Showing posts with label Majipu. Show all posts
Showing posts with label Majipu. Show all posts

21 May 2016


Nianze makala hii kwa kumpongeza Rais John Magufuli kwa hatua aliyochukua jana ‘kumtumbua’ aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga, kwa kosa la kuingia Bungeni akiwa amelewa.

Kadhalika, ningependa kutumia fursa hii kumshukuru kwa kuwa kiongozi msikivu. Binafsi, ‘nilikomalia’ sana kuhusu uwaziri wa Kitangwa hasa kutokana na tuhuma kuwa ni mhusika katika skandali ya Lugumi (na tetesi kuwa alikuwa mlevi - japo sikuwahi kuongelea ishu hiyo ya ulevi kwa vile niliona kama suala binafsi, alimradi haliathiri utendaji wake wa kazi). 

Kwa ‘mtaani’ hatua hiyo ya Rais Magufuli inaweza kuonekana ni ya kawaida tu, yaani kiongozi aliyefanya uteuzi wa mtu flani, hatimaye kuamua kuteungua uteuzi huo. Lakini kwa hakika, hatua hiyo ya Rais Magufuli haikuwa rahisi. 

Kwa mujibu wa taarifa, Rais Magufuli na Kitwanga wamekuwa marafiki wa muda mrefu. Wajuzi wa mambo wanaeleza kuwa hata uamuzi wa kumteua Kitwanga kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi ulitokana na imani ya Rais Magufuli kwa rafiki yake huyo. Ikumbukwe kuwa wizara hiyo ni moja ya wizara nyeti ambazo kwa kiasi kikubwa hukabidhiwa kwa watu wanaoaminika mno kwa rais husika. 

Kuna kipande cha video kilichosambaa mtandaoni siku za nyuma ambacho kilikuwa kinamwonyesha Rais Magufuli kabla hajawa rais wala mgombea wa CCM, akiwa na Kitwanga, na katika maongezi yao, Kitwanga anasikika akimwambia Magufuli agombee urais (japo ni katika hali ya utani). 

Lakini pia inaelezwa kuwa hata kabla Rais Magufuli hajatangaza baraza lake la mawaziri, Kitwanga alikuwa akijigamba kuwa angepewa wizara nyeti, mara baada ya Magufuli kutangaza kabineti yake, na wizara nyeti ya mambo ya ndani ya nchi akapewa baada ya kutangazwa kabineti hiyo. 

Hata hivyo, suala hili la Kitwanga linapaswa kuamsha maswali kuhuru Idara yetu ya Usalama wa Taifa na utaratibu wa ‘kuwatafiti wateule watarajiwa wa Rais,’ kitu kinachofahamika kitaalam kama ‘vetting.’ Nina uhakika wa asilimia 100 kuwa ‘dossier’ (kabrasha maalum kuhusu mtu maalum) la Kitwanga lilipaswa kueleza bayana kuhusu tabia yake ya ulevi. Je ilikuwaje sio tu akateuliwa kuwa waziri bali pia kuteuliwa kuwa waziri katika wizara nyeti kabisa kwa usalama wa raia na nchi. Je kulikuwa na mapungufu huko Idara ya Usalama wa Taifa au walieleza hilo kabla Kitwanga hajateuliwa lakini likapuuzwa? Ni vigumu kuwa na uhakika wa kipi kilitokea. 

Kwa kuwa lengo ni kwenda mbele na si kunyoosheana vidole tu bila kutoa uushauri au kuleta ufumbuzi, binafsi ninashauri wahusika waangalie wapi walijikwaa, ili wasirudie tena kosa hilo. Vetting ya wateuliwa watarajiwa ni muhimu mno kwa sababu licha ya kuiingiza gharama serikali pale inapolazimu uteuzi husika kutenguliwa, pia inahatarisha usalama wa taifa (watu wanaotimuliwa madarakani ni rahisi kuwa recruited na maadui wa taifa ili 'kulipa kisasi').

Tukiweka kando mapungufu hayo, kitendo cha Dkt Magufuli kumtumbua Kitwanga kinapeleka ujumbe mzito kwa kila mtumishi wa serikali. Kwanza, kinaashiria kuwa Rais anafanyia kazi taarifa anazoletewa (maana hakuwepo Bungeni Dodoma wakati Kitwanga akiwa 'bwii' mjengoni. 

Lakini pia kitendo hicho kinaashiria kuwa mfumo wa mawasiliano ndani ya serikali umerejea kama wa zama za Nyerere, pasipo 'taarifa kuvuja' kabla ya kufika mahali stahili. Hali hii itapelekea watendaji wa serikali ikiwa ni pamoja na mawaziri kuwa makini zaidi kwani hawajui nani anawachunguza au nini kinaripotiwa kwa Rais kuhusu wao.

Tukiweka hilo kando, binafsi nimefarijika sana baada ya kusikia taarifa za Kitwanga ‘kutumbuliwa’ kwa sababu nilipiga kelele za kutosha kuhusu uongozi usioridhisha wa mheshimiwa huyo. Nilianza kitambo kuhoji kuhusu utendaji kazi wa waziri huyo.

Suala la kwanza ‘kumshikia bango’ lilikuwa kauli zake za utata kuhusu kupambana na biashara haramu ya madawa ya kulevya. Hili nililiandikia MAKALA HII. 







Baadaye, ikaibuka skandali ya Lugumi, na kwa hakika sikuchoka kupiga kelele, hususan kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter kama inavyoonekana hapa chini 



Sambamba na kelele hizo hatimaye niliamua kuandika MAKALA HII 


Ni matarajio yangu makubwa kuwa makala hii itamhamasisha kila msomaji kuwa na msimamo, na kisha kusimama imara katika msimamo huo, sambamba na kuhakikisha kuwa anachosimamia ni sahihi, na kuendelea kuupigania hadi mafanikio yapatikane. Sio kazi rahisi lakini mara nyingi vitu vizuri, au vinavyodumu, huwa havipatikani kirahisi. 

Mwaka 2006, niliandika MAKALA HII kuhusu suala la mkataba wa kufua umeme, uliopelekea skendo ya Richmond, na nikaendelea kupiga kelele hadi mwaka Februari 2008 baada ya mhusika mkuu katika skendo hiyo, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, kujiuzulu. Hata hivyo, ishu hiyo ilinigharimu mno kimaisha. 

Na hivi majuzi, nilijaribu ‘kuwashikia bango’ wahusika wa Mamlaka ya Mawasiliano TCRA, na nikawatwanga MAKALA hii. 


Siku chache baadaye, bosi wa taasisi hiyo akatumbuliwa. 


Na majuzi tu, Ubalozi wetu hapa Uingereza ulitaka kutufanyia 'uhuni' katika ziara ya Waziri Mkuu, ambapo awali kulikuwa na mpango wa kumkutanisha Waziri Mkuu na kundi dogo tu la Watanzania wanaoishi hapa. Kelele nilizoshiriki kuibua zilisaidia, na hatimaye mkutano huo wa Waziri Mkuu ulifanywa kuwa wa wazi kwa kila Mtanzania mkazi wa hapa kuhudhuria. Nimeelezea kwa kirefu kuhusu sakata hili katika MAKALA HII.

Sitaki kujisifu kuwa kelele zangu pekee ndio zinapelekea hatua kusudiwa kuchukuliwa. Hapana. Ninachojaribu kuonyesha ni ushiriki wangu katika harakati za kudai mabadiliko kwa kupitia maandishi, “kelele zetu” iwe hapa bloguni, kwenye mitandao ya kijamii au kwa njia ya makala. Pia, kwa kuwaeleza wasomaji kuhusu mafanikio ya 'kelele zetu' inasaidia kuhamaisha watu wengi zaidi kutambua umuhimu wa harakati kama hizi katika kuleta mabadiliko kusudiwa


Mara nyingi tunapopiga kelele hizo tunaishiwa kukebehiwa, kuonekana vimbelembele, tusio na vitu muhimu vya kufanya katika maisha yetu binafsi, na shutuma kama hizo. Lakini pindi kelele zetu zinapozaa matunda, walewale waliokuwa wakitukebehi huwa mstari wa mbele “kusaka sifa.” 

Kimsingi, harakati hizi sio za kusaka ujiko au madaraka. Ni kile nilichoeleza awali: kuwa na msimamo na kusimama thabiti katika msimamo huo hadi ufumbuzi wa tatizo husika upatikane.

Nimalizie makala hii kwa kumpongeza sana Rais Magufuli kwa ‘kumtumbua’ Kitwanga. Wanaohisi kuwa kutambuliwa huko ni ‘kuficha kombe’ la ishu ya Lugumi, ombi langu kwao ni wavute subira. 

Sakata la Lugumi sasa litachukua sura mpya, na tusishangae kusikia watu wakiburuzwa mahakamani hivi karibuni. Pia suala hili la kutambuliwa Kitwanga linaweza kumpa fursa Rais Magufuli fursa ya kuwatumbua angalau mawaziri mawili hivi ambao mwenendo wao umekuwa wa kusuasua. Fursa ya kuwatumbua inatokana na kutambuliwa kwa Kitwanga ambako kutamlazimu Rais kufanya ‘reshuffle’ ndogo.

14 May 2016


Jana nilibandika makala kuhusu manung'uniko ya Watanzania wengi wanaoishi hapa Uingereza ambao walikuwa hatarini kukosa fursa ya kuhudhuria mkutano na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ambaye yupo nchini hapa kikazi.

'Kelele' hizo zimezaa matunda, na leo Waziri Mkuu Majaliwa atakutana na Watanzania wote wanaoishi nchini humu wanaoweza kumudu kufika ubalozini London saa kumi alasiri. Awali, maofisa husika katika ubalozi huo walialika kundi dogo tu la Watanzania kuhudhuria mkutano huo, hatua iliyotafsiriwa na wengi kama ubaguzi na pengine jitihada za kuficha majipu yanayoukabili ubalozi huo.

Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu imeandikwa kidiplomasia, ambapo kwa upande mmoja imejitoa lawama ya kuhusika na maandalizi ya mkutano huo (na hakuna aliyemlaumu Waziri Mkuu au Ofisi yake bali lawama zilielekezwa kwa ubalozi) .



Kwa upande mwingine ni kama imekanusha 'madai ya watu' kuwa kuna watu maalum waliochaguliwa kuhudhuria mkutano huo (badala ya kuwa mkutano wa wazi kwa kila Mtanzania anayeishi hapa). Nimesema ni "lugha ya kidiplomasia" kwa sababu uthibitisho kwamba awali mpango wa ubalozi ulikuwa ni kama ulivyolalamikiwa jana , yaani kundi la watu kadhaa tu ndio wakutane na Waziri Mkuu, na uthibitisho huo unasikika katika audio hii ya mmoja wa maofisa wa ubalozi wetu anayetukebehi kwa kudai haki ya kukutana na Waziri Mkuu. Msikilize kwa kubonyeza play


Ni wazi kuwa laiti afisa ubalozi huyo ndio angekuwa na mamlaka ya mwisho basi ni wazi angebaki na hao watu wachache ambao awali ndio waliteuliwa kuhudhuria mkutano huo kana kwamba ni wa siri.

Badala ya kukiri kwamba ubalozi ulifanya makosa kuteua watu wachache tu, afisa huyo anaelekea kutuona kituko kwa kudai haki ya msingi ya kukutana na viongozi wetu wa kitaifa. Na badala ya kutumia fursa hiyo kuwaeleza Watanzania ratiba ya mkutano huo (tetesi zinasema utafanyika ubalozni mida ya saa 10 jioni) yeye ameamua kutunanga. Madaraka huwafanya baadhi ya wenzetu kujisahau sana.

Tukiweka kando lugha ya kidiplomasia ya Ofisa ya Waziri Mkuu na kebehi za afisa ubalozi, la muhimu ni kwamba sasa Watanzania wote wanaoishi hapa Uingereza wamepewa fursa ya kuhudhuria mkutano huo muhimu na Waziri Mkuu. Binafsi nimefarijika sana kwa sababu nilijitahidi kulipigia kelele suala hilo kwenye kundi la Whatsapp la jumuiya ya Watanzania ambayo ipo katika hatua za awali za kuundwa, japo mapokeo hayakuwa ya kuridhisha (watu wanahimiza umoja lakini walikalia kimya 'ubaguzi' uliotaka kufanywa na baadhi ya maafisa ubalozi wetu hapo London). 

"Kelele" zangu hazikutokana na mie kutopewa mwaliko, kwa sababu hata kama ningekuwa miongoni mwa watu hao takriban 40 walioalikwa bado nisingehudhuria (na leo sintohudhuria...kwa sababu zangu binafsi). Nilipiga kelele kwa maslahi ya walio wengi ambao pengine kwa namna moja au nyingine walishindwa kupiga kelele hizo wao wenyewe. Sie wengine tuna kumbi kama hii ya blogu au makala magazetini ambazo ni rahisi kupiga kelele na watawala kutusikia. Lakini si kila mtu ni blogs au mwandishi wa makala. Ni matumaini yangu kuwa 'kelele' hizi zitawahamasisha wengi kutambua kuwa 'kelele dhidi ya jambo lisilofaa' sio uchizi, kusaka umaarufu au ukorofi. Marehemu Kighoma Ali Malima aliwahi kutuusia kwamba "HAKI HAIPASWI KUOMBWA KAMA ZAWADI. HAKI HUDAIWA...KWA NGUVU IKIBIDI."

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.