Showing posts with label HAPPY NEW YEAR 2017. Show all posts
Showing posts with label HAPPY NEW YEAR 2017. Show all posts

5 Jan 2017

KHERI ya mwaka mpya 2017. Kama ilivyo kawaida ya safu hii, kila makala ya mwanzo wa mwaka hujikita kwenye ubashiri wa masuala mbalimbali yanayotarajiwa katika mwaka mpya husika.
Kutokana na ufinyu wa nafasi, ubashiri kuhusu mwaka huu mpya utaelemea zaidi katika mwenendo wa siasa kitaifa na kimataifa.
Kimataifa, mtihani wa kwanza kabisa wa siasa za kimataifa utaanza Januari 20, 2017 siku ambayo Rais mteule wa Marekani, Donald Trump ataapishwa rasmi.
Ni vigumu kubashiri nini kinaweza kutokea siku ya kwanza tu tangu Trump aapishwe, lakini kilicho bayana ni uwezekano mkubwa kwa tajiri huyo, aliyeshinda urais katika mazingira ya kushangaza yaliyoambatana na kila aina ya hadaa, si tu kuendelea kuwa ‘kituko’ bali pia hata kuhatarisha usalama wa kimataifa.
Wakati wa kampeni za urais, profesa mmoja wa historia ya siasa, Allan Lichtman, alibashiri kuwa Trump angeshinda licha ya kura za maoni kuonyesha mgombea kwa tiketi ya Democrats, Hillary Clinton akiongoza. Nilikerwa sana na ubashiri wa profesa huyo.
Baada ya Trump kumbwaga Hillary, Profesa Lichtman aliibuka na ubashiri mwingine, akidai kuwa urais wa tajiri huyo utakuwa wa muda mfupi tu kwani atang’olewa madarakani pengine kabla ya kutimiza mwaka madarakani. Nami ambaye awali nilikerwa na profesa huyo sasa natamani ubashiri wake utimie.
Na kwa hakika kati ya mambo yanayoweza kutokea mwaka huu ni Trump kuondolewa madarakani. Lakini hilo si kubwa kulinganisha na uwezekano wa machafuko nchini humo hususan, baada ya wapigakura kubaini kuwa ‘waliingizwa mkenge’ na tajiri huyo.
Ikumbukwe huyu atakuwa ndiye rais wa kwanza aliyeingia rasmi madarakani kwa udanganyifu na hadaa.
Jingine kuhusu Trump ni uwezekano wa kuwatibua washirika wa Marekani miongoni mwa mataifa ya Kiislamu, kama vile Saudi Arabia, Jordan na Pakistan. Uwezekano huo unatokana zaidi na msimamo wa kibaguzi wa Trump na wengi wa wasaidizi wake.
Kadhalika, kuna uwezekano uswahiba kati ya Trump na Rais wa Urusi, Vladimir Putin, ‘ukatumbukia nyongo,’ kwa sababu mataifa hayo yana mgongano wa kimaslahi. Vilevile, kuna uwezekano wa dalili za mgogoro kati ya Marekani na China kupanuka zaidi, chanzo kikiwa Trump huyohuyo.
Kwingineko kimataifa, Uholanzi itafanya uchaguzi wake mkuu Machi, Ufaransa Aprili hadi Juni, na Ujerumani Oktoba.
Chaguzi hizo ni mtihani mgumu kwa nchi hizo kutokana na tishio kubwa kutoka kwa vyama vyenye mrengo mkali wa kulia ambavyo vinazidi kupata umaarufu barani Ulaya kutokana na matishio ya ugaidi, ambayo pia yanahusishwa na sera za kukaribisha wahamiaji.
Chaguzi nyingine zinazotarajiwa kugusa hisia ni nchini Hong Kong (Machi), Iran (Mei) na Korea ya Kusini (Desemba).
Japo kuna dalili za amani huko Syria kufuatia jitihada zinazofanywa na Russia, kuna uwezekano kwa nchi hiyo kujikuta kwenye machafuko zaidi hasa ikizingatiwa kuwa serikali ya Rais Bashir Assad inamiliki sehemu tu ya nchi hiyo, huku sehemu nyingine zikiwa chini ya makundi mbalimbali.
Hali ya usalama nchi Uturuki inatarajiwa kuendelea kuwa tete, kutokana na matishio makuu mawili, ya vikundi vya Kikurdi vinavyopigania uhuru na kikundi cha kigaidi cha ISIS, ambacho pia kinatarajiwa kuendelea kuwa tishio katika eneo la Ghuba, nchi za Ulaya Magharibi na Marekani.
Barani Afrika, mwaka huu kuna chaguzi kadhaa, lakini ambazo zinavuta hisia zaidi ni nchini Kenya mwezi Agosti na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ambako hali bado ni ya wasiwasi kutokana na jitihada za Rais Joseph Kabila kutaka kung’ang’ania kuwa madarakani ingawa tayari kuna maneno kwamba amekubali kuachia ngazi.
Kuhusu majirani zetu wa Kenya, tatizo mara zote limekuwa kwenye siasa za ukabila. Kwa bahati mbaya, nchi hiyo itaingia kwenye uchaguzi wake mkuu wakati ‘kirusi cha ukabila kikiwa hai na chenye nguvu.’
Tukigeukia huko nyumbani, mwaka huu utashuhudia CCM ikifanya uchaguzi wake ndani. Tunasubiri kuona jinsi ambavyo Mwenyekiti wa Taifa, Rais Magufuli, atachezesha kete zake.
Ifahamike kuwa licha ya mwonekano kuwa ‘CCM ni wamoja,’ ukweli ni kwamba ndani ya chama hicho kuna ‘mambo yanayoendelea chinichini.’
Kwa upande mmoja, kwa muda mrefu CCM imekuwa hifadhi ya ‘watu mbalimbali wenye wasifu usiopendeza,’ ikiwa ni pamoja na mafisadi. Hawa ni wahanga wa wazi wa jitihada za Rais Magufuli kupambana na ufisadi. Yayumkinika kuhisi kuwa wanaweza kutumia uchaguzi huo kama fursa ya kujipangia vema kumdhibiti Dk. Magufuli katika uchaguzi wa mgombea urais mwaka 2020.
‘Wapinzani wa Magufuli’ ndani ya CCM wanapewa nguvu na mtazamo wa baadhi ya wananchi mitaani kwamba hali ya maisha inazidi kuwa ngumu pasipo dalili za kupatikana nafuu hivi karibuni.
Wakati wengine twaelewa kuwa ‘inabidi tupitie maumivu kabla ya kupata nafuu,’ kwa baadhi ya wananchi ‘mtaani’ wanaona kama utawala wa Magufuli ni wa ‘kuwapa maumivu mfululizo pasi dalili ya ahueni.’
Nje ya CCM, changamoto kubwa kwa utawala wa Rais Magufuli ni kuibuka kwa nidhamu ya uoga, ambapo taratibu kunaanza kujengeka hisia kuwa ‘kiongozi atayediriki kupishana kimtazamo na Rais, atatumbuliwa.’
Nidhamu ya uoga haiwezi kuleta tija wala ufanisi. Wakati ninaandaa makala hii nilipewa taarifa kuhusu tishio la janga la njaa kwenye wilaya kadhaa lakini inadaiwa kuwa watendaji katika maeneo hayo wanahofia kutoa taarifa kwa wakichelea kutumbuliwa.
Ili dhamira ya Dk. Magufuli kuiletea neema Tanzania itimie kwa kuongeza kasi ya uzalishaji mali na mchango wa sekta mbalimbali kwenye uchumi, sambamba na kukabiliana na rushwa na ufisadi, ni lazima Watanzania wawe ‘kitu kimoja.’
Serikali ya Dk. Magufuli inapaswa kuepuka ‘ugomvi usio wa lazima’ hasa matamshi ya kuwafanya watu wazima wajione kama watoto, ‘maguvu’ badala ya busara, na kutofanya haki za Watanzania kuwa zawadi kutoka kwa watawala.
Uamuzi wa kufuta matangazo ya moja kwa moja ya Bunge, kuzuwia mikutano na maandamano ya vyama vya siasa, viongozi wa Upinzani kubughudhiwa mara kwa mara, kubinya uhuru wa habari  ambao japo waweza kutumika vibaya, ni muhimu katika ujenzi wa utawala bora. Na bila kuuma maneno, Rais Magufuli asizuwie kukosolewa.
Kwa upande wa vyama vya Upinzani, dalili za suluhu katika mgogoro wa CUF ni ndogo. Kadhalika, ‘afya’ ya ACT Wazalendo inaweza kuendelea kudhoofika, tatizo likiwa ugumu wa ‘siasa za chama cha mtu mmoja.’
Kwa Chadema, kunaweza kuibuka harakati za kudai mabadiliko ndani ya chama hicho hasa kutokana ukweli kuwa chama hicho kwa sasa hakina ajenda ya kitaifa zaidi ya ‘kudandia hoja.’
Nihitimishe makala hii kwa kukumbushia kuwa ubashiri si ‘sayansi yenye uhakika wa asilimia 100 (exact science). Ubashiri huu umetokana na uchambuzi mienendo (trends) mbalimbali na si uhakika kuwa ‘lazima itakuwa hivi au vile.’
Niwatakie tena heri ya mwaka mpya 2017.


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.