Showing posts with label MAISHA BORA KWA KILA MTANZANIA. Show all posts
Showing posts with label MAISHA BORA KWA KILA MTANZANIA. Show all posts

20 Jul 2010

SIKU moja baada ya Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete kueleza umma wa Watanzania kwamba ongezeko la magari na kero ya msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam ni dalili ya maisha bora, wanazuoni na wanasiasa nchini wameikosoa kauli hiyo na kuilaani vikali.

Wamesema kauli hiyo ni dalili tosha kwamba CCM imekosa mwelekeo halisi ya maendeleo ya nchi hivyo haistahili kuendelea kutawala kwa kuwa haina dira ya kubali maisha ya Watanzania.

Mhadhiri katika kitivo cha Sayansi ya Siasa ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Bw. Bashiru Ally aliliambia Majira kuwa ni aibu kwa kauli hiyo kutolewa na kiongozi wa nchi aliyebeba dhamana ya taifa zima.

Alisema ongezeko la fedha, majumba ya kifahari kwa watu wachache na foleni za magari jijini Dar es Salaam hakuwezi kuchukuliwa kama kipimo cha maisha bora kwa kuwa hivyo si vigezo vinavyopaswa kutumiwa kupima kiwango cha maendeleo katika nchi yoyote duniani.

Alisema maisha bora na maendeleo yoyote katika nchi yanapaswa kupimwa kwa kuzingatia ongezeko la watu, upatikanaji wa ardhi, siasa safi na uongozi bora mambo ambayo bado ni ya taabu na yanayozua migogoro mikubwa nchini.

"Kauli hii inanikumbusha kauli ya hayati Korimba (Horance), kuwa CCM haina dira wala mwelekeo, huwezi kupima maisha bora ya mwananchi wa Masasi au Kagera kwa kuangalia foleni za magari Dar es Salaam, laiti kama Mwalimu (Nyerere) na Sokoine (Moringe) wangekwepo leo kauli hii ingewapandisha presha," alisema Bw. Bashiru.

Alisema ni vema Rais Kikwete akaangalia uwiano wa ngezeko la foleni hizo na uboreshaji wa miundombinu hususan barabara, shule na mfumko wa bei za bidhaa na thamani ya fedha ambavyo vimekuwa vikiporomoka kwa kasi katika kipindi cha uongozi wake.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Bw. Freeman Mbowe, alisema kauli hiyo inaonesha jinsi serikali ya CCM isivyokuwa na jambo la kujivunia kwa wananchi katika kipindi chote cha miaka mitano iliyopita.

Alisema kimsingi msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam inasababishwa na ukosefu wa miundombinu ambayo chimbuko lake ni uongozi mbovu ulioko madarakani.

Alisema kinachotokea Dar es Salaam si kuboreka kwa maisha ya wananchi bali ni ongezeko la tabaka kati ya walionacho na wasio nacho hasa masikini walioko vijijini hali ambayo inasababisha ongezeko la watu mijini wasiokuwa na ajira wala mahali pa kulala.

"Foleni za magari Dar es Salaam si dalili ya maisha bora, na kama ukifanya utafiti utagundua kuwa foleni kubwa ni katika baadhi ya barabara zinazoelekea kwa matajiri wachache ambao baba, mama na watoto kila mmoja ana gari lake, sasa maendeleo ya watu wachache huwezi kuyatumia kupima kiwango cha maisha ya Watanzania wengine," alisema Bw. Mbowe.

Naye Mhadhiri Mwandamizi katika Kitivo cha uchumi na Biashara Chuo Kikuu cha Dar Salaam, Profesa Humphrey Moshi, alisema si sahihi kwa rais wa nchi kupima maisha ya Watanzania wachache wengi kwa kutumia mfano wa watu wachache wenye uwezo wa magari.

Alisema licha ya ukweli kuwa ongezeko la idadi ya watu wanaomiliki magari linaweza kutumika kuonesha ongezeko la kipato kwa wananchi lakini haikuwa sahihi kwa kiongozi wa nchi kupima maisha ya Watanzania kwa kuangalia wenye uwezo wachache walioko Dar es Salaam.

Alisema Dar es Salaam ni mji wa kibiashara wenye viwanda, mashirika na taasisi karibuni zote za serikali ambazo katika shughuli za kawaida zinahitaji usafiri wa magari, hivyo kuna uwezekano kuwa foleni kubwa husababishwa na magari ya taasisi, hizo lakini si mabadiliko ya maisha ya Watanzania.

"Magari mengi si ya watu binafsi, idara nyingi za serikali ziko hapa, kuanzia ikulu, bunge, wizara zote, taasisi binafsi, mashirika ya dini, viwanda na wafanyabiashara mbalimbali ambao ndio wamiliki wa magari, sio wananchi wa kawaida, sasa huwezi kusema kuwepo kwa foleni za magari ya idara hizi ni maisha bora kwa wananchi," alisema Prof. Humpherey.

Alisema maendeleo yanapimwa kwa kuangalia maisha ya jumla si ya mwananchi mmoja mmoja, ikiwa ni pamoja na kuangalia uwezo wa kuzalisha mali wa wananchi, thamani ya fedha, kiwango cha elimu na uimara wa sekta za viwanda na kilimo, na si kuangalia msongamano wa magari yaliyokosa barabara za kupita.

Akihutubia wana CCM na wananchi wa Mkoa wa Dar es Salaam katika mkutano wa kuwatambulisha wagombea urais, mgombea mwenza na Rais wa Tanzania Visiwani katika viwanja vya Mnazi Mmoja, Rais Kikwete alisema ongezeko kubwa la magari na kusababisha msongamano wa magari ni mijawapo ya dalili za maisha bora.

CHANZO: Majira

3 Mar 2010

NI IDADI INAYOKARIBIA WALIOPIGA KURA MWAKA 2005

na Mwandishi Wetu

WATANZANIA wapatao milioni 8.4 wanashinda na njaa au kulala njaa ili kukabiliana na ukali wa maisha, utafiti umeonyesha.

Kwa mujibu wa utafiti wa Synovate uliofanyika kati ya Septemba na Desemba 2009, wananchi wanaahirisha milo kwa sababu hali ya kiuchumi ya Watanzania milioni 20 imezidi kuwa mbaya.

Mbali na wale waliopunguza bajeti zao (asilimia 43), na wale walioamua kuacha kula baadhi ya milo kwa siku (asilimia 21), watu milioni 11.2 (wanaowakilishwa na asilimia 28 ya wahojiwa), walisema hawajachukua hatua zozote dhidi ya kuongezeka huko kwa gharama za chakula wakati watu milioni 1.6 (asilimia 4) walisema wamekopa kutoka kwenye benki za biashara na hawajui jinsi ya kurejesha mikopo hiyo.

“Idadi ya wale waliosema kuwa hali zao za kiuchumi zimebakia vile vile ilikuwa ni watu milioni 16.8, ambao ni asilimia 42 ya wahojiwa.

“Ni watu milioni 1.4 sawa na asilimia 4 tu ya waliohojiwa, ndio waliosema maisha yao yameboreka, huku watu wengine milioni 2 sawa na asilimia 5 ya waliohojiwa wakisema hawajui,” alisema meneja huduma wa Taasisi ya Synovate, Jane Meela.

Kwa mujibu wa utafiti huo, idadi ya waliosema hali zao za kiuchumi zimekuwa mbaya zaidi ilikuwa kubwa zaidi kwa upande wa wanawake kuliko wanaume, wakati wanaume kidogo walisema hali zao za kiuchumi zilibakia vile vile.

Kwa kuzingatia kipimo cha maendeleo ya jamii, kisiasa na kiuchumi (SPEC), wananchi milioni 17.2 pia wamelazimika kupunguza matumizi yao ya vitu vya nyumbani kutokana na kupanda kwa gharama za mahitaji ya msingi.

Matokeo hayo yalitolewa na meneja utafiti na mawasiliano wa taasisi hiyo, Abdallah Gunda na meneja huduma, Meela, katika mkutano wao na wanahabari uliofanyika juzi jijini Dar es Salaam.

“Makali ya maisha nchini yamefikia hatua mbaya zaidi tangu utafiti wetu uliopita, na mwenendo wa sasa unatisha,” alisema Meela.

Alisema kinachoonekana ni kuwa watu maskini wameendelea kutokomea kwenye umaskini, huku kukiwa na watu wachache tu wanaoona kuwa hali za maisha yao zimekuwa bora.

Meela alisema serikali inahitaji sera na mikakati iliyojengwa na matokeo ya tafiti kama hizo kufanya gharama za maisha ziwe nafuu kwa kila mtu.

Utafiti huo ulihusisha sampuli nasibu za idadi ya watu 2,000 waliopatikana katika mikoa yote 21 ya Tanzania Bara, na visiwa vya Unguja na Pemba.

Alisema matokeo ya sampuli hizo yalipangwa katika jedwali na kufanyiwa upembuzi uliozingatia makadirio ya idadi ya watu milioni 40 nchi nzima ili kupata takwimu zilizokaririwa katika ripoti hiyo.

Matokeo hayo yanaonekana kuakisi hali halisi yakilinganishwa na mwenendo wa hivi karibuni wa mfumuko wa bei za vyakula.

Takwimu za Benki Kuu ya Tanzania (BoT) zinaonyesha kuwa mfumuko wa bei nchini umebaki katika tarakimu mbili.

Rais Kikwete aliingia madarakani kukiwa na nafuu ya mfumuko wa bei, kwani ulikuwa asilimia 5.8.

Hali ilikuwa mbaya zaidi mwaka jana mwezi Agosti, ambapo ulifikia asilimia 18.9, mwezi mmoja tu kabla ya kufanyika kwa utafiti huo wa Synovate.

Kiwango hicho kilishuka hadi kufikia asilimia 17.3 Septemba na kupanda hadi asilimia 18.1 Oktoba, na tangu wakati huo kimekuwa kikishuka na kupanda kati ya asilimia 14.5 na 17 kwa miezi iliyofuatia.

Wachumi wamekuwa wakitumia kigezo hiki kuthibitisha jinsi serikali ya awamu ya nne ilivyoshindwa kuboresha maisha ya mwananchi.

Na wanaharakati wametumia kigezo hiki, na kukithiri kwa ufisadi miongoni mwa vigogo serikalini, kama kielelezo cha Serikali ya Rais Kikwete kushindwa kutimiza ndoto zake za ‘maisha bora kwa kila Mtanzania.’

Naye Gunda alisema tatizo la rushwa na hongo ndilo lililotajwa kuwa sugu kwani linaathiri wengi nchini na lilipewa asilimia 53, likifuatiwa na tatizo la umaskini lililopewa asilimia 42, gharama za vyakula, asilimia 39, uhaba wa chakula na njaa, asilimia 38.

Tatizo la ajira, ukimwi na VVU, maji, kupanda kwa gharama za maisha, afya, umeme, ukame, barabara, elimu, kilimo, kutokuwepo kwa usalama na matumizi ya dawa za kulevya pia vilitajwa kama miongoni mwa matatizo makubwa nchini.

Utafiti huo umebainisha kuwa rushwa na umaskini ni matatizo yanayowaathiri zaidi wanaume kuliko wanawake.

CHANZO: Tanzania Daima

16 Oct 2009



Picha kwa hisani ya vyanzo mbalimbali mtandaoni.

20 Jun 2009


Ahadi tupu za kiwete zaelekea kutengeneza kitanzi cha CCM 2010

Na Mwandishi Wetu

IKIWA imesalia takriban miezi 18 kabla ya Uchaguzi Mkuu Oktoba mwakani, sasa ni dhahiri kuwa Rais Jakaya Kikwete ana kibarua kigumu cha kukamilisha ahadi lukuki alizotoa wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005.

Mazingira hayo pia yanawaweka njiapanda wabunge wengi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika kutetea tena nafasi zao.

Baadhi ya wabunge tayari wameliona hilo na miongoni wamelisema bungeni wakiwashutumu mawaziri ambao wamekuwa wakilimbikiza miradi ya maendeleo kwa upendeleo kwenye maeneo yao bila kuzingatia vipaumbele vya taifa, hata baadhi yao walifikia hatua ya kutishia kukwamisha bajeti iliyopitishwa Alhamisi iliyopita.

Kauli kali zaidi ilitoka kwa Mbunge wa Nzega, Lucas Selelii aliyeomba dua kwa Mungu awalaami mawaziri hao.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa, ahadi kadhaa alizozitoa Rais Kikwete bado hazijatekelezwa na kwa kipindi kilichosalia ni vigumu kufanya hivyo.

Miongoni mwa ahadi alizotoa Rais Kikwete na hazijaonekana matunda yake dhahiri ni zile zilizoandamana na kaulimbiu yake ya Ari Mpya, Nguvu Mpya, Kasi Mpya na mpango wa ‘Maisha bora kwa kila Mtanzania’.

Kigogo mmoja ndani ya CCM amelieleza gazeti hili kwamba ahadi hiyo ya maisha bora ndiyo ilimpatia Kikwete kura za kishindo na isipotengenezewa mkakati maalumu inaweza kuwa ndio kitanzi chake na wabunge wengi wa CCM.

Alisema ahadi hiyo imesababisha baadhi ya vigogo wa chama na serikali kubadili kauli, na kusema kwamba maisha bora hayatawafuata wananchi kama hawafanyi kazi kwa bidii.

Kwa mujibu wa watu mbalimbali waliozungumza na Mwananchi Jumapili, na hata kauli za wabunge wanapochangia bungeni, Watanzania walio wengi bado wana hali duni ya kimaisha, jambo ambalo litakuwa gumu kulieleza kwa wapigakura hapo mwakani.

Kutokana na ahadi hiyo serikali ilitoa Sh30 bilioni ambazo zilipewa jina la mabilioni ya Kikwete, lakini hazikufika kwa maskini walio wengi kutokana na masharti yake kuwa magumu, na kuangukia kwenye mikono ya wasio wajasiriamali wadogo, hivyo kukwamisha mpango huo wa rais.

Ahadi nyingine zinazoelekea kushindikana ni ya mwafaka wa kisiasa wa Zanzibar ambao Rais Kikwete aliuweka kwenye kipaumbele, lakini hadi sasa hakuna mafanikio yoyote na tayari Chama cha Wananchi (CUF), kimetangaza kujitoa katika mazungumzo.

Ahadi nyingine ni ujenzi wa madaraja ya Kilombero mkoani Morogoro na Kigamboni, jijini Dar es Salaam ni miongoni mwa ahadi kubwa alizotoa Kikwete na hadi sasa hakuna dalili zinazoweza kuashiria kuwa ipo nia ya utekelezaji.

Hata hivyo, Waziri wa Miundombinu, Dk Shukuru Kawambwa alipoulizwa alisema kwamba daraja la Kilombero limetengewa fedha katika bajeti ya mwaka 2009/10.

Kuhusu daraja la Kigamboni, alirudia kauli za muda mrefu kuwa hilo limo kwenye mkakati wa kuanza kujengwa wakati wowote chini ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kwa kushirikiana na wahisani mbalimbali.

Ahadi nyingine ambazo hazijatekelezwa, zimeelezwa kuwa ni kilio cha mahakama nchini juu ya suala la masilahi ya watumishi na vifaa vya kazi.

Hivi karibuni, Jaji Mkuu, Augustino Ramadhan alisikika akilalamika kuwa kiwango cha mafungu yanayoahidiwa kutengwa kwa mahakama hufika kwao kikiwa pungufu.

Suala jingine limeelezwa kuwa ni uboreshaji wa mashirika ya umma ambayo bado yako mikononi mwa serikali, lakini kila kukicha yamekuwa na matatizo na kuzua malalamiko mengi.

Kwa upande wa barabara ambazo ziliahidiwa kujengwa kwa kiwango cha lami na ambazo bado ni Tabora-Nzega, Bunda-Ukerewe na Marangu-Mkuu Rombo-Tarakea-Kamwanga.

Aliahidi pia kulifanya jimbo la Rorya mkoani Mara kuwa wilaya, lakini utekelezaji wake umekuwa ukisuasua.

Mambo mengine ilikuwa ni kupambana na rushwa, lakini pamoja na hali hiyo kuonekana kuzaa matunda kwa mambo mengi yaliyokuwa yamejificha kuchimbuliwa na kuwekwa hadharani, malalamiko yanayoibuka ni baadhi ya watuhumiwa kutofikishwa mahakamani.

Rais Kikwete pia aliahidi kuondoa kero nyingi za Muungano lakini licha ya kuunda kamati ya kuzijadili na kuzishughulikia chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais, zipo dalili za baadhi ya wananchi kutoridhika.

Tatizo kubwa linalojitokeza ni baadhi ya Wazanzibari, wakiwamo viongozi wa SMZ kutoa kauli zinazoonyesha dalili za waziwazi kwamba wanadhulumiwa ndani ya Muungano.

Pamoja na hali hiyo, Rais Kikwete atajivunia kwa kutekeleza ahadi yake ya kulifanya Bunge kuwa huru kwani limeonyesha dhahiri kuwa na meno kwa kufichua udhaifu wa baadhi ya vigogo serikali bila kuwa na woga.

Ameonyesha mafanikio pia katika ahadi yake ya kuendesha dola kwa misingi ya utawala bora na uwajibikaji; utawala wa sheria unaoheshimu na kulinda haki za binadamu.

Hata hivyo, katika kipengele hicho kuna manung’uniko kadhaa kama vile baadhi ya viongozi wanaotuhumiwa kuendelea na nyadhifa zao wakati taratibu za utumishi wa umma ziko wazi kwamba wangepaswa kusimamishwa au kupewa likizo ama kuhamishiwa sehemu nyingine, ili uchunguzi huru ufanyike.

Mafanikio mengine ni kutekeleza ahadi ya kuongeza nafasi za elimu ya juu baada ya kuanzishwa kwa Chuo Kikuu cha Dodoma.

Ahadi nyingine ambayo Rais Kikwete ameonekana wazi kuivalia njuga ni kuboresha kilimo; na tayari mikakati kadhaa ikiwepo ya pembejeo za kilimo imewekwa, ingawa kuna malalamiko ya pembejeo kutofika kwa wakulima na wakulima wa karafuu na kahawa kutokuwa huru kutafuta masoko yao nje ya nchi.

Nguvu kubwa ya serikali yake kuielekeza kwenye kilimo imechagizwa na mtikisiko wa uchumi duniani ambao umetishia uchumi wa nchi nyingi hasa maskini ambazo zinategemea chakula kutoka nje.

Licha ya mafanikio hayo, serikali ya Kikwete inakabiliwa na changamoto kadhaa hasa za wananchi kutoridhika na mambo mbalimbali yanayotendwa na serikali yake.

Lingine ni wananchi kuona kuwa bado serikali ina matumizi makubwa ya fedha na wakati huo huo inawabidi kufunga mkanda ili kuihudumia huku wakikabiliwa na mazingira magumu ya kipato.

Malalamiko mengine ni baadhi ya watendaji serikalini kuendelea kutumia magari ya kifahari na kutenga Sh19 bilioni kwa ajili ya chai maofisini.

CHANZO: Mwananchi

22 Mar 2009


Na Khamis Mkotya

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA), imesema orodha ya majina ya watumishi wasio waaminifu kwenye kitengo cha kudhibiti mapato bandarini (TISCAN), bado haijawasilishwa Makao Makuu kama ilivyoahidiwa na Rais Jakaya Kikwete. Akizungumza Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Elimu kwa Walipa Kodi, Protus Mmanda, alisema Menejimenti ya TRA chini ya Kamishna Mkuu, Hary Kitillya, inayasubiri majini hayo kuweza kuchukua hatua stahili.

Mmanda alisema, watumishi wote wa TRA watakaotajwa kwenye orodha hiyo watashughulikiwa kwa mujibu wa sheria na taratibu zote za nidhamu, ikiwa ni pamoja na kufukuzwa kazi kama Rais alivyoagiza. Machi 2, mwaka huu, Rais Kikwete alifanya ziara ya ghafla bandarini kukagua utekelezaji wa maagizo yake kuhusu ufanisi katika utendaji kazi wa bandari ya Dar es Salaam, hasa kuhusu mrundikano wa makontena. Katika ziara hiyo, Rais alionyesha kukerwa na baadhi ya watumishi wa TISCAN ambao wamekuwa wakishirikiana na wafanyabiashara wakubwa kuwaonyesha mbinu za kukwepa kodi, vitendo vinavyolisababishia taifa hasara. Rais Kikwete alisema, orodha ya watumishi wanaoendekeza mchezo huo mchafu anayo na kumtaka Kamishna Mkuu wa TRA, kuwafukuza kazi watumishi hao atakapokabidhiwa majina.

Orodha ya majina hayo bado haijafika kwetu, tunaendelea kusubiri sijui yatakuja lini, maana mimi kwa wadhifa wangu siwezi kwenda Ikulu kuuliza majina hayo yataletwa lini. “Labda kwa kuwa nyinyi waandishi wa habari mnakutana na Salva Rweyemamu, (Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu) muulizeni hayo majini yatakuja lini, lakini sisi huku hatuwezi kuuliza, hadi hapo yatakapoletwa,” alisema. Mmanda alisema kuwa, wakati majina hayo yanasubiriwa, TRA imechukua hatua kadhaa zinazolenga kuweka mfumo mzuri wa utendaji, ikiwa ni pamoja na kufanya mabadiliko kwa baadhi ya maofisa wake.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo, TRA imeshafanya mabadiliko kwa kuwahamisha idara baadhi ya maofisa wake, wanaoonekana kuwa na chembe za ukosefu wa maadili kama hatua za awali za kutekeleza maagizo ya Rais. “Hatuwezi kukaa tu bila kufanya tathimini yoyote juu ya utendaji kazi wetu, kwa sababu tunasubiri majina kutoka kwa Rais. Baadhi ya hatua tulizochukua ni pamoja na kufanya mabadiliko katika baadhi ya idara zetu. “Tumefanya marekebisho pale palipostahili, mahala palipokuwa na watumishi wazembe wasiokuwa waadilifu tumewaondoa na kuweka watumishi wengine,” alisema Mmanda, ingawa hakutaja idara na maofisa wake walioguswa na zoezi hilo.

Mkurugenzi huyo alisema, hatua nyingine zilizochukuliwa ni pamoja na kurahisisha taratibu za usajili wa magari, kuondoa kero ya muda mrefu ambayo imekuwa ikilalamikiwa kuhusu uchelewashaji wa usajili wa magari. Kwa mujibu wa Mmanda, taratibu zote za usajili wa magari yanayoingizwa nchini hivi sasa zitafanywa na ofisi moja, ili kuondoa usumbufu kwa watu, tofauti na zamani ambako taratibu hizo zilikuwa zikishughulikiwa na ofisi zaidi ya moja. Alisema kuwa, utaratibu huo mpya pia utasaidia kuondokana na watu wa ‘kijiweni’ maarufu kwa jina la ‘vishoka’, ambao wamekuwa wakiwatapeli watu kwa kisingizio cha kuwasaidia katika taratibu za usajili wa magari.

CHANZO: Mtanzania

15 Oct 2008

Wanakijiji Ichonde wakimbia makazi 

BAADHI ya wanakijiji cha Ichonde wilayani Kilombero, Morogoro, wamedaiwa kukimbia makazi yao kutokana na mateso ya viongozi wa kijiji hicho .Kwa nyakati tofauti wanakijiji hao walizungumza na Tanzania Daima, wakilalamikia mateso na fedheha wanazofanyiwa na viongozi wao wanapolazimishwa kuchangia elimu.

Haji Kawogo, mkazi wa Ichonde, alisema uongozi wa kijiji hutumia mgambo wa vijiji vingine kuwakamata nyakati za usiku, kuwafunga kamba na kuwaweka kwenye moja ya madarasa ya shule ya msingi kijijini hapo.

Alisema, wanakijiji hao hulazimishwa kuchangia elimu huku viongozi hao wakishindwa kuitisha mikutano ya kijiji na kuwasomea mapato na matumizi kama inavyotakiwa.

“Viongozi wetu wanatudhalilisha hasa sisi wanaume maana usiku umelala na familia yako wanakuvamia tena kwa kuwatumia mgambo wa vijiji vingine.

“…Wanatutoa nje ya nyumba zetu usiku, wanatufunga kamba na kutulazimisha kulala sehemu moja ndani ya darasa la shule ya msingi Ichonde,” alisema Kawogo.

Naye Asha Hassan, alisema kukosekana kwa maendeleo ya Kijiji cha Ichonde, kunasababishwa na uongozi mbovu uliopo hivyo aliiomba halmashauri ya wilaya kuingilia kati, ili kunusuru ubabe wa viongozi hao.

“Kijiji cha Ichonde, tunakosa maendeleo kwa sababu ya viongozi wetu, hawatushirikishi katika bajeti ya kijiji wanachojua ni kukusanya michango, lakini hawatuelezi kiasi kilichopatikana wala matumizi yake,” alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kijiji hicho Deogratias Makinda, akana tuhuma hizo na kueleza kwamba hana taarifa za kukamatwa, kufungwa kamba wala kulazwa katika shule ya msingi.

“Mimi sina dola ya kuwakamata wanakijiji, sina taarifa za wao kuteswa ndiyo kwanza nasikia hapa,” alisema mwenyekiti huyo.

Aidha, Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Ichonde, Salum Sadala, alikiri kwamba wapo wanakijiji wanaokamatwa na kupelekwa katika shule hiyo kwa lengo la kuhamasisha uchangiaji wa maendeleo ya kijiji.


13 Oct 2008

Serikali isilaumiwe kwa hali ngumu ya maisha-JK
 
2008-10-13 10:24:10 
Na Thobias Mwanakatwe, Kyela

Rais Jakaya Kikwete amesema kushuka kwa uchumi wa dunia hivi sasa ni lazima kutaathiri uchumi wa taifa, na hivyo hakuna sababu kwa wananchi kulaumu kwamba serikali inawatesa kutokana na hali ngumu ya maisha. 

Akiwahutubia wananchi wa mji wa Kyela juzi, alisema hivi sasa uchumi wa dunia umekumbwa na msukosuko mkubwa kuliko yote katika historia toka mwaka 1930 ambapo hali hiyo haijawahi kujitokeza. 

Alisema pamoja na kuwepo kwa msukosuko huo wa uchumi wa dunia,
hata hivyo serikali bado haijaanza kujipanga kukabiliana na hali hiyo lakini baada ya miezi michache ijayo athari zitaanza kujitokeza. 

Hata hivyo, Rais Kikwete alisema
serikali inaendelea kutafakari ni jinsi gani itaikabili hali hiyo ili kusijitokeze athari zaidi katika uchumi. 

Alisema hivi sasa kutokana na msukosuko wa uchumi, serikali ya Marekani imetenga Dola 700 bilioni kujaribu kuokoa mabenki yanayofilisika, mkakati ambao pia unafanywa na Uingereza,Ujerumani, Japan pamoja na nchi nyingine. 

``Wenzetu wanao uwezo mkubwa wa kiuchumi
sijui yakitufika sisi itakuwaje, tunaendelea kutafakari ili na sisi yatakapotukuta tufanye nini lakini siyo kazi rahisi,`` alisema Rais Kikwete. 

Aliongeza kuwa kutokana na hali hiyo hakuna sababu kwa wananchi kulalamika kuwa serikali inatutesa kwa sababu kushuka kwa uchumi wa dunia athari zake zinazikumba nchi maskini ikiwemo Tanzania.

CHANZO: Nipashe


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.