Showing posts with label JUMA MWAPACHU. Show all posts
Showing posts with label JUMA MWAPACHU. Show all posts

17 Mar 2016


Nilianza kumsikia Balozi Mwapachu tangu nikiwa mtoto mdogo. Huyu ni miongoni mwa yale majina ambayo miaka nenda miaka rudi utayasikia, kama sio kwenye uwaziri basi ni kwenye ukurgenzi wa taasisi flani, au uongozi wa tume flani kama sio ubunge. Wenzetu hawa ni kama watu waliozaliwa ili kuwa viongozi. Lakini hio sio dhambi wala kosa, maana yawezekana kuzeekea kwao katika uongozi ni matokeo ya uongozi wao wa kupigiwa mstari.

Hold on, nimesema 'uongozi wa kupigiwa mstari'? May be, maana dunia hii tunayoishi sasa hata sifa za uognzi hazijulikani ni zipi. Na sababu ya wazi ya sifa za uongozi kupoteza maana yake ni ubabaishaji, usanii,ufisadi, ujambazi, na kila baya unaloweza kulihusisha na tasnia ya uongozi.

Sie wengine tulikulia zama za chama kimoja. Tulishuhudia uongozi uliotukuka wa Mwalimu Nyerere. Ndio, kulikuwa na kasoro zake, kama vile viongozi kuonekana kama miungu-watu, lakini hawakuonekana miungu-watu kwa sababu ya utajiri wao bali angalau waliutumikia umma kwa namna moja au nyingine.

Tuliwaona viognozi mashambani, tuliwaona wakishiriki katika shughuli za ujenzi wa taifa, matengenezo ya barabara, ushiriki katika ujenzi wa miradi ya maendeleo, na vitu kama hivyo. Kumbuka, enzi hizo tulikuwa nchi ya ujamaa na kujitegemea, na miongoni mwa features za kujitegemea ilikuwa kutumia raslimali zetu, sio siku hizi zama za kutembeza bakuli kwa wafadhili, kisha kinachopatikana 'kinapigwa panga,' watu wanaporomosha mahekalu, wanaongeza idadi za magari yao ya kifahari, na sensa ya nyumba ndogo zao inazidi kukua.

Kwanini nimeandika 'kwa hasira' hivi? Jana nimesikia kituko kilichonichefua. Mmoja wa Watanzania wenye majina makubwa katika medani za uongozi, Balozi Juma Mwapachu, jana alitangaza kurejea CCM baada ya kukihama chama hicho tawala wakati tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu.

Kama nilivyosema awali, nimekuwa nikimsikia Juma Mwapachu tangu nikiwa mdogo. Lakini, mwaka jana nilipata fursa ya kuwasiliana nae. Sio uso kwa uso bali kupitia kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter. Sijui tulikuwa tunajadili nini lakini moja ya ajenda iliyojitokeza ni sapoti yake kwa Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa, ambaye baadaye aliteuliwa kuwa mgombea Urais kwa tiketi ya UKAWA. 

Balizo Mwapachu alijitokeza kuwa miongoni mwa watetezi wakuu wa Lowassa, huku nyakati kadhaa akitukumbusha 'yeye ni nani.' Wapo walioungana nae mkono lakini baadhi yetu tulimpinga waziwazi na kueleza bayana kuwa ni 'wazee' kama yeye walioifikisha Tanzania yetu mahali hapa pasipoeleweka. Baadaye akapotea mtandaoni, pengine kwa sababu 'wazee' kama yeye hawajazowea sana 'mbinde' za social media.

Alipotangaza kuachana na CCM na kumfuata Lowassa, halikuwa jambo la kushangaza kwa sie tuliowahi kushuhudia akimtetea huko Twitter. Baada ya kuhama CCM akajitahidi kutumia uweledi wake kueleza, kwanza kwanini CCM ni 'kimeo,' na pia kwanini Lowassa ndio ufumbuzi wa matatizo yanayoikabili Tanzania. Baadhi ya aliyoyasema yalikuwa na ukweli, lakini baadhi yetu hatukumuelewa kwa sababu moja tu: "alikuwa wapi siku zote hizo?" Yaleyale ya akina Lowassa, Kingunge, Sumaye na wengineo waliogeuka wakosoaji wakubwa wa mfumo walioshiriki kuuasisi huko CCM, mfumo wa wateule wachache huku mamilioni ya walalahoi wakiishia kuahidiwa hili kama sio lile.

Sasa jana akaamua kubadili gea angani, akatangaza kurudi CCM. Good, kuhama sio dhambi. Tatizo la msingi ni baadhi ya sababu alizoeleza kuwa zilimpelekea kuhama CCM na sasa kuamua kurejea.

Anadai 'alilewa' na ahadi ya Lowassa kuwa angepewa Uwaziri wa Mambo ya Nje. Hivi inaingilia akilini kweli kwa mtu kama huyo ambaye alikuwa miongoni mwa 'vijana wa Nyerere' kuhama chama alichokiasisi baba wa taifa kwa sababu tu alitarajia kupewa uwaziri wa mambo ya nje? Pengine sio kosa kwa sababu ni watu wangapi wasiotaka madaraka?

Lakini ili umuelewe vema ni muhimu kurejea posts zake mbalimbali huko Facebook na kwingineko alivyokuwa akiwahadaa vijana kuhusu ajenda ya mabadiliko. Kwanini nasema alihadaa? Kwa sababu mwenyewe amekiri jana kuwa kilichomvutia kwa Lowassa ni ahadi ya uwaziri wa mambo ya nje. Kule anahubiri kuhusu mabadiliko, huku anawazia uwaziri wa mambo ya nje. Baada ya Lowassa kushindwa kupata urais, na ndoto ya Mwapachu kuwa waziri wa mambi ya nje kuota mbawa, kaamua kurejea CCM. 

Tabia kama hizi zinaweza kuigharimu CCM huko mbeleni. Watu walioikimbia wakati wa shida (kwa maana ya mapambano ya kumwingiza mgombea wake Ikulu) wanaruhusiwa kurejea kiulaini tu na kigeugeu chao kurushwa na vyombo vya habari kana kwamba ni matukio yenye umuhimu mkubwa kihistoria.

Laiti ningekuwa na mamlaka huko CCM, ningemweka benchi Mwapachu kwa sababu kama alivyoondoka akiwa hana umuhimu wowote kwa chama hicho, ndivyo alivyorudi akiwa na umuhimu mdogo zaidi ya ule ambao hakuwa nao wakati anahama.

Nimalizie makala hii ya dharura kwa kutamka bayana kuwa Tanzania yetu imefikishwa hapa na vipongozi kama hawa, walafi wa madaraka licha ya kuwepo madarakani miaka nenda miaka rudi, viongozi wasio na msimamo, wanaoweza kuhadaa umma kuhusu mabadiliko ilhali mabadiliko pekee wanayopigania ni ya maslahi yao binafsi.

Nigusie jambo moja dogo baada ya majuzi kutangazwa viongozi wapya na wa zamani kuongoza mikoa yetu kama ma-RC. Sina tatizo na wengi walioteuliwa lakini kilichonisikitisha ni kuona baadhi ya sura zilezile za miaka nenda miaka rudi zikirudishwa kwenye uongozi. Kama mtu alikataliwa na wapigakura jimboni kwake kwanini apelekwe kuongoza watu wa mkoa mwingine? 

Na lini vijana wapya watapewa fursa ya kuongoza Watanzania wenzao iwapo tunaendelea ku-recycle sura zilezile? Mimi ni sapota mkubwa wa Rais Magufuli, tangu wakati wa kampeni hadi sasa. Ninaridhishwa mno na uongozi wake. Hata hivyo, hiyo haimaanishi akikosea sintomkosoa. Na kama nina moja la kumkosoa ni kutujazia sura za watu waliokaa kwenye uongozi miaka nenda miaka rudi [na usidhani ninalaumu kuhusu hilo kwa vile nilikuwa/nina matarajio ya uongozi. Licha ya kuridhiska na kidogo ninachopata hapa, pia ninaamini kuwa ili kuitumikia Tanzania yetu sio lazima mtu awe kiongozi. Just be a good mwananchi]

Yayumkinika kuhisi kuwa watu wa aina hiyo hawana cha kupoteza wakiboronga na kutimuliwa, kwa sababu baadhi yao tayari wanakula pensheni za ubunge au ukurugenzi wa kitu gani sijui. Wakitimuliwa, watanufaika kwa nyongeza ya fedha tu.

Na sintoshangaa pengine Mwapachu karudi CCM kubahatisha kupewa 'pande' la ubalozi. Na huwezi kumlaumu sana kwa sababu medani ya uongozi wetu imekuwa ni suala la ku-recycle watu walewale, wengi wakiwa ndio walioifikisha Tanzania yetu hapa tusipostahili kuwa.





4 Jul 2010

Kwanza naomba samahani kwa kupotea kwa zaidi ya wiki sasa.Afya iliyumba kidogo.Napenda kutumia fursa hii kuwashukuru wote walionitumia meseji za kunitakia afya njema.Bwana Amesikiliza sala na dua zenu.

Jana,katika pitapita zangu mtandaoni nilikutana na habari kwamba Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki,Juma Mwapachu,amewashukia wasomi wa vyuo vikuu kwa kuwapotosha wananchi kuhusiana na serikali kujiunga na soko la pamoja la Jumuiya ya Afrika Mashariki lililofunguliwa majuzi.

Kwa mujibu wa habari hiyo,Balozi Mwapachu alitoa kauli hiyo kufuatia ya baadhi ya wasomi kudai kuwa soko hilo linaweza kuwaathiri watanzania katika ushindani wa ajira.Akizungumza jana kwenye ufunguzi wa maonyesho ya 34 ya biashara ya kimataifa yanayoendelea jijini Dar es Salaam, Balozi Mwapachu alisema wasomi hao ambao wamesomea uchumi, wameshindwa kusema ukweli kuhusiana na kujiunga na soko hilo, na kusababisha wananchi kuingia uoga.

Alisema wasomi walipaswa kuwa mstari wa mbele kuwaelimisha wananchi kuhusu jumuiya hiyo na faida zake badala ya kuwapotosha wananchi kuhusu suala hilo na kusababisha baadhi ya nchi wanachama wa jumuiya hiyo kuhofia.

Alisema kabla ya kufungua milango hiyo aliweza kuzunguka katika kila nchi kwa ajili ya kuzungumza na wadau mbalimbali kuhusu suala hilo, lakini wananchi wamekuwa waoga na kusababisha kutoa maoni mbalimbali ya kupotosha.

"Niwashaangaa sana wasomi tena wamesomea uchumi, lakini wamekuwa wa mbele kuwapotosha wananchi kuhusu soko la pamoja la jumuiya ya Afrika Mashariki, hii imesababisha wanachi washindwe kujiamini na kufikiri kuwa wanaweza kukosa ajira,"alisema Mwapachu.

Alisema watanzania wengi wanawaogopa wakenya kwa madai kuwa wanaweza kushindwa kuingia kwenye ushindani wa soko la ajira.

Nadhani kwa mtu mwenye uelewa mkubwa kama Balozi Mwapachu kutoa kauli hizo ni jambo la kusikitisha sana na ni uthibitisho mwingine wa namna maslahi binafsi na ya kisiasa yanavyowekwa mbele ya maslahi ya taifa,sambamba na kupuuza ushauri wa kitaalam.

Yayumkinika kuamini kuwa kwa wadhifa wake kama Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo,ni lazima Mwapachu aipigie debe ili iendelee kuwepo kwani kinyume chake ni kuwa hatakuwa na ajira.Hata hivyo,laiti Mwapachu angeangalia mantiki ya hoja za wasomi (ambazo kwa hakika ziko shared na hata "wasio wasomi") badala ya kuwashambulia kama kundi la kijamii (yaani kujadili hoja badala ya kumjadili mtoa hoja)angeweza kabisa kufahamu kwanini wanaonyesha wasiwasi wao.

Hivi kama kabla ya ujio wa soko la pamoja la Jumuiya hiyo tayari wageni (licha ya hao wanaotoka Kenya na nchi nyingine za Jumuiya) tayari soko la ajira na bidhaa limetawaliwa kwa kiasi kikubwa na wageni,kwanini basi tusihofu kuwa "kuhalalisha" huko kutapelekea hali kuwa mbaya zaidi kwa Watanzania?

Na wakati Mwapachu anatoa porojo zake kuhusu mafanikio ya soko la pamoja,mbona hatuambii yeye na viongozi wenzie wa Kitanzania wameshafanya jitihada zipi kuhamasisha Watanzania kumudu ushindani uliopo na ujao?Siafikiani na mawazo potofu ya Mwapachu kuwa tatizo la Watanzania ni uoga.Na hata kama tatizo lingekuwa ni uoga basi bado hoja ingekuwa iwapo uoga huo ni halali au potofu kwani uoga kama uoga sio dhambi au kosa kama unajengwa kutokana na mantiki.Tatizo la msingi linalowakabili Watanzania kukabiliana na changamoto za mfumuko wa nguvu za nje katika soko la ndani la ajira na bidhaa ni complex sana,na makala hii fupi haiwezi kujadili yote bali itaangalia kwa ufupi.

Kwa upande wa biashara,kuna tatizo sugu la urasimu ambalo kwa kiasi kikubwa linachangiwa na ufisadi.Urasimu kuanzia kwenye utaratibu wa kuandikisha biashara hadi kwenye masuala ya kodi.Sijawahi kufanya biashara lakini nina marafiki kadhaa wanaojaribu kumudu maisha yao kwa kujihusisha na biashara.Kwa kifupi,ajira ya Mtanzania kwa kutegemea biashara ni suala gumu sana.Katika mazingira ya kawaida sio rahisi kwa biashara kudumu kwa angalau miezi kadhaa kama mhusika hatokuwa tayari kutoa chochote kitu kwa wahusika.Yayumkinika kusema kuwa ili biashara halali ishamiri vema ni lazima ikaribishe illegality ya namna flani,yaani uharamu wa biashara ili kuwa halali.

Na wakati Watanzania wengi tu wangependa kujishughulisha na biashara zao kihalali ili wamudu maisha yao,wanakumbana na ushindani kutoka kwa wenzao "wanaobebwa" na vigogo.Hivi mfanyabiashara anayelipa mlolongo wa kodi huku anauza bidhaa za ndani atamudu vipi kupambana na mfanyabiashara anayeagiza vitu kutoka nje (huku vingine vikiwa feki) lakini anavilipia kodi pungufu au halipi kodi kabisa?Ni dhahiri biashara ya huyo "anayebebwa" itashamiri zaidi kuliko ya huyo mnyonge anayejikongoja peke yake.

Lakini pia kuna suala la utamaduni wa kuthamini baidhaa za nje kuliko za ndani.Baadhi ya wachambuzi wanaeleza kuwa miongoni mwa madhara ya utandawazi ni kuibuka kwa mapambano kati ya vitu vya nje dhidi ya vya ndani au vya asili.Hapa simaanishi kuwa kila element ya utandawazi ni mbaya.Sasa kama serikali yetu inaagiza kila kitu kutoka nje kwa ajili ya matumizi yake huku ikiwaacha mafundi seremala wetu "wakidodewa" na samani zao,na hiyo ni kabla ya ufunguzi wa soko hilo,sasa kwanini wasomi wasihofu kuwa soko hilo linaweza kuwa habari mbaya zaidi kwa Watanzania wengi?

Tukija kwenye ajira,hali ndio mbaya zaidi.Wakati Watanzania wamekuwa mahiri zaidi kupeleka watoto wao Kenya na Uganda,wenzetu hao wamekuwa wakileta nguvu kazi yao ya ziada kuchukua nafasi mbalimbali za kazi.Na kama ilivyo kwenye suala la bidhaa,waajiri wetu nao wanaelekea kuwa na ugonjwa uleule wa kuthamini zaidi wageni kuliko wazawa.Mwapachu alipaswa kutueleza ni Watanzania wangapi wana ajira nchini Kenya,Uganda au Rwanda kulinganisha na raia wa nchi hizo waliokamata ajira hapo nyumbani kabla ya ujio wa soko la pamoja.Najua hawezi kusema hilo sio kwa vile hana takwimu (na inawezekana kabisa akawa hana) bali anafahamu kuwa kwa kweka hilo bayana atalazimika kuungana na hofu walionayo wasomi na Watanzania wengine.

Kilichoua Jumuiya ya awali ya Afrika Mashariki ni kuweka siasa mbele ya maslahi ya nchi.sambamba na kupuuza ushauri wa wataalamu.Na akina Mwapachu ambao walikuwa watu wazima muda huo wanataka kurejea makosa hayohayo.Wanajifanya vipofu wa ukweli kwamba ni vigumu kuwa na ushirikiano wa maana palipo na viwango tofauti vya maendeleo kati ya nchi husika.Tunafahamu vema uchumi wa Kenya,Uganda na Rwanda unavyofanya vema zaidi ya uchumi wetu.Sasa kama tunafahamu hilo kwanini basi tusihofu kuwa soko hili jipya linaweza kufanya hali kuwa mbaya zaidi?Au Mwapachu na wenzake wanadhani kuwa ukigusana na tajiri nawe unapata utajiri?They are completely wrong.Mahusiano ya mwenye uwezo wa kiuchumi na mwenye uwezo duni mara nyingi huishia kumnufaisha zaidi mwenye uwezo kwani nguvu ya uchumi inapelekea kuwa na nguvu kwenye maeneo mengine pia.

Akina Mwapachu wanapaswa kufuatilia kwa karibu mambo yanayoyumbisha jumuiya ya Ulaya ambapo nchi kama Uingereza zimeendelea kuwa na msimamo wa kujihusisha kwa kiasi flani tu na sio kwa asilimia 100 kwa vile wanatambua kuwa kuna nchi zenye uchumi duni zinazotarajia ushirikiano huo uwanufaishe wao zaidi at the expense of wale wanaojimudu.

Mwisho,ili Tanzania ijikomboe kutoka uchumi unaomilikiwa kwa zaidi ya asilimia 90 na wageni ni lazima siasa iwekwe kando,ushauri wa kitaalamu uzingatiwe,na kubwa zaidi,maslahi ya taifa yawekwe mbele ya maslahi binafsi.Vinginevyo,soko la pamoja la Afrika Mashariki litaishia kuwa soko la bidhaa na ajira kwa Wakenya,Waganda,Wanyarwanda na Warundi na sie "tukiishia kunufaika" kwa uwepo wa akina Mwapachu kama viongozi wa jumuiya ilhali uchumi wetu ukizidi kuelekea shimoni.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.