Showing posts with label DEMOKRASIA TANZANIA. Show all posts
Showing posts with label DEMOKRASIA TANZANIA. Show all posts

16 Apr 2018






Africa Confidential Toleo la 28 Machi 2018


27 Machi 2018

Hatua za kidikteta za Magufuli zinakumbana na upinzani unaoongezeka lakini ndio Ameshika uelekeo huo na anatishia wanaomkosoa

Katikati ya muhula wake wa kwanza, Rais John Magufuli anakabiliwa na shinikizo. Huku akikabiliwa na tishio kubwa kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), vikundi vya kiraia, viongozi wa kanisa, na sasa vijana kwenye mitandao ya kijamii, anaonekana kufurahia mapambano hayo. Dola pia inatishiwa na makundi yenye silaha yaliyokuwa viongozi wa serikali na chama mkoani Pwani (MKIRU). Majibu ya serikali kukabiliana na changamoto hizo yametawaliwa na ukatili ambao haujawahi kuonekana kamwe, na kupelekea kulaaniwa kutoka kila upande.

Kuongezeka kwa vurugu za kisiasa, hasa wakati wa uchaguzi mdogo wa jimbo la Kinondoni, kulipelekea lawama dhidi ya utawala wa mabavu wa Magufuli. Ubalozi wa Marekani ulitaka kufanyike uchunguzi kuhusu utekaji na mauaji ya kiongozi wa upinzani jijini Dar es Salaam wakati wa kampeni. Umoja wa Ulaya baadaye ulionyesha wasiwasi wake kuhusu "mwenendo wa hivi karibuni unaotishia kanuni za demokrasia" baada ya polisi kutumia risasi katika maandamano ya Chadema katika mkesha wa siku ya kupiga kura Februari 17, hali iliyopelekea majeruhi watatu na kuuawa kwa mpita njia.

Wiki mbili baada ya matamko hayo, Wizara ya Mambo ya Nje ilijibu kwa taarifa yenye kurasa tatu na nusu ikiyahusisha matukio ya huko MKIRU na "vikundi vya ndani na nje ya nchi vinavyochukizwa na jitihada za Magufuli kuondoa ufisadi, biashara ya mihadarati, ujangili, ukwepaji kodi na kujenga uwajibikaji."

Vikundi hivyo vyenye silaha, ambapo baadhi vinadaiwa kuwa na mahusiano na Al-Shabaab ya Somalia, vimewauwa viongozi wa Chama Cha Mapinduzi na baadhi ya watendaji wa serikali. Tatizo hilo lilianza tangu mwaka 2014 lakini likafikia kilele mwaka 2017 baada ya operesheni ya kikatili ya vyombo vya dola kushambulia. Serikali inajaribu kuushawishi umma kwamba maandamano ya amani dhidi ya haki za kiraia na mauaji hayo ya MKIRU ni pande mbili za kitu kimoja. Ni watu wachache tu wanaoshawishika kuamini.
Katika ujumbe wao kwa msimu wa Kwaresma, maaskofu wa Katoliki walionya kwamba kuendelea kwa ukandamizaji wa kisiasa kutapelekea migawanyiko itakayohatarisha misingi ya kitaifa ya umoja na mshikamano. Walieleza kwamba kuzuwia shughuli za kisiasa sio halali na kunakiuka katiba. Kituo ch Demokrasia (TCD), ambacho huvileta pamoja vyama vya siasa kilitoa tamko la pamoja na viongozi wa Kikristo na Kiislamu kudai mapitio ya Katiba. Hii ilifuatiwa na kauli ya kuunga mkono ya vikundi zaidi ya 100 vya kiraia.

Jumapili ya Majivu Machi 25 ilishuhudia maaskofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (ELCT) wakitoa tamko kali wakiilaani utekaji watu, utesaji watu, upoteaji watu, mashambulizi ya silaha dhidi ya wanasiasa, mauaji yanayotokana na itikadi za kisiasa, vitisho, kesi za kubambikizwa, na unyanyaswaji wa raia unaofanywa na vyombo vya dola. Pia walitaka katiba mpya iwepo kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020. "Taifa huongozwa na katiba ambayo ndio msingi wa sheria zote", walisema. "Haiongozwi na ilani za vyama."

Pia kuna changamoto za kisheria. Mahakama Kuu inatarajiwa kusikia kesi mbili za kikatiba zilizoletwa na watetezi wa haki za binadamu ikiwa ni pamoja na Chama cha Wanasheria TLS, Umoja wa Watetezi wa Haki za Binadamu (the Tanzania Human Rights Defenders Coalition), na Taasisi ya sheria na haki za binadamu (the Legal and Human Rights Centre). Kesi zote zinaongozwa na Fatma Karume wa kampuni ya uwakili ya IMMA, ambayo ofisi zake zilichomwa moto Agosti mwaka jana. Akiwa anatoka kwenye familia yenye nguvu ya Karume, amekuwa mwiba kwa utawala uliopo madarakani. TLS inaongizwa na mmoja wa wateja wake, kiongozi wa Chadema Tundu Lissu, ambaye bado yupo Ubelgiji anakopata matibabu ya majeraha ya risasi kufuatia jaribio la kumuuwa.

Kumekuwa na ukosoaji ndani ya CCM pia. Nape Nnauye, mbunge aliyetimuliwa uwaziri mwaka jana, ametoa wito wa kuifanyia marekebisho Idara ya Usalama wa Taifa (TISS) akieleza "kwa macho makavu" kuwa kama ambavyo taasisi hiyo imekuwa ikifanya kazi kwa manufaa ya dola, pia imekuwa ikiitumikia CCM, inaendeshwa kisiasa.

Mbunge mwingine wa CCM, Hussein Bashe, ambaye awali hakufahamika kuwa na mtazamo huru, na aliongoza kampeni ya Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa kuwania urais, naye ametokea kuwa mtetezi wa uhuru wa kujieleza na mawazo mbadala.

Haya na matamko mengine yanaashiria demokrasia ya Tanzania ipo katika kipindi kigumu. Akiongea kwenye shughuli ya TCD ambayo ilipelekea wito wa katiba mpya, Askofu Benson Bagonza wa Kanisa la Kilutheri alitanabaisha kuwa kamwe hajawahi kuona polisi wakitumia risasi dhidi ya waandamanaji. "Nini kimebadilika?" aliulizwa.

Moja ya majibu kwa swali lake hilo ni "hakuna kikubwa (kilichobadilika)." Kunapokuwa na upinzani mkali kwenye chaguzi zilizopita, dola na chama tawala vimekuwa vikikimbilia kwenye ukatili. Kufanya vema kwa Chadema katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 kulipelekea angalau miaka miwili ya ukatili. Ilianza Januari 2011 ambapo polisi walitumia risasi dhidi ya maandamano ya wafuasi wa Chadema Arusha.
Februari 2012, wanaharakati 16 wa haki za binadamu walikamatwa kwa kuunga mkono mgomo wa madaktari. Agosti mwaka huohuo, polisi walimuua kwa risasi muuza magazeti huko Morogoro wakati wa maandamano ya Chadema. Mwezi uliofuata, mwandishi wa habari Daudi Mwangosi aliuawa na polisi kufuatia kupigwa na bomu la kutoa machozi huku akiwa amekandamizwa chini na polisi. Katika mwezi huohuo, kiongozi wa maandamano ya madaktari, Steven Ulimboka alitekwa, akateswa na kuachwa ajifie mwenyewe kwenye msitu nje ya jiji la Dar es Salaam, tukio linalodhaniwa kufanywa na maafisa wa TISS. Baadaye mwaka huo huo, na pia Mei 2013, njia za kikatili zilitumika kukabiliana na maandamano yaliyoambana na wimbi kubwa la machafuko katika historia ya Tanzania.

CCM inakabiliwa na changamoto kubwa kudumisha utawala wake. Kwa kutoongelea suala la ufisadi mkubwa (katika kampeni zake za uchaguzi mkuu wa) mwaka 2015, ilitoa fursa kwa Chadema kupata mafanikio (ya kuridhisha) katika uchaguzi huo. Wimbo la ukandamizaji linaloendelea hivi sasa, linailenga Chadema, na pia linachangiwa na hofu kuhusu vikundi vyenye msimamo mkali vyenye silaha (kama ilivyokuwa huko MKIRU).

Sintofahaumu hiyo inaweza kueleza ukatili mkubwa uliotumika kukabiliana na kilichokuwa kikijiri katika mkoa wa Pwani. Miili kadhaa iliyofungwa kwenye 'viroba' iliyokutwa inaelea maeneo ya (Msasani) Peninsula jijini Dar es Salaam inaashiria jinsi hali ilivyokuwa.

Wizara ya Mambo ya Nje ilitoa tamko masaa tu baada ya tovuti ya African Arguments ya Royal African Society kuchapisha habari iliyoeleza kuhusu matumizi ya silaha za moto dhidi ya waandamanaji huko wilayani Rufiji katika ofisi za halmashauri ya mji.

Kwa kuunganisha vitendo vya vikundi hivyo vilivyokuwa vinavyotumia silaha (huko MKIRU) na upinzani dhidi ya mageuzi yanayofanywa na Magufuli, inatoa kisingizio kwa dola kutumia nguvu dhidi ya makundi yote mawili (vikundi vya MKIRU na upinzani dhidi ya Magufuli).

Mkuu wa Majeshi Jenerali Venance Mabeyo aliwataka Watanzania kuwa wazalendo dhidi ya tishio kwa amani, umoja, uhuru na mshikamano. Kichekesho ni kwamba aliyasema hayo katika maadhimisho ya viongozi waliopambana na utawala wa mkoloni mwaka 1907 katika Vita ya Maji Maji. Jinsi dola inavyopambana na vurugu na upinzani inarejesha kumbukumbu za jinsi serikali ya mkoloni ilivyopambana na upinzani dhidi yake.

Mafanikio yoyote ya kuelezea kuhusu tishio linaloukabili demokrasia nchini Tanzania yatategemea zaidi makundi mbalimbali ndani ya CCM na tabaka tawala. Wanaoonekana kama wapinzani ndani ya CCM kama Nape na Bashe watabaki ndani ya chama hicho kwa gharama yoyote, wakicheza mchezo mrefu wa subira hadi uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 ambapo inatarajiwa Magufuli atamaliza muda wake.

Viongozi wa dini – Magufuli anajitambulisha kama Mkatoliki mcha Mungu – wanaweza kufanikiwa kumshawishi kupunguza matumizi ya vyombo vya dola dhidi ya upinzani. Lakini wanaharakati na wanasiasa wa upinzani wanafahamu fika kuwa kudhibitiwa kwa asilimia 100.

MHALAKI (SOCIALITE) AONGOZA MAPAMBANO KUPITIA MTANDAO WA KIJAMII WA INSTAGRAM

Mashtaka yanayofunguliwa na taasisi za kiraia na matamko ya viongozi wa dini ni kitu kimoja, lakini wito wa kufanyika maandamano unaotolewa na bloga mwenye makazi yake Los Angeles (Marekani), Mange Kimambi, ni changamoto tofauti kabisa kwa Magufuli. Kimambi amekuwa sura ya hadharani ya wito wa maandamano ya nchi nzima tarehe 26 Aprili dhidi ya Magufuli.

Akifahamika zaidi kwa masuala ya fasheni na habari zinazohusu watu maarufu, akaunti ya Instagram ya Kimambi imekuwa ikihamasisha na kuyapa umaarufu maandamano hayo, yanayotarajiwa kufanyika siku ya Muungano, ambayo ni kumbukumbu ya Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar.

Kimambi anayedhaniwa kuwa anashirikiana na wanaharakati nchini Tanzania, anachukuliwa kwa uzito mkubwa na mamlaka za nchi hiyo. Akiongea kwenye tukio moja Machi 9 kijijini kwake Chato, Magufuli alisema "tusubiri na tuone wakiandamana, na watanitambua." Siku chache kabla, Waziri wa Mambo ya Ndani Mwigulu Nchemba aliwatuhumu waandaaji wa maandamano hayo kuwa wanapanga kuuwa watu na kisha kuvitupia lawama vyombo vya dola. Maonyo mengine yametolewa na angalau makamanda wa polisi wa mikoa saba. Inafahamika kuwa viongozi wa serikali na chama (tawala) wameelekezwa kuhamasisha upinzani dhidi ya maandamano hayo na tayari watu kadhaa wameshakamatwa.

Kimambi ni mwanaharakati ambaye haingekuwa rahisi zamani kumtarajia. Alipata umaarufu mwaka 2009 kupitia blogu yake ya 'U-Turn' ambayo ilikuwa ikisimulia kuhusu maisha yake kama mhalaki huko Dubai. Baadaye alihamia katika makazi yake ya sasa, Los Angeles, kabla ya kuanza kuiteka Instagram mwaka 2015, ambapo alimpigia Magufuli kampeni yenye ufanisi, licha ya yeye kushindwa kuteuliwa kugombea ubunge jimbo la Kinondoni.

Alimgeuka Magufuli takriban Mei 2016 ambapo alipinga vikali kusitishwa kwa matangazo ya moja kwa moja ya vikao vya bunge. Anachanganya upinzani wa kisiasa na nguvu yake kama mhalaki anayeweza kumjenga au kumbomoa mtu kwa kutumia mitandao ya kijamii. Awali ilikuwa kuhusu picha zake binafsi na "selfies" lakini baadaye mabadiliko yakajitokeza. Kufikia mwishoni mwa mwaka 2016, akaunti yake ikawa sehemu kuu ya harakati za mtandaoni za upinzani dhidi ya serikali, na sehemu ya kuona nyaraka mbalimbali zilizovuja.

Akaunti yake imechukua nafasi ya Jamii Forums, jukwaa la maoni mtandaoni lililokuwa kitovu cha upinzani mtandaoni, na ambalo waanzilishi wake wanakabiliwa na kesi mahakamani na wamekuwa wakisumbuliwa na mamlaka kwa muda mrefu.

Huku akiwa na wafuasi zaidi ya milioni 1.4* kwenye Instagram, uwezo wa Kimambi kuwafikia watu unawazidi wanasiasa wote wa Tanzania, japo kuna shaka kuhusu maandamano ya April 26. Kujitokeza kwa watu wengi kwenye maandamano hayo kutategemea uwezo wa waandaaji wake wa maandamano hayo nchini Tanzania, ambao wanaokabiliana na utawala usio na huruma – polisi watamwaga risasi kwa ajili ya kuuwa, kama ambavyo wamefanya huko nyuma.

Haitojalisha hata kama hakuna mtu atayejitokeza kuandamana Aprili 26. Kutoka umbali wa kilomita 26,000, Kimambi tayari ameweza kufanya zaidi ya kutikisa mkia wa chui kwa kutumia simu ya mkononi tu. Na laiti ikitokea asalimisha yeye mwenyewe, mara moja kukamatwa kwake kutakuwa tukio kubwa kabisa litakaloiweka Tanzania kwenye macho na masikio ya dunia nzima.

MAELEZO YANGU: Makala hii ni tafsiri ya neno kwa neno ya makala ya gazeti maarufu la duniani la habari za kuchunguza kuhusu bara la Afrika la AFRICA CONFIDENTIAL Toleo laMachi 28, 2018 lililokuwa na kichwa cha habari "Enemies Without And Within."

Nimejitahidi kadri nilivyoweza kufanya tafsiri ya karibu kabisa kutoka Kiingereza kwenda Kiswahili. Ni vigumu kufanya tafsiri timilifu kwa asilimia 100 hasa pale mwandishi na mtafsiri ni watu wanaoongea lugha mbili tofauti. Ni rahisi kwa mtu aliyeandika mwenyewe kufanya tafsiri ya alichoandika kuliko kazi hiyo kufanywa na mtu mwingine.
* Idadi ya "followers" kwenye akaunti ya Mange kwa sasa ni watu milioni 1.8.






24 Jan 2017

Mazingira yote yalikuwa 'yameiva' kwa vyama vya upinzani kufanya vizuri kwenye chaguzi za madiwani. Angalau kwenye uchaguzi mdogo uliofanyika Zanzibar, vyama vya upinzani 'vya Bara' (Chadema, ACT- Wazalendo, nk, isipokuwa CUF) vinaweza kuwa na 'kisingizio' kuwa upinzani huko, kwa maana ya CUF pekee, umepaganyika mno na isingekuwa rahisi kuchukua jimbo la Dimani. 

Lakini vyama vyetu vya upinzani haviwezi kuwa na excuse ya maana kutokana na matokeo mabaya kabisa waliyopata katika chaguzi hizo. 

Mwaka juzi, wakati Tanzania yetu inakwenda kwenye uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani, uchaguzi ambao mie binafsi nililazimika kumpigia debe mgombea wa CCM, Dkt John Magufuli, baada ya 'Chadema kutusaliti' kwa kumpokea aliyekuwa kada maarufu wa CCM, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, niliwakumbusha mara kwa mara ndugu zangu wa UKAWA kwamba, kwanza, ni ukosefu wa busara kutegemea vyama vya upinzani kufanya vema katika mazingira yaleyale yaliyowafanya wafanye vibaya katika chaguzi zilizotangulia.

Vyama vya upizani vilivyoshiriki katika chaguzi hizo za madiwani viliingia vikiwa katika mazingira yaleyale yaliyovifanywa vibwagwe na CCM katika uchaguzi mkuu wa 2015.

Kibaya zaidi, hadi leo, si Chadema, NCCR Mageuzi, CUF au ACT-Wazalendo waliofanya 'post-mortem' (taarifa ya uchunguzi inayoeleza chanzo cha kifo) ya kwanini vyama husika vilifeli. Badala ya kufanya tathmini ya kina kuhusu sababu zilizovikwamisha vyama hivyo mwaka 2015, kumekuwa na mwendelezo wa porojo kuwa "njia ya Ikulu 2020 ni nyeupe."

save image


Kama kuna chama ambacho kinapaswa 'kusikia maumivu zaidi' kutokana na matokeo ya chaguzi hizo basi ni Chadema, kwa sababu wafuasi wa chama hicho - na kidogo ACT-Wazalendo - ndio pekee miongoni mwa vyma vyote vya upinzani nchini Tanzania, kuendeleza harakati za siasa, licha ya zuwio la serikali ya Rais Magufuli.

Kwamba, zuio hilo halijaathiri wafuasi wa Chadema kutumia teknolojia ya  mitandao ya kijamii, kuanzia Twitter, Whatsapp, Facebook, Jamii Forums, nk kuiban a mfululizoCCM na serikali yake. 

Lakini hapohapo kuna walakini. Ndio, ni wajibu wa vyama vya upinzani kuikosoa CCM na serikali yake. Hata hivyo, kukosoa tu hakutoshi hasa pale ambapo panapohitajika ufumbuzi.

Mifano ni mingi, lakini tuchukulie tishio la baa la njaa. Wakati serikali ya Rais Magufuli na CCM wakisisitiza kuwa hakuna tishio hilo, vyama vya upinzani vikiongozwa na Chadema vimekuwa mstari wa mbele kuonyesha kuwa tatizo hilo lipo.

Lakini kuonyesha tatizo tu bila kujaribu kutafuta ufumbuzi sio busara sana. Na baadhi yetu tulipomsikia Lowassa akisema, namnukuu "Serikali imesema haitoi chakula, mimi nimejadiliana na chama changu tumeona tufanye mpango wa kuwatafutia chakula Watanzania.”

Hicho chakula kiko wapi? Kuwapa wananchi matumaini kisha kutotekeleza ahadi husika ni hadaa. Lakini kuna wanaoshangaa eti "mbona licha ya 'kiburi cha serikali ya CCM kuhusu tishio la njaa' badi chama hicho kimeibuka kidedea kwenye chaguzi za madiwani?"

Jibu jepesi ni kwamba CCM "is the devil they know," kwamba pamoja na mapungufu yake, inaweza kutoa mifano hai ya ilivyowahi kuwasaidia wananchi siku za nyuma. Na hata kama inafanya 'kiburi' kuhusu tishio la njaa, angalau "haijatoa ahadi hewa" kama hiyo ya Bwana Lowassa.

Hebu pata picha: siku chache kabla ya chaguzi hizo, CCM 'yajipiga bao yenyewe' kwa kushikilia msimamo kuwa hakuna njaa na hata ikiwepo hakutokuwa na chakula cha msaada. Chadema kwa kushushiwa bahati hiyo, wanachangamka, wanakusanya misaada ya chakula, na kufanya harambee ya kuwasaidia watu wenye uhaba wa chakula. Naam, pengine serikali ingetaka kuingilia, lakini ninaamini nguvu ya umma ingekuwa upande mmoja na Chadema katika dhamira yao hiyo nzuri. Kwa bahati mbaya imebaki kuwa nzuri tu, na haijatekelezwa.

Kutekelezwa kwa ahadi hiyo kungeweza kutafsiriwa na CCM kama rushwa kwa wapigakura lakini mwenye njaa anachojali ni mkono kwenda kinywani na wala sio amepewa chakula kama msaada au rushwa. Ninaamini kabisa kuwa laiti ahadi ya Lowassa na Chadema yake kuhusu kuwasaidia wananchi wanaokabiliwa na baa la njaa ingetimizwa, basi pengine muda huu chama hicho kingekuwa kinachelekea ushindi.

Tukiweka kando suala hilo, ndugu zangu wa Upinzani, hususan Chadema wameendelea kuwa na imani fyongo kuwa "CCM inachukiwa mno," na "chuki hiyo dhidi ya CCM itapelekea kura kwa Wapinzani." Wanachopuuza ndugu zangu hawa ni ukweli kwamba udhaifu wa CCM sio uimara wa Upinzani. 

Ikumbukwe kuwa wakati CCM inaweza kusubiri hadi mwaka 2020 ili ianze kampeni za kubaki madarakani, Wapinzani wanapaswa kutumia muda huu kuwaonyesha Watanzania kuwa wao wanaweza kuwa mbadala wa kweli wa CCM. Lakini tunachoshuhudia ni Upinzani kuwa 'bize zaidi' kuiongelea CCM badala ya kutenda vitu vitakavyowapa matumaini Watanzania kuwa vyama hivyo ni mbadala sawia.

Ndugu zangu wa Chadema wana mtihani mkubwa zaidi. Pengo lililoachwa na Dokta Slaa limeshindwa kuzibika. Katibu Mkuu aliyepo madarakani anaweza kukisaidia sana chama hicho akiamua kuachia ngazi kwa hiari yake mwenyewe. Ninaamini mtu kama Godlisten Malisa, kada mwenye uwezo mkubwa, anaweza kushika wadhifa huo na akaibadili Chadema. 

Kwa upande mwingine, Mwenyekiti wa chama hicho Bwana Freeman Mbowe, yupo kwenye wakati mgumu mno pengine kuliko muda wowote ule wa maisha yake ya kisiasa. Mbowe anaandamwa na madeni yanayoweza kuathiri mno biashara zake. Japo deni sio jinai, kiongozi wa upinzani kuandamwa na madeni au kutolipa kodi kwa miaka kadhaa ni kitu kinachotoa taswira mbaya kwa wananchi.

Kuna lawama kadhaa zinazorushwa kwa Rais Magufuli kuwa anazitumia taasisi za serikali kama  vile TRA na NHC "kumwandama" Mbowe, lakini ukweli ni kwamba dawa ya deni ni kulipa. Na Chadema inaweza kuingia matatani ikitetea "ukwepaji kodi wa Mbowe" kwa sababu sote twajua kuwa hilo ni kosa (japo si la jinai).

Halafu kuna hizi 'drama' zinazoweza kuwavunja moyo watu wasio na chama lakini wanatafuta chama cha kukiunga mkono. Suala la 'kupotea' kwa kada wa Chadema, Ben Saanane, limeacha doa kubwa kwa chama hicho. Kwa upande mmoja, ilichukua wiki tatu tangu kada huyo adaiwe kupotea kabla ya uongozi wa chama hicho kutoa tamko rasmi. Lawama zaidi zaweza kwenda kwa Mbowe kwa vile Ben alikuwa msaidizi wake binafsi. 

Na Chadema walipotoa tamko rasmi kukfuatiwa na mkanganyiko mkubwa zaidi: huku Mbowe anadai Ben katekwa, kule Tundu Lissu anadai vyombo vya dola vinajua kada huyo yuko wapi, na pale, gazeti la Mwanahalisi la mbunge wa chama hicho Saed Kubenea likaeleza kuwa "Ben yupo, amekuwa akionekana kwenye vijiwe vya chama hicho." Na baada ya jithada fupi mtandaoni zilizoambatana na alama ya reli #BringBenBackAlive na kuchapishwa fulana, suala hilo limekufa kifo cha asili. Huu ni uhuni wa kisiasa maana hatutegemea chama makini kinachojitanabaisha kuwa mbadala wa CCM kuendesha mambo yake kienyeji hivyo.

Kuna tatizo jingine ambalo Chadema wamekataa katakata kulishughulikia. Kabla ya kumpokea Lowassa, ajenda kuu ya Chadema ilikuwa vita dhidi ya ufisadi. Ujio wa Waziri Mkuu huyo wa zamani ulikilazimisha chama hicho kuachana na ajenda hiyo ambayo kwa kiasi kikubwa sana ndio iliyokiwezesha chama hicho kuwa chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania.

Na kwa vile Rais Magufuli amejaribu kuifanya vita dhidi ya ufisadi kuwa moja ya ajenda zake kuu, Chadema kwa muda huu haina ajenda kuu yenye mvuto kwa wananchi. Chama hicho kimegeuka kuwa cha kusubiri matukio kisha kuyadandia. Sawa, ni kazi ya vyama vya upinzani kukikosoa chama tawala/kuikosoa serikali, lakini hiyo sio kazi pekee. Na kwa kusubiri matukio, Chadema inakuwa kama "inaendeshwa na CCM."

Niliandika kwa kirefu katika vitabu vyangu viwili kuhusu uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, kimoja kabla ya uchaguzi huo na kingine baada, kwamba asilimia kubwa ya wapigakura nchini Tanzania sio wanachama wa CCM au vyama vya upinzani. Kwamba mtaji  mkubwa kwa chama chochote kinachotaka kushinda uchaguzi ni ku-win hearts and minds za hao wasio na chama chochote. Kundi hili ndilo lililompa ushindi Magufuli mwaka 2015.

Katika hilo, tatizo kubwa la vyama vyetu vya upinzani ni 'kudanganganyana wao kwa wao kuhusu mshikamano, umoja na wingi wao.' Badala ya kufanya jtihada za ku-reach out kudni la watu wasio na vyama, wao wapo bize kuhamasishana wenyewe kwa wenyewe. Basi angalau kuhamasishana huko kungeendana na kuwavuta watu wasio na vyama, ambao ni turufu muhimu kwenye chaguzi zetu.

Nilwahi kuandika huko Facebook, kuwa 'hasira sio mkakati (wa kisiasa)' kwa kimombo "anger is not a strategy.' Sio siri kuwa wafuasi wa upinzani wana hasira, ni hii sio dhambi wala kosa, lakini wanakosea kudhani kuwa hasira hiyo itawaletea mafaniko ya kisiasa. Hawataki kujifunza kwenye mifano hai ya hasira ambazo zimebaki kuwa hasira tu: hasira dhidi ya Tanesko zimeshindwa kuifanya taasisi hiyo iache uhuni wa mgao wa umeme wa milele; hasira dhidi ya huduma mbovu zinazotolewa na baadhi ya makampuni ya simu hazijaziathiri kwa namna yoyote ile; hasira dhidi ya TFF haijaweza kuifanya Taifa Stars iache kuwa kichwa cha mwendawazimu.

Hasira ili iwe na manufaa shurti iambatane na programu makini ya kuleta mabadiliko kusudiwa. Na hili liliusiwa na Dkt Slaa, kwamba mabadiliko ya kweli yatapatikana tu kwa kuwa na programu makini zitakazohusisha watu makini.

Pengine wapinzani watajitetea kuwa zuio la Dkt Magufuli linalokataza mikutano na maandamano ya vyama vya siasa (isipokuwa CCM) limewaathiri kwa kiasi kikubwa katika kujitengenezes mazingira bora ya ushindi kwenye chaguzi hizo. Mie siafikia kabisa zuio hilo la Rasi Magufuli, lakini wapinzani wangeweza kulitumia 'kumpiga bao yeye na CCM' kwa kulitekeleza kwa kuelekeza nguvu zao 'mtaani,' kuwatumikia wananchi zaidi ya 'wanavyoangushwa na CCM/Serikali.'

Nihitimishe makala hii kwa kutoa wito kwa vyama vya upinzani kukaa chini na kufanya post-mortem ya chaguzi za madiwani, na kutengeneza programu makini (sio hizo operesheni zisizo na kichwa wala miguu) zitakazosimamiwa na kutekelezwa na watu makini. Na wafuasi wa vyama hivyo waache kupoteza muda mwingi kwenye kukosoa tu CCM na serikali huku wakikwepa kuelekea focus yao kwenye vyama vyao. Ni hivi, kama vyama vya upinzani vimeweza kumng'oa moja wa madikteta hatari duniani huko Gambia, Yahya Jammeh, basi hakuna sehemu ambapo upinzani hauwezi kukiong'oa chama tawala madarakani. Lakini hilo halitotokea kwa kujidanganya kuwa "CCM inachukiwa sana." Kuchukiwa kwa CCM sio kupendwa kwa Chadema, au Cuf, au chama kingine cha upinzani. 

ANGALIZO: Mada husika ilikuwa kwa ajili ya makala kwenye gazeti la Raia Mwema lakini nimechukua mapumziko ya uandishi wa makala kwenye gazeti hilo wakati nikisubiri marekebisho flani kutoka kwao.


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.