Showing posts with label Rais John Magufuli. Show all posts
Showing posts with label Rais John Magufuli. Show all posts

7 Dec 2016

ANGALIZO: Makala hii ilipaswa kuchapishwa katika toleo la wiki iliyopita la gazeti la Raia Mwema lakini haikuchapishwa kutokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu.

Mwanzoni mwa mwezi huu, Rais Dokta John Magufuli alitimiza mwaka kamili tangu aapishwe kuwa Rais wa tano wa nchi yetu. Nyingi ya tathmini mbalimbali zilizofanyika kuhusu mwaka wake mmoja wa urais zilionyesha anafanya kazi nzuri.

Hata hivyo, tukifuatilia kwa karibu utendaji kazi wa Rais, twaweza kubaini kuwa baadhi ya mawaziri wake hawaendani na kasi yake. Katika mazingira ya kawaida, Rais angelazimika kuchukua hatua pale tu hatua stahili zisingewezekana kufanywa na mawaziri wake.

Japo wanachohitaji wananchi ni kuona serikali inachukua hatua stahili, lakini suala la mtendaji gani wa serikali anayechukua hatua husika linaweza kueleza kiwango cha ushirikiano na uchapakazi kwa pamoja.

Na kwa ‘kusubiri hadi Rais achukue hatua’ kuna uwezekano wa kujengeka taswira kuwa ‘Rais anaingilia kazi za watendaji wake,’ au mbaya zaidi ni pale maagizo yake yatapokutana na upinzani wa namna flani.

Mfano mzuri ni hatua ya majuzi ambapo Rais aliitumbua Bodi ya Mamlaka ya Mapato (TRA).  Baadaye alieleza kuwa Bodi hiyo iliyokuwa na watendaji hao wakuu wa idara na taasisi za Serikali ilifanya dhambi ya kuidhinisha uamuzi wa menejimenti kuweka mabilioni ya shilingi katika benki za binafsi.

Juzi hapa tumekuta Sh26 bilioni zilizokuwa zimetolewa TRA kwa ajili ya matumizi ya TRA zikapelekwa kwenye mabenki matatu kama ‘fixed deposit account’ na bodi ikapitisha. Ndiyo maana nilipozipata hizo hela; hela nikazichukua na bodi kwaheri,” Rais alikaririwa

Swali hadi hapo ni je Waziri husika na wasaidizi wake walikuwa wapi wakati hayo yanatokea? Je inawezekana maamuzi hayo ya menejimenti na Bodi ya TRA yalikuwa na baraka za Waziri husika, na ndio maana hakuna hatua zilizochukuliwa hadi Rais alipoingilia kati?

Miongoni mwa wajumbe wa Bodi iliyotumbuliwa ni Gavana wa Benki Kuu, Profesa Benno Ndulu, ambaye wiki iliyopita alinukuliwa akitoa kauli inayokinzana na msimamo wa Rais. Gavana Ndulu alidai kuwa TRA kuweka fedha kwenye fixed accounts sio kosa kisheria, na hakuna hasara kiuchumi kuweka fedha kwenye akaunti ya aina hiyo.

Kwa tunaojua ‘kusoma katikati ya mistari’ Tunaelewa bayana kuwa Gavana Ndulu alikuwa anamjibu Rais Magufuli. Na pengine sio kumjibu tu bali kumkosoa. Na hii si mara ya kwanza kwa ‘kiongozi huyo wa benki kuu kupishana lugha na Rais.’ Mwezi Machi mwaka huu Dkt Magufuli alifanya ziara ya kushtukiza huko Benki Kuu, ambapo pamoja na mambo mengine, alitoa agizo kwa Gavana Ndulu kupitia upya orodha ya wafanyakazi wa Benki hiyo, na kuwaondoa mara moja wale wote ambao hawana ulazima wa kuwa wafanyakazi katika benki hiyo.

Siku chache baadaye, Gavana huyo alinukuliwa na vyombo vya habari akieleza kuwa orodha yenye majina 14 ya ‘watoto wa vigogo’ iliyokuwa ikisambaa kwenye mitandao ya kijamii ‘haina jipya.’ Hata hivyo alieleza kuwa agizo la Rais kuhusu kupunguza wafanyakazi lingejadiliwa kwenye vikao vya taasisi hiyo na taarifa rasmi ingetolewa. Kwa kumbukumbu zangu, hadi leo hakujatolewa taarifa yoyote.

Wakati akieleza kuhusu sababu zilizopelekea kuvunja Bodi ya TRA, Rais pia aliionya Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) kwamba imepewa zaidi ya shilingi bilioni 30 na “badala ya kuzipeleka kwenye miradi ya elimu kama kujengea madarasa na kusaidia masuala mengine ya elimu nchini lakini wameamua kuweka kwenye fixed account wakati kuna miradi ya elimu imesimama kwa kukosa pesa.

Na hapa tena tunapaswa kujiuliza, Waziri husika (na wasaidizi wake) yupo wapi? Au hapa pia, uamuzi huo wa Mamlaka hiyo una baraka za Waziri husika ndio maana haikuchukua hatua hadi Rais alipoingilia kati?

Tukiweka kando hilo la ‘kila jambo kusubiri hadi Rais achukue hatua,’ maamuzi ya baadhi ya mawaziri yanaweza ‘kumgombanisha’ kiongozi huyo mkuu wa nchi na sie wananchi anaotuongoza. 

Wiki mbili  zilizopita, Waziri wa Sheria na Katiba, Dokta Harrison Mwakyembe, ‘alilipuka’ kwa kutangaza kuwa serikali ina mpango wa kuwatimua kazi mahakimu wote wa mahakama ya mwanzo wenye elimu ya cheti na diploma. Waziri huyo ambaye ni mwanasheria kitaaluma, alisema, “Tunahitaji mahakimu wenye uwezo wa sheria ambao wamehitimu shahada ya kwanza, hivyo serikali itawafuta kazi mahakimu wote wenye elimu ya cheti na diploma.”

Tungetegemea kuwa kiongozi msomi kama Dkt Mwakyembe angetambua bayana athari za tamko hilo kwa ari na tija wa mahakimu wa mahakama za mwanzo, wengi wao wakiwa wanafanya kazi katika mazingira magumu na hatarishi. Tamko hilo la Mwakyembe linaweza kupelekea mahakimu kuamua “serikali inataka kumwaga ugali, basi nasi tutamwaga mboga.”

Lakini hata tukiweka kando athari za tamko hilo kwa ari na tija ya mahakimu wa mahakama za mwanzo, kwanini Mwakyembe na wenzake hawakuzingatia busara kwamba elimu pekee sio kigezo cha ufanisi wa mwajiriwa bali pia uzoefu ni muhimu kwenye utaalamu.

Kwahiyo, serikali yenye busara ingeandaa mazingira ya kuwahamasisha mahakimu hao kujiongezea viwango vya elimu wakiwa kazini, hususan kwa kusaka shahada ya sheria kupitia Chuo Kikuu Huria.

Tukio jingine linaloashiria kuwa baadhi ya watendaji wa Dkt Magufuli 'wanamwangusha' ni sakata kati ya serikali ya jiji la Mwanza na wamachinga. Kwa mara nyingine tena, tumeshuhudia ikilazimu Rais kuingilia kati na kumuru kuwa wamachinga waliokuwa wakibughudhiwa huko Mwanza wasisumbuliwe tena.

Hapa pia waweza kujiuliza kuhusu Waziri husika. Alikuwa usingizini kiasi cha kutofahamu kilichokuwa kinaendelea Mwanza hadi imlazimu Rais kuingilia kati? Au Waziri huyo aliridhia kuhusu unyanyaswaji wa wamachinga na ndio maana hakuchukua hatua stahili?

Kuna suala la kiwanda cha Dangote. Kauli za mawaziri husika na watendaji wengine wa serikali zimekuwa sawa na 'kujiumauma.' Sio ngumu kuhisi kuwa 'kuna namna' katika sakata hilo ambalo miongoni mwa atahri zake ni pamoja na kupotea kwa ajira za Watazania wenzetu zaidi ya 1,000.

Kwa jinsi mazingira yalivyo ambapo 'kila kitu lazima kimsubiri Rais,' yayumkinika kuhisi kuwa ufumbuzi pekee wa sakata hilo a Dangote utapatikana kwa Rais kuingilia kati. 

Wakati watendaji 'wanaomwangusha' hawawezi kuwa na kisingizio zaidi ya aidha uzembe wao au hujuma dhidi ya Rais, kwa uapnde mwingine Rais naye anaweza kubeba lawama kwa kuyavumilia majipu yanayomzunguka.


Nihitimishe makala hii kwa kutarajiwa kuwa Rais Magufuli atawakumbusha watendaji wake majukumu yao ili kuondoa taswira ya ‘kila kitu mpaka aje Rais,’ sambamba na kuwakumbusha kutumia busara hasa pale wanapotoa kauli zinazoweza kujenga chuki kati ya ‘waathirika’ wa kauli hizo na serikali


Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  




17 Sept 2016

Nianze makala hii kwa kurejea salamu zangu za rambirambi kwa wafiwa na pole kwa majeruhi wa janga la tetemeko la ardhi lililotokea Jumamosi iliyopita huko Bukoba. 

Kadhalika, ningependa kuchukua fursa hii kuwapongeza wote waliojitokeza kuchangia kwa hali na mali kwa wahanga wa tukio hilo. Kipimo cha utu wetu ni katika nyakati ngumu kama hizi.

Pengine kabla ya kuingia kiundani zaidi katika mada ninayotaka kuongelea, nitoe mfano mmoja unaonihusu. Julai 8 mwaka jana, nilifiwa na baba yangu Mzee Philemon Chahali. Japo miaka saba kabla, yaani mwaka 2008, nilimpoteza mama yangu pia, lakini kuondokewa na mtu wa karibu, hususan mzazi, ni moja ya matukio magumu mno kukabiliana nayo maishani. Sikia tu watu wakilia kwa kufiwa na wazazi au ndugu wengine wa karibu, lakini in reality ni kitu kigumu mno 'kudili' nacho.

Sasa, katika mila zetu za Kiafrika, kipimo kikuu cha urafiki ni jinsi wenzetu wanavyoguswa na matukio makubwa maishani mwetu, pengine zaidi kwa yale ya majonzi kuliko ya furaha. Tunatarajia zaidi wenzetu kuwa karibu nasi kwenye misiba pengine kuliko kwenye harusi, birthday party au mahafali.

Wanasema "nikwepe kwenye sherehe yangu lakini usikose kuwepo kwenye msiba unaonihusu." Ni kwamba wakati wa furaha, hatuhitaji mtu wa kutuliwaza. Ni furaha, twafurahi wenyewe hata pale wenzetu wa karibu wasipokuwepo.Lakini kwenye majonzi twahitaji mno watu wa kutuliwaza. 

Kufupisha stori, nilipopatwa na msiba wa baba yangu mwaka jana nilikuwa nina-follow takriban watu 500 kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter. Japo haimaanishi kuwa mtu ambaye sim-'follow back' sio muhimu kwangu (nina-interact zaidi na watu ambao siwa-follow kuliko hao ninaowa-follow), hao takriban 500 niliokuwa ninawa-follow walikuwa na ukaribu wa aina flani nami.

Naam, katika dunia yetu ya sasa ambapo ni vigumu kuchora mstari unaotenganisha maisha yetu mtandaoni na maisha yetu halisi, kum-follow mtu ni sawa na kuanzisha nae urafiki. Na ni kwa mantiki hiyo, tunapowa-follow watu tunakuwa na matarajio flani kutoka kwao kama ilivyo kwa watu tunaofahamiana nao katika maisha yetu halisi nje ya mtandao.

Nifupishe stori, baada ya wiki kama mbili hivi za maombolezo ya kifo cha baba nilirejea mtandaoni, na kitu cha kwanza kilikuwa kupitia lundo la salamu za rambirambi kwa msiba huo. Na kwa hakika zilikuwa nyingi mno. Hata hivyo, baadhi ya watu niliokuwa ninawa-follow "walinikwepa." Na haikunichukua muda kuwa-unfollow kwa kigezo chepesi tu cha "nini thamani ya urafiki wetu kama mmeshindwa japo kunipa pole ya msiba?" Nika-unfollow takriban watu 400 kwa mkupuo.

Kama kum-unfollow mtu kwa vile "kakuangusha" ni jambo la busara au upuuzi, nadhani inategemea zaidi na jinsi mtu anavyothamini mahusiano, yawe ya mtandaoni au katika maisha yetu halisi.  

Lengo la makala hii sio kuelezea kuhusu tukio hilo linalonihusu bali nimelitumia tu kujenga msingi wa mada ninayoizungumzia leo, ambayo ni kile kinachoelezwa kama "ukimya wa Rais Dokta John Magufuli kuhusiana na tetemeko la ardhi huko Bukoba."

Katika makala yangu kwenye toleo la wiki hii la gazeti la Raia Mwema nimeongelea, pamoja na mambo mengine, uamuzi wa Rais Magufuli kuahirisha safari ya kwenda Zambia kuhudhuria kuapishwa kwa Rais Edgar Lungu. Japo niliwakosoa wasaidizi wa Rais kwa kutoa taarifa ya safari hiyo (kabla ya kutoa taarifa nyingine kuwa imeahirishwa na badala yake Rais angewakilishwa na Makamu wake) huku wakielewa bayana kuwa 'Rais angeonekana kituko' laiti angesafiri huku taifa likiwa kwenye maombolezo, nilipongeza uamuzi huo wa kuahirisha safari hiyo kwa mantiki ya kile  Waingereza wanasema 'the end justifies the means,' kwamba haikujalisha kama awali wasaidizi wa Rais 'walilikoroga,' cha muhimu ni kuwa Rais alionyesha kujali wananchi anaotuongoza, kwa kuahirisha safari hiyo.

Hata hivyo, kama ambavyo baada ya matanga ya msiba wa baba mwaka jana nilikerwa na ukimya wa 'baadhi ya watu niliokuwa ninawa-follow Twitter,' ndivyo ambavyo baadhi ya Watanzania wameanza kuguswa na kile wanachotafsiri kama ukimya wa Rais Magufuli kuhusiana na janga la tetemeko la ardhi huko Bukoba. 

Naomba sana nieleweke vizuri katika maelezo haya ya mfano hayamaanishi kwa namna yoyote ile kulinganisha msiba wa baba yangu na janga kubwa la kitaifa lililotokana na tetemeko la ardhi huko Bukoba. Na wala siwalingishi waliokuwa followers wangu huko Twitter na wananchi wanaohoji kuhusu 'ukimya wa Rais Magufuli.' Nimetumia 'case yangu' kwa minajili ya mfano tu.

Katika kumtendea haki Rais Magufuli, ukweli ni kwamba hajakuwa kimya 'kihivyo.' Mara baada ya kupata taarifa ya janga hilo, Rais alitoa salamu zake za rambirambi kama inavyoonekana pichani chini



Lakini binafsi ninawaelewa vema wanaohoji 'ukimya' wa Rais wetu kuhusu janga hilo. Kwamba Dkt Magufuli sio tu ni Rais wetu bali pia ni Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, na pengine anatarajiwa kusikika kwa 'maneno ya mdomo' (na sio tamko tu la maandishi) akizungumzia suala hilo. Na pengine wanaohoji 'ukimya' wake walitarajia angekwenda eneo la tukio (hasa ikizingatiwa kuwa yeye ni 'mwenyeji' wa maeneo yaliyokumbwa na janga hilo). Hata hivyo, binafsi ninaamini kuwa Rais atazuru huko hivi karibuni tu.

Kadhalika, kwa vile Rais ndiye mkuu halisi wa serikali, taasisi yenye jukumu la usalama wa wananchi, basi huenda wanaohoji 'ukimya wake' wanatarajia yeye kuongoza jitihada za serikali kuwapatia confidence wahanga wa tetemeko hilo.

Na vilevile, licha ya ukweli kwamba kuna kundi flani ambalo limejiapiza kumkosoa Dokta Magufuli kwa kila atakalofanya, wanaohoji 'ukimya' wake sio tu wanaruhusiwa na Katiba kufanya hivyo bali pia wanaweza kuwa wanamsaidia Rais wetu ili kuepusha lawama za mapungufu ya kiuongozi wakati wa majanga.

Nihitimishe makala hii kwa kushauri kuwa pengine itakuwa vema iwapo Rais atafanya ziara huko Bukoba mapema zaidi au hata kuongea na taifa kwa njia ya hotuba, sio kwa minajili ya kuwajibu wanaohoji ukimya wake bali kutekeleza kwa ufanisi wajibu wake kama 'baba' wa taifa letu katika nyakati kama hizi.

Naomba pia kutoa angalizo hususan kwa makada wanaoweza kujaribu kupotosha lengo la makala hii kuwa ni kumlaumu Rais (japo sio kosa kikatiba kufanya hivyo) au kumfundisha kazi (pia sio uhaini wala jinai kumshauri Rais). Dokta Magufuli ametuomba mara kadhaa kuwa tumsaidie, na moja ya njia za kumsaidia ni kumfikishia ujumbe kama huu (nimesikia watu wakihoji kuhusu 'ukimya' wake kuhusu tetemeko la Bukoba nami namjulisha kuhusu hilo). Kama tunampenda kweli Rais wetu basi na tusiwe wagumu  kumshauri au hata kumkosoa pale inapostahili.

UPDATE: Apparently, wanaohoji 'ukimya' wa Rais kuhusu tetemeko la ardhi huko Bukoba wamepata 'hoja mpya,' kwamba walitarajia asubuhi hii angeungana na wakazi wa jiji la Dar es Salaam kwenye matembezi ya hiari ya kuchangia wahanga wa tetemeko hilo, lakini badala yake mgeni rasmi amekuwa Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi. 

Binafsi nadhani sio vema kulaumu bila kujua sababu. Na ukiniuliza kwanini Rais Magufuli hakushiriki matembezi hayo, jibu langu la haraka haraka laweza kuwa 'sababu za kiusalama.' Hilo ni kwa sie 'tunaoelewa,' lakini si kila mtu anaweza kuelewa hivyo, na hatuwezi kuwalaumu wakohoji.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.