Showing posts with label GORDIAN MAPANGO. Show all posts
Showing posts with label GORDIAN MAPANGO. Show all posts

1 Nov 2008

Picha kwa hisani ya SPOTI NA STAREHE

Ubabaishaji unakwamisha sana maendeleo ya taifa letu.Lakini hapa nataka nizungumzie ubabaishaji kwenye uongozi na uendeshaji wa vilabu vya Simba na Yanga.Hebu soma kwanza hapa chini kabla hatujaendelea na mada hii ya kupotezea muda.
MWENYEKITI wa klabu ya Simba Hassan Dalali amemteua Mkurugenzi wa Kampuni ya Aurora Security, Ally Suleiman kuwa mshauri wake atakayesaidia kumshauri kuhusiana na mambo yote yanayohusu masuala ya uongozi wa Simba. 

Akizungumza Dar es Salaam jana, Dalali alisema ameamua kuwa na mshauri ili aweze kuiendesha klabu yake kwa umakini na kufuata mwongozo ambao utaisadia klabu hiyo. 

Dalali alisema Suleiman amekuwa mtu wa karibu, ambaye ametoa mchango mkubwa ndani na nje ya klabu, hivyo ameona ni muhimu na kuwa uteuzi huo ni kujenga Simba yenye umoja na mshikamano.
Alisema klabu yake ipo katika mikakati ya kuhakikisha Simba inakuwa klabu kubwa, huku ikiimarisha timu yake na kuwa mfano wa kuigwa. 

"Uteuzi wa mshauri wangu umezingatia vigezo vingi ikiwemo ukaribu wake katika mambo ya msingi yanayoihusu klabu yetu," alisema Dalali.

Akizungumzia uteuzi huo, Suleiman alisema amefurahi kupata wadhifa huo na kuahidi kuisaidia klabu hiyo kwa hali na mali lengo likiwa ni kujenga Simba imara
CHANZO:Majira
Baada ya kufungwa na Yanga ndio Dalali anakumbuka umuhimu wa kuwa na mshauri!?Kwa tafsiri nyingine ni kwamba kwa muda wote tangu apate uenyekiti wa Simba m-babaishaji huyu amekuwa akiongoza kwa kubahatisha.Ndio!Kama sio hivyo,mshauri wa nini muda huu? Yaani ni ubabaishaji juu ya ubabaishaji.

Mimi ni mpenzi wa Simba.Zamani Simba ikifungwa basi ni majonzi makubwa.Katika familia yetu,watoto wote wanane tunaipenda Simba.Marehemu Mama (Mungu Amlaze Mahali Pema Peponi) alikuwa mpenzi wa Pan Africa,kwa sababu mpwae,Gordian Mapango,alikuwa mchezaji wa timu hiyo.Baba aliamua kuisapoti Yanga,sio kwa vile anaipenda bali kuleta "usawa" ndani ya familia.

Kwa miaka kadhaa sasa,nimebaki kuwa mpenzi-jina tu,it doesnt really make any difference Simba ikishinda au ikifungwa.Sababu kuu ya kupoteza mapenzi kwa Simba,na soka ya Tanzania kwa ujumla,ni ubabaishaji uliopita kiasi wa viongozi wa klabu hiyo kongwe.Ubabaishaji huo umepelekea timu hiyo kukimbiwa na wafadhili kibao na kupoteza udhamini mbalimbali.Nani mwenye akili timamu atawekeza kwenye biashara kichaa?Ukiona mtu anapanda mpunga jangwani basi hicho sio kilimo bali tambiko.Ndo maana nashawishika kuamini kwamba uwepo wa Manji hapo Yanga unaweza kuwa ni "zaidi ya mambo ya soka".

Nirudi kwenye title ya post hii.Nilitegemea Simba ingefungwa na Yanga.Na nilitegemea kipigo kikubwa zaidi ya hilo bao moja.Kama Toto Africa waliweza kutufunga bao 4-1,tungetegemea nini katika mechi na Yanga?Anyway,kipigo ni kipigo.Mategemeo yangu ya kipigo yametimia,japo kwa idadi tofauti na niliyokuwa naitarajia.Kingine nilichadhani kingeandamana na kipigo hicho ni kuutimua uongozi mzima wa Simba.Hilo halijatokea lakini naamini viongozi hao wamekalia kuti kavu.By the way,uongozi wa Simba na Yanga ni zaidi ya kukalia kuti kavu;ni sawa na kibonge cha mtu kuning'inia kwenye utando wa buibui.Mtu mwenye mtizamo makini hawezi kutamani kuongoza timu hizi za kibabaishaji,ambazo lugha wanayoelewa "wanachama" ni ushindi tu.

Of course,timu inatakiwa ishinde kila mechi.Lakini timu itashinda vipi ikiwa haina vyanzo vya mapato zaidi ya kutembeza bakuli kama ombaomba?Hao wachezaji wanakula nini kabla ya kujituma uwanjani?Au ni timu za kiroho ambapo Neno la Mungu linashinda mahitaji ya fedha na vifaa?Kwanini wachezaji wasipokee rushwa iwapo viongozi wanawaibia mishahara yao kiduchu inayopatikana kwa migomo?Wanachama wababaishaji wa klabu hizi wanajua kupiga majungu tu lakini hawana mchango wowote kwa ustawi wa klabu hizi.Ndio maana akiondoka mfadhili mmoja timu inakuwa hohehahe.Na ndio maana Manji amekuwa mungu-mtu hapo Yanga (na mwenyekiti Madega amegeuka kuwa msemaji wa familia ya mfadhili kuhusu ugonjwa wa mfadhili huyo!)

Je kuna ufumbuzi wa tatizo hili la ubabaishaji wa viongozi na wanachama wa Simba na/au Yanga?Kwa mtizamo wangu nadhani ufumbuzi upo lakini unahitaji udikteta wa aina flani.Unajua kuna udikteta kwa ajili ya watu na udikteta dhidi ya watu.Udikteta kwa ajili ya watu ni kama ule wa Sokoine:kwa wahujumu wa uchumi Sokoine alikuwa dikteta,lakini kwa wananchi wengi kiongozi huyo alikuwa ni shujaa na mkombozi.Sihitaji kuelezea dikteta dhidi ya watu ni wa aina gani,lakini anaweza kuwa hata anayethamini haki za binadamu za mafisadi wachache badala ya walalahoi walio wengi.Je udikteta kwa ajili ya watu unawezaje kuokoa vilabu vyetu na soka la Tanzania kwa ujumla?Ni kwa serikali kutumia sheria kali katika kuleta mageuzi ya kudumu katika vilabu vya soka.Najua kuna ishu za watu kwenda mahakamani kupinga maamuzi flani,lakini ukweli unabaki kwamba sheria zikiandaliwa na kusimamiwa vizuri basi wahuni wanaokimbilia mahakamani watafyata mkia.Njia nyepesi ya kuvibana vilabu hivyo ni kutunga sheria inayovitaka kujisajili upya,kwa mfano.Pia sheria hiyo inaweza kutamka bayana aina ya viongozi,namna ya uendeshaji wa vilabu unavyopaswa kuwa na hata aina za wanachama.FIFA itatufungia kwa vile serikali imeingilia mambo ya soka?Why care!kwani sasa hatujafungiwa na tumeendelea kuwa kichekesho kila mwaka?Bora tu tufungiwe ili tuweze kujipanga vyema kuliko kuendeleza ubabaishaji huu.Au msomaji unasemaje?

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.