Showing posts with label NDULU. Show all posts
Showing posts with label NDULU. Show all posts

13 Feb 2011



Kumekuwa na tetesi za muda mrefu kuwa hali ya uchumi wa Tanzania ni mbaya.Hata hivyo,kama ilivyozoeleka,wahusika serikalini wameendelea kuwanyima Watanzania haki yao ya msingi ya kufahamishwa hali ya uchumi wa taifa lao. 

Hivi karibuni Gavana wa Benki Kuu,Profesa Benno Ndulu,alizungumza na waandishi wa habari kuhusu ubora wa noti mpya.Licha ya kuonekana kufahamu kuwa wananchi hawaridhishwi na kiwango duni cha noti hizo,Gavana Ndulu alizitetea kwa nguvu zote.Akemee ili ifahamike kuwa 'zimechakachuliwa'?

Akiichambua hali ya uchumi, gavana huyo alisema kwa sasa hali ya uchumi ni nzuri na kwamba nchi ina uwezo wa kulipa huduma kwa miezi sita bila kutegemea sehemu yoyote.Lakini katika kile kinachoweza kiashirikia kiwa kauli hiyo ilikuwa ya kisiasa zaidi kuliko ya kitaalamu,Gavana alidai kuwa mwenye dhamana ya kueleza athari za mgao wa umeme kwa uchumi ni Waziri wa Nishati na Madini.Huku sio tu kukwepa majukumu bali mwendelezo wa danadana za kibabaishaji zinazoeleka kuunda mfumo wa utendaji wa viongozi wengi wa taasisi za umma.Na kwa vile 'Mteuzi Mkuu' Serikalini,yaani Rais,anaonekana kama yupo usingizini kubaini mapungufu ya baadhi ya watendaji aliowateua,ni dhahiri utendaji kwa mfumo wa 'bora liende' utaendelea kuwepo kwa muda mrefu.

Kwa hapa Uingereza,Benki Kuu imekuwa ikitoa taarifa kuhusu viwango vya riba kila mwezi.Taarifa hiyo huambatana na maelezo ya kutosha kuhusu mwenendo wa uchumi wa nchi hii.Na kila baada ya miezi michache,ofisi ya takwimu nayo hutoa taarifa yenye takwimu zinzoashiria kupanda,kutuama au kushuka kwa uchumi.Kadhalika,vielekezo muhimu kuhusu uchumi wa nchi kama vile idadi ya wasio na ajira,mfumuko wa bei,wastani wa thamani ya sarafu,nk vimekuwa vikiwekwa wazi kwa umma.

Na huko nchini Marekani,Serikali ya Rais Barack Obama,imekuwa ikitoa taarifa za hali ya uchumi wa nchi hiyo mara kwa mara,hata kama kufanya hivyo kufanya hivyo kunaathiri namna wananchi wanavyoridhishwa au kutoridhishwa na serikali hiyo.Huku sio tu kutambua haki ya wananchi kuhabarishwa bali pia kuelewa kuwa kuficha ukweli kuhusu hali ya uchumi hakuwezi kuufanya uchumi husika kuboreka.

Na ndio maana licha ya kuwaficha Watanzania kuhusu hali ya uchumi wa nchi yao,sambamba na kauli mbalimbali za kisiasa kuwa 'hali cha uchumi ni poa' gazeti la Mwananchi katika toleo lake la leo linaripoti kuwa Serikali imelazimika kufumua bajeti yake ya mwaka wa fedha 2010/11 kwa kupunguza matumizi ya Wizara ili kufidia upungufu wa Sh670.4 bilioni zilizotegemewa kupatikana kutokana na makusanyo ya kodi katika mwaka huu wa fedha.

Hata hivyo,gazeti hilo lilipomtaka Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustaffa Mkullo, kuihusina na hali hiyo alisema taarifa ya hali ya uchumi wa nchi alishaitoa hivi karibuni kwenye chombo kimoja nchini, hivyo hahitaji kuitoa tena."Nilitoa taarifa kwa wenzenu wa gazeti (sio Mwananchi) sasa siwezi tena kuirudia," alisema.Ni dhahiri kuwa laiti hali ingekuwa nzuri,Mkulo asingefanya dharau hiyo hasa kwa vile viongozi dhaifu huwa wepesi sana kumwaga hadharani habari njema wakiamini zitawaletea sifa.

Wakati Watanzania wanasubiri 'waletewe' Katiba mpya,ni muhimu kuangalia tatizo hili la ukandamizwaji wa makusudi wa haki ya kuhabarishwa.Nchi mbalimbali zina sheria zinazoilazimisha Serikali na taasisi za umma kutoa au kuruhusu upatikanaji wa taarifa.Japo tunafahamu kuwa taarifa nyingi nchini 'zinachakachuliwa' kwa minajli ya kufisadi,kudanganya wapiga kura,kughilibu wafadhili,au sehemu tu ya utamaduni wa kutowajibika,uwepo wa sheria ya Haki ya Habari (Freedom of Information act) utakomesha tabia kama hiyo ya dharau Waziri Mkulo kupuuza kuwaeleza Watanzania kuhusu hali ya uchumi wa nchi yao

17 Jan 2008


Gavana mpya wa Benki Kuu,Profesa Benno Ndulu,amefanya mabadiliko kadhaa katika uongozi wa benki hiyo.Katika mabadiliko hayo,Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala (DAP) wa B.O.T,AMATUS LIYUMBA (pichani) ameondolewa katika wadhifa huo.Habari kamili soma hapa.
(Picha hii ya zamani ya Liyumba ni alipokuwa Mkuu wa Chuo cha BoT 1993-2000)

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.