Showing posts with label Maswali Magumu. Show all posts
Showing posts with label Maswali Magumu. Show all posts

17 Apr 2011



Chomoa, chomeka itainusuru CCM?

Ansbert Ngurumo

SAKATA la CCM kujivua gamba limezaa maswali mengi ambayo hayajajibiwa. Na limetusaidia kujua zaidi upeo wa watawala wetu, na uwezo wa kukabiliana na misukosuko ya ndani na nje ya chama tawala.

Na kwa kuwa wanapima upeo wa Watanzania kwa mizani ya upeo wao wenyewe, watawala wetu wamediriki kujitapa kwamba CCM imezaliwa upya. Wengine wanasema CCM imefufuka. Wamekosea!

Ni fursa kwa CCM ya Kikwete kujiuliza au kuulizwa. Kama CCM ya Julius Nyerere, Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa ilionekana imara, ni nani ameidhoofika CCM ya Kikwete?

Mtu mmoja alinieleza miezi mitatu iliyopita, kwamba Rais Jakaya Kikwete alisikika akimweleza rafiki yake mmoja wa Iringa kwamba anavyoona chama kimeanza kumfia mikononi, na hilo ni jambo analoogopa sana. Je, mabadiliko haya ya kuchomoa na kuchomeka sura ndiyo yanaweza kuinusuru CCM inayokufa?

Tumesikia wanajitapa kwamba wameondoa mafisadi kwenye Kamati Kuu, na sasa wanataka waliobaki kwenye Halmashauri Kuu na vyombo vingine vya chama wajiondoe wenyewe, la sivyo watafukuzwa! Jambo jema.

Lakini CCM wameanza lini kukiri kwamba chama chao ni cha mafisadi au kina mafisadi? Si hawa hawa ndio walibeza na kulaani kauli ya wapinzani, iliyotolewa na Dk. Willibrod Slaa Septemba 2007, Mwembeyanga, Dar es Salaam, alipotaja orodha ya mafisadi na kufafanua ufisadi wa kila mmoja wao?

Si ndio hawa waliotishia, na baadaye wakaogopa kumshitaki Dk. Slaa, lakini wakaendelea kuwatumia mawaziri na makada wengine kuzunguka mikoani kushambulia wapinzani kwa kile walichoita ‘uzushi?’

Hoja ya ufisadi si ndiyo ilimfanya Rais Kikwete awabeze na kuwakejeli wapinzani akidai kelele za mlango hazitamzuia mwenye nyumba (yeye) kulala?

CCM hii si ndiyo iliwatuma Yusuph Makamba, Kingunge Ngombale-Mwiru, Jaji Joseph Warioba, Sofia Simba na makada wengine kubeza na kudhihaki wapinzani na vyombo vya habari, wakidai wanaendekeza habari za ufisadi badala ya masuala ya maendeleo?

Kama Rais Kikwete na wenzake wanasema kuwa umefika wakati chama kiondokane na mafisadi, basi wamethibitisha kwamba Dk. Slaa na wenzake walikuwa sahihi. Sasa tuwaamini CCM au akina Dk. Slaa?

Pili, dhana hii ya kujivua gamba bado ni tata hata kwa wenyewe wanaoipigia debe. Mwenyekiti mwenyewe aliyeianzisha alidhani CCM ina gamba moja tu inalopaswa kujivua; na akadhani inatosha tu kuvua gamba. Inasikitisha kwamba yeye anaishia hapo, lakini hata sisi tusio wana CCM tunajua kuwa CCM haikuhitaji kuvua gamba, bali kuwa na moyo mpya.

Lakini wale waliopenda kuendelea kuchambua hoja ya gamba wameshaorodhesha magamba ya CCM. Na wengine wamesisitiza kwamba Rais Kikwete, kwa staili yake ya uongozi, na baada ya kutathimni alikokitoa na alikokifikisha chama, naye ni gamba.

Kwa bahati mbaya, inavyoonekana, hata watawala wenyewe bado hawajajua idadi, na aina ya magamba wanayopaswa kukivua chama chao. Vile vile, hawajajua kwamba hata kama wangefanikiwa kuyatambua na kuyavua mgamba hayo, bado chama chao hakitaweza kuwa kipya.

Tatu, na hili ndilo la msingi kwangu, hivi watawala wanadhani kwamba nyoka anapojivua gamba anabadilika na kuwa mjusi au kinyonga?

Tunaona, na tunasema wazi kwamba CCM ya Kikwete, yenye gamba na isiyo na gamba, ni ile ile. Wanachofanya sasa ni kujaribu (na kufanikiwa kwa sehemu kubwa) kuwafukuza ’wabaya wao’ wa sasa na kuingiza marafiki wapya. Na bahati mbaya, ni sura zile zile tulizozizoea, tunazozifahamu, na ambazo tunapata shida kuzitenganisha na ufisadi uliowakumba kina Yusuph Makamba, Rostam Aziz, Andrew Chenge na wenzao.

Kikubwa zaidi ni mamlaka ya kimaadili yanayotumika kuwafukuza wengine na kuingiza wengine. Maana kama tunaendelea kukuza na kusisitiza hoja ya Mwembeyanga, waliotajwa kwenye orodha ya mafisadi ni hawa hapa:

1. Daudi Balali
2. Andrew Chenge
3. Basil Mramba
4. Gray Mgonja
5. Patrick Rutabanzibwa
6. Nazir Karamagi
7. Nimrod Mkono
8. Rostam Aziz
9. Edward Lowassa
10. Benjamin Mkapa
11. Jakaya Kikwete

Chama kinachojivua gamba, kwa mfano, kitajitapaje kwamba kimeondokana na mafisadi, wakati hata mwenyekiti mwenyewe yumo kwenye orodha?

Si hilo tu. Kwa misingi ya kikatiba, kihistoria na kitamadumi, CCM inaongozwa na mwenyekiti. Na hii ndiyo asili ya kaulimbiu ya siku nyingi ya CCM ya ‘zidumu fikra za mwenyekiti.’

Kwa mantiki hiyo, chama kinapofanikiwa au kinapokwama, mtu wa kwanza ambaye wana CCM wanapaswa kumhoji si katibu mkuu (maana utendaji wake unasimamiwa), bali mwenyekiti.

Sekretariti na Kamati Kuu ni zao la mwenyekiti. Ni mikono ya kazi anayotumia kuendesha chama. Ni kweli, Yusuph Makamba, kwa elimu na upeo wake, alibebeshwa mzigo mzito. Lakini ndiye huyo ambaye mwenyekiti aliridhika naye kwa miaka mitano.

Kwa hiyo, mwenyekiti ndiye aliyepaswa kubeba udhaifu wa katibu na chama kwa ujumla. Maana wana CCM walipohoji na kubeza uteuzi wa Makamba mwaka 2006 kurithi nafasi ya Philip Mangula, mwenyekiti hakujali.

Hata ilipopatikana fursa ya kubadilisha uongozi wa chama hapa katikati, Rais Kikwete aliridhika na utendaji wa Makamba. Huyu huyu hawezi kuibuka leo na kusema Makamba na sekretarieti yake hawajamsaidia kazi.

Nionavyo mimi, yaliyomkuta Makamba na Sekretarieti na Kamati Kuu yake ni sawa na yaliyomkumba Lowassa na Baraza la Mawaziri lililokuwa chini yake mwaka 2008.

Uamuzi wa kuondokana na Lowassa ilikuwa njia pekee ya kumnusuru Kikwete na anguko la kisiasa akiwa madarakani, kwa maana kashfa yenyewe iliyomsomba Lowassa iliwahusu wote.

Na hili la Makamba limeharakishwa na vuguvugu la mapinduzi ya ndani, baada ya mwenyekiti kuletewa taarifa kwamba kuna watu wananadi uenyekiti wake kwa maelezo kuwa ameshindwa kuongoza vema chama. Walitaka (na bado wanataka) abaki na urais, aachie uenyekiti.

Wanajua kuwa kwa utamaduni wao, mwenyekiti ndiye kiongozi wa chama. Anakotaka chama kiende, ndiko kinakokwenda. Na wandhani kuwa wakipata mwenyekiti mzuri watakuwa na chama kizuri.

Katika mazingira haya, njia pekee ya mwenyekiti kujinusuru ilikuwa kuwashughulikia walio chini yake ili ajipange upya, abadili hoja, na apate pa kuning’iniza propaganda za CCM mpya.

Na kwa maana hiyo, kujiuzulu kwa wajumbe wa Kamati Kuu na Sekretarieti (kwa shinikizo la mwenyekiti) ilikuwa faraja kwake binafsi si kwa CCM. Na ndiyo maana sisi wengine tunakataa kukubaliana na propaganda za akina Nape Nnauye eti chama kimezaliwa upya!

Nne, upya wa chama hauletwei na upya wa sura za wajumbe. Kama muono wa chama ni ule ule; itikadi ni ile il; sera zake ni zile zile; i wapi CCM mpya inayozungumzwa?

Bahati nzuri Katibu Mkuu mwenyewe ameshakiri kwamba hana jipya, bali anataka kurejesha na kusimamia misingi ile iliyokiasisi chama. Mwisho wa fikra!

Zaidi ya yote, kama huyu anayeteua, kupendekeza na kufukuza wajumbe wa kamati ndiye aliyesimamia waliopita, amepata wapi njozi mpya za kusimamia wapya kwa ufanisi? Au ni yale yale tuliyozoea kuona kila anapoteua baraza la mawaziri? Kama ndivyo, je, udhaifu wa uteuzi na utendaji tunaoshuhudia serikalini hautaendelezwa kwenye chama?

Kumwondoa Makamba na kumwingiza Mukama ni mabadiliko ya mwelekeo? Kumwondoa John Chiligati na kumwingiza Nape Nnauye ni kukipa chama dira mpya?

Kumwondoa Amosi Makala na kumwingiza Mwigulu Nchemba ni kukipa chama moyo mpya? Kumwondoa Bernard Membe na kumwingiza January Makamba ni kukipa chama katiba mpya? Kurejeshwa kwa Zakia Meghji kunakipa chama itikadi mpya?

Lililo wazi ni kwamba CCM ni chama kinacho kufa. Kina sura zile zile na mawazo yale yale. Na kwa sababu wameishiwa mapya, wamebaki katika siasa za kuwindana na kumalizana. Wanachomoa hawa na kuchomeka wale. Inatosha kuwanusuru?


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.