Showing posts with label RUSHWA. Show all posts
Showing posts with label RUSHWA. Show all posts

16 May 2011


Rais wetu mpendwa Jakaya Mrisho Kikwete kwa kushangaa hajambo.Sasa anashangaa kwanini kuna utitiri wa mabango yenye ujumbe dhidi ya rushwa lakini rushwa inaendelea kutawala katika wizara mbalimbali bila uoga.

Tell you what Mr President,jibu la kinachokushangaza ni rahisi sana.Kama wewe mwenye kila nyenzo ya kukabiliana na rushwa,na ambaye ulitangaza hadharani kuwajua wala rushwa ila uliwapa muda wa kujirekebisha-na wakagoma kujirekebisha,lakini unaogopa kuwachukulia hatua-unasuasua katika kutekeleza ahadi uliztoa mwenyewe,unatarajia nini kutoka kwa watu wasio na uwezo wala mamlaka ya kupambana na rushwa?

Wewe unashangaa na sie tunakushangaa pia.One thing for sure,rushwa haiwezi kumalizwa kwa Rais kushangaa.Kinachohitajika ni vitendo na sio kubembelezana katika semina elekezi zinazozidi kuwatwisha mzigo walipa kodi masikini.

Jaribu kuwa mkali kidogo,punguza kushangaa,fanya vitendo.

Habari kamili ni hii hapa chini

Kikwete ataka vita vya rushwa kwa vitendo

na Danson Kaijage, Dodoma

RAIS Jakaya Kikwete, ameagiza mabango yote ya kupambana na rushwa yanayobandikwa katika wizara na taasisi za serikali na za umma yaendane na matendo yanayofanywa na maofisa katika ofisi husika.

Alitoa agizo hilo jana alipokuwa akifunga semina elekezi kwa viongozi na watendaji wakuu wa serikali iliyofanyika mjini Dodoma kwa siku saba.

Alisema wananchi wangependa kuona ukusanyaji wa mapato unaimarika na nidhamu ya matumizi ya fedha na mali za umma inakuwa bora zaidi badala ya kujaza mabango mengi yasiyokuwa na faida.

Alisema wananchi wanatarajia kuona juhudi za mapambano ya kweli kwa kudhibiti mianya ya rushwa badala ya kuona mabango mengi bila kuwepo na juhudi za makusudi.

Rais Kikwete alisema kinachoshangaza ni kuona wingi wa mabago katika kila kona wakati rushwa inaendelea kutawala ndani ya wizara mbalimbali bila woga.

Aidha, alisema kutokana na kuwepo kwa rushwa kuanzia ngazi ya juu ni wazi kuwa rushwa itaendelea kutendeka hadi ngazi ya chini kwa kuwa misingi ya rushwa inaanzia ngazi ya juu na kushuka ngazi ya chini.

Aliwataka vingozi na watendaji wakuu hao, kuonyesha ujasiri mkubwa juu ya kupiga vita masuala ya rushwa badala ya kuoneana aibu na kufichiana siri.

Rias Kikwete alisema semina hiyo ambayo ilikuwa na mikakati ya kuimarisha utendaji ndani ya serikali inapaswa kuzaa matunda hasa katika mapambano dhidi ya rushwa.

Hata hivyo, alisema wananchi wanatazamia kuona viongozi wa ngazi ya juu wakiwa mfano mzuri wa utawala bora, kuheshimu Katiba, utawala wa sheria na nidhamu ya kazi na uwajibikaji.

Naye Katibu Mkuu Kiongozi, Philimon Luhanjo, alisema waliazimia mazimio 14 ambayo viongozi hao wanatakiwa kuyatekeleza na kuyawasilisha katika ofisi yake kila baada ya miezi mitatu.

Semina hiyo iliwashirikisha mawaziri, makatibu wakuu, manaibu makatibu wakuu na wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama.



4 Mar 2010


Katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi,Rais Jakaya Kikwete alieleza kwa undani matarajio yake kuhusu ufanisi wa Sheria mpya ya Uchaguzi.Pamoja na mambo mengine,sheria hiyo inatarajiwa kuziba mianya ya rushwa kwa wanasiasa wanaowania uwakilishi wa wananchi katika Bunge.Hata hivyo,pamoja na nia njema na umuhimu wa kuwa na sheria hiyo,ushahidi wa kimazingira unaashiria kuwa itabaki kuwa sheria tu kama zilivyo nyingine nyingi pasipo kuzaa matunda yanayokusudiwa


Tatizo la nchi yetu halijawahi kuwa ukosefu wa sheria bali usimamizi na utekelezaji wake.Mifano ni mingi,lakini kwa vile sheria hii ya Uchaguzi inalenga kudhibiti mianya ya rushwa,ni vema tukaangalia kwanza ufanisi wa sheria nyinginezo zilizopo ambazo kwa hakika zingeaidia sana kupunguza tatizo la rushwa laiti zingetumika ipasavyo.

Kinachokwaza zaidi usimamizi na utekelezaji wa sheria zetu nyingi ni ukosefu wa uzalendo miongoni mwa waliokabidhiwa dhamana ya kuzisimamia na kuzitekeleza.Ni kichekesho kusikia miongoni mwa taasisi zinazotarajiwa kuwa na dhamana ya hali ya juu katika usimamizi na utekelezaji wa sheria hiyo ni TAKUKURU,chombo ambacho wengi wetu tunaamini kuwa kimeshindwa kazi yake.Hivi TAKUKURU iliyoshindwa sio tu kuchukua hatua dhidi ya wezi wa Richmond bali pia kutengeneza ripoti feki ya kuwasafisha watuhumiwa itawezaje kusimamia na kutekeleza sheria hiyo mpya ya uchaguzi?

Ikumbukwe pia kuwa kwa kiasi kikubwa vyombo vyetu vya dola bado vina fikra ya zama za chama kimoja ambapo "madhambi" ya wana-CCM yanachukuliwa kama "ubinadamu" na hivyo vyombo hivyo kusuasua kuchukua hatua zinazostahili.Kwa baadhi ya taasisi za dola,hata kukemea maovu yanayotendwa na baadhi ya vigogo wa CCM ni kama na kuvunja sheria za nchi!

Kwa mwenendo huu,ni dhahiri basi sheria hiyo inaweza kutumika kuvibana vyama vya upinzani huku wana-CCM wakiendeleza libeneke la takrima kana kwamba imehalalishwa.Sheria hii imeletwa na serikali ya CCM ambayo rekodi yake katika mapambano dhid ya rushwa ina walakini mkubwa.Iweje chama kilichounda serikali kiendelee kuwa na mwenyekiti wa kamati yake ya maadili (Andrew Chenge) ambaye ana tuhuma katika suala la rada?

Pengine badala ya kupoteza muda kwa kuja na sheria mpya,ungefanyika mchakato wa kupitia sheria zilizopo na kuhakikisha zinasimamiwa na kutekelzwa ipasavyo.Vinginevyo,itakuwa ni hadithi ileile ya kuja na sheria mpya zenye kuleta matumaini mithili ya kauli-mbiu "mAisha Bora kwa Kila Mtanzania" huku matokeo yake yakibaki sifuri.

26 Dec 2008

CHAGUZI NDANI YA CCM HAZIISHIWI VIOJA.RUSHWA IMETAPAKAA MNO NDANI YA CHAMA HICHO KANA KWAMBA NI SEHEMU YA KATIBA YAKE.SIO MATUSI KUAMINI KWAMBA PENGINE INGEKUWA RAHISI ZAIDI KWA CCM KUAHIDI KUENDELEZA LIBENEKE LA RUSHWA KWENYE MANIFESTO YAKE YA 2005 KULIKO AHADI ZA MAISHA BORA,MAHAKAMA YA KADHI,NK MAMBO AMBAYO HADI SASA YAMEENDELEA KUWA AHADI ZISIZOTEKELEZEKA.NI WAZI,RUSHWA HUZAA VIONGOZI WABOVU,MAFISADI NA WABABAISHAJI.HABARI MBAYA NI KWAMBA HAKUNA DALILI ZA KUISHA KWA GONJWA HILO HATARI NDANI YA CHAMA TAWALA.TAASISI ZA UMMA ZA KUKABILIANA NA RUSHWA ZINAISHIA KUALIKWA TU KWENYE CHAGUZI "KUZUIA RUSHWA" NA VIONGOZI WAANDAMIZI WA CHAMA HICHO WAMEISHIA KUPIGA KELELE TU (SINA HAKIKA KAMA NI ZA DHATI) KUHUSU RUSHWA KWENYE CHAGUZI,LAKINI SOTE TUNAJUA KWAMBA KELELE ZA CHURA HAZIMZUII NG'OMBE KUNYWA MAJI.ENEWEI,HEBU CHEKI MKASA HUU HAPA CHINI KISHA SOMA HITIMISHO LANGU BAADA YA HABARI HII:
Zikiwa zimesalia siku 14 kufika siku ya uchaguzi wa viongozi wa ngazi ya taifa wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), mambo si shwari katika mchakato wa kumpata mwenyekiti wake. 

Uchaguzi huo unatarajiwa kufanyika mjini Dodoma Januari 7, mwakani ambapo nafasi ya uenyekiti itagombewa na Janet Kahama, Sophia Simba na Joyce Masunga. 

Hali hiyo, ambayo inazidi kuipaka matope CCM, imedhihirika baada ya mgombea wa nafasi ya Janeth Kahama kuwasilisha rasmi malalamiko kwa Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, akimtuhumu mpinzani wake, Sophia Simba kwamba amewahonga wajumbe wote wa Mkutano Mkuu rushwa ya Sh. 100,000 ili wampe kura. 

Mbali na tuhuma za rushwa, Simba, ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora), anatuhumiwa pia na Kahama kuwa yeye na wapambe wake wamekuwa wakiitumia Ikulu kuwaomba kura wajumbe wa Mkutano Mkuu. 

Kahama, ambaye ni Mbunge wa Viti Maalum (CCM), amewasilisha malalamiko hayo kupitia barua yake yenye kumbukumbu Na. JBK/01/08 ya Desemba 20, mwaka huu, iliyopelekwa kwa Rais Kikwete, Ikulu, jijini Dar es Salaam. 

Nakala ya barua hiyo, ambayo Nipashe inayo, imepelekwa kwa Katibu Mkuu wa UWT Taifa na Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba. 

Makamba alipoulizwa na Nipashe juzi jioni kama amepokea nakala ya barua hiyo, alithibitisha kuipokea. 
Simba anadaiwa kutoa hongo hiyo kupitia kadi alizochapisha kwa lengo la kuwatakia heri ya Mwaka Mpya wajumbe wa Mkutano Mkuu wa UWT Taifa. 

Kadi hizo, ambazo zinadaiwa kusambazwa na Diwani wa Kata ya Ilala, Moshi Kondo, zina picha, jina na saini ya Waziri Simba, kalenda ya Mwaka Mpya wa 2009 na nembo ya CCM. 

Barua hiyo yenye kichwa cha habari kisemacho: `Yah: Malalamiko dhidi ya Mhe. Sophia Simba kugawa vipeperushi mikoani`, Kahama anamueleza Mwenyekiti Kikwete kama ifuatavyo: 

``Kwa heshima ya pekee, nakuomba uhusike na mada ya barua hii kama inavyosomeka hapo juu. Mheshimiwa Mwenyekiti, kama unavyofahamu, Jumuiya yetu ya UWT hivi sasa ipo katika mchakato wa uchaguzi wa viongozi wa ngazi ya taifa unaotarajiwa kufanyika mapema mwakani.`` 

``Mimi nikiwa mmoja wa wagombea wa nafasi hiyo ya Mwenyekiti wa Taifa wa UWT, natambua kuwa wagombea wote tulizuiwa na vikao vya UWT Taifa kutoa vipeperushi vya aina yoyote kwa minajili ya kujinadi kwa wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa wa UWT.`` 

``Lakini, ajabu ni kwamba, mgombea mwenzangu, Bi Sophia Simba amechapisha kalenda na kadi za `Heri ya Mwaka Mpya` zenye picha yake na nembo ya CCM na kuzisambaza kwa wajumbe wote wa Mkutano Mkuu wa UWT Taifa nchi nzima, ndani zikiwa na kitita cha Sh. 100,000 (kwa kila kadi).`` 

``Mheshimiwa Mwenyekiti, nalazimika kukuandikia waraka huu ili kukupa angalizo juu ya suala hilo hasa ikizingatiwa kuwa Mheshimiwa Sophia Simba ni Waziri katika ofisi yako mwenye dhamana ya Utawala Bora.`` 

``Hivyo hatua yake na nembo ya CCM, inakwenda kinyume na kanuni za uchaguzi za CCM, kipengele cha Miiko ya Kuzingatiwa wakati wa Shughuli za Uteuzi na Uchaguzi`, ibara ya 33 kifungu kidogo cha 14 kinachosema: `Ni mwiko kutumia makaratasi ya kampeni nje ya utaratibu wa chama au kutumia vishawishi vya aina yoyote ile kwa minajili ya kupata kura.`` 

``Je, hatua hii ya Mheshimiwa Simba kuchapisha nyaraka hizo zenye picha yake na nembo ya CCM na kuzitawanya nchi nzima, si uvunjaji wa makusudi wa kanuni hizo za uchaguzi za CCM tena kipindi hiki cha kuelekea kwenye Uchaguzi Mkuu wa UWT?`` 

``Je hatuoni kwamba hatua yake hiyo ambayo haijakemewa mpaka sasa ni kielelezo kingine cha ubabe na matumizi mabaya ya madaraka yake kama Waziri tena mwenye dhamana ya Utawala Bora? 

Nasisitiza hili kwa sababu Mheshimiwa Simba na wapambe wake wamekuwa wakipita mikoani na kupotosha wapigakura kuwa yeye ndiye chaguo la Ikulu.`` 

``Mheshimiwa Mwenyekiti, nawasilisha kwako waraka huu wenye malalamiko haya ili uweze kujua nini kinaendelea na kuchukua hatua kwani kama kitaachwa, kinaweza kujenga matabaka ndani ya UWT na mpasuko usio wa lazima ndani ya chama chetu, hasa pale hisia za mgombea mmoja kuandaliwa mazingira ya ushindi dhidi ya wenzake zinapoanza kujengwa.`` 

``Naambatanisha moja ya vipeperushi hivyo vya Mheshimiwa Simba vilivyosambazwa mikoani kinyume na utaratibu nilioueleza hapo juu.`` 

Makamba alipoulizwa na Nipashe juzi, licha ya kukiri kupokea nakala ya barua hiyo ya Kahama, alimtaka mwandishi kama ana swali lolote kuhusiana na suala hilo, akamuulize Rais Kikwete kwa vile ndiye aliyeandikiwa barua hiyo. 

``Mtafute Mwenyekiti wa CCM, yeye ndiye aliyeandikiwa barua, aliyeandikiwa ndiye anayejibu. Mimi nimepewa nakala, anayepewa nakala, anaarifiwa tu,`` alisema Makamba. 

Nipashe ilipowasiliana na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Ikulu, Salvatory Rweyemamu, alisema kwa vile malalamiko ya Kahama yanahusiana na Chama, anayepaswa kujibu suala hilo ni Katibu Mkuu. 

Baada ya Makamba kuulizwa tena, alisema: ``Mimi sina cha kusema, sijaisoma (hiyo barua), sijajua maudhui. 

Nitakapoisoma na kujua maudhui, nitatoa maoni yangu.`` 

Kahama alipoulizwa na Nipashe jana kama barua hiyo ndiye aliyeiandika, hakukiri wala kukanusha, badala yake alisema kwa sasa hawezi kuzungumza lolote kwa vile kipindi hiki ni cha sikukuu ya Krismasi, ambayo yeye kama Mkristo anapaswa kuitukuza. 

``Sina comments (maoni) kabisa kabisa, mpaka nionane na Katibu Mkuu. Pia mimi ni Mkristo na kipindi hiki ni cha Krismasi,`` alisema. 

Naye Diwani wa Kata ya Ilala, Moshi Kondo, alipoulizwa juzi, alikataa kuzungumzia suala hilo, badala yake alimtaka mwandishi akamuulize Simba. 

``Kwani Sophia Simba mimi ni nani kwake?`` alihoji Kondo, ambaye alipojibiwa na mwandishi kuwa ``Simba anadaiwa kuwa ni mtu wake wa karibu``, alisema: ``Nenda kamuulize Simba.`` 

Tangu juzi hadi jana jioni Nipashe ilimtafuta Simba bila kumpata na baadaye kuelezwa na mmoja wa wanafamilia yake kuwa yuko safarini Malaysia. 

CHANZO:Nipashe

WAKATI MAMA KAHAMA AMETUMIA HAKI YAKE YA MSINGI KAMA MGOMBEA NA MWANANCHAMA WA UWT/CCM KUWASILISHA MALALAMIKO YAKE KWA MWENYEKITI WA CCM TAIFA (JK),NADHANI ANGEWEZA PIA KUWASILISHA TUHUMA HIZO POLISI AU TAKUKURU.HIVI KUTOA RUSHWA SI NI KOSA LA JINAI?JE MAMA KAHAMA YUKO MORE CONCERNED NA RUSHWA HIYO KUATHIRI NAFASI YAKE YA KUCHAGULIWA KULIKO UKWELI KWAMBA MTUHUMIWA (SOPHIA SIMBA) SIO WAZIRI TU BALI NI WAZIRI MWENYE DHAMANA YA UTAWALA BORA (ISOMEKE MAPAMBANO DHIDI YA RUSHWA)?


17 Oct 2008

2008-10-17 10:38:12 
Na Simon Mhina

Jaji Mkuu wa Tanzania, Augustino Ramadhani, ametoboa siri ya ufisadi unaokua kila kukicha nchini kwamba unatokana na uchaguzi. 

Ameonya kama rushwa kwenye uchaguzi haitadhibitiwa basi ufisadi ambao umekithiri kila eneo utaendelea kuitafuna nchi. 

Alisema rushwa na ufisadi katika nchi ni sawa na watoto mapacha, na mama yao ni uchaguzi. 

Jaji Mkuu alisema hayo jana wakati akitoa mada katika kongamano la siku mbili la kujadili rushwa katika siasa na ugharimiaji wa shughuli za kisiasa katika vyama. 

Katika hutuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Msajili wa Mahakama Kuu, Ferdinand Wambali, Jaji Mkuu alisisitiza kuwa bila kudhibiti rushwa kwenye uchaguzi, uovu huo utaendelea hata katika vyombo vya kutunga sheria na vile vya utoaji haki kama mahakama. 

``Ukimpitisha mgombea kwa misingi ya rushwa, ujue kiongozi huyo ndiye utakayekutana naye mbele ya safari katika kukuhudumia. Mtu aliyetokana na rushwa kwake ni vigumu kukemea rushwa hata kama imemzunguka,`` alisema. 

Naye Jaji Kiongozi Mstaafu, Amir Manento, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, alisema umefika wakati sasa kumpa nafasi Rais kuteua mawaziri nje ya wabunge kwa kuwa wengi wao wamepata nafasi hizo kwa kutoa rushwa. 

Alisema wabunge ambao huingia bungeni kwa njia ya rushwa, wanapoteuliwa kuwa mawaziri hutumia fursa hiyo kurudisha fadhila kwa wale waliowakopesha takrima. 

Alionya kwamba hakuna mfadhili yeyote ambaye anaweza kutoa fedha zake bure bila kuwa na lengo ya kupata faida baadaye. 

Naye Waziri Mkuu Mstaafu, Jaji Joseph Warioba, alisema chanzo cha rushwa, ufisadi na aina zote za ubadhirifu wa mali ya umma, ambavyo vimeshamiri nchini vinatokana na viongozi kuingia madarakani kwa njia ya rushwa. 

Aidha, alisema bila kukomesha rushwa katika uchaguzi, itakuwa vigumu kukomesha ufisadi nchini, kwa vile viongozi wengi wameogolea katika rushwa hadi kufikia katika ngazi walizo nazo. 

Kutokana na sababu hizo, Warioba aliona kwamba ni vigumu kwa viongozi waliochaguliwa kwa rushwa kuweza kupambana na janga hilo. 

Kongamano hilo lililoandaliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kwa kushirikiana na Tasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru) lilianza jana jijini Dar es Salaam na linamalizika leo. 

Jaji Warioba alisema hivi sasa Tanzania inaelekea kubaya kwani rushwa inaonekana kukubalika kabisa kuwa moja ya kigezo cha kumpima mgombea. 

``Hivi sasa hata kama utahubiri sera nzuri kiasi gani, hata kama mgombea anayo sifa kubwa kiasi gani, hawezi kupita bila kutoa rushwa, hizi ni dalili mbaya,``alisema. 

Jaji Warioba alisema kutokana na rushwa kushamiri, hivi sasa kampeni za mgombea kuomba kuteuliwa na chama chake zimekuwa nzito kuliko kampeni za ujumla za kiserikali. 

Alisema hata baada ya sheria ya takrima kufutwa bado wagombea wamekwa wakibuni mbinu mbalimbali za kugawa rushwa. 

Warioba alipinga vikali madai kwamba umasikini wa wananchi ndio unasababisha rushwa kushamiri. 

Alisema kwa maoni yake, rushwa inashamirishwa nchini na matajiri pamoja na viongozi ambao tayari wanazo pesa. 
Alisema hata hapa nchini, miaka ya nyuma watu walikuwa masikini wa kutupwa, lakini hapakuwa na rushwa katika uchaguzi. 

``Kwa hiyo si kweli kwamba umasikini ndio unasababisha rushwa katika uchaguzi, wanaosababisha rushwa na kuwafundisha watu waamini katika rushwa ni viongozi na matajiri,`` alisema. 

Jaji warioba alisema kunatokea matatizo makubwa wakati wa upigaji kura, kwani imebainika kwamba baadhi ya wasimamizi, wanapokea rushwa ili `kuvizima` vyama ambavyo hawavipendi. 

Alisema japokuwa wagombea huwaamini sana mawakala, lakini sio siri kwamba mawakala hao pia hutumiwa kuwahujumu baada ya kupewa rushwa. 

Alionya kuwa kutunga sheria nyingi za kuzuia rushwa hakusaidii kama jamii yenyewe haijaamua kupinga suala hilo. 

Vilevile, alisema daftari la kudumu la wapiga kura kimsingi sio mwarobaini wa matatizo ya uchaguzi nchini, kwani linaweza kuchezewa ili kuharibu kumbukumbu sahihi. 

Kuhusu mapato ya vyama, Warioba alisema kunahitajika uwazi kwa wale wanaofadhili vyama, ili kuviepusha vyama hivyo visigeuke kuwa vibaraka. 

Mathalan, alisema kuna uwezekano mkubwa wa viongozi kugeuka vibaraka wa mafisadi kama waliingia madarakani kwa kufadhiliwa kwa njia za rushwa. 

Alionya kuwa si sahihi kutoa ruzuku kwa vyama vyenye wabunge pekee, na kutaka utafutwe taratibu wa kuvipatia vyama vyote ruzuku ili kuweka uwiano. 

Vilevile, alisema si sahihi kuvifuta vyama vitakavyokosa kura kabisa, badala yake ameshauri viachwe kwani huenda kuna siku wananchi wakavihitaji. 

``Kanu kilikuwa chama kikubwa sana, lakini sasa ni kidogo na vile vidogo sasa vimekuwa vikubwa, hivyo tusifute chama eti kwa vile ni kidogo au hakikubaliki, kuna siku kitakubalika,`` alisema. 

Naye Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (Chadema) akichangia katika kongamano hilo alisema kwamba ufisadi nchini unashamiri kutokana na matajiri na wanasiasa kuendeleza tabia hiyo na wala si umaskini kama wengi wanavyopotosha. 

Dk. Emmanuel Makaidi, Mwenyekiti wa National Legue for Democracy (NLD) alisema kwamba serikali ilifuta sheria ya takrima ambayo ilikuwa uchochoro wa kutoa rushwa, lakini inataka kuirudisha kwa njia nyingine ambayo ni mfuko wa jimbo. 

Pia alisema daftari la wapigakura linapaswa kuhakikiwa mara kwa mara kuepusha chama kimoja kutumia watendaji kufuta au kuongeza majina kwa manufaa ya chama chao.

CHANZO: Nipashe


7 Oct 2007

MTANZANIA UGHAIBUNI-2

Asalam aleykum,

Niseme bayana kwamba napenda sana kuangalia runinga kila nafasi inaporuhusu. Na kwa mazoea hayo, napenda kutamka bayana kwamba mara nyingi huwa nafahamu mengi ya yanayojiri katika sayari yetu hii. Lakini pia ni vema nikisema kwamba “mahaba” yangu kwa runinga huwa mara kadhaa yananiacha na maswali mengi kuliko ajibu, na kuna nyakati huwa nabaki na majonzi napoona namna wanadamu wenzetu wanavyosumbuka na kuteseka katika sehemu flani za dunia yetu. Ni mengi, lakini linalovuma sana kwa sasa hivi katika “channels” mbalimbali za ni namna utawala wa kidikteta huko Burma unavyoendesha kampeni zao za kimyama dhidi ya watu wasio na hatia ambao wamechoshwa na miongo kadhaa ya utawala wa kijeshi. Inatia uchungu kuona picha za miili ya watawa wa Kibudha (Buddhist monks) iliyotelekezwa mitaani au inayoelea kwenye maji yote yakiwa ni matokeo ya mtangange kati ya vyombo vya dola vya nchi hiyo dhidi ya waandamanaji waliokuwa wakidai demokrasia na kupinga udikteta. Inaumiza zaidi kuona kauli “za kisanii” za Umoja wa Mataifa, Jumuiya ya Nchi za Ulaya au Marekani zinazodai kuwa “duni inaona unyama huo na haitavumilia” ilhali hakuna mikakati yoyote thabiti ya kuwapa matumaini watu wanaoteseka huko Burma kwamba siku moja wataamka wakiwa na amani ya kudumu. Ni hadithi zisizotofautiana sana na zile walizosikia wenzetu wa Rwanda wakati wa mauaji ya halaiki,au zile zinazoleta matumaini “hewa” kila kukicha huko Darfur au Somalia.Hili dude linalooitwa “Jumuiya ya Kimataifa” limezidi kuthibitisha kuwa ni la kufikirika zaidi kuliko lenye ufanisi kwani laiti lingetafsiri kauli zake katika vitendo basi kwa hakika dunia ingekuwa ni mahala salama sana.

Hivi runinga zingeendelea kutuonyesha picha hizi za kusikitisha sembuse nchi kama Marekani ingeamua kwa dhati kukomesha mateso yanayoendelea sehemu mbalimbali duniani?Hivi mamilioni ya waliokata tamaa na maisha ingeendelea iwapo tamaa ya mafuta katika seheu kama Iraki ingekuwa ajenda ndogo kuliko kapata haki halisi za binadamu katika sehemu zilizogubikwa na mateso duniani?Kwa hakika dunia ingeweza kabisa kuwa sehemu mwafaka ya kuishi kwa kila binadamu iwapo wale wenye uwezo wa kukomesha mateso hayo wangedhamiria kwa dhati kuhakikisha kwamba hakuna nafasi kwa madikteta kunyanyasa wale wasio na hatia.Nakubali kwaba ugaidi ni tishio kubwa kwa amani ya dunia yetu lakini kuna matishio mengine ambayo yanawaathiri wanadamu kila kukicha kuliko huo ugaidi,matishio hayo yakiwa ni pamoja na ukiukaji wa haki za binadamu na rushwa zinazodumaza maendeleo ya nchi nyingi za dunia ya tatu licha ya misaada lukuki inayomwagwa kuzikwamua nchi hizo.

Mimi naamini kuwa nchi tajiri na zenye nguvu za kuamua namna gani sie maskini tuishi zina uwezo wa kukomesha uonevu huu.Hivi mabenki makubwa katika nchi hizo yangeamua kwa dhati kuwabana wale ambao wanawekeza mabilioni ya dola kwenye akaunti katika mabenki hayo (ilhali maelfu kwa maelfu ya wanaowaongoza ni maskini wakutupwa ) kwa kuwauliza tu swali jepesi la “mmepata wapi fedha hizi” isingesaidia kuwafanya wabadhirifu,wala rushwa na wezi wa raslimali kujiuliza mara mbilimbili kabla ya kuiba?Mjuzi mmoja wa wizi wa raslimali za baadhi ya nchi za dunia ya tatu alinieleza kwamba kwa kuhofia kutaifishwa raslimali zao,wezi wengi katika nchi hizo hupendelea kuweka fedha zao katika mabenki ya nje kwa vile huko ndiko salama zaidi.Mjuzi huyo alidai pia kwamba nchi na mashirika wahisani hawajali sana kuhusu vilio vya wanaoibiwa au kuwa na uchungu na misaada wanayotoa kwa vile wanafahamu fika kuwa fedha hizo haramu zitarudi mikononi mwao (wahisani) kupitia akaunti za siri za wezi hao.

Siku moja niliwahi kuulizwa na rafiki yangu mmoja Mkenya kwamba kwanini Tanzania ina amani zaidi kulinganisha na jirani zake.Nikamweleza kwamba pamoja na sababu nyingine ikiwa ni pamoja na hekima na busara za Baba wa Taifa za kuwaunganisha Watanzania na mchango wa lugha ya Kiswahili,sababu muhimu ni kwamba Watanzania licha ya kuwa na makabila zaidi ya 120 ni kama watu wa ukoo mmoja.Sensa zetu huwa hazichanganui mwingiliano wa makabila huko nyumbani,lakini ni dhahiri kuwa zoezi hilo likijaribiwa litakuwa gumu sana kwa vile kuna mwingiliano mkubwa mno.Nikiangalia kwenye ukoo wetu nakuta kuna ninaowaita ndugu zangu ambao kimsingi asili yao ni makabila tofauti na asili ya ukoo wetu.Na hata hiyo asili yenyewe ya ukoo wetu inaweza kuwa ni ya jumlajumla tu (general) kwani historia inaonyesha kuwa mengi ya makabila ya kibantu yaliyopo huko nyumbani yapo yalipo sasa baada ya mtawanyiko wa Wanguni walioingia nchini kutokea sehemu nyingine.Mama yangu ni M-bena lakini makazi ya Wabena hawa ni Malinyi wilayani Ulanga.Na kuna Wabena wengine huko Iringa ambao kuna madai ya kihistoria kuwa hawa ni watu wa asili moja na hao Wabena wa Malinyi.Ngoja “nisichanganye madawa” (nisikoroge mambo) hapa.Hoja nayotaka kuitengeneza hapa ni kwamba mtu anaweza kufanya ubadhirifu akidhani anainufaisha familia yake pekee kumbe wakati huohuo anawaathiri ndugu zake wengine ambao kwa sababu za kihistoria wako katika makabila mengine.Laiti sote tungeangaliana kama Watanzania wenye asili zinazoshabihiana basi yayumkinika kusema kwamba baadhi ya wala rushwa na wabadhirifu wangeweza kuwa na huruma kwa ndugu zao.Lakini hata tusipoiangalia hoja hii ya umoja katika tofauti zetu (yaani kuwa katika makabila tofauti japo asili zetu zinashabihiana) kuna ukweli usiopingika kwamba kukwaza maendeleo katika kipindi hiki ni sawa na kuvichimbia makaburi vijukuu vitakavyokuwa vinahitaji baadhi ya huduma ambazo baadhi ya wabadhirifu wanazibinafsisha kuwa zao binafsi badala ya kujenga misingi ya vizazi vijavyo.Kuna wakati huwa nashindwa kupata majibu naposikia mtu amekwiba fedha za ujenzi wa mradi flani wa maendeleo japo ana watoto kadhaa katika familia yake na wengine kadhaa zaidi nje ya ndoa.Laiti mtu huyu angekuwa na akili basi ni dhahiri angetambua kuwa watoto wake lukuki aliokuwa nao sasa watamletea wajukuu baadae ambao nao wataleta watoto na wajukuu zaidi,na kwa maana hiyo kitendo chochote cha kukwaza maendeleo hivi sasa kitaathiri vizazi vyake vijavyo.Napenda kuamini kabisa kuwa yeyote yule mwenye upendo wa dhati na vizazi vyake vijavyo,achilia mbali vile vya wenzie,atafanya kila liwezekanalo kuitumikia nchi yetu kwa namna ambayo vizazi hivyo vijavyo havitapatwa na hasira za kubomoa makaburi yetu miaka 20 au 50 ijayo kwa hasira za kutengenezewa msingi mbaya wa maisha.Na kwa wale wanaoamini kuwa kuna moto wa kiyama baada ya kifo basi naamini watafanya kila wawezalo kukata tamaa zao za kidunia kwani bila kufanya hivyo watageuzwa kuwa kuni kwenye moto wa ahera.

Nimalizie kwa kuzungumzia kituko kimoja nilichokisoma katika gazeti flani la wiki iliyopita.Kituko hicho kinahusu kesi ya Profesa Mahalu,ambapo kwa mujibu wa gazeti hilo,wanasheria wa serikali wamekiri kuwa kesi hiyo “haina mwenyewe”.Nachojiuliza ni hiki,kama kesi haina mwenyewe sasa wao wanakwenda mahakamani hapo kumwakilisha nani!Hivi zile kesi za Jamhuri dhidi ya flani zimekufa siku hizi?Ningeelewa walichosema wanasheria hao wa serikali kama wangekuwa wametoka taasisi zinazotoa msaada wa kisheria,ambazo kimsingi zinaweza kudakia kesi yoyote ile kwa minajili ya kutaka haki itendeke.Mie sio mwanasheria,lakini pamoja na umbumbumbu wangu katika taaluma hiyo nadhani hawa waungwana wangeweza kabisa kuitaja Jamhuri kuwa ndio yenye kesi dhidi ya mwanadiplomasia huyo,hasa kwa vile wao ni waajiriwa wa Jamhuri na sio magazeti yaliyoibua madai hayo.Na iwapo walikuwa wakiamini kwamba chanzo za kesi hiyo ni hayo magazeti basi pengine ingeleta maana zaidi iwapo wangeyashawishi magazeti hayo kufungua kesi halafu wao wayasaidie katika kesi hiyo.Lakini pia kama wanadhani hakuna mlalamikaji katika kesi hiyo basi ni bora waachane nayo tu kwa vile kwa namna “wanavyowajibika” ni dhahiri kuwa huko mbele tutasikia vituko vikubwa zaidi ya hiki nachokielezea hapa.Kama dada yangu Freda anavyopenda kusema,hii ni kaaazi kweli kweli.

Alamiski






9 Sept 2007

Asalam aleykum,

Joji W.Bush anafahamika kama rais wa taifa lenye nguvu zaidi ulimwenguni.Lakini Bush ni maarufu pia kwa “kuchapia” maneno.Juzijuzi alimshangaza Malkia Elizabeth alipomshukuru kwa ziara yake ya “mwaka 1776”! kabla hajajikosoa yeye mwenyewe baada ya kugundua kwamba ameboronga.Wiki iliyopita alirudia tena “mchemsho wake” huko Australia.Kwanza alimshukuru John Howard,waziri mkuu wa Australia,pamoja na nchi yake kwa mchango wa jeshi la “Austria” huko Iraki (ni kweli majina ya nchi mbili hizo yanachanganya lakini si vigumu kubaini kwamba moja iko bara la Ulaya na nyingine iko Oceania).Na hakuishia hapo.Alianza hotuba yake moja kwa kumshukuru Howard kwa ukarimu wake na kuwa mwenyeji mzuri wa kikao cha OPEC (ilhali ukweli ni kwamba Australia ilikuwa mwenyeji wa kikao cha APEC).Lakini “machale” yalimcheza na kurekebisha haraka “blunder” hiyo.OPEC ni “Organization of Petroleum Exporting Countries” (ambapo Australia haijawahi kuwa mwanachama) wakati APEC ni kifupi cha “Asia Pacific Economic Co-operation”.Ukidhani ngoma iliishia hapo basi umekosea kwani Bush alijikuta akijiumauma kwenye kutamka jina la kikundi kimoja cha kigaidi cha Jemmiah Islamia.Na katika hotuba yake hiyo alimwacha kiongozi mmoja kutoka ukanda wa Pacific akitabasamu baada ya “kulichapia” jina lake.Huyo ndio Joji Bush!!!

Tukiwa bado kwenye anga hizo,majuzi Osama bin Laden alitoa hotuba yake ya “kuadhimisha” mashambulizi ya kigaidi ya September 11,2001 huko Marekani ambapo takriban watu 3000 walipoteza maisha.Katika hotuba hiyo Osama alikuwa akiongea kama mwanasiasa flani ambapo pamoja na mambo mengine aliwataka Wamarekani kujiunga na Uislam,alizungumzia pia “upinzani” wa baadhi ya wanasiasa wa Marekani katika suala la “global warming” na kugusia baadhi ya matatizo ya ndani ya uchumi wa nchi hiyo.Ikumbukwe kwamba Osama hajawahi kusikika hewani tangu mwaka 2004,na kujitokeza kwake kumezua maswali zaidi kuliko majibu.Nilikuwa naangalia kipindi cha “Late Edition” cha Wolf Blitzer wa CNN ambapo alimdadisi msaidizi mmoja wa White House kwamba je haoni kwamba kwa miaka sita tangu Osama na Al-Qaeda yake wafanye mashambulizi yao huko Marekani bado gaidi huyo sio tu kuwa yuko hai bali pia anajaribu ku-“influence” siasa za Marekani (mfano kwa kuwahubiria kuhusu “madhambi” ya viongozi wao).Wapo wanaodhani kwamba “kosa” la msingi katika msako dhidi ya Osama na kuiteketeza Al-Qaeda lilikuwa katika kuelekeza nguvu nyingi dhidi ya Saddam Hussein (ambaye madai kwamba anashirikiana na Al-Qaeda yalikuja kubainika kuwa sio sahihi) badala ya kukazania kwenye jitihada dhidi ya “adui halisi” Osama na wafuasi wake.Taarifa kutoka huko Afghanistan hazitoi picha nzuri kwani inaelekea kwamba washirika wakuu wa Al-Qaeda,kikundi cha Taliban,wamekuwa wakijiimarisha vizuri na huenda wakawa na nguvu kama walizokuwa nao kabla ya uvamizi dhidi ya Afghanistan uliiongozwa na Marekani.Na moja ya mambo yanayowaumiza vichwa watengeneza sera wa nchi mbalimbali ni hofu ya uwezekano wa Osama,Al-Qaeda,Taliban na vikundi vingine vya kigaidi kupata silaha za maangamizi ya halaiki (kwa mfano za kikemikali au kibaiolojia).Hofu hiyo inachochewa zaidi na ukweli kwamba mbio (kama zile za zama za Vita Baridi ) za kutengeneza na kuongeza uzalishaji wa silaha za nyukilia zimekuwa zikiongezeka kwa kasi.

Ukiachia Mataifa “yenye ruhusa” ya kumiliki nguvu za nyuklia (kwa mfano Marekani na Israel) mataifa mengine yaliyolazimisha “haki hiyo” (kwa mfano Pakistan na India) yanaendeleza kasi ya uzalishaji huku nchi kama Iran ikilazimisha kwa nguvu kujiunga na “klabu hiyo ya nyuklia.” Wajuzi wa mambo wanabashiri kwamba kuna uwezekano mkubwa wa nchi kama Misri na Saudi Arabia nazo kujikuta zinalazimika kuingia kwenye harakati hizo (inaaminika kuwa Saudi Arabia iko mbioni kununua silaha za nyuklia iwapo tishio inaloliona kutoka Iran halitadhibitiwa).Lakini hofu hiyo inaongezeka pia kutokana na taarifa zinazodai kwamba Russia imekuwa ikizidisha uzalishaji wa silaha hizo,na kutokana na mazingira ya kihistoria na sababu za kiuchumi,nchi hiyo inaweza kuuza teknolojia na silaha za nyuklia kwa “mikono isiyostahili” (wrong hands).Je kuna uwezekano kwa nchi kama Iran,China au Russia kuuza uwezo wa kinyuklia kwa kikundi kama Al-Qaeda?Jibu langu ni hapana.Kwanini?Kwa vile naamini nchi hizo zina busara ya kutosha ya kutofanya kosa la aina hiyo ambalo pia linaweza kuwagharimu hata wao.Je kuna uwezekano wa vita vya kinyuklia kati ya taifa moja na jingine?Sidhani kama uwezekano huo ni mkubwa sana japo upo kwa mbali.Je kuna uwezekano wa shambulizi la kikemikali au kibaiolojia litakalofanywa na kikundi cha kigaidi?Jibu la kutisha ni kwamba uwezekano huo upo kwani malengo ya mashambulizi yanayofanywa na vikundi hivyo yamekuwa ni kusababisha vifo vingi,na silaha gani ni bora zaidi katika kuleta madhara ya juu kabisa zaidi ya silaha hizo.Na inajulikana kwamba vikundi vya kigaidi vimekuwa vikihangaika sana kupata teknolojia na silaha za aina hiyo.Hiyo ndio dunia tunayoishi sasa.

Tuangalie mambo yalivyo huko nyumbani.Habari zinazovuma kwa sasa ni madai ya rushwa kwenye mchakato kuelekea kwenye uchaguzi ndani ya CCM.Naamini kuwa wanaofuatilia makala zangu wanafahamu bayana msimamo wangu dhidi ya rushwa na wala rushwa.Lakini niseme bayana kwamba madai ya rushwa kwenye uchaguzi huo hayanishangazi hata kidogo.Nadhani tatizo liko kwenye mkanganyiko wa suala zima la matumizi ya fedha katika harakati za kisiasa.Sidhani kama niko peke yangu katika kuamini kwamba nchi yetu inaimba wimbo wa Ujamaa ilhali staili ya kucheza wimbo huo ni ya Ubepari.Na ukiangalia kwa mfano namna mbio za kuelekea Ikulu ya Marekani hapo mwakani utabaini kwamba matumizi ya fedha ni makubwa sana.Tofauti yao na sisi ni kwamba kuna utaratibu maalumu uliowekwa katika namna gani mtu anaweza kuchangisha fedha,kutoa misaada au zawadi au hata namna ya kutoa fedha kwa ajili ya kujiimarisha kisiasa.Mantiki nyepesi ni hii: ukiwa unahitaji nafasi flani basi yayumkinika kusema kwamba utatumia kila nyenzo uliyonayo kuhakikisha unapata nafasi hiyo.Kinachodhibiti matumizi mabaya ya nyenzo hiyo ni sheria zinazotekelezeka na kufuatiliwa kwa makini.Wanachofanya watoa rushwa katika mchakato huo wa uchaguzi wa CCM ni kutumia “nyenzo” (fedha) walizonazo.Wanaofanya hivyo wanajua bayana kwamba kutumia uwezo sio kosa alimradi kama wanazingatia sheria zinazotawala zoezi zima.Lakini hawajali sana kuhusu kuvunja sheria kwa vile kwa namna flani mazingira yanawapa nafasi ya kufanya hivyo.Rushwa ni kama mmea,unastawi pale tu kwenye ardhi yenye rutuba.Inahitajika busara ya namna flani kuelewa nachomaanisha hapa vinginevyo unaweza kunishangaa kwa kudhani natetea matumizi ya rushwa kwenye jamii yetu.

Mwisho ni habari mbili za kusikitisha zilizojiri mwishoni mwa wiki.Ya kwanza ni matokeo mabaya ya Taifa Stars.Katika hilo naweza kuwafariji Watanzania wenzangu kwamba hata hapa Scotland,ambapo wana kila nyenzo wanayohitaji,timu yao ya taifa imehangaika kweli kufika ilipo sasa.Mafanikio ya Taifa Stars hayawezi kupatikana “overnight.” Tujifunze kwa hawa wenzetu ambao kwao matokeo mabaya ni changamoto ya kujipanga vyema kwa ajili ya mashindano yajayo.Hilo linawezekana kama kutakuwa na subira,uvumilivu na mipango bora.Kutambua ugonjwa,kupata dawa ya ugonjwa huo na kuitumia dawa husika ni hatua tu ya kuelekea kupona,haimaanishi kuwa ugonjwa utaondoka dakika hiyohiyo.Inaweza kufikia wakati ikalazimu kubadili dawa.Tuwe na subira,tutafika.Habari ya pili ni vifo vya Watanzania wenzetu katika ajali huko Mbeya.Hivi maisha ya wenzetu yataendelea kupotea hadi lini?Mbunge Shabbiby aliongea bungeni kuhusu “usanii” unaofanywa na baadhi ya wamiliki wa mabasi ambapo wanapandikiza bodi mpya za mabasi hayo kwenye chasis za zamani au za malori.Simaanishi kuwa basi lililopata ajali ni miongoni mwa yaliyofanyiwa usanii huo lakini kinachosikitisha ni kwamba mamlaka husika bado hazijaanza kufanyia kazi ushauri wa Mbunge huyo.Lakini eneo jingine linalopaswa kurekebishwa kwa haraka ni sheria za usalama barabarani.Semina lukuki na maadhimisho ya kila mwaka ya wiki ya “nenda kwa usalama barabarani” hayawezi kuepusha ajali zinazopoteza maisha takriban kila wiki pasipo kuzisimamia kwa makini sheria zilizopo.Yule “mzalendo” aliyekuja na wazo la “spidi gavana” alikuwa na busara sana lakini sijui mkakati huo umefia wapi!!!Tukiendelea kuamini kuwa spidi gavana bora ni madereva na askari wa trafiki basi, “unfortunately”,habari za kuhudhunisha kuhusu ajali zitaendelea kutusumbua kwa muda mrefu.

Alamsiki

27 Jul 2007

Asalam aleykum,

Katika makala iliyopita niliwapa kituko kimoja kuhusu memba 7 wa kabineti ya Bwana Gordon Brown ambao walikiri hadharani kuwa walishawahi kuvuta bangi wakati wa ujana wao.Maendeleo zaidi (“update”) kuhusu stori hiyo ni kwamba hadi sasa idadi hiyo imefikia mawaziri 10.Lakini wananchi wanaonekana hawajashtushwa sana na “confessions” (vitubio…naamini niko sahihi hapa,au kuna neno jingine linalowakilisha wingi wa kutubu?BAKITA msaada tafadhali) pengine kwa sababu wananchi mawaziri hao watahukumiwa na utendaji wao wa kazi na sio historia zao za kale.Joji Bushi,huyu raisi wa sasa wa Marekani alikuwa “mtu wa matingas” (mlevi) kabla hajamrejea Bwana,lakini ulevi wake wa zamani haukuwa kikwazo kwa yeye kugombea nafasi hiyo ya juu kabisa ulimwenguni.Hata mie nadhani sio vema kumhukumu mtu kwa mambo alofanya zamani,alimradi anayofanya sasa yawe yanaridhisha.Wengi tunafahamu kwamba kuna wale waliosoma seminari na baadae kuingia kuutumikia umma,lakini si ajabu kukuta baadhi yao ni wala rushwa.Kwa maana hiyo,yayumkinika kusema kuwa bora kuwa mtu ambaye kwenye ujana wake alifanya mambo yasiyopendeza lakini sasa anafanya yale yanayotakiw,a kuliko yule ambaye CV yake ya ujana wake ni “supa” lakini kwa sasa anashiriki kuhujumu uchumi wa Taifa letu “changa” (nadhani neno “changa” sasa limeshapitwa na wakati maana taifa letu lina umri wa miaka 45,na naamini huko mtaani ukimwita mtu mwenye umri huo “mchanga” basi patakuwa hapakaliki hapo).

Kwa wale waliokuwa wanafuatilia stori ya Shambo,yule ng’ombe “mtakatifu” kwa Wahindu wa huko Skanda Valle,magharibi ya Wales,habari “latest” ni kwamba “ng’ombe-mungu” huyo amepelekwa mbele ya haki baada ya polisi 30 kuvamia hekalu lake na kumchukua kwa ajili ya kwenda kumchinja.Kwa wale ambao stori hii iliwapitia kando,ni kwamba Shambo alitakiwa kuuwawa baada ya kugundulika kuwa ana kifua kikuu (TB),na hivyo kuhatarisha afya za mifugo mingine katika eneo hilo.Lakini,Shambo si ng’ombe wa kawaida,bali ni “mungu” wa Wahindu,na waumini waliapa kuwa hawako tayari kuona “mungu” wao huyo akiuawa na binadamu.Baada ya mamlaka husika (DEFRA) kuwafahamisha waumini kuwa Shambo anapaswa kuuawa ili kuzuwia kuenea ugonjwa aliokuwa nao.Waumini walipinga uamuzi huo na hatimaye wakakata rufaa Mahakama Kuu ambapo amri ya kumuua “mungu” huyo ilitengeliwa.Lakini mamlaka husika zikaamua kukata rufaa Mahakama ya Rufaa ambapo iliamualiwa kuwa Shambo anastahili kuuawa.Zoezi la kumchukua “ng’ombe-mungu” huyo halikuwa jepesi kwani waumini walijitutumua kadri ya uwezo wao kuhakikisha kuwa Shambo hachukuliwi,na hapo ndipo ikabidi waletwe polisi kumaliza songombingo hiyo iliyochukua zaidi ya masaa 12,huku sakata zima kati ya waumini na DEFRA likiwa limedumu kwa wiki 12.Pengine kufanana kwa namba 12 katika matukio hayo kunaweza kuwa uhusiano na “umungu” wa ng’ombe huyo.

Tukiachana na “safari ya mwisho” ya ngombe-mungu Shambo,tuelekeze macho yetu huko nyumbani.Hebu ngoja kidogo.Kuna nchi inaitwa Guam.Je unaweza ku-guess iko wapi?Enewei,nilikuwa nachemsha kidogo ubongo wako.Nchi hiyo ni “koloni” la Marekani (well,iko chini ya mamlaka ya Marekani) na kwa mujibu wa sensa ya karibuni Guam ina wakazi 173,456.Bila kuingia kwa undani kuhusu jiographia,siasa na porojo nyingie kuhusu ka-nchi hako ambako ni kisiwa,ngoja nikudokezee kuhusu timu yake ya taifa.Hebu angalia matokeo ya mechi zake za hivi karibuni.Ilifungwa 10-0 na China,ikafungwa 15-1 na Hong Kong,na ikalambwa 9-0 na Korea ya Kusini.Kwa sasa inashilia nafasi ya 199 kwenye listi ya FIFA ya ubora wa soka duniani.Nafasi hiyo ndio ya mwisho kabisa,lakini habari njema kwa nchi hiyo ni kwamba haiko pekee kwenye nafasi hiyo kwani Djibouti, East Timor, Belize, the US Virgin Islands, Montserrat, American Samoa, Sao Tome e Príncipe na Aruba pia zinashikilia kwa pamoja nafasi hiyo ya 199.Wahenga walisema kilio cha wengi ni harusi.Kocha wa timu hiyo anawalaumu zaidi wachezaji wake kwa tabia yao ya kuendekeza pati,kujichanganya na magelifrendi wao (au wake zao) na kuthamini zaidi mambo ya binafsi kuliko majukumu yao ya soka.Pia wachezaji wa timu hiyo wanashutumiwa kwa kuzembea mazoezi,na hata wanapofika mazoezini wengi wao huwa wamechoka kutokana na “kujirusha” (sio kujirusha kimazoezi bali “kiaina”).Kiungo wa timu hiyo,Alan Jamison,ameeleza kuwa mara kwa mara akiwa usingizini amekuwa akisumbiliwa na ndoto moja:anaota kuwa amefunga goli (la mpirani…) na uwanja unalipuka kwa mayowe.Kwa bahati mbaya kila asubuhi anapoamka anagundua kuwa timu yake haijapata na haitarajii kupata ushindi hivi karibuni.

Nimeizungumzia timu ya taifa ya Guam ili kutengeneza mazingira mazuri ya kuitupia madongo timu yetu ya iliyokwenda kutuaibisha huko Aljeria.Kulikuwa na umuhimu gani wa kuingia gharama ya kuwapeleka watalii hao kama walikuwa hawajajiaanda kwa mashindano?Enewei,mie najua kwanini walipelekwa hivyohivyo:POSHO.Posho ya safari.Linapokuja suala la posho ya safari usishangae chama cha mchezo wa bao au drafti (kwa mfano) kumpeleka mchezaji kipofu.Wanajua kabisa kuwa kipofu hawezi kucheza drafti au bao lakini hilo haliwasumbui viongozi hao kwani tayari watakuwa wamejipatia visenti vya kupeleka kwenye nyumba ndogo zao (utafiti usio rasmi umeonyesha kuwa asilimia kubwa ya fedha inayopatikana kwa rushwa au ubadhirifu inaishia kwenye nyumba ndogo).Viongozi walichagua wanamichezo wazembe wanastahili lawama nyingi zaidi kuliko wazembe hao waliokwenda kututia aibu huko Aljeria (ukiachia huyo mmoja aliyeambulia medali ya fedha).Nawalaumu zaidi viongozi hao kwa vile hawana cha kujitetea kwa kuchagua wanamichezo wasio na uwezo wa kutuletea ushindi.Angalau timu ya taifa ya Guam inaweza kujitetea kwani kijinchi chenyewe kina watu wachache zaidi ya wilaya ya Kinondoni.Tanzania ina watu zaidi ya milioni 30,na miongoni mwao ni wanamichezo wenye vipaji ambavyo aidha vinapuuzwa,haviendelezwi au vinaminywa na viongozi walafi wa madaraka na fedha lakini hawana hata chembe ya mawazo endelevu ya ushindi kwenye michezo.Kwenye nchi za kidikteta viongozi kama hawa wanaporejea kutoka mashindanoni wanapokelewa na karandinga kuelekea Segerea.

Majuzi tumesikia EWURA ikidai kwamba waziri Meghji kadanganya kuhusu uwezo wa mamlaka hiyo kuwabana wafanyabiashara wa mafuta.Sijui nani anasema ukweli kwani sijaona sheria iliyoanzisha mamlaka hiyo ila ni dhahiri kuwa kuna kitu hakiko sawia.Kuna umuhimu gani wa kuwa na mamlaka isiyo na uwezo wa kisheria katika kutekeleza majukumu yake?Au kwa mfano sahihi,kuna umuhimu gani wa kufuga mbwa mwenye mapengo na ambaye akisikia kelele za “mwizi,mwizi” anakwenda kujificha?Inanikumbusha mchapo mmoja nilowahi kusimuliwa huko Tanga kuwa baba mwenye nyumba mmoja alipoamshwa na mkewe na wanawe kuwa wamesikia watu wanavunja dirisha akaanza kulia na kuwaacha watoto hawajui la kufanya.Tukiachana na mifano hiyo,swali la muhimu ni kuwa hivi huku kurushiana mpira kunamsaidia vipi mwananchi wa kawaida?Nilishapendekeza huko nyuma kwamba njia nyepesi ya kudhibiti bei ya mafuta ni “kuchimba mkwara wa nguvu” kwamba atakayezidisha bei stahili ya mafuta atafutiwa leseni.La muhimu hapa sio kwamba amri hiyo itolewe na Meghji au EWURA,bali itekelezwe.Hakuna mfanyabiashara aliye tayari kufutiwa leseni na kwa hakika watatekeleza amri hiyo.

Mwisho,tumeambiwa na Profesa Maghembe kuwa wizara yake ina baadhi ya watendaji ambao kwa jina jepesi tunaweza kuwaita mafisadi.Hao ni pamoja na wale wanaoshiriki kwenye biashara ilopigwa marufuku ya kusafirisha magogo nje.Waziri anastahili pongezi kwa kuweka bayana uozo huo.Lakini unategemea nini kwenye wizara ambayo Severe alipewa uhamisho na akagoma kuhama na hadi leo bado anapeta?Prof Maghembe anasema amepeleka majina ya wahusika kwenye “ngazi za juu” kwa vile yeye hana uwezo kisheria kuwawajibisha.Pengine tunachopaswa kufahamu ni kuwa lini majina hayo yamewasilishwa huko ngazi za juu,na kwanini mafisadi hao bado wanaendelea kuuza maliasili zetu.Sintoshangaa kusikia mmoja wao akiitisha press conference kama ile ya gavana wetu na “kutupa somo la uzalendo.”Kwa vile mafisadi hawa wanajulikana,kuendelea kuwaacha madarakani ni sawa na kuwapa nafasi ya kufuja kwa kasi zaidi (kwa vile wanaelewa kuwa maamuzi kutoka “ngazi za juu” yanaweza kuwahamisha kutoka kwenye ulaji) na kuharibu ushahidi dhidi ya tuhuma zinazowakabili.Sheria ichukue mkondo wake ili kuzuia virusi vya ufisadi kusambaa zaidi (wanaoona mafisadi hao wanazidi kupeta wanashawishika kuiga ufisadi wao).

Nimalizie kwa kumpongeza Waziri Mwapachu kwa kuhitimisha bethidei yake kwa kuwatembelea watumishi wa Wizara yake huko Dodoma.Ni mfano wa kuigwa.Pia hoja yake ya kuwa na “data bank” ya simu ni nzuri (japo ufanisi wake ni mgumu) na inaweza kuigwa kwenye maeneo mengine kwa mfano kuanzisha daftari la kudumu la wala rushwa.

Alamsiki


20 Jul 2007

Asalam aleykum,

Juzi nilipata barua-pepe kutoka kwa rafiki yangu mmoja aliyeko huko nyumbani.Huyu jamaa alikuwa akinilaumu “kirafiki” kwamba inaelekea nimeanza kuishiwa pointi za kuandika ndio maana takriban nusu ya makala yangu iliyopita ilikuwa ina habari “nyepesi nyepesi.”Sikukasirika kwani siku zote nathamini sana ushauri wenye lengo la kujenga au kuleta maendeleo.Nilimjibu kwamba nina pointi lukuki za kuandika,lakini kuna wakati inabidi “tupunguze kasi ya maisha” kwa kuangalia habari za vituko mbalimbali hususan vinavyojiri huku Ughaibuni.Pia nilimhakikishia kuwa “nyepesi nyepesi” hizo sio “fiksi” bali ni habari zinazohusu matukio ya kweli,ila tu yanachekesha kwa namna moja au nyingine.Kicheko ni afya.

“Nyepesi” za wiki hii ni pamoja na taarifa kwamba “wanene” 7 ndani ya baraza jipya la mawaziri la Gordon Brown (mrithi wa Tony Blair) wamekiri katika nyakati tofauti kuwa walishawahi kutumia “widi” (kwa wale ambao lugha ya mtaani ni mgogoro, “widi” ni bangi au marijuana).Siku kadhaa zilizopita,kiongozi wa chama cha wahafidhina (Conservative Party) David Cameron naye alijikuta kwenye wakati mgumu baada ya kupatikana nyeti kuwa alikuwa akivuta bangi katika siku za ujana wake.Cameron amekataa kuendelea na mjadala wa suala hilo akisema kuwa kila binadamu anaweza kufanya makosa hususan akiwa kijana.Alitaka wanaomshupalia wamhukumu kwa utendaji wake wa kazi wa sasa na sio mambo aliyofanya nyma.Kali zaidi ya zote ni pale Katibu wa Ofisi ya Mambo ya Ndani (Home Office-yaani ni sawa na Wizara ya Mambo ya Ndani huko nyumbani),Jacqui Smith,na waziri mmoja katika ofisi hiyo (hapa katibu wa wizara ni mkubwa kicheo kuliko waziri),Tony McNulty,walipotangaza hadharani kuwa nao walishawahi kuvuta bangi huko nyuma.Na “ushuhuda” huo umekuja wakati mwanamama huyo (Smith) akitangaza mpango wa serikali kuangalia upya uamuzi wa awali wa serikali ya Blair wa kushusha daraja (declassifying) la bangi.Habari kwamba viongozi hao wawili (ambao pamoja na majukumu mengine wana dhamana ya kudhibiti mihadarati) waliowahi kuwa wavuta bangi zimezua mjadala kama kweli wanapaswa kuendelea na nyadhifa zao.Pengine kinachowasaidia ni ukweli kwamba kuna wanasiasa wengine (wakiwamo mawaziri vivuli wa upinzani) ambao nao wameweka bayana kuwa walishawahi kuvuta bangi walipokuwa vijana.Uwazi na ukweli au vituko vya siasa?


Kuna habari nyingine ya majonzi lakini kwa namna flani inaweza inachekesha.Mwanamke aliyekuwa na uzito mkubwa kuliko wote hapa Uingereza,Nazima Hussein,amefariki na kuwaacha wanandugu wakiwa na wakati mgumu baada ya kubambikwa ushuru wa pauni 4,000 (zaidi ya shilingi milioni 8) kutoka kwa manispaa huko Southall,London.Ushuru huo ulitokana na gharama za kuuhudumia mwili wa marehemu ambao ulihitaji watumishi wa kikosi cha zima moto (firemen) 13 kuutoa mwili huo (uliokuwa na unene wa futi 3) kutoka katika flati aliyokuwa akaishi.Na walipoufikisha mochwari huko Uxbridge ilizuka kasheshe nyingine kwani hakuna toroli la kubebea maiti lililomtosha marehemu na pia mafriji yote ya kuhifadhia maiti hayakuweza kumudu ukubwa wa mwili wa marehemu huyo.Marehemu Nazima alifariki akiwa na uzito wa kilo 349 .Habari njema ni kwamba baada ya watu wa Manispaa “kusomeshwa” walikubali kupunguza gharama hadi pauni 3,000 (zaidi ya shilingi milioni 6).Ukiskia msiba mzito ndio huo.

Turejee nyumbani.Siku chache taifa limepewa changamoto ya kutosha kutoka kwa JK kuhusu suala la “kupima ngoma” (ukimwi).Na kwa mujibu wa taarifa za magazeti mbalimbali ya huko nyumbani watu kadhaa wameitikia wito wa Rais kwa kwenda kwenye vituo vya afya kupima ukimwi.Kwa mtizamo wangu,hamasa aliyotoa JK inaweza kuwa na matokeo makubwa sana kwani kwa upande mmoja inaweza kuwasaidia wale waliokuwa hawajui kama wameathirika kuanza kuchukua tahadhari ambazo zitawasaidia kuishi maisha marefu zaidi.Pia kwa wale ambao vipimo vitaonyesha hawajaathirika wanaweza kuachana kabisa na matendo ya ngono zisizo salama,na hata kumrejea Mola wao.Kadhalika,kwa wale watakaokutwa wana virusi vya ukimwi na wakati huohuo wana familia zinazowategemea wanaweza kupata nafasi mwafaka ya kuandaa “future” za familia zao.Jingine ni kwamba kampeni hiyo inaweza kuwafumbua macho wale vichwa sugu na viwembe wanaopenda kujidanganya kuwa ukimwi ni ajali kazini,na eti ajali haina kinga.

Waziri wa Afya amelielezea Bunge kuwa kuna mpango wa kuwapima ukimwi wale wote wanaofika hospitali kwa matibabu.Wazo hilo ni zuri sana lakini linahitaji tahadhari ya namna flani.Wapo wanaosema kuwa ukimwi ni sawa na maradhi mengine yasiyo na tiba kama kansa au kisukari.Hapana,ukimwi ni tofauti sana hasa kwenye namna jamii yetu inavyowaangalia walioathirika na ukimwi (unyanyapaa).Nadhani wapo watakaokubaliana nami kwamba baadhi ya watumishi wa taasisi za afya wana tabia ya kukiuka maadili ya taaluma yao kwa kutoa siri kuhusu afya za wagonjwa.Naamini baadhi ya wasomaji wameshawahi kunong’onezwa na dokta au nesi flani kuwa “yule nanihii anao (ukimwi).” Sasa kama Wizara ya Afya itatekeleza dhamira yake ya kutaka watu wote wanaofika hospitali wapime ukimwi inapaswa pia kuboresha mambo kadhaa ikiwa pamoja na kuhakikisha kuna washauri nasaha wa kutosha watakaoweza kuwasaidia hao watakaobainika kuwa “wanao.” Naamini pia kuwa kuna sheria inayowabana watumishi wa afya kutoa “siri” ya ugonjwa wa mtu,na katika mpango huu wa Wizara ni muhimu sheria hiyo ikaimarishwa zaidi kwani bila kufanya hivyo si ajabu watu wanaweza kukwepa kwenda hospitali sio kwa kuhofia kupimwa na kukutwa wanao bali kwa kuwaogopa hao wauguzi wasioweza kuhifadhi siri za wagonjwa.Pia Wizara inapaswa kuweka bayana iwapo mpango huo wa kumpima kila mgonjwa utakuwa ni suala la hiari au la lazima.Kwa hapa,wagonjwa wanahamasishwa kupima ukimwi lakini hawalazimishwi.Pasipo kuweka misingi mizuri,nia nzuri ya Wizara ya Afya inaweza kuleta mkorogano usio wa lazima,maana si ajabu tukasikia flani kanyimwa nafasi ya kuonana na daktari kwa vile tu kukataa kupima ukimwi.Ifahamike kuwa suala la kupima au kutopima ni haki ya mtu binafsi.

Pia nimesoma habari iliyonisikitisha husu kilio cha Kamisheni ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kwamba imekuwa ikipata ushirikiano hafifu kutoka kwa waajiri katika suala la kuhakiki vyeti vya taaluma za waajiriwa.Unajua utandawazi umeleta mambo mengi sana ikiwa ni pamoja na fursa ya mtu kujipatia taaluma bila kutia mguu chuoni.Vipo vyuo kadhaa duniani vinavyotoa kozi kwa njia ya mtandao,lakini tatizo ambalo limekuwa likizisumbua hata nchi za Magharibi ni lile la baadhi ya vyuo vya kitapeli ambavyo vinaweza kukupatia cheti cha Udaktari wa Falsafa kwa wiki moja.Ukiona mfumuko wa madokta (sio wale wa hospitali) usikimbilie kufikira kuwa pengine siku hizi PhD zimekuwa rahisi.Ukweli ni kwamba PhD feki zimetapakaa sana kutokana na vyuo feki (japo vingine vimeandikishwa kisheria) ambavyo wanachojali wao ni fedha tu ya huyo anayehitaji PhD ya chapchap.Inatuuma sana sie wengine ambao tunazeekea maktaba kutafuta huo udokta “wa kwelikweli” huku wenzetu “wanasomea baa au kwenye nyumba ndogo zao” na wanaamka asubuhi na “hangover” wakiwa madaktari wa falsafa.Nadhani falsafa pekee waliyonayo “vilaza” hawa ni kuhusu waganga gani wa kienyeji wanasaidia mtu kula rushwa na aendelee kuonekana mwadilifu au namna ya kutogonganisha magari kati ya mama watoto na nyumba ndogo.

Ukweli mchungu ni kwamba TCU ina wakati mgumu kufanikiwa katika azma yake hiyo njema,kwani wengi wetu tunajua kuwa baadhi ya waajiri nao wana elimu za kutilia mashaka.Pia nadhani kuna mapungufu ya kisheria kuhusu matumizi ya vyeti feki,kwani nakumbuka jeshi la polisi halikuchukua hatua yoyote lilipobaini kuwa mbunge mmoja hakuwa mkweli kuhusu elimu yake ya sekondari.Sasa kama ufeki wa vyeti vya sekondari “sio big deal” kwa polisi je hao wenye PhD feki wataweza kuguswa?Enewei,tuna vita kadhaa tunazopenda zianze dakika hii:dhidi ya wala rushwa,majambazi,wabadhirifu,wauza unga,nk.Pengine siku moja itatangazwa vita ya kitaifa dhidi ya vyeti na taaluma feki.Yote yanawezekana.

Alamsiki


18 Jun 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum wasomaji wapendwa wa gazeti hili.

Leo tuzungumzie muziki.Muda mfupi uliopita nilikuwa nasoma makala flani kumhusu msanii wa kizazi kipya Albert Mangwea.Yalikuwa ni mahojiano kati ya msaanii huyo na tovuti ya Darhotwire.com.Niliguswa sana na kilio cha msanii huyo ambacho kimekuwa pia kikisikika kutoka kwa takribani kila msanii wa Bongofleva.Kuna wajanja flani,(hapana,hawa si wajanja,bali ni WEZI) ambao wamekuwa wakiwanyonya vijana wetu bila hata chembe ya huruma.Wezi hawa wanafahamika zaidi kwa jina la “wadosi”.Binafsi sijui kwanini wanaitwa wadosi lakini la muhimu hawa sio jina wanaloitwa bali unyonyaji wanaowafanyia wasanii wetu.

Pengine kabla ya kujadili wizi wa mchana mweupe unaofanywa na wadosi hao,tuangalie maendeleo ya Bongofleva huko nyumbani na huku Ughaibuni.Mimi ni mfuatiliaji sana wa mambo yanayotokea huko Bongo. “Ibada” yangu ya kila asubuhi inaanza kwa kutembelea tovuti za ki-Tanzania ili kujua yanayojiri huko.Sasa,kabla ya kuja huko mwaka jana mwishoni mwa mwaka jana nilikuwa nahisi kuwa habari kwamba Bongofleva imeikamata Tanzania kwa “kasi ya tsunami” ni porojo tu.Lakini nilipokuja nilishihudia mwenyewe jinsi gani hatimaye nyimbo zinazotengenezwa na kuimbwa na Watanzania zilivyokamata soko na mioyo ya wapenzi wa muziki.Wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu nilibahatika kushuhudia tamasha la “Piga Kura au Upigike” kwenye viwanja vya Biafra Kinondoni.Licha ya picha kadhaa nilizochukua kwa ajili ya kuwajulisha marafiki zangu hapa,nilijionea jinsi gani watu wa rika mbalimbali wanavyovutiwa na kazi za wasanii wa muziki wa kizazi kipya.Nadiriki kuamini kuwa mashabiki waliofika viwanja hivyo walikuwa wanawakilisha karibu kila kona ya jiji la Dar es Salaam.Kitu kingine nilichobaini ni kwamba jinsi gani wasanii wanavyotumika katika masuala ya muhiu kwa Taifa.

Nakumbuka niliwahi kusoma katika gazeti moja la huko nyumbani kwamba msanii Juma Nature “alimfunika” mwenyeji wake-mgombea aliyemwalika msanii huyo katika kampeni zake.Yaani watu walikuwa na kiu zaidi ya kusikia muziki wa Nature kuliko hotuba ya mheshimiwa huyo.Na pengine umati kubwa uliojitokeza kwenye mkutano huo ulifuata buridani hiyo ya bure.Yayumkinika kusema kuwa mchango wa wasanii katika kufanikisha uchaguzi,na hata kuwapatia ushindi baadhi ya wagombea,ulikuwa mkubwa.Kwa bahati mbaya,au pengine kwa makusudi,baada ya kukamilisha kazi ya kuhamasisha jamii kuhusu uchaguzi na wagombea,wasanii wetu wamerudi kulekule walikokuwa:wamesahauliwa na wanaendelea kunyonywa.

Napenda kuwafumbua macho wasanii wetu kwa kuwaambia kuwa muziki wao huku guhaibuni unauzika sana miongoni mwa watu waliotoka Afrika Mashariki.Wamuulize Banana Zorro aliyealikwa hapo London kwenye pati ya Muungano,wamuulize Mr Nice,Ray C na TID,na Profesa J ambaye nasikia amewachengua vilivyo huko Sweden na Holland.Wasanii wa nyumbani wakija huku wanababaikiwa kama vile akina Shaggy au Sean Paul wanavyobabaikiwa wakija huko nyumbani.Lakini,safari za nje sio jambo la kukurupuka tu,ni kitu kinachotaka maandalizi.Kwa mantiki hiyo si lazima kusafiri ili kunufaika na kazi za sanaa bali hata kutafuta namna ya kupenyeza muziki katika soko la kimataifa kunaweza sana kuwainua wasanii wetu.Hivi wasanii wetu wanajua kuwa CD zao huku zinauzwa hadi paundi 10 (zaidi ya shs 24,000/=)?Nimesoma kwenye internet kwamba tarehe 12/06/2006 kampuni moja iitwayo Townsend Records itatoa CD iitwayo Bongoflava (Swahili Rap from Tanzania) ambayo itauzwa paundi 10.99 (takriban shs 27,000/= kwa exchange rate za leo).Sijui kama na hawa ni wadosi au la,lakini huo ni uthibitisho kuwa Bongoflava ina soko zuri tu kuhu Ughaibuni.Na watu wanapenda kweli kazi za wasanii wa nyumbani.Niliporudi kutoka Tanzania jamaa zangu kibao walikuwa wananiulizia kama nimekuja na CD za Bongofleva.Kila mmoja anasema wanaposikia wasanii wetu wanakumbuka sana nyumbani.

Mheshimiwa Kikwete alinukuliwa akiwataka Watanzania walioko nje kuwasaidia wenzao walio nyumbani hasa katika nafasi za masomo.Ujumbe huo unaweza pia kupanuliwa na kuwahusisha wasanii wa nyumbani,kwa maana kuwa Watanzania walio nje hasa wale wenye upeo na mambo ya muziki wawasaidie wasanii wetu wa nyumbani kwa namna yoyote ile inayowezekana.Lakini ili hilo liwezekane wasanii wetu hawana budi “kuchangamka.”Wanaoitwa “wadosi” wanawanyonya na kuwaibia kwa vile wanajua dhahiri kuwa wasanii hao hawana njia mbadala.Jamani,dunia siku hizi imekuwa kama kijiji (japo ni kinadharia) na unachohitaji ni kwenda tu kwenye internet café na kuperuza kurasa za mtandao kujua wapi unaweza kupata huduma au kuuza ulichonacho kwa mtu aliye bara jingine.Hapa ndipo umuhimu wa shule (elimu) unapojidhihirisha.Lakini hata kama shule haipandi,si unaweza kumwomba rafiki yako akusaidie kutafuta soko la kazi zako za sanaa nje ya nchi?

Serikali inapaswa kuwasaidia wasanii wetu kwa kuipa meno sheria ya hatimiliki.Sambamba na hilo ni wasanii wenyewe kusimama kidete kutetea maslahi yao badala ya kuendelea kulalamika au kufikiria kuingia kwenye fani nyingine kukwepa wizi wa kazi zao.Pia wasione aibu kuomba msaada kwa wenzao walio nje.Mwisho naiomba serikali ipanue vita dhidi ya wala rushwa na majambazi na kujumuisha “wadosi” pia.

Alamsiki

KULIKONI UGHAIBUNI:

Mambo?

Siku chache zilizopita nilibahatika kuwa na maongezi na babu mmoja wa Kiskotishi ambaye kwa maelezo yake mwenyewe yeye ni “mkazi wa dunia nzima” (global citizen).Babu huyo anadai kuwa dunia ingekuwa mahala bora sana kama kusingekuwa na mipaka na sheria kali za uhamiaji.Na katika kutimiza azma yake ya kuwa mkazi wa dunia nzima anadai ametembelea takribani nchi 10 katika kila bara.Sijui kama alikuwa anasema ukweli au “ananifunga kamba” tu.Katika maongezi yetu hayo aligusia jambo flani ambalo liliniingia sana na ambalo ndio mada yangu ya wiki hii:UZALENDO.

Kwa mujibu wa babu huyo,enzi zao wakiwa vijana suala la uzalendo lilikuwa likitiliwa mkazo sana.Alidai kuwa japo kwa sasa hali ni tofauti kidogo lakini bado nchi nyingi za magharibi zinatilia mkazo sana suala hilo.Alieleza kwamba akiwa kijana babu yake alikuwa akimwambia kuwa mazingira mazuri watakayoyaweka wakati huo yatakuja kuvinufaisha zaidi vizazi vijavyo.Baba yake pia alikuwa akimweleza hivyo hivyo.Na yeye alipokuwa mtu mzima alikuwa akiwaeleza wanae hivyohivyo.Na sasa anasema amekuwa akitoa changamoto ya aina hiyohiyo kwa wajukuu wake.Furaha aliyonayo ni kwamba utabiri wa babu na baba yake umetimia.Maendeleo yaliyopo hivi sasa yamechangiwa na msingi mzuri uliojengwa karne kadhaa zilizopita.Na kilichowasukuma hao waliotengeneza misingi hiyo si kingine zaidi ya uchungu wao kwa taifa lao na vizazi vijavyo.

Huko nyumbani kuna tatizo kuhusiana na suala la uzalendo.Wapo wapuuzi fulani ambao wanaendesha mambo utadhani hakuna kesho au labda Tanzania haitakuwepo miaka 50 ijayo.Na hawa ndio baadhi yao waliripotiwa kutishia maisha ya waandishi wa KULIKONI na THIS DAY kwa sababu magazeti hayo yameapa “kula nao sahani moja” (kuwaweka hadharani).Hawa ni watu ambao hawana uchungu si kwa nchi yao tu bali hata kwa wajukuu zao.Ukweli ni kwamba mtu anayekula fedha iliyotolewa kwa ajili ya ujenzi wa shule hana upeo wa kufikiria kwamba kwa kufanya hivyo huenda wajukuu wa mtoto wake wa mwisho watakaopaswa kwenda shule miaka 20 ijayo wanaweza kukosa nafasi hiyo kwa upuuzi uliofanyika mwaka 2006.Kuna watu wanafanya mchezo na maisha ya Watanzania wenzao kwa kutumia fedha za wenzao bila hata kuwashirikisha hao waliowekeza.Jamani,hata sheria za kawaida mtaani si kwamba bwana au bibi harusi mtarajiwa hawezi kutumia michango ya harusi yake mwenyewe pasipo kuwajulisha wanakamati?Sembuse hao ambao wamekabidhiwa fedha ambazo baadae wanapaswa kuzirejesha kwa wahusika!Nadhani mnaniapata hapo.

Wabadhirifu wa mali za umma na wala rushwa ni sawa na majambazi tu.Ni majambazi ambao silaha yao kubwa ni dhamana walizokabidhiwa kuwatumikia wananchi.Majambazi hawa wanachoiba sio fedha tu bali hata haki za Watanzania wenzao.Na kama walivyo majambazi wengine,hawa wakishahisi kuwa wanafahamika hukimbilia kutumia silaha kuu mbili:rushwa na vitisho.Kama gazeti linachimba maovu yanayofanywa na watu flani wasio na uchungu na nchi yao,basi waandishi wa gazeti hilo watafuatwa ili “wadakishwe kitu kidogo kuua soo.”Na itapoonekana kuwa gazeti hilo na waandishi wake wako ngangari katika kutetea maslahi ya Taifa na hivyo kukataa kuuza taaluma yao kwa kupokea rushwa basi hapo ndipo vitakapoanza vitisho.Sio huko nyumbani pekee ambako waandishi wa habari wanaovalia njuga kufichua maovu katika jamii wanakumbana na vitisho kutoka kwa wahusika.Mwaka 1996,Veronica Guerin, mwandishi wa habari wa kike huko Northern Ireland alipigwa risasi na kuuawa kutokana na makala za uchunguzi kuhusu biashara ya madawa ya kulevya nchini humo.Mwaka juzi,waandishi kadhaa wa magazeti ya Daily Record na Sunday Mail ya hapa Uingereza waliripoti kupokea vitisho kutokana na habari za uchunguzi walizokuwa wakiandika kuhusiana na magenge ya uhalifu.Kadhalika,mwaka jana waandishi wa habari wa magazeti kadhaa nchini Italia waliripoti kupokea vitisho baada ya kuripoti tuhuma za rushwa kuhusiana na klabu ya soka ya Genoa ya nchini humo.

Mifano hiyo michache inaonyesha ni jinsi gani watu waovu wanavyopenda kuendelea na maovu yao bila kubughudhiwa.Lakini haiwezekani watu wenye uchungu na nchi yetu wawaachie kufanya ufisadi wao wapendavyo.Naamini kila mzalendo anaelitakia mema Taifa letu atahakikisha kuwa wanahabari wanaosimama kidete kuwafichua wala rushwa na wabadhirifu hawabughudhiwi hata kidogo.Mjenga nchi ni mwananchi na mvunja nchi ni mwanachi pia.Tukiendelea kuwalea hawa majambazi wa mali na haki zetu basi tujue kuwa sio tu tunajitengezea “future” mbaya bali pia vizazi vijavyo vitatuhukumu kwa kuwaachia watu wachache wasio na uchungu na nchi yetu kutuharibia mambo.Tukiamua kwa nia moja tunaweza kuwadhibiti majambazi hao.

Alamsiki.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.