Showing posts with label MAKALA. Show all posts
Showing posts with label MAKALA. Show all posts

26 Jul 2014




 Mara ngapi unakutana na tweet, au post kwenye Facebook, au picha Instagram ikiambatana na maneno 'I am happy'? Nina hakika ni takriban kila siku. Si dhambi kutamka hadharani kuwa una furaha, lakini uzoefu waonyesha kuwa wenye furaha za dhati wala hawahitaji kuishawishi dunia kuwa wana furaha: ukiwa na furaha ya kweli itaonekana tu bila hata kuitangaza.

Hebu tuangalie tabia 20  za watu wenye furaha ya dhati lakini wala hawana muda wa kujitangaza kuwa wana furaha, kwa vile furaha hujionyesha nyenyewe pasi haja ya matangazo.

1.  Hawana muda na drama za watu wengine: Kamwe usianzishe drama, na kamwe usiruhusu drama za watu wengine zikuhusu. Wengi wa watu wenye furaha hawajali nini kinachosemwa dhidi yao na watu 'wasio muhimu' kwao. Kwa hakika, watu wenye furaha huwashukuru wanaowasema vibaya kwani ni fundisho kwao kuhusu wasivyostahili kuwa ,yaani kutostahili kutokuwa na furaha.

2. Hupendelea kutoa/kusaidia kila wanapoweza: Nadhani ushaskia usemi 'kutoa ni moyo si utajiri. Watu wenye furaha ni wepesi kutoa/kusaidia, lengo kuu likiwa kusambaza furaha waliyonayo.

3. Wanathamini mahusiano yao muhimu: Mara nyingi watu wenye furaha wana marafiki wengi kwa sababu wanathamini marafiki, na marafiki hao in return wanatambua kuthaminiwa kwa urafiki wao.Hata hivyo, umuhimu wa marafiki hao hutegemea mchango walionao kwa furaha ya wenye furaha hao.Ni vema kuepuka watu watakapa mawazo fyongo.

4. Wanatenga muda kwa ajili ya kujipenda wenyewe pia: huwezi kupenda wengine wakati hujipendi mwenyewe. Ushakskia msemo 'charity begins at home.' Na Maandiko Matakatifu yanausia kuwa huwezi kumpenda Mungu usiyemuona ilhali huwapendi wanadamu unaowaona. Kadhalika,huwezi kuwapenda wengine ilhali wajichukia mwenyewe.Tenga muda ujipende.And by the way, kama mwenyewe hujipendi nani atakuwa na muda wa kukupenda?

5. Huthamini ufanisi kuliko umaarufu: Kamwe usi-confuse ufanisi na umaarufu.Kuwa maarufu kwamaanisha unapendwa kwa kipindi flani tu,lakini kuwa na ufanisi kunamaanisha unaleta tofauti chanya katika maisha ya wengine, na kuleta tofauti chanya katika maisha ya wengine kunamfanya mtu kuwa na furaha zaidi kwani inatambulisha umhimu wake kwa wengine.

6. Wanasema 'hapana' pale inapobidi: kuna msemo wa Kiswahili kwamba mkono hujikuna pale unapofiki.Huwezi kutaka kumridhisha mtu kwa kujiumiza mwenyewe. Na ni vema kusema 'hapana' ya dhati kuliko 'ndio' ya uongo. Kumbuka,kuwa mkweli ni kiungo muhimu cha kukufanya uwe mwenye furaha.

7. Wanajua kushukuru/kuthamini: Shukrani ni mfalme wa furaha, wanasema Waingereza (gratitude is the king of happiness).Watu wenye shukrani huwa na furaha maishani kwani ni nadra kwao kuwa na kinyongo au hasira. Shukrani ninayoonglea hapa ni pamoja na kuridhika na yale tuliyojaaliwa au tulofanikiwa kuwa nayo. Kwa mfano rahisi kabisa ni kumshukuru Mungu kwa kuamka ukiwa hai.

8. Hujenga matumaini: Watu wenye furaha huyaangalia maisha kwa mtizamo chanya. Kisaikolojia,ukiliangalia jambo kwa mtizamo hasi waweza kufanya matokeo ya jambo hilo kuwa hasi pia.Kumbuka kwamba mtizamo wetu ni sehemu muhimu ya kinachotusukuma au kutuzuwia kufanya/kutofanya vitu katika maisha yetu.

9. Hawajihusishi na kila fanikio au anguko: Watu wenye furaha hawachukulii kila anguko kuwa ndo mwisho wa kila kitu na kamwe hawavimbishwi vichwa na mafanikio. Hawaruhusu anguko (failure) kuwakaa moyoni na hawaruhusu mafanikio/sifa kuwalevya kichwani.

10. Hujenga mikakati ya kukabiliana na nyakati ngumu: Sote twatambua kuwa si kila leo ni kama jana, na si kila kesho ni kama juzi. Siku huwa tofauti,na ndo maana leo kuna mvua kesho kuna jua kali. Cha muhimu ni kuwa na mikakati madhubuti ya kukabiliana na matatizo.Na moja ya njia nzuri ni kujifunza kutoka kwa wengine.Twaweza kujifunza kwa kujali experiences za wengine ma kusoma pia.

11. Huchukulia kukataliwa kama kinga dhidi ya mabaya: Kuna namna njema ya kudili na kukataliwa- kuangalia kukataliwa kama kinga ya kukuepusha na jambo bayana. Sio kila kukataliwa kunamaanisha wewe si bora,wakati mwingine kunamaanisha kwamba alokukataa ameshindwa kutambua jinsi gani ulivyo bora.Ukikataliwa, amini kwamba kuna jema zaidi lipo njiani kwa ajili yako.

12. Wanaweka mkazo katika wakati uliopo: Kuendelea kunung'unika kuhusu mabaya yaliyopita hakusaidii kubadili hali ilivyo sasa. Cha muhimu ni kujifunza kutoka kwa mabaya hayo na kujitahidi kuhakikisha kuwa hakujitokezi tena. Kwa kujifunza kutokana na mabaya yaliyopita,watu wenye furaha wanatengeneza mazingira bora ya muda uliopo na kuweka 'bima' kwa ajili ya wakati ujao. 

13. Wanawekeza nguvu na muda kwa mambo ya msingi: Ukipanda upupu utavuna upupu. Mawazo chanya huzaa matokeo chanya, mawazo hasi huzaa matokeo hasi.Hilo halina ubishi. Kesho ni matokeo ya bidii za leo, na kwa kuwekeza nguvu na muda kwa mambo bora sasa, kehso ina uhakika wa kuvuna matokeo bora ya jitihada hizo za leo.

14. Wanaji-commit katika vipaumbele vyao: Ushaskia msemo'mshika mawili moja humponyoka.' Huwezi kuchanganya shule na mapenzi na ukafainikiwa katika vyote viwili.Lakini ili uweze kuwa na mafanikio ni muhimu kutambnua vipaumbele vyako, na si kutambua tu bali pia kufahamu mbinu za kuvifikia. Na ukishavitambua na kufahamu namna ya kuvifikia,yalazimu kuwekeza mtaji wa kutosha (sio lazima fedha bali nguvu, akili na muda) kuhakikisha unavifikia.

15. Wanaangalia kutopendezwa kama sehemu ya kuboresha uwezo wao: Kuna nyakati utafanya hili lakini huotfanikiwa. Lakini badala ya kubaki na hasira au manung'uniko ni vema kutumia fursa hiyo kujiuliza kipi kilikwenda mrama hadi ukashindwa kufanikiwa.Na kwa kufanya hivyo,unatengeneza mazingira mazuri ya kupata matokeo bora kwa kitu kilekile kilichoshindikana hapo awali.

16. Wanajali afya zao: Mwili wenye afya ni kama koti la akili yenye afya: Pasipo afya bora ni vigumu mno kuwa na furaha.Na katika hali ya kawaida tu, ukiwa unaumwa na kichwa, huwezi kuwa na furaha. Watu wenye furaha huwekeza vya kutosha katika kula vizuri,kufanya mzoezi,kuepusha vitu vinavyoweza kuathiri afya zao na pia kujali mapumziko.

17. Hutumia fedha kupata uzoefu badala ya vitu wasivyohitaji: Watu wenye furaha wapo makini katika matumizi yao, hasa kuepuka manunuzi ya vitu wasivohitaji na badala yake kufanya manunuzi ya vitu muhimu kwa maisha yao. Kuna kitu kinaitwa manunuzi ya uzoefu (experiential purchase),yaani kununua uzoefu, kwa mfano kutumia fedha kwenda likizo ya kujifunza kitu flani kinachoweza kukubailishia maisha yako, au kutumia fedha kujiunga na kozi flani itakayokuongezea ujuzi, na vitu kama hivyo.

18. Wanathamini furaha japo kidogo: Ili uweze kuwa na furaha kubwa shurti uweze kuthamini furaha ndogo,kwani hata wahenga walisema haba na haba hujaza kibaba.Kidogo unachopata katika dakika moja,kitakuwa kingi kikipatikana katika saa nzima,na kingi zaidi katika siku,na kwa mwezi,mwaka au miaka kitakuwa kingi kabisa. Furaha ni ku-enjoy vitu vidogo wakati tunafukuzia vitu vikubwa.

19. Wanatambua hali ya vitu kutodumu milele: Ni hivi, kwa vile kitu kizuri hakikudumu, haimaanishi kuwa kilikuwa kibaya. Kila kitu kina muda na wakati wake.

20. Huishi maisha wanayotaka kuishi: Tatizo la watu wengi wasio na furaha ni kuhangaika kuishi maisha ya wengine.Hakuna ubaya katika kutamani jinsi flani anavyoishi lakini ni vema kutambua wewe sio yeye, na kinachompa furaha yeye si lazima kukupe furaha wewe pia.Ndege wanaweza kuruka angani, na pengine nawe ungependa kuwa na uwezo huo,lakini wewe si ndege. Wanachofokiria watu wengine kuhusu wewe,hususan usiowajua- hakijalishili. cha muhimu ni ndoto zako,malengo yako na matarajio yako. Jitahidi kuzungukwa na watu ambao sio wanaotaka uwe wao wanavyotaka bali wanaojali na kuthamini wewe unavyota kuwa au ulivyo.Tengenezeza marafiki wa kweli na dumisha mawasiliano nao. Na la muhimu kabisa ni kutambua kwamba furaha ni chaguo lako mwenyewe, kama ilivyo kwa kutokuwa na furaha.





23 Oct 2011


Makala hii ilitarajiwa kuchapishwa katika tole la wiki hii la jarida la Raia Mwema.Sina hakika kama ilichapishwa au la kwa viletovuti ya gazeti hilo haipatikani mtandaoni hadi muda huu


Kuna msemo miongoni mwa Wamarekani Weusi kwamba unaweza kumtoa Mtu (Mmarekani) Mweusi kutoka ghetto lakini huwezi kutoa ghetto ndani ya Mtu Mweusi. Kwa kifupi kabisa, ghetto ni makazi ambayo kwa tafsiri isiyo rasmi ni kama ‘uswahilini.’

Kadhalika, katika mazingira yetu tunaweza kabisa kusema unaweza kumtoa mshamba kutoka kijijini lakini huwezi kuondoa ukijijini ndani ya mshamba. Hapa neno mshamba halina maana ya kudharau watu ambao hawakuzaliwa mijini, mie nikiwa mmoja wao.

Wakati nikiwa kijana mdogo kulikuwa na mtizamo kuwa ushamba (kwa maana ya kutozaliwa mjini) ni kama ugonjwa flani hususan kwenye mikusanyiko kama mashuleni au hata vijiweni (mijini).Ninakumbuka wakati ninasoma Tabora Boys’ High School, rafiki yangu mmoja aliomba nimpatie albamu yenye picha zangu.

Nyingi ya picha hizo, kama si zote, nilipiga katika mjini mdogo wa Ifakara, ambapo katika suala la mjini na kijijini, inaangukia kundi la pili. Si kwamba Ifakara ni kijiji au sehemu iliyojaa mashamba lakini pia Ifakara si mjini kama Dar es Salaam. Kwahiyo kwa minajili ya makala hii, tuafikiane kuiita Ifakara kijijini.

Basi picha hizo kwa rafiki yangu huyo ambaye sio tu alikulia mjini bali pia alizaliwa “hospitali ambayo kila mtoto wa mjini kazaliwa,” (nikimaanisha hospitali ya Ocean Road) zilizua vicheko miongoni mwa wanafunzi wengine ambao walikuwa wanatokea Dar. Sikujilaumu kwa uamuzi huo wala sikuona aibu. Kwako ni kwako hata kukiwa porini.

Nilifika Dar kwa mara ya kwanza nilipokuwa kidato cha pili (katikati ya miaka ya 80).Nakumbuka jinsi lafidhi yangu ya Ifakara ilivyogeuzwa chanzo cha vichekesho kila nilipokwenda kwenye magenge ya maongezi (vijiweni).Lakini sikuona aibu kwa sababu lafidhi ya ‘kishamba’ si ugonjwa.

Nilipokuja Uingereza mara ya kwanza nikakumbana na tatizo kama hilo, ambapo lafidhi ya Kiingereza change ilikuwa imetawaliwa sana na Kiswahili, kiasi kwamba mara nyingi nilipoongea na wenyeji wa hapa waliuliza mara mbili mbili nilichokuwa nakiongea. Miaka 10 baadaye, lafidhi yangu haijabadilika sana.

Ahueni niliyopata kwa huku Scotland ni ukweli kwamba lafidhi ya Kiingereza cha Waskochi inawasumbua hata Waingereza wenzao wa sehemu nyingine (kwa mfano England).Lakini kikubwa zaidi kwa hapa ni ukweli kwamba lafidhi yako ni kitu cha kujivunia, ni sawa na utambulisho wako.

Msimamizi  (Supervisor) wangu wa kwanza wa kozi yangu ambaye alikuwa mzaliwa wa Wales (na hivyo kujikuta anahangaika na lafidhi za Waskochi) alinitia hamasa kwa maelezo haya, “ukiongea huku una lafidhi flani basi inamaanisha una lugha au utamaduni zaidi ya mmoja, na hiyo ni faida kwako.”

Lengo la makala hii si kuchambua lafidhi au lugha bali kuzungumzia nafasi ya tabaka la kati ambalo kwa kiasi kikubwa linapatikana mijini, hususan jijini Dar. Katika jamii ya kinadharia, tunaweza kuwa na matabaka makuu matatu: tabaka la juu (Upper Class),tabaka la kati (Middle Class) na tabaka la chini (Lower Class).Kwa kifupi, kinachotenganisha matabaka hayo ni nguvu yao katika jamii (au power kwa kimombo).Kwa mantiki hiyo, tunaweza kuigawa jamii katika makundi ya ‘wenye nguvu’ (the powerful) na ‘wasio na nguvu’ (the powerless).  

Ugumu uliopo katika kuielezea dhana ya matabaka katika jamii inatokana na ukweli kwamba takriban kila fani inayaangalia matabaka kwa mtizamo wake. Japo kuna mwingiliano, lakini dhana ya matabaka inaweza kueleweka tofauti kati ya fani ya siasa, uchumi, elimu jamii (Sociology), nk. Hapa nitaizungumzia dhana hiyo kwa mtizamo wa jumla pasipo kuelemea fani moja.

Ukiingia kwa undani sana utakuta kati ya matabaka hayo matatu kuna matabaka madogo madogo kwa namna hii: tabaka la kati la juu (Upper Middle Class), tabaka la kati la chini (Lower Middle Class), na tabaka la wafanyakazi (Working Class).Labda nitumie mchoro kama hivi: Tabaka la JuuTabaka la Kati la JuuTabaka la Kati la ChiniTabaka la WafanyakaziTabaka la Chini. Hii ni kwa mujibu wa mchanganuo wa kitaaluma wa matabaka wa karibuni zaidi (mwaka 2005) na ni kwa mujibu wa mtizamo mmoja wa kitaaluma wa Marekani.

Ili tuelewane, ni muhimu kuzingatia tahadhari niliyoitoa awali kuwa mgawanyiko huu ni wa jumla-jumla kwani kuna tofauti za kimtizamo miongoni mwa wachambuzi, fani na kanuni (theories) zinazohusu mada ya matabaka.

Pengine katika kurahisisha maelezo, mfano mwepesi ni wa kijana kama mie niliyekulia kijijini, mtoto wa mkulima, kisha nikaja mjini kupata elimu ya juu, na hatimaye kupata kazi. Ukiangalia mlolongo huo unaweza kubaini kuwa, kwa namna flani, nimetoka tabaka la chini na kuingia tabaka la kati. Pengine nikagombea ubunge (hapana, sina wazo hilo) nikamudu kuingia tabaka la juu.

Kwanini tabaka la kati lina umuhimu mkubwa katika mabadiliko ya jamii? Jibu jepesi ni kwamba tabaka hilo linatarajiwa kuelewa zaidi masahibu yanayolikabili tabaka la chini. Yaani kwa kutumia mfano wetu wa mie niliyetoka kijijini, sio tu ile lafidhi yangu iliyonifanya nichekwe mjini bali pia uzoefu wangu wa kijijini kuulinganisha na wa mjini unaweza kuniweka katika nafasi nzuri zaidi ya kuwa na msaada wa namna flani kwa ‘tabaka la kijijini’ (la chini).

Lakini tatizo lililopo katika jamii yetu (na hii ni kwa jumla-jumla) ni tabaka hilo la kati kutamani kuwa tabaka la juu, na hapo hapo kulipuuza tabaka la chini. Kwa kutumia mfano, kijana aliyetoka kijijini na kuwaacha wazazi wake wakihangaika na ufukara uliozoeleka kwenye tabaka la chini, anapata ajira baada ya kuhitimu masomo, na anajaribu kuishi maisha kama yale ya vigogo au watoto wao.

Ofkoz, Wanasema ukienda Roma inabidi uishi kama Warumi. Lakini hiyo haimaanishi usahau ulipotoka. Hapa ninamaanisha kuwa hakuna ubaya kwa kijana kutoka kijijini kujaribu kuendana na maisha ya ‘kimjini’ bali tatizo ni pale anaposahau ‘wajibu’ wake (ambao si wa lazima) wa kutumia nafasi aliyonayo kuhamasisha au kuchangia kuboresha tabaka wanaloishi wazazi, ndugu, nk huko kijijini.

Naomba pia tuelewane kuwa hapa ninatumia ‘umjini’ kama aina ya maisha ya jumla (kinadharia na wakati mwingine kiuhalisia) ya wakazi wa mjini. Yaani katika dhana ya kufikirika, chaguo la makazi kwa tabaka la juu ni mjini (japo haimaanishi kila anayeishi mjini yupo kwenye tabaka hilo).

Kuna wenzetu ambao hawajawahi kufika kijijini, na kwao Tanzania ni ile wanayoishi na kuiona mijini. Lakini kama ilivyo kwa nchi nyingi masikini, idadi kubwa ya wananchi wake wanaishia vijijini. Ukiwa umezaliwa na kukulia Masaki, Upanga, Mbezi Beach, nk na sehemu yako ya kazi ikawa Mjini Kati na maeneo kama hayo (na ikatokea hajawahi kufika kijijini) basi inaweza kuwa vigumu kwako kuielewa ‘Tanzania nyingine’ huko vijijini.

Wakati nipo huko nyumbani, kila mara niliposafiri kati ya Dar na Ifakara nilikuwa ninajaribu kuangalia namna mandhari na pengine hali ya mjini ‘inavyoyeyuka’ kadri safari ya kuelekea ‘kijijini’ ilivyokuwa inashika kasi. Na Nilipofika kijijini tofauti zilikuwa ni za wazi. Kwa mfano, wakati vitu kama magari na runinga vilionekana vya ‘kawaida’ kwa kijijini viliangaliwa kwa mtizamo ‘zaidi ya wa kawaida.’

Lakini pia hata katika suala la tabia za kibinadamu kulikuwa na tofauti. Kwa mfano, wakati mwanamke kuvaa suruali mjini halikuwa jambo ‘kubwa, kwa kijijini lingeweza kuzua picha tofauti. Ninasisitiza, huu ni mtizamo wa jumla na haimaanishi hali iko hivyo kila kijiji.

Wakati Tanzania yetu inahitaji mno maendeleo na kuondokana na umasikini (hususan huko vijijini), tabaka la kati lingeweza kuwa kiungo na nyenzo muhimu kwa, aidha kushiriki au kuunga mkono harakati za tabaka la chini, au kwa vile lina ukaribu na tabaka la juu, kujaribu kushawishi-au hata kuilazimisha- tabaka la juu liangalie na/au kushughulikia matatizo ya tabaka la chini.

Mabadiliko tunayoshuhudia yakiendelea kutokea sehemu mbalimbali duniani (kwa mfano nchini Tunisia, Misri, Libya, nk) yamechangiwa zaidi na muungano wa nguvu za matabaka haya mawili-la kati na la chini. Kwa bahati mbaya (au makusudi) kwa kiasi kikubwa tabaka la kati kwetu limekuwa likitamani zaidi kuwa tabaka la juu (kitu ambacho si kibaya endapo kitasaidia kulikwamua tabaka la chini) na kulisahau tabaka la walalahoi.

Nimalizie kwa kukiri kuwa ninafahamu mada hii inaweza kuleta mkanganyiko wa aina fulani lakini lengo ni kuhamasisha tabaka la kati kuunganisha nguvu na tabaka la chini katika kuikwamua Tanzania yetu kutoka kwenye lindi la umasikini (na ufisadi) na hatimaye kila Mtanzania aone fahari ya kuwa mwananchi wa Tanzania.

Inawezekana, timiza wajibu wako

Barua-pepe: [email protected]
Blogu: www.chahali.com  


7 Jul 2011


Na Nova Kambota,

Rais wa awamu ya tatu Mzee Benjamin Mkapa aliwahi kusema kuwa maisha bila vipaumbele ni ujinga mtupu, bilashaka hili halina ubishi kabisa taifa lolote linaloishi bila vipaumbele hugeuka taifa la wahuni, waporaji, mafisadi, wajinga,duni na zaidi huwa taifa legelege na dhaifu.

Wageni mbalimbali kutoka Ulaya, Marekani ,Asia na sehemu nyingine za ulimwengu waliowahi kufika nchini huwa wanashangazwa sana na umasikini wa kutisha unaowaandama wananchi wa taifa hili. Wageni wanatushangaa sana na wataendelea kushangaa kuanzia Mlima Kilimanjaro,Mlima Meru, Udzungwa, Usambara, Ziwa Tanganyika, Victoria, Bahari ya Hindi mbuga nzuri za wanyama kama Mikumi na Ngorongoro lakini pia misitu ya kumwaga tu,mito mingi, mabonde ndiyo usiseme na ardhi yenye rutuba na

ya kutosha lakini bado miaka hamsini baada ya uhuru mamilioni ya watanzania bado ni masikini wa kutupwa.

Kwa mtiririko huu wa mantiki hapa ndiyo inaibuka hoja kuwa watanzania hawafanani na nchi yao hata kidogo kwa maana ni watu mafukara waliozungukwa na utajiri wa kutisha , hakika kuna utofauti mkubwa kati ya watanzania na utajiri wa taifa lao, hata ukifika pale mbuga ya Ngorongoro wanyama wanacheza na kufurahi na ndege wanarukaruka kwa furaha kubwa, nenda kandokando ya bahari ya Hindi uone mawimbi yanavyopanda na kushuka kwa furaha kisha angalia samaki walivyo na furaha kisha sasa rudi katika maisha ya walalahoi wa nchi hii, kweli inahuzunisha kuona wanyama wana furaha kushinda watanzania, inauma sana!

Kuna kisa kimoja cha kuhuzunisha sana ambacho nadhani watoto wetu wanapaswa kufundishwa madarasani. Inaelezwa kuwa mwaka jana 2010 wakati wa uchaguzi mkuu mwangalizi mmoja wa kimataifa kutoka nje alitembelea Tunduru akaona watu wanavyoogelea kwenye umasikini wa kutisha kisha akatupa macho kwa mbali akaona misitu mizuri na mto Ruvuma kisha akahoji kuwa inakuwaje watu hao ni masikini sana? Wananchi hawakuwa na la kujibu baadaye mzungu huyo akasema kuwa “siamini kabisa na hainiingii akilini kuwa CCM huwa inashinda kihalali kwa maana haiwezekani watu masikini kama hawa waichague CCM”

Hivi nani atanishawishi kuwa CCM inashinda kihalali? Hapa uhalali unaozungumzwa sio wa kura tu bali hata wa kuwaacha watu huru, kwa maana haiwezekani watu wanakuwa masikini, wanafanywa wajinga na mifumo mibovu kiasi kwamba hawajui umuhimu wa kura halafu wanajiandikisha watu milioni 19 kupiga kura lakini siku ya kupiga kura wanajitokeza milioni 5 na CCM wanashinda! Kisha uniambie hapo kuna ushindi? Ushindi gani? wakati milioni 14 nzima hawajapiga kura? Idadi hii inaweza kubadili matokeo, kwa maana nyingine yule mwangalizi wa kimataifa yupo sahihi kabisa kuwa watanzania hawaichagui CCM badala yake inajichagua yenyewe na kujipa madaraka, ajabu sana!

Watanzania wanalia kwa mengi, heri wote wangekuwa masikini lakini kuna wenzao “wajanja wachache” wanaishi kama wafalme kwa jasho la watanzania. Cha ajabu katika umasikini huu wa kutisha wa watanzania kuna baadhi ya watanzania wachache wamejigeuza “miungu watu” wamejimilikisha utajiri wote huu wakisaidiana na waporaji mabeberu kutoka Ulaya na Marekani, hawa hawajui njaa ni nini? hawafahamu masikini anafananaje? Wenyewe wanajua kuvaa suti na tai na mwisho wa mwaka wanaenda kwenye maduka makubwa ya nguo huko London na Dubai ili kuwafanyia “shopping” wake zao na watoto wao wapendwa.

Nchi imekuwa ya matabaka kiasi kwamba mpaka taifa linayumba . Leo hii imefika mahali kuna watu wana nguvu za kutisha kwenye nchi mpaka mkurugenzi wa TAKUKURU anakiri kwenye mtandao wa Wikileaks kuwa Tanzania kuna “untouchables” hawagusiki hawa. Katika mazingira haya bado CCM inahubiri usawa, usawa gani? hata mtoto mdogo hawezi kushawishika kuwa kuna hata chembe ya huo usawa kwenye nchi hii, labda kidogo CCM waje na hoja ya kuwa na nchi mbili za kimatabaka kwenye taifa moja ndiyo! Kuna Tanzania ya tabaka la juu na Tanzania ya tabaka la chini.

Huu ndiyo ukweli wa mambo , na matabaka haya mwanzo wake ni kuwa kuna wale walioshikilia utajiri wa taifa na wale waliotengwa na utajiri huo. Cha kusikitisha zaidi serikali inapigia chapuo mpasuko huu wa kitabaka kiasi kwamba imejenga shule za kata maalumu kwa masikini ili wakafeli na kuna mashule ya kimataifa yenye ubora haya ni maalumu kwa ajili ya watoto wao na maswahiba zao. Serikali haijaishia hapo tu sasa hivi Tanzania fedha iko juu ya sheria , nani asiyefahamu ukiwa na fedha nchi hii unaweza kupindisha sheria? Zaidi ya yote kuonyesha kuwa serikali yetu ni legelege ni jinsi inavyozitekeleza hospitali za serikali kiasi kwamba ni kama majengo tu bila dawa na ili kuonyesha kweli ubaguzi ni mfumo rasmi kwenye nchii hii hakuna “mkubwa” anaayekwenda kwenye hospitali za serikali huko ni kwa kapuku na walalahoi, ubaguzi wa kutisha!

Viongozi hawaishii hapo tu kwenye juhudi zao za kuwafukarisha wananchi na kuwaibia mali zao, sasa wameanzisha soko huria la kura na wapiga kura na mnada kila baada ya miaka mitano. Hivi kwanini viongozi wasiwaache huru watanzania? Kwanini wasiwaache wakajichagulia watu wanaowaamini ni viongozi bora? Huu kama sio ujambazi wa haki za masikini ni nini? yaani hao walioko madarakani mwaka jana tu walipambana kununua kura kama sio kwenye ngazi ya chama basi kwenye uchaguzi kamili lakini ndiyo hivyo ukweli ni kuwa wamenunua kura kwa pesa nyingi na sasa wapo madarakani wanashindana kupora mali za wavuja jasho.

Taifa limekosa vipaumbele , limehalalisha rushwa, uporaji na ufisadi, taifa linapepesuka kwa uhuni na tamaa za viongozi , dola imedhoofika sana hata kamanda mkuu Rais Jakaya Kikwete analifahamu hili lakini tatizo “kupe” wamejaa kuanzia huko CCM mpaka serikalini. Kile alichokitabiri Mwalimu Nyerere sasa kinatokea kweli, Mwalimu aliwahi kusema “serikali isiyojali wananchi wake haina uhalali hata kama imepigiwa kura” sitaki kuamini kuwa serikali ya CCM haina uhalali ila nashawishika kuwa haijali wala kuthamini wananchi wake hivyo kwa maana nyingine imeanza kupoteza uhalali wake.

Imefika sehemu sasa watanzania wanapaswa kufanana na utajiri wa nchi yao, viongozi inabidi wafahamu kuwa watanzania hawana sababu ya kuwa masikini kama walivyo sasa. Watanzania lazima wafanywe kujivunia utanzania wao tofauti na hivi sasa ambapo kuna watanzania wanajilaani kwa kuwa watanzania yote kwasababu ya ubabaishaji wa viongozi wao ambao badala ya kuwatumikia wananchi wao wako “busy” kutumikia matumbo yao na familia zao.

Lakini kama kawaida ya viongozi wetu wana tabia ya kuweka pamba masikioni hawataki kusikia bilashaka hata hili watapuuzia lakini nawapa angalizo kuwa watanzania wanafahamu kuwa hawakuumbwa walivyo bali umasikini wao umetengenezwa hivyo ni swala la muda tu lakini siku ikifika uvumilivu utakapowashinda basi watawang’oa wababaishaji wote wanaojineemesha na mali zao tena kwa njia yoyote ile, hizi ni zama za ukweli na uwazi ni wakati sahihi wa kuwa na mgawanyo sawa wa keki ya taifa…..Allutacontinua!

Nova Kambota Mwanaharakati,



+255717 709618

Tanzania, East Africa

07/07/2011, Alhamisi

Naomba kura yako kwenye tuzo za blog Tanzania kwenye category ya best collaboration/group blog, best informative political blog na best political blog kunipigia kura nenda http://www.tanzanianblogawards.com/


 

14 Oct 2010



Tunahitaji taasisi ya kijasusi ya uchumi na biashara?

Na Idd Amiri

Julai mosi mwaka huu soko la pamoja la Jumuiya ya Afrika Mashariki lilianza rasmi, soko hili linajumuisha nchi za Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda na Burundi. Ni soko ambalo moja ya mihimili yake ni kuruhusu bidhaa kuuzwa au kusafirishwa toka nchi moja mwanachama kwenda nyingine pasipo kutozwa kodi.

Wakati huo huo wiki iliyopita Jumuiya ya Uchumi na Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ilitimiza miaka 30 toka ianzishwe ambayo Tanzania ni Mwanachama. Malengo na Madhumuni ya Jumuiya zote mbili ni kama yanafanana ingawa kuna tofauti za hapa na pale. Wakati Tanzania inajitoa kutoka Umoja wa soko la pamoja la ushuru na forodha kwa nchi za kusini na mashariki mwa Afrika(COMESA) ilikuwa na nia ya kujiimarisha zaidi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki(EAC) kama alivyotamka wakati huo aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara Idd Simba.

Lakini mwanachama mwingine wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Kenya bado ni mwanachama wa COMESA na hata Zambia ambayo ni mwanachama wa SADC bado ni mwanachama wa COMESA vile vile. Nchi zote mbili zimeendelea kuwepo katika Jumuiya hizo kwa maslahi ya kiuchumi zaidi. Kwa Tanzania bado hatujapata kuelezwa au kuona faida za moja kwa moja ambazo kama nchi imepata kwa kuwepo katika Jumuiya ya SADC kwa kipindi chote cha Miaka 30 iliyopita ingawa wanasiasa na baadhi ya wachumi wanaendelea kuhudhuria vikao vya Jumuiya hii. SADC ilitokana na nguvu ya kisiasa ya wakati huo ya nchi zilizokuwa mstari wa mbele katika ukombozi kusini mwa Afrika.

Lengo la kuleta mada hii katika safu hii ni kujaribu kuona kama wanaohusika na sera katika Serikali ya Tanzania wamekuwa wakifanya utafiti wa kutosha kwa nia ya kujua faida halisi za kuwa katika jumuiya yoyote kabla ya kujiingiza au imekuwa ni kufuata mkumbo. Faidi kubwa ambayo kama nchi inaingia katika jumuiya yoyote siyo siasa na maneno ya kuremba, kinachotizamwa zaidi ni kuendeleza ajira kwa watu wa nchi ile na hivyo kujenga usitawi wa kiuchumi na kijamii mengine huwa ni ziada tu, kwa mfano Afrika ya Kusini kwa kuwa Mwanachama wa SADC imefanikiwa kuuza bidhaa za viwanda kwa kiasi kikubwa sana kwa nchi hizi bila mizengwe na hivyo kujenga, kulinda, kupanua na kuimarisha mfumo wa ajira katika nchi ya Afrika ya Kusini, suala hapa ni uhakika wa kuwepo kwa soko la bidhaa zake ili kuneemesha watu wake na kupunguza vurugu za kijamii ambazo huchochewa na kutokuwepo kwa ajira.

Kumekuwa na mazoea ya kufikiri kuwa kuendelea kwetu kunategemea kujiingiza katika jumuiya hizi kwani wenzetu katika nchi zao wamekuwa na ujanja wa kutoa maelezo mengi kama vile kupitia SADC au EAC kutakuwepo na maendeleo ya Sekta ya nishati, barabara, Afya na mambo chungu mbovu lakini mwishoni mwa siku tunajikuta kama umeme, maji, barabara na vinginevyo tunajitafutia wenyewe kwa sababu kila nchi inataka kupata soko kwa mwenzie na hivyo haiko tayari kusaidia kuondoa matatizo ya umeme kwa mwenzie kwani kwa kufanya hivyo itakuwa inamwendeleza kiviwanda na hatimaye itakosa mahali pa kuuza bidhaa zake. Ni jambo liliowazi kuwa kama viwanda vya Tanzania havifanyi vizuri Afrika ya Kusini itafurahi vile vile Kenya itafanya inafurahi zaidi.

Hapa lipo angalizo dogo tu, Kenya inapanua Bandari yake ya Mombasa kwa sababu bidhaa nyingi ambazo zingepitia Dar Es Salaam kwa sasa zinapitia huko hivyo basi haitaki kumwamsha aliyelala ingawa ni Mwanafrika Msahariki mwenzie!

Nikirejea katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, yapo masuala mengine kama kuruhusu watu wa nchi hizi kusafiri, kuishi katika nchi nyingine na kupata ajira pasipo vikwazo kwa kazi za aina fulani, soko la ajira lililo huru na yapo mambo mengine mengi ambayo sina shaka wananchi katika nchi hizi wanayajua kwani tunaambiwa serikali zote tano zimefanya juhudi kubwa kuwafahamisha watu wake ingawa bado nina mashaka juu ya hili.

Nia yangu katika kuzungumzia suala hili la kuwemo katika Jumuiya hizi za ushirikiano ni kujaribu kuamusha hoja ya kuwa na Economic Intelligence au taasisi ya uchunguzi wa kijasusi wa uchumi na biashara ambayo kuna wakati ilipendekezwa na Mheshimiwa mmoja ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lakini haikuuungwa mkono na Waheshimiwa wengi na hatimaye ilikufa kifo cha mende.

Najua kuwa zipo taasisi zinazofanya tafiti (Think Tank) mbalimbali katika masuala ya uchumi na biashara hapa nchini lakini bado kunahitajika uamusho wa kujua nia ya wanaoshawishi kuwepo kwa jumuiya hizi, kwa sababu Kenya ambayo ndiyo ilikuwa kinara wa kuvunjika kwa iliyokuwa Jumuiya Afrika Mashariki wakati huo ndiyo hiyo imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa Jumuiya ya sasa inafanikiwa tena kwa kasi ya ajabu na tumekwishaona kuwa yenyewe ndiyo inayofaidi sana na kuwepo kwake!

Taasisi hii ingekuwa inakusanya taarifa mbalimbali kutoka kwa nchi hizi ili kujua baadhi ya mambo ya msingi ambayo kwa kila nchi inayahitaji au ilikuwa inafikiri itapata faida ikiwa itaingia katika soko hili au lile na mengine ambayo labda kwa ujanja inayaweka kando ili kufunika kombe ili mwanaharamu apite na wakati mwafaka ukifika iyaibue. Kazi yake ingekuwa kujua nini msimamo wa kila nchi na kuwasilisha taarifa yake kwa wajumbe wetu ambao wanaingia katika vikao mbalimbali vya majadiliano kwa nia ya kulinda maslahi ya Taifa na siyo kwenda kukusanya posho za vikao na masurufu ya safari.

Wakati haya na mengine yakiendelea kuna habari kuwa kuna majadiliano yanaendelea ili watalii wanaotembelea nchi hizi washukie nchi yoyote na kwenda popote katika nchi hizi bila kufuata taratibu za kimipaka kwa Watalii.

Kenya kwa muda mrefu imekuwa ikitangaza kuwa Mlima Kilimanjaro upo nchini humo na kwa kutumia shirika lake la ndege na mawakala mbalimbali wa utalii imefanikisha hilo na wakazi wa nchi za magharibi wanaotembelea Afrika Mashariki kwa nia ya kufanya utalii wameamini hivyo na wameutumia uwanja wa ndege wa Nairobi kama njia ya kwenda kupanda na kuuona mlima Kilimanjaro. Nenda nchi yoyote barani Ulaya uone maajabu ya matangazo hayo ndipo utaposhindwa kuelewa kama kweli tuna watu katika taasisi zetu zinazoshughulika na utalii kwa nini hawabishi na wao kutoa matangazo yanasema siyo kweli kuwa Mlima Kilimanjaro uko Kenya!

Hili likikubaliwa itakuwa faida kubwa kwa Kenya ambayo miaka nenda miaka rudi imedanganya watalii wa nchi zote duniani kuwa mlima Kilimanjaro upo kwake na siyo Tanzania na hivyo imefanikiwa sana kuteka makundi ya watalii kutoka sehemu mbalimbali duniania, kwa kukubaliana na hili Kenya haitakuwa na kazi nyingine ya kuutangaza mlima Kilimanjaro kwa hadaa tena, kazi imekwisha!

Wakati Kenya inaendelea na mikakati yake hiyo kwetu tumelala usingizi fofo na hakuna anayebisha si tunahudhuria vikao ili tulipwe posho kuna ubaya ugani? Wenzetu wa Kenya huwa wanatusoma mapema kuwa tunataka nini na wao wachukue vipi kile wanachokihitaji. Wengi tunaona jinsi Jumuiya hii inavyowanufaishi wao zaidi kuliko sisi.

Kwa siku za hivi karibuni kumekuwa na kutoelewana kwa nchi mbili wanachama za Tanzania na Kenya katika suala la kuuza meno ya tembo yaliyopo katika maghala mbalimbali hapa nchini, wakati Tanzania inataka kuuza meno hayo imekuwa ikitafuta kibali kutoka katika shirika lisilo la kiserikali la Kimataifa la CITES ambalo huwa linajishulisha zaidi na kuzuia uvunaji wa wanyama au viumbe walio katika hatari ya kutoweka duniani.

Tanzania na Kenya wote ni wanachama wa Taasisi hii, Tanzania inataka kuuza meno hayo ili fedha zitakazopatikana ziweze kusaidia katika kupambana na vitendo vya ujangili vinavyoendelea katika mbuga na hifadhi zake za kitaifa. Kenya inapinga kwa kudai kuwa kwa kuuza meno hayo kutachochea vitendo vya ujangili katika mbuga zake na inaishauri Tanzania ichome kwani hata yenyewe ilifanya hivyo miaka ya nyuma na hivyo majangili watakosa upenyo wa kuendesha shughuli zao.

Hizi ni nchi mbili ndugu na marafiki ambazo zipo katika jumuiya moja, zinapingana kwa jambo moja ambalo zingekubaliana wala kusengekuwa na aibu ya ujumbe wa Tanzania kwenda kwenye mkutano wa CITES uliofanyika mwezi wa julai huko Doha, Quatar na kuangukia patupu baada ya Kenya kuendesha kampeni ya kuhakikisha kuwa Tanzania haipati kibali kutoka kwa wanachama wengine wa CITES ili iweze kuuza shehena ya meno ya tembo.

Ni kwa kuona mambo haya mawili ndipo nilipoamua kaundika makala haya ili kuwaamusha walio katika serikali wasiendelee kulala na kuamini kuwa wako na jirani na ndugu mwema wakati ukweli wa mambo hauko hivyo. Jirani yetu ni mjanja sana na anajua nyendo zetu.

Nikianza na lile la kwanza la meno ya tembo utaona kuwa Kenya ilishakuwa na msimamo wa kupinga mapema pale tu Tanzania ilipoanza kusambaza habari zake chini kwa chini kuwa inataka kuuza shehena ya meno yake ya tembo. Sababu kubwa ni kuwa Kenya inataka kulinda mbuga zake na kwa hilo hakuna ujomba wa Afrika Mashariki hapa. Swali la kujiuliza ni je, tunao watu ndani ya serikali ambao kazi yao kubwa ni kufanya ujasusi wa kiuchumi na kibiashara wa kujua nani analenga kuzuia maslahi yetu ya kiuchumi na kibishara kabla hatujayaweka wazi?

Jibu la swali hili ni kuwa hatuna watu wa aina hiyo na ndiyo sababu tumefika tulipo kwa sasa na aibu tuliyo nayo. Watu wa kazi hii wapo katika kila nchi duniani hasa ile inayolenga kulinda utaifa wake katika ajira, maliasili, teknolojia, viwanda, sayansi na katika yale mambo yote ambayo kwayo inaamini yana maslahi kwa kizazi cha sasa na kijacho. Tumekabidhi utaifa wetu ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, SADC wakati wenzetu wanaendelea kulinda maslahi yao ya kiuchumi na kibiashara kwa nia ya ustawi wa viwanda vyao na Mataifa yao.

Katika majadiliano ambayo yanaendelea kuhusu Soko la pamoja la Afrika Mashariki aliyewahi kuwa Waziri wa Utawala Bora katika Serikali ya Awamu ya tatu ya Benjamini Mkapa, Dk. Hassy Kitine alisema kuwa unapotafuta uhusiano na mtu masikini lazima ujiulize kuwa muda mwingi atataka kusaidiwa na wewe na ni hivyo hivyo Tanzania ilitakiwa kuunda jumuiya ya soko la pamoja na nchi tajiri za kiwango chake za Kongo DRC na Angola na siyo hizi za Afrika Mashariki ambazo kilaslimali zinaitegemea Tanzania.

Maneno ya Dk. Kitine yalinifanya nitafute baadhi ya watu ambao wamewahi kufika na wengine kuishi nchini Angola na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Kongo, maelezo waliyonipa yanakubaliana na DK. Kitine, ni nchi zenye utajiri wa maliasili na kama soko la bidhaa za vyakula huko ni mahali pake. Tatizo ni kuwa zote mbili hazikuwa kuiomba Tanzania kuunda umoja wa aina fulani na hivyo hivyo Watanzania tuliolala hatukuona utajiri wa wenzetu.

Majasusi wa shughuli za biashara na uchumi wanaliona hili ni halali kabisa kwani hata Biblia imeagiza hivyo pale Canaan alipokwenda kutafuta nchi ya asali na maziwa, Ipo mifano mingi lakini kwa uchache nitachukua kwa nchi za Marekani na Ufaransa ambapo Mwandishi wa Habari za Kijasusi na Ulinzi wa Gazeti la Daily Telegraph, nchini Uingereza Michael Smith katika kitabu chake The Spying Game, the secret history of British Espionage, anabainisha kuwa mnamo mwaka 1971 Ufaransa kwa kutumia taasisi yake ya kijasusi SDECE (Service de Documentation Exeterieure et de Contre-Espionage) aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi hiyo Alexandre de Marenches aliongoza shughuli za kijasusi na kufanikiwa kuujua mapema mpango wa Marekani wa kushusha thamani ya sarafu yake ya dola na kwa kufanya hivyo Wizara ya fedha ya Ufaransa ilitengeneza faidi kubwa katika soko lake la fedha.

Utafutaji wa Habari za siri kuhusu masuala ya kifedha, kiuchumi, maendeleo ya Viwanda na Sayansi na teknolojia katika Ulinzi na usalama yaliendelea kwa Ufaransa dhidi ya Marekani hata pale mwaka 1981 SDECE ilipobadili jina na kuitwa DGSE (DirectionGenerale de la Securite Exterieure) ambapo Mkurugenzi wake Mkuu wakati huo Pierre Marion alifanikiwa kupata taarifa za ushindani wa kibiashara katika mauzo ya ndege kwa India na kuipiku Marekani na Urusi wakati ambapo zote zilikuwa zikiwania biashara hiyo na baadaye kwa maneno yake mwenyewe akasema “Siyo jambo la kawaida kuwa tunafanya shughuli za kijasusi dhidi ya nchi hizi kwani kisiasa na kijeshi ni marafiki lakini katika mashindano ya kiuchumi na kiteknolojia ni washindani wetu.”

Vile vile kwa Ufaransa nayo ilipata pigo pale mwaka 1994 wakati Waziri Mkuu wa wakati huo Edouard Balladur aliposafiri kwenda Jeddah, Saudi Arabia kusaini mkataba wa dola bilioni sita ambapo Ufaransa ingeiuzia Saudia meli za kivita na makombora na pia kubadilisha ndege za abiria za shirika la ndege la nchi hiyo kutoka zile zilizotengenezwa Marekani ili kuipa bishara hiyo Airbus ambayo ni kampuni ya Ulaya ambapo Ufaransa ina hisa.

Mkataba huo haukusaniwa kwani mashirika ya kijasusi ya Marekani yakiongozwa na CIA (Central Intelligence Agency) yalipata habari za kina kuhusu mpango huo na Serikali ya Marekani ikiongozwa na Bill Clinton iliitia shinikizo serikali ya Saudia na Clinton alipimpigia simu Mfalme Fahd na mabadiliko yakafanywa ili Makampuni ya Kimarekani ya Boeing na Mcdonnell Douglas yakafanikiwa kupata mkataba huo na hatimaye kuiuzia Saudia ndege za kiraia na kijeshi.

Si hivyo tu hata katika majadiliano juu ya makubaliano ya kibiashara katika shirika la maendeleo ya bishara la kimataifa la wakati huo yaani GATT Marekani na Ufaransa kila moja ilikuwa ikitafuta siri za mwenzake ili kujua msimamo wa mwenziwe kabla ya kuhudhuria vikao vya Shirika hilo. DGSE iliwahi kuitisha mkutano wa wandishi wa habari na kuwafahamisha kuwa ilikuwa imemkamata jasusi moja kutoka CIA ambaye alikuwa akitoa hongo ya fedha kwa ofisa moja wa Ufaransa aliyekuwa akijua siri na msimamo wa nchi hiyo kuhusu mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea wakati huo.

Kwa wale wanaofuatilia habari za mataifa mbalimbali watakuwa wanajua kuwa Japan ina taasisi yake ya ujasusi wa kiuchumi na kibiashara(JETRO) toka mwaka 1958 ambayo iko chini ya Wizara ya Viwanda na Bishara ni kwa kupitia taasisi hii Japan imefanikiwa sana kuhodhi masoko ya vifaa vya electoniki na magari hadi katika masoko yenye masharti magumu na vikwazo ya Ulaya na Marekani.

Hivyo basi hata Tanzania kwa kuangalia mifano hiyo ni dhahiri kuwa ujumbe wa Tanzania uliokuwa umeongozwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Mheshimiwa Shamsa Mwangunga na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dr. Ladislaus Komba, ulitakiwa kujua mapema ni nchi ngapi na zipi zilikuwa na msimamo tofauti na Tanzania na ingetumia mikakati gani kuzima misimamo kinzani wakati wa mkutano wenyewe kwa kuendesha kampeni ya nchi kwa nchi ili kuhakikisha kuwa inasonga mbele.

Waliporejea nchini wote wawili waliitisha mkutano na waandishi wa habari, kuelezea kile kilichowasibu na wakaahidi kuwa wataendelea na mapambano ya kuhakikisha kuwa wanauza shehena hiyo ya meno ya tembo, lakini kama hawatakuwa na mkakati mbadala ya ule walioutumia itakuwa ni vigumu sana kushinda vita hiyo. Bila kufanya hivyo itakuwa mchezo wa kuvaa suti na kusafiri Business Class katika ndege kwa gharama za watanzania bila kuleta tija.


Wapiganaji husema: “Huwezi kwenda kupigana na adui usiyemjua uwezo wake.” Ni kwa kutumia watu ambao wako tayari kulinda maslahi yetu ndipo tutakuwa taifa lenye heshima mbele ya wengine. Watu hawa watakuwa watoa habari tu na watawapa wale wanaohusika katika majjadiliano ili kusoma alama za nyakati kwa upande mwingine.

Tanzania kama zilivyo nchi nyingene inapasa kutambua kuwa siyo kila utuchekeaye ana mapenzi na sisi kwani upo msemo wa kiswahili usemao hapendwi mtu ni pochi tu na pochi letu sisi ni raslimali zetu ambazo kwa wingi wake yapo mataifa mengi yanatolea macho. Watu wetu wengekaa katika ofisi za ubalozi hadi kwenye migodi ya dhahabu, almasi, tanzanite, rubi na kote kule ambako kizazi hiki na kijacho kinategemea kuvuna maliasili hizo. Kuwa na Economic Intelligence siyo kwa majirani tu hata katika mataifa yaliyoendelea ambapo watakuwepo wachambuzi wa mambo kujua nia ya dola fulani kwetu ni ipi?

Niandikie [email protected] 

ASANTE SANA MDAU IDD KWA DARASA HILI MARIDHAWA.WADAU WENGINE WENYE MADA KAMA HII AU NYINGINEZO MNAKARIBISHWA KWA MIKONO MIWILI


27 Jun 2008

Katika toleo la wiki hii la jarida la Raia Mwema nazungumzia dalili zakutimia kwa utabiri wa Mwalimu Nyerere kwamba upinzani wa kweli unaweza kutoka ndani ya CCM.Kwa namna mambo yanavyokwenda mramba ndani ya chama hicho nidhahiri kwamba kuna tofauti kubwa za kiimani na kimtazamo miongoni mwa viongozi wake.Ili kutokukunyima uhondo zaidi,bingirika na makala hiyo,pamoja na nyinginezo zilizopanda vidato,kwa KUBONYEZA HAPA

19 Jun 2008

Makala yangu katika toleo la wiki hii la gazeti la Raia Mwema inaanza kwa kuwashutumu watangazaji wa radio na runinga za Bongo ambao wanafanya mzaha kwenye shughuli muhimu.Makala inawalenga watangaza taarifa za habari ambao aidha hawajiandai vya kutosha kabla ya news bulletins kiasi cha kuchapia maneno,especially majina ya watu na sehemu,au wanaokuwa too obsessed na sauti za akina Jacob Tesha,Ahmed Kipozi,Ahmed Jongo,Abubakari Liongo,Charles Hillary,nk to an extent wanaishia kusoma madudu badala ya habari.Kuiga sauti sio uhaini lakini kwa kufanya hivyo isiwe sababu ya kusoma vitu vya ajabu.


Pia makala yangu inazungumzia suala zima la ushirikina hapa nyumbani ambapo nimejaribu kulitazama kwa upande mmoja kama mwanafunzi wa zamani wa sosholojia ya dini (sociology of religion) na kwa upande mwingine kama mwanajamii ninayeelewa nini kinanizunguka,hata kama tunaona aibu kukiongelea.Sio siri kwamba mambo ya ushirikina yameshika hatamu sana katika jamii mbalimbali za Kiafrika,lakini hii ya Fisadi Mzee wa Vijisenti kumwaga ndumba ndani ya Bunge inaonyesha jinsi gani mambo yanakwenda mrama sana katika nchi hii tuliyoahidiwa kuwa maisha bora kwa kila aliyezaliwa hapa yanawezekana.Nisikunyime uhodno,bingirika na makala hiyo pamoja na nyingine zilizokwenda shule ya kutosha KWA KUBONYEZA HAPA

14 Jun 2008

Wapendwa,naomba mniwie radhi kwa kupotea hewani kwa muda mrefu.Nilikuja nyumbani kumuuguza mama mzazi lakini kwa bahati mbaya tarehe 29/05 Bwana aliamua kumchukua na kumrejesha kwake.Makanisani wanatuambia tulitoka kwenye mavumbi na tutarejea kwenye mavumbi.Nawashukuru nyote mlioshiriana nasi kumuombea mama apone na nyote mliotoa salamu za rambiarambi ambazo kwa hakika ndio zinazotuwezesha kuwa na nguvu ya kuingia tena bloguni.
Naomba kuwapatia makala chache ambazo kutokana na matatizo niliyokuwa nayo sikuweza kuzitundika hapa.Katika makala yangu ndani ya gazeti la Raia Mwema la tarehe 28/05 nilizungumzia suala la wagombea binafsi na kutabiri kwamba huo unaweza kuwa ndio kifo cha mafisadi.Makalahiyo ilikwenda kwa kichwa WAGOMBEA BINAFSI:KIFO CHA MAFISADI CHAJA. Katika toleo lililofuatia,yaani la tarehe 04/06,nilizunguzmia kuhusu utendaji kazi wa Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Ikulu,Bwana Salva Rweyemamu.Zaidi,soma makala hiyo yenye kichwa KAULI ZA MKURUGENZI IKULU KUHUSU BALLALI MKANGANYIKO MTUPU.Makala ya wiki hii,yaani iliyotoka Jumatano ya tarehe 11/06 inazungumzia Mkutano wa Sullivan uliomalizika huko Arusha hivi karibuni.Katika makala hiyo nimejaribu kuhoji iwapo Mkutano huo umekuwa/utakuwa na faida yoyote kwa Watanzania.Makala hiyo imebeba kichwa kisemacho MKUTANO WA SULLIVAN:WAZAWA WAMENUFAIKA VIPI?

10 May 2008

Hapa nilipo,mtandao unasumbua sana.Kwahiyo,nawaomba mniruhusu niwape tu LINK HII ya makala yangu katika toleo la wiki hii la gazeti la Raia Mwema.

3 May 2008

Sina budi kuwataka radhi wasomaji wapendwa kwa kutoweka chochote hapa kwa zaidi ya wiki sasa.Napenda sana ku-update blog hii lakini wakati mwingine mazingira ya hapa yanakuwa kikwazo.Hata hivyo,nadhani mtaburudika na makala yangu katika gazeti la Raia Mwema toleo la wiki inayoisha leo.Makala hiyo ni reaction dhidi ya wababaishaji flani ambao wanajaribu kuhoji usafi wa akina-sie tulioamua "liwalo na liwe" dhidi ya mafisadi.In fact sio kama wanahoji as such,wanachofanya ni kuwa servants wa mafisadi,nisicho na uhakika ni whether wanafanya hivyo kutokana na njaa zao au mfilisiko wa mawazo.Anyway,makala nzima inapatikana kwa kubonyeza hapa

16 Apr 2008

Katika makala yangu ndani ya toleo la wiki hii la gazeti la Raia Mwema,nazungumzia suala zima la huduma bora.Makala inaanza kwa kuondoa fikra za "u-tambarare" wa maisha ya ughaibuni,zinazochochewa na taswira za runinga na magazeti ya kimataifa.Ni rahisi baadhi ya wenzetu walioko nyumbani kuhisi kwamba mambo huko "majuu" ni asali na maziwa (land of honey and milk).Kilicho sahihi zaidi kuhusu maisha ya sehemu nyingi za dunia ya kwanza ni huduma inayoendana na matarajio ya mteja.Yaani mteja sio tu mfalme au malkia,bali sehemu ya familia ya watoa huduma (of course kuna exceptions...na kwa UK,tuna wahuni kama British Telecoms-BT,na wababaishaji wengine lakini ni wachache).Maudhui ya makala ni hiyo kwenye title ya post hii:TANZANIA YENYE HUDUMA BORA INAWEZEKANA.Pamoja na habari na makala nyingine za daraja la juu kabisa,binjuka na makala hiyo kwa KUBONYEZA HAPA.

10 Apr 2008

Huduma za afya hapa nyumbani ni duni na hazileti matumaini ya Maisha Bora kwa Kila Mtanzania (by the way,tangu nifike hapa sijaona ile hamasa niliyoikuta 2005 kuhusiana na kauli-mbiu hiyo.Sijui imekufa kifo cha asili au imepotea kama Gavana Daudi Ballali!).Hospitali za umma zinaweza kujitetea kuhusu huduma zao mbovu,na utetezi unaweza kuwa ule uliozoeleka:serikali haitengi fungu la kutosha kwenye sekta ya afya,mishahara ya watumishi ni midogo,na mlolongo wa sababu ambapo mlengwa mkuu ni serikali.Lakini haitarajiwi hospitali binafsi,ambazo gharama zake ni za juu sana,zitoe huduma ya chini ya kiwango.Nimeelezea kwa kirefu kuhusu suala hilo katika makala yangu ndani ya toleo la wiki hii la gazeti la Raia Mwema.Pamoja na makala nyingine na habari motomoto,bingirika na vyote hivyo kwa KUBONYEZA HAPA

11 Mar 2008

MAKALA HII YANGU ILITOKA KATIKA GAZETI LA MTANZANIA TAREHE 07 MACHI 2008

Unafiki wa viongozi wetu wa dini

na evarist chahali, uskochi

MADA yangu ya leo, najua dhahiri itawakera wateule wachache wa aina fulani. Lakini kabla ya kuwapasha, naomba nizungumzie suala la imani na dini hapa ninapoishi Ughaibuni.

Nilipofika hapa kwa mara ya kwanza, nilionyeshwa majengo kadhaa ambayo huko nyuma yalikuwa Makanisa, lakini sasa yamegeuzwa kuwa kumbi za disko na klabu za usiku.

Na hao walioyageuza Makanisa hayo kuwa sehemu za starehe, wala hawakujishughulisha kabisa katika kubadili mwonekano wake, bali wameyaacha yatoe ushuhuda kuwa huko nyuma yalikuwa sehemu za ibada.

Nilipofanya udadisi kwa wenyeji, niliambiwa kwamba makanisa hayo yaliuzwa baada ya kuwa matupu kutokana na ukosefu wa waumini. Wengi wa waumini wa makanisa ya mji huu ninaoishi, ni ama wahamiaji waliotoka nje ya nchi hii kama mimi, na au vikongwe vya hapa hapa.

Binafsi, sina majibu ya moja kwa moja kwamba tatizo la hawa wenzetu ni nini. Hata hivyo, ninachofahamu ni kwamba kuna watu kadhaa ambao wanajitambulisha kuwa hawana dini, na au hawaamini kuwapo kwa Mungu.

Imani ni suala la mtu binafsi, na hivyo pengine si mwafaka kuhoji kwa nini fulani anaamini, ama haamini kuwapo au kutokuwapo kwa Mungu.Ingawa binafsi, ni muumini kwa aina fulani, huwa sisiti kuwasifu wale wasiowaumini wa dini yoyote, lakini wasioona aibu kuelezea msimamo wao wa kidini. Kwa lugha nyingine, watu hao si wanafiki. Wanaeleza bayana kile wanachokiamini na kutokiamini.

Kuna tatizo la msingi huko nyumbani, ingawa natambua dhahiri kwamba watu wengi hawapendi kujadili mambo ya dini kwa sababu ile ile ya unafiki!

Baadhi ya viongozi wetu wa dini, wamekuwa mstari wa mbele kukemea wale ambao wanakwenda kinyume na imani zao, lakini viongozi hao hao wakishiriki kwenye maovu wanayoyakemea.

Ndiyo, tunatambua kwamba mara nyingi viongozi wetu wa dini wana wafadhili wao nje ya nchi. Lakini hicho si kigezo cha wao kuishi maisha tofauti kabisa na wafuasi wao.

Utakuta katika kijiji fulani ambacho kimegubikwa kabisa na umasikini, kiongozi fulani wa dini yeye akiishi kama yuko peponi. Na bila huruma, huyo huyo anayeishi maisha kama ya peponi katikati ya waumini masikini, kwa kutumia kisingizio cha maandiko matakatifu, anawashurutisha waumini wake kujipigapiga ili kuongeza sadaka wanazotoa.

Kinachokera zaidi, ni hili suala la baadhi ya viongozi wa madhehebu fulani kuwa na watoto mitaani, huku sheria za madhehebu yao zikiwa haziwaruhusu kufanya hivyo.

Tatizo hili ni sugu sana, hususan maeneo ya vijijini. Kinachosikitisha ni ukweli kwamba waumini wanafahamu kwamba kiongozi wao wa dini, anaishi kinyume na maadili ya huduma yake, lakini hawachukui hatua yoyote zaidi ya kulalamika chini chini.

Binafsi, ninayo mifano hai ya baadhi ya viongozi wa madhehebu yangu ambao wana watoto lukuki mitaani. Baadhi yao wanatoa huduma kwa wazazi wa watoto wao hao, lakini wengine wamewatelekeza kabisa.

Hawa watu ni wanafiki ambao hawastahili kuachwa waendeleze uhuni kwa kisingizio kwamba daraja walilofikia, haliwezi kutenguliwa.

Mitume wetu waliishi maisha ya uadilifu, ambayo yalishabihiana kwa asilimia 100 na kile walichokuwa wakikihubiri. Na si katika suala la uzinzi pekee, bali hata kwenye dili za kibiashara.Majanga kama ya ukimwi yataondoka vipi iwapo baadhi ya wale wanaopaswa kukemea vitendo vya ngono, kwa vile vinavunja amri ya Mungu, nao ni washirika wa vitendo hivyo?

Pamoja na mapungufu waliyonayo baadhi ya viongozi wa dini, hivi karibuni tumeshuhudia wengi wakijitokeza kuungana na Watanzania wenzao kukemea masuala yanayohatarisha umoja wa kitaifa.

Suala ambalo baadhi ya viongozi hao wa dini wanastahili pongezi, ni katika kukemea vitendo vya kifisadi, ingawa tatizo linakuwapo, pale msimamo huo unapokuwa wa kiongozi mmoja zaidi, badala ya kuwa msimamo wa taasisi ya dini.

Katika hili, napenda nichukue fursa hii kumpongeza Askofu Mkuu mpya wa Kanisa la Anglikana Tanzania, ambaye ameweka bayana msimamo wake dhidi ya vitendo vya kifisadi. Hiyo inatia moyo sana!

Licha ya kukemea ufisadi na maovu mengine katika jamii, asasi za dini zinaweza kubadili tabia za waumini wao kwa kuwawekea vikwazo vya aina fulani. Taratibu za aina hiyo, zipo katika baadhi ya imani, kwa mfano, Wakatoliki, ambao muumini akikiuka kanuni fulani, anazuiwa kushiriki baadhi ya sakramenti.

Kwa nini basi tunaendelea kujumuika na mafisadi makanisani, na au misikitini ilhali matendo yao yanalenga kutuumiza kimaisha? Nafahamu kuwa dini zote zinahimiza upendo, lakini hiyo si sababu ya kutowabana wale wasio na upendo kwa Watanzania wenzao.

Inawezekana kwamba kikwazo kikubwa kwa dini zetu kuwa mstari wa mbele katika kukemea maovu na kubadili tabia za wanaokwenda kinyume na maadili ya kimwili na kiroho, ni hofu ya usafi wa baadhi ya viongozi wa dini hizo, kama nilivyoeleza mwanzoni mwa makala haya.Tatizo hilo linaweza kupatiwa ufumbuzi iwapo viongozi wa madhehebu wataepuka mtindo wa kulindana, na hivyo kuchukua hatua kali kwa walio chini yao, ambao wanakwenda kinyume cha kanuni na taratibu za madhehebu.

Ni wazi kwamba viongozi waadilifu wa dini, hawawezi kuogopa kumnyooshea kidole fisadi fulani, kwa kuwa hata kama fisadi huyo atataka kulipa kisasi, atajikuta hana jambo lolote analoweza kulitumia kushusha heshima ya kiongozi wa dini aliyemkemea.

Busara za Kiswahili zinatueleza kwamba kujikwaa si kuanguka, na hata kuanguka si mwisho wa safari. Wito wangu kwa viongozi wetu wa dini, ni kuongeza jitihada za kuwahudumia waumini wao kiroho na kimwili.

Ni muhimu kwa viongozi hao kuishi kama Mitume ambao mafundisho yao yalikubalika na kuvuta watu wengi, kwa vile wao wenyewe walikuwa waadilifu na mifano bora ya kuigwa na wanadamu.




20 Feb 2008

Makala yangu katika toleo la wiki hii la gazeti la Raia Mwema inazungumzia UHURU.Inaanza kwa kuhabarisha kuhusu tangazo la Uhuru wa Kosovo,kisha inachambua "urafiki mpya" wa Marekani na China kwa Bara la Afrika na kuhitimisha kwamba urafiki huo ni mithili ya Mkutano wa Berlin 1884-5 ulioligawa bara la Afrika miongoni mwa wakoloni.Makala hii inakumbushia pia kwamba kuna uwezekano ziara ya Bush barani Afrika ikabaki kumbukumbu muhimu kwake kutokana na namna alivyonyenyekewa katika kipindi ambacho ni mmoja ya marais wanaochukiwa sana katika sehemu mbalimbali duniani,na very unpopular nyumbani kwake US of A.Kadhalika makala inawashikia bango Mwanyika na Hosea kwamba wajiuzulu haraka sana,sambamba na wale wote waliotajwa kwenye ripoti ya Tume ya Mwakyembe.Pamoja na makala nyingine zilizokwenda shule ya hali ya juu,bingirika na makala hiyo kwa KUBONYEZA HAPA.

19 Dec 2007

Wiki hii nazungumzia unafiki wa baadhi ya wanasiasa wetu wakongwe waliokuwa karibu na Mwalimu Nyerere.Mwalimu aliwaamini,nasi pia tuliwaamini.Walikuwa wakiongea "lugha" ya Mwalimu:ujenzi wa jamii sawa isiyo na matabaka,inayothamini utu wa binadamu na yenye kumpa Mtanzania matumaini katika ardhi aliyozaliwa.

Lakini wakongwe hawa wa siasa waligeuka kama vinyonga mara tu baada ya Mwalimu kung'atuka,lakini their true colours zimejidhihirisha zaidi baada ya kifo cha Baba wa Taifa.Unaweza kujiuliza:walikuwa wapi akina Kingunge wakati linapitisha Azimio la Zanzibar (lililoua Azimio la Arusha)?Au kwa hivi karibuni,wako wapi maswahiba wa Mwalimu wakati tunashuhudia taifa letu likimung'unywa na mafisadi kwa "madili-kichaa" kama ya IPTL,Richmond,Buzwagi,nk?

Katika makala hiyo nimejaribu kutoa mfano hai wa maisha yangu udogoni kuonyesha namna nilivyokwepa kuwa mnafiki,lakini nisikumalizie uhondo.Bingirika na makala hiyo HAPA na ufaidike pia na makala nyingine zilizokwenda shule ndani ya Gazeti la RAIA MWEMA.




28 Nov 2007

KILA MUDA UNAPORUHUSU,NAPENDELEA KUTEMBELEA KIJI-LIBRARY CHANGU CHA DVDs






COLLECTION INAKUA,200+ DVDs SI HABA.


KUSOMA NOVELS ZA SYDNEY SHELDON na JOHN GRISHAM NI MITHILI YA KUANGALIA DVDs



POLISHING LANGUAGE SKILLS AND EMPOWERING MYSELF SPIRITUALLY







KAULIMBIU YA KUHAMASISHA ZOEZI LA KUPIMA UKIMWI KWA HIARI ILIKUWA "TANZANIA BILA UKIMWI INAWEZEKANA".TAFADHALI UNGANA NAMI KWENYE "TAKE" YANGU KUHUSU UWEZEKANO HUO,KATIKA MAKALA YANGU YA WIKI HII NDANI YA GAZETI LA RAIA MWEMA






---------------------------------------------------------------------------------------------------------------
CHECK OUT THIS CLIP.DEFINITELY,A LOW-BUDGET VIDEO BUT I LIKE THE VIBE,DO YOU?



Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.