozungumzia corruption hatumaanishi tu kuhonga au kuhongwa fedha, bali hata kupindisha sheria kwa maslahi binafsi au kukomoana.Sasa katika hilo, tuna tatizo katika nyingi ya sheria zetu.Ni wangapi wanaporwa viwanja kutokana na corruption katika sheria na sekta ya ardhi? Ni wangapi wapo gerezani muda huu kwa sababu tu walishindwa kuhonga polis au hakimu? Ni vigumu kwa sheria yoyote kuwa na ufanisi katika mfumo corrupt.Ni jukumu letu sote kupambana na corruption ili sheria zenye maslahi kwa jamii zisiishie kuathiri wasio na hatia.

Muswada huu ni kwa maslahi ya kila Mtanzania. Kama wewe si mhalifu wa mtandaoni, sheria hii haitokudhuru. As to itatumika vibaya na serikali, tatizo hapo sio sheria husika bali corruption.Kuna sheria nyingi tu na pengine kali zaidi ya hii tarajiwa, kwa mfano Sheria ya Usalama wa Taifa 1970, Sheria ya Idara ya Usalama wa Taifa 1996 na Sheria ya Kuzuwia vitendo vya Ugaidi ya mwaka 2002, zinazoweza kutumika vibaya kutokana na corruption. Sina hakika wangapi miongoni mwa wanaopinga muswada wa Cybercrime wameshakuwa wahanga wa 'matumizi mabaya' ya sheria hizo kali kuliko hii tarajiwa.

Hofu yetu dhidi ya matumizi mabaya ya sheria isiwe sababu ya kutokuwa na sheria kabisa. Tusielemee kwenye hofu yetu tu bali tutambue kuwa takriban kila siku kuna victims kadhaa kutokana na ukosefu wa sheria ya kudhibiti uhalifu wa mtandaoni.

ANGALIZO: Huu ni mtizamo wangu binafsi na unaweza kuonekana fyongo kwa mwingine.Twaweza kujadiliana pasipo haja ya 'kupigana.'

MUNGU IBARIKI TANZANIA



29 Mar 2015



Kwa muda mrefu, baadhi ya watumiaji wa mtandao wa kompyuta (Internet) wamekuwa na wakati mgumu kufuatia kushamiri kwa unyanyasaji mtandaoni, kwa kimombo CYBERBULLYING.

Kwa kiasi kikubwa, tatizo hili linaakisi tabia zetu nje ya mtandao. Mtu aliyezowea kunyanyasa wenzie mtaani, akiingia mtandaoni anaweza kuendeleza tabia hiyo kirahisi. Kadri mtandao unavyozidi kuwa sehemu ya maisha yetu ya kila siku ,ndivyo unavyoakisi maisha yetu 'ya kawaida' nje ya mtandao. 

Kwa upande mwingine, mtandao unatoa fursa ya watu wenye tabia tofauti kukutana. Ndio maana si ajabu kukuta mtu mmoja akiweka bandiko kuhusu dini, mwingine akaweka bandiko kuhusu matusi.

Licha ya tabia, mtandao pia huwakutanisha watu wenye sifa tofauti: wapole na wakorofi, wapenda amani na wagomvi, wenye elimu na mbumbumbu, wenye aibu na wasio na mishipa ya aibu, nk. 

Kadhalika, mtandao unatoa fursa mbalimbali, nzuri na mbaya. Kwa mfano, mtandao unatuwezesha kuwa karibu na viongozi wa nyanja mbalimbali, kutoka mawaziri hadi viongozi wa taasisi binafsi.Uzuri wa fursa hiyo ni pamoja na kurahisisha mawasiliano baina ya watu wanaotoka 'madaraja' tofauti ya kijamii. Kadhalika, fursa hiyo inatuwezesha kujifunza kutoka kwao, sambamba na kufuatilia masuala mbalimbali ambayo kutokana na nafasi zao yanagusa maisha yetu binafsi au ya jamii kwa ujumla.

Fursa hiyo pia inatuwezesha kuwa karibu na watu mbalimbali, muhimu na wa kawaida. Katika mazingira ya kawaida, ni vigumu kufahamiana na Waziri, kwa mfano, labda kuwe na undugu, kufahamiana au mahusiano kikazi.

Hata hivyo, mtandao pia unatoa fursa 'mbaya.' Binadamu tupo tofauti, kuna wenzetu ambao wakiiona fursa wanaitumia kwa manufaa, lakini kuna wengine sio tu hawataki kujifunza 'mazuri' ya wenzao (ambayo wao hawana) pia hujenga chuki na jitihada za kuwachafua au kuwadhalilisha wenzao wenye 'mazuri.' Kwa mfano, unaweza kukutana na mtu ambaye hakubahatika kupata elimu ya kutosha, au hakusoma kabisa. Anapokutana na mwenye elimu kiasi au ya juu, badala ya kutumia fursa hiyo kama 'darasa nje ya shule' anaanzisha chuki na uhasama usio na manufaa.

Kama dunia ilivyo uwanja wa fujo, ndivyo ilivyo kwa mtandaoni. Kuna mazuri na mabaya. Kuna baadhi yetu ambao tumenufaika sana kwa uwepo wetu mtandaoni, kwa maana ya kutengeneza urafiki na watu muhimu, lakini pia kuna nyakati tumejikuta tukikutana na 'maadui.'

Ofkoz, mtandano sio sehemu ya kubadilisha mawazo, kujifunza au kuuliza maswali tu bali pia ni sehemu ya burudani. Utani ni ruksa lakini utani wenyewe usizidi kiwango. Na kanuni ya mtaani kuwa usimtanie mtu asiyekutania, ina-apply mtandaoni pia.

Kwa bahati mbaya kuna wenzetu ambao hulazimisha utani.Wengine huenda mbali zaidi kwa kulazimisha kumjua mtu zaidi ya anavyojijua yeye mwenyewe.

Kwa bahati nzuri, hatimaye serikali imesikia kilio dhidi ya unyanyasaji wa mtandaoni na Jumanne ijayo inatarajia kuwasilisha muswada kuhusu uhalifu wa mtandaoni ambao pamoja na mambo mengine unaharamisha unyanyasaji wa mtandaoni (cyberbullying) 

Katika muswada huo unajulikana kwa kimombo kama The Cyebrcrimes Act, 2015, ibara ya 23 inaharamisha unyanyasaji mtandaoni (cyberbullying) na kutaja adhabu husika. 

Muswada unafafanua maana ya cyberbullying, kwamba "mtu hataruhusiwa kuanzisha au kutuma mawasiliano ya kielektroniki kwa kutumia kompyuta kwa mtu mwingine kwa malengo ya 'kumsukuma kwa nguvu' (coerce), kumtisha, kumyanyasa au kumsababishia msongo wa mawazo, na mtu atakayekiuka kipengele hocho atakuwa anafanya kosa, na adhabu yake ni sio chini ya shilingi milioni tatu au kifungo cha sio chini ya mwaka mmoja au adhabu zote pamoja."  

Muswada kamili ni huu hapa chini (kwa bahati mbaya au makusudi, watawala wetu hawakuona umuhimu wa kuupatia tafsiri ya Kiswahili)



Wakati muswada huu ni habari njema kwa wahanga wa unyanyaswaji mtandaoni, unatarajiwa pia angalau kupunguza kushamiri kwa matusi na picha zisizofaa mtandaoni. Sio siri kwamba baadhi ya mitandao ya kijamii, hususan Instagram, imegeuka uwanja wa matusi.

Kibaya zaidi, umahiri wa matusi umegeuka moja ya vyanzo vya umaarufu mtandaoni. Kama nilivyobainisha hapo juu,mtandao unatoa fursa 'mbaya' kwa wenzetu  wasio  na cha kuelimisha, kujadili au hata kujivunia hadharani, na matokeo yake ni kuwabughudhi watu wengine au kubandika picha zisizofaa kama mbinu ya kusaka sifa za kipuuzi.

Hata hivyo, ni muhimu kukumbushana kuwa Tanzania yetu haina uhaba wa sheria.Tatizo kubwa ni katika kuziheshimu na kuzitekeleza. Twaweza kuwa na sheria kali dhidi ya uhalifu wa mtandaoni lakini utekelezaji ukiwa hafifu basi sheria hizo zitabaki maandiko tu vitabuni.

Kadhalika, ni muhimu kutahadharisha kwamba sheria hii ya uhalifu wa mtandaoni isitumiwe vibaya na serikali kuwanyima wananchi uhuru wa mawasiliano, au kibaya zaidi, kuitumia kwa minajili ya kuficha maovu na kuwalinda waovu. Sitarajii kuona sheria hii ikitumika iwapo chombo cha habari kitaibua utovu wa maadili wa kiongozi, kwa mfano.

Mwisho, ni matarajio yangu kuwa vitendo vya uhalifu wa mtandaoni, ikiwa ni pamoja na cyberbullying, vitapungua kufuatia sheria hii, iwapo itapitishwa na bunge. Angalau sasa, cyberbullies watafikiria mara mbili kabla ya kumwaga sumu zao kuwanyanyasa watu wasio na hatia.

15 Sept 2014

By Masembe Tambwe

THOUGH still low, technology and communication experts in the country are seeing signs of increased cyber crimes like bullying, harassing and stalking if the use of the internet is not controlled.
Speaking exclusively to the 'Sunday News,' the Head of Corporate Communications at the Tanzania Communications Regulatory Authority (TCRA), Mr Innocent Mungy, said that whilst there are many crimes using the internet as a platform, incidents of cyber bullying are still very small.
 
"Due to ignorance, a lot of people today think when they have been swindled online through various social media, they have been cyber bullied but this isn't so.
 
There are certain elements that qualify as bullying and evidence shows the levels are still small but will increase with time," he said. Stopcyberbullying.org website defines cyber bullying as when a child, preteen or teen is tormented, threatened, harassed, humiliated, embarrassed or otherwise targeted by another child, preteen or teen using the internet, interactive and digital technologies or mobile phones.
 
It has to have a minor on both sides or at least have been instigated by a minor against another minor. Once adults become involved, it is plain and simple cyber-harassment or cyber stalking.
 
Adult cyber-harassment or cyber stalking is never called cyber bullying. In a recent incident that left a young lady dead and that created quite a stir in many social media networks, many users christened the incident as 'cyber bullying' calling various authorities to take action.
 
Mr Mungy said that there was no law in the country that is specific to cyber bullying because the law is universal and that irrespective of where a person is insulted or degraded, whether on the sidewalk or online, it is against the law and therefore punishable.
 
"Whilst cyber bullying is seen to be at a minimal, cyber stalking and harassment is something we are increasingly seeing on social media, cases of cyber bullying can be sought at the cyber crime unit of the police," he said.
 
According to Domestic Violence Resource Centre Victoria website, cyber harassment is not just about being teased - it's repeated behaviour that is designed to humiliate, control or scare the person being targeted and is not legal or alright, while if someone keeps contacting you on Facebook or any kind of online site and it's making you scared and upset, it sounds like you're being stalked.
 
Mr Mungy said that as a country, Tanzania has leapfrogged technology and that technology advancement and development is catching up with us instead of the other way round.
 
"The challenge to stop these crimes starts with us and the media; they have to play a part in this. At the moment it is not a catastrophe because only between 17 and 20 per cent are internet users mostly aged between 18 and 25 and these are abusers," he said.
 
He cautioned users to be careful who they befriend online because one can't guarantee identity. Online, he noted, there are predators, bad people, thieves, prostitutes, con artists who use it as a platform to do what they would have done physically. "Our online presence affects our being, meaning that our character profile.
If you upload inappropriate pictures, people will harass you and later you will come to claim that you were bullied yet you caused it, let's be smart, use communication for good, it's good to make friends online because having an enemy online can be your enemy physically," he advised.
 
A cyber crime expert, Mr Sebastian Marondo, said that one advantage cyber bullies have is that they can operate under the anonymity of not being able to be seen.
 
"Cyber bullying unlike ordinary bullying is a practice that's difficult to control given the fact that it relies on the internet and like other forms of technology that require communication or sending files.
The government is supposed to enact laws protecting internet users, mobile phone subscribers from fraudsters, stalkers and in general unwelcomed callers," he urged.
 
He called on mobile phone companies to create platforms for reporting and penalising callers who misbehave in mobile communication. For instance, telecom companies can block numbers that have been identified as abusive to others.
 
The Dar Teknohama Business Incubator Chief Executive Officer, Eng. George Mulamula, told this paper that schools can be very effective brokers in working with parents to stop and remedy cyber bullying as well as educate students on cyber ethics and laws.
 
Eng. Mulamula commended TCRA for doing a good job in trying to educate the public on the correct use of digital communication technologies and have even gone on road shows around the country, educating users on best practices on the use of cell phones and the internet.
 
"Parents can help stop cyber bullying. You can start by talking to kids about the issue and teaching them the rules that will help prevent cyber bullying from happening to them or someone they know," he advised.
 
During the first ever cyber crime conference in Dar es Salaam earlier this year, the government said it is planning to enact three laws on data, internet business and cyber crime in a bid to eradicate cyber crime in the country.
 
SOURCE: Daily News

3 Sept 2014


Mnyanyasaji wa mtandaoni, Peter Nunn (pichani) anakabiliwa na uwezekano wa kifungo jela baada ya mahakama kumkuta na hatia ya kumtumia mbunge Stella Creasy  wa jimbo la Walthamstow kwa tiketi ya Chama cha Labour, hapa Uingereza, tweets za kutishia kumbaka.

Mnyanyasaji huyo alitumia mtandao wa kijamii wa Twitter kumwandama mbunge huyo aliyemwita mchawi katika tweets zake.

Nunn alijitetea kwamba hakuzungumzia suala la kumbaka mbunge huyo bali ujumbe  wake ulikuwa utani tu.

Kadhalika alikanusha kuendesha kampeni ya chuki dhidi ya mwanasiasa huyo wa kike, ambaye alikuwa akimsapoti mwanaharakati wa masuala ya wanawake  (feminist), Caroline Criado-Perez, katika kampeni ya  kudai noti ya Paundi 10 ya Uingereza iwe na picha ya mwanamke mwingine zaidi ya Malkia Elizabeth wa Pili ilivyo sasa.

Mnyanyasaji huyo ambaye ni dereva kutoka mji wa Bristol jana alipatikana na hatia ya kutuma ujumbe wa kudhalilisha na kutisha kwa kutumia mtandao wa wazi wa kielektroniki kati ya Juni 28 na Agosti 5 mwaka jana.

Jaji wa mahakama ya wilaya Elizabeth Roscoe alisema, "yeye (Nunn) anasema hadhani mbunge huyo na mwenzie walikwazwa na ujumbe wake. Hapana, siwezi kuamini maelezo hayo hata kidogo."

"Nina uhakika timilifu kabisa kuwa tweets zake zilikuwa na malengo mabaya."

Nunn alionekana kutahayari wakati hukumu hiyo dhidi yake inasomwa.katika mahakama ya City of London.

Baada ya hukumu hiyo, mbunge huyo ambaye hakuwepo mahakamani ali-tweet "sasa kesi ya mnyanyasaji Twitter imekwisha, ujumbe upo wazi: tishio ni tishio, iwe kwenye karatasi, picha au uso kwa uso."

Mnyanyasaji huyo alizana kampeni yake ya za kubughudhi Julai 29 mwaka jana, siku 5 baada ya Benki Kuu ya Uingereza kutangaza kuwa Jane Austen, mwandishi wa riwaya wa Kiingereza wa karne ya 18 atakuwa  sura mpya katika noti za Paundi 10.

Nunn aliposti tweets luluki dhidi ya kwa mwanasiasa huyo wa kike, ikiwa ni pamoja na video 6. Katika tweet yake moja, alieleza kuwa njia mwafaka ya kumbaka mbunge huyo ni kwa kumzamisha majini kwanza.

Baadaye ali-tweet "kama huwezi kutishia kumbaka mtu maarufu (celebrity), kuna haja gani ya kuwa nao?"

Nunn atahukumiwa tarehe 29 mwezi huu na waendesha mashtaka wameeleza kuwa wataomba kibali cha kumzuwia kuwasiliana na Mbunge huyo mwanamke.

CHANZO : Daily Express 

31 Aug 2014


Siku moja nilipokea barua-pepe kutoka kwa msomaji mmoja wa makala zangu katika jarida la Raia Mwema. Licha ya kupongeza kuhusu makala hizo, alinipa ombi ambalo kwa kiasi flani liliniacha na tabasamu. Namnukuu, "... tuna matatizo mengi huku kwetu, kila anayekuja anajali maslahi yake tu. Nakushauri ufikirie kuhusu kugombea katika jimbo letu mwakani." Nilimshukuru msomaji huyo kwa pongezi zake lakini nikamweleza bayana kuwa kamwe sintojiingiza katika uongozi wa kisiasa. Nilimfahamisha kuwa mie ni muumini wa falsafa kuwa yawezekana kuutumikia umma kwa ufanisi pasi haja ya kuwa kiongozi.

Falsafa hiyo inachangiwa na ukweli kwamba nimeshawahi kuwa kiongozi mara mbili, maishani mwangu. Mwaka 1991 nikiwa mwanafunzi wa kidato cha tano katika Shule ya Sekondari ya Wavulana ya Tabora (Tabora Boys') nilichaguliwa kuwa kiranja mkuu.Lakini kwa vile shule hiyo ilikuwa ya mchepuo wa kijeshi, wadhifa wa kiranja mkuu ulikuwa ukijulikana kama Kamanda Mkuu wa Wanafunzi (Students' Chief Commander), na sare ziliambatana na 'vijimkasi' viwili mabegani.

Japo wadhifa huo ulinipa fursa ya kwanza ya uongozi, tukio moja la mgomo wa wanafunzi lililojiri wakati nipo madarakani sio tu lilinipa mtihani mgumu sana bali pia lilinionyesha sura nyingine chungu ya uongozi. Kwa upande mmoja nilipaswa kuwa kiungo kati ya uongozi wa shule na wanafunzi, lakini wakati huohuo nami ni mwanafunzi na walitarajia niwe upande wao, huku walimu nao wakitaka niwe upande wao. Kwa busara na skills nilizopata kabla ya tukio hilo, mgomo huo ulimalizika salama na sikujenga maadui upande wowote kwa vile nilisimamia kwenye kanuni na taratibu na haki.

Fursa nyingine ya uongozi ilijitokeza mwaka 2000 nilipokuwa mtumishi wa taasisi flani ya serikali huko nyumbani. Niliteuliwa kuwa mkuu wa wilaya ya kiutendaji (operational district/zone), nafasi niliyoshika hadi ninaondoka huko nyumbani miaka miwili baadaye. Ugumu mkubwa wa wadhifa huu ulikuwa kwenye 'kuwa macho masaa 24'...na wakati mwingine kukurupushwa usingizini na kuulizwa 'nifahamishe kilichotokea sehemu flani' ilhali sina habari ya nini kimetokea. Lakini jingine gumu lilikuwa kwenye kuwaongoza watu nilioanza ajira nao pamoja na wengine walionizidi miaka kadhaa ya uzoefu. Kadhalika, wasaidizi wetu mtaani walikuwa na matarajio makubwa ya 'uzalishaji' wao pamoja na maisha yao binafsi. Hata hivyo niliondoka nikiwa na rekodi ya kujivunia.

Kwa kifupi, fursa zote hio zilinifundisha kuwa uongozi ni mzigo mzito na unahitaji kujitolea kwa kiasi kikubwa. Ndio maana kila nikisikia mawazo ya kujihusisha na uongozi, jibu langu jepesi ni HAPANA.Not again. Sio kwamba ninakwepa majukumu lakini kwa muda mrefu sasa nimekuwa nikijihusisha na uraia kama uongozi, kwa maana ya kutumainia nguvu za raia katika ujenzi wa taifa. Ndio hizo kelele tunazopiga magazetini, hapa bloguni na kwenye mitandao ya kijamii.

Lengo la makala hii sio kuelezea historia yangu au uwezo wa uongozi bali suala lililojitokeza katika mtandao wa kijamii wa Twitter juzi. Nadhani wengi wenu wasomaji mnafahamu kilichomsibu Betty Ndejembi, aliyetutoka juzi. Kabla ya kufariki kwake aliandamwa na unyanyasaji wa kutosha katika mtandao huo. Baada ya kifo hicho, mie niliungana na 'wenye mapenzi mema kwa jamii' kukemea unyanyasaji mtandaoni, kwa kimombo 'cyberbullying.' Hata hivyo, katika kuhamasisha mapambano hayo sikumtaja wala kumtuhumu mtu kuwa ni mnyanyasaji wa wenzie mtandaoni. Nilichohamasisha ndicho hicho nilichoeleza hapo juu: sie watumiaji wa mtandao kama wahanga wa unyanyasaji wa mtandaoni kuunganisha nguvu zetu dhidi ya wanaofanya vitendo hivyo. Na kwa hakika mapokeo yamekuwa mazuri sana. Watu wengi wamewasiliana nami kunifahamisha jinsi walivyokuwa wahanga wa cyberbullying.

Wito wangu kwa jamii umekuwa sio kusubiri serikali au wanasiasa kuchukua hatua ya kukomesha tabia hiyo bali sie kama wananchi na wahanga wa tabia hiyo kuunganisha kuvu na kupambana nayo. Kwa lugha nyingine, sie wenyewe tuchukue uongozi wa mapambano dhidi ya wanyanyasaji wa mtandaoni.

Hata hivyo, jioni ya leo likaibuka kundi la watu waliaonza kunishambulia vikali kuhusiana na kampeni hiyo ya kupambana na unyanyasaji mtandaoni. Kikubwa ni tuhuma kwamba mie wanayeniita 'mwanaharakati wa cyberbullying' ni 'bully' (mnyanyasaji) pia. Na mmoja wao akapata ujasiri wa kupitia tweets zangu za nyuma na kuzi-screenshot ili 'kuthibitisha kuwa mie ni mnafiki nisyestahili kukemea cyberbullying.' Wakati mwingine huwa nashangazwa na 'ujasiri' wa aina hii ambao hata kwa mwenye uelewa mdogo tu wa sheria anaweza kujua athari zake.

Hadi hapo sikuona tatizo sana japo nilishangazwa na 'hasira' za watu hao ilhali sikuwahi kuwatuhumu kuwa wao ni bullies. Na hata asubuhi nilitwiti kuhoji ''kama tunapozungumzia ufisadi, hukasiriki kwa vile wewe si fisadi, kwanini tukizungumzia cyberbullying ukasirike ilhali wewe sio cyberbully?"

Lakini katika mwendelezo wa shutuma zao dhidi yangu, mmoja wao akavuka mstari wa kisheria. Siwezi kuliongelea kiundani suala hili kwa sababu za kisheria.

Awali nilipoamua kuungana na wengine kukemea unyanyasaji mtandaoni sikudhani kwamba itafika mahala pa kuchukua vitendo kulazimisha wanyanyasaji hao waache tabia hiyo. Hata hivyo, kwa kilichotokea leo, nimeamua kuhamia kwenye vitendo.

Tuna tatizo kama Watanzania, ni wepesi wa kulalamikia matatizo yanayotukabili lakini ni wagumu kuchukua hatua za vitendo kuyatatua. Mgao wa umeme, huduma mbovu za baadhi ya makampuni, tatizo la ajali zisizoisha, ufisadi, na kadhalika. Kwa kiasi kikubwa tumekuwa watu wa kulalamika tu kana kwamba malalamiko hayo yataleta mabadiliko.

Katika hili la unyanyasaji mtandaoni, asilimia kubwa ya watu wanaotaka 'kuishi kwa amani mtandaoni' wameunga mkono japo kwa maneno haja ya kukemea unyanyasaji mtandaoni. Lakini kama ilivyojitokeza leo jioni ambapo nimekuwa mhanga wa ushiriki katika harakati hizo, bado kuna wenzetu wanadhani wana hatimiliki ya kuwabughudhi watu mtandaoni watakavyo. Inabidi tuseme enough is enough. Kwa vile haijawahi kutokea huko nyumbani kwa mtu kuingia matatizoni kutokana na alichoandika mtandaoni, watu wengi tu wanaendelea kudhani kuwa akiwa mbele ya keyboard ya kompyuta yake ana uhuru wa kunyanyasa, kudhalilisha, kutukana na kufanya matendo mengine ambayo kimsingi ni makosa kisheria.

Ukweli ni kwamba tukiacha 'njia za asili' za kudhibiti 'wakorofi' kwenye mitandao ya kijamii, yaani aidha kuwa-mute, kuwa-unfollow au kuwa-block, kuna njia za ufanisi zaidi kama vile za kisheria alimradi kuna ushahidi wa kutosha.

Hatimaye nimefikia uamuzi wa kuchukua hatua za vitendo dhidi ya unyanyasaji mtandaoni (cyberbullying). Sifanyi hivi kwa minajili ya kuingia kwenye vitabu vya historia kama Mtanzania wa kwanza kupambana na cyberbullies kwa vitendo bali ninafanya huduma kwa umma. Huhitaji kuwa kiongozi ili kuitumikia jamii. Na sihitaji madaraka ili niweze kupambana na tabia hii isiyofaa. Hakuna miujiza itakayowalazimisha wanyanyasaji wa mtandaoni kuacha tabia hiyo. Kitu pekee ni pale wanapofunzwa madhara ya vitendo vya aina hiyo.

Japo ningependa kuwa sehemu ya kundi linalopambana na suala hili, hadi sasa hakuna dalili zozote za uwepo wa mkusanyiko wa kukabiliana na tatizo hili ambalo kwa hakika linawasumbua wengi. Lakini tukisema tusubiri mpaka watu wajipange na kuunda kikundi, wenzetu wengi zaidi watazidi kuwa wahanga wa unyanyasaji huo wa mtandaoni.

Natambua ugumu wa mapambano haya lakini kila mapambano ni magumu. Natambua kutakuwa na lawama na kukatishana tamaa lakini liwalo na liwe lazima mtu flani awe mfano kwa wenzie kwamba cyberbullying is not just wrong but also a criminal offence. 

Lengo la makala hii sio kumtisha wala kumzuwia mtu kunituhumu kuwa nami ni cyberbully. Ninaheshimu uhuru wa kujieleza alimradi hauvuki mpaka.Na kitu ambacho kamwe siwezi kukivumilia  ni uvunjifu wa sheria dhidi yangu.

Ni matumaini yangu kuwa kama inavyofundisha Biblia Takatifu kuwa 'ukipiga mchungaji kondoo watasambaa,' kumwajibisha mmoja wa wanaodhani mitandao ya kijamii ni fursa ya kuwanyima wenzao amani kutapeleka ujumbe kwa wengine wanaoamini hivyo pia. Mafundisho ya Kiislam yanatueleza kwamba "ukiona jambo baya basi aidha lichukie, au likemee au liondoe." Nimeshachukia unyanyasaji mtandaoni vya kutosha, nimeukemea vya kutosha, na sasa ni wakati wa kuuondosha kwa vitendo. Haitokuwa rahisi lakini nina hakika nitafanikiwa. Inshallah!

Na mwisho, lengo la harakati ninazoanza si kumkomoa mtu au watu flani. Hao waliotumia muda wao kunishambulia ni dalili tu za tatizo, ninacholenga kupambana nacho ni chanzo cha tatizo. Mtu anaposkia baridi kwa vile ana homa, huwezi kumtibu kwa kumpa maji ya moto bali tiba ya homa. Kadhalika, unyanyasaji mtandaoni hauwezi kukomeshwa kwa kubana watu flani tu bali kulikabili tatizo lenyewe. Ifike mahala mtu ajiulize mara mbili kabla ya kuposti 'maneno yasiyofaa' dhidi ya mtu mwingine mtandaoni.

Ili mabadiliko ya kweli yatokee hasa ya kuondoa jambo baya ni lazima kujitoa mhanga. Iwapo uamuzi wangu wa kupambana na tabia hii utapelekea madhara kwangu basi na iwe. Ninaamini kuwa mwenye haki ataanguka saba mara sabini lakini hatimaye atasimama. Nikisema 'mwenye haki' simaanishi kuwa harakati hizi ni za kutafuta haki yangu bali ya wanyonge mbalimbali wahanga wa unyanyasaji mtandaoni. Tukiwakalia kimya bullies sio tu watadhani tunaridhia vitendo vyao bali pia wataendelea kutengeneza victims.

INAWEZEKANA, NA NITATIMIZA WAJIBU WANGU



Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.