Showing posts with label MTANZANIA. Show all posts
Showing posts with label MTANZANIA. Show all posts

11 Mar 2008

MAKALA HII YANGU ILITOKA KATIKA GAZETI LA MTANZANIA TAREHE 07 MACHI 2008

Unafiki wa viongozi wetu wa dini

na evarist chahali, uskochi

MADA yangu ya leo, najua dhahiri itawakera wateule wachache wa aina fulani. Lakini kabla ya kuwapasha, naomba nizungumzie suala la imani na dini hapa ninapoishi Ughaibuni.

Nilipofika hapa kwa mara ya kwanza, nilionyeshwa majengo kadhaa ambayo huko nyuma yalikuwa Makanisa, lakini sasa yamegeuzwa kuwa kumbi za disko na klabu za usiku.

Na hao walioyageuza Makanisa hayo kuwa sehemu za starehe, wala hawakujishughulisha kabisa katika kubadili mwonekano wake, bali wameyaacha yatoe ushuhuda kuwa huko nyuma yalikuwa sehemu za ibada.

Nilipofanya udadisi kwa wenyeji, niliambiwa kwamba makanisa hayo yaliuzwa baada ya kuwa matupu kutokana na ukosefu wa waumini. Wengi wa waumini wa makanisa ya mji huu ninaoishi, ni ama wahamiaji waliotoka nje ya nchi hii kama mimi, na au vikongwe vya hapa hapa.

Binafsi, sina majibu ya moja kwa moja kwamba tatizo la hawa wenzetu ni nini. Hata hivyo, ninachofahamu ni kwamba kuna watu kadhaa ambao wanajitambulisha kuwa hawana dini, na au hawaamini kuwapo kwa Mungu.

Imani ni suala la mtu binafsi, na hivyo pengine si mwafaka kuhoji kwa nini fulani anaamini, ama haamini kuwapo au kutokuwapo kwa Mungu.Ingawa binafsi, ni muumini kwa aina fulani, huwa sisiti kuwasifu wale wasiowaumini wa dini yoyote, lakini wasioona aibu kuelezea msimamo wao wa kidini. Kwa lugha nyingine, watu hao si wanafiki. Wanaeleza bayana kile wanachokiamini na kutokiamini.

Kuna tatizo la msingi huko nyumbani, ingawa natambua dhahiri kwamba watu wengi hawapendi kujadili mambo ya dini kwa sababu ile ile ya unafiki!

Baadhi ya viongozi wetu wa dini, wamekuwa mstari wa mbele kukemea wale ambao wanakwenda kinyume na imani zao, lakini viongozi hao hao wakishiriki kwenye maovu wanayoyakemea.

Ndiyo, tunatambua kwamba mara nyingi viongozi wetu wa dini wana wafadhili wao nje ya nchi. Lakini hicho si kigezo cha wao kuishi maisha tofauti kabisa na wafuasi wao.

Utakuta katika kijiji fulani ambacho kimegubikwa kabisa na umasikini, kiongozi fulani wa dini yeye akiishi kama yuko peponi. Na bila huruma, huyo huyo anayeishi maisha kama ya peponi katikati ya waumini masikini, kwa kutumia kisingizio cha maandiko matakatifu, anawashurutisha waumini wake kujipigapiga ili kuongeza sadaka wanazotoa.

Kinachokera zaidi, ni hili suala la baadhi ya viongozi wa madhehebu fulani kuwa na watoto mitaani, huku sheria za madhehebu yao zikiwa haziwaruhusu kufanya hivyo.

Tatizo hili ni sugu sana, hususan maeneo ya vijijini. Kinachosikitisha ni ukweli kwamba waumini wanafahamu kwamba kiongozi wao wa dini, anaishi kinyume na maadili ya huduma yake, lakini hawachukui hatua yoyote zaidi ya kulalamika chini chini.

Binafsi, ninayo mifano hai ya baadhi ya viongozi wa madhehebu yangu ambao wana watoto lukuki mitaani. Baadhi yao wanatoa huduma kwa wazazi wa watoto wao hao, lakini wengine wamewatelekeza kabisa.

Hawa watu ni wanafiki ambao hawastahili kuachwa waendeleze uhuni kwa kisingizio kwamba daraja walilofikia, haliwezi kutenguliwa.

Mitume wetu waliishi maisha ya uadilifu, ambayo yalishabihiana kwa asilimia 100 na kile walichokuwa wakikihubiri. Na si katika suala la uzinzi pekee, bali hata kwenye dili za kibiashara.Majanga kama ya ukimwi yataondoka vipi iwapo baadhi ya wale wanaopaswa kukemea vitendo vya ngono, kwa vile vinavunja amri ya Mungu, nao ni washirika wa vitendo hivyo?

Pamoja na mapungufu waliyonayo baadhi ya viongozi wa dini, hivi karibuni tumeshuhudia wengi wakijitokeza kuungana na Watanzania wenzao kukemea masuala yanayohatarisha umoja wa kitaifa.

Suala ambalo baadhi ya viongozi hao wa dini wanastahili pongezi, ni katika kukemea vitendo vya kifisadi, ingawa tatizo linakuwapo, pale msimamo huo unapokuwa wa kiongozi mmoja zaidi, badala ya kuwa msimamo wa taasisi ya dini.

Katika hili, napenda nichukue fursa hii kumpongeza Askofu Mkuu mpya wa Kanisa la Anglikana Tanzania, ambaye ameweka bayana msimamo wake dhidi ya vitendo vya kifisadi. Hiyo inatia moyo sana!

Licha ya kukemea ufisadi na maovu mengine katika jamii, asasi za dini zinaweza kubadili tabia za waumini wao kwa kuwawekea vikwazo vya aina fulani. Taratibu za aina hiyo, zipo katika baadhi ya imani, kwa mfano, Wakatoliki, ambao muumini akikiuka kanuni fulani, anazuiwa kushiriki baadhi ya sakramenti.

Kwa nini basi tunaendelea kujumuika na mafisadi makanisani, na au misikitini ilhali matendo yao yanalenga kutuumiza kimaisha? Nafahamu kuwa dini zote zinahimiza upendo, lakini hiyo si sababu ya kutowabana wale wasio na upendo kwa Watanzania wenzao.

Inawezekana kwamba kikwazo kikubwa kwa dini zetu kuwa mstari wa mbele katika kukemea maovu na kubadili tabia za wanaokwenda kinyume na maadili ya kimwili na kiroho, ni hofu ya usafi wa baadhi ya viongozi wa dini hizo, kama nilivyoeleza mwanzoni mwa makala haya.Tatizo hilo linaweza kupatiwa ufumbuzi iwapo viongozi wa madhehebu wataepuka mtindo wa kulindana, na hivyo kuchukua hatua kali kwa walio chini yao, ambao wanakwenda kinyume cha kanuni na taratibu za madhehebu.

Ni wazi kwamba viongozi waadilifu wa dini, hawawezi kuogopa kumnyooshea kidole fisadi fulani, kwa kuwa hata kama fisadi huyo atataka kulipa kisasi, atajikuta hana jambo lolote analoweza kulitumia kushusha heshima ya kiongozi wa dini aliyemkemea.

Busara za Kiswahili zinatueleza kwamba kujikwaa si kuanguka, na hata kuanguka si mwisho wa safari. Wito wangu kwa viongozi wetu wa dini, ni kuongeza jitihada za kuwahudumia waumini wao kiroho na kimwili.

Ni muhimu kwa viongozi hao kuishi kama Mitume ambao mafundisho yao yalikubalika na kuvuta watu wengi, kwa vile wao wenyewe walikuwa waadilifu na mifano bora ya kuigwa na wanadamu.




2 Mar 2008

MTANZANIA UGHAIBUNI

Sakata la mkataba wa Kampuni ya Richmond linaelekea kuchukua mwelekeo mpya kila kukicha. Ni rahisi kutafsiri kwamba suala hili lisipopatiwa ufumbuzi wa kudumu linaweza kuwa na madhara makubwa kwa nchi na kwa chama tawala, CCM.

Tangu ripoti ya “Tume ya Mwakyembe” ilipowekwa hadharani katika kikao kilichopita cha Bunge la Jamhuri ya Muungano, kumejitokeza kauli kadhaa za utatanishi ambazo japo zinaweza kuwa ni za kawaida tu, tafsiri ya ndani inaashiria matatizo makubwa huko tuendako.

Naomba niwe muwazi zaidi katika makala hii, na ningependa kutamka bayana kwamba sina nia ya kumshushia heshima yeyote nitakayemtaja. Lengo kuu la makala hii ni kuikumbusha kila pande inayoguswa na sakata hilo kutambua kwamba taifa letu ni muhimu zaidi kuliko maslahi ya mtu mmoja.

Naikumbuka sana siku taifa lilipotangaziwa kifo cha Baba wa Taifa.Watanzania wengi walitokwa na machozi sio tu kwa vile hawangemwona tena Mwalimu bali pia ni ile hali ya kutokuwa na uhakika taifa letu lingekuwaje bila Nyerere.Naamini kwamba laiti Mwalimu angekuwepo, baadhi ya upuuzi kama huo wa mkataba wa Richmond wala usingetokea, lakini ndio hivyo tena, hatuko naye duniani.

Wanaoilaumu “Tume ya Mwakyembe” kuwa imewaonea wanasahau kwamba tume hiyo haikuundwa baada ya Mwakyembe na wenzake kutuma maombi ya kuwa kwenye tume hiyo.Inashangaza wanaolalamika sasa kwamba ripoti ya tume hiyo ilikuwa na ajenda za kumalizana kisiasa,ilhali hawakuipinga wakati inaundwa na pale ilipokuwa ikitimiza majukumu yake.Ina maana ajenda hizo za kisiasa zilianza baada ya akina Mwakyembe kuwa wajumbe wa tume au zilikuwapo kabla.Kama zilikuwapo kabla,kwanini basi waliotajwa kuhusika na kuliingiza taifa katika hasara kubwa kwa mkataba huo wa kizembe hawakulalamika?

Na iwapo ajenda hizo zilianza baada baada ya wajumbe hao kuingia kwenye tume,kwanini basi watajwa walikimbilia kujiuzulu (huku wengine wakigoma waziwazi kujiuzulu kwa kuendelea kung’ang’ania madaraka) badala ya kudai haki itendeke?Ni rahisi kuhitimisha kuwa kelele zinazoendelea hivi sasa ni za mfa maji.

Nakumbuka kwenye miaka ya tisini nilipokuwa mwanafunzi wa sekondari ya wavulana ya Tabora (Tabora Boys) tulibahatika kutembelewa na Komandoo Salmin Amour.Nayakumbuka baadhi ya maneno yake ambayo kimsingi yalikuwa na lengo la kutupa changamoto ya mafanikio ya kielimu na hatimaye kufanikiwa maishani (japo sio kila mara kufanikiwa kielimu ni tiketi ya moja kwa moja ya kufanikiwa kimaisha).Alitueleza kwamba madaraka ni mazuri na kutupa mifano ya namna yeye kama rais alivyokuwa na wasaidizi kibao wa kuhakikisha kila kitu kinakwenda vema.

Nilikubaliana na Komando wakati huo,na nakubaliana nae sasa,kwamba madaraka ni mazuri na matamu,na ndio maana tunashuhudia hizi kelele zinazoendelea kutoka kwa waliokumbwa na zahma ya kisiasa baada ya skandali ya mkataba wa kampeni ya Richmond.Hakuna dhambi kwa madaraka kuwa matamu kwani hata njia ya kuyafikia sio nyepesi.Inahitaji jitihada na juhudi za kutosha kufikia hatua ya kuongoza watu wenye akili timamu.Na inatarajiwa kwamba mtu akishapata bahati ya kuwa kiongozi atatambua kwamba wengi,kama sio wote,wa aliokuwa akiwaongoza ni watu wenye akili timamu,uwezo wa kufanya maamuzi na wanaostahili heshima.

Waziri Mkuu aliyepita,Edward Lowassa,ameendelea kuonyesha kwamba japo aliamua kubwaga manyanga kwa hiari yake,alifanya hivyo huku roho ikimuuma.Nasema hivyo kwa sababu kauli zake za hivi karibuni zinaashiria wazi kwamba bado ana kinyongo kikubwa na matokeo ya uchunguzi wa “Tume ya Mwakyembe.”

Lowassa anaamini kwamba atarejea tena kwenye ulingo wa juu wa kisiasa kama Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi ambaye alipokuwa Waziri alilazimika kujiuzulu kutokana na skandali iliyoikumba Wizara yake.Tofauti ya msingi kati ya Mwinyi na Lowassa ni ukweli kwamba wakati Mwinyi alijiuzulu kutokana na tukio lililotokea mbali kabisa na mahala alipokuwa akifanyia kazi (lilitokea Shinyanga wakati ofisi ya Mwinyi ilikuwa Dar es Salaam),Lowassa alijikuta akikumbwa na shutuma kuhusu mkataba huo kwa vile katika hatua flani ulipita machoni mwake na akaamua “kusikiliza maamuzi ya wataalamu.”

Uongozi ni pamoja na kuwa na maamuzi ya haraka na yanayoangalia athari zinazoweza kujitokeza mbeleni iwapo yatafanyika maamuzi potofu.Haiyumkiniki kwamba Waziri Mkuu mzima anaweza kusikiliza ushauri mbovu na kuafikiana nao pasipo kujiridhisha iwapo ushauri huo ni wa manufaa kwa taifa.Hilo pekee linamvua sifa ya uongozi mtu yeyote aliye katika nafasi ya juu kitaifa.

Hivi kama mkataba wa Richmond ungekuwa na madhara ya moja kwa moja kwa familia ya Lowassa,kiongozi huyo angeendelea kusikiliza ushauri asio na uhakika na matokeo yake au angetaka kujiridhisha kwamba kilichokuwa kikifanyika hakingekuwa na madhara kwa familia yake?

Tukimweka kando Lowassa kwa muda,tumeshuhudia vituko vingine kutoka kwa Mkurugenzi wa TIC Emmanuel Ole Naiko ambaye anadai kuna dalili za “mauaji ya halaiki” dhidi ya watu wenye asili ya wilaya ya Monduli.Hizi ni hoja mufilisi ambazo kama zitaachwa bila kudhibitiwa zinaweza kuliingiza taifa kwenye matatizo yasiyo na msingi.


Hivi Ole Naiko amefanya utafiti wa kutosha kiasi gani kuthibitisha kwamba kuna mpango wa “ethnic cleansing” dhidi ya watu wa Monduli?Kwa hakika serikali inapswa kumhoji kwa undani mtu huyu mwenye heshima kubwa ndani na nje ya nchi kutokana na matamshi hayo ambayo yanaweza kabisa kuathiri hata utendaji wa ofisi yake (hakuna mwekezaji aliye tayari kuwekeza kwenye nchi inayoelekea kwenye “ethnic cleansing.”)

Kuna tetesi kwamba upo mkakati mkubwa wa “kujibu mashambulizi” dhidi ya ripoti ya “Tume ya Mwakyembe.” CCM imekuwa ikituaminisha kila siku kwamba vikao nje ya chama ni majungu,sasa basi inapaswa kuhakikisha kwamba wote wenye kudhani hawakutendewa haki wawasilishe malalamiko yao kwa ngazi hsuika katika chama hicho au hata bungeni.

Kama taarifa tunazozisoma katika vyanzo mbalimbali kwamba kuna mgawanyiko mkubwa ndani ya CCM kutokana na skandali la Richmond zina ukweli, basi ni muhimu kwa uongozi wa juu wa chama hicho kuachana na itifaki zake za kawaida za kuwasifia hata wanaostahili kukemewa na badala yake kuwawekwa “kiti moto” waeleze malalamiko yao mbele ya vikao halali badala ya kuendeleza mbinu za chini chini ambazo zinaweza kabisa kuathiri hali ya usalama wa nchi yetu.

Tusirejee makosa yaliyojitokeza katika mkataba wa Richmond ambapo baadhi ya watu walitahadharisha mapema kuhusu uhalali wa kampuni hiyo lakini wakapuuzwa.Kuna watu wanataka urais kwa kutimia njia yoyote ile hata kama kwa kufanya hivyo wanahatarisha uhai wa chama.

Lakini wakati tunawalaumu wanaolalamika kwamba wameonewa na “Tume ya Mwakyembe” tunapaswa pia kujiuliza kama hawapati jeuri hiyo kutokana na uzembe unaendelea wa kutowachukulia hatua wahusika.Pengine jeuri waliyonayo inatokana na ukweli kwamba wanaamini kuwa hakuna mwenye jeuri ya kuwachukulia hatua hasa ikizingatiwa kuwa baadhi yao wameishia kupongezwa kwa “ushujaa wao” badala ya kushutumiwa kwa hasara waliyoisababisha kwa taifa.

Nadhani anachopaswa kufanya Lowassa,Ole Naiko na wengine wote waliohusishwa na mkataba wa Richmond ni kutafuta msaada wa kisheria kuona haki inatendeka upande wao iwapo wanaamini kuwa hawakutendewa haki,badala ya kuendeleza hizi porojo ambazo kwa hakika zinaweza kuua kabisa ndoto zao za kurejea kwenye ulingo wa juu wa siasa za nchi yetu.Mahakama zipo,vikao vya chama vipo,sasa kwanini kelele za kuonewa zisipelekwe huko?TANZANIA NI MUHIMU ZAIDI KULIKO MASLAHI YA MTU BINAFSI.

BAADA YA KUMALIZA KUSOMA MAKALA HII,UNAWEZA KUANGALIA VITUKO VYA SIASA ZA URUSI AMBAVYO VIMEZAA TERM MPYA YA NANO PRESIDENT (as in iPod Nano).BONYEZA HAPA

HALAFU KWA WALE AKINA DADA "WENYE ULIMI MZITO",CLIP IFUATAYO INAWEZA KUWA YA MSAADA WA INA FLANI



1 Feb 2008

Makala yangu hii ilitoka katika toleo la jana la gazeti la Mtanzania

Miongoni mwa adha za kumiliki runinga hapa Uingereza ni kuilipia ada ya leseni (TV Licence Fee).Ada hiyo kwa kiasi kikubwa hutumika kuendesha BBC ambalo ni shirika la utangazaji la nchi hii.Wananchi wengi wamekuwa wakilalamika kwamba baadhi ya vipindi vya BBC havina ladha inayoweza kuhalalisha shirika hilo kuendelea kupewa ruzuku inayotokana na ada ya leseni za runinga.Hata hivyo,BBC imeendelea kuwa shirika la habari maarufu na lenye mtandao mkubwa sio tu ndani ya Uingereza bali duniani kwa ujumla.Na miongoni mwa vipindi maarufu vya shirika hilo la habari ni Newsnight,kipindi kinachoonyeshwa siku za wiki kuanzia saa 4.30 usiku.

Kipindi hicho huchambua habari muhimu zilizojitokeza katika siku husika ndani na nje ya nchi hii.Hivi karibuni,Newsnight ilizungumzia machafuko yanayoendelea nchini Kenya.Kwa hakika ilikuwa inatia uchungu kuona namna watu wanavyotaabika nchini humo.Moja kati ya mambo yaliyolinisikitisha zaidi ni mahojiano mafupi kati ya mtangazaji wa BBC aliyeko nchini Kenya na mwanamama mmoja ambaye wakati wa mahojiano hayo alikuwa kamanda wa polisi wa eneo flani (jina la afande huyo na mahala alipokuwa anaongoza vimenitoka kidogo).

Kamanda huyo alianza mahojiano hayo kwa kukanusha madai kwamba jeshi la polisi la Kenya limekuwa likiuwa raia wasio na hatia katika kutekeleza sera ya “piga risasi kuua” (shoot-to-kill policy).Alidai kuwa wanachofanya wanausalama ni kudhibiti machafuko na uhalifu.Mwishoni mwa mahojiano,afande huyo alieleza uchungu alionao kuona nchi yake ikiteketea.Alisema kwamba ameshatembelea sehemu nyingi duniani na kuona watu wa nchi hizo wakiwa na fahari na nchi zao,jambo ambalo lilimwongezea mapenzi kwa nchi yake.Aliwalaumu wanasiasa wa Kenya kwa kuzorotesha jitihada za kuleta amani.

Cha kusikitisha ni kwamba kamanda huyo aliyeonekana kuguswa sana na madhila yanayowakumba Wakenya wenzie aliondolewa kwenye usimamizi wa operesheni za mitaani na kukabidhiwa majukumu ya kiofisi (desk job).Yaani aliadhibiwa kwa kusema ukweli wa moyoni mwake kuhusu namna wanasiasa wanavyoendekeza maslahi yao kuliko ya nchi na wananchi.Naamini mwanamama huyo ni mmoja tu kati ya askari wengi ambao wanalazimika kupiga na hata kuua Wakenya wenzao katika kutekeleza amri “halali” za serikali.

Ilielezwa katika kipindi hicho cha Newsnight kwamba licha ya matokeo ya uchaguzi mkuu wa rais na wabunge mwezi Desemba mwaka jana kuwa chanzo kikuu cha machafuko hayo yasiyoonyesha dalili ya kupungua,msingi wa matatizo ulijengwa miaka kadhaa iliyopita.Kwa mujibu wa uchambuzi wa wajuzi wa siasa za Kenya,kwa muda mrefu kumekuwa na manung’uniko miongoni mwa baadhi ya makabila kuhusu umiliki wa njia za uchumi ambapo inadaiwa Wakikuyu wamekuwa na upendeleo zaidi.

Tofauti za kikabila na kidini ni miongoni mwa vyanzo vikubwa vya machafuko sehemu mbalimbali duniani hususan barani Afrika.Lakini tofauti hizo hustawi vizuri zaidi mahala ambapo kuna manung’uniko kuhusu haki na usawa hasa katika uchumi.Ni rahisi kumshauri fukara aingie mtaani “kujikomboa” kuliko kumshawishi mtu afunge biashara zake akashiriki maandamano.Pia ni vigumu kwa watu wa makabila au dini tofauti wanaoshirikiana katika ajira na utoaji au upokeaji huduma kuanzisha vurugu ambazo kwa vyovyote zitapelekea kuathiri mahusiano yao (kwa mfano, mahusiano kati ya mfanyabiashara na mteja au mwajiri na mwajiriwa).

Tofauti na nchi kama Uingereza ambapo mvuto wa kisiasa miongoni mwa wapiga kura uko chini hasa kwa vijana,wengi wetu tulishuhudia namna kampeni za uchaguzi nchini Kenya zilivyogusa karibu kila sehemu ya maisha ya Wakenya,kama ambavyo chaguzi zetu huko nyumbani zinavyokuwa na mvuto mkubwa.Ni dhahiri kwamba amani ingeshapatikana iwapo nguvu nyingi zilizotumiwa na wanasiasa wa Kenya na vyama vyao kushawishi wapiga kura zingeelekezwa pia kwenye kutafuta mwafaka katika vurugu zinazoendelea.

Ni vigumu kubashiri namna gani vurugu hizo zitadhibitiwa na kumalizwa kwa vile Kibaki na Raila wanaonekana kutokubaliana katika njia sahihi za kuleta amani.Yayumkinika kusema kwamba hakuna uwezekano wa Kibaki na serikali yake kukubali mapungufu yaliyojitokeza kwenye uchaguzi huo kwa vile kwa kufanya hivyo watakuwa wameongeza nguvu kwenye hoja za Raila na wafuasi wake kwamba matokeo ya uchaguzi huo ni feki.

Kwa upande mwingine,Raila anafahamu gharama kubwa ya maisha na mali wanayoipata wafuasi wake kwa kupinga matokeo ya uchaguzi huo,na kukubali kushirikiana na Kibaki pasipo makubaliano ya kutengua ushindi wa rais itakuwa ni sawa na usaliti wa daraja la kwanza.Historia nayo haitoi matumaini ya amani kwa jirani zetu wa Kenya kwani hakuna rais yeyote (hasa barani Afrika) anayeamini alishinda uchaguzi kwa njia halali aliye tayari kukubali uchaguzi urejewe kwa minajili tu ya kuridhisha wapinzani wake au kutuliza machafuko nchini mwake.

Madhara ya muda mrefu ya kinachoendelea nchini Kenya ni kuzaliwa kwa kizazi chenye kinyongo.Ni kipi kinachoweza kufuta kinyongo cha mtoto aliyepoteza wazazi wake katika machafuko hayo?Kibaya zaidi ni kwamba kadri machafuko yanavyoendelea ndivyo kizazi hicho cha kinyongo kinavyozidi kuongezeka.

Miezi michache iliyopita Watanzania walitoa maoni kuhusu wazo la kuunda muungano wa nchi za Afrika Mashariki,na wengi wao walipinga uharakishaji wa muungano huo.Ni kama walifahamu kwamba kelele za kuwa na muungano zilikuwa za kisiasa zaidi kuliko kuzingatia hali halisi ndani ya nchi husika. “Mikoa” ambayo ingeunda “nchi” hiyo (yaani sie na Uganda,na pengine Burundi na Rwanda) imeshindwa kuwa na mchango wa maana wakati “mkoa mwingine” (Kenya) unazidi kuteketea.Sijui ingekuwaje iwapo haya yangekuwa yanatokea ndani ya muungano huo!

Baadhi ya wapinzani wa muungano huo walieleza bayana kwamba japo wanafahamu umuhimu wa ushirikiano,au hata kuungana kisiasa,ukweli unabaki kwamba nchi husika zina matatizo yake lukuki ambayo yanapaswa kushughulikiwa kwanza kabla ya kuyakuza kwa kuunda “nchi” kubwa zaidi iliyojaa vipande vyenye matatizo binafsi.

Jeuri za wanasiasa wa Kenya kutosikiliza vilio vya wananchi wao na kupuuza jitihada mbalimbali zinazofanywa na wasio Wakenya ni onyo muhimu kwa wenye ndoto za ya muungano wa Afrika Mashariki kwamba kama wanashindwa kuweka mbele maslahi ya nchi yao na wananchi wao watajali vipi maslahi ya Watanzania au Waganda.

Kubwa la kujifunza katika sakata hili ni jinsi ilivyo amani iliyojengwa kwa miaka miongo kadhaa inavyoweza kuyeyuka ndani ya kipindi kifupi kabisa.Harakati za kumfukuza mkoloni nchini Kenya zilichukua miaka mingi na kugharimu maisha mengi.Wakenya walikuwa bado wako katika harakati za kupata uhuru wa kweli hadi wakati machafuko yanaanza nchini humo.Kinachoendelea sasa ni sawa na kusigina jitihada na damu za mashujaa waliopigania uhuru wa nchi hiyo.

Kwa Watanzania,wakati tunaendelea kuwaombea jirani zetu amani (yaelekea hakuna la ziada tunaloweza kufanya zaidi ya hilo) ni muhimu kutambua kwamba amani na utulivu tulionao unaweza kudumu milele iwapo tu jitihada za makusudi zitafanyika kuondoa umasikini,kuhakikisha pato la taifa linatumika kwa maslahi ya wote na “haki” kuwa haki ya kweli kwa kila Mtanzania bila kuangalia tabaka.Kelele dhidi ya ufisadi na mafisadi ni sehemu muhimu ya harakati za kuhakikisha amani na utulivu nchini inadumu milele.

24 Jan 2008

Alfajiri hii nimepata barua-pepe kutoka kwa mtu mmoja anayeelekea kuumia moyo kwa namna navyoshutumu ufisadi na mafisadi.Mzembe huyo ametoa shutuma lukuki kuhusu makala zangu magazetini na humu "bloguni" kuhusiana na suala la ufisadi.Kwa kutompa ujiko aliokuwa anatafuta,nimeamua kupuuza barua-pepe hiyo na sikumjibu.Binafsi,nilikuwa natambua bayana kwamba mafisadi wameshabaini kwamba mtandao una nguvu pengine zaidi ya magazeti yetu huko nyumbani,hasa ikizingatiwa kwamba ni machache tu yaliyopo kwenye mtandao.Mapepe aliyeniandikia barua-pepe amejitahidi kadri ya uwezo wake mdogo alionao kuni-discourage kuandika chochote dhidi ya mafisadi,huku akidai kwamba sie tulio ughaibuni tuna tabia ya kujifanya tunajua kila kitu (cha ajabu ni kwamba naye anadai yuko ughaibuni,tena hapahapa Uingereza).

Sitaki kuifanya case yangu kuwa universal lakini naamini kwamba teknolojia ya habari kupitia mtandao imetokea kuwa silaha kubwa dhidi ya wanyonge na wakati huohuo ikiwa mwiba mkali dhidi ya ufisadi na mafisadi.Kuna watakaopambana nasi tunaopigia kelele ufisadi kwa vile wao ni vibaraka wa mafisadi na wengine watasigishana nasi kwa vile wao wenyewe ni mafisadi.Wito wangu kwa wale wote ambao kwa namna moja au nyingine wameamua kusimama kidete kupigania haki na usawa kwa kila Mtanzania,Mwafrika na raia wengine wa dunia wanaonaoporwa stahili zao,ni huu:kila kelele ya fisadi itafsiriwe kama full tank za mafuta ya mtambo wa kukabiliana na maovu kwenye jamii.

Kwa fisadi "wangu" Mapepe,pokea zawadi hii kutoka kwa Ludacris kwenye clip ya Get Back (Caution: explicit lyrics)


18 Jan 2008


Nimekuwa mwandishi wa makala magazetini tangu mwaka 1998,takriban miaka 10 sasa.Mtu aliyenipa changamoto la kufanya hivyo anaitwa Albert Memba,mwandishi wa zamani wa habari za michezo katika gazeti la Nipashe na Guardian.Huyu jamaa anaimudu lugha vilivyo.Nilianzaia kwenye magazeti "ya udaku" kama Sanifu (lilifariki zamani hizo) na baadaye Kasheshe na Komesha,ambako nilikuwa naandika unajimu "wa kuchekesha usio na chembe ya ukweli" (tuuite humorous horoscope) kwa kutumia jina la uandishi Ustaadh Bonge (hadi leo baadhi ya rafiki zangu wanaendelea kuniita hivyo).Baadaye nikamahimia kwenye uandishi wa makala za mambo muhimu zaidi ya vichekesho na udaku.Anyway,ni hadithi ndefu.

Nilipata wazo la ku-blog katikati ya mwaka juzi.Nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sintampongeza Ndesanjo Macha,kwani mwongozo wake wa namna ya kuanzisha blogu ndio ulionifanya niwe hapa nilipo.Wazo la kuanzisha blog hii lilitokana na ukweli kwamba gazeti lililokuwa linatoa makala zangu halikuwa na tovuti,hivyo awali blog hii ilikuwa kwa ajili ya kuwawezesha watu wote wanaojua Kiswahili popote walipo duniani wapate fursa ya kusoma makala hizo ambazo hazikuwa mtandaoni.Baadaye nikatanua wigo wa uandishi wa makala kwa kuanza kuandika kwenye magazeti ya Mtanzania na Raia Mwema ambako makala zangu hutoka mara moja kwa wiki.

Mmmoja ya watu waliosaidia sana kuitangaza blog ni hii ni rafiki yangu Haki Ngowi.Huyu hana hiana linapokuja suala la kupromoti blog ya bloga mwenzie.Nakumbuka waungwana flani waliwahi "kunitosa" nilipowatumia ombi la kubadilishana vinganishi (exchange links) kwa vile sikuwa naendana na maudhui ya blog yao.Nawashukuru kwani walinipa changamoto kubwa sana.

Mie ni muumini wa msemo "beauty should never be imprisoned",kitu kizuri shurti kisifiwe.Lakini mpewa sifa asibweteke bali anapaswa kuendeleza jitihada (sio kwa ajili ya kupata sifa zaidi) bali kuhalalisha kwamba waliompa sifa hapo awali hawakuwa "wanampaka mafuta kwa mgongo wa chupa",au kwa lugha ya mtaani, hawakuwa "wanamzuga".Nawashukuru nyote mnaonitumia barua-pepe za pongezi kuhusu makala zinazotoka kwenye magazeti nayoandikia pamona na zile zinazotoka kwenye blog hii.Nyie ndio chachu ya ya mafanikio ya makala hizo.

Nina tabia moja ambayo imenitengenezra marafiki na maadui wengi,nayo ni kusema ukweli.Huwa sioni aibu kukiri kwamba nimejifunza kitu flani kutoka mahala flani,kama ambavyo huwa sioni dhambi kumkosoa mtu naedhani amekosea jambo flani.Huko nyuma nilishawahi kuingia kwenye mgogoro na kampuni flani ya magazeti kwa vile tu niliwakosoa pale nilipoona wamepotoka.Tofauti na matarajio yangu,waungwana hao wakaanza kuhoji kuhusu maendeleo yangu ya elimu.Binafsi,huwa sipendi kabisa majadiliano kuhusu masuala ya shule yangu kwani naamini ni suala binafsi (only exception,ni pale majadiliano hayo yanapokuwa ya kitaaluma).

Kuna bloga anaitwa Mpayukaji Msemaovyo.Laiti kungekuwa na mashindano ya kutafuta blogu zenye "kiwango cha juu cha uchungu kwa nchi" basi naamini Mpayukaji angekamata nafasi ya juu kabisa.Simsifii kwa vile tu napenda anachaondika,bali ni ukweli kwamba blog yake imekuwa ni darasa zuri kwangu kujifunza "uchungu kwa nchi yangu na mapambano dhidi ya ufisadi na mafisadi".Uzuri wa makala za Mpayukaji,ambazo hupatikana pia kwenye gazeti la Tanzania Daima,ni ile tabia yake ya kuliita jiwe ni jiwe na sio tofali (calling a spade a spade).Unajua,kuna kusifia kitu kwa matarajio ya kupewa asante flani (kitu ambacho nakipinga kwa nguvu zote) na kuna kusifia kitu kwa vile kina kila sababu ya kusifiwa,na hicho ndicho nachokifanya hapa.Kuna wakati huwa nasoma makala za Mpayukaji huko Tanzania Daima mpaka najikuta naijiwa na taswira ya nyuso za mafisadi zinavyokunjamana kwa hasira iliyochanganyika na aibu+maumivu (truth pains) kutokana na uzito wa hoja za Mpayukaji.

Nitaendelea kuwapongeza waandishi na bloggers wengine ambao wanawatumia Watanzania kwa upenyo huu "mpya" uliojitokeza (mtandao) kuwasilisha vilio,kero,manung'uniko,lawama na hata pongezi kuhusu taifa letu.Pia nitaendela kuwapongeza wenzetu wanaotuletea habari kwa njia ya picha kwani taswira (image) inaweza kuwakilisha maneno elfu kadhaa kwa wakati mmoja.

(Picha ya Mpayukaji nimeipata kutoka kwenye profile ya blogu yake pasipo idhini yake,nitaomba idhini baadaye).

Almanusura nisahau.Hivi huko nyumbani watoto wangapi wanaoamua kutoroka majumbani kwao kutokana na sababu moja au nyingine?Je kuna mahauzigeli wangapi wanaoamua kutoroka kwa waajiri wao kutokana na manyanyaso yaliyopita kiasi?Katika mfumo ambao mnyonge licha ya kutokuwa na haki ananyang'anywa hata ile haki ndogo aliyozaliwa nayo (utu),kundi hili linabaki kuwa halina mtetezi.Clip hii ya Ludacris ft Mary J. Blidge katika wimbo Runaway Love inaweza kutukumbusha wajibu wetu kama jamii


1 Oct 2007

Kwanza,samahani nyingi kwa wapendwa wa blogu hii,maana niliadimika kidogo na hakukuwa na updates zozote.Ni vijimambo tu vilivyosababisha hali hiyo,lakini nimesharejea kamili-kamili.Badala ya title ya post kuwa Kulikoni Ughaibuni sasa tutakuwa na Mtanzania Ughaibuni.Sababu ya msingi ya kubadili jina ni ukweli kwamba makala zinazopatikana katika blogu hii ni kumbukumbu ya zile zinazotoka kwenye moja ya magazeti ya huko nyumbani.Kwa sasa makala zinazounda blogu hii zitakuwa zinapatikana kwenye gazeti la Mtanzania Jumapili badala ya gazeti la Kulikoni.Jina la blogu litaendelea kuwa hilohilo la Kulikoni Ughaibuni.Enjoy!!!
MTANZANIA UGHAIBUNI-1

Asalam aleykum,

Kwanza nianze na salam kwa wale wote waliojaaliwa “kuuona mwezi” na kwa sasa wanaendelea na funga ya Ramadhan.Salam pia kwa wale ambao kwa sababu moja au nyingine hawajaouna mwezi mpaka leo.Salam nyingi zaidi ni kwa wasomaji wote wa gazeti hili la Mtanzania Jumapili.Baada ya salam,nadhani ni vema nikajitambilisha maana hii ndio makala yangu ya kwanza kabisa katika gazeti hili maridhawa.

Jina la makala hii linashabihiana kabisa na maelezo yangu binafsi na mahali nilipo kwa sasa.Mie ni Mtanzania (halisi,Mndamba kutoka Ifakara) ambaye kwa sasa nipo masomoni huku Ughaibuni.Naomba kutamka mapema kwamba mie sio mwandishi wa habari kitaaluma,ila naipenda na kuiheshimu sana taaluma hiyo,na ni katika kuonyesha “mahaba” yangu kwa taaluma hiyo ndio nikaelekeza nguvu zangu kwenye uandishi wa makala.Nadhani wasomaji wengi wa magazeti wanafahamu kwamba makala inaweza kuandikwa na mwandishi aliyesomea kwenye fani hiyo,na pia inaweza kaundikwa na akina sie ambao kwa sababu moja au nyingine hatukubahatika kusomea.Yayumkinika kusema kwamba kinachomvutia msomaji ni ubora wa makala na sio sifa za kitaaluma za mwandishi.Kimsingi,makala zangu zitalenga kuhabarisha,kufundisha,kukosoa,kuchochea mijadala (pale inapobidi) na mwisho ni kuburudisha.Makala zangu ni za picha mbili katika moja,yaani kwa upande mmoja nitazileta kwa mtizamo wa Mtanzania aliye Ughaibuni (Mtanzania ambaye anajua alikotoka,anaijali lugha yake ya taifa,ana uchungu na nchi yake na sio mingoni mwa wale waliosahau kuwa nyumbani ni nyumbani),na kwa upande mwingine ni mtizamo wa Mtanzania kama Mtanzania,yaani hapo namaanisha kuwa nitachoandika kingebaki hivyohivyo hata kama ningekuwa Namtumbo,Kiberege,Nkasi au Temeke.Labda nifafanue kidogo katika suala hili la mitizamo ya makala zangu.Kwanza,zitakuwa na mambo ya Ughaibuni na pili zitakuwa na mambo ya huko nyumbani.Lakini,kuna nyakati haitakuwa directly (moja kwa moja) namna hiyo,bali nitajaribu pia kufanya comparative analysis (tuite mchanganuo linganifu) ambapo masuala,habari na matukio ya huku Ughaibuni yataletwa kwa namna ya kuyalinganisha na yale yanayoshabihiana na huko nyumbani.Hapo kutakuwa na mazuri tunayoweza kujifunza kutoka kwa hawa wenzetu na mabaya ambayo huko nyumbani tumebahatika kuwa nayo lakini hawa wenzetu wameyakosa.Enewei,mengi mtayaona katika makala zijazo.

Hebu tuangalie nini kinachoendelea hapa kwa “Kwin Elizabeti” (Uingereza).Kwa kawaida,kipindi hiki cha kuelekea kumalizika kwa majira ya joto (summer season) vyama vikuu vya siasa hapa hufanya mikutano yao ya mwaka.Tayari chama cha demokrasia ya kiliberali (Liberal Democrats) na chama tawala cha Labour wameshamaliza mikutano yao.Kwa Liberal Democrats “ishu” kubwa ilikuwa ni mwenendo usioridhisha wa chama hicho ambao kwa kiasi kikubwa umekuwa ukihusishwa na uongozi wa Sir Menzies Campbell.Wapo waliokuwa wanaomwona kiongozi huyo kama mzee asiye na jipya wala mvuto wa kukifanya chama hicho kipate umaarufu unaohitajika.Habari njema kwa Sir Campbell ni ukweli kwamba wengi wa wanachama wa chama hicho bado wanaelekea kuwa na imani na kiongozi huyo pengine kwa kuamini kuwa “utu uzima ni dawa” (Campbell ana umri mkubwa zaidi kulinganisha na viongozi wengine wa vyama vikuu vya siasa vya hapa).Kwa upande wa Labour ya Gordon Brown,mkutano mkuu haukuwa na “mbinde” yoyote hasa ikizingatiwa kuwa kura za maoni zinaonyesha kwamba Waingereza wengi wanaelekea kuridhishwa na utendaji wa Waziri Mkuu Brown na chama cha Labour kwa ujumla.Pengine kinachomsaidia Brown ni rekodi yake akiwa mwangalizi mkuu (kansela) wa uchumi wa Uingereza na “uzembe” wa Tony Blair katika siasa za kimataifa hususan uswahiba wake na Joji Bushi na “ishu” nzima ya Iraki.Lakini “kimuhemuhe” kikubwa kiko kwa chama cha wahafidhina (Conservatives) ambacho kimeanza mkutano wake Jumapili iliyopita.Kiongozi wa chama hicho David Camron ana mtihani mkubwa sana,sio tu kwa vile kura za maoni zinamweka nyuma ya Gordon Brown,bali pia ukweli kwamba mawazo yake ya kukibadili chama hicho kiendane na wakati yamekuwa yakipata upinzani mkali miongoni mwa wale “waliokunywa maji ya bendera” ya chama hicho.Cameron amekuwa muwazi kwa wahafidhina wenzie kwa kusema kuwa chama hicho kinaonekana mingoni mwa wengi kama kinachowakilisha “tabaka la wenye nazo” na “masapota” wake wakubwa ni wazungu weupe ilhali makundi ambayo yanakuwa kwa kasi nchini hapa kama watu weusi na wahindi wakikiona chama hicho kama cha kibaguzi.Cameron amekuwa akijitahidi kwa udi na uvumba kuonyesha kwamba uhafidhina haimaanishi kuwa tofauti na watu wa kawaida,lakini wakongwe katika chama hicho wanaonekana kutovutiwa na mwenendo wa kiongozi huyo kijana.Pia Cameron amewaeleza bayana wananchama wenzie kwamba pasipo dhamira ya dhati ya kukibadili chama hicho kwenda na wakati basi ni dhahiri kuwa sio tu hakitaweza kupata ridhaa ya kuongoza nchi hii bali pia kinaweza kujiandalia kifo chake siku za usoni.

Nadhani mazingira yanayokizunguka chama cha Conservative yanashabihiana kwa namna flani na chama tawala huko nyumbani,chama dume,CCM,japo tofauti ya wazi ni kuwa wakati Conservative ni chama cha upinzani hapa Uingereza,CCM ni chama tawala huko nyumbani.Lakini kabla sijaenda mbali naomba niseme yafuatayo.Miongoni mwa matatizo yanayozikabili siasa za nchi zetu za Kiafrika ni kwa wahusika kutopenda kuambiwa yale wasiyotaka kusikia (ikiwa ni pamoja na kuambiwa hivyo wanavyofanya sivyo inavyopaswa kuwa,yaani ndivyo sivyo).Kwa mantiki hiyo,ushauri wa maana kabisa kwa CCM unaweza kutafsiriwa na baadhi ya wakereketwa kuwa mtoa maoni ni mpinzani.Mie si mfuasi wa chama chochote,na japo nasomea siasa (za kimataifa) lakini huwa sioni aibu kusema kwamba naichukia siasa hasa kwa vile nadharia (theories) zinakinzana sana na vitendo kwenye dunia halisi tunayoshi.Angalau kwenye siasa za kimataifa (International Relations) ninapata fursa ya kuelewa kwanini kuna ubabaishaji au uimara kwenye siasa za eneo flani.Baadhi ya rafiki zangu huwa wananiuliza iwapo niliamua kusoma siasa ili baadae nije kuwa kiongozi lakini (baada ya kicheko) huwa nawafahamisha kuwa katika siasa za Afrika kinachomata sio digrii ya siasa bali “nyenzo” zitakazowafanya wapiga kura wawe tayari hata kung’oana macho kuhakikisha unapata madaraka.

Changamoto linalokikabili chama cha Conservative linashabihiana kwa namna flani na lile linaloikabili CCM kwa namna hii:Kwa mtazamo wangu,wapo wana CCM wanaogombea madaraka kwa vile wanaamini kuwa ni kwa kufanya hivyo ndio watapata nafasi ya kuwataumikia Watanzania wenzao.Lakini wapo pia wale ambao wanafahamu u-chama dume wa CCM na wanagombea madaraka ili kufanikisha tu mahitaji yao binafsi ikiwa ni pamoja na kujitengenezea mazingira mazuri ya kuendelea na madaraka hapo 2010.Lakini kundi la hatari zaidi ni lile la wasio na idea yoyote kuhusu siasa bali ustawi wa matumbo yao (na pengine nyumba ndogo zao).Hili kundi la tatu ni la kuogopwa zaidi ya lile la pili kwani wakati lile kundi la pili linajumisha watu wanaoweza kuwa wanagombea ili waendelee kuwa madarakani kama wanasiasa,hawa wa kundi la tatu hawajali sana kama watarejea madarakani kwa vile la msingi kwao ni wamechuma kiasi gani katika kipindi walicho madarakani.Changamoto kubwa kwa CCM ni kutengeneza utaratibu ambao utakihakikishia chama hicho kinaendelea kuwa chama cha wakulima na wafanyakazi (na wafanyabiashara ).Tofauti na wale wanaonekana kuwa na hofu kutokana na wafanyabiashara kuingia kwenye siasa,mie sina tatizo na kundi hilo alimradi lengo lao ni kuwatumikia wananchi (na pengine kuna umuhimu kwa bendera ya CCM kuongeza alama ya fedha kuashiria kuwa chama hicho ni cha wakulima,wafanyakazi na wafanyabiashara).Ikumbukwe kuwa hata wamachinga ni wafanyabiashara pia na miongoni mwao wapo wale wenye mwamko wa kisiasa sambamba na wakulima na wafanyakazi.

Naomba nimalizie kwa kuwa muwazi zaidi kwa hoja kwamba kwa namna flani “vimbwanga” vilivyojitokeza kwenye kinyang’anyiro cha kuwapata viongozi waCCM katika ngazi mbalimbali vimechafua jina la chama hicho tawala.Huo ni ukweli ambao kila mwenye mapenzi na chama hicho na uchungu na nchi yake atakuwa anaufahamu.Yayumkinika kusema kuwa baadhi ya hoja za vyama vya upinzani zinajengwa na CCM yenyewe kwani iwapo kungekuwa na “kuwekana sawa” katika masuala yanayogusa hisia za wananchi wa kawaida basi ni dhahiri kwamba akina Slaa au Kabwe wasingekuwa na hoja za kujaza maelfu kwa maelfu ya watu kwenye mikutano yao.Hii inaitwa na Waingereza kuwa ni “wake up call” au kwa lugha nyepesi ni changamoto.Kwa vile maslahi ya Taifa ni muhimu kuliko vyama vya siasa (vyama vya siasa huzaliwa,kukuwa na pengine kufa wakati nchi ni lazima iishi milele) basi naamini kuwa wenye mapenzi ya dhati na Taifa letu watanielewa na kufanyia kazi nilichoeleza.

Alamsik



Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.