Showing posts with label SAMUEL SITTA. Show all posts
Showing posts with label SAMUEL SITTA. Show all posts

2 Oct 2014

Bado ninakumbuka vizuri maongezi yangu ya mwaka 2005 na mtu mmoja jijini Dar, ambaye sio tu ni mwajiriwa katika taasisi moja nyeti lakini pia ana uelewa mkubwa wa masuala yanayojiri 'nyuma ya pazia' (yaani masuala mbalimbali mazito ambayo kamwe huwezi kuyasikia au kuyaona kwenye vyombo vya habari). Nikiwa huko nyumbani kwa likizo katika kipindi ambacho Tanzania yetu ilikuwa katika harakati za uchaguzi mkuu ambao hatimaye ulimwingiza madarakani Rasi Jakaya Kikwete, mwandamizi huyo alinieleza kwa undani kwanini aliamini JK angeshinda uchaguzi huo kwa ushindi wa kishindo.

Kadhalika, mtu huyo alibashiri kuwa Watanzania watajuta kumwingiza Kikwete Ikulu kwa kile alichokieleza kuwa "mtu huyu hayupo serious kiasi cha kumkabidhi dhamana ya kuongoza nchi hii yenye matatizo kibao." Alikwenda mbali zaidi na kunisimulia masuala kadhaa yaliyojiri katika utawala wa Rais Benjamin Mkapa (ambapo mie nilikuwa nje ya nchi kwa zaidi ya nusu ya awamu ya pili ya utawala wa Mkapa). Alieleza kuwa hali ilikuwa mbaya wakati huo, na laiti JK akiingia madarakani itakuwa mbaya zaidi.

Mtu huyo ameendelea kunijulisha mengi yanayojiri 'nyuma ya pazia,' na hivi karibuni aliniambia kuwa ana uhakika Watzanai wengi watapatwa na mshtuko mkubwa baada ya JK kuondoka madarakani hapo mwakani, pindi watakapopata fursa ya kufahamu jinsi nchi yao ilivyoendeshwa katika kipindi hiki cha miaka 10 (2005-2015). Alidai kwamba kinachofahamika kwa umma ni tone tu la maji kwenye bahari kwani kuna mlolongo wa 'madudu' yanayoendelea lakini nguvu iliyojengwa na mtandao wa JK 1995-2005 inafanya jitihada kubwa kuyadhibiti yasijulikane hadharani.

Lakini sidhani kama kuna Mtanzania anayehitaji kuwa na 'mjuzi wa mambo' kama  huyo jamaa yangu, kufahamu kwamba mwelekeo wa nchi yetu ni shaghalabaghala. Kwa wenye uelewa wa 'kusoma kati ya mistari' (reading between the lines) watabaini kuwa mengi ya yanayojiri huko nyumbani katika medani ya uongozi wa taifa letu ni matokeo ya ombwe kubwa la uongozi wa JK.

Wengi twakumbuka kauli ya Mbunge wa Ubungu kwa tiketi ya Chadema, Mheshimiwa John Mnyika, kuwa 'JK ni dhaifu.' Na kwa hakika watendaji wengi wa serikali ikiwa ni pamoja na mawaziri wake wanautumia vyema udhaifu huo wa bosi wao.

Hebu angalia mfano huu rahisi. Wakati lawama nyingi kuhusu sintofahamu ya hatma ya Katiba Mpya inaelekezwa kwa Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katika, Samuel Sitta, mtu ambaye hawezi kukwepa lawama katika kuukoroga mchakato huo ni JK mwenyewe. Kana kwamba alilazimishwa kuteua Tume ya Kukusanya Maoni ya Katiba (Tume ya Warioba), JK pasi kujali athri za matendo yake alianzisha upizani wa waziwazi dhidi ya mapendekezo ya Tume hiyo ya Warioba. Mara kadhaa akiwa kama Mweneykiti wa Taifa wa CCM aliweka bayana upinzani wa chama tawala kwa mapendekezo ya Tume hiyo. Lakini yote tisa, kumi ni siku ya uzinduzi wa Bunge Maalum la Katiba ambapo badala ya kuwaunganisha Watanzania, hotuba yake ilipandikiza mbegu ambazo kwa hakika ndizo tunavyna matuonda yake sasa.

Ilipotokea baadhi ya wajumbe wa Bunge hilo kuunda umoja wao wa UKAWA, na hatimaye kususia vikao vya bunge hilo, kauli za kujikanganya za JK hazikusaidia kuleta mwafaka, kwani mara aonekane anayetaka suluhu mara awatupie lawama UKAWA, mara awaombe viongozi wa dini wasaidie kuokoa mchakato huo, mara atumie ubabe kuzima hoja za UKAWA. Kwa kifupi, ukosefu wake wa msimamo wenye kulinda maslahi ya taifa ulitoa fursa kwa kila 'Dick, Toim na Harry' kujiropokea chochote kilichomuijia akilini.

Fast foward hadi hapa tulipo sasa, katika mazingira ya kawaida tu usingetegemea JK aende Marekani TENA kwa wiki mbili ilhali hatma ya Katiba mpya na Bunge Maalum la Katiba ni tata. Tumeshazungumza vya kutosha kuhusu jinsi JK anavyopenda kuzurura nje ya nchi, hususan ziara za Marekani. Kwa wanaofuatilia safari zake watafahamu kuwa alikuwa Marekani hivi majuzi tu kwa siku kibao, lakini hiyo haikumzuwia kwenda tena huko kwa wiki mbili kwa kisingizio cha kuhudhuria kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa. Je isingewezekana kwenda siku moja kabla ya siku yake ya kutoa hotuba na kisha kurejea nyumbani kushughulikia hatma ya Katiba mpya?

Kituko ni kwamba wakati akiwa ziarani Marekani, alifanya 'safari ndani ya safari' na kuja hapa Uingereza, kabla ya kurejea tena Marekani. Kwa hakika ni vigumu kubashiri maisha ya Rais wetu huyu atakapostaafu mwakani kwani ni wazi kuwa moja ya vitu atakavyovi-miss sana ni hizo safari mfululizo za nje ya nchi. Japo kuwa Rais mstaafu hakutomzuwia kusafiri mfululizo, lakini angalau kwa wakati huo 'hatokuwa na jeuri' ya kuambatana na lundo la watu kwenye misafara yake. Na hatuwezi kujua, huenda Rais ajaye akadhibiti safari za viongozi au viongozi wastaafu nje ya nchi pasipo sababu za msingi.

Ombwe la uongozi wa JK, ukichanganya na mchango wake katika kuukoroga mchakato wa Katiba mpya, ndio moja ya fursa zilizotumiwa kikamilifu na Sitta katika kufanikisha uhuni wa kisiasa/ mzaha wa kidemokrasia unaoendelea huko Dodoma. Kwa lugha nyingine, kiburi, ubishi, nyodo, na kila kisichopendeza kutoka kwa Sitta na uendeshaji wake wa Bunge Maalum la Katiba ni dalili tu za ugonjwa, ilhali chanzo cha ugonjwa huo ni ombwe hilo linalouandama utawala wa JK.

Hivi tuwe wakweli. Laiti JK angemkalisha Sitta kitako kama Waziri wake na ' kumpa darasa la kiutu-uzima' Mwenyekiti huyo wa BMK angeendeleza kufanya madudu tunayoshuhudia? Ni suala jepesi tu la bosi kukaa chini na anayemwongoza, kisha kumwambia bayana kuwa , "No, Mr Sitta, this is wrong." Na hata kama kuna watakaodhani huo ni sawa na udikteta, basi na bora iwe hivyo kwani udikteta kwa maslahi ya umma ni suala linalokubalika.Uzoefu unaonyesha kuwa kumpa mtu uhuru usio na mipaka unaweza kuufanya uhuru huo kuleta madhara yasiyokusudiwa. Rais asipokuwa na uwezo wa kumkaripia Waziri wake, au hata kumshauri tu abadili mwelekeo basi ana ,udhaifu mkubwa.

Twafahamu kuwa JK aliafikiana na Kituo cha Demokrasia kuhusu njia mwafaka za kukamilisha mchakato wa Katiba mpya kwa ufanisi, ikiwa ni pamoja na kuliendesha zoezi hilo taratibu badala ya kuliharakisha kama Sitta anavyofanya sasa. Kwa makusudi kabisa, Sitta akaamua kupuuza ushauri wa JK, na kuendesha BMK atakavyo. Si vigumu kufahamu kuwa kilichompa jeuri Sitta ni ufahamu mzuri kwamba bosi wake, yaani JK, ni dhaifu asiyeweza kumwajibisha kwa kiburi hicho. Na muda wa kumshughulikia Sitta ataupata wapi ilhali yupo bize na safari zake za kuzunguka dunia?

Uongozi katika zama hizi za JK umekuwa kama mzaha flani, mchezo wa kuingiza usiopendeza, yaani a bad comedy, Hebu angalia picha hizi hapa chini kupata uthibitisho wa ninachoandika





Pichani juu ni vimemo vya Sitta akilazimisha matakwa yake.

Lakini tukiangalia kwa upana zaidi kuhusu ombwe lililosababishwa na udhaifu wa JK, tunakutana na kituko hiki hapa chini. Kimsingi, moja ya kumbukumbu za muda mrefu kuhusu utawala wa JK itabaki kuwa kuibuka kwa wanasiasa/viongozi ambao pengine sifa pekee waliyonayo katika uanasiasa/ uongozi wao ni vituko, kashfa, mazingaombwe, na mambo mengine yasiyopendeza. Kama nilivyotanabaisha hapo awali, ombwe hilo liletoa fursa kwa kila Dick, Tom na Harry kufanya atakavyo. Hebu angalia kioja hiki


Nimalizie makala hii kwa kutoa wito kwa Watanzania wenzangu kukazani katika dua/sala ili JK amalize muda wake kwa amani, maana mustakabali wa taifa letu upo hatarini. Ni muhimu kufahamu kuwa amani na utulivu tuliyonayo yahitaji vitendo vya wapuuzi wachache tu kabla haijatokomea. Na uzoefu waonyesha kuwa amani ikipotea ni ngumu sana kuirejesha. Na kubwa tunalohitaji ni kukoma mara moja kwa vitendo vya watawala wetu kuwaona Watanzania kama 'hamnazo' kama tunavyoshuhudia katika BMK huko Dodoma.

Tumtegemee Mungu katika hili, sambamba na jitihada zetu wenyewe kukabiliana na tabia inayozidi kukota mizizi ya kugeuza uongozi kuwa uhuni flani.

MUNGU IBARIKI TANZANIA 


30 May 2013

Magufuli amkana Sitta, asema hana ubia naye urais 2015


Siku chache baada ya Waziri wa Afrika Mashariki Samuel Sitta kumhusisha Dk John Magufuli na kundi la urais la mwaka 2015, Waziri huyo wa Ujenzi, ameibuka na kupinga kauli hiyo, akisisitiza hafikirii kuwania nafasi hiyo.
Waziri Sitta alinukuliwa na gazeti hili juzi akieleza kuwa wakati ukifika, yeye na rafiki zake Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Waziri wa Ujenzi, Dk Magufuli na Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe, watachagua mmoja wao watakayeona anafaa kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa 2015. Alisema hayo juzi kwenye Kongamano la Mawasiliano katika Nyanja za Digitali la wanafunzi wa Idara ya Uhusiano na Masoko, Chuo Kikuu cha St. Augustine (SAUT), Mwanza.
Kabla ya hapo alikuwa amewataja rafiki zake hao wakati wa hafla ya kuchangia Kanisa Katoliki, Josephine Bakita, Parokia ya Igoma, Mwanza, Jumapili iliyopita.
Alisema hatagombea tena ubunge mwaka 2015, baada ya kuwa katika ulingo wa siasa kwa miaka 35 na badala yake ataangalia namna nyingine ya kuwatumikia wananchi huku akigusia mchakato wa kuwania urais ambao alieleza anamwachia Mungu.
“Kwa ubunge nimekwishawaeleza inatosha, sitagombea tena kwani miaka 35 inatosha, … lakini hatima yangu ni nini siwezi kujua lakini nina afya nzuri na mmoja wa wanasiasa wakongwe, wenye afya nzuri, mnaona ninavyopendeza... kwa urais namwachia Mungu tutaona,” alisema Sitta.
Kauli ya Magufuli
Akizungumza na gazeti hili nje ya ukumbi wa Bunge jana, Dk Magufuli alisema haelewi msingi wa kauli ya waziri mwenzake huyo, kwani hajui chochote katika mtandao wa urais alioutaja.
Magufuli alisisitiza kusema hana kundi, hakuwahi kuzungumza wala kuhudhuria vikao vya kundi lolote, na kwamba kundi lake ni CCM na Mwenyekiti wake ni Jakaya Kikwete.
“Sina kundi. Sijawahi kuwa na kundi na sitarajii kuwa na kundi lolote. Ninachojua kundi langu ni CCM na kiongozi wake ni mwenyekiti wake, Rais Kikwete,” alisema Dk Magufuli.
Hata hivyo, Dk Magufuli pia alipuuza taarifa kuwa alichangia harambee hiyo akisema, “Si kweli, Mwanza sijatoa hata senti na hata siku ilipofanyika hafla hiyo, nilikuwa Dar es Salaam katika mkutano na makandarasi.” Licha ya kutajwa kuwa miongoni mwa vinara wa urais 2015, Magufuli alieleza kuwa hakuwahi kuzungumza na Sitta suala hilo linalohusu makundi ya urais mwaka 2015.
CHANZO: Mwananchi
WAKATI HAYO YAKITOKEA, JANA PIA ILIKUWA SIKU CHUNGU  KWA SITTA,KAMA INAVYOONYESHA HABARI HII HAPA CHINI
Wassira amvaa Sitta
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Mahusiano na Uratibu, Stephen Wassira, amemtaka waziri wa ushirikiano wa Afrika Mashariki Samwel Sitta, aweke wazi njia anazotumia kupambana na ufisadi nchini ambazo mawaziri wengine wa serikali ya CCM hawawezi kuzitumia.

Wakati Wassira akitaka ufafanuzi huo, Waziri wa Katiba na Sheria Mathias Chikawe kwa upande wake alikataa kuzungumzia mbinu anazotumia Samwel Sitta kwa kile alichoeleza kuwa hawezi kuongelea masuala ya serikali na mtu asiyemjua.

Wassira na Chikawe walitoa kauli hiyo jana wakati gazeti hili lilipotaka maoni yao juu ya kauli ya Sitta iliyonukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari akisema kuwa katika serikali nzima ni mawaziri wanne waliojipambanua kupambana na ufasadi na kutetea wanyonge.

Wassira alisema kwa sasa hawezi kuchangia jambo lolote juu ya kauli hiyo ya Sitta kwa kuwa hajaliona katika vyombo vya habari au kumsikia waziri huyo akisema hadharani.

Alisema kama kauli hiyo imetolewa na Sitta ni vema angefafanua mbinu anazotumia ili wengine waige.
“Mimi siwezi kuzungumzia hayo; mmeyasema nyie pia ingekuwa ni vema kama angeulizwa Sitta mwenyewe na atueleze mbinu zake tuone na wengine wanafanya nini,” alisema Wassira.

Alipoulizwa kama majina yaliyotajwa ni miongoni mwa makundi yanayodaiwa kujipanga ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), kwa ajili ya urais wa 2015; Wassira alisisitiza jambo hilo aulizwe Sitta.

Kwa upande wake Waziri wa Katiba na Sheria Mathias Chikawe, alipopigiwa simu kwa ajili ya ufafanuzi wa kauli hiyo, alikataa kuzungumzia jambo lolote kwa madai kuwa alishajeruhiwa kwa kutoa habari kwa njia ya simu.

“Sitaki na sizungumzi mambo ya serikali na mtu nisiyemjua tena katika simu…siku moja alinipigia mtu akasema anatoka Daily News nilipompa habari akaandika anavyojua na ikaniletea matatizo, kwanza kwa sasa niko Arusha,” alisema Chikawe na kukata simu.

Juzi wakati Waziri Sitta, akishiriki harambee ya kuchangia ujenzi wa Kanisa la Mtakatifu Joseph katika Parokia ya Igoma jijini Mwanza, aliwataka Watanzania kujihadhari na watu wasio waadilifu katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwaka 2015.

Alisema watuhumiwa wa kashfa ya ufisadi wa kampuni ya kufua umeme ya Richmond na Dowans ni hatari na hawastahili kuungwa mkono katika uongozi.

Alisema kutokana na hali hiyo ya ufisadi yeye pamoja na mawaziri wengine watatu wako pamoja katika fikra za kupambana na vitendo vya kifisadi, uonevu na mikataba tata.

Aliwataja mawaziri hao kuwa ni Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe, pamoja na Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli.


31 Aug 2012


CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimemshukia Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, kikisema kiongozi huyo si mwadilifu, si mwaminifu na mnafiki, akiwa ni mwakilishi na kielelezo cha mfumo uliooza katika serikali ya CCM uliolifikisha taifa hapa lilipo.
Kimesema kuwa tabia za Sitta hasa katika kuua mijadala ya kifisadi ndani ya bunge, kwa ajili ya kulinda maslahi yake binafsi ya kusaka vyeo, inamfanya asiwe tofauti na watuhumiwa wengine wa ufisadi ndani ya chama chake na serikalini, kikishutumu kuwa mlinda ufisadi na mafisadi ama ni naye ni fisadi kama wenzake au ni fisadi mkubwa kuliko mafisadi wenyewe.
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari mjini Iringa jana Ijumaa, Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dkt. Willibroad Slaa alisema kuwa Sitta hana uwezo wowote wa kukisema chama hicho wala viongozi wake, akimtaka amalize kwanza matatizo waliyonayo yeye na wenzake ndani ya CCM, likiwemo la kujivua gamba, ambalo linaonekana kuwashinda.

Katika mkutano huo chama hicho kilisema pia kuwa hatua ya polisi kuzuia mikutano ya Operesheni Sangara-M4C kwa siku tano, kupisha shughuli ya sensa, kumekisaidia chama hicho kugundua mbinu na mikakati mizuri ya kuwafikia wananchi kwa mikutano ya ndani, ikiwa ni maandalizi ya mikutano ya hadhara, hivyo kupata mafanikio zaidi mkoani Iringa kuliko ilivyokuwa mkoani Morogoro.

Sitta ni kielelezo

Katibu Mkuu huyo wa CHADEMA ambaye aliwaambia waandishi wa habari kuwa amelazimika kumzungumzia mtu lakini kwa nia ya kuonesha alivyo kielelezo cha ubovu wa mfumo na uongozi wa serikali na CCM, alidai kuwa kwa sababu ya tabia ya unafiki aliyonayo Sitta, kiongozi huyo ni sawa na viongozi wengi wa serikali ya CCM akiwafafanisha na mbwa mwitu waliovaa ngozi ya kondoo.

“Nchi hii imefika hapa ilipo kwa sababu ya viongozi aina ya Sitta ambao hawasiti kusema uongo hadharani, wanafiki, hawana uadilifu, waongo, walio tayari kusaliti maslahi ya umma kulinda maslahi ya tumbo, Sitta yeye ana uzoefu gani, huu wa kulinda mafisadi bungeni kwa kupindisha hoja za ufisadi ili apate ubunge na uspika.

“Hivi Sitta atuambie anaposema CHADEMA haina watu wenye uwezo lini tuliwahi kusema tukiingia serikalini tutakuja na watu wetu wote au ndiyo yale mawazo ya kijinga kwamba CHADEMA wakishika nchi watapata wapi ikulu…atuambie kuna chuo kikuu chochote kinafundisha uwaziri au kuna chuo kikuu kinafundisha ukatibu mkuu wa wizara, asitupangie sisi namna ya kupata viongozi wetu.

“Hivi hajui kuwa Mwalimu alipopata nchi aliandaa watendaji. Hoja za kipuuzi, mtu akitoa hoja za kipuuzi, naye atakuwa mpuuzi tu wa kupuuzwa, tumefika hapa, nchi imegubikwa na uozo wa ufisadi kwa sababu ya mawaziri wa aina ya Sitta ambaye haogopi kuropoka hadharani, tena akiwatukana wapiga kura, ambao pia wengi wao ni vijana.

Hoja ya kuchezesha disko

“Anaposema Mbowe ni mchezesha disko anataka kupeleka ujumbe gani, anataka kusema nini…kwamba ni kosa, kwa hiyo anamaanisha wacheza disko ni criminals (watenda jinai), kwa hiyo wacheza disko ambao pia ni wapiga kura na wengi ni vijana ni criminals, je hajui kuwa kuna mawaziri wenzake wanaokesha pale Billicanas Club,” alisema Dkt. Slaa.

Aliongeza kusema kuwa hoja hiyo ya kumshambulia Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe kwa sababu ya kumiliki ukumbi wa mziki, kuwa nayo ni hoja mbele ya watu makini, Dkt. Slaa alisema waziri huyo amedhihirisha alivyo mbumbumbu wa sheria na hajui lolote, tofauti na ambavyo siku zote ametaka kuonekana mbele ya jamii.

“Ni dhahiri hana uzoefu wowote na hajui, ndiyo maana ameishia kwenda kuwatukana wapiga kura yeye akifikiri anaimaliza CHADEMA, maana wacheza disko ndiyo wapiga kura hao hao, lakini yeye kama msomi kweli, tena anasema ni mwanasheria, alipaswa aelewe kuwa duniani kuna nyumba za disko za staha, zimesajiliwa na zinafanya kazi kwa mujibu wa sheria na zimepewa leseni na serikali.

“Huyu Sitta kila siku anajiita yeye mwanasheria kumbe mbumbumbu kupindukia tu hana tofauti na wana CCM wenzake ambao jamii inawashangaa kwa matendo na kauli zao, ku-run club ni sawa na ku-run biashara nyingine yoyote, almuradi iendeshwe kisheria na kihalali, sasa kama anaona ni kosa aiambie serikali yake ifute leseni ya biashara hizo.

“Tulitegemea mtu ambaye anataka kuonekana ni mstaarabu, anahoji uzoefu wa wenzake nay eye anasema ana uzoefu angekuja na mawazo ya kupeleka nchi mbele kumbe yuko sawasawa tu na wenzake ndani ya CCM,” alisema Dkt. Slaa.

Ameingia kichwakichwa, kwenye tope

“Leo nalazimika kumzungumzia mtu, Watanzania wanajua mara chache sana CHADEMA huwa tunalazimika kuzungumzia watu badala ya masuala…lakini nitazungumza kwa namna ambayo huyo mtu atakuwa anawakilisha mfumo huu wa serikali ya CCM na chama chao jinsi ulivyooza na kutufikisha Watanzania hapa tulipo.

“Samuel Sitta ameingia kichwa kichwa kwenye matope ambayo hawezi kutoka wala kujinasua, muda mrefu tumemhifadhi lakini leo tutampiga ngumi za uso lakini kwa namna ambayo atakuwa anawakilisha mfumo huu uliooza…

“Ghafla tu ameamua kuibuka na kuzingumzia CHADEMA, badala ya kujenga chama chake, bila kujua amedhihirisha kuwa CHADEMA sasa ni tishio kwao, maana huwezi kuzungumzia kitu ambacho hakikuathiri, amedhihirisha namna ambavyo yeye wenzake sasa wanatapatapa kweli kwa sababu ya CHADEMA.”

Makombora zaidi; mlinda ufisadi na mafisadi

Dkt. Slaa alisema kuwa wakati chama hicho kilipoanza kuasisi hoja ya ufisadi nchini kikiwa mstari wa mbele kupiga vita kila aina ya ufisadi, Sitta wakati huo akiwa Spika wa Bunge, ndiye alikuwa mtu wa kwanza kuweka vikwanzo na vizingiti akilinda maslahi yake nay ale ya chama chake, badala ya maslahi ya wananchi.


“Yeye ndiye aliyepindisha hoja ya Zitto katika kashfa ya Buzwagi ambapo waziri alikuwa amesaini mkataba uliokuwa kinyume kabisa na maslahi ya nchi, tena akasaini nje ya nchi hotelini. Zitto aliposimama bungeni, Sitta badala ya kuangalia hoja hiyo kwa maslahi ya nchi, yeye na wenzake akaipindua kuwa Zitto amesema uongo bungeni.

“Huyu bwana hastahili hata kuwa waziri, anajidai yeye mpiganaji na mpambanaji, wapi? Katika hoja ile nani alikuwa mpiganaji Zitto au Sitta, akapindisha makusudi hoja ya ufisadi mkubwa wa Buzwagi kulinda maslahi anayoyajua mwenyewe. Wakamfukuza Zitto bungeni kwa miezi minne, baadae kelele zilivyozidi huku nje, wakaamua kumrejesha bungeni kimya kimya baada ya mwezi mmoja tu hivi.

“Lakini pia ni Sitta huyu huyu alizima hoja ya ufisadi wa BoT, mambo yote yale ya EPA, Kagoda, Deep Green sijui nini kila kitu kilichokuwa kikihusu BoT. Mtakumbuka aliwatangazia Watanzania kuwa nyaraka za Dokta Slaa ni fake za kuokoteza kwenye internet na nitampeleka polisi, mpaka leo hakunipeleka. Lakini Sitta alikuwa anajua tangu mwanzo, kadri nilivyokuwa nikikusanya documents alikuwa anajua na nampatia copy, mpaka ikafikia ile document kubwa ya mwisho.

“Lakini kwa unafiki wake ameahirisha bunge Ijumaa, Jumamosi akachukua ile document na kwenda nazo TBC akisema ni fake na atanipeleka polisi, lakini leo yako wapi…sasa mtu wa namna hii hafai hata kuwa naibu waziri, mtu yeyote anayelinda mafisadi na ufisadi ni fisadi kuliko mafisadi wenyewe, nawaambia haya kwa sababu tumefika hapa kwa sababu ya kuwa na viongozi, wakiwemo mawaziri wanafiki na waongo kama hawa.

“Lakini ili mjue Sitta ni mtu wa aina gani na kwamba hastahili kuaminika na Watanzania, haikuishia hapo, ufisadi wa Richmond mnajua alivyomaliza mjadala ule kihuni bungeni. Hadi leo hoja ile haina majibu, wakati tunahoji bungeni akafunga hoja ile kidikteta, sasa tunauliza huo ndiyo uzoefu alionao yeye au walionao wenzake, uzoefu wa kulinda mafisadi na ufisadi wa CCM na serikali yao, lakini sisi tunajua kwa nini alipindisha hoja ya Richmond, wakati huo alikuwa anabembeleza ili ateuliwe kuwania ubunge na baadae uspika, mnaona huyu ni mtu wa kuaminika kweli?”

“Hivi kwa matendo ya aina hii Sitta anaweza kutoka nje na kusema yeye ni jasiri na mzalendo, katika majasiri na wazalendo wa kweli Sitta hana sifa hizo, ndiyo maana wameshindwa hata kuyavua magamba kama walivyosema, sasa aende kwanza kwenye chama chake na serikalini, asaidie kuyaondoa magamba kabla hajaanza kutafuta aibu ya kuanikwa zaidi,” alisema Dkt. Slaa.

Siri zaidi; Sitta haaminiki

Dkt. Slaa aliongeza kusema kwa kutoboa siri zaidi namna ambavyo, yeye na Mwenyekiti wa CHADEMA Mbowe, walikuwa wakiendesha mazungumzo na Sitta wakati mwingine kwenye Ofisi ya Spika juu ya Sitta kuhamia CHADEMA na kuwania urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, akisema kuwa ulikuwa ni wakati ambapo waziri huyo pamoja na wenzake walipokuwa wameunda Chama Cha Jamii (CCJ) wakiwa bado wako CCM.

Alisema kuwa hata wakati huo bado Sitta alikuwa akionekana kutojiamini na maamuzi yake, ambapo wakati wa majadiliano ya kugombea urais, Sitta alisema kuwa kuna kundi la wabunge takriban 55 watiifu kwake ambao walikuwa tayari kuhama naye kumfuata CHADEMA. 

“Leo natoa siri ambayo sijawahi kuitoa, Sitta ni mhanini. Tumekutana naye mara 100 na zaidi, tumeandikiana vimemo bungeni vya kukutana, wakati mwingine tumekutana hata Speaker’s lounge, tumekutana na Sitta na Mwenyekiti Mbowe, ambaye leo anamwita ni mchezesha disko mara nyingi tu. Lakini hata wakati huo pia hakuonekana kuwa jasiri, maana alikuwa ana wasiwasi nani wanamfuatilia au nani wanamuona, si mtu jasiri hivyo. 

“Zikiwa zimebaki kama siku tano kabla ya kumaliza bunge la mwezi wa saba, kila nikimwandikia kimemo, hataki hata kunitazama, Sitta akayeyuka bila hata kutuaga, baadae CHADEMA tukaamua kutumia utaratibu mwingine na tukaweza kusonga mbele mpaka kufika pale tulipofika. Lakini baada ya uchaguzi akaja mwenyewe kunifuata akinishukuru sana na kunipongeza kuwa nilikuja na hoja tofauti kwenye uchaguzi akisema hata yeye asingeweza kufika tulipofika.

“Lakini hapo sasa tulishamshtukia na kugundua kuwa anataka kugombea uspika kupitia CHADEMA, nataka kuonesha namna huyu mtu alivyo mnafiki, mpotoshaji, nampatia challenge kama kweli yeye ni muumini mzuri akanushe haya, maana ametulazimisha kusema, kwa hoja zake za kupotosha watu na akumbuke, maana huwa anakwenda makanisani na anachanga mapesa, akumbuke maandiko yanasema, yeyote atakayepotosha wadogo hawa, anastahili kutoswa baharini, Makamu Mwenyekiti hapa ametumia Quran kufafanua vizuri,” alisema Dkt. Slaa.

“Maana kwa hakika anataka kupotosha watu ili waone kuwa kuchezesha disko ni suala lisilokuwa sahihi, huo ni upotoshaji, kama anataka kuonesha si sahihi mbona serikali yake hiyo hiyo inaendelea kukusanya kodi. Sasa ilipofikia kwenye suala la kugombea uspika, siku ile jina lake limekatwa kwa sababu walitaka mgombea mwanamke, alinipigia simu usiku wa saa tisa, bahati mbaya nilikuwa nimeweka simu silence, hakunipata.

“Saa 12 nikapokea simu ya mke wake, Margreth Sitta, anasema baba anakutafuta tangu usiku, anataka kuzungumza nawe, nikasema sawa, akaniambia Dokta Slaa wamenifanyia kitu kibaya sana, mimi nimeamua sasa nitagombea uspika kwa tiketi ya CHADEMA, najua umeshateua tayari mtu wa kugombea tayari, lakini naomba nikuhakikishie nafanya press conference saa 4 asubuhi leo, natangaza rasmi kugombea uspika kupitia CHADEMA. Nikamjibu CHADEMA maamuzi hayafanywi na mtu mmoja, nikamwambia asubiri niwasiliane na Mwenyekiti wangu wa chama.

“Baadae tukakubaliana tukutane nyumbani kwake, lakini akawa anasema tusubiri kwanza anamalizia kupanga mikakati na wabunge 55 wa CCM, lakini akisisitiza kuwa uamuzi wake uko pale pale, nikamuuliza vipi kuhusu press conference mbona muda unakaribia, akasema hakuna shida yeye atatuma tu watu wake wataitisha haraka, akasema lakini wanataka kumpatia unaibu waziri, hivyo bado anasumbuana nao, kengele ikalia kichwani sasa huyu mtu akipewa uwaziri itakuwaje.

“Baadae ananiambia, Dokta Slaa nimepigiwa simu na bwana mkubwa naenda kuonana naye, tangu wakati huo Sitta akapotea mpaka saa 8 ndiyo anapatikana, akaanza kuniambia ni lazima aende kwanza Urambo kuwaaga wazee, maana hawezi kuhama bila baraka zao, nikamuuliza vipi kuhusu press conference akasema tutaifanya Jumatatu ijayo Dar es Salaam, akaniambia; tena saa 9 uje uone statement ambayo nimeshaiandika ili na wewe uongeze inputs, Sitta huyu akaniambia kuwa Anne Makinda hatakaa zaidi ya miezi sita kwenye kiti cha uspika.”

Dkt. Slaa alisisitiza akisema kuwa nchi imefika hapa ilipo ikiwa imegubikwa na uozo wa ufisadi kila kona, ukiongeza idadi ya maadui wa taifa, kutoka watatu hadi wanne (umaskini, ujinga, maradhi na ufisadi/CCM) kuanzia ngazi ya chini hadi juu, kwa sababu ya ukosefu wa uadilifu, uaminifu kama Waziri Sitta.

Atalipuliwa zaidi


Dkt. Slaa alisema kuwa ameamua kuzungumza hayo machache kwa sasa, lakini ataongeza ‘kumlipua’ zaidi Sitta endapo atajitokeza kujibu haya ya sasa.

“Yeye ana uzoefu gani Sitta, hana uadilifu, si mwaminifu, nchi hii imeoza kwa sababu ya viongozi ya aina ya Sitta, nataka ajibu kwanza hayo kisha nitamlipua zaidi. Ana uadilifu gani katika nchi hii, ametumia mabilioni ya hela ya walipa kodi wa Tanzania kujijengea Ofisi ya Spika Urambo, tunauliza kuna spika wa Urambo au alijua yeye atakuwa spika wa milele au basi Makinda awe anakwenda Urambo wakati wa mapumziko ya bunge.
“Tulichoamua bungeni ni kwamba kila mbunge ajengewe ofisi yenye thamani isiyozidi milioni 40, lakini yeye akaenda kujijengea ofisi ya milioni 350 tena kwa kasma tofauti na inavyotakiwa lakini kibaya zaidi tendering process ya vifaa vya ofisi haikufutwa na vililetwa na kampuni ambayo majuzi imehusishwa na Blandina Nyoni, hakuna mahali tendering imefanyika, amefanyia ufisadi mali ya taifa,” alisema Dkt. Slaa.


More still to come about the press conference...


CHANZO: Afisa Habari wa Chadema TUMAINI MAKENE

9 Aug 2012




Picha zote mbili zinamwonyesha Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki Samwel Sitta alipotembelea maonyesho ya kilimo ya Nane Nane mkoani Morogoro.Katika picha zote,Waziri Sitta ameambatana na mlinzi (BODIGADI) kutoka Idara ya Usalama wa Taifa.Ninakumbuka,uamuzi wa kumpatia Sitta ulinzi ulifanywa na Serikali wakati waziri huyo alipokuwa Spika wa bunge lililopita,na alidai anatishiwa maisha.Je matishio hayo bado yanaendelea?Ikumbukwe,gharama za kutoa ulinzi kwa kiongozi ni kubwa sana,na kimsingi,kiprotokali,Sitta hastahili kuwa na bodyguard....unless tumembiwe kuwa tishio dhidi ya maisha yake bado lipo hai 



Picha kwa hisani ya AudifaceJackson Blog


22 Jul 2011

Samuel Sitta mwenyewe anayepigwa mkwara na Guninita yupo hoi kwa usingizi.Labda hapo anaota yeye bado Spika

Guninita ‘amvaa’ Sitta
Posted By admin On July 22, 2011 @ 7:59 am In Habari kuu,Mtanzania |

• Adai ni mzigo, anawadanganya na kuwapotosha wananchi
• Asisitiza ni sehemu ya tatizo la mgawo wa umeme
• Asema si mgeni serikalini, ni mchochezi, mnafiki na mfitini
• Aonya anaigawa, anaitumbukiza CCM kwenye shimo
• Asema mambo yakiendelea hicho mwaka 2015 CCM itaambulia patupu

Na Habakuki Urio

MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dar es Salaam, John Guninita amemlaumu Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samwel Sitta akidai ni mnafiki na mchochezi anayetumika kuigawa CCM na kukitumbukiza chama hicho kwenye shimo.

“Sitta ni sehemu ya serikali na si mgeni serikalini. Alikuwapo tangu kipindi cha Mwalimu Nyerere, na pia alikuwa Spika wa Bunge. Kwa nafasi hizi yeye ni sehemu ya tatizo na siyo kuwadanganya wananchi na kuwapotosha kwa kuirushia serikali lawama.

‘Anaudanganya umma. Anataka kujenga umaarufu ambao siyo wa kwake. Kama ni kuharibu waliharibu wote na siyo kusema tatizo ni la serikali.
‘Sitta amekuwa mchawi wa CCM… chama kinajimaliza chenyewe tena kwa kutumia viongozi wa nafasi za juu.,” alisema Guninita.

Guninita alikuwa akizungumza katika mkutano wa hadhara Mbezi na Mbezi kwa Msigani katika jana, katika ziara ya kutekeleza agizo la Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete la kuleta mageuzi ndani ya chama hicho na ‘kujivua gamba’.

Alisema hali ya siasa ndani ya chama hicho si shwari kutokana na mgawanyiko mkubwa wa baadhi ya viongozi ambao wanazungumza wanavyojisikia bila kujali maslahi na ukweli ndani ya Chama hicho.

“Kilichotufikisha hapa tulipo leo ni unafiki na fitina za viongozi kama Sitta ambao hawaeleweki wanafanya nini ndani ya chama chetu. Ndiyo maana viongozi wanajiuzulu ovyo, kitu ambacho siyo sahihi, chama kinapoteza makada muhimu na kuwaacha watu mizigo na wafitini.

“Namshangaa Waziri Sitta, ana uwezo wa kwenda kwa Rais muda anaojisikia na pia alikuwa na nafasi ya kuyasema mambo yale katika vikao vya chana “party caucus”, na pia kwenye vikao vya Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) lakini anaropoka mambo kama hayo mbele ya umma wa watanzania na kuwapa umaarufu wapinzani.

“Amekosa busara kwa kuwa amekiuka maagizo ya Rais. Tunajua hakutumwa na Rais, bali alikurupuka tu, na bila kujijua anaiponda Ilani ya Uchaguzi ya CCM ambayo ndiyo muongozo wa kutekeleza majukumu yetu.
‘Mawaziri na wabunge wanasema tofauti na Rais anavyosema kuhusu matatizo ya umeme kwa sasa,” alisema Guninita

Alisema kauli mbovu za baadhi ya viongozi ambazo hazina ukweli zinabomoa chama, na kama CCM haitakauwa makini na kuwaonya wapotoshaji hao katika uchaguzi mkuu wa 2015 chama hicho kitaambulia patupu.

“Upinzani wanajipanga vizuri katika kuhakikisha mwaka 2015 wanachukua nchi, na kwa hali hii tulio nayo … kwa kauli za akina Sitta watafanikiwa kwa kuwa chama kitakuwa kimeyumba na kukosa imani kwa wapigakura wake.

“Haya siyo maneno ya Waziri, huyu jamaa ana mambo yake anayotekeleza… haiwezekani Sitta leo kuyasema haya, labda ana hasira za kukosa Uspika wakati yalikuwa makubaliano ya CCM kumuondoa kwa mafanikio ya chama na kutimiza sera ya 50 kwa 50.

‘Nilimsikia akisema kuwa atatembea mikoa yote kulisema hilo, lakini nawahakikishia kuwa hatafika Dar es Salaam labda aje na barua ya Mwenyekiti au Katibu Mkuu wa CCM kuwa wamemruhusu kupotosha jamii. Nasema kuwa hatutakubaliana na uongo wake,” alisisitiza Guninita.

Hivi karibuni, katika mkutano wa hadharani mjini Mbeya, Sitta pamoja na mambo mengine, alikaririwa akishauri serikali iwaombe radhi wananchi kutokana na tatizo la mgawo wa umeme unaoendelea nchini hivi sasa.

Guninita alisema mkutano wa jana ni matunda ya makubaliano ya kujivua gamba kama alivyoagiza Mwenyekiti Kikwete na kuwataka viongozi wote wa CCM kutembelea matawi na mashina katika maeneo yao kuyajua matatizo ya wapiga kura wao na kuimarisha mizizi ya chama ambayo ipo katika mashina na matawi.

17 Jun 2010

Desemba 9 mwakani,Tanzania yetu itatimiza miaka 50 tangu ipate uhuru.Pengine tarakimu 50 inapunguza uzito,kwahiyo ni vema kubainisha kuwa umri huo ni sawa na NUSU KARNE (herufi kubwa kuonyesha msisitizo).Wakati umri huo wa mtu mzima ungepaswa kuwa habari njema,hali ni tofauti kwetu.Tulowakabidhi dhamana ya kutuongoza wanakurupuka na mambo ya ajabu ajabu kana kwamba wako ndotoni au wako kwenye mchezo wa kuigiza usio na ujumbe wowote.

Ngoja niende moja kwa moja kwenye pointi.Hivi Mtanzania mwenzangu inakuingia akilini kweli kusikia kauli kwamba jengo la Bunge letu tukufu "litafanyiwa ukarabati wa kufa mtu" unaotarajiwa kugharimu shilingi bilioni 30.9 "ili kuwawezesha waheshimiwa sana waendane na teknolojia ya kisasa wanapokuwa Bungeni"!!!?Kwa mujibu wa Spika Samuel Sitta mchakato wa ukarabati huo umeshakamilika na unatarajiwa kuanza mara moja,ambapo utapokamilika kila kiti cha mbunge kitakuwa na runinga pamoja na mawasilino ya kisasa ya kompyuta.

Ofkozi,ni muhimu kwenda na wakati katika suala zima la teknolojia lakini pamoja na umuhimu huo shilingi bilioni 30 na ushee ni nyingi mno na tunazihitaji kwenye maeneo mengine yaliyo hio bin taaban kama vile miundombinu,huduma za afya,maji,nk.Hivi kweli runinga kwenye kiti cha mbunge ni muhimu kuliko madawati au nyumba za walimu?Je hizo bilioni 30 zingeweza kujenga zahanati ngapi au visima vingapi vya kuwapatia walalahoi huduma ya maji ya uhakika?

Lakini kabla sijatuliza hasira zangu kutokana na kauli hiyo ya Spika Sitta,JK nae amekuja na mpya akidai kwamba katika miaka mitano ijayo kila mwalimu atakuwa na laptop.Namheshimu sana Rais wangu lakini baadhi ya kauli zake zinanitatiza sana.Hivi kipaumbele katika elimu yetu ya kusuasua ni laptop kwa walimu au makazi bora kwa walimu hao sambamba na kuboreshewa maslahi yao na mazingira yao ya kazi?Mwalimu mwenye laptop anafundishaje wanafunzi waliokaa chini ya mti?Na wakati JK anatoa mpya hiyo hajatuambia umeme wa kuziwezesha laptop hizo utakuwa wa nguvu za jua au zitatumia mafuta ya taa kwani sote tunafahamu uhuni wa TANESCO.


Sijui ni uzembe wa watawala wetu kuelewa matatizo yetu na vipaumbele vyetu kama taifa au ni makusudi tu lakini kwa mwenendo huu itatuwia vigumu kutembea vifua mbele hapo mwakani tutaposherehekea nusu karne tangu tupate uhuru. 

Enewei,hebu soma mazingaombwe hayo HAPA na HAPA.

23 Feb 2010

Angalia "mchemsho" huu  wa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano Samuel SITTA.Anarusha tuhuma nzito dhidi ya wanaharakati wanaokusudia kuandamana kupinga "mahitimisho ya mjadala wa Richmond bungeni" ilhali katika habari husika ameshindwa kuthibitisha tuhuma hizo.Kibaya zaidi,yeye mwenyewe aliporushiwa tuhuma kama hizo aligeuka mbongo.Hebu soma kwanza habari husika (hasa maneno ya rangi nyekundu)

Salim Said
SPIKA wa Bunge Samuel Sitta amewashukia wana-mtandao wa asasi za kiraia zinazotetea usawa wa jinsia, haki za binadamu na maendeleo ya ukombozi wa Wanawake, akisema wanatia mashaka na kwamba wanaendeshwa na utashi binafsi wa wajanja wachache, huku wenyewe wakisema maandamano yapo palepale.
Wanaharakati hao, walitangaza maandamano makubwa ya amani yatakayoendeshwa nchi nzima kupinga kuvungwavungwa kwa hoja za mikataba ya Richmond, TICTS, TRL, taarifa ya uchafuzi wa mazingira kwa kemikali za sumu katika mgodi wa North Mara na ukiukwaji wa haki za binadamu, Loliondo.
Akizungumza na Mwananchi jana Spika Samuel Sitta alipingana vikali na madai ya wanaharakati hao, kuhusu Bunge na kueleza kwamba mtu yeyote akitaka kupima uwezo na uzuri wa bunge katika maamuzi na kusimamia serikali aangalie rekodi ya kazi za bunge kuanzi mwaka 2005 hadi sasa.
'Mimi sikubaliani na wanaharakati hawa hata kidogo. Maandamano ni haki yao na waandamane, lakini hawawezi kupima kazi za bunge kwa kuangalia kipindi cha mitafaruku ," alisema Spika Sitta.
Spika Sitta alisema kuimarisha Bunge si kazi ya lele mama, bali ni mapambano yanayohitaji ujasiri wa hali ya juu.
"Mimi naamini kwamba bunge letu limeimarika katika kuisimamia serikali ukilinganisha na lilikotoka, wanaharakati wanapaswa kujua pia kuimarisha bunge ni mapambano," alisema Spika.
Kuhusu suala la bunge la mfumo shirikishi wa demokrasia, Spika Sitta alisema hilo ni kinyume na katiba, lakini aliwataka wanaharakati hao wajaribu kujenga hoja.
"Mimi naona mfumo wa demokrasia ya uwakilishi bungeni ni mzuri tu, kwa sababu unapatikana kupitia uchaguzi ambayo ni ridhaa ya wananchi, lakini mfumo shirikishi utapatikana wapi.
"Huwezi kushirikisha mashirika au taasisi hizo katika bunge, kwanza zinamwakilisha nani, kwanza haziwawakilishi wanawake ni utashi tu wa baadhi ya wajanja," alihoji Spika Sitta.
Alisema mitandao hiyo inatia mashaka kwa wahisani kwani baadhi ya taasisi zinakula fedha bila ya kupeleka mrejesho kwa wahusika.
"Mambo yote ya bunge yanajadiliwa hadharani na kila mtanzania anayetaka anasikia, lakini je mambo ya hawa wanaharakati na mitandao yao yanajadiliwa na nani," alihoji Spika Sitta.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Concern for Development Initiatives in Africa (ForDIA), Bubelwa Kaiza alisema ujumbe wao mkubwa katika maandamano hayo, ni kwamba hoja hizo zimevungwavungwa na bunge halitambui nguvu na mamlaka liliyopewa kikatiba, badala yake linafanya kazi kwa maslahi ya vyama vya siaasa na sio wananchi.
"Wapo wanaotaka tusiandamane, lakini huo ni woga wao tu, maandamano yapo palepale nchi nzima, tuna sababu za msingi za kuandamana kwani bunge halikuwajibika katika kushughulikia hoja mbalimbali katika kikao cha 18, badala yake limezivungavunga hoja hizo kwa maslahi ya vyama vyao vya siasa.
"Sisi pamoja na wananchi hatukuridhika kuhusu hoja zile zilivyohitimishwa, hakuna pia aliyewajibishwa, kwa hiyo tunaitaka serikali iachane na mfumo wa demokrasia wakilishi na ianzishe mfumo wa demokrasia shirikishi wa bunge ili wabunge waweze kuwajibika moja kwa moja kwa wananchi," alisema Kaiza.
CHANZO: Mwananchi

Tatizo kubwa linalomkabili Spika wetu Samuel Sitta ni uropokaji,yaani kuongea bila ktafakari athari zinazoweza kusababishwa na matamshi yake.Kama kiongozi mkuu wa chombo chenye dhima ya kutunga sheria za nchi,Sitta alipaswa kutambua kuwa baadhi ya kauli na tuhuma alizotoa dhidi ya wanaharakati ni za kihuni.Na bahati yake ni kwamba wanaharakati hao hawana muda wa kumburuza mahakamani kuthibitisha kashfa alizotoa dhidi yao.

Hivi Spika Sitta anaweza kuuthibitishia umma kuwa mitandao inatia mashaka kwa vile baadhi ya taasisi zinakula pesa bila kurejesha fedha kwa wahusika?Ameyajuaje hayo?Hivi hao wanaotoa fedha zao (wanaofadhili mashirika hayo) wamekuwa wajinga kiasi gani cha kutohitaji taarifa za matumizi ya fedha wanazotoa?

Sitta ni mropokaji kwa vile yeye alipotuhumiwa kukumbatia ufisadi katika ofisi ya Bunge aliwaka kama nini akidai ni njama za mafisadi dhidi yake.Iweje leo akurupuke kuwatuhumu wanamtandao kwa vile tu wameonyesha nia ya kuandamana kupingana na ubabaishaji wa Bunge linaloongozwa na Sitta?

Sitta asijione Mungu-mtu.Kila Mtanzania ana haki kama yeye Sitta kutoa mawazo yake hadharani alimradi havunji sheria za nchi.Kama Sitta anaona Bunge analoongoza limefanya vizuri katika utendaji kazi wake,si lazima kwa kila Mtanzania kuona hivyo au kukubaliana na mtizamo wa aina hiyo.Na ni vigezo vipi anavyoweza kutuonyesha Mheshimiwa Sitta kuwa Bunge lake limewajibika ipasavyo?Huko kutuzuga kwa zaidi ya miaka miwili kuwa yeye na wenzake ni wapambanaji dhidi ya mafisadi kisha kusalimu amri kama kondoo walionyeshewa mvua?

Na hata kama Bunge analoongoza Sitta linawajibika akama anavyotaka tuamini,si ndio kazi yake?Na si kazi ya kawaida kwani kwa mshahara wa mamilioni na kiinua mgongo cha mamilioni mengine kwanini waheshimiwa hawa wasiwajibikie kwa kiwango cha juu?

Sitta anakasirika kwa vile alitangaza kuwa "mjadala umefungwa",na kwa jinsi anavyojihisi ni Mungu-mtu anaona kitendo cha wanaharakati "kuendeleza mjadala" ni kama "wanavunja amri ya Mungu".Katika habari husika hapo juu,Sitta anathibitisha ubinafsi wake kwa kurudiarudia kutumia neno "MIMI".Anaweza kuwa sahihi katika mtazamo wake binafsi,lakini jamii hailazimiki kuafikiana nae wala kushurutishwa kutenda atakayo yeye.





16 Feb 2010


Pamoja na kuwa moja ya nchi maskini kabisa duniani, Tanzania yetu bado inaendelea kusifika kwa mambo kadhaa. Ukiachia mbali vivutio vya asili kama Mlima Kilimanjaro, utitiri wa wanyama huko Selous, Mikumi na kwingineko, na “utajiri” wa madini kama Tanzanite,dhahabu, almasi na madini mengineyo,nchi yetu pia inasifika kwa watu wenye uwezo wa kuongea.

Ndio maana jirani zetu wanapenda kututania kuwa “nyie Watanzania iko maneno mingi” wakimaanisha tunaongea sana. Na pengine mahala mwafaka pa kuthibitisha uwezo wetu wa kuongea ni katika vikao vya bunge letu tukufu. Laiti yote yanayoongewa katika vikao hivyo yangekuwa yanatafsiriwa kwa vitendo, basi kwa hakika tungekuwa mbali sana.

Lakini licha ya sifa hiyo ya kuongea sana, Watanzania tuna sifa nyingine ya usikivu na kuamini kirahisi kila tusikiacho hata kama ni “wizi mtupu”. Ndio maana basi watu wenye akili na busara zao walidanganyika kwamba miongoni mwa wabunge wa CCM kuna kundi la WAPIGANAJI DHIDI YA UFISADI.Kundi hilo lililojipatia umaarufu usiostahili linadaiwa kuwa chini ya Spika wa Bunge, Samuel Sitta.

Na kwa katika kile kinachoweza kutafsiriwa kwamba ni jitihada za kujiongezea sifa za “upambanaji” , Spika Sitta na wabunge wawili kutoka vyama vya upinzani,Dr Wilbroad Slaa (Chadema) na John Cheyo (UDP) walichapisha kitabu walichokipa jina “BUNGE LENYE MENO”. Si lengo la makala haya kurejea yaliyomo katika kitabu hicho, lakini kwa kifupi ni mwendelezo wa sifa tulizonazo Watanzania: maneno meeeengi lakini vitendo SIFURI.

Sijui Sitta wa “wapiganaji” wenzie walikuwa na mawazo gani kurefusha mjadala wa ujambazi wa Richmond kwa takriban miaka miwili lakini tukashuhudia wakilamba matapishi yao walipounga mkono kile kinachoitwa “utekelezaji wa serikali wa maazimio ya bunge kuhusu suala la Richmond”.Kwanini hawakuiunga mono serikali tangu siku ya kwanza badala ya kuwazuga Watanzania kwa muda wote huu?

Binafsi siamini kabisa kuwa Spika Sitta ni mpambanaji dhidi ya ufisadi.Ni usanii tu ambao unaelekea kuwa moja ya sifa muhimu za wanasiasa wetu.Sitta atakuwaje kamanda wa vita dhidi ya ufisadi ilhali ndiye aliyemfungia Zitto Kabwe alipohoji ufisadi wa Buzwagi?Je sio Sitta huyohuyo aliyetishia kumpeleka Dr Slaa kwenye vyombo vya sheria pale (Slaa) alipoibua ufisadi wa EPA?

Spika Sitta,akisaidiwa na vyombo vyetu vya habari vinavyosifika kwa umahiri wa kukariri kikasuku kila kinachosemwa na wanasiasa (badala ya kwenda mbali zaidi na kuchambua kauli hizo), alitambua vema kuwa Watanzania wengi wanahitaji wanasiasa watakaoungana nao kupambana na ufisadi.Kwa lugha nyingine,alifahamu fika kuwa mapambano dhidi ya ufisadi ni mtaji maridhawa kisiasa na ungeweza kuimarisha nafasi yake.

Na kwa vile anafahamu kuwa Watanzania ni wasikivu sana hata kama wanadanganywa,akawa anapita huku na kule akijigamba kwamba “kamwe hatatishwa na wanaomwandama kisiasa kutokana na msimamo wake thabiti wa kupiga vita ufisadi”. Sitta, na wasanii wenzake waliotuhadaa kuwa ni “wapiganaji dhidi ya ufisadi” walibinafsisha ajenda ya vita dhidi ya ufisadi kiasi kwamba “kila aliyeonyesha dalili ya kutamani MAJIMBO YAO alionekana anasukumwa na umahiri ya akina Sitta katika kupambana na ufisadi”.Yaani hawakubinafisha tu hoja ya ufisadi bali wamegeuza majimbo yao kuwa mali zao za urithi ambazo hazipaswi kuguswa na Mtanzani mwengine yeyote yule.

Na Sitta anadai atawania tena kiti cha Uspika katika bunge lijalo.Kuna dalili kuwa anaweza kurejea bungeni kwa vile ametumia vema nafasi yake ya uspika kujiimariusha jimboni kwake Urambo.Lakini kama bunge lijalo litakuwa na wabunge wanaowajali wapiga kura wao basi ni dhahiri Sitta atabaki kuwa historia tu.Hatastahili hata unaibu Spika,pamoja na naibu wake wa sasa Anne Makinda,viumbe wawili waliotumia vibaya sana madaraka yao na kuendesha taasisi hiyo kwa utashi wao huku wakitumia kanuni zilizopitwa na wakati kuwaokoa mawaziri wazembe walioshindwa kutoa majibu sahihi kwenye mijadala bungeni.

“Wapiganaji feki wa ufisadi” wametuchezea shere.Upande mmoja wao ni sehemu ya mfumo wa kifisadi unaoshamiri kwa kulindana,na hawana jeuri ya kujitenga nao kwa vile ni wabinafsi.Lakini kwa upande mwingine wanataka tuwaone wao ni wenzetu,wanaguswa na matatizo yetu na wana uchungu wa dhati na nchi yetu.Wasanii hawa wanatuona sie wajinga tusiojua kuwa mishahara yao minono ni ushahidi tosha kuwa wanaishi dunia nyingine kulinganisha na walimu,madaktari,manesi,wakulima na walalahoi wengine.Wanarefusha vikao vya bunge ili posho zao nonoi ziendelee kutunisha akaunti zao.

Spika Sitta na wasanii wengine waliotudanganya kuwa wao ni wapiganaji dhidi ya ufisadi hawana sababu hata moja ya kuwaacha majambazi wa Richmond wakisafishwa na pasipo kuchukuliwa hatua yoyote.Kuna baadhi yetu tulikuwa tukifahamu tangu mwanzo kuwa hakutakuwa na hatua yoyote dhidi ya Lowassa,Karamagi,Msabaha,Mwanyika ,Hoseah na wengineo waliohishwa na ufisadi huo.Tulifahamu hivyo kwa vile kimsingi,ufisadi huo-kama ilivyo kwenye ishu za EPA,Kiwira,na kwingineko-ni matokeo ya ushirika wa kijambazi uliobuniwa na kufanikishwa kwenye korido za utawala za CCM.Kuwachukulia hatua watuhumiwa hawa kungeweza kabisa kupelekea vigogo wengine kuadhiriwa hadharani.

Hiyo haimaanishi kuwa kuadhirishwa kwa vigogo hao ni kosa,bali ni muhimu kwetu kuelewa kuwa mtandao huu wa kifisadi uliundwa kwa madhumuni ambayo mpaka sasa bado yana umuhimu kwa wahusika.Kwa lugha nyepesi.mfumo wa kifisadi ni matokeo ya moja kwa moja ya kundi la WANAMTANDAO.Na kama walivyoshirikiana kuingizana madarakani,wanaendelea kulindana ili Mtandao huu uendelee kututawala.

Na Watanzania tuna sifa nyingine ya ziada:UPOLE. Ungetarajia kusikia wananchi wakiandamana kupinga majambazi wa Richmond “kuachiwa huru na Bunge” huku wakihakikishiwa kuwa “kuna siku watarejea madarakani”. Yaani tumetapeliwa,tukachezewa akili kwa zaidi ya miaka miwili na sasa tunashuhudia majambazi wakisafishwa bungeni lakini hakuna tumetulia kana kwamba Katiba inatuelekeza tufanye hivyo!Ama kweli hiyo ndio amani na utulivu-sio kwako na kwangu bali AMANI KWA WANAOTAFUNA NCHI YETU NA UTULIVU KWA AKAUNTI ZAO ZILIZESHEHENI MAMILIONI YA FEDHA ZA KIFISADI.

Habari njema kwa mafisadi ni dalili kuwa wengi wao watarejea tena madarakani baada ya uchaguzi mkuu hapo Oktoba.Na habari njema zaidi kwao,ni kuwepo kwa kila ishara kuwa chama kinacholea ufisadi,CCM,kitaunda serikali ya awamu ya tano huku kikilindwa na idadi kubwa ya wabunge.Japo baadhi yetu tungependa kuona mabadiliko lakini ni muhimu kwetu kuwa wakweli kwa nafsi zetu.Hakuna dalili ya CCM kushindwa uchaguzi mkuu ujao kwa vile mazingira yaliyopo yanakwaza mabadiliko ya aina yoyote ile.

Hata hivyo,kama wewe Mtanzania umechoshwa na ufisadi,kulindana,ahadi hewa na ubabaishaji mwingine,una nafasi ya pekee ya kutimiza hasira zako kwa kuinyima kura CCM.Vinginevyo,hali sio tu itaendelea kuwa mbaya bali tunaweza kufika mahala watu wakalazimisha mabadiliko yatakayopelekea kutuathiri sote.Ni muhimu kwako mpiga kura kujisuta kwa makosa uliyofanya 2005 na huko nyuma,lakini kufanya kosa si kosa bali kurejea kosa.Ni mwaka huu au ndio tumeumia milele.Timiza wajibu wako.


10 Feb 2010


Baada ya danadana za muda mrefu ndani na nje ya bunge,hatimaye mjadala wa ujambazi wa Richmond umefungwa rasmi.Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana kutoka Dodoma,bunge limeridhia taarifa ya utekelezaji wa Azimio lake kuhusu suala la Richmond.Kwa lugha nyepesi,wawakilishi wetu wameridhia ujambazi uliofanywa na wahusika wa mradi huo wa kitapeli.

Kama ilivyo ada,CCM imeendelea kutumia wingi wa wabunge wake kuhakikisha kuwa matakwa yake yanatimia hata kama ni kinyume na matarajio ya Watanzania walio wengi.Wingi wa wabunge wa CCM umeendelea kuwa nyenzo muhimu kupunguza/kuondoa umuhimu wa wabunge kutoka vyama vya upinzani

Inasemekana kwamba msimamo wa pamoja wa wabunge wa CCM ulifikiwa katika kikao chake cha "kuwekana sawa",utaratibu uliiota miziz ndani ya chama hicho kila linapojiri jambo linaloashiria upinzani kwa ajili ya maslahi ya wananchi.

Wabunge wote walioamua kuzika mjadala wa Richmond ni sawa na wasaliti kwa vile nafsini na akilini mwao wanafahamu bayana kuwa namna pekee ya kumaliza suala hilo ilikuwa kwa wahusika kuwajibishwa.Madhara ya muda mrefu ya usaliti huo ni uwezekano wa kusambaa kwa virusi vya ufisadi ambavyo vinatambua bayana kuwa vina ulinzi wa kutosha kutoka chama tawala.

Kulikuwa na ugumu gani kuagiza suala hilo lipelekwe mahakamani ili kama wahusika walionewa basi iwe hivyo,na kama waliliingiza "mkenge" taifa basi wavune walichopanda?Hizi siasa za kulindana zitaendelea mpaka lini?CCM wanasahau kwamba hiki ni kipindi cha mpito tu,watafanya maamuzi ya kulindana mpaka wachoke,lakini siku ya siku watajilaumu kwa uzembe wao katika maamuzi.

Na kama kuna wa kusutwa basi na wale waliokuwa wakipata huku na kule wakijitambulisha kuwa ni "makamanda wa vita ya ufisadi".Nimeshaandika mara kadhaa kuhusu tunavyodanganyika kirahisi kila tunapowasikia akina Sitta wakidai "wanahujumiwa kwa vile wamesimama kidete kwenye mapambano dhidi ya ufisadi".Kwanini mapambano hayo yabaki ya kihisia/kufikirika zaidi kuliko vitendo?I just hope kwamba uamuzi wa kuzika hoja ya Richmond utajumuisha pia kuzikwa kwa kundi la wanafiki wajiitao "makamanda wa vita ya ufisadi".Kama ni makamanda basi ni wa mbao (wooden soldiers).

Lakini wenye uchungu wa dhati na nchi yetu bado wana fursa kubwa tu ya kutoa hukumu yao hapo Oktoba mwaka huu.Naendelea kuamini kuwa njia pekee ya kuikomboa Tanzania kutoka kwenye lindi na umasikini na bahari ya ufisadi ni kwa kuiondoa CCM madarakani.Tusitarajie lolote jipya kutoka kwa chama hicho kilichochoka kimawazo na kilichoishiwa na uwezo wa kutawala.Kuendelea kukiweka madarakani ni kukionea tu kwa vile kimeshatuthibitishia vipaumbele vyake.

Akina Muro wakituhumiwa rushwa basi hata kichanga kilichozaliwa jioni hii kitatambua namna dola "inavyowajibika".Yakija masuala ya akina Lowassa,Chenge,Kamragi,Msabaha na watuhumiwa wengine basi zinaanza ngonjera moja baada ya nyingine.Sasa kama walikuwa wanajua hatma ya mazingaombwe haya ni hii basi kulikuwa na haja gani ya kutuzingua kila kilipojiri kikao cha bunge?Na kama kawaida ya mengi ya magazeti yetu,danganya toto kuwa "bungeni hapatakalika kwa mjadala wa Richmond,Kiwira,TICTS,nk" ziliendelea kutawala vichwa vya habari.

Sababu nyingine ya ziada ya kuinyima CCM kura yako hapo Oktoba.

31 Oct 2009


Sometimes I am left wondering if democracy means anything to a common man on the street.Look at Tanzania.Our elected representatives in the National Assembly have,arguably,made democracy look like a joke.How on earth would they defend accepting (or rather demanding) extra allowances despite their hefty packages in terms of their sitting allowances and salaries?

It's more than ironic when a body entrusted with the task of making laws becomes a champion in breaking the law.Our MPs should understand that it's simply unacceptable for them to demand or receive hospitality allowances not only because it could impact their opinions but also they are already receiving more benefits an ordinary Tanzanian could only imagine about.

I am even more disgusted by the stance taken by the Speaker of the House Samuel Sitta who claims that 'hospitality allowance is offered in accordance with African tradition.Bribe is not an African tradition,and that is exactly what our MPs are doing.It is widely understood that hospitality accorded to MPs when they visit an organisation for a fact-finding mission could very well be an attempt to soften their stance towards it.In other words,our MPs could easily be bribed by lunch allowances simply because they can't have enough.

Of course, I have been one of the strongest critic of PCCB,especially after its Director General Edward Hosea was implicated by a Parliamentary Committee which was investigating the Richmond scam.However,despite "getting it right at a wrong time" PCCB has every right to investigate the said claims against our MPs.

And it is ridiculous for Speaker Sitta to give statements which imply that MPs are above the law,and therefore have a divine right to break the law.Although it could be true that the decision by PCCB ot investigate the hospitality allowances was prompted by the much anticipated House debate on the Richmond scam,it still does not make our MPs,Sitta included,immune to scrutiny on favours accorded to our representatives.

Back to my point about how ironic democracy could look when analysing African politics,it makes one wonder if the 300 plus MPs representing Tanzanians in Dodoma are actually useful.Arguably,the only thing that most of our MPs have been so effective is in demanding improvement in their benefits.They have so far failed to pressurise the Government to act responsibly in dealing with such important issues as the Richmond scandal,stupid mining contracts and the likes.How could they while they rely on the Government for 'improving' their welfare?

It looks as if the Government's trick to bring the hospitality allowance issue ahead of the debate on the Richmond scam has worked perfectly.Our MPs are so busy to justify that they deserve 'bribes' in a form of hospitality allowances that they have completely forgotten about pressing the Government to come clean on the Richmond saga.

As I have frequently written in my previous posts,I strongly believe that despite of what majority of Tanzanians would like to see or hear,the Government will never bring the Richmond farce to an end because most of the key players are still useful for its (the government's) survival.Unless you are dreaming,Lowassa and Co are too important to wanamtandao to have him on the dock to tell us how we ended up signing such a silly contract with Richmond.

17 Sept 2009


HIZI SIO HARAKATI ZA SIASA BALI NI UTOTO.NA UTOTO HUU UNAENDELEA KWA VILE CHAMA TAWALA KINA IMANI YA KUTOSHA KUWA WANAOCHEZEWA SHERE (WAPIGA KURA) BADO WAKO USINGIZINI,NA KINACHOENDELEA (UTOTO HUO) NI SAWA NA NJOZI.

HEBU SOMA HII,KISHA TAFAKARI:

Makamba amfuata Spika Sitta Urambo, ampigia magoti

*ASEMA HANA UGOMVI NAYE, ASEMA ALIKUWA MLEZI WA NDOA ZA WANAYE

Na John Dotto, Tabora

KATIKA kile kilichoelezwa kwamba, ni kujisafisha mbele ya Spika wa Bunge, Samuel Sitta, CCM imesema ipo pamoja naye katika kutekeleza majukumu yake kama Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kauli hiyo ilitolewa jana na Katibu Mkuu wa CCM, Yusufu Makamba; ikiwa ni siku chache baada ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete kuondoa utata uliotokana na maazimio ya Halmashauri Kuu ya chama hicho ulioonyesha kuwa wabunge wanaopiga kelele dhidi ya ufisadi, wanakichafua chama na serikali yake.

Akizungumza na viongozi wa CCM wilaya ya Urambo kwenye mkutano wa ndani uliohudhuriwa na Spika Sitta, Makamba, alitumia muda mwingi kumsifia Sitta kwamba ni mtu muelewa, asiyetetereka na wala kuyumbishwa na mtu yeyote na kwamba anachokifanya ni utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya chama hicho.

Makamba aliwaambia wanaCCM hao kwamba, hana chuki na Sitta, kwani hata alipokuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam alimkaribisha katika ndoa za wanawe na akapewa nafasi ya kuzungumza kama baba mlezi, heshima ambayo alisema hataisahau katika maisha yake.

Alisema wana CCM wanatakiwa kupuuza maneno ya watu wanaodai chama kina mgogoro na Spika, kwasababu hakuna kitu kama hicho na yote anayoyatekeleza kwenye Bunge ni kwa niaba ya chama chake.

Hata hivyo, baada ya kikao cha NEC, Makamba alikuwa mstari wa mbele kudai kuwa kikao kile kina uwezo wa kumuhoji mbunge yoyote hata Sitta kama anakwenda tofauti na chama.

Makamba alinukuliwa akisema NEC ni mama na akina Spika ni watoto hivyo ina mamlaka ya kuhoji mienendo yao.

Mara baada ya kikao cha NEC, Sitta alifanya ziara mkoani Tabora na kulalamika kwamba, CCM makao makuu wamewakataza viongozi wa chama hicho mkoani kumpokea.

Hatua ya Makamba kwenda Urambo kuhutubia na Sitta, inatafsiriwa kama njia ya kuweka mambo sawa na kufuta makovu ya huko nyuma baina yake na Spika.

Kwa upande wake, Sitta alimshukuru Makamba kwa kutembelea jimboni kwake na mkoa wa Tabora kwa ujumla.

Katika mkutano wa hadhara uliofanyika baada ya kikao cha ndani kumalizika, Makamba aliwahakikishia wananchi wa Urambo kwamba CCM kipo pamoja na mbunge wao Sitta, ndiyo maana wanatekeleza ahadi zote ikiwemo ujenzi wa barabara ya Urambo Kaliua mpaka Tabora Mjini.

Akizungumzia suala la ufisadi, Makamba alisema kuwa wanaCCM wote kuanzia ngazi ya matawi wanapaswa kuungana na wabunge wanaopiga vita ufisadi, kwani vita dhidi ya rushwa ni ya wanaCCM wote.

Alisema anakerwa na watu wanaosema CCM ni chama cha mafisadi kwani ufisadi wa mtu mmoja si wa CCM na akatoa mfano kuwa dhambi ya Mkatoliki mmoja si dhambi ya Askofu Kilaini wala kanisa lote.

Makamba alimaliza ziara yake jana mkoani Tabora na juzi alipokuwa akizungumza na viongozi wa CCM wakiwemo makatibu wote wa wilaya za Tabora kwenye ukumbi wa mikutano wa CCM mkoa, aliwalaumu viongozi hao kukaa kimya wakati wapinzani wanakishambulia chama hicho kwa kukipakazia maneno machafu.

Aliwataka waamke na kukipigania chama na kuacha kukaa kimya na kusubiri makao makuu ama Makamba kujibu mashambulizi.

Baada ya kikao cha Nec kilichofanyika Dodoma mwezi uliopita, Makamba na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, John Chilligati kwa nyakati tofauti walisema CCM imeunda kamati ya watu watatu, inayoongozwa na Rais Mstaafu, Ali Hassan Mwinyi kuwachunguza wabunge wenye tabia ya kuishambulia serikali nje ya vikao vya chama.

Habari za ndani ya kikao hicho ambazo baadaye zilivuja kwa vyombo vya habari, zilieleza kuwa Nec ilimweka kitimoto Spika Sitta kwa madai kuwa anaruhusu mijadala inayokichafua chama na serikali, huku baadhi ya wajumbe wakishinikiza anyang'anywe kadi ya CCM kwa madai kuwa anawapa uhuru bungeni watu wanaoishambulia serikali kwa ufisadi.

Hata hivyo, mwanzoni mwa wiki hii baada ya hotuba ya Rais, Chilligati alisema chama hicho hakina ugomvi wala uadui na wabunge wake wanaoongoza vita dhidi ya mafisadi nchini.

Kabla ya hapo, Mwenyekiti wa Mkoa wa Dar es Salaam, John Guninita ambaye alisemekana kumwandama Spika Sitta katika kikao cha NEC na akamwita faru aliyejeruhiwa anayetakiwa kumalizwa kabla hajasababisha madhara zaidi, naye alibadili msimamo na kuwaunga mkono wapiganaji wa ufisadi pamoja na Spika Sitta kwamba, wanatekeleza ilani ya CCM, hivyo wanastahili kuungwa mkono.

Mabadiliko haya ya siasa ndani ya chama hiki tawala na mfululizo wa matukio ya aina hiyo likiwemo la Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, John Mwakipesile ambaye amekaririwa katika vyombo vya habari akisema hana ugomvi na Mbunge wa Kyela, Dk Harrison Mwakyembe, anayesemekana kuwa ni hasimu wake kisiasa.

CHANZO: Mwananchi


NA HAWA NDIO TUNAOTARAJIA WAREJEE KUTUTAWALA 2010!

31 Jul 2009


Ushaskia kuhusu political conmanship?Hebu soma kwanza habari ifuatayo kisha tujadili




Spika Sitta aomba ulinzi zaidi, adai nguvu ya mafisadi inahatarisha maisha yake

Spika wa Bunge la Jamuhuri ya Muuangano wa Tanzania sasa anahofia maisha yake kutokana na vitisho vya mafisadi

Spika Sitta aomba ulinzi zaidi, adai nguvu ya mafisadi inahatarisha maisha yake

Kizitto Noya, Dodoma na Boniface Meena

SPIKA wa Bunge Samuel Sitta ameiomba Serikali kumwongezea ulinzi kwa kuwa mafisadi wameongeza nguvu ya vita dhidi yake.

Spika Sitta alisema hayo alipokuwa akizungumzia tuhuma dhidi yake, zilizoripotiwa jana na baadhi ya vyombo vya habari (sio Mwananchi) kuwa anafanya njama kuchoma nyaraka za Bunge.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, Spika anadaiwa kula njama ili kuchoma ofisi ya mhasibu wa Bunge ili kuharibu nyaraka muhimu zinazomhusisha na ubadhirifu wa fedha za Bunge.

Lakini Spika Sitta alijibu tuhuma hizo bungeni akisema taarifa hizo zina mkono wa wabaya wake, wenye lengo la kumchafua katika utendaji wake.

“Hivi kama kweli nataka kuficha faili la Bunge nani anaweza kunizuia humu ndani?” alihoji Spika Sitta na kuongeza:

“Hizi ni taarifa za wabaya wangu, wanachofanya ni kuziweka kwenye internet kwanza halafu wanazisambaza kwenye vyombo vyao maalum, magazeti manne; gazeti la Tazama, Tanzania Daima na mengine mnayoyaona," alisema Spika na kuongeza:

“Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba mnipe ulinzi zaidi, hii vita ni ngumu na kubwa sasa. Ulinzi mnaonipa naona hautoshi,” alilalamika Spika Sitta na kuwaponda wanaomwandama kuwa hata iweje, ataendelea kushinda ubunge jimboni kwake na kuwa Spika kama bado atakuwa hai mwakani.

Alifafanua kuwa fedha wanazopeleka maadui zake jimboni kwake Urambo zinasaidia kuimarisha maendeleo, lakini hazitomng’oa madarakani.

"Wananchi wangu wanajua ninachokifanya jimboni kwangu, hata wakipeleka pikipiki bado nitashinda," alisema Sitta.

Mara kwa mara Spika Sitta amekuwa akidai kwamba anaandamwa na mafisadi ambao wanataka aache kufichua maovu yao.

Spika Sitta alisema hayo muda mfupi baada ya kumaliza kutoa mwongozo kwa mbunge wa Micheweni (CUF), Shoka Khamis Juma, kwamba chama fulani kina tabia ya kununua shahada za kura wakati wa chaguzi.

Katika mwongozo wake, Spika alimtaka mbunge huyo kufuta kauli yake bungeni kwa kuwa ushahidi aliotoa kuthibitisha kauli hiyo ni dhaifu.

“Madai ya Shoka ni tuhuma kama tuhuma zozote zinazotolewa na wanasiasa wengine,” alisema.

Akifafanua kuwa Shoka ameshindwa kuthibitisha tuhuma zake kwa kuwa ametoa ushahidi wa magazeti ambayo sio yote yanaweza kuaminika.

“Magazeti yanaweza kuwa chanzo cha taarifa kwa wabunge katika kuchangia hoja zao, lakini sio kigezo pekee cha kumwezesha Spika kutoa mwongozo,” alisema Sitta na kuendelea:

“Hivyo mheshimiwa Shoka hawezi kulindwa na kifungu namba 63 (2), kwa mantiki hiyo namtaka kwa kanuni namba 63 (1) afute kauli yake humu bungeni kabla ya kumalizika kikao hiki cha Bunge”.

Juni 12 mwaka huu mbunge huyo wa CUF alitamka bungeni alipokuwa akiuliza swali la nyongeza kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimekuwa na tabia ya kuiba shahada za kupigia katika maeneo ambayo kinaona hakiungwi mkono.

Naibu Spika Anne Makinda ambaye alikuwa anaongoza kikao cha Bunge siku hiyo, alimtaka mbunge huyo athibitishe kauli yake, naye alifanya hivyo Juni 17, mwaka huu kwa kuwasilisha kwa Spika nakala za magazeti yaliyoripoti uchaguzi wa Jimbo la Busanda.

Hata hivyo, Spika Sitta alisema kwa kuwa hakuna ushahidi wa hukumu kuhusu tuhuma hizo, madai ya Shoka ni tuhuma kama tuhuma zingine zinazotolewa na wanasiasa majukwaani, hivyo kumtaka afute madai yake.




CHANZO: Mwananchi

Nadhani sasa kuna umuhimu wa kuangalia kama Spika huyu wa Viwango na Spidi bado anastahili kuendelea na wadhifa wake ambao ni wa nne kitaifa.Natoa hoja hiyo kwa vile kuna kila dalili kuwa Spika Samwel Sitta sasa anaogopa kivuli chake mwenyewe.




Ni hatari kwa kiongozi wa kitaifa kama Spika kutoa madai mazito namna hiyo pasipo kuwa na uthibitisho wowote.Hivi hao mafisadi wanaohatarisha maisha yake ni akina nani?Nauliza hivyo kwa vile kwa mujibu wa maelezo yake inaonyesha anawafahamu hata kwa majina.Sasa tunapokuwa na kiongozi wa kitaifa ambaye pindi maisha yake yanapokuwa hatarini (kama unaamini anachosema) anakimbilia kuomba aongezewe ulinzi hadharani,then hapo kuna mushkeli.



Ni hatari zaidi kumsikia Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,taasisi tukufu yenye jukumu la kutunga sheria za nchi,akiuliza bila aibui wala uoga "Hivi kama kweli nataka kuficha faili la Bunge nani anaweza kunizuia humu ndani?” You can't be serious,Mzee wa Spidi na Viwango!Yaani unatuambia kuwa kwa wadhifa wako unaweza kuficha nyaraka muhimu za Taifa (mfano faili la Bunge) na hakuna mwenye uwezo wa kukuzuia?Nadhani unatafsiri vibaya madaraka yako.Uspika ni nafasi inayoongozwa kwa taratibu na sheria,za nchi na za Bunge unaloongoza.Sasa unapotuambia kuwa hakuna wa kukuzuia ndani ya Bunge kuficha faili (ukijiskia kufanya hivyo) unatuaminisha kuwa aidha huelewi mipaka ya kazi yako,au unadhani Uspika ni kuwa juu ya sheria za nchi na Bunge,au kulewa madaraka.



Tukiwa hapohapo kwenye hoja yako ya "hakuna wa kukuzuia...",na tukiamini kuwa ni kweli hakuna wa kukuzuia,je utalalamika kuwa mafisadi wanakuwinda wakikuzushia zengwe kwamba umeficha nyaraka muhimu zaidi ya faili la Bunge?Sawa utasema wanakuandama lakini ushawapa hoja kwamba "ukitaka kuficha faili la bunge hakuna wa kukuzuia".Well,wao wanaweza kuja na tuhuma kubwa zaidi ya kuficha faili.Laiti busara zingetumika,ungeishia tu kukanusha tuhuma za kwamba una mpango wa kuchoma moto ofisi za bunge,na sio kukurupuka kudai una uwezo wa kuficha faili la bunge pasipo kuwapo wa kukuzuwia.



Ni rahisi kwa Spika kuomba aongezewe ulinzi (kwa kigezo kuwa ulinzi alionao sasa hautoshi) kwa vile gharama za kuongezewa ulinzi zitabebwa na walipa kodi na si kutoka mfukoni mwa Spika.Hoja hii ya Spika Sitta pia inaweza kufanya tujiulize iwapo licha ya nafasi yake ya Uspika,Mheshimiwa Sitta pia ni mtaalam wa mambo ya ulinzi wa viongozi,na review aliyofanya katika protection anayopewa hivi sasa imempelekea kuhitimisha kuwa ulinzi alionao hautoshi.Hii ni sawa na kuwadharau professionals wenye jukumu hilo,ambao naamini wangetambua mapungufu hayo kabla hata ya Spika Sitta kutamka hadharani.



Lakini twende mbali zaidi kwenye hili la "ulinzi alionao Spika hautoshi"Je anaweza kututhibitishia japo tukio moja linaloashiria kutotosha kwa ulinzi alionao hivi sasa?Yaani kutuhumiwa kuwa anataka kuchoma moto ofisi za bunge, na "maadui zake kumwaga fedha jimboni kwake" vimekuwa matishio ya kiusalama yanayotosheleza kufikia uamuzi wa kumuongezea ulinzi?



Kichekesho ni kwamba wakati Spika akimtaka Mbunge wa Cuf (Mheshimiwa Shoka Hamis Juma) afute kauli yake kwa kuwa "ushahidi aliotoa-katika madai kuwa kuna chama flani kinanunua shahada wakati wa chaguzi-ni dhaifu",yeye mwenyewe anafanya kilekile cha kutoa madai dhaifu kuwa nguvu ya mafisadi inahatarisha usalama wake ilhali hajaweza kutoa uthibitisho wowote zaidi ya "kauli za kisiasa" kuwa maadui zake wanapeleka pesa jimboni kwake ili asirejee bungeni.Ana uhakika gani kuwa hao anaowaita maadui zake si wananchi wenye dhamira ya kuleta maendeleo katika jimbo hilo pasipo kuwa na ajenda za kisiasa?Au Spika Sitta anataka kutuambia kuwa ni yeye tu aliye na hatimiliki ya kupeleka misaada katika jimbo hilo?Jamani,yaani hadi maendeleo ya jimbo yanafanywa kuwa mithili ya maamuzi ya mtu binafsi!?



Kuna mengi ya kujadili kuhusu kauli za Spika Sitta,lakini lililo wazi ni kwamba nafasi anayojipachika ya ukinara wa mapambano dhidi ya ufisadi ni sawa na political conmanship.Kwa lipi hasa?Sio Sitta huyu aliyempa "kifungo" Zitto Kabwe kwa "kosa" la kumkalia kooni Karamagi kuhusu Buzwagi?Sio Spika Sitta huyu aliyetishia kumfungulia mashtaka Dkt Wilbroad Slaa pale mbunge huyo wa Karatu aliposhikilia bango kuhusu ishu za ufisadi?Ni lipi alilofanya Samweli Sitta,kama Spika wa Bunge la Jamhuri au Mbunge wa Urambo linaloweza kumjumuisha kwenye kundi la vinara wa mapambano dhidi ya ufisadi?Yaani Watanzania wenzake kutamani jimbo la Urambo imekuwa ufisadi?Au mtu kutamani nafasi ya uspika imekuwa ufisadi?



Lakini kwa vile siasa zetu kwa sasa zinaruhusu mambo ya ajabu kabisa kutokea,kauli hizi za Spika Sitta hazitawahangaisha wenye dhaman ya uchambuzi wa kauli hatari kama hizi na kuchukua hatua za haraka.Ni business as usual,kauli imetolewa,siku imepita,and life goes on!



Na kwa vile magazeti yetu yako bize zaidi kuripoti habari badala ya kuchambua mantiki ya habari husika,yayumkinika tutasikia makubwa zaidi ya kauli hizi za wanasiasa wanaoogopa vivuli vyao wenyewe.Na kwa vile kilio,kicheko,kuchafua hewa na hata kukoroma kwa mwanasiasa kunatosha kuwa leading news kwenye magazeti yetu,basi tutarajia vimbwanga zaidi.



Trust me,tutashuhudia vituko vingi zaidi na zaidi kadri siku zinavyoyoyoma kuelekea uchaguzi mkuu wa 2010.By the way,si ndio tunaelekea kile kipindi cha usanii wa kisiasa ambapo watu wazima hupiga magoti majukwani na wengine kutoa shikamoo hata kwa watoto wadogo alimradi wahakikishiwe kura?




Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.