Showing posts with label HIGHER EDUCATION IN TANZANIA. Show all posts
Showing posts with label HIGHER EDUCATION IN TANZANIA. Show all posts

16 Nov 2016

Moja ya vipaumbele vya Serikali ya Awamu ya Tano ya Rais Dkt John Magufuli ni ukusanyaji mapato, ikiwa ni pamoja na yale yatokanayo na madeni. Ni katika utekelezaji wa kipaumbele hicho, Bodi ya Mikopo kwa Wanafunzi wa taasisi za Elimu ya Juu (HESLB) imeanza 'msako mkali' dhidi ya 'wadaiwa sugu.' watu walionufaika na mikopo hiyo lakini hawajaanze kuirejesha.

Kwanza, nianze makala hii kwa kuipongeza serikali kwa hatua hii muhimu ambayo ikifanyika kw aufanisi, itasaidia ukusanyaji wa mapato makubwa yatakayowezesha udhamini wa serikali kwa wanafunzi wengi zaidi. Sote twatambua umasikini wa Tanzania yetu, na ni jukumu letu kuisaidia nchi yetu.

Binafsi, nilisoma kwa mkopo wa serikali kuanzia mwaka 1996 hadi nilipohitimu mwaka 1999. Wakati huo, na hadi ninaondokaTanzania mwaka 2002, hakukuwa na utaratibu wowote wa urejeshaji wa mkopo huo.

Hali hiyo imeendelea hadi mwaka huu 2016, ambapo ghafla serikali kupitia HESLB imeamka usingizini na kuanza kufuatilia fedha inayotudai, lakini sio kistaarabu (kwani sio kosa letu wadaiwa kutotengenezewa mfumo stahili wa kufanya marejesho ya mikopo tuliyopewa, bali kosa la serikali) na tunaitwa WADAIWA SUGU. Mdaiwa sugu ni mtu ambaye amedaiwa zaidi ya mara moja na hajalipa. Si sahihi kumwita mtu 'mdaiwa sugu' wakati hujamwelekeza jinsi ya kulipa deni unalomdai wala hujahangaika kumdai.



Sina hakika kama kuna watu walishawahi kupewa utaratibu wa kurejesha mikopo ya elimu waliyopewa, lakini kwa uelewa wangu na ufuatiliaji wa yanayojiri huko nyumbani, sijawahi kuona hilo.

Hata hivyo, kwa vile lawama hazijengi, na lengo la serikali 'kukurupuka' ni jema (kukusanya mapato), basi ni vema kuweka kando lawama na sote tunaodaiwa kuanza utaratibu wa malipo ya fedha tunazodaiwa.

Kwa upande wangu, nimetuma barua pepe kwa HESLB kuulizia kiwango ninachodaiwa na taratibu za malipo. 


Nimefainya hivyo ili, kwanza, kuunga mkono jitihada za serikali kukusanya mapato ikiwa ni pamoja na malipo ya mikopo tuliyokopeshwa. Pili, dawa ya deni ni kulipa. Ninawahamasisha wadaiwa wenzangu kuhusu umuhimu wa kulipa fedha tunazodaiwa. Na, tatu, ku- preempty jitihada zozote za watakaotaka kutumia suala hili la 'udaiwa sugu' kuchafua jina langu. Ni matarajio yangu kuwa kwa hatua hizi za dhati nilizochukua hakutajitokeza 'mchawi' wa kusema "ah wewe Chahali unajifanya mzalendo kumbe fisadi unadaiwa..." haha. 

Anyway, nitatumia ukumbi wangu huu kuwafahamisha majipu nitakayoletewa na HESLB na mustakabali wa 'udaiwa sugu.' 

14 Oct 2010


Profesa Nkunya na vyuo vya kutengeneza shahada.

Na Idd Amiri



Wiki iliyopita Profesa Mayunga Nkunya, Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania, aliongea na waandishi wa habari na baadaye akatoa tangazo juu ya kuwepo kwa vyuo vikuu visivyotambulika hapa nchini na huko nchi za nje vinavyotoa shahada za udaktari wa heshima wa falsafa kwa watu mbalimbali mashuhuri hapa nchini na kwingineko barani Afrika hususa ni kwa Wabunge, Mawaziri na hata Marais. Marais wetu wawili nao ni madaktari wa falsafa.

Katika tangazo lake kuhusu kuzuka kwa vyuo hivyo amebainisha kuwa kumekuwa na mbadilishano wa fedha kati ya wahusika na vyuo hivyo na hili ni kwa nia ya kujipa hadhi wasiyositahili waheshimiwa hao kwa wanajamii.

Profesa Nkunya amekuja na kauli hii baada ya Mheshimiwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi profesa Jumanne Maghembe, kutoa ufafanuzi juu ya kutolewa kwa shahada hizo kutoka katika vyuo hivyo ambavyo kwake yeye hakuviita visivyotambulika au vyuo vya kutengeneza shahada kama profesa Nkunya alivyoviita.

Profesa Maghembe alitoa ufafanuzi katika mkutano wa mwisho wa Bunge La Jamhuri ya Muungano wa Tanzania huko Dodoma, Waheshimiwa aliowataja Profesa Maghembe ni pamoja na aliyekuwa Mbunge wa Kwera, Mheshimiwa Chrisant Mzindakaya na Rais wa Zanzibar, Mheshimiwa Amani Abeid Karume.

Katika kikao hicho cha Bunge wakati wa kuchangia mijadala mbalimbali Mheshimiwa Juma Ngasongwa, ambaye kwa kiwango cha elimu au usomi ni daktari wa falsafa alilalamika kuwa pamoja na kuwa na shahada nzuri ya udaktari wa falsafa katika uchumi lakini haiitwi Member of the learned brothers!. Mara nyingi wanasheria huiitwa hivyo ingawa binafsi sijui inakuwaje msomi mwenye shahada ya kwanza awe katika kundi hilo na madaktari wa falsafa katika fani nyingine wasiwe katika kundi hilo, Kwa leo hilo siyo sehemu ya mjadala wangu.

Profesa Maghembe alisema kuwa Mheshimiwa Mzindakaya amepewa shahada ya heshima ya udakatari wa falsafa kwa kutambua mchango wake katika upenzi, ujenzi na maendeleo ya viwanda na Mheshimiwa Karume alitunukiwa shahada yake kwa kufanikiwa kutokomeza malaria katika visiwa vya Zanzibar.

Lakini hii si mara ya kwanza kuhojiwa kwa shahada za heshima za watu mbalimbali, katika vikao vya Bunge miaka ya nyuma huko Mheshimiwa Dr. Hansy Kitine aliwahi kuongelea suala hilo na aliyekuwa Waziri wa Elimu ya Juu Sayansi na Teknolojia Dr. Pius Sabasi Ng’wandu alimjibu kuwa haoni kama kuna ubaya wowote kwani hakuna madhara kwa mtu kupewa hadhi hiyo. Lakini hoja ya Kitine ilikuwa zaidi kwa maprofesa wa mitishamba. 

Kwa wale waliowahi kutembelea makumbusho ya Bagamoyo watakuwa wanamfahamu Profesa Kejeli, huyu jamaa ni mahiri kwa kuelezea historia ya mji wa Bagamoyo tena kwa kasi ya ajabu, Kumbukumbu za watu, miaka na mahali alizonazo profesa Kejeli kwa kweli zinakuacha mdomo wazi anaposimulia. Nilibahatika kumwuliza ilikuwaje akaitwa profesa alinijibu kuwa alipewa hadhi hiyo na Marehemu Meshack Maganga aliyekuwa Mkuu wa Chuo Cha Uandishi wa Habari Tanzania (TSJ).

Miaka mitatu iliyopita nilikuwa nikifuatilia mwendelezo wa kipindi cha kweli (Reality show) cha kila mwaka cha runinga ya shirika la utangazaji la uingereza (BBC) katika BBC Two, kinachoitwa You’re Fired ambacho huongozwa na Milionea wa Kiingereza Sir Alan Sugar. Lengo la kipindi hiki huwa ni kutafuta mtu mmoja ambaye bila kuangalia kiwango cha elimu yake anaweza kuwa na mbinu za kijasiliamali na kimenejimenti kwa kuwaongoza wenzie katika kutafuta faidi iwe katika hoteli, kiwanda na mahali popote ambapo uzalishaji kwa lengo la kutafuta faidi unafanyika. Mshindi wa mchakato huo huajiriwa katika moja ya makampuni ya milionea huyo na kwa mwaka analipwa paundi za kiingereza laki moja (100,000). 

Ili kufanikisha mkakati wake huo Sir Alan Sugar, aliwagawa washiriki wake wapatao 20 katika makundi mawili ya kila upande watu kumi, akawagawia mtaji wa kuendesha biashara ya kufua nguo ambapo makundi yote mawili yalitakiwa kupita kwa wateja majumbani na kujitangaza na hatimaye wateja walikubali kuwapa nguo zao zikafuliwe na kunyooshwa kwa gharama walizokubaliana.

Hatimaye ikafika wakati wa kuangalia nani kapata nini na kapoteza nini, makundi yote mawili yalipata faidi lakini moja lilipata faidi ndogo na hapo Sir Alan akawa mbogo akitaka kujua nani kasababisha kutopatikana kwa faidi kubwa na kwa bahati mbaya nguo za mmoja wa wateja zilikwenda kwa mteja ambaye siye mwenye nazo!

Katika kutafuta uzembe ulikuwa wapi alijitokeza mshiriki mmoja katika kundi hilo akapaza sauti kuwa tatizo katika kundi lao kuna washiriki ambao siyo wasomi, ndipo Sir Alan akamwuliza kuwa ana elimu ya kiwango gani? mshiriki yule akajibu kuwa ana shahada ya uzamili katika uchumi. Swali la mwisho na ambalo lilimwondoa katika ushiriki ule lilikuwa ametumiaje elimu yake katika kuleta faida, mshiriki akawa kimya na Sir Alan hakuwa na la ziada ila kumfukuza huku akisema wale wafanyakazi wake ambao hawana shahada lakini wanamwingizia faida wana tatizo gani.

Mshiriki aliyekuja kushinda na hatimaye kuajiriwa kwa mshahara wa paundi 100,000 alikuwa ni yule aliyekaa chuo kikuu kwa miezi mitatu na kuacha kwa sababu alionyesha kuwa ana mbinu za kijasiliamali na kimenejimenti za kuweza kuzalisha faida katika kampuni.

Sasa nirejee kwenye usomi na shahada za bandia na za kweli, hapa najiuliza maswali mengi lakini kwa uchache ni inawezekana vipi kwa msomi ambaye ni profesa kuteuliwa kuwa waziri wa mawasiliano na uchukuzi na baada ya muda Fulani anapoondoka wizara ile mashirika karibu yote katika ile wizara yanakuwa taabani? Msomi mwingine ambaye ni profesa anaanzisha taasisi isiyokuwa ya kiserikali huku fedha zote za kuendeshea taasisi hiyo zikitoka nje kwa wahisani wake, anajenga jumba lake kubwa la kifahari, ananunua gari la kifahari pia na anasomesha watoto wake ughaibuni na katika kufanikisha mradi anaendesha utafiti ambao mara zote ni kuangalia kama mwanasiasa fulani anapendwa na watanzania au la? Fikra zangu duni ni kuwa baada ya kuwa mtu yeyote amesoma na kuwa na hadhi ya profesa na chuo kumkubali nadhani anatakiwa kuonyesha kwa vitendo thamani ya elimu aliyopata.

Kwahiyo unaweza kujiuliza kutokana na yale niliyoeleza hapo juu kuwa hii ndiyo gharama ya kodi za watanzania walizotumia kumlipia yeye wakati akisoma inasaidia nini kujua kuwa fulani anapendwa au hapendwi? Unakuwa na msomi mwingine ambaye ni daktari wa falsafa na waziri vilevile lakini hajui hata kutoka Mwenge jijini Dar es Salaam hadi jimboni kwake ni kilomita ngapi na huyu ndiye anayetakiwa kusimamia ujenzi wa barabara? Jambo linalonipa taabu ni kama kwa utashi wangu niwape heshima ya usomi waheshimiwa hawa? Upo mfano mmoja hivi inakuwaje kwa msomi kung’ang’ania kufanya kazi katika chuo kimoja tu wakati anaweza kusaidia mahala pengine hata kama siyo kwa kufundisha, kwanini msomi kama huyu asifanye kazi nyingine yoyote zaidi ya kufundisha na kufanya utafiti ambao matumizi yake ni yamkini?

Kwa bahati mbaya nimekuwa nikijikuta nawasilikiza au kuwatazama wasomi mbalimbali wakiongea katika runinga na redio na wengi ni wakosoaji wazuri, kuna wakati Mzee Ali Hassani Mwinyi alipokuwa rais wa Tanzania alikuwa na mshauri wa uchumi ambaye ni profesa na ni huyo huyo leo hii anasema kuwa serikali inategemea sana misaada katika bajeti yake na ijaribu kuja na mbinu za kujitegemea, lakini wote tunajua jinsi nchi hii ilivyopoteza viwanda na raslimali chungu mbovu wakati msomi huyu alipokuwa msahuri wa mzee ruksa.

Wakati Rais Jakaya Kikwete akitoa hutoba ya kulivunja Bunge, Mjini Dodoma kulikuwa na wasomi wawili ambao walialikwa na Runinga ya Taifa(TBC) ili watoe tathmini yao kutokana na hutoba ile na kwa kuwa ilikuwa na takwimu nyingi hapo ulikuwa ni uwanja wao. Kilichonishangaza ni moja wa wasomi wale alipokuwa akiunga mkono takwimu zile kwa kusema kuwa zinatokana na utafiti uliofanyika wakati hali halisi haiendani kabisa na yaliyokuwa yakitoka kwenye takwimu zile, hii ilinipa simanzi sana.

Kwa mfano, katika hotuba ile kulitajwa kuwa umasikini umeshuka kwa kiwango cha kuridhisha na kwa bahati mbaya wiki ile ile katika kituo kingine cha televisheni ilionyesha mama moja akiwa katika kijiji kimoja wilayani Kyela akiomba msaada wa kujengewa nyumba na wazungu waliokuwa katika ziara ya kujifunza maisha ya watu wa nchi hii. Mama yule ana watoto saba ambao bado hawajawa na uwezo wa kujitegemea, yeye mwenyewe ni mgonjwa, nyumba anayoishi ipo mbioni kudondoka, katika hali ile takwimu za Mheshimiwa zilizopata baraka za wasomi zilikuwa sahihi kweli?

Nirudi kwa kuuliza swali usomi wake umeisaidiaje nchi hii? Kuwa daktari wa falsafa, profesa kama hakuna ulichosaidia kupambana na matatizo ya watanzania na kwa bahati mbaya ukafanya mambo kama siyo msomi bado ni hasara kwa taifa.

Kwa wale tunaofuatilia mienendo ya hawa wote wawili naamini hatuna shaka kwa sababu zilizotolewa na vyuo hivyo kuamua kuwaenzi kwa kwatunuku shahada za falsafa za udaktari wa heshima kwani michango yao tumeiona na hata profesa Maghembe alikubaliana na vyuo hivyo kutoa shahada hizo.

Hivi Karume kuitwa daktari kwa kuwaondolea wazanzibari gonjwa linalotafuna maisha ya watu chungu mbovu katika nchi za kitropiki kuna ubaya? Wasomi wanaotambulika kwa kupitia vyuo vinavyotambulika mbona wameshindwa kuwaangamiza wale mbu pale Hospitali ya taifa Muhimbili? Mzindakaya kuanzia kwenye uanzishaji wa SIDO hadi kuwa na kiwanda chake mwenyewe hilo ni tatizo? Wasomi wangapi hatujui wameifanyia nini nchi hii?

Ninao mfano moja wa kijana aliyemaliza masomo yake kutoka chuo cha maji pale ubungo, jijini Dar Esa salaam, miaka ya mwanzo ya themanini aliporudi kijijini kwake mkoani Iringa alijaribu kufanya matembezi katika moja ya milima inayozunguka kijiji chake, kwa bahati nzuri alifanikiwa kuona chemchem ya maji katika moja ya milima ile, wazo likamjia akawasilisha serikalini na wanakijiji wakafanya harambee ya kuchimba mtaro wa kupitishia mabomba ya maji na yeye akatumia utaalamu wake kukinga maji yale ili yatiririke kuelekea vijiji vya karibu.

Kwa bahati nzuri serikali ilimsikia na kwa juhudi na maarifa aliyokuwa nayo mradi ule unatoa maji kwa vijiji zaidi ya 10 leo hii na hakuna hata siku moja maji yamekatika na wanachi wanaulinda mlima ule kama almasi yao.  Baada ya mradi ule kufanikiwa aliendelea kufanya kazi katika miradi ya maji sehemu mbalimbali nchini na kila alipokwenda na kuondoka wananchi walimlilia, je huyu akipewa shahada ya heshima ya udaktari wa falsafa kuna tatizo?

Kuna wakati niliwahi kuuliza swali kwa raia moja wa nchi za magharibi kuwa kwanini Waziri Mkuu wa Uingereza wakati huo Gordon Brown, aliyekuwa Waziri wa Mambo ya nje wa Marekani, Condereza Rice hawapendi kuitwa kwa majina ya kisomi ya Daktari na profesa wakati wanasitahili hivyo kwa elimu zao, alinijibu kuwa siyo vizuri kuitwa msomi na kesho yake ukafanya mambo kama siyo mtu aliyekwenda shule.

Lakini hoja ya Profesa Nkunya ni kama hapendezwi na tunu wanazopata watu mbalimbali kutoka katika vyuo visivyotambulika na kwa hili yuko sahihi, angependa shahada hizi zitolewe zaidi kwa wale wanaosomea kwa kukaa vyuoni na kusimamiwa na wahadhiri na kwa vile huwezi kupata shahada ya udaktari wa falsafa bila kufanya utafiti kwa vigezo vilivyowekwa na chuo ni dhahiri ni lazima uhenyeke au utaabike kabla hujavaa joho hilo.

Kwangu mimi ambaye siyo msomi sioni tofauti yoyote kati ya viwanda vya kutengeneza shahada kama profesa Nkunya alivyoviita na vyuo vinavyotambulika. Lazima tukubali kuwa Vyuo vyetu ni mahali pa kwenda kuchukua vyeti ili kupata ajira kwa sababu hilo ndilo sharti kubwa kuwa na elimu ya shahada ya kwanza, ya pili, tatu hadi mwisho na hii yote inategemea mshahara atakaolipwa mtarajiwa kwa elimu yake na majukumu atakayopangiwa na ofisi inayomwajiri.

Hapa ni kama mashindano ya Bongo Star Search kwani aliyeshinda mwaka jana amefanya kazi yoyote ya muziki? Si ni fedha tu ndizo zinazotafutwa kipaji ni jambo la wengine, unaweza kuiga mwanamuzi unayempenda na kumudu vizuri ili watu wakupigie kura upate mahela! Na kwa upande wa shahada ni hivyo hivyo kinatafutwa cheti kwa gharama yoyote iwe kwa kuiba mitihani, kuhonga mwalimu kwa fedha na ngono, kukodi mtu akufanyie mtihani, kunakili utafiti wa mtu mwingine na hata kukodi mtu wa kufanya utafiti wenyewe suala ni maisha nani anabisha?

Siyo siri kuwa kupata shahada hakuendani na hadhi au muktadha na mantiki ya shahada hiyo, tujiulize wakati tuna wanasheria wenye shahada lukuki inakuwaje mikataba ya madini inakuwa kama ya akina Mangungo wa Msovelo? Taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali kuwa chafu na wahasibu wasomi ndiyo hao? Waandishi wa habari wanaofanya uandishi wa habari kama maofisa uhusiano wa makampuni na shahada zao? Makocha wa mpira wasioleta kombe hata moja la kimataifa huku wakitaka waitwe super coach? Wahandisi wa barabara zinazoharibika siku ya kwanza ya ufunguzi na shahada zao? Wahandisi wa maji wanaotandaza mabomba ya maji wakati wakijua kuwa hakuna maji yatakayotoka na shahada zao? Fani zote zina matatizo na ni wasomi wa vyuo vyetu tunavyovipenda sana na kuviita vinatambulika. Kutambulika kwa chuo bila ufanisi ni sifuri tu. Kama wasomi wetu wangekuwa wanaonyesha mifano kwa wasiosoma ingekuwa ni halali kuwanyooshea kidole wanaofanya ujanja wa kielimu. Msomi hawezi kutuonyesha jinsi alivyoweza kutumia elimu yake kuwa na shamba lenye mazao na mifugo iliyonona kila siku anafanya utafiti ili kiwe nini?

Kwa hapa nirudi miaka ya nyuma kwa upande wa Mahakama, kulikuwa na Mawakili ambao watu wengi walipenda kwenda kuwaona wakitoa hoja zao mahakamani kwa mfano, akina Murtaza Lakha, Ismail Mukhadam, Francis Uzanda na baadaye wakaja akina Abasi Mselem, Dr. Masumbuko Lamwai na Michael Wambali.

Wakati huo mashahidi walikuwa na wakati mgumu sana kwa waheshimiwa hawa kwa hoja na maswali waliyokuwa wakiwatupia wakati wakitoa ushahidi wao mahakamani nilitegemea leo tungekuwa na wanasheria wakali zaidi ya hawa lakini hilo halipo na bado tuendelea kuzalisha kundi la werevu ambao ni members of the learned brothers kila mwaka katika vyuo mbalimbali hapa ndani na nje ya nchi kwani sivinatambulika kwenye mafaili yetu!

Kwa waandishi wa habari ambao kwa kweli kwa wakati huo kulikuwa hakuna hata chuo kimoja ambacho kilikuwa kikitoa shahada za uandishi wa habari watawakumbuka akina Stanley Katabalo na John Rutayisingwa, hawa wote ni marehemu kwa sasa kwa jinsi walivyoweza kuandika habari za uchunguzi wa kikachero na kuwafanya wasomaji wa magazeti kufuatilia habari zao kila magazeti yalipokuwa yakitoka, naye Mnenge Suluja alivyokuwa akiandika habari za mahakamani na kumfanya msomaji ahisi kama alikuwepo mahakamani siku ya shauri. Leo tunao wenye shahada si ndiyo! Habari gani ambayo wameandika ikionyesha kuwa inaendana na usomi wao?

Nimeanzisha mjadala huu ili wachangiaji wengine wanisaidie kupata picha halisi ya viwanda vya kutengeneza shahada na vyuo vinavyotambulika kwani mimi siyo msomi na sina nia mbaya ya kuleta utetezi wa shahada za heshima tatizo langu ni ujinga na uelewa mdogo nilio nao, bado sielewi tofauti iko wapi na nini mchango wa wale tunaowaita wasomi waliobobea katika maendeleo ya nchi hii?


Waweza kunisaidia kwa hili kwa kuniandikia barua pepe kwa anwani hii [email protected]

ASANTE SANA MDAU IDD KWA MAKALA HII MWANANA.WADAU WENGINE PIA MNAKARIBISHWA KUTUMA MAKALA ZENU AU CHOCHOTE KILE CHA MANUFAA KWA JAMII.


19 Apr 2010

Kuna busara moja inayotuasa kuwa mpuuzi husema kwa vile anajiskia kusema (hata kama ni upuuzi) ilhali mwenye busara husema tu pale anapokuwa na kitu cha kusema (ikimaanisha kama hana cha kusema,au haoni umuhimu wa kusema kitu,atakaa kimya. Busara zaidi zinatuasa kuwa makini na tunayosema hadharani kwa vile mara nyingi jamii humtambua zaidi mtu kwa kauli zake.Sema upuuzi,utaonekana mpuuzi.Sema ya busara,utaonekana mwenye busara.Sasa kuna huyu msomi,Dokta Benson Bana,ambaye licha ya kuwa mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam,ni mkuu wa idara ya Sayansi za Siasa na Uongozi na pia ni Mwenyekiti Mwenza wa REDET.Yayumkinika kusema Dkt Bana amekuwa mahiri zaidi wa kutoa kauli zisizoendana na wasifu wake kitaaluma kuliko umahiri wa wa usomi wake

Na leo,kwa mujibu wa habari katika gazeti la Mwananchi,msomi huyo 'amelipuka' tena kwa kauli kwamba tuhuma zilizokithiri dhidi ya ufisadi zinaweza kusababisha taifa kukosa viongozi wazuri wakati wa uchaguzi mkuu wa Oktoba.Huhitaji kuwa na hata asilimia moja ya kiwango cha elimu ya Dkt Bana kutambua kuwa tuhuma zilizotapakaa kuhusu ufisadi ni matokeo ya kuwepo kwa ufisadi.Msomi huyu anaishi Tanzania lakini yaelekea hafahamu mazingira yanayomzunguka,na hilo linaleta wasiwasi mkubwa kuhusu mchango wa wanataaluma katika maendeleo ya nchi yetu.

Katika habari hiyo Dk Bana aliwataka watu "waaache siasa chafu za kuhubiri na kudai kuwa watuhumiwa wa ufisadi hawafai kupewa kura au kuchaguliwa katika nafasi mbalimbali za uongozi kana kwamba wameshathibitika".Huu ni zaidi ya ubabaishaji wa kitaaluma,na kwa kiasi flani inaaibisha Udaktari wa Filosofia tunaohenyea akina sie.Kwanza,Dkt Bana amepata wapi mamlaka ya kuwataka wananchi waache kulalamikia ufisadi?Usomi hautoi mamlaka ya kuizuia jamii kulalamikia maovu yanayoisumbua.Pili,kwa mtizamo wa msomi huyu,kwa vile tuhuma za ufisadi hazijathibitika basi watu wakae kimya hadi 'miujiza itapotokea kwa watawala wetu kuamua kuchukua hatua za kisheria dhidi ya mafisadi'!Hii ni sawa na kuingiliwa ndani na kibaka halafu ukakaa kimya kwa vile tu wewe sio chombo cha sheria.Ukifanya hivyo,hata hao polisi watakuona mpumbavu na unawapotezea muda.La kufanya ni kumdhibiti kibaka au kupiga kelele kuwashtua majirani wakusaidie kumdhibiti.

Binafsi,pamoja na kuheshimu uhuru wa kutoa mawazo,nadhani tatizo kubwa la Dkt Bana ni tabia yake ya 'kusema chochote' hata kama hana cha kusema.Inaelekea aidha hafahamu athari za tabia hiyo au anapuuza tu.Matokeo yake ni kuonekana mbabaishaji wa namna flani.Si lazima jina lake lionekane magazetini au kusikika radioni kama hana la muhimu kuieleza jamii.Eti anatuasa kuwa "si vizuri kwa watu kunyimwa kura kwa sababu ya kutuhumiwa kwa ufisadi hadi hapo watakapothibitika na kutaka wanasiasa waache kuhukumu wenzao bila kosa".Kwanini hajiulizi inakuwaje watu hao wanatuhumiwa ufisadi in the first place?Kwanini ni wao na si Dokta Bana,kwa mfano?

Hivi lipi lililo muhimu zaidi kwa Tanzania kama taifa: kukosa viongozi bora kwa vile wanatuhumiwa kwa ufisadi au kupata viongozi bora watakaowajibika kulitumikia taifa kupambana na ufisadi?Wasiwasi wa Dkt Bana ulipaswa kuwa kwenye athari za ufisadi kwa jamii na sio tuhuma za wananchi dhidi ya mafisadi.Ni mlevi tu atakayeshindwa kuelewa kuwa kinachoumiza Watanzania kwa sasa ni UFISADI na sio TUHUMA DHIDI YA MAFISADI.

Mwanataaluma huyu anaongoza taasisi ya REDET ambayo mara imekuwa ikishutumiwa kwa upendeleo inapotoa taarifa za kura zake za maoni (opinion polls) kuhusu CCM na vyama vingine vya siasa.Sina hakika kuwa matokeo ya kura hizo huwa 'yanapikwa' ili kuridhisha watawala lakini kinachozua maswali dhidi ya polls hizo ni kutoendana na hali halisi na dalili za upendeleo.

Wito wangu kwa Dkt Bana ni huu: wakati mwingine jaribu kuitendea haki taaluma yako kwa kukaa kimya pale usipokuwa na cha kuongea.Kwa kufanya hivyo,utawatendea haki pia wasomi wenzako,taasisi unazoongoza na fani nzima ya usomi.Ni muhimu pia unapotoa matamshi mazito ukajitahidi kutumia theories za kusapoti matamshi hayo badala ya kutoa hisia zenye mwelekeo wa kijiweni.


.

22 Jan 2009

Askari wa kikosi cha kutuliza ghasia wakifanya patrol hapo Mlimani (UDSM).Picha kwa hisani ya MICHUZI JR.

Nilimaliza ngwe yangu hapo Mlimani (UDSM) takriban miaka kumi iliyopita.Kuna yaliyobadilika kwa kipindi cha miaka mitatu niliyokuwa hapo,na kuna mengine yamebaki kama yalivyo.Kwa kifupi sana,katika miaka hiyo mitatu,sikumbuki kama kuna academic year iliyopita pasipo mbinde ya aina moja au nyingine kati ya wanafunzi na serikali.Na kila mara chanzo kilikuwa kilekile:FEDHA.

Binafsi nadhani chanzo cha matatizo ya migogoro kati ya wanavyuo na serikali ni mapungufu katika sera nzima ya uchangiaji gaharama za elimu ya juu.Kwa nchi masikini kama yetu,haihitaji busara kufahamu kwamba kuna wanafunzi lukuki wanaotoka katika familia ambazo kumudu gharama za maisha ya kila siku ni mgogoro,achilia uwezo wa kumudu gharama za kumsomesha mtoto chuo kikuu.Kwa mantiki hiyo,ajenda ya kulipa ada na gharama nyingine kwa silimia 100 ni suala lisilowezekana kwa wanafunzi wanaotoka familia za aina hii,ambao kwa hakika ni wengi zaidi.

Kinachohitajika ni usimamizi mzuri wa mikopo kwa wanafunzi wa aina hiyo.Hii ni investment nzuri kwa future ya taifa letu.Iwapo serikali itakuwa na nia ya dhati kuhakikisha kuwa wakopeshwaji wanarejesha fedha hizo,ni dhahiri itajitahidi kuwatengenezea mazingira mazuri ya ajira pindi watapohitimu masomo yao...kwa vile ajira hiyo ndio inayotarajiwa kuwawezesha kulipa mikopo hiyo ya serikali.

Kama tunaweza kuwakopesha wabunge mashangingi yenye thamani ya mamilioni ya shilingi,naamini kabisa kuwa kuwakopesha wanavyuo wetu ni swala linalowezekana pasipo kusababisha hizi mbinde za kila mwaka au muhula wa masomo.Tatizo sio sera ya uchangiaji gharama per se bali,kama ilivyo kwenye maeneo mengine mengi,ni utekelezaji wa sera hiyo.FFU wanaweza kutuliza ghasia chuoni hapo kwa muda lakini hawawezi kuwa ufumbuzi wa tatizo hilo.

19 Nov 2008


UONGOZI wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) umekifunga chuo hicho kwa muda usiojulikana kutokana na mgomo wa wanafunzi.

Uongozi wa chuo hicho umefikia uamuzi huo, baada ya wanafunzi katika chuo hicho kufanya mgomo kuishinikiza serikali kuwarudisha vyuoni wanafunzi waliofungiwa.

Kabla ya kufungwa kwa chuo hicho jana, bodi ya chuo hicho ilifanya kikao, ili kujua wachukue uamuzi gani.

Awali, akizungumza na Tanzania Daima jana chuoni hapo, Rais wa DIT, Cleophace Maharangata, alisema mgomo wao bado unaendelea lakini bodi ya chuo inafanya kikao kuamua kama chuo kifungwe ama la.

“Sisi tunasubiri tamko baada ya kikao…uamuzi wowote utakaotolewa sisi tupo tayari,” alisema.

Naye mwalimu wa chuo hicho ambaye hakutaka kutajwa jina lake gazetini alisema mgomo huo upo kwa wanafunzi wa shahada ya kwanza, huku wanafunzi wa astashahada (diploma) wakiendelea na masomo kama kawaida.

Awali Rais wa wanafunzi hao, alisema mgomo huo ulianza rasmi juzi baada ya wanafunzi kutoingia madarasani huku wakiwa wameshika mabango yaliyobeba ujumbe mbalimbali.

Kufungwa kwa chuo hicho kunafanya idadi ya vyuo vilivyofungwa kufikia saba. Vyuo vingine ambavyo vimeshafungwa ni Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Chuo Kikuu cha Ardhi (ARU), Chuo Kikuu cha Elimu Mkwawa (MUCE), Chuo Kikuu cha Elimu Dar es Salaam (DUCE), Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) na Moshi Ushirika.


18 Nov 2008

Chuo Kikuu cha Ushirika na Biashara mkoani Kilimanjaro (MUCCoBS) kimewatimua wanafunzi 595 wa mwaka wa kwanza kutokana na kuanzisha mgomo chuoni hapo. 

Aidha wanafunzi hao pamoja na mgomo huo,wametuhumiwa pia kuhatarisha maisha ya baadhi ya wanafunzi wenzao wa mwaka wa pili na wa tatu sambamba na wahadhiri chuoni hapo baada ya kuwamwagia mchanga na kuwarushia mawe wakiwa darasani. 

Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Suleiman Chambo alisema jana kuwa kutokana na mgomo huo, menejimenti iliamua kuwasimamisha masomo wanafunzi hao kwa muda usiojulikana na umewataka wawe wameondoka chuoni hapo hadi kufikia jana saa 10 jioni. 

"Wanafunzi wa mwaka wa kwanza walipoona wenzao wa mwaka wa pili na tatu hawawaungi mkono waliamua kuwafuata madarasani na kuwamwagia mchanga na kuwarushia mawe huku mhadhiri mmoja akiwa darasani, Profesa Temba, ambaye alinusurika kipigo na ilimbidi kuingia chini ya meza ili kujinusuru," alisema. 

Aliongeza kudai kuwa wanafunzi hao hawana madai ya msingi na kwamba moja ya madai yao ni kuishinikiza Serikali kuwalipia mikopo kwa asilimia 100 huku madai mengine ni kuwaunga mkono wanafunzi wenzao katika vyuo vikuu vilivyofungwa. 

"Tumeamua kuwarudisha nyumbani kwa muda usiojulikana, na wakirudi waandike barua wathibitishe kulipa ada kwa asilimia 100, waombe kurudi chuoni na kufuata taratibu za chuo na walete vyeti vya kuonesha kwamba wana sifa za kurudia shahada wanayosomea," alisema. 

Alidai kuwa wanafunzi hao pia walitishia maisha ya Rais wa Serikali ya wanafunzi chuoni hapo, Zamu Mlimila ambaye alilazimika kuokolewa na polisi baada ya wanafunzi kumzonga kwa lengo la kumshinikiza atangaze mgomo chuoni hapo.

CHANZO: Majira

15 Nov 2008

Na Francis Godwin, Iringa 

SIKU moja baada ya askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) mkoa wa Iringa kulazimika kutumia mabomu ya machozi kutuliza vurugu za wanafunzi wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Mkwawa (MUCE), uongozi wa chuo hicho umetangaza kukifunga kwa muda usiojulikana. 

Uamuzi huo umeifanya idadi ya vyuo vishiriki vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam vilivyofungwa hadi sasa kufikia vitatu. Awali Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kampasi kuu na juzi Chuo Kishiriki cha Elimu Chang'ombe vilifungwa kutokana na wanafunzi kugoma na kuandamana ndani ya vyuo hivyo wakipinga sera ya kuchangia elimu ya juu. 

Juzi majira ya saa 9 alasiri wanafunzi hao walianza kuwashinikiza wenzao kuanza mgomo usio na kikomo kwa lengo la kutaka kutimiziwa mikopo yote na serikali kwa asilimia 100. 

Kutokana na taarifa ya mgomo huo kuwa ya ghafla kwa wanafunzi hao baadhi yao waliamua kuendelea kujisomea katika vyumba vya madarasa hali iliyopelekea kundi hilo la wanafunzi wanaotaka wenzao wagome kuanza kuwashambulia kwa virungu na fimbo huku wakidai kuwa ni wasaliti wa mgomo huo. 

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mmoja kati ya viongozi wa serikali ya wanafunzi chuoni hapo ambaye hakupenda kutaja jina lake kwa kuwa si msemaji wa juu wa serikali ya wanafunzi chuoni hapo alisema kuwa katika vurugu hizo za wanafunzi zaidi ya wanafunzi watatu wamejeruhiwa vibaya na kulazwa katika zahanati ya chuo kwa matibabu zaidi. 

Wanafunzi waliojeruhiwa ni Bw. Leslea Mkuchika, Bi Naima Kalaghe na Bi. Gloria Nyagawa ambapo Mganga Mfawidhi wa zahanati hiyo ya chuo, Bi. Iluminata Mbilinyi alisema kuwa wanafunzi hao wametibiwa na kuondoka katika eneo la chuo hicho kuelekea majumbani kwao. 

Barua ya kukifunga chuo hicho iliyosainiwa na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam, Prof. Rwekaza Mukandala na kubandikwa katika mbao za matangazo za chuo hicho iliwataka wanafunzi hao kuondoka mara moja chuoni hapo kwani wamekaidi amri ya Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Prof. Jumanne Maghembe ya kuwataka kusitisha mgomo huo. 

Mwandishi wa habari hizi alishuhudia kundi la wanafunzi takribani 2000 waliokuwepo katika chuo hicho wakiondoka chuoni hapo kwa makundi. 

Pamoja na wanafunzi hao kukubali kuondoka chuoni hapo bado baadhi yao waliapa kuendelea na mgomo mpaka kieleweke iwapo Serikali haitakubali maombi yao ya kutaka kuondolewa kwa sera ya uchangiaji elimu. 

Naye Mwandishi Wetu Peter Masangwa anaripoti kutoka Dar es Salaam kuwa Jumuiya ya Wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam (UDASA) imeunda kamati ya watu watano kuchunguza kiini cha tatizo linalopelekea migomo ya wanafunzi wa vyuo vikuu nchini mara kwa mara. 

Akizungumza na gazeti hili jana ofisini kwake Katibu wa UDASA Dkt. Deoscorous Ndoloi alisema tangu Bodi ya Mikopo ianzishwe imekuwa na migogoro na wanafunzi na kusababisha migomo isiyo ya lazima. 

Alionesha wasiwasi wake kuhusu uhalali wa sifa za kutolewa mikopo hiyo akisema wapo baadhi ya wanafunzi wamekasirika kuona mtu ambaye wanajua ana uwezo ndiye amefadhiliwa kwa asilimia 100 huku wale wasio na uwezo wakipewa asilimia 80 au 60 tu ya mkopo na kulazimika kutafuta vyanzo vingine kuweza kuendelea na masomo. 

Naye Mwandishi Wetu, Eckland Mwaffisi anaripoti kuwa siku moja baada ya kufungwa kwa muda usiojulikana, viongozi wa Serikali ya Wanafunzi kwenye Chuo Cha Ualimu Chang'ombe wameapa kuendeleza mgomo huo hata watakaporejeshwa iwapo madai yao hayatasikilizwa. 

Rais wa wanafunzi chuoni hapo, Bw. Ambege Uswege, alisema Dar es Salaam jana alisema, uamuzi wa kuwasimamisha masomo kwa muda usiojulikana, sio kigezo cha kumaliza tatizo na kwamba ufumbuzi wa tatizo hilo ni kutekeleza madai ya wanafunzi hao. 

"Pamoja na kukubali kuondoka katika mazingira ya chuo, tunasubili tamko la Serikali na kama watatoa tamko tofauti na lile tunalolitazamia, nitalazimika kukaa na Serikali yangu ili tuweze kutoa tamko la pamoja," alisema BW. Uswege. 

Alisema katika jitihada za kumaliza mgogoro huo, ni wajibu wa Serikali kuangalia uwezekano wa kupunguza kero za wanafunzi hao ikiwa ni pamoja na kuwapa ahadi za kutekeleza madai yao. 

"Serikali ya wanafunzi DUCE, ipo tayari kukaa meza moja na Serikali ili kuangalia uwezekano wa kumaliza mgogoro huu ambao unaangaliwa kwa mtazamo tofauti na wananchi mbalimbali," alisema.

CHANZO:Majira

TAFAKURI: MIGOGORO MINGI INAEPUKIKA IWAPO PANDE MOJA AU ZOTE ZITAJIBIDIISHA KUTAFUTA KINGA BADALA YA TIBA.WANAVYUO HUFIKIA HATUA YA KUGOMA KAMA SILAHA YAO PEKEE YA MWISHO.KWA AKINA SIE TULIO WANAFUNZI TUNAFAHAMU KUWA MWATHIRIKA MKUU WA MGOMO WA MASOMO NI MWANAFUNZI MWENYEWE,NA NDIO MAANA UAMUZI HUO HUWA MGUMU SANA.LAKINI WAFANYEJE?WAZAZI HAWANA UWEZO WA KUMUDU GHARAMA KUBWA ZA ELIMU YA JUU,NA IWAPO TUNATHAMINI ELIMU KWA DHATI BASI KUNA UMUHIMU WA KUPUNGUZA MASHANGINGI,SAMANI ZA OFISINI KUTOKA NJE NA ANASA NYINGINE KATIKA MATUMIZI ILI TUWEKEZE KATIKA SEKTA MUHIMU KAMA HII YA ELIMU.KUFUNGA CHUO NI KUAHIRISHA TU UTATUZI WA TATIZO.

12 Nov 2008


Serikali imewataka wanafunzi wote wa vyuo vya elimu ya juu nchini kuingia madarasani mara moja ifikapo saa moja asubuhi leo. Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari jana ofisini kwake, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Jumanne Maghembe alisema sera ya uchangiaji huduma za jamii ikiwamo elimu, halikwepeki katika mazingira haya ya kiuchumi. 

“Sera yoyote ile haiwezi kubadilishwa mara moja bila ya majadiliano ya kina yanahusisha wadau wote,” alisisitiza Profesa Maghembe, katika kujibu madai ya wanafunzi hao wanaopinga sera ya uchangiaji elimu ya juu hasa suala la mikopo wakitaka kulipwa asilimia 100. 

Waziri huyo wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi alisema matatizo yote ya kiutendaji katika utekelezaji wa sera ya elimu yatatafutiwa ufumbuzi. “Itaundwa kamati itakayowashirikisha wadau wote mkiwamo wanafunzi,” alisema Profesa Maghembe, ingawa hakufafanua hatua zitakazochukuliwa endapo wanafunzi watakataa kutii agizo hilo la kurejea madarasani leo. 

Akiahirisha Bunge mjini Dodoma Ijumaa iliyopita, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alisema hivi sasa serikali inabeba gharama za kuchangia elimu ya juu, na haitawezekana kutoa mikopo kwa asilimia 100. “Kwa hali ya kawaida, hii mikopo ilitakiwa ilipiwe riba kwa wanafunzi, lakini kwa sasa serikali inabeba mzigo huo. 

Hatuna uchaguzi mwingine, bali kuendelea kuchangia gharama za elimu ili wanafunzi wengi zaidi wapate elimu ya juu,” alisema Pinda bungeni na kuongeza: “Napenda nirudie kusema kwamba serikali wakati wote itakuwa mstari wa mbele kuhakikisha wanafunzi wanapata kile wanachostahili kujiendeleza kielimu. 

Naomba nitamke kuwa wanafunzi wale wanaotaka wanafunzi wote kupewa mikopo asilimia 100 haiwezekani.” Awali, jana wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam sehemu ya Mlimani wameendelea kusisitiza kuendelea na mgomo leo baada ya Mkurugenzi wa Elimu ya Juu kutotokea chuoni hapo. 

Akihutubia wanafunzi waliokusanyika kwa shauku katika Ukumbi wa Nkrumah kusubiri tamko la serikali, Rais wa Serikali ya Wanafunzi (DARUSO), Anthony Machibya alidai amepata taarifa kuwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Mkurugenzi wa Elimu ya Juu, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu pamoja na wasaidizi wake waliitwa Ikulu na Rais kwenda kujadili matatizo yao. 

“Profesa Mukandala ameondoka kimya kimya na wasaidizi wake wameenda Ikulu kujadili mgomo wetu, nimepigiwa simu na Karani wake, kwa hiyo tusikate tamaa tuendelee na msimamo wetu mpaka tuone hatima yetu,” alisema Machibya na kuongeza kuwa mgomo utaendelea kama kawaida hawatarudi nyuma. Aidha, magari matatu yakiwa na askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), yalikuwa yakirandaranda katika maeneo ya chuo hicho tangu juzi na jana kuhakikisha usalama wa mali na watu unakuwapo.

CHANZO: Habari Leo

29 Oct 2008

Wanafunzi wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) Dar es Salaam, wameamua kufunga mageti ya chuo hicho kuzuia uongozi wa chuo kuingia na kutoka baada ya Menejimenti kutotimiza ahadi ya kuongea nao, kutokana na mgogoro wa kufeli kwa wanafunzi wengi katika mitihani yao. 

Akipitisha azimio la kufunga mageti hayo, Rais wa Serikali ya Wanafunzi, Ali Mayay, aliwatangazia wanafunzi kuwa magari ya walimu yaliyoko ndani hayatatoka na yaliyoko nje hayataruhusiwa kuingia hadi uongozi wa chuo uzungumze na wanafunzi. 

Makamu Mkuu wa Chuo aliyetajwa kwa jina la A. Ahamed, ndiye aliyeahidi kukutana na wanafunzi hao saa nane mchana, lakini hakutokea hali iliyowakasirisha wanafunzi hao na kuanza kufanya fujo. Awali, wanafunzi hao ambao wamegoma kuingia madarasani, walidai kuwa kiini cha wanafunzi wengi kufelishwa ni mgogoro uliopo baina ya Mkuu wa Chuo na walimu wa CBE. 

Matokeo ya wanafunzi ambayo yametoka hivi karibuni yanaonyesha kuwa matokeo ni mabaya, hali iliyowashtua wanafunzi wanaotaka kupata maelezo kutoka kwa uongozi wa chuo hicho sababu ya wanafunzi kufeli kiasi hicho. Matokeo hayo ya mitihani yamekuwa mabaya kwa wanafunzi wa jioni waliofanya mitihani ya semista ya tatu pamoja na matokeo ya wanafunzi wanaosoma asubuhi ambao walifanya mitihani ya marudio. 

“Sisi tunaamini kuwa mgogoro uliopo baina ya Mkuu wa Chuo na walimu ndio chanzo cha wanafunzi kufelishwa kiasi hiki na sisi tangu Ijumaa tumeamua kutoingia madarasani hadi tupate maelezo kutoka kwa uongozi wa chuo,” alisema Makamu Rais wa Serikali ya Wanafunzi (Cobeso), Godrey Misso. Alisema hawaingii madarasani hadi watakapopata maelekezo kutoka kwa uongozi wa chuo. 

“Waliahidi kuongea na sisi jana (Jumatatu), lakini ikashindikana, wameahidi leo (jana) tunawasubiri,” alisema. Alisema haijawahi kutokea katika historia ya chuo hicho wanafunzi kufeli kiasi hicho. “Haiwezekani katika darasa la watu 400 wafaulu watu sita, ina maana wanafunzi wengine hawana akili?…hiki ndicho tunachopinga,” alisema. Baadhi ya walimu waliozungumza na gazeti hili, walikiri kuwa Mkuu wa Chuo hicho, Dk. Wilclif Lugoe tangu ajiunge na chuo hicho miezi 10 iliyopita, amefanya marekebisho ya mfumo wa uendeshaji ambayo yanawaathiri walimu kimapato.

CHANZO: HabariLeo

18 Oct 2008

Wanafunzi 5,300 na wahadhiri wao zaidi ya 100 wa Chuo Kikuu cha Dodoma, wameanza mgomo usio na ukomo wakishinikiza uongozi wa chuo hicho kuwalipa stahili zao mbalimbali.Wanafunzi hao walikuwa wamebeba mabango mbalimbali yenye ujumbe wa kumtaka Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Shabani Mlacha, kujiuzulu kwa madai kuwa ndiye kikwazo. 

Pia walikuwa wakiimba nyimbo za kuhamasisha mshikamano huku wakimtaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kwenda chuoni hapo kuwasikiliza. 

Askari Polisi wakiwa kwenye magari walikuwa pembeni ya wanafunzi hao wakiwa tayari kupambana na wanafunzi hao kama wangefanya fujo hivyo kusababisha uvunjifu wa amani chuoni hapo. 

Hata hivyo, polisi hao walijikuta hawana kazi ya kufanya kwani hakukuwa na hali yoyote ya uvunjifu wa amani na wanafunzi hao walionekana kuwa watulivu wakati wote wa kuimba nyimbo zao. 

Katika mgomo huo ulioanza jana, wanafunzi hao wanalalamikia uhaba wa malazi kwa madai kuwa wanachangia Sh. 500 kila siku, lakini baadhi yao wanalala kwenye nyumba za kulala wageni na wengine wakilazimika kulala kwenye chumba kimoja watu wanne. 

Akizungumzia mgomo huo, Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo hicho, Malimi Joramu, alisema sababu nyingine ni uongozi wa chuo hicho kuwatoza wanafunzi Sh. 100,000 kama gharama za matibabu kwa miaka mitatu. 

Alisema malalamiko yao yapo upande wa wanafunzi ambao ni watumishi wa umma ambao hulazimika kuchangia gharama hizo kupitia Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, lakini uongozi wa chuo umewataka wote kulipia gharama hizo bila kujali ni mtumishi wa umma au la. 

``Tulishakubaliana na Uongozi wa Chuo mwaka jana kuwa wanafunzi hao wasichangie gharama hizo na wale waliokwisha changia warudishiwe gharama zao, lakini tumeshangaa kwa wanafunzi wa mwaka huu, gharama hizo zimerudishwa tena na wale waliorudishiwa fedha zao, wametakiwa kurudisha gharama hizo,`` alisema Rais huyo. 

Madai mengine alisema ni pamoja na Uongozi wa Chuo kuweka muda mfupi wa usajili wa wanafunzi, ambapo chuo hicho kimetangaza kwamba jana ndiyo mwisho na wale ambao watakuwa hawajajisajiliwa, Chuo hicho hakitawatambua. 

Rais huyo anadai kuwa, muda huo ni mfupi mno ukilinganisha kuwa wanafunzi wengi wanaosoma chuoni hapo wanatoka katika familia maskini na hata walipouomba uongozi wa chuo kuwaongezea muda, ulikataa kufanya hivyo na kushikilia msimamo wake wa kuwafukuza. 

``Tunajiuliza hivi iweje mafisadi wa EPA ambao ni wezi wameongezewa muda wa kulipa fedha walizoiba, sisi ambao ni wanafunzi na tunatoka kwenye familia maskini tunakataliwa kuongezewa muda hata wa mwezi mmoja tu, hii sio haki kabisa,`` alilalamika Joramu. 

Kwa upande wa wahadhiri wa chuo hicho, wao wanadai kutolipwa posho ya kujikimu ya wiki moja ya kuripoti chuoni hapo pamoja na fedha za uhamisho kwa baadhi ya wahadhiri. 

Wengine wamedai hawajalipwa mishahara yao ya mwezi uliopita hali inayowafanya waishi maisha ya kuombaomba, hasa kutokana makali ya maisha kupanda. 

Wahadhiri hao wanaokadiriwa kupita 100, wamegoma kuingia madarasani wakishinikiza kulipwa posho hizo, pamoja na mishahara yao na ikiwa ni vinginevyo, mgomo huo hautakuwa na ukomo. 

Akijibu tuhuma za wanafunzi, Profesa Mlacha alisema gharama za malazi wanazolipia wanafunzi hao, zimepunguzwa kutoka shilingi 700 kwa siku mwaka jana, hadi kufikia Sh. 500 mwaka huu. 

Alisema sababu za kupunguza gharama hizo ni malalamiko ya wanafunzi hao wakidai kuwa ni kubwa na wazazi wao wanashindwa kumudu kulipa. 

``Kutoka na hali halisi ya maisha, tuliwaelewa na tukaamua kushusha hadi kufikia Sh. 500, lakini pamoja na kushusha huko, bado baadhi yao wanaendelea kulalamika kuwa gharama hizo ni kubwa,`` alisema. 

Hata hivyo, Profesa Mlacha alisema chuo hicho kina malazi ya kutosha na kila chumba wanalala wanafunzi wanne kutokana na ukubwa wa vyumba hivyo, kwa kuwa kila mwanafunzi ana kitanda chake. 

Alisema hivi sasa kuna vitanda na magodoro zaidi ya 1,000 ambayo hayajalaliwa na wanafunzi kutokana na wengi wao kuwa hawajaripoti chuoni hapo hadi sasa na kushangazwa na malalamiko ya wanafunzi ambayo aliyaita kuwa ni ya uzushi. 

Kwa upande wa malipo ya matibabu alisema, chuo hicho kilikutana na watendaji wa Mfuko wa Bima ya Afya na kuzungumza nao kuangalia utaratibu wa matibabu ambapo walibaini kuwa, kuna baadhi ya magonjwa ambayo mfuko huo hauyalipii. 

Kuhusu madai ya usajili alisema, hizo ni sheria za chuo kwamba mwanafunzi ambaye hajasajiliwa na chuo, hatambuliki kama ni mwanafunzi. 

``Tangu siku ya kwanza ya mwanafunzi kupata barua ya kuitwa chuoni, anaorodhoshwewa mahitaji yote anayotakiwa kuja nayo, sasa iweje mwanafunzi aje shuleni akiwa hana fedha hata nusu ya gharama hizo, chuo hakitakubali hata kidogo kumsajili mwanafunzi ambaye hajalipa hata nusu ya gharama zinazohitajika,`` alisisitiza. 

Akijibu malalamiko ya wahadhiri, Profesa Mlacha alisema sheria iliyokuwa ikitaka wahadhari hao kulipwa posho hiyo imefutwa, lakini hata hivyo, chuo hicho kimetumia busara ya kuwaombea fedha hizo serikalini na taratibu hizo zilikuwa zinaendelea. 

Hata hivyo, alisema pamoja na kwamba asilimia 80 ya walimu hao hawana sifa za kulipiwa gharama za malazi na chuo, chuo hicho kimejitahidi kuwapatia nyumba ambazo zina kila kitu na kwamba hakuna mhadhiri anayekaa kwenye nyumba za kulala wageni. 

``Wahadhiri hao nao wametufikisha mahali ambapo tunashangaa, mwaka jana tuliwalipa, lakini kutokana na sheria hiyo kufutwa bado tukatumia ubinadamu wa kuwaombea fedha hizo serikalini, lakini wakati suala hilo likishughulikiwa tunashangaa nao wanagoma, chuo hakielewi nia yao ni nini,`` alihoji Prof. Mlacha. 

Aidha, Profesa Mlacha alisema, uchunguzi wa chuo hicho umebaini kuwa, wapo wahadhiri wachache wanaojifanya wanazijua siasa au wanataka kutumia chuo hicho kujifunza siasa. 

``Tumebaini wahadhiri hao ndiyo walioshinikiza mgomo huu, inawezekana wanajifunza siasa ndani ya chuo hiki, lakini tunawaeleza kuwa, hiki sio chuo cha siasa na kama wanataka siasa waende kwenye vyama vya siasa kuonyesha uwezo wao wa kujua siasa,`` alisema Profesa Mlacha. 

Hadi mwandishi wa habari hizi anaondoka eneo la chuo hicho bado wanafunzi hao walikuwa wakiendelea na mgomo wao.

CHANZO: Nipashe

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.