Showing posts with label MUUNGANO. Show all posts
Showing posts with label MUUNGANO. Show all posts

1 Jun 2012




FRIDAY, JUNE 1, 2012


#ZANZIBAR REVEALED

 kuna dhana ya kuwa karume aliuawa kulinda muungano, mazingira yote ya kuuawa kwa karume haiihusishi tanganyika kwa namna moja ama nyengine katika mauaji hayo na kwamba ni wananchi walichoshwa na serikali yao. kinachotokea leo zanzibar, ni msingi mbovu wa utawala wa tokea awali na kamwe tanganyika isihusishwe. 

jarida moja la kila mwezi 'Africa Events' la Agosti 1992 (uk. 27) ,linadai sababu za kuuawa kwa Karume zilikuwa za kibinafsi kwa njia ya kulipa kisasi. Inaelezwa kwamba Muhammed Hamud, mtoto wa Hamud Muhammed Hamud, aliyetiwa kizuizini miezi michache baa­da ya mapinduzi ya 1964 akituhumiwa kutaka kuipindua Serikali ya Karume.
Miaka, rnichache baadaye, Luteni Hamud Muhammed Hamud akiwa katika mafunzo ya kijeshi huko Tashkent (Urusi ya zamani), aliambiwa na mwanafun­zi mwenzake kwamba mzee Hamud alinyongwa na Karume akiwa kizuizini hila kufunguliwa mashtaka. Kwa taarifa hiyo, Luteni Hamud alisikika akiapa ange­muua Karume akirejea Zanzibar.
Taarifa ya kusudio la Hamud la kuua ilifikishwa kwa vyombo vya usalama Visiwani na wenzake, lakini hakukamatwa wala kuwekwa wa chini ya uchunguzi mkali ali­porejea Zanzibar; badala yake ali­pandishwa cheo kuwa luteni na Karume mwenyewe.
Jarida hili halisemi lolote juu ya raja Ali Khatibu Chwaya na ko­plo mwingine juu ya kushiriki kwao katika mauaji haya. Hata hivyo,. Kushiriki kwao kunaelekea kutetea dhana ya pili kwamba kwa sababu Serikali Karume ilishindwa kukidhi matarajio ya Wazanzibari wengi, hapakuwa na njia mbadala ila kumwondoa Karume ili kuleta mabadiliko.


Hapa panazuka swali; kama lengo la Hamud la kumuua Karume lilikuwa kulipa kisasi, kwa nini tukio hili lilihusisha watu zaidi ya mmoja? Si hivyo tu; kwa nini watu zaidi ya 1,000 walikamatwa kutokana na mauaji hayo kama haukuwa mpango mpana?
Dhana ya kulipiza kisasi inapungua nguvu kwa kushindwa kusimama kwa miguu miwili. inatuacha njia panda wakati huo ikijaribu kumezwa na dhana mpango wa mapinduzi, kama ilivyodai Serikali.
Inadaiwa kuwa mpango kuipindua, Serikali ya Karume ulibuniwa mwaka 1968 na wanharakati wa mapinduzi ya 1964 wakiwemo raia  na Wanajeshi wachache.
Inasemekana kikao cha mwisho cha mpango huo kilifanyika Aprili 2, 1972 nyumbani kwa Luteni Hamud, ambapo ilikubaliwa kwamba mauaji hayo yafanyike Aprili 7, 1972.
Mpango wa utekelezaji ulikuwa kwamba Hamud na Ahmada wachukue jukumu zito sana la kuiba silaha kutoka Kambi ya Jeshi yaBavuai.


Katika kutekeleza mapinduzi hayo, ambayo mipango na operesheni yake ilifanana kabisa na ya mapinduzi ya 1964, mtu mmoja, Suleiman Sisi, alipewa jukumu la kuongoza mashambulizi kwenye Kambi ya Jeshi la Mtoni na Ahmada alipewa jukumu la Kambi ya Bavuai, Makao Makuu ya Jeshi la Chuo cha Jeshi la Ma­funzo ya Redio ambazo zote ziko eneo la Migombani.


Kambi ya Ubago haikupangi­wa mtekaji kwa kuamini kwamba kama kikosi cha Ahmada kingeweza kuziteka sehemu kili­chopangiwa, Ubago ingesalimu amri sawia.


Kituo cha Polisi Malindi kingetekwa na kikosi ambacho kingeongozwa na Hamud, am­bapo magari yenye redio za mawasiliano yangepatikana kwa watekaji. Ilipangwa kuwa wakati mashambulizi haya yakiendelea, kituo cha Polisi Ziwani kingevamiwa na askari polisi walitarajiwa kuajiriwa na kuongozwa na askari Yusuf Ramadhan.


Mtu mwingine, Amour Dughesh, alipangwa kuteka Ikulu na alipewa jukumu lakumkamata­Karume na kumpeleka Kituo cha Redio kutangaza kupinduliwa kwa Serikali rake.


Inaelezwa pia kwamba baada ya redio kutekwa, ingewekwa chi­ni ya udhibiti wa Badawi Qual­letein, Miraji Mpatani na Ali Mtendeni. Uwanja wa Ndege ungedhibitiwa na Ali Sultan Issa, ambapo Makao Makuu ya Umoja wa Vi­jana wa AS P (ASPYL) yangetekwa na Baramia.


Makao Makuu ya ASPYL ya­likuwa Kituo Kikuu cha Mkuu wa Usalama wa Ndani ya Serikali ya Karume, Kanali Seif Bakari. Kanali Bakari aliongoza kikun­di cha ukatili kilichojiita kamati ya watu 14, kilichotesa na kuua waliodhaniwa wapinzani na Karume. Abdulrahman Mo­hammed Babu, akiandikia jarida la kila mwezi 'CHANGE' (Vol 4 No. 7,) la 1996, ukurasa 11, anakiri:- "Kutaja pekee jina la Kamati ya Watu 14 kulitosha kumtia mtu woga na kutishika”.


 Kamati hii ili­husika na mauaji ya mamia ya Wazanzibari wasio na hatia, waki­wemo, viongozi, wana’mapinduzi wa kimaendeleo kama Abdallah Kassim Hanga, Abdulaziz Twala, Saleh Saadala, Othman shariff na wengine wale waliuawa kwa jina la Karume."


Abdallah Ameir alipewa jukumu la kuzuia mashambulizi kutoka nje siku hiyo yamapinduzi.
Inadaiwa kuwa katika kikao hicho, Aprili 2, 1972 mtu mmoja, Amar Salim Kuku, alidokeza kuwa Ali Salim Hafidh ambaye nafasi yake haikutajwa katika mpango wa mapinduzi wa Aprili 7, angefi­ka Zanzibar na Abdulrahman Babu na wafuasi wake wa Dar es salaam, usiku wa Aprili 6 kwa mtumbwi kuungana na wanamapinduzi wengine.


Ukiwaondoa Luteni Hamud na Kepteni Ahmada katika mpango huu, na kama ni kweli kwam­ba mpango wote ilikuwa jaribio la mapinduzi (coup d'etat) kama ilivyodai Serikali ya Zanzibar, 'basi staili ya mpango huo haiwezi kut­ofuatishwa na ile ya mapinduzi ya umwagaji damu ya Aprili 12, 1964 ,ambao haukuhusisha jeshi.
Mapinduzi ya 1964 ya kushtukizwa dhidi ya utawala wa Sultan Jamshid na majeshi yake, yali­fanikiwa kwa sababu ya utawala huu kujitenga mbali na wananchi, hivyo haikuweza kupata taarifa za mipango ya mapinduzi hayo mapema.


Na kama ni kweli ilivyosema Serikali ya Zanzibar, kwamba mpango wa mapinduzi ya 1972 uli­buniwa tangu mwaka 1968, ilikuwaje JWTZ na Usalama wa Taifa, achilia mbali kikosi cha Us­alama wa Ndani cha Karume (Gestapo), kilichoongozwa na Kanali Seif Bakari kisibaini mapema hadi siku ya kupoteza uhai wa Kiongozi wa.taifa hilo?  Je, si kweli kwamba historia ya 1964 ilikuwa ikijirudia?


Haya yanaweza kuwa maoni ya wengi, wakiwamo wachunguzi wa mambo ya siasa. Mwanazuoni mahiri barani Afrika, Ali Mazrui anabainisha katika kitabu chake 'Africa's International Relations' (uk. 11); "ukizingatia jinsi Sheikh Abeid Karume alivyoitawala Zanz­ibar kwa ukatili na ubaguzi mkubwa, lolote lilitarajiwa kutokea kwake; hakuna aliyetarajia kwam­ba angedumu kwa miaka minane madarakani. Ndiyo maana hati­maye wengi hawakushangaa alipouawa mwaka 1972."

2 Nov 2007

Ama kweli ni rahisi kupanga sera na kutegemea ifanikiwe lakini ni habari nyingine kwa mpanga sera kuwa sehemu ya utekelezaji huo.Hilo limejihidhirisha katika taarifa kutoka nchini Marekani ambapo maafisa wa mambo ya nje wa nchi hiyo wamefahamishwa kwamba watakuwa wakipelekwa nchini Irak kama sehemu ya utekelezaji wa majukumu yao ya kazi.Pamoja na kukumbushwa kwamba wakati wanakubali ajira waliapa kufanya kazi mahala popote watakapopangiwa na mwajiri wao,maofisa hao wameonekana kutoafikiana na pango huo ambapo baadhi yao wamefikia hatua ya kuuita “mpango wa kujipeleka kwenye hukumu ya kifo” hasa kwa vile “ziara” za aina hiyo tayari zimeshagharimu maisha ya maofisa watatu tangu kuanza kwa vita ya Irak.Maofisa wanaokaidi agizo hilo wanakabiliwa na hatari ya kuchukuliwa hatua kali ikiwa ni pamoja na kufukuzwa kazi.Nadhani pamoja na hatari inayoweza kuwakabili maofisa wanaopelekwa huko,nadhani utekelezaji wa agizo hilo utawasaidia kufahamu namna hali halisi ilivyo kwenye uwanja wa mapambano ni ambayo ni ngumu zaidi kuliko urahisi wa kuandaa sera,mikakati na mipango mizuri.



Kwa hapa UK,moja ya masuala ambayo kwa siku kadhaa sasa yametawala duru za habari ni kuhusu “Muungano” wa Uingereza (the United Kingdom of Great Britain and Northern Ireland). Kumekuwa na mjadala wa muda mrefu kuhusu mambo makuu mawili: kwa upande mmoja ni umuhimu wa Muungano huo (miongoni mwa wale wanaopendelea kuona unadumu milele) na upande mwingine ni hoja kwamba muungano huo unazipunja baadhi ya sehemu zinazounda nchi hii.Katika uchaguzi mkuu uliopita,chama tawala cha Labour kilibwagwa na chama cha SNP (Scottish National Party) kwa upande wa Scotland.Hofu ya awali kwa Labour na “wapenda Muungano” baada ya ushindi wa SNP ilikuwa kwenye ukweli kwamba miongoni mwa malengo ya muda mrefu ya SNP ni kuiona Scotland ikiwa nchi huru inayojiendesha pasipo kuelekezwa na “serikali” ya London.Na katika manifesto yao ya uchaguzi,SNP hawakuogopa kutamka bayana matamanio yao uhuru wa Scotland.Chama hicho kilikuwa kinaelewa bayana kwamba sera hiyo ingeweza kuwapatia ushindi au kushindwa kwenye uchaguzi huo,kwani suala la uhuru wa Scotland ni miongoni mwa mambo yanayowagawa sana watu hawa.Kura mbalimbali za maoni kuhusu suala hilo zimekuwa na matokeo yanayothibitisha mgawanyiko huo,ambapo takriban nusu ya Waskotishi wanadhani uhuru ni wazo zuri huku takriban nusu nyingine wakipinga wazo hilo.Jeuri ya madai ya uhuru inachangiwa na kile Waskotishi wengi wanachokiona kama utajiri katika eneo hili (mafuta) ambao wanadhani unapaswa kuwanufaisha zaidi wao sambamba na kuwa na maamuzi ya namna ya kutumia utajiri huo badala ya kusubiri maelekezo kutoka England.Lakini wapo wanaoonya kwamba Scotland haiwezi kujimudu yenyewe kwa kutegemea tu utajiri wa mafuta,na baadhi ya wachumi wamekwenda mbali zaidi kwa kuonyesha pengo la bajeti litakaloikumba Scotland pindi ikijitoa kwenye Muungano huu.

Mjadala bado unaendelea na ni vigumu kusema bayana iwapo uhuru utapatikana au Muungano utaendelea.Majuzi,kiongozi wa chama pinzani cha Conservatives,David Cameron amewasha tena moto kuhusu suala hilo baada ya kutamka kwamba ana nia ya kusukuma sheria itakayowabana wabunge wa Scotland waliopo kwenye bunge la jumla la Uingereza (yaani linalojumuisha wabunge wa England,Wales,Scotland na Northern Ireland) wasipige kura kwenye masuala yanayoihusu England pekee.Hili ni suala linalujulikana kama “the West Lothian Question” (jina linalotokana na swali lililoulizwa mwaka 1977 na mbunge wa jimbo la Scotland la West Lothian,Tam Dalyell,wakati wa mjadala wa bunge kuhusu kuanzisha serikali-devolved governments-za Scotland na Wales).Swali hilo lilihusu uhalali wa wabunge wa “nchi” hizo mbili kushiriki katika mijadala na maamuzi yanayowahusu watu wa England pekee,ilhali wabunge wa England hawana nafasi kama hiyo kwa vile hawaingii kwenye mabunge ya sehemu hizo.Chama cha Labour kimemshutumu Cameron kwa kile walichokiita sera za kuvunja Muungano lakini kwa vyovyote vile hoja hiyo ni habari njema kwa Alec Salmond (First Minister wa Scotland) na chama chake cha SNP pamoja na wale wote wanaotaka uhuru.

Na kuna mambo yanayoshangaza kuhusu Muungano huu.Kwa mfano,wakati noti zinazotolewa na benki ya England (English Pounds) zinatumika nchi nzima,na zinakubalika mahala popote duniani kama sarafu halali ya nchi hii,noti zinazotolewa na mabenki ya Scotland (ambazo zina thamani sawa na English pounds) zinakataliwa katika baadhi ya maeneo ya England.Nilipokuja huko nyumbani mwaka jana,nilishindwa kabisa kubadilisha Scottish pounds na ilinilazimu nizitume huku ili zibadilishwe kuwa English pounds.Sheria za elimu ya juu na huduma za afya pia zinatofautiana kwa namna flani,ambapo kwa Scotland huduma nyingi zinatolewa bure ilhali kwa England zinaendelea kulipiwa.Scotland pia imekuwa ikilalamikia suala la uhamiaji ambapo sheria zinazotawala ni zile za nchi nzima ilhali mahitaji ya “nguvu-kazi” kutoka nje (kupitia uhamiaji wa wageni) unaathiriwa na sheria “kali” zinazotawala nchi zote zilizopo kwenye Muungano huu. Wakati Scotland imekuwa ikiendesha program kadhaa za kuvutia wageni,ikiwa ni pamoja na kuwashawishi wale walio hapa waifanye “nchi” hii kuwa makazi ya pili (second home) au makazi ya kudumu,kelele za wanasiasa huko England ni kwamba wageni wamezidi na lazima serikali idhibiti zaidi wahamiaji.

Masuala ya muungano ni nyeti na yamekuwa chanzo cha matatizo katika sehemu mbalimbali duniani.Lakini tofauti na wenzetu hawa ambao wanadiriki kutoa mawazo yao hadharani na kukaribisha mijadala kuhusu suala hilo,huko nyumbani kuzungumzia kuhusu Muungano inaelekea kuwa sio wazo la busara sana kwa mwanasiasa anayotaka mafanikio.Kuna kile kinachoitwa “jinamizi la Mwalimu kwa atakayetaka kuvunja Muungano” ambacho kimsingi nakiona ni kama kikwazo kwa wale wote wanaodhani kwamba ni muhimu kuwa na mjadala kuhusu hatima ya Muungano wetu.Tukiendelea kuogopa kuujadili,yayumkinika kusema kwamba tunautengenezea mazingira mazuri ya kuuharibu.Sio siri kwamba wenzetu wa Visiwani wamekuwa wakipiga kelele sana kwamba Muungano unawaumiza,lakini hofu yangu kubwa ni pale wenzao wa Bara nao “watakaposhikilia bango” hoja hiyo ya kuumizwa na mzigo wa Muungano.Na “the West Lothian Question” ya Uingereza “ina-fit” kabisa mazingira yalivyo huko nyumbani ambapo wabunge kutoka Zanzibar wamekuwa wakishiriki (katika bunge la Muungano) katika kujadili na kutoa maamuzi katika baadhi ya mambo ambayo yanayowahusu Wabara pekee ilhali wabunge wa Bara hawana nafasi hiyo kwani hawaingii kwenye Baraza la Wawakilishi huko Zanzibar.

Nafahamu kuwa kuna kitu kama “tume” au “kamati” iliyoundwa kujadili kero za Muungano,lakini japo sijui imefikia hatua gani katika majadiliano yao,yayumkinika kusema kwamba kasi nzima ya kulitafutia ufumbuzi wa kudumu suala hilo sio ya kuridhisha.Pengine katika kuepuka maamuzi yanayotoka juu kwenda chini (yaani kutoka kwa viongozi kwenda kwa wananchi) japo waathirika au wafaidika wakubwa ni hao wa chini,sio wazo baya kufikiria kuitisha kura ya maoni ili kupata mawazo ya wadau wakubwa wa Muungano huo (wananchi).Ashakum si matusi,lakini ni vema Muungano ukavunjika kwa ridhaa kuliko ukadumu kwa manung’uniko,kwani manung’uniko hayo yasipopatiwa tiba yanaweza kabisa kuuvunja Muungano huo pasipo kusubiri ridhaa ya wadau.Kikubwa nilichojifunza katika mjadala wa Muungano wa Uingereza ni namna ambavyo unavyoendeshwa kwa uwazi na upana zaidi kiasi kwamba sauti zote,zinazopinga na kukubali suala hilo,zinasikika waziwazi.Ukiniuliza iwapo Muungano wetu ni muhimu,jibu nitakalokupa hata niwapo usingizini ni “ndio”.Hata hivyo,umuhimu wa Muungano huo hauondoi haja ya kuufanya uwe bora zaidi,wa manufaa kwa pande zote mbili na wenye mazingira yatakayoufanya udumu daima dumu.Tusipoziba ufa leo,kesho tutajenga ukuta.

Mwisho, napenda kutoa pongezi kwa kizazi kipya cha vijana wabunifu. Hivi karibuni, mchora katuni na mtangazaji maarufu Masudi “Kipanya” alizindua duka la nguo za lebo yake ya “KP Wear”. Na msanii wa bongoflava AY nae anaelekea kufuata mkondo huo. Hawa na wengineo wenye mawazo kama hayo wanatumia vizuri umaarufu walionao kwenye jamii na wanastahili sapoti yetu. Wito wangu kwao ni kwamba wanapomiminiwa sifa kwa jitihada zao, wazitumie sifa hizo kuwa chemchem ya kusaka mafanikio zaidi. Pia wanaweza kwenda mbali zaidi kwa kutumia mianya ya biashara ya kimataifa kama vile katika e-Bay ili kuwawezesha Watanzania popote walipo duniani kunufaika na ubunifu wao. Kwa lugha ya mtaani, mie “nawapa tano”.Tanzania ya “masupastaa” wanaovuma kwa ubunifu wao,na sio kwa skendo,inawezekana.

Alamsiki


27 Aug 2007

Asalam aleykum,


Kuna habari flani nimeiona gazetini imeniacha nakenua meno kwa kicheko.Kwa mujibu wa gazeti moja la Daily Mail la hapa Uingereza eti inadaiwa kwamba wanawake warefu “wanawazimia sana” wanaume wafupi.Kilichopelekea madai hayo ni maswali wanayojiuliza wafuatiliaji wa mambo ya watu (wambeya?) eti kwanini mwanamitindo wa kimataifa Sophia Dahl “amekolea” kwa mwanamuziki “andunje” wa midundo ya jazz,Jamie Callum.Gazeti hilo linadai kwamba wanaume wafupi huwa wanafanya jitihada sana kuhakikisha kuwa wanafidia “pengo” la urefu wao kwa kujituma kwenye maeneo mengine.Hoja nyingine ya kuchekesha ni ile inayodai kuwa watu wafupi ni “vipotabo” kwa wanawake warefu,na hata wakialikwa kwenye nyumba za watu warefu basi ni rahisi kwa “masoti chesisi” hao kufiti kwenye makochi pasipo kulalamika kuwa miguu inauma iwapo kochi lenyewe ni la kujibana.Sijui habari hiyo inawahusu wanaume wafupi wa nchi za Magharibi pekee au dunia nzima lakini lililo wazi ni kwamba suala la mwanamke kumzimia mwanaume au mwanaume kumzimia mwanamke ni la mtu binafsi,na ufupi,urefu,wembamba au unene sio kigezo muhimu sana japo sote tunafahamu kwamba wengi wetu tuna “mapendezeo” yetu.


Wiki iliyopita nilipata nafasi ya kushuhudia mchezo wa kirafiki wa soka kati ya timu ya taifa ya Scotland dhidi ya ile ya Afrika Kusini (Bafana Bafana),mechi iliyofanyika kwenye uwanja wa Pittodrie hapa Aberdeen.Ilipendeza kuona Waafrika wachache wanaoishi hapa wakiwa wametinga jezi za Bafana kuonyesha sapoti yao kwa timu hiyo.Japo mechi hiyo iliisha kwa Scotland kuibuka na ushindi kiduchu wa bao moja kwa bila, “sie” tuliofungwa (Waafrika wote siku hiyo tuligeuka kuwa Wasauzi) tulifarijika kuiona timu ya “nyumbani” ikitandaza kabumbu la kuvutia.Unajua mara nyingi hawa watu weupe wanakupa heshima pale utapowaonyesha una uwezo sawa nao au pengine zaidi yao.

Na wikiendi nilipata fursa ya kuangalia (kwenye runinga) michuano ya kimataifa ya riadha kutoka huko Osaka,Japan.Kama kawaida,Waethiopia na Wakenya wametesa vilivyo.Nimesoma kwenye magazeti yahuko nyumbani kuwa nasi tunawakilishwa na wanariadha kadhaa.Sijui tutaambulia chochote au itaendelea kuwa hadithi ile ile ya kuwa wasindikizaji wa kudumu.Lakini naamini kwamba kama Wakenya na Waethiopia wanaweza kutawala kwenye anga hizo,basi nasi pia tunaweza kabisa kufanya vizuri.Ni lini tutapata akina Filbert Bayi na Suleiman Nyambui wengine?Upeo wangu mdogo wa Jiografia unanishawishi kuamini kwamba hali ya hewa ya mkoa kama Arusha unatupatia mazingira mazuri ya kuzalisha wanariadha ya viwango vya kimataifa.Na ushahidi upo kwa kuangalia “perfomance” ya baadhi ya mashujaa wetu wa miaka ya nyuma.Penye nia pana njia,na kama tutawekeza vya kutosha basi kwa hakika tutaweza kurejesha historia ambayo kwa sasa imeshaanza kusahaulika.

Kuna dalili za mafanikio huko mbele ya safari kwenye soka letu. “Uchawi wa Kibrazil” wa Maximo na mwenzie Tinoco unaelekea kuzaa matunda.Ukichanganya na sapoti ya kutosha kutoka kwa JK mwenyewe basi si ajabu nasi tukajikuta tunaingia kwenye ramani ya soka ulimwenguni.Kinachonipa shaka ni matatizo ya uongozi kwenye vilabu vyetu vya soka.Maana kila kukicha utasikia wanachama Simba wanataka kupindua uongozi,au wenzao wa Yanga wanamkalia kooni kiongozi flani,au mara usikie kocha flani kabwaga manyanga kwa vile hajalipwa stahili zake,na vioja vingine visivyo na mwisho.Katika makala yangu iliyopita niliwausia viongozi wa Simba kutumia vizuri mkataba walioingia na kampuni moja kupromoti “chata” ya Adidas.Hee!haujapita muda mrefu nasikia baadhi ya wanachama wanapania kuung’oa uongozi ulio madarakani.Na hapohapo nasikia kocha Twalib Hilal anasema anarejea umangani kwa vile hajakamilishiwa malipo yake.Kiongozi mmoja anang’aka jukumu la kumlipa kocha huyo kwa kudai kwamba aliletwa na Friends of Simba.Ok,tuseme kuwa mapenzi ya Friends of Simba kwa klabu yao yaliwasukuma kumtafuta kocha mwenye uwezo wa kuipeleka mbali klabu ya Simba,na wakamsomesha Twalib hadi akakubali kusamehe mshahara mnono huko Umangani.Sasa,viongozi hawakupaswa kubweteka na kuliacha jukumu la mshahara kwa Frienda of Simba pekee.Kwanza,msaada uliotolewa na kikundi hicho unaweza kutafsiriwa kama msaada kwa uongozi kwani sote tunajua “politiki” za Simba na Yanga:matokeo yakiwa mabaya basi uhai wa viongozi kuwa madarakani unakuwa unaning’inia kwenye utando wa buibui.

Ni kama kichekesho vile kwa sababu miezi michache iliyopita,uongozi huohuo wa Simba uliweka msimamo thabiti dhidi ya kundi la Friends of Simba wakidai kundi hilo linaihujumu klabu hiyo.Navyoelewa mimi ni kwamba kwa vile klabu hiyo inajiendesha “Kiswahili” ni lazima wawepo watu wa kuikwamua kifedha pale inapokwama,na kwa namna mambo yalivyo,kila wakati uchumi wa vilabu vyetu ni wa kusuasua kama suala la amani huko Somalia.Ufumbuzi wa matatizo sio Mapinduzi,kwani yameshafanyika mengi tu na hakuna lolote la msingi lililopatikana.Wala kukimbilia mahakamani sio ufumbuzi wa matatizo.Na kuwa na mahusiano mazuri na vipoba hakuwezi kuwa ufumbuzi wa kudumu wa matatizo ya klabu kama Simba.Ufumbuzi pekee ni kwa vilabu hivyo kujiendesha kibiashara.Soka ni zaidi ya burudani kwani ikiendeshwa kisasa inaweza kuwa chanzo kizuri cha mapato.Unaposikia Manchester United,Chelsea au Liverpool zinavutia wawekezaji kutoka nje ya Uingereza sio kwamba matajiri hao ni wakereketwa sana wa soka (ingekuwa ni ukereketwa basi wangenunua vilabu katika nchi zao) bali wanajua bayana kwamba soka ni biashara yenye faida.

Twanga Pepeta wako ziarani hapa Uingereza,na wametapisha kumbi walizotembelea.Hivi kwa mfano Simba au Yanga wangefanya ziara sehemu mbalimbali duniani wasingeweza kujichumia mapato mkubwa pengine zaidi ya hayo wanayopata Twanga?Na kwa kufanya ziara nje ya nchi vilabu vyetu vingeweza kuua ndege wawili kwa jiwe moja:kutengeneza mapato ya kutosha na kuitangaza vipaji vya wanasoka wao,ambao wakipata timu huku nje inamaanisha mapato zaidi kwa vilabu hivyo.Najua wapo wanaoniona kama nimechanganyikiwa kwa kutoa mawazo kama haya.Siwalaumu kwani kwa jinsi wanavyofahamu ubabaishaji uliokithiri kwenye vilabu vyetu,hata ziara za mikoani zinahitaji mitulinga ili ziwe na mafanikio.

Mwisho,ningependa kutumia fursa hii kuwapongeza marais wa nchi za Afrika Mashariki kwa kuzingatia maoni ya wananchi wao kuhusu suala la kuharakisha Muungano wa nchi hizo.Mimi ni muumini wa hekima ya umoja,yaani umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu.Lakini umoja kati ya watu wenye “backgrounds” zinazotofautiana unaweza usizae matokeo yanayokusudiwa.Nilisoma sehemu flani ambapo DCI Manumba aliweka bayana kuwa kuongezeka kwa wimbi la ujambazi huko nyumbani kunachangiwa kwa kiasi kikubwa na wageni wanaoingiza nchini pasipo kufuata taratibu za uhamiaji.Ni ukweli usiopingika kuwa hali ya amani iliyopo Tanzania ni kivutio kizuri kwa “watu wa shari” kutoka nchi jirani.Unadhani hali itakuwaje pindi “washari” hao watakuwa wanaweza kuingia Tanzania kirahisi kama vile mtu anavyotoka Ilala kwenda Temeke hapo Muungano huo utakapokuwa umekamilika.Lakini hoja hiyo ya uhalifu ni ndogo tu ukilinganisha na ukweli kwamba tuna mambo yetu kadhaa ya muhimu tunayopaswa kuyashughulikia kwanza kabla ya kufikiria kujitanua.Na miongoni mwa mambo hayo muhimu ni suala la Muungano kati ya “Tanganyika” na Zanzibar.Halafu kuna hii “lulu” yetu ya amani na utulivu.Najua kila mtu ana tafsiri yake ya neno “amani na utulivu” lakini naamini sote tunakubaliana kuwa hatuwezi kulinganisha nchi yetu na mbinde za Wahutu na Watutsi huko Rwanda na Burundi au tatizo la ukabila huko Kenya (bila kusahau Mungiki).Na yayumkinika kusema kuwa “uwekezaji” wa wenzetu hapo nyumbani ni mkubwa zaidi ya wetu huko kwao.Mazingira yaliyoiua jumuiya ya awali ya Afrika Mashariki bado yapo,na ni vema yakarekebishwa kabla ya kufikiria wazo la Muungano mpya.

Alamsiki






13 Jul 2007

Asalam aleykum,

Baada ya matukio ya hivi karibuni yaliyotuweka matumbo moto kufuatiwa mahayawani flani kuamua kuendesha kampeni yao ya kishetani ya kutaka kulipua mabomu huko London na hapo Glasgow (Waskotishi bado hawaamini kuwa ugaidi umeingia kwenye ardhi yao) sio wazo baya kuanza makala hii kwa habari “nyepesi nyepesi.” Gazeti la Daily Mail la hapa liliripoti hivi karibuni kuhusu matokeo ya utafiti yaliyoonyesha kuwa wanaume wenye aibu wana nafasi kubwa ya kupata magonjwa ya moyo kuliko wale wasio na aibu!Hizi tafiti nyingine…we acha tu.Kwa mujibu wa gazeti hilo,utafiti huo ulifanyika kwa kipindi cha miaka 30 uliwahusisha maelfu ya wanaume ambapo watafiti kutoka chuo kikuu cha Northwestern cha Chicago,Marekani walipokuwa wanafanya ufuatiliaji wa wawaliowahoji kwenye utafiti huo walibaini kuwa asilimia 60 kati yao (waliohojiwa) walikuwa wameshafariki,huku chanzo kikuu cha vifo kikiwa “heart attack” (nadhani kwa Kiswahili sahihi ni msongo wa moyo).Mambo hayo!

Na ukisikia duniani kuna mambo usidhani ni utani.Mzembe mmoja amekamatwa huko New Hampshire (Manchester) baada ya kushindikana kwa jaribio lake la kutaka kufanya uporaji benki huku akiwa amejivika matawi ya miti kama “camouflage” (kificho) yake.Jamaa huyo,James Coldwell,aliingia kwenye tawi la benki ya ushirika ya Citizens,huku akiwa amejivika majani na kuwatisha wahudumu wa benki hiyo kabla ya kufanikiwa kuondoka na kitita cha fedha,lakini alinaswa na polisi muda mfupi baadaye kwani triki yake ya “uninja wa majani” haikumsaidia kwa vile majani hayo hayakufunika sura yake,na wanausalama waliweza kuitambua vizuri kwenye CCTV.

Jumuiya ya Ulaya (EU) nayo ilijikuta kwenye wakati mgumu hivi karibuni baada ya kutoa filamu fupi kwa ajili ya promosheni ya kuhamasisha Jumuiya hiyo ambapo wahusika kwenye filamu hiyo ya sekunde 44 yenye jina “Let’s Come Together” walikuwa wakifanya “ngono nyepesi” (soft porn).Wapinzani wa wazo la Muungano wa nchi za Ulaya waliishambulia EU kwa kupoteza fedha za walipa kodi kwa kutengeneza filamu hiyo waliyoiona kuwa ni mwendelezo wa ubabaishaji wa Jumuiya hiyo.Nilipomtumia rafiki yangu flani habari hiyo kutoka gazetini alitania kwa kusema labda na sie tunahitaji “kampeni chafu” kama hiyo ya EU “kuuza” wazo la Muungano wa Afrika Mashariki ambao unaelekea kuwakera wadau wengi.

Nae mwanamama Amy Beth Ballamura amaepigwa marufuku kutia mguu kwenye pwani yoyote ya Uingereza baada ya kufanya majaribio zaidi ya 50 ya kujiua kwa kurusha baharini.Miongoni mwa sababu zilizopelekea kuchukuliwa kwa hatua ya kumdibiti mwanamama huyo ni pamoja na kuzitia huduma ya uokoji (emergency services) gharama ya zaidi ya pauni milioni 1 (zaidi ya shilingi bilioni mbili za huko nyumbani) kila wanapoitwa kwenda kumuokoa.Lakini pamoja na “tamaa” yake ya kujitoa roho,askari mmoja aliambulia tuzo ya ushujaa mwaka 2003 baada ya kusikia kelele za kuomba msaada kutoka baharini na kuamua kujitosa majini kufuata kelele hizo,ambapo alifanikiwa kumuokoa mwanamama huyo mwenye umri wa miaka 44.Cha kushangaza ni kwamba kama kweli alikuwa na nia ya kujitoa uhai sasa hizo kelele za kuomba msaada zilikuwa za nini?

Enewei,baada ya "nyepesi nyepesi" hizo (zote ni habari za kweli na wala sio kuwa “nawapiga fiksi” wasomaji wangu wapendwa) sasa tuangalie mambo ya muhimu zaidi huko nyumbani.Kwanza niseme siafikiani na hoja za Waziri wa Sheria Mama Nagu kwamba Bunge halipaswi kufanya kazi ya kupitia mikataba kabla ya kutiwa saini ili libaki na uhalali wake wa kuiwajibisha Serikali kwa mujibu wa dhamana ya mgawanyo wa mamlaka, kuchunguzana na kuwajibishana.Siafikiani naye kwa sababu hoja za baadhi ya wabunge kuwa mikataba hiyo ifikishwe kwao kabla ya kusainiwa zilizingatia ukweli kwamba kuna mapungufu makubwa yanayoendelea katika suala zima la kusaini mikataba mbalimbali.Mantiki nyepesi (simple logic) inaweza kutueleza kwamba maslahi ya nchi ni muhimu zaidi ya huo mgawanyiko wa madaraka.Hivi kwa mfano wazo la mikataba kuletwa bungeni lingekubaliwa,halafu nchi inufaike kwa kuingia mikataba yenye maslahi kwa Taifa,tatizo linakuwa wapi?Hivi kipi bora,kulinda mgawanyiko wa madaraka huku mikataba ya ajabu ajabu ikiendelea kuwepo au “kupindisha sheria” kwa kuileta mikataba hiyo bungeni kabla haijasainiwa halafu nchi ikanufaika nayo?

Pia nimesoma kwenye gazeti moja la huko nyumbani kwamba lile tishio la wafugaji huko wilayani Kilombero limerejea tena.Nitamke bayana kuwa hili linanihusu binafsi kwa vile mie ni “mwana wa pakaya” naetokea mitaa ya huko.Hawa wafugaji ni wakorofi,watovu wa nidhamu na wavunja sheria wakubwa.Maagizo kadhaa yameshatolewa kuwataka waheshimu sheria za nchi lakini wameamua kuweka pamba masikio.Mamlaka husika zinapaswa kuliangalia suala hili kwa makini zaidi kwani wanachofanya wafugaji hao sio tu kinahatarisha amani (mifugo yao inakula mazao ya wakulima,na hilo pekee linatosha kuzusha ugomvi) lakini pia hawawatakii mema wakulima kwani kwa kuswaga mifugo yao kwenye mashamba wanamaanisha kuwa wanataka wakulima hao wakose chakula na hela wanazojipatia kwa kuuza akiba ya mavuno yao.Hili ni bomu la wakati (time bomb) kwani japo hakuna bondia wa Kindamba (kama yupo basi samahani kwani sijamsikia) lakini hiyo haimaanishi kuwa mtu atakaeswaga mifugo yake kwenye mashamba ataachwa afanye anavyotaka.Hapo itakuwa kuchukua sheria mkononi,na japo mie ni mpinzani mkubwa wa kuchukua sheria mkononi,natambua dhahiri kuwa mtu “anapoletewa za kuleta” anaweza kabisa kuiweka sheria kando,hususan pale haki yake inapopuuzwa kwa makusudi.Kwa vile mkoa wa Morogoro umebahatika kuwa na RC ambaye ni “mjeshi” mstaafu basi hapana shaka Brigedia Jenerali Kalembo huyo atatumia “mbinu za medani” kuwadhibiti wafugaji hao wenye uhaba wa nidhamu.

Kikao cha Bunge kinaelekea ukingoni na miongoni mwa hoja nilizovutiwa nazo ni ile ya Mheshimiwa Shabiby (wa Gairo) kuhusu ujanja unaofanywa na baadhi ya wamiliki wa mabasi makubwa ya abiria.Alieleza kuwa mengi ya mabasi yanayotumika sasa yamefanyiwa “usanii” kwa kuweka mabodi mapya kwenye “chasis” na injini za malori au za kale.Kuna jina moja tu linalowafaa “wasanii” hawa nalo ni “WAUAJI.” Wanathamini sana kukwepa gharama za kununua mabasi mapya lakini hawajali hata chembe madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na vitendo vyao vya “kuunda mabasi feki.” Kwa upande mwingine tuseme bila kuonekana aibu kwamba mabasi ya namna hiyo yanafahamika hata bila kuwa na ujuzi wa umakanika kwani ulifika pale stendi ya mabasi Ubungo unaweza kukutana na basi ambalo linaonekana dhahiri kuwa bodi yake “imepachikwa” sehemu isiyostahili.Trafiki yeyote aliyehitimu mafunzo yake vyema na mwenye uchungu na maisha ya Watanzania wenzie hawezi kuliruhusu basi “lililovimba mbavuni utadhani lina ujauzito” liendelee na safari,na mabasi ya namna hiyo yako mengi tu.Wanaofanya hivyo wanajua bayana kuwa wanavunja sheria na kuhatarisha maisha ya abiria wao lakini hawajali kwa vile hakuna aliyechukuliwa sheria hadi leo.Si ajabu tukisikia kuwa baadhi ya mabasi hayo yanatumia injini za matrekta au hata za mashine za kusaga….(nashindwa kumalizia,nimekabwa na kicheko japo jambo hili sio la kuchekesha hata chembe.)

Mwisho,wakati Gavana wetu keshatamka bayana kuwa hatojiuzulu (utadhani alijichagua mwenyewe kwenye posti hiyo),sie wapenzi wa Simba tunajipoza kwa kusherehekea ubingwa wetu ambao kidogo umetibuliwa na hizi habari za viongozi kugombea mapato ya mechi huko Morogoro.Wito kwa watani wetu wa jadi Yanga ni huu:Micho akirudi (kama kweli atarudi) ashauriwe kukutana na Twalib Hilal apewe darasa kuwa ukocha sio sawa na ukatibu mwenezi wa klabu: ukocha ni vitendo vingi maneno machache lakini Mserbia Micho kila siku “anachonga” kuhusu hili au lile lakini matunda ya kazi yake kwenye dimba ni haba.Enewei,asilaumiwe sana kwani alishawahi kusema kuwa wachezaji wake hawafundishiki,na katika mechi ya juzi anaweza kuongeza sababu kuwa “lile tumbo la kuendesha” limechangia kukosa ushindi.

Alamsiki






18 Jun 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Habari za huko nyumbani

Mojawapo ya tofauti kubwa kati ya jamii ya hawa wenzetu na huko nyumbani ni namna uhuru wa kujieleza (freedom of expression) unavyothaminiwa.Of course,uhuru huo unaambatana na wajibu,kwa sababu kama wanataaluma wa kanuni za maisha wanavyosema,uhuru bila wajibu ni sawa na kukaribisha vurugu.Kadhalika,uhuru huo sio wa asilimia 100 (absolute),kwa vile hakuna kitu kama hicho duniani.Lakini ukilinganisha na huko nyumbani,yayumkinika kusema kwamba hawa wenzetu wana uhuru mkubwa zaidi wa kujieleza.Sambamba na hilo ni uhuru wa taasisi zinazopaswa kuujulisha umma nini kinaendelea katika jamii yao na hata nje ya jamii hiyo.Hapa nalenga zaidi kwenye taasisi za habari:hususan magazeti na vituo vya radio na runinga.

Kuna magazeti hapa ambayo ni mithili ya hayo yanayoitwa “ya udaku” huko nyumbani.Magazeti kama The Sun,News of the World,Daily Mirror,nk yamebobea sana katika kuibua skandali mbalimbali hapa Uingereza.Inapotokea kwamba habari flani imepotoshwa basi hao walioguswa na habari hiyo wataamua aidha kukanusha au kukimbilia mahakamani kudai fidia.Wakati mwingine watajwa kwenye habari hizo hulazimika kukiri makosa yao hadharani.Kwa mfano,juzijuzi iliripotiwa kuna Naibu Waziri Mkuu John Prescott alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na katibu muhtasi wake Tracey Temple.Katika sekeseke hilo ambalo bado halijatulia ilimzalimu Bwana Prescott kukiri kuwa yaliyosemwa na magazeti ni kweli.

Nakumbuka mwanataaluma mmoja huko nyumbani aliwahi kuvitaka vyombo vya habari kuwa na ujasiri wa kutaja majina ya watuhumiwa bila kuwa na hofu ya kuburuzwa mahakamani,iwapo vyombo hivyo vina uhakika na walinachoripoti.Hebu chukulia mfano wa habari kama hii: “kiongozi wa chama kimoja cha siasa kinachoanzia na herufi C anadaiwa kuwa na uhusianowa kimapenzi na mtangazaji flani ambaye jina lake linaanzia na herufi D…”Hivi habari kama hiyo si ni sawa na chemsha bongo kwa msomaji?Hali ilikuwa mbaya sana miaka ya nyuma kwa sababu ilikuwa ni vigumu mno kujua ni mtuhumiwa gani hasa anazungumziwa katika stori husika.Hata hivyo,kuna dalili kwamba mambo huenda yakabadilika hasa baada ya ujio wa magazeti jasiri ambayo yako tayari kwa lolote.Ukweli ni kwamba kama ushahidi upo wa kutosha hakuna haja ya kuficha jina la mhusika (labda ithibitike kuwa kumtaja kutaathiri uchunguzi,au kwa sababu za kimaadili).

Siyalaumu magazeti yanayoshindwa kutaja majina ya wahusika katika skendo flani japokuwa nayapa changamoto kufanya hivyo.Siyalaumu kwa sababu sio kosa lao,sio uoga,bali ni mazingira yaliyopo.Siasa za nchi yetu baada ya uhuru hadi mwanzoni mwa miaka ya 1990 zilikuwa zimegubikwa na usiri mkubwa.Kutaja madhambi ya kiongozi ilikuwa dhambi,na hapa tunazungumzia kuanzia ngazi ya mtaa hadi taifa.Usiri sio mbaya kama unatumiwa kwa manufaa ya wengi,lakini kwa bahati mbaya baadhi ya watu walikuwa wanautumia kuficha maovu yao.Waliofilisi mashirika ya umma walinufaika sana na siasa za usiri.Viongozi hawakuwa tayari kusikia kauli nyingine zaidi ya sifa,na kuwakosoa ilikuwa ni kujichimbia kaburi.Kwa hiyo,hali tuliyonayo sasa ni matokeo ya miongo kadhaa ya kuishi katika siasa za kusifia na si kukosoa.

Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni miongoni mwa maeneo ambayo yameathiriwa sana na kutokuwepo uhuru wa kutoa mawazo sambamba na uoga wa kuadhibiwa unapoongea kinyume na matakwa ya wakubwa.Nilikuwa sijazaliwa wakati mataifa haya yanaungana,na sijafanya utafiti wa kutosha iwapo Muungano huo ulifanywa kwa ridhaa ya wadau (wananchi) au yalikuwa ni maamuzi tu ya viongozi.Miaka nenda miaka rudi watu wamekuwa wakiongea “chini ya uvungu” kwamba Muungano huu una matatizo mengi tu japokuwa yanaweza kutatuliwa pale penye nia.Baadhi ya viongozi wamekuwa wanakwepa kuzungumzia matatizo yaliyopo kwa madai ya “kukwepa jinamizi la Muungano.”

Hivi karibuni kumekuwa na harakati za kisheria na kisiasa kuhusu Muungano.Kundi la Wazanzibari limefungua kesi kuhusu Muungano,Mchungaji Mtikila nae anaonekana kuukalia kooni Muungano,na viongozi wa serikali kutoka Bara walikutana na wale wa viswani kujadiliana kuhusu suala la Muungano.Juu ya hayo serikali ya awamu ya nne ina waziri anaeshughulikia suala la Muungano.Hata hivyo,kauli za Waziri Kiongozi wa Zanzibar Samsi Vuai Nahodha kuwa suala la mafuta ni la kisiwa hicho pekee,sio kitu cha kukiacha kipite hivihivi tu.Scotland,sehemu ya muungano unaounda United Kingdom (Uingereza) ina utajiri mkubwa wa mafuta.Lakini japokuwa kumekuwa na kelele za hapa na pale kuhusu muungano huo,utajiri wa mafuta haujawahi kuipa kiburi Scotland ifikirie kujitoa katika muungano huo au itumie mapato yote ya mafuta peke yake.Sasa kelele zimeanza hata kabla hayo mafuta hayajapatikana huko Zanzibar,je yakipatikana si ndio itakuwa mshikeshike!

Mimi nadhani suala la Muungano linazungumzika.Ikibidi kufanya kura ya maoni kujua matakwa ya sasa ya wananchi kuhusu Muungano,basi na ifanyike bila kuogopa matokeo yake.Siasa za kuogopana na kubembelezana zimepitwa na wakati,na iwapo itathibitika kuwa upande mmoja wa Muungano hauridhiki na muundo au kuwepo kwake,basi jitihada za dhati zifanyike kupata ufumbuzi.Tukiendelea na siasa za usiri na kujidanganya kwamba kila kitu kinakwenda vizuri,si ajabu siku moja Muungano huu ukavunjikia mahakamani.Hiyo itakuwa aibu sana hasa kwa wale wanaodai kukwepa “jinamizi la kuvunjikiwa na Muungano.”Inatokea huko Serbia-Montenegro,inaweza pia kutokea huko nyumbani iwapo wanasiasa wetu hawatafanya jitihada za makusudi.

Alamsiki

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.