Showing posts with label RASHID OTHMAN. Show all posts
Showing posts with label RASHID OTHMAN. Show all posts

27 Aug 2016

Tarehe 24 mwezi huu, Rais Dokta John Magufuli alimteua Dokta Modestus Kipilimba kuwa Mkurugenzi Mkuu (DGIS) wa Idara ya Usalama wa Taifa (TISS). Uteuzi huo umefanyika kufuatia kustaafu kwa mkurugenzi aliyemaliza muda wake, Othman Rashid.

Makala hii inajikita katika uchambuzi wa uteuzi huo kwa kuangalia changamoto na fursa zinazomkabili kiongozi huyo mkuu wa taasisi hiyo nyeti kabisa. Kwa mtizamo wangu, kama kuna kitu ambacho kinaweza kuzua maswali kuhusu uteuzi huo basi ni wadhifa wa Director of Risk Management alioshikilia Dokta Kipilimba huko nyuma alipokuwa mtumishi wa Benki Kuu ya Tanzania.

Sote twafahamu jinsi Benki Kuu yetu imekuwa ikiandamwa na matukio mfululizo ya ufisadi, kuanzia EPA hadi Tegeta Escrow. Kwa wadhifa wake katika taasisi hiyo, kuna uwezekano wa bosi huyo mpya wa mashushushu kuonekana ‘sehemu ya mfumo ulioshindwa kudhibiti ufisadi.’ Hata hivyo, utetezi unaweza kuwa huenda yeye alitekeleza majukumu yake vema lakini walio juu yake hawakuchukua hatua stahili.

Kadhalika, huko mtandaoni kuna ‘tuhuma’ kadhaa kuhusu Dokta Kipilimba, lakini itakuwa sio kumtendea haki yeye, blogu hii na mie mwenyewe kujadili tuhuma ambazo hazina ushahidi wowote. Ni muhimu kutambua kuwa Tanzania yetu licha ya kuwa kisiwa cha amani pia ni kisiwa cha majungu, uzandiki, fitna, umbeya na uzushi.

Changamoto kubwa kwa Dokta Kipilimba ni pamoja na kurejesha hadhi na heshima ya Idara ya Usalama wa Taifa. Katika miaka ya hivi karibuni, taasisi hiyo muhimu kabisa imekuwa ikishutumiwa kuwa inachangia ustawi wa ufisadi, ujangili, biashara ya madawa ya kulevya, nk.

Wanaoilaumu taasisi hiyo hawamaanishi kuwa watumishi wake wanahusika katika matukio hayo ya kihalifu as such bali kushindwa kwa Idara hiyo kukabiliana na kushamiri kwa matendo hayo ya kihalifu, ambayo kimsingi ni matishio kwa usalama wa taifa, na kazi kuu ya Idara hiyo ni kukabiliana na matishio kwa usalama wa taifa la Tanzania.

Ninaamini kuwa Dokta Kipilimba anafahamu kanuni muhimu kuhusu ufanisi au mapungufu ya idara ya usalama wa taifa popote pale duniani, kwamba “kushamiri kwa vitendo vinavyotishia usalama wa taifa lolote lile ni kiashiria cha mapungufu ya idara ya usalama wa taifa ya nchi husika, na kudhibitiwa kwa vitendo vinavyotishia usalama wa taifa popote pale duniani ni kiashiria cha uimara wa idara ya usalama wa taifa ya nchi husika.”

Kwahiyo, kwa kuzingatia kanuni hiyo, kushamiri kwa biashara ya madawa ya kulevya, ujangili, rushwa, na ufisadi mwingine ni viashiria vya mapungufu ya Idara yetu ya Usalama wa Taifa.

Changamoto nyingine kwa Dokta Kipilimba ni tuhuma za mara kwa mara dhidi taasisi hiyo muhimu kabisa kuwa katika utendaji kazi wake imegeuka kuwa kama ‘kitengo cha usalama cha chama tawala CCM.’ Idara hiyo imekuwa ikituhumiwa kuwa kwa kiasi kikubwa imeweka kando taaluma ya ushushushu (tradecraft) na kutekeleza majukumu yake kisiasa.

Madhara ya muda mfupi ya kasoro hiyo ni taasisi hiyo kujenga uhasama na vyama vya upinzani na kwa namna flani kupoteza heshima na uhalali wake. Lakini la kuogofya zaidi ni madhara ya muda mrefu, ambapo watu wanaoweza kuwa ni matishio kwa usalama wa taifa letu wanaweza kutumia ‘urafiki’ unaodaiwa kuwepo kati ya Idara ya Usalama wa Taifa na CCM, wakitambua bayana kuwa ‘Idara haina muda na makada wa chama tawala,’ na hatimaye kufanikiwa kutimiza azma zao ovu.

Baadhi ya watumishi wa zamani wa taasisi hiyo walijikuta matatizoni kwa vile tu walitekeleza majukumu yao dhidi ya wanasiasa wa chama tawala, na wakaishia kuonekana kama wahaini.

Changamoto nyingine kwa Dokta Kipilimba ni tuhuma zinazoikabili taasisi hiyo kuhusu mfumo wa ajira ambapo inadaiwa kuwa zimekuwa zikitolewa kwa upendeleo kwa ndugu na jamaa za ‘vigogo.’ Tatizo kubwa hapa ni kwamba utiifu wa ‘ndugu na jamaa hao wa vigogo’ haupo kwa taifa bali kwa vigogo hao waliowaingiza Idarani. Pengine sio vibaya kufikiria ‘utaratibu wa wazi’ katika ‘recruitment’ kama inavyofanywa na wenzetu wa CIA, NSA, MI5, MI6, HGCQ, nk wanaotangaza nafasi za ajira kwenye vyombo vya habari.

Pia kuna tatizo la baadhi ya maafisa usalama wa taifa ‘kujiumbua’ kwa makusudi kwa sababu wanazojua wao wenyewe, kubwa ikiwa kutaka sifa tu, au waogopwe ‘mtaani.’ Hii inaathiri sana ufanisi wa maafisa wa aina hiyo kwani ni vigumu kutekeleza majukumu yao ipasavyo pasi usiri.

Sambamba na hilo ni kasumba ya muda mrefu ambapo baadhi ya maafisa wa Idara hiyo waliopo kwenye vitengo mbalimbali kuwepo huko kwa muda mrefu mno kiasi cha kuathiri utendaji wao. Miongoni mwa maeneo hayo ni pamoja na ‘vituo muhimu’ na kwenye ofisi za balozi zetu nje ya nchi. Ikumbukwe kuwa unless afisa ametengeneza deep cover, uwepo wake kwa muda mrefu katika sehemu aliyokuwa ‘penetrated’ au kituo chake cha kazi kwingineko (mfano ubalozini) unaweza kupelekea ‘akaungua’ (burned).

Changamoto nyingine kubwa ni uwepo wa majasusi kibao nchini mwetu, hususan kutoka nchi moja jirani, huku wengi wa majasusi hao wakiwa wameajiriwa katika taasisi za umma na binafsi. Hili ni tishio kubwa kwa usalama wa taifa wa Tanzania yetu.

Kwa upande fursa kwa Dokta Kipilimba, licha ya kuwa ‘mwenyeji’ katika taasisi hiyo muhimu, wasifu wake kitaaluma unamweka katika nafasi nzuri sana kukabiliana na changamoto za karne ya 21 ambayo imetawaliwa zaidi na teknolojia ya kisasa.

Dokta Kipilimba ni msomi aliyebobea kwenye teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA) na yayumkinika kuamini kuwa anaweza kutumia usomi wake kuibadilisha Idara yetu ya Usalama wa Taifa kwenda na wakati, kufanya kazi kama taasisi ya kishushushu ya karne ya 21, ambayo licha ya kutegemea HUMINT inaweza pia kutumia njia nyingine za kukusanya taarifa za kiusalama kwa kutumia teknolojia (GEOINT, MASINT, SIGINT, CYBINT, FININT na TECHINT kwa ujumla)

Na katika kwenda na teknolojia ya kisasa, basi pengine si vibaya iwapo Idara yetu ikafikiria haja ya uwepo wake kwenye mtandao, kwa kuwa na tovuti yake kamili na pia kufungua akaunti kwenye mitandao ya kijamii, hususan Twitter na Facebook. Hii sio tu inaweza kusaidia kutengeneza "human face" ya intel service bali pia yatoa fursa nzuri katika OSINT.

Fursa nyingine kwa Dokta Kipilimba ni matarajio ya sapoti ya kutosha kutoka kwa Rais Dokta Magufuli ambaye kama alivyoahidi wakati wa kampeni za kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka jana, mapambano dhidi ya ufisadi yamepewa kipaumbe cha hali ya juu kabisa. Kama ‘sponsor’ na ‘consumer’ wa taarifa za kila siku usalama, inatarajiwa kuwa Dokta Magufuli atatekeleza ushauri wa Idara katika kukabiliana na matishio mbalimbali ya usalama wa taifa letu.

Dokta Kipilimba ana fursa ya kuleta mageuzi kwa Idara ya Usalama wa Taifa kwa kuangalia uwezekano wa kuwafikia watu walio nje ya taasisi hiyo, hasa pale uwezo wa Idara yetu unapokuwa limited. Nitoe mfano. Katika kupata taarifa mwafaka wa kudumu kuhusu, kwa mfano, mgogoro wa kisiasa huko Zanzibar, Idara inaweza ku-reach out wanazuoni wa historia ya taifa letu walipo ndani na nje ya nchi yetu.

Ikumbukwe kuwa sio rahisi kwa taasisi hiyo kuwa na maafisa au watoa habari katika kila eneo. Wenzetu wa nchi za Magharibi wamekuwa wakikabiliana na hali hiyo kwa kufanya kazi na ‘makandarasi’ (contractors), ambao of course, wamekidhi taratibu kama vile vetting.

Sambamba na hilo ni Idara hiyo kuangalia uwezekano wa kutumia hazina kubwa tu ya maafisa wake wa zamani, hususan wastaafu. Ikumbukwe kuwa wengi wao ni watu wanaowindwa na ‘subjects’ mbalimbali wanaolenga kulihujumu taifa letu.

Nimalizie makala hii kwa kutoa pongezi za dhati kwa Dokta Kipilimba na Naibu wake (DDGIS) Robert Msalika, sambamba na kumtakia mapumziko mema Mkurugenzi mstaafu Othman, na kumkaribisha ‘uraiani.’

MUNGU IBARIKI TANZANIA, MUNGU IBARIKI IDARA YETU YA USALAMA WA TAIFA




6 Jul 2011

Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalam wa Taifa Rashid Othman (wa tatu kushoto,mwenye shati la kitenge)
Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TISS, Jack Zoka

Wabunge walipua Usalama wa Taifa  
Tuesday, 05 July 2011 21:00

Ramadhan Semtawa, Dar
WABUNGE watatu jana waliishambulia Idara ya Usalama wa Taifa (TISS), bungeni baada ya kueleza kuwa imeshindwa kuzuia uhujumu uchumi na badala yake imejikita kwenye siasa za kukipendelea chama tawala, CCM na kuukandamiza upinzani.

Tuhuma hizo zinakuja wakati tayari nchi imetikiswa na matukio kadhaa ya ufisadi ikiwamo wizi wa zaidi ya Sh133 bilioni katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ununuzi wa rada ya kijeshi na ufisadi unaodaiwa kufanywa katika kampuni za Meremeta, Tangold na Deep Green Finance.

Kwa nyakati tofauti wakichangia Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (Utumishi, Utawala Bora na Uratibu na Mahusiano ya Jamii), wabunge hao waliirushia makombora idara hiyo na kupendekeza ikajifunze nje jinsi ya kufanya kazi zake.

Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, ndiye alikuwa mwiba zaidi baada ya kuweka bayana kwamba idara hiyo imeshindwa kusaidiana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kuzuia rushwa kubwa zinazohujumu uchumi wa nchi.

Mchungaji Msigwa ambaye alizungumza kwa hisia kali, alisema idara hiyo imegeuka chombo cha kulinda maslahi ya kisiasa hasa ya CCM na kukandamiza upinzani huku ikiacha uchumi wa nchi ukiendelea kuhujumiwa.

Kwa mujibu wa Msigwa, endapo Idara ya Usalama wa Taifa, ingetumia nguvu nyingi kuzuia uhujumu uchumi kama inavyotumia kukandamiza upinzani kwa kujihusisha kwenye siasa, nchi ingeweza kupiga hatua kubwa.

Alitaka watendaji wake kwenda kujifunza majukumu yao nje ya nchi badala ya kuendelea kujihusisha na siasa kama wanavyofanya sasa.Mchungaji Msigwa alisema nchi inakabiliwa na maadui ndani na nje hivyo ni vema idara ikajikita katika kuwashughulikia hao kuliko kujiingiza zaidi kwenye siasa na kugeuka idara ya usalama ya CCM.


Takukuru na rushwa
Akizungumzia Takukuru na mapambano dhidi ya rushwa kubwa, Mchungaji Msigwa alimtaka Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo, Dk Edward Hoseah, kuendeleza mapambano na kama wakubwa wakimwekea kiwingu katika utendaji wake, bora aachie ngazi.

Msigwa alifafanua kwamba, hata katika nchi za Kenya na Uganda, wakuu wa taasisi za kupambana na rushwa walipoona mambo ni magumu kutokana na wakubwa kuwadhibiti, waliamua kuachia nyadhifa zao.

Mnyika naye ashambulia usalama
Mbunge wa Ubungo John Mnyika, naye alitumia mjadala huo kuipa somo TISS akiitaka iachane na siasa za kukandamiza upinzani bali ijikite katika kulinda maslahi ya taifa.

Katibu huyo wa wabunge wote wa Chadema bungeni, alisema kazi kubwa za idara hiyo isiwe kujiingiza kwenye siasa kwa kukandamiza upinzani bali kuangalia mustakabali mzuri wa nchi.

Mnyaa: Idara imejikita Bara
Mbunge wa Mkanyageni (CUF), Habib Mnyaa, alisema awali Usalama wa Taifa ulikuwa ukijitegemea kwa upande wa Zanzibar na iliyokuwa Tanganyika ambayo kwa sasa inaitambulika kwa mwavuli wa Tanzania Bara.

Hata hivyo, alisema baada ya idara hiyo kuunganishwa miaka ya 1980, idara hiyo inaonekana kujikita zaidi Bara huku Zanzibar ikikosa hata ofisi kubwa ya maana kwa ajili ya operesheni.

Maji Marefu aikingia kifua
Hata hivyo, mbunge wa Korogwe Vijijini (CCM), Stephen Ngonyani maarufu kama Profesa Majimarefu, alipinga hoja za wabunge wenzake hao, akisema hawaitendei haki kwani imekuwa ikifanya kazi kubwa kulinda usalama wa taifa.

Kwa mujibu wa Ngonyani, wakosoaji hao wa TISS wanapaswa kuwa mashuhuda kwa kwenda nchi jirani na nyingine za Afrika, ambako usalama wa taifa ni mbaya, huku zikikabiliwa na vitisho vikubwa vya mauaji na vurugu.

Akisisitiza alitoa mfano wa nchi moja (hakuitaja) ambako aliwahi kuingizwa ndani kulala wakati wa mchana kutokana na hali mbaya ya usalama katika taifa na kusisisiza, "ninyi mnaoisema Idara ya Usalama wa Taifa hebu acheni kauli zenu hizo."

"Nendeni nchi jirani au kwingine mkaangalie, mimi niliwahi kuingizwa ndani mchana kwenda kulala kutokana na hali mbaya ya usalama. Hapa kwetu Idara inafanya kazi kubwa, nchi imetulia," alizidi kuikingia kifua na kuwararua wakosoaji.

Katika kuonyesha jinsi idara hiyo inavyofanya kazi kwa ufanisi, Ngonyani alitaka Serikali kuongezea mishahara watumishi wa TISS na kuongeza, "hawa vijana tunashinda nao hapa hadi saa 4:00 usiku wanaangalia usalama halafu tunawasema hawafanyi kazi!"

"Tena nasema waongezewe mishara, vijana wanafanya kazi nzuri na kubwa ya kulinda nchi. Tunapaswa kuwapa nguvu siyo kuwalaumu siyo sahihi hata kidogo," alisisitiza Ngonyani.

Katika miaka ya karibuni hasa baada ya kuongezeka vuguvugu la vyama vingi vya siasa, TISS imekuwa ikikokosolewa na baadhi ya watu kutokana na kuacha baadhi ya misingi yake ya kulinda maslahi ya taifa ikiwamo uchumi, kama ilivyokuwa ikifanya wakati wa Awamu ya Kwanza chini ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

Mwaka jana baada ya matokeo ya Uchaguzi Mkuu, idara hiyo pia ilijikuta katika tuhuma za kile kilichoelezwa na Chadema kwamba, ilitumikia kuchakachua matokeo ya kura za urais, hali iliyomlazimu Naibu Mkirugenzi Mkuu Jack Zoka, kujitokeza hadharani na kufanya mkutano na waandishi wa habari kuondoa hali tete na giza lililokuwa limegubika nchi. Zoka alikanusha tuhuma hizo kwamba Idara ilihusika katika kuchakachukua matokeo ya urais.

CHANZO: Mwananchi

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.