Showing posts with label MZEE WA VIJISENTI. Show all posts
Showing posts with label MZEE WA VIJISENTI. Show all posts

10 Nov 2010


Muungwana mmoja amenitumia comment ambayo kwa hakika imenigusa sana.Naomba niinukuu
Mbona umekatisha mijadala ya kuendeleza nchi ghafla mno. nilitegemea utakuwa na tasmini ya matokeo ya uchaguzi lakini umezimika ghafla. Vipi au jamani inakuwaje uchungu na nchi unakuwa kwa muda tu? Au wameshakutishia na wewe?
Naelewa kwanini mzalendo huyu anataka tufanye tathmini ya uchaguzi mkuu ambao wengi wetu tuliupa umuhimu wa kipekee kutokana na mwenendo wa mambo ulivyo huko nyumbani.Baada ya kushuhudia taifa likienda mrama kwa kugubikwa na ufisadi ilionekana ni lazima Watanzania wenye uchungu wa dhati kwa nchi yao wachukue hatua zinazostahili.Na hatua mwafaka ilionekana kuwa ni kuing'oa CCM madarakani.

Mgombea urais kwa tiketi ya Chadema,Dkt Wilbroad Slaa,ameweka bayana msimamo wake kuwa uchaguzi huo ulichakachuliwa.Baadhi ya taasisi zilizotuhumiwa kufanya uchakachuaji huo zimejitokeza hadharani na kukanusha tuhuma hizo.Haihitaji hata cheti cha kozi ya siku 1 ya uchambuzi wa siasa kumaizi kuwa hakuna hata mmoja kati ya wanaotuhumiwa atakiri mchango wake katika kuirejesha CCM madarakani.Wakubali ili waadhibiwe?

Kadhalika,kuna dhana iliyojengeka kuwa katika uhalisia barani Afrika na katika baadhi ya nchi "za dunia ya tatu" sio rahisi kwa chama tawala kushindwa uchaguzi,na ikitokea kimeshindwa basi yayumkinika kuhitimisha kuwa hayo ni matokeo ya uzembe wa chama husika au migogoro ndani ya chama hicho.Hebu chukulia mfano mazingira ya uchaguzi wetu.Vyombo vya dola vilionyesha waziwazi kuipendelea CCM huku watendaji wa taasisi zinazopaswa kuwa huru wakijibidiisha kumlinda mgombea wa chama tawala.Ndio maana haikumtia hofu Mhariri wa Daily News,gazeti linaloendeshwa kwa kodi za walalahoi,kutamka bayana kuwa Dkt Slaa asingeweza kuwa rais hata baada ya miaka mitano.Kujiamini huko hakukutokana na uimara wa CCM bali ndoa ya kifisadi kati ya taasisi za umma na chama hicho tawala.

Tulisikia taarifa kadhaa kuhusu watendaji wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kutowatendea haki wagombea wa vyama vya upinzani.Kadhalika,ilifika mahala Msajili wa Vyama vya Siasa akaamua kuweka wazi mahaba yake kwa CCM na kujipachika jukumubla kuitetea hata pale ilipokosea waziwazi.

Sasa unaweza kujiuliza,"kama tulishaona mwenendo wa aina hiyo ie wa kuitengenezea CCM mazingira ya ushindi,kwanini tulijipa matumaini kuwa Dkt Slaa angeibuka mshindi?".Jibu rahisi kwa mtizamo wangu ni kwamba kulikuwa na matumaini kuwa sauti kubwa ya umma ingeweza kukwaza jitihada zozote za uchakachuaji.Au hata kama jitihada hizo zingefanyika basi zingezidiwa nguvu na sauti hiyo ya umma.

Naomba kukiri hadharani kuwa hofu yangu kubwa haikuwa kwenye mikakati ya kundi dogo lakini lenye nguvu kubwa la mafisadi bali MTAJI MKUU WA CCM yaani umasikini wa Watanzania walio wengi.CCM inategemea sana masikini na hata matokeo "halali" yanathibitisha hilo ambapo maeneo yaliyogubikwa na umasikini ndio yaliyoipa CCM kura nyingi.Huu ni uhusiano ambao kitaaluma unaweza kuelezwa kama wa mnyanyasaji na mnyanywasaji (abuser-abused relationship).Mnyanyasaji anawekeza nguvu nyingi kumwaminisha mnyanyaswaji kuwa pasipo uwepo wake (mnyanyasaji) basi mnyanyaswaji hatakuwa na maisha.Ndio hadithi za amani na utulivu,umoja wa kitaifa,mshikamano,na madude mengine kama hayo.

Kitaaluma,mnyanyaswaji anaweza kufikia mahala akawa anaskia raha kunyanyaswa (punch drunk).Ni kama hali ya kuzowea makonde kwa bondia.Hakuna maelezo mengine mwafaka ya kuelezea namna watu wanaoamka wakiwa hawajui siku iyaisha vipi,wanaotembea maili kadhaa kusaka maji safi japo wafadhili wanamwaga fedha za miradi ya maji,wanaoshinda juani kutwa nzima na kulala vibambazani wakiuza peremende lakini bado wanaandamwa na jeshi la mgambo huku polisi wakiwawinda wawabambikizie kesi,wanaokwenda mahospitalini na kuambulia matibabu hewa kwa vile hakuna madawa,watu wenye watoto ambao makalio yanaota sugu kwa kukaa sakafuni mashuleni,watu ambao haki zao hazipatikani bila kutoa "kitu kidogo" kisha watu haohao wakipigie kura chama kinachostawisha mateso yao.

Na kwa waliodhani akina sie tuliokuwa tukipiga kelele za nguvu kutaka CCM iondoke tulikuwa na chuki binafsi basi matukio mawili yaliyojiri hata masaa 72 hayajapita baada ya CCM kurejea madarakani yanapaswa kuwafumbua macho.Tukio la kwanza ni la mtuhumiwa wa ufisadi wa rada,Mzee wa Vijisenti Andrew Chenge kuchukua fomu ya kugombea Uspika kisha kufanya press conference iliyojaa ngebe,nyodo na dharau kwa wote wanaokerwa na ufisadi.Binafsi,naamini kuwa Chenge katumwa na kundi flani linalotaka kuifakamia keki ya taifa kwa kasi ya marathon hasa kwa vile wanaelewa kuwa Awamu hii ya Tano inaweza kuwa ni lala salama.Chenge ameonyesha bayana kuwa anataka kuwa Spika ili kusafisha majina ya "waliosingiziwa kuwa mafisadi".

Lakini kubwa zaidi ni hisia zangu kuwa Chenge ana baraka kamili za uongozi wa juu wa CCM ikiwa ni pamoja na Mwenyekiti Jakaya Kikwete.Si bado tunakumbuka jinsi Kikwete alivyokwenda jimboni kwa Chenge kumpigia debe na kisha akatetea uamuzi wake wa kuwapigia debe watuhumiwa wa ufisadi kwa kudai kuwa kinachowakabili ni tuhuma tu.Kama tuhuma si tatizo mbona Bashe aliondolewa kwenye mchakato wa mchujo wa kupata wagombea ubunge kwa tiketi ya CCM kwa tuhuma kuwa sio raia wa Tanzania?Kwahiyo tuhuma kwa Chenge,Mramba,nk zinapaswa kubaki tuhuma tu lakini kwa wengine tuhuma ni sawa na hukumu!

Na kwa wanaidhani Chenge anafanya utani mbaya ( a bad joke) basi labda hawaielewi CCM vizuri.Chenge anaweza kabisa kupitishwa katika mfumo wa "kidemokrasia" wa CCM.Yea,kama ameendelea kuongoza kamati ya maadili ya chama hicho na kupitishwa kugombea ubunge (na kushinda) iweje basi kuukwaa uspika liwe suala gumu?Nguvu anayo,sababu anazo,sapoti anayo na VIJISENTI anavyo.Kipi cha kumzuwia kumrithi Samuel Sitta?

Tukio la pili linahisiana na hilo la kwanza ambapo Taasisi ya Kuzuwia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imekurupuka na kudai kuwa Chenge alishasafishwa katika tuhuma za ufisadi wa rada.Yaleyale ya kuisafisha Richmond japo angalau katika ishu ya Richmond serikali ya Kikwete ilikuwa na umri wa zaidi ya mwaka madarakani.Safari hii vimbwanga vimeanza hata kabla ya wiki kumalizika tangu iingie madarakani!Maumivu ya kichwa huanza polepole...

Na kwa kuthibitisha kuwa kura za kuirejesha CCM madarakani zilikuwa kura za kuubariki ufisadi,Ubalozi wa Uingereza umeishushua TAKUKURU kwa kutoa ufafanuzi kuhusu suala la ufisadi wa rada.Sijui nani ameipa TAKUKURU madaraka ya kusafisha watuhumiwa lakini hata sie tusio na uelewa mkubwa wa masuala ya sheria tunafahamu kuwa jukumu la kuhukumu ni la mahakama.Badala ya taasisi hiyo kumpeleka Chenge mahakamani ili kama kusafishwa asafishwe huku,yenyewe imekurupuka na utetezi wake wa kifisadi pasipo hoja za msingi.Hii yote ni katika kuandaa mazingira mazuri kwa Chenge kuwa Spika wa Bunge jipya.

Nitaendelea na tathmini yangu kadri siku zinavyosonga mbele.Najua kuna mengi tu ya kuyazungumzia hasa tukizingatia mazingaombwe yaliyotawala Awamu iliyopita hivyo ni suala la muda tu kabla hayajajiri mengine mengi ya kuwasuta wale wote waliotarajia miujiza kutoka kwa CCM.

5 Aug 2010

RAIS Jakaya Kikwete amewekewa pingamizi kortini kugombea urais mwaka huu kwa madai ya matumizi mabaya ya madaraka na ufujaji wa fedha za umma katika safari zake za nje.

Hayo yameelezwa na Mwalimu Mstaafu na Mkazi wa Dar es Salaam, Bw. Paul Mhozya ambaye amefungua kesi katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam kupinga mgombea huyo katika uchaguzi wa Oktoba 31, mwaka huu.

Akizungumza na Majira jana, Bw. Mhozya alisema amefungua pingamizi hilo chini ya hati ya dharura akiitaka mahakama kulisikiliza mapema kabla kampeni kuanza, hivyo akaishauri CCM kuteua mgombea mbadala mapema, badala ya kusubiri uamuzi wa mahakama.

Katika hati ya mashtaka yenye sababu kumi za kuiomba mahakama imuengue Rais Kikwete kwenye kinyang'anyiro cha urais Bw. Mhozya anasema, rais ametumia nafasi aliyopewa kwa mambo binafsi, amekiuka katiba na kuvunja haki za binaadamu pamoja na matumizi holele ya fedha za watanzania kwa mambo yake mwenyewe.

Gazeti la The Citizen toleo la jana lilimkariri Bw. Mhozya kuwa aliwahi kufungua kesi ya kikatiba kama hiyo mwaka 1993 dhidi ya Rais Mstaafu, Ali Hassan Mwinyi kuwa alivunja katiba kwa kuruhusu Zanzibar kujiunga na Jumuiya ya Kiislamu (OIC), lakini ikatupwa na Jaji Barnabas Samatta kuwa mamlaka ya kumwondoa rais madarakani yalikuwa mikononi mwa bunge peke yake, chini ya kifungu cha 46A cha katiba.

Bw. Mhozya alisema amefikia uamuzi wa kufungua kesi hiyo kutokana na ujeuri uliooneshwa na Rais Kikwete katika miaka mitano ya uongozi wake, hivyo ni vema akazuiwa kuurudia kwa kumzuia asirudi madarakani.

Alisema anayo orodha ndefu ya mambo mabaya aliyofanya Rais Kikwete wakati wa uongozi wake, ambayo anatarajia kuyatumia kama ushahidi na uthibitisho wa malalamiko aliyopeleka mahakamani, ambayo anaamini yatakubaliwa na kumwondoa kwenye kinyang'anyiro.

"Mwenyekiti wa Tume ya uchaguzi (NEC), Jaji Lewis Makame alikwishasema kuwa tume iko tayari kupokea pingamizi dhidi ya mgombea yoyote kwa maslahi ya umma na kuwa itachukua hatua stahili, ninasubiri kauli ya mahakama na ninaamini itasikiliza hoja zangu na kuzifanyia kazi," alisema.

Alisema kuwa yeye kama Mtanzania anayo mamlaka chini ya ibara ya 30 (3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufungua kesi dhidi ya uvunjaji wa ibara yoyote ndani ya katiba hasa zinazohusu haki za binaadamu.

Ibara ya 30 (3) inasema "Mtu yeyote anayedai kuwa sharti lolote katika Sehemu hii ya Sura hii au katika sheria yoyote inayohusu haki yake au wajibu kwake limevunjwa, linavunjwa au inaelekea litavunjwa na mtu yeyote popote katika Jamhuri ya Muungano, anaweza kufungua shauri katika Mahakama Kuu"

Bw. Mhozya anasema pamoja na kuwa Rais ana kinga kisheria lakini Kikwete hana kinga ya kuwekewa pingamizi kama mgombea kwa sasa, ndio maana akaamua kufungua kesi hii wakati huu badala ya kusubiri atakaposhinda na kuwa rais, kwani atakuwa na uwezo wa kutumia kinga yake.

Alisema katika kipindi cha uongozi wake rais amefanya safari za ughaibuni zisizo za lazima nyingi kwa fedha za umma, jambo ambalo limesababisha wananch wengi kuishi maisha ya taabu na umaskini mkubwa, huku akidai kuwa urais ni suala binafsi, akisema kuwa ndio maana alimteua mwanawe kumtafutia wadhamini.

Alisema sheria inaitaka NEC kutoa muda wa ziada kwa chama ambacho mgombea wake amekufa au ameshindwa kuendelea kukiwakilisha, ili chama hicho kiweze kuteua mgombea mwingine, hivyo anaamini kuwa baada ya pingamizi hilo kukubaliwa mahakamani, NEC itawaamuru CCM kufanya hivyo kwa kuwaongezea muda.

"Sasa kwa vile sheria inasema NEC itawaongezea muda wa kuteua mgombea mwingine, mimi nashauri wakateua kabisa mgombea mwingine na kumshauri niliyemwekea pingamizi kujitoa, hii itaepusha kupoteza muda pindi pingamizi likikubaliwa, hakuna jinsi," alisema Bw. Mhozya.



Alisema yeye anahofia zaidi mustakabali wa nchi na vizazi vijavyo kuliko anavyohofia maisha yake, hivyo pamoja na vitisho anavyopata bado hataogopa kusimamia ukweli na kuwafichua waovu kama anavyofanya.

"Nimetoka mahakamani leo (jana), nilikwenda kuwaona makarani wa wanipatie 'samansi'(hati ya kuhudhuria mahakamani iliyo na tarehe ya kusikilizwa kesi) lakini walisema bado haijatoka naamini itatoka hivi karibuni ili tukasikilizwe. Matatizo yapo na nilikwisha yazoea," alisema Bw. Mhozya.

CHANZO: Majira

Wakati hayo yakimkumba JK,aliyekuwa Mbunge wa CCM (Bariadi) Andrew Chenge a.k.a Mzee wa Vijisenti nae anakabiliwa na tishio la pingamizi kutoka kwa mmoja ya wana-CCM waliokuwa wakiwania nafasi ya kupitishwa kugombea ubunge kwa tiketi ya chama hicho
. Bonyeza HAPA Kusoma Zaidi Kuhusu Chenge.

16 Oct 2009


MBUNGE wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge jana alinguruma ndani ya Kamati ya Bunge ya Fedha na Uchumi, alipowataka Watanzania kuacha kutafuta mchawi aliyeua mashirika ya umma, akisema kuwa mengi yalikufa yakiwa mikononi mwao na si mwa wageni.

Chenge, mwanasheria mkuu wa zamani wa serikali, ametoa kauli hiyo wakati wananchi wengi wakilalamikia mikataba mibovu ya uwekezaji na uendeshaji mashirika ya umma kuwa ndiyo iliyochangia baadhi kufa na mengine kuwa katika hali mbaya.

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana wakati akichangia Taarifa ya Utekelezaji wa Moboresho ya Shirika la Bima (NIC), Chenge alisema makaburi mengi ya mashirika ya umma yamechimbwa na Watanzania wenyewe.

"Leo (jana) wakati tunamalizia kuadhimisha miaka kumi ya kifo cha Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, shirika hili la Bima lilikuwa moja ya malengo yake," alisema Chenge akirejea NIC ambayo ilikua na kutapakaa nchi nzima kabla ya kuanguka kiuchumi kiasi cha kusababisha serikali kuingilia kati na kuitengenezea muundo mpya.

"Lakini shirika hili leo liko hoi; kwa vyovyote vile serikali haiwezi kusimamia shirika hili kwa asilimia 100, lazima likabidhiwe kwa sekta binafsi, lakini Watanzania tumekuwa ni watu wa kupenda kupiga kelele hasa tunapoamua kubinafsisha. Mashirika haya tumeyaua wenyewe wala si wageni."

Chenge alisema: "Watanzania hatupaswi kutafuta mchawi wa mashirika yetu haya. Sisi wenyewe ndiyo tumeyaua na makaburi mengi leo hii yanaonekana."

Alifafanua kwamba, umefika wakati sasa Watanzania wakaachana na dhana ya kulalamika na badala yake wafanye kazi kwa bidii, huku pia akiitaka serikali iondoe dhana ya kuendesha mashirika kijamaa, akitolea mfano uwekaji wa kiwango cha chini cha bei na kutaka bei ya soko ishike hatamu.

Hata hivyo, alionyesha wasiwasi na Kikosi Kazi kinachofanya marekebisho kutokana na kukosa bodi na kuongeza: "Napata shaka kidogo, chombo ambacho kinaandaa taarifa halafu chenyewe pia ndio kijitathmini, nafikiri inapaswa kuundwa bodi."

Akichangia katika kikao hicho cha Kamati ya Fedha na Uchumi, Mbunge wa Tabora Mjini, Juma Kaboyonga aliitaka serikali kuharakisha ununuzi wa nyumba za NIC ambazo thamani yake ni Sh31.7 bilioni.

Mbunge huyo ambaye kitaaluma ni mchumi alisema serikali haipaswi kucheza na NIC, hivyo ni lazima itafute fedha hizo ili kuliwezesha shirika kwenda kwa kasi zaidi.

Kaboyonga alidai kuwa kumekuwa na hujuma dhidi ya NIC na kuhoji kwamba "kama mashirika binafsi yanaweza, vipi NIC ya serikali ishindwe".

Alisema: "Ipo dhana kwamba mashirika ya serikali hayana wenyewe, lakini mimi nasema yana wenyewe na wenyewe ni wananchi, lazima NIC iangaliwe, iwezeshwe na ipewe mtaji."

Akijibu hoja mbalimbali, Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi, Jeremia Sumari alisema serikali imepanga kuendeleza huduma nafuu na zenye ubora kutokana na kuamini NIC inaweza kujiendesha kwa faida zaidi.

Sumari alisema uamuzi huo wa serikali kupanga kutoa huduma bora na za gharama nafuu haumaanishi kuwa nchi inarejea kwenye ujamaa, bali ni kuangalia uwezo wa shirika na mahitaji ya Watanzania.

Kuhusu mtaji na mpango wa kununua nyumba za NIC kwa Sh31.7 bilioni, alisema hilo liko katika hatua nzuri na za mwisho na kuongeza: "Lakini hadi sasa nyumba hizi ni za serikali, kuna mahitaji ya nyumba kwa watumishi wetu kama waheshimiwa majaji n.k."

Dk Abdallah Kigoda, ambaye ni mwenyekiti wa kamati hiyo, alisema katika majumuisho yake kuwa kuna umuhimu wa serikali kulipatia shirika kiasi hicho cha fedha.

Alisema:" Sioni tatizo kwa serikali kutoa au kukopa Sh31.7 bilioni kuokoa shirika kubwa la umma kama hili, nafikiri kuna umuhimu wa kulipatia kiasi cha fedha kwa sasa."

NIC iko katika kipindi cha mageuzi baada ya kuwepo mvutano kati ya serikali na bunge, hasa tathmini ya mali ambayo awali ilikuwa Sh18 bilioni, lakini Kamati ya Fedha ikaikataa na kutaka ifanyike upya.

Tathmini mpya iliyoonyesha kuwa thamani ya mali za NIC ni Sh31.7 bilioni ilikubaliwa na mwezi Februari, Rais Jakaya Kikwete aliunda Kikosi Kazi kilicho chini ya Balozi Charles Mutalemwa kufanya mageuzi ya shirika hilo.

Hadi Februari wafanyakazi waliokuwa nje ya ajira wakati huo walilipwa malimbikizo ya mishahara yao kwa jumla ya Sh1.90 bilioni.

CHANZO: Mwananchi

MBONA MAMBO!?

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.