Showing posts with label Lawama. Show all posts
Showing posts with label Lawama. Show all posts

29 Jan 2012


Problem Solving Flowchart
CHADEMA ndio wamesababisha mgomo wa madaktari

Wanabidii
TAARIFA za kiintelijensia zimebaini kuwa CHADEMA ndio wamesababisha mgomo wa madaktari, mgomo ambao umeendelea kwa siku kadhaa sasa na umehatarisha maisha ya wagonjwa wengi na umesababisha hata madaktari kuvuana uanachama kwenye chama chao cha madaktari.

CHADEMA ndio hao hao wamekuwa wanaratibu migomo mingi kwenye vyuo vikuu, ndio haohao wameratibu mgomo wa madereva wa malori kule Mbeya lakini pia ni CHADEMA walio hakikisha Naibu Waziri wa Afya anagoma kwenda kuonana na madaktari pale kwenye ule ukumbi walioandaa wao maana protokali na
usalama wake ulikuwa hatarini.

Hawa CHADEMA hawafai, maana wanataka nchi isitawalike, Wanafanya haya wakijua kuwa Rais Kikwete yuko kwenye mkutano wa uchumi duniani na kule anakutana na kuongea ikiwa ni pamoja na kupiga picha na Bill Gates na matajiri wengine wa dunia ili watusaidie kujikwamua kutoka kwenye mkwamo wa njaa na uchumi mbovu.

CHADEMA ndio hawa hawa wamesababisha sasa hivi shilingi yetu imeshuka thamani maana muda mwingi wanautumia kuwasumbua watu waliokuwa wanajua matumizi ya shilingi na sasa wamekasirika na matokeo yake shilingi imeshuka thamani.

CHADEMA ni watu wabaya sana, maana baada ya mgomo huu wa madaktari wataandaa mgomo mwingine waliouahirisha na walimu mwaka jana, wanachowaza CHADEMA ni migomo tu ili serikali idorore na nchi isitawalike, CHADEMA ni chama cha fujo na maandamano.

Chama hicho kimewezesha mgomo mpaka ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na kusababisha wale makada wenye magamba kugoma kuvua magamba yao! Hiki chama ni kibaya sana kinawanyima usingizi viongozi na makada wa chama cha magamba.

Watanzania mtambue kuwa CHADEMA ni chama kibaya sana maana ndicho kimesababisha minong’ono, eti Dk. Harrison Mwakyembe amewekewa SUMU! Nani amuue kiongozi huyo?

Mwakyembe hana tatizo kubwa anaugua tu mafua na hata ripoti yake ni CHADEMA hao hao ndio wameizua, maana wanajua kuwa ikiwekwa hadharani italeta tena mambo yake yenye harufu ya ki - Richmond.

CHADEMA ni watu wabaya sana, maana wamesababisha maisha magumu kwa kila Mtanzania, tofauti na ahadi za CCM kutaka kuwapa maisha bora kila Mtanzania, chama hicho kimesababisha mpaka umeme unatolewa kwa mgawo na unakatika katika mara kwa mara.

Tusiwaamini watu hawa, maana wanataka kuiondoa serikali iliyoko madarakani kwa maandamano kwa madai kuwa imeshindwa kuboresha huduma za msingi kwa Watanzania.

Nadhani sasa ni wakati muafaka kwa CHADEMA kimsababishe Rais Jakaya Kikwete agome kuingia IKULU, ili nchi iingie kwenye uchaguzi kabla ya mwaka 2015, kwakuwa huko kote kutakuwa mbali sana.

Hii ni siri yako! Hata yale mafuriko yaliyotokea jijini Dar es Salaam na kusababisha ndugu zetu kuhamia kwenye majumba ya nguvu kule Mabwepande, ni jamaa hawahawa wakiongozwa na makamanda wao. Hawa jamaa ni nuksi!


CHANZO: Tanzania Daima

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.