Showing posts with label PUTIN. Show all posts
Showing posts with label PUTIN. Show all posts

29 Jan 2015

AlexanderLitvinenko.jpg
Ushushushu unaendelea kuwa ni moja ya taaluma hatari kabisa kwa maana ya kutembea na roho mkononi pindi mambo yakienda mrama. Tatizo kubwa la ushushushu sio kutoka kwa maadui wa nje (kwa maana ya taifa la nje au maadui wasio wa kitaifa- non-state actors) bali pia hata maadui wa ndani. Kiasili, migogoro au kukosana ni sehemu ya 'kawaida' katika maisha yetu wanadamu.

Mie katika familia yetu tumejaaliwa kuwa na mapacha. Vitinda mimba katika familia yetu ni Kulwa na Doto. Hawa walipishana kuzaliwa kwa dakika chache tu, na wamefanana mno kiasi kwamba ninapokutana nao baada ya kupotean kidogo tu inabidi niwaulize yupi ni Kulwa na yupi ni Doto. Pamoja na hali hiyo, kuna nyakati hutofautiana na hata kugombana. 

Kwa mantiki hiyo, si suala la ajabu kwa mwajiriwa kukosana na mwajiriwa wake. Wakati kukosana na mwajiri wako katika taaluma nyingine kwaweza kupelekea kushushwa cheo, kuhamishwa au kupoteza ajira, kwa ushushushu hali ni tofauti kabisa. Kutibuana na mwajiri kwaweza kupelekea kifo, kama stori hii hapa chini inavyotanabaisha.

Ukisoma au kusikia balaa lililomwandama Alexander Litvinenko (pichani juu) hadi kifo chake, waweza kudhani ni simulizi kutoka kwenye filamu au riwaya flani. Litvinenko aliwa shushushu wa shirika la ushushushu la Russia, FSB, katika kitendo cha kubaliana na uhalifu mkubwa (organised crime). Kabla ya kuwa shushushu, Litvinenko alikuwa mwanajeshi ambapo alipanda cheo hadi kufikia ngazi ya ukamanda wa platuni.

Mwaka 1986, Litvinenko alianza kuingia kwenye taaluma ya ushushushu baada ya kuwa 'recruited' kuwa mtoa habari (informant) Shirika la zamani la ushushushu la Russia KGB, katika kitengo cha kupambana na ujasusi (counterintelligence). Miaka miwili baadaye, Litvinenko alihamishiwa rasmi KGB kwenye Kurugenzi Kuu ya Tatu iliyokuwa inahusika na military counterintelligence. Mwaka huohuo, baada ya kuhudhuria mafunzo ya ushushushu, Litvinenko akawa shushushu kamili katika eneo la kupambana na ujasusi hadi mwaka 1991, ambapo alipandishwa cheo na kuingia katika Federal Counterintelligence Service, shirika la ushushushu baada ya KGB, ambalo lilidumu kutoka mwaka 1991 hadi 1995lilipoundwa upya kuwa shirika la sasa la ushushushu la Russia yaani FSB. Shushushu huyo alipangiwa kitengo kilichohusika na kukabiliana na ugaidi sambamba na kujipenyeza (infiltration) kwenye makundi ya uhalifu mkubwa. Kadhalika, alikuwa na jukumu la kufuatilia 'maeneo ya moto' (hot spots), yaani maeneo nyeti ndani ya Russia na katika nchi znyingine zilizokuwa ndani ya USSR. Wakati wa vita ya Chechnya, Litvinenko alifanikiwa kupandikiza mashushushu kadhaa ndani ya Chechnya.

Mwaka 1994, Litvitenko alikutana na mmoja wa waliokuwa matajiri wakubwa nchini Russia, Boris Berezovsky (pichani chini) alipokuwa anafuatilia jaribio la mauaji dhidi ya tajiri huyo.


 Hatimaye akaanza kufanya kazi za pembeni kwa ajili ya Boris, na baadaye akawa msimamizi mkuu wa ulinzi wa kibopa huyo. Ofkoz 'ajira' hiyo ya Litvitenko kwa tajiri huyo ilikuwa sio halali lakini dola iliwavumilia hasa ikizingatiwa kuwa mishahara ya mashushushu kama yeye ilikuwa kiduchu.

Mwaka 1997 shushushu huyo alipandishwa cheo na kuingia Kurugenzi ya Uchambuzi na Ukandamizaji wa makundi ya uhalifu mkubwa, akiwa na wadhifa wa mtendaji mwandamizi na naibu mkuu wa Idara ya Saba.

Mwishoni mwa mwaka huo, shushushu huyo alitoa tuhuma nzito kuwa alipewa amri ya kumuua Boris.Mwaka uliofuata, Boris alimtambulisha Litvinenko kwa Vladmir Putin, rais wa sasa wa Russia lakini wakati huo akiwa shushushu mwandamizi wa FSB.
Putin akiwa amezungukwa na walinzi wake

Tatizo ni kwamba Litvinenko alikuwa akipeleleza ufisadi ambao Putin anadaiwa kuwa mhusika. Mwaka huohuo, shushushu huyo na baadhi ya wenzake wallijitokeza hadharani kueleza kuhusu njama za kutaka kumuuwa tajiri Boris.Baada ya tukio hilo, shushushu huyo alitimuliwa FSB na Putin alitanabaisha kuwa ndiye aliyetoa uamuzi huo.

Oktoba 2000, Litvinenko alitoroka Russia na familia yake na kwend Uturuki ambako aliomba hifadhi ya ukimbizi katika Ubalozi wa Marekani jijini Ankara lakini maombi yake yalikataliwa. Inaaminika kuwa kukataliwa huko kulitokana na hofu kuwa kuyakubali maombi hayo kungezua matatizo kati ya Marekani na Russia. Mwaka huohuo,shushushu huyo alinunua tiketi ya kusafiri kwa ndege kutoka Ankara kwenda Moscow kupitia London, Uingereza. Alipofika uwanja wa ndege wa Heatrhow kusbiri ndege ya kwenda Moscow, shushushu huyo aliomba hifadhi ya ukimbizi wa kisiasa, ambapo maombi yake yalikubaliwa mwaka mmoja baadaye, si kwa sababu ya uelewa wake wa mambo ya ushushushu bali kwa sababu za kibinaadamu (humanitarian grounds).

Wakati akiwa London, Litivnenko alijihusisha na uandishi wa habari, sambamba na kumsapoti tajiri Boris (aliyekimbilia Uingereza) katika mapambano ya kiharakati dhidi ya utawala wa Putin. Oktoba 2006, shushushu huyo alipatiwa uraia wa Uingereza.

Wakati huohuo, gazeti la Independent la hapa, liliripoti kuwa Litvinenko alikuwa akitumia na shirika la ujasusi la Uingereza, MI6 kutokana na ushahidi wa malipo yaliyokuwa yakifanywa na shirika hilo kwa shushushu huyo.

Makao makuu ya shirika la ujasusi la Uingereza MI6 kwenye kingo za Mto Thames, eneo la Vauxhall, jijini London


Mwaka 2007, gazeti moja la Poland lilidai kuwa picha ya Litvinenko ilikuwa ikitumika kwenye mazoezi ya kulenga shabaha (kama huelewi, hiyo ni ishara ya kuwindwa kuuawa). Kabla ya hapo, mwaka 2002, shushushu mmoja wa FSB, Mikhail Trepashkin, alimwonya Litvinenko kuwa kulikuwa na mpango wa kumuuwa uliokuwa ukiandaliwa na FSB. Mwaka huohuo, shushushu huyo alihukumiwa kifungo cha miaka mitatu jela kwa tuhuma za rushwa, japo alikuwa nje ya Russia.
50pxx50pxpx
Nembo ya Shirika la Ushushushu la Russia FSB

Hata hivyo, wakati flani, wasifu wa shushushu huyo ulichafuka baada ya kupatikana taarifa kuwa alikuwa akiwatishia kuwaumbua matajiri kadhaa wa Russia kuhusu uhusika wao kwenye uhalifu mkubwa, na kudai pauni 10,000 kila mara ili asiwaumbue.

Wakati wa uhai wake, shushushu huyo alitoa tuhuma kadhaa dhidi ya Putin, Russia na mwajiri wake wa zamani FSB. Miongoni mwa tuhuma hjizo ni Russia kuhusika na mashambulizi katika bunge la Armenia yaliyopelekea kifo cha Waziri Mkuu wa nchi hiyo Vazgen Sargsyan, FSB kufanya mauaji nchi Russia na kuwalaumu magaidi wa nje ili kupata uhalali wa kufanya ubabe nje ya nchi hiyo, mdai ya uhusiano kati ya Russia na Al-Qaeda, nk.

Novemba 2006, Litvinenko aliugua ghafla na kulazwa. Baadaye, vipimo vilibaini kuwa alidhuriwa kwa kemikali ya sumu ya Radionuclide Polonium-210. 

Litvinenko akiwa hospitalini jijini London baada ya kudhuriwa na sumu

Katika mahojiano, shushushu huyo alieleza kuwa alikutana na mashushushu wawili wa FSB Dmitry Kovtun na Andrei Lugovoi.Japo wote wawili walikanusha kumdhuru shushushu mwenzao, nyaraka zilizovuja za Ubalozi wa Marekani zinaeleza kuwa chembechembe za kemikali iliyomdhuru Litvinenko zilikutwa kwenye gari alilotumia Kovtun huko Ujerumani.

Dmitry Kovtun, right, with Andrei Lugovoi in 2007. Both deny murdering Alexander Litvinenko
Andrei Lugovoy (kushoto) na Dmitr Kovtun 

Baadaye mwezi huo, Litvinenko alifariki baada ya moyo wake kushindwa kufanya kazi kutokana na sumu iliyomdhuru. Kabla ya kifo chake, shushushu huyo aliandika taarifa iliyoeleza ameuawa.

Juzi, taarifa ya uchunguzi wa kifo chake ilieleza kuwa njia iliyotumika kumuuwa ilikuwa ni ya hatari zaidi kutokea katika Nchi za Magharibi.

Dokta Nathaniel Cary alieleza kuwa kifo cha shushushu huyo mwili wake ulidhurika vibaya mno kabla ya kifo chake kiasi kwamba ililazimu awekwe katika wodi maalum amapo wagonjwa hutengwa kwa ajili ya uchunguzi wa hali ya juu. Alisema kuwa shushushu huyo aliuawa kwa mionzi ya sumu. Kifo chake kilitokea takriban wiki tatu baada ya kunywa chai ambayo baadaye ilifahamika kuwa ilinyunyiziwa sumu ya Polonium.

Dokta Cary alieleza kuwa yye na timu yake walilazimika kuvaa suti mbili za kujikinga (kama zile za matabibu wa Ebola) ambazo ziliwekwa hewa ndanikupitia mirija maalum ili kukwepa athari za sumu husika. Alisema, "uchunguzi huo wa maiti ulikuwa ni usio wa kawaida kabisa katika historia ya nchi za Magharibi"

Natumaini habari hii imekusaidia msomaji kutambua hatari zinazowakabili mashushushu katika utendaji kazi wao, na hasa pale 'wanapotibuana' na aidha waajiri wao au watawala.





12 Sept 2007

Asalam aleykum,

Katika makala yangu iliyopita,nilizungumzia kuhusu kile ambacho wachambuzi wa siasa za kimataifa wanakiona kama kurejea kwa kasi kwa mbio za silaha (arms race) zenye uwezo mkubwa na wa kisasa zaidi kuliko hapo awali au sasa.Nchi za Magharibi zikiongozwa na Marekani zimeonekana kuguswa na namna Russia inavyoongeza kasi katika teknolojia na uzalishaji wa silaha za kisasa.Muda mfupi kabla ya kuandaa makala hii,nimeona taarifa moja inayoeleza kuwa Russia imefanikiwa kufanya majaribio ya kile inachokiita “Baba wa Mabomu Yote” (Father of all Bombs).Teknolojia hiyo mpya inaelezwa kuwa na uwezo mara nne zaidi ya ile ya Marekani inayojulikana kama “GBU-43 Massive Ordnance Air Blast” (MOAB) au “Mother of all Bombs” (yaani “Mama wa Mabomu Yote”) ambayo ilifanyiwa majaribio yenye mafanikio mwaka 2003.Tofauti na teknolojia ya awali ya mabomu,hilo la kisasa la Russia ni la “thermobaric,” yaani linatumia oksijeni iliyopo hewani (atmospheric oxygen) kusababisha mlipuko badala ya kutumia kemikali nyingine (oxidizing agent) kuleta matokeo hayo (mlipuko).Silaha za ki-“thermobaric” zina tabia ya kutoa nishati kubwa zaidi kuliko zile zisizotumia teknolojia hiyo,na inaelezwa kwamba bomu hilo jipya la Russia lina uwezo wa kuteketeza kabisa maisha katika eneo mzunguko la maili nne.

Kinachochochea mbio za silaha ni sawa na kile wanafalsafa wanachokiita “domino effect” yaani badiliko (change) moja linapelekea badiliko jingine jirani,nalo linapekea badiliko jingine,na jingine kwa jingine,na kadhalika.Yaani ni kama kugongwa gari la kwanza kwenye foleni ndefu ambapo la kwanza litaligonga la pili,la pili litaligonga la tatu,na kadhalika,na kadhalika.Kwa Russia kutambulisha mafanikio yake hayo,ni dhahiri kwamba Wamarekani nao watakuna vichwa ili waibuke na teknolojia kali zaidi ya hiyo ya Russia (pengine wataamua kuiita “babu wa mabomu yote” maana tayari tuna “baba” na “mama,” na si ajabu Russia nao watajibu mapigo kwa kuja na “bibi wa mabomu yote”).Wajuzi wa mambo wanadai kuwa miongoni mwa mambo yanayoichochea Russia kuelekeza nguvu zake kwenye uboreshaji wa teknolojia ya silaha ni faida kubwa inayopata nchi hiyo kwenye biashara ya mafuta na gesi,na ukweli kwamba Rais Putin alikuwa shushushu mwandamizi ndani ya shirika la kijasusi la uliokuwa Muungano wa Jamuhuri za Kisovieti (USSR) ambapo shirika hilo lilikuwa sehemu muhimu ya maendeleo ya teknolojia ya silaha.
Habari nyingine “nyepesi” kutoka Russia zinasema kwamba jiji la Ulyanovsk nchini humo limetoa “off” kwa wafanyakazi wote ili wapate fursa ya kufanya tendo la ndoa katika maadhimisho ya “Siku ya Kutunga Mimba jijini Ulyanovsk” (the Day of Conception in Ulyanovsk).Ruhusa hiyo ya mapumziko imetolewa kama sehemu ya mpango wa manispaa ya jiji hilo ujulikanao kama “Give Birth to a Patriot” (Zaa Mzalendo) ambapo watakaofanikiwa kudunga au kudungwa wanaweza kuibuka na zawadi ya gari,fedha au friji.Jiji hilo ndipo alipozaliwa Vladmir Lennin, na mpango huo wa kuhamasisha uzazi ni sehemu ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwa Lenin mwezi huu.Washindi wanatarajiwa kupatikana kwa kuzingatia heshima ya ndoa yao pamoja na sifa bora kama wazazi,na watapatikana kutokana na maamuzi ya jopo la majaji.Mambo hayo!!

Kabla ya kugeukia masuala ya huko nyumbani,ngoja nizungumzie suala moja ambalo mie binafsi linanigusa.Nilipokuwa Mlimani (UDSM) nilibahatika kuchukua somo liitwalo “Gender and Family Relations” (yaani Jinsia na Mahusiano ya familia).Naomba kukiri kwamba kabla ya hapo,sikuwa na uelewa wa kutosha kuhusu nafasi ya mwanamke katika jamii na picha nzima ya usawa wa kijinsia katika jamii mbalimbali.Sasa majuzi nilisoma gazeti la Guardian la hapa Uingereza na kukutana na habari isemayo kwamba serikali (ya hapa) ina mpango wa kuwachukulia hatua wanaume wanaonunua huduma ya ngono.Kimsingi,huduma nyingi,ikiwemo ngono,huhusisha mtoaji huduma na mpokeaji huduma,lakini katika dunia yetu ambayo tumezowea kuyaona makosa ya wanawake pekee ilhali yetu wanaume yakionekana ni ya “ya kishujaa,” suala la ukahaba limeendelea kwa kiasi kikubwa kuwa kosa la wanawake wanaojihusisha na biashara hiyo kuliko wateja wao ambao ni wanaume (hapa sizungumzii ukahaba kati ya watu wa jinsia moja).Neno “malaya” ni maarufu zaidi kuliko neno “fuska” na baadhi ya wachambuzi wa mahusiano ya jamii wanadai hiyo inasababishwa na tabia ya kuona matendo hasi (negative) ya mwanamke kuwa mabaya zaidi ya yale hasi ya mwanaume.Hata linapokuja suala la nyumba ndogo,tunashuhudia kuwa ni rahisi kwa mwanaume kuwa nazo hata 10 kama ana uwezo wa kuzimudu lakini mwanamke akijaribu hilo basi muda si mrefu anaweza kujikuta anafungashiwa virago vyake.Nchi za Magharibi zimepiga hatua flani katika kuleta usawa wa kijinsia,na miongoni mwa mitihani mikubwa katika eneo hilo ni ugombea (candidacy) wa Hillary Clinton kwenye kinyang’anyiro cha kuteuliwa kuwa mgombea urais wa Marekani kwa tiketi ya chama cha Democrat.Na mshawasha zaidi unaeletwa na mgombea mwingine kutoka jamii ambayo hadi sasa bado inaonekana ni ya kuongozwa zaidi badala ya kuongeza,yaani watu weusi (Blacks).Historia inasubiri kuandikwa iwapo Hillary atafanikiwa kuwa mwanamke wa kwanza kuwa rais wa Marekani,au Barack Obama atafanikiwa kuwa Mweusi wa kwanza kuwa rais.Bibi,mama na dada zetu wanastahili pongezi (au hukumu) sawa na sie akina kaka,baba na babu.

Sasa mambo ya huko nyumbani.Nilipigwa na butwaa niliposoma habari katika gazeti moja la nyumbani kuwa huko Mwanza kampeni za kugombea uongozi wa CCM ziligeuka kuwa uwanja wa vita pale washabiki wa kambi za wagombea flani walipoamua “kufanyiana kweli” na kutupiana mawe.Sijui wangapi walijeruhiwa katika patashika hiyo lakini nachoshindwa kuelewa ni namna kila raslimali,ikiwemo vurugu,inavyotumika kutafuta uongozi wa kisiasa.Hivi kuna nini huko kwenye uongozi hadi watu watake kutoana roho?Yaani ukereketwa umekolea namna hiyo hadi watu wawe tayari kuweka rehani usalama wao kwa ajili ya mgombea flani?Cha kusikitisha ni kwamba si ajabu wapambe hawa hawa ndio watakuwa wa kwanza kulalamika kuwa mgombea wao “hafai” pale atapowatelekeza baada ya kupata anachohitaji (uongozi).Pasipo busara za haraka kutumika tunaweza kujiwekea katika mahali pabaya sana kama tutawaruhusu baadhi ya watu kuhatarisha amani kwa vile tu wanataka kupata uongozi.

Nimesoma pia ushauri wa aliyekuwa Katibu Mkuu wa CCM,Philip Mangula,ambaye baada ya kubwagwa huko Iringa alitahadharisha kwamba kuna wakati itafika uongozi wa chama hicho utagombewa kwa mfumo wa tenda (bid) na “bidder” mkubwa ndiye atakayeibuka kidedea.Pengine ana hoja ya msingi hapo,lakini inaweza kufunikwa na ukweli kwamba haya anayoyaona sasa yamekuwa yakitokea kwa muda mrefu,na kipindi hicho alikuwa katika nafasi nzuri zaidi ya sio tu kukosoa bali hata kukomesha matumizi ya “takrima” kwenye kusaka uongozi.Hata wazo lake kwamba ni vema kwa wanachama wa CCM wenye madaraka mengine (kama ubunge au uwaziri) wakatoa mwanya kwa wale wasio na madaraka (japo sio kosa,si ajabu baada ya uchaguzi huu kumkuta mtu akiwa na vyeo zaidi vitano) mawazo hayo yangekuwa na “mwangwi” mkubwa zaidi iwapo yangetolewa katika kipindi ambacho Mangula alikuwa madarakani.Yayumkinika kusema kuwa ni vigumu kurekebisha mapishi pindi ukiwa nje ya jiko,na majaribio ya kufanya hivyo nje ya jiko yanaweza kutafsiriwa tofauti na baadhi ya watu.

Na huko Morogoro,baada ya kushindwa kwenye uchaguzi wa miongoni mwa nafasi katika mkoa huo,Waziri Ngasongwa nae “aliwatolea macho” TAKUKURU kwa kile alichodai walishindwa kuzuwia baadhi ya wagombea kutoa “takrima” kwa wapiga kura.Swali pana zaidi ni je waziri anadhani taasisi hiyo ilishindwa (kwa mujibu wake) kutekeleza majukumu yake kwa vile ni sehemu ya mapungufu yake ya kila siku au ni katika tukio hilo tu?Iwapo jibu ni hilo la pili basi wapo wanaoweza kuhisi kuwa waziri ameweza kuona matatizo hayo kwa vile tu yamemgusa yeye binafsi. “Bottom line” ni kwamba iwapo mlolongo wa vimbwanga vinavyoendelea kwenye uchaguzi wa CCM vitachukuliwa kuwa ni mambo ya kawaida tu basi tunaweza kufika mahala tukajilaumu huku tukisema “laiti tungejua wakati ule…”Bahati mbaya,kwa wakati huo tutakuwa tumechelewa kuweza kufanya mabadiliko yoyote ya msingi.Ushauri huu sio wa kupandikiza chuki bali ni kwa ajili ya hatma ya taifa letu kwa manufaa yetu sasa na kwa vizazi vijavyo.

Neno la mwisho kabisa ni kuungana na wapenzi na mashabiki wa msanii maarufu anti Shenaz ambaye alikutana na mauti kwenye ajali ya basi huko Mbeya.Kwa tunaomfahamu,dada huyo alikuwa akipendezesha kila shughuli aliyokuwepo.Na tofauti na umaarufu wake,alikuwa mcheshi na asiye na chembe ya dharau.Mungu airehemu roho ya marehemu,Amina.

Alamsiki


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.