Showing posts with label SEIF SHARIF HAMAD. Show all posts
Showing posts with label SEIF SHARIF HAMAD. Show all posts

4 Mar 2020



Kuna njia mbalimbali za kufanya uchambuzi wa kiintelijensia, njia zinazotegemea vigezo mbalimbali, kigezo muhimu zaidi kikiwa tukio husika na/au "key players" (kwenye ushushushu tunawaita "subjects") katika tukio hilo.

Katika kufanya uchambuzi wa kiintelijensia kuhusu tukio la jana ambapo Rais Magufuli alikutana na viongozi wakuu watatu wa upinzani, Maalim Seif Sharif Hamad wa ACT-Wazalendo, James Mbatia wa NCCR-Mageuzi, na Ibrahim Lipumba wa CUF, nitatumia kanuni ijulikanayo kama 'Linchpin,' ambayo ni mwafaka zaidi pale ambapo "ukweli mzima" upo bayana (au "vipande vya ukweli).



Kanuni hii ya Linchpin ilibuniwa na Naibu Mkurugenzi wa zamani wa Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA), Douglas MacEachin, na inahusu "matukio ya ghafla/ya kushangaza," ambapo aliitumia kanuni hiyo kueleza tukio la ghafla na Iraki kuivamia Kuwait mwaka 1990. 

Katika kanuni hii, uchambuzi wa kiintelijensia unatathmini tukio/matukio husika kwa kuzingatia "ukweli uliopo/unaofahamika," kitu tofauti kidogo na mbinu nyingine za uchambuzi wa kiintelijensia zinazoanza na hisia au dhana (kama ile ya ACH -Dhana Zinazoshindana -nilioutumia majuzi kuchambua tukio la Membe kufukuzwa uanachama wa CCM)

Kwa vile lengo la makala hii sio kutoa darasa la "mbinu za uchambuzi wa kiintelijensia," bali kutumia kanuni ya Linchpin kueleza "tukio la ghafla," la Jiwe kukutana na Maalim Seif, Mbatia na Lipumba, ni vema nikahamia kwenye uchambuzi husika.

Kwa kutumia kanuni hiyo, kuna "ukweli " (facts) kadhaa ambao ni msingi wa uchambuzi huu. Ukweli mkubwa zaidi ni kitu nilichokiongea wiki iliyopita baada ya mwandishi Erick Kabendera kuachiwa baada ya kuwekwa jela kwa uonevu kwa zaidi ya miezi sita.



Awali nilieleza kuhusu hilo la "Jiwe kukaliwa kooni na mabeberu" katika chapisho langu hili


Kwahiyo ukweli mmoja - na muhimu zaidi - uliopelekea "tukio hilo la ghafla" ni shinikizo la mabeberu. Shinikizo ambalo wiki iliyopita lilipelekea mwandishi Kabendera kuachiwa, na wiki hii limepelekea Jiwe kukutana na viongozi hao watatu wa upinzani.

Nimetanabaisha kuwa huo ni "ukweli muhimu zaidi" kwa sababu kuna ukweli mwingine japo sio wenye uzito sana. 

Uamuzi wa Jiwe kukutana na akina Maalim Seif jana ni sawa na "kuua ndege wawili kwa JIWE moja." Kwa upande mmoja amefanikiwa kutuliza shinikizo la mabeberu ambao wameweka bayana msimamo wao kuwa wanaweza kutochangia bajeti ijayo endapo ukandamizwaji wa demokrasia na haki za binadamu utaendelea. Amewatuliza mabeberu kwa kuwaonyesha kuwa "demokrasia ipo" na ndio maana ameweza kukutana na sio kiongozi mmoja tu wa upinzani bali watatu kwa mkupuo.

Nimesema "ameua ndege wawili kwa jiwe moja." Na "ndege" wa pili ni Membe. Mkutano wake huo na akina Maalim Seif unafikisha salamu muhimu kwa Membe aliyefukuzwa uanachama wa CCM wiki iliyopita, kwamba "hao unaotaka kujiunga nao ndo hawa niko nao hapa Ikulu kwangu."

Kama nilivyoeleza katika uchambuzi kuhusu tukio hilo la Membe kufukuzwa uanachama wa CCM, kuna uwezekano mkubwa wa mwanasiasa huyo kujiunga na ACT-Wazalendo. Na kwa vilekufukuzwa kwake CCM ni matokeo ya uoga wa Jiwe kuhusu upinzani kwenye nafasi ya urais, Membe "kuwa mgombea wa urais kwa tiketi ya ACT-Wazalendo" ni worst nightmare kwa Jiwe. 

Naomba nirudie kusisitiza kuwa uoga huo wa Jiwe hauna msingi kwa sababu Membe hana uwezo wa kumwangusha Jiwe kwa sababu nilizowahi kutanabaisha katika makala hii.



Kwahiyo Jiwe akiweza kumzuwia Membe kisaikolojia asiwaamini Wapinzani itakuwa ni nafuu kubwa kwake na uoga wake.

Ukweli mwingine kuhusu mkutano huo kati ya Jiwe na viongozi hao wa upinzani ni "busara ya kisiasa" inayosema "kuwa karibu na marafiki zako, lakini kuwa karibu zaidi na maadui zako."

Ukweli mchungu kuhusu wanasiasa wetu - wa CCM na hao wa upinzani - ni huu: wote wapo katika "tabaka tawala" (ruling class). Hapana, simaanishi kuwa akina Seif, Mbatia na Lipumba ni sehemu ya utawala wa Jiwe bali ukiangalia kwa undani wasifu wa viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa, unaweza kubaini kuwa "wote ni wale wale."

Na ukiangalia wasifu wa Maalim Seif, Mbatia na Lipumba hutoshindwa kubaini kuwa ni watu ambao tumekuwa tukiwasikia "miaka nenda miaka rudi" lakini "wakiwa upande wa pili," kwa maana "sio upande wetu" watu wa tabaka la chini. Kwa kuazima neno la mtaani, hawa ni "vigogo."

Ukweli mwingine ni kwamba mkutano huo wa Jiwe na akina Maalim Seif "ndio siasa ilivyo." Kuna kitu kwenye siasa kinaitwa "realpolitik" ambacho kwa tafsiri isiyo rasmi ni "siasa ilivyo kimatendo kuliko kinadharia/kiitikadi." 

Sasa kwenye "siasa halisi" iwe ya kitaifa au ya kimataifa, "hakuna marafiki au maadui wa kudumu bali maslahi tu." Na ndio maana licha ya msimamo wake msimamo wake mkali dhidi ya vikundi vya kigaidi, na kauli maarufu kuwa "we don't negotiate with terrorists," majuzi Marekani ilifikia makubaliano na kundi la kigaidi la Taliban.

Na jana ilifahamika kuwa Rais wa nchi hiyo Donald Trump aliwapigia simu viongozi wa kundi hilo, kitu ambacho kabla ya tukio hilo kilikuwa sio rahisi kukifikiria.



Baada ya kuangalia "ukweli"(facts) huo unaojenga msingi wa uchambuzi huu, kanuni ya Linchpin inawezesha kujenga picha ya matarajio yanayohusiana na tukio/watu husika. Hapa ninamaanisha kuwa hadi kufikia hapa, yawezekana kueleza nini kinaweza kujirihivi karibuni au huko mbeleni.

Moja ni hiyo sintofahamu inayoweza kumkumba Membe baada ya kumuona Maalim Seif akiwa Ikulu na Jiwe. Ikumbukwe tu Lowassa alipoonekana Ikulu bila kutarajiwa "waumini"wake walimtetea na kuamini porojo zake kuwa kaambiwa arudi CCM lakini amegoma. Baadaye ukweli ukadhihirika baada ya Waziri Mkuu huyo wa zamani kurejea CCM.

Simaanishi kuwa Maalim Seif atakubali kurudi CCM. La hasha. Kinachoweza kutokea ni Jiwe kujaribu tena "kuua ndege wawili kwa JIWE moja." Anaweza kumfarakanisha Maalim Seif na Zitto na hapohapo kupunguza tishio kubwa kwake kutoka kwa Zitto kama Zitto, na Zitto akiwa na Maalim Seif.

Ikumbukwe tu kuwa japo Lowassa alikuwa kama 'mungu-mtu' huko Chadema, kitendo chake cha kuonekana Ikulu na Jiwe kiliwafanya hata baadhi ya "waumini" wake waanze kuwa na hofu nae.

Sina uhakika hali ikoje huko ACT-Wazalendo baada ya Maalim Seif kukutana na Jiwe, lakini ni siri ya wazi kuwa Jiwe na Zitto "picha haziivi," na wala sio jambo la kushangaza kuona Zitto hakualikwa kwenye mkutano huo.Na wala  sina hakika kama angekubali mwaliko wa Jiwe.

Kuhusu Mbatia na Lipumba, hakuna haja ya kupoteza muda kuwajadili maana "wapo kama hawapo." 

Moja ya maswali muhimu kuhusu Malim Seif kwenda Ikulu kukutana na Jiwe ni je alipata ridhaa ya Zitto na chama kwa ujumla? Na je tukio hili linaweza kuzua mpasuko huko ACT-Wazalendo? Pengine kukusaidia kuelewa vema "siasa za ACT-Wazalendo," pitia uchambuzi wangu huu nilioufanya mara baada ya Maalim Seif kujiunga ACT-Wazalendo.

Huhitaji kuwa na uelewa mkubwa wa siasa za Tanzania yetu kubaini kuwa mnufaika mkubwa wa mkutano huo kati ya Jiwe na viongozi hao watatu wa upinzani ni Jiwe mwenyewe. 

Hilo lipo wazi. Lisilo wazi ni "yanayoweza kujiri" kutokana na mkutano huo. Je Maalim Seif anaweza kuangaliwa kama "msaliti" kwa kukubali "kukutana na dikteta ambaye majuzi tu akiwa Zanzibar alikuwa anamwaga sumu kwa Dkt Shein kuhusu jinsi ya kumdhibiti Maalim Seif?"

Kwa upande mwingine, kama kweli Jiwe alikuwa na nia njema ya kukutana na viongozi wa upinzani basi pengine wa kwanza kabisa kupewa kipaumbele cha kukutana nae angekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, ambaye majuzi tu alimuomba Jiwe kuwe na MARIDHIANO. Lakini ni vema "kuweka akiba ya maneno" kwani haitokuwa jambo la kushangaza tukimuona Mbowe Ikulu kama alivyoongozana na timu yake Mwanza kwenye sherehe za Uhuru Desemba 9 mwaka jana. 

Nihitimishe uchambuzi huu kwa kutahadharisha kuwa intelijensia sio sayansi timilifu (intelligence is not exact science) licha ya uchambuzi huu kuongozwa na kanuni ya Linchpin ambayo ina ufanisi mkubwa penye uwepo wa ukweli kuhusu tukio/mtu husika.


18 Mar 2019


 
Leo Machi 18, 2019 ni siku ambayo lazima iingie kwenye vitabu vya kumbukumbu kwa sababu kuu tatu, ambazo zote zinamhusu mwanasiasa mkongwe Seif Sharif Hamad na Chama cha Wananchi (CUF)

Sababu ya kwanza, leo ni siku ambayo mwanasiasa huyo, maarufu kwa jina la Maalim Seif, "ametimuliwa" rasmi kutoka chama alichoshiriki kukiasisi (CUF).
Kibaya zaidi, "kutimuliwa" huko kumekuwa na baraka kisheria, baada ya Mahakama Kuu kumtambua Profesa Ibrahim Lipumba kuwa mwenyekiti halali wa chama hicho.

Ikumbukwe tu Lipumba alitangaza kujiuzulu uenyekiti kwa sababu anazozijua yeye kabla ya kuamua kurejea kwenye wadhifa huo "kwa mabavu." Kwa bahati mbaya – au pengine makusudi – sheria na kanuni za CUF zilikuwa zinatoa mwanya kwa Lipumba (au mwanasiasa mwingine yeyote yule) kufanya "uhuni" kama huo.

Sababu ya pili, ni kwamba leo CUF imekabidhiwa rasmi kwa Lipumba. Kisheria. Mahakama imetenda haki kwake kwa sababu japo alichofanya ni uhuni, kisheria uhuni huo ulihalalishwa na CUF yenyewe.

Hili la Lipumba kukabidhiwa chama si jambo dogo. Kuna mawili hapa. Moja, hii inaweza kuwa fursa nzuri kwa Lipumba kukijenga chama hicho na hatimaye kukirejesha kwenye nafasi ya kuaminika kama "mbadala wa CCM."

Lakini la pili, na hili ndilo ninahisi litatokea, ni mwanzo wa mwisho wa CUF. Sio siri kuwa Lipumba amesaidiwa sana na CCM kuipora CUF kutoka mikononi mwa Maalim Seif. CCM hawajafanya hayo kwa vile wanampenda Lipumba.Hapana. Wanamtumia tu kumdhibiti Maalim Seif ambaye licha ya kila hujuma zilizokuwa zikifanywa na CCM na taasisi zake, ameendelea kuwa mwanasiasa maarufu zaidi kuliko wote katika siasa za Zanzibar.

Sasa, baada ya Lipumba kutumika "kummaliza Seif ndani ya CUF," kuna uwezekano wa aina mbili tu. Wa kwanza ni kwa mwanasiasa huyo msomi kukubali kuendelea kutumika kama kibaraka wa CCM huku CUF ikigeuka kuwa CCM-B, na wa pili, ni kujaribu kusimama kama chama halisi cha upinzani na hapohapo "kumwagiwa radhi na CCM" na hatimaye kupelekea kifo cha chama hicho.

Uwezekano mkubwa zaidi ni huo wa kwanza - ukibaraka. Kwamba CUF haitokufa. CUF itaendelea kushiriki chaguzi mbalimbali. CUF itajenga taswira ya chama kamili cha upinzani. Lakini uwepo huo wa CUF hautokuwa kwa manufaa ya chama hicho au siasa za upinzani bali kwa manufaa ya CCM.

Kuna kila dalili kuwa CCM itaisaidia CUF kujitanua nchi nzima kwa sababu moja kuu: uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 utakuwa mbovu kuliko chaguzi zote zilizowahi kutokea Tanzania. Kuna uwezekano mkubwa tu kwa baadhi ya vyama vikuu vya upinzani kutishia kususia uchaguzi huo. Na hapo ndipo CUF ya Lipumba itakapotumika kuhalalisha "ushindi wa Magufuli/CCM."

CCM itaisaidia CUF kuweza kusimamisha wagombea takriban kila jimbo kwa upande wa Tanzania Bara. Lakini pia CCM itaisaidia CUF kuendelea kuwa chama imara cha upinzani huko Zanzibar, ambako uimara wake utasaidia kugawa kura dhidi ya CCM na wagombea wake.

Hata hivyo, "laana ya kutumika" itaikumba CUF baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 na kama isipoishia kusambaratika basi itabaki "chama jina" kama TLP ya Mrema.

Kuhusu uamuzi wa Maalim Seif kuhamia ACT- Wazalendo, japo hatua hiyo inaweza kuwashangaza baadhi ya watu, ukweli mchungu baada ya Mahakama Kuu kuhalalisha "uhuni" wa Lipumba, sambamba na "uhuni" wake mwingine majuzi ambapo "alijitangaza" kuwa Mwenyekiti kupitia "uchaguzi mkuu hewa" ambao pia "ulimtimua Maalim Seif" kwa kuteua mtu mwingine kushika wadhifa wa Katibu Mkuu.

Kwa kuzingatia muda mfupi uliosalia kabbla ya uchaguzi mkuu wa mwakani, Maalim Seif kuendelea kutafuta haki yake mahakamani kungeweza kumkuta akiwa bado kwenye korido za mahakama wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu ujao. Ni vigumu mno kwa chama cha siasa kushiriki kikamilifu kwenye uchaguzi mkuu huku kikiwa kinakabiliwa na mpasuko katika uongozi wake wa juu.

Kwahiyo, kimkakati, uamuzi huo wa Maalim Seif unaeleweka, na unaweza kuwa ni mbinu muhimu kwake kuendelea kuwa relevant kisiasa.

Hata hivyo, kuna uwezekano wa aina mbili kuhusu mustakabali wa Maalim Seif na wa chama chake kipya cha ACT- Wazalendo.

Uwezekano wa kwanza ni kwa chama hicho kuibuka kuwa tishio katika siasa za Tanzania. ACT – Wazalendo ni chama kizuri lakini ambacho hakikui. Kimeendelea kuwa "chama cha mtu mmoja" chini ya uongozi wa Zitto Kabwe. Kwa muda mwingine, chama hicho kimekuwa cha kiharakati zaidi kuliko cha kisiasa.

Mapungufu hayo yanaweza kubadilika kwa njia kuu tatu. Kwanza, Maalim Seif hajawahi kupata fursa nzuri ya kunadi mvuto wake kwenye majukwaa ya siasa za Tanzania Bara. ACT-Wazalendo wanaweza kuwa Jukwaa muhimu katika hilo.

Pili, Zitto  hajawahi kupata jukwaa mwafaka kunadi mvuto wake wa kisiasa huko Zanzibar. Kwa kuungana na Maalim Seif, hii inaweza kuwa ndio fursa mwafaka kwake.

Tatu, ACT-Wazalendo kama chama inaweza kupata fursa mwafaja kabisa ya kuwa chama cha kitaifa badala ya kuwa "chama cha Kigoma."

Haya yote yatawezekana tu endapo kutakuwa na "kujitoa mhanga" kati ya mwenyeji Zitto na mgeni Maalim Seif. Kwa mara ya kwanza, Zitto atajikuta akiongoza chama ambacho ndani yake kuna mwanasiasa maarufu zaidi yake. Naam, Maalim Seif ni mkongwe zaidi kisiasa kuliko Zitto. Endapo Zitto "atajitoa mhanga" (make a sacrifice) na kukubali "kumezwa" na umaarufu wa Maalim Seif, basi chama hicho kitakuwa na fursa kubwa ya kupanuka zaidi na hata kuja kuwa chama kikuu cha upinzani katika pande zote za Muungano.

Lakini endapo kutakuwa na mgongano wa ego kati ya wanasiasa hao, basi mustakabali wa chama hicho utakuwa mashakani. Lakini pengine uwezekano wa hili kutokea ni mdogo kutokana na ukweli kwamba suala la Maalim Seif kujiunga na ACT-Wazalendo sio limetokea tu ghafla. Ni dhahiri kuwa kulikuwa na majadiliano ya muda mrefu na yayumkinika kuhisi kwamba tofauti kati ya wanasiasa hao wawili (Maalim Seif na Zitto) zilifanyiwa kazi wakati wa majadiliano hayo.

Suala jingine ambalo linaweza kuijenga ACT-Wazalendo "mpya" (ya Zitto na Maalim Seif) au kuibomoa ni mtihani ulioikumba Chadema mwaka 2015.

Kwa mwelekeo ulivyo ndani ya CCM ambapo Magufuli hafanyi siri kuwa anataka chama hicho kiwe chini ya uongozi wa watu wake (wengi wao wakiwa wana-Kanda ya Ziwa wenzake), kuna uwezekano mkubwa wa kuibuka wimbi kubwa tu la wanasiasa wenye majina watakaotaka kuhamia Upinzani. Na endapo Zitto na Maalim Seif watakuwa "dream team" ya kuaminika, basi ACT-Wazalendo inaweza kuwa na mvuto zaidi kwa "wakimbizi kutoka CCM" kuliko Chadema.

Si ajabu kwa wanasiasa kama Nape Nnauye, Mwigulu Nchemba, Bernard Membe kujiunga na ACT-Wazalendo endapo chama hicho kitaonekana kuwa kinaweza kutoa ushindani wa dhati dhidi ya CCM hapo mwakani.

Sasa, wakati kupokea "majina makubwa" kutoka CCM husaidia kuongeaza umaarufu wa chama, uzoefu umeonyesha kuwa wengi wao wenye majina hayo makubwa ni wanafiki wanaokwenda upinzani kwa sababu zao binafsi na sio kwa maslahi ya vyama husika vya upinzani.
Kibaya zaidi, kila ujio wa "wahamiaji" hao ni fursa mwafaka kwa CCM kupandikiza "mamluki" wake kama ilivyotokea kwa Chadema ilipompokea Lowassa mwaka 2015.

Je ACT-Wazalendo "mpya" inaweza kutoa upinzani wa dhati dhidi ya CCM hapo mwakani? Jibu fupi ni "muda ndio utaongea" (time will tell). Jibu pana zaidi ni kwamba japo uwezekano huo upo lakini sidhani kama muda unatosha kukitanua chama hicho nchi nzima hususan katika kipindi hiki ambacho chama pekee cha siasa kinachoruhusiwa kufanya shughuli za siasa ni CCM tu.

Hata hivyo, endapo mkazo wa ACT-Wazalendo utakuwa katika sio tu kuongeza idadi ya wanachama bali kujenga kuaminika kwa "Watanzania wasio na vyama," basi huenda chama hicho kikafanya vizuri kwenye uchaguzi mkuu huo.

Ni hivi, kundi muhimu kabisa la wapigakura katika uchaguzi mkuu wowote ule nchini Tanzania ni "Watanzania wasio na vyama." Kwamba, hakuna chama cha upinzani kinachohitaji kupoteza muda wake kuwashawishi wafuasi wa CCM wakipigia kura, kama ambavyo CCM haina muda na wafuasi wa upinzani kuwashawishi waipigie kura. Vilevile, si CCM wala vyama vya upinzani vinavyohitaji kuwashawishi wanachama/wafuasi wao wapigie kura vyama vyao. Watu wanaohitaji kushawishiwa ni hao wasio na vyama. Na habari njema ni kwamba kundi hilo ndilo lwenye idadi kubwa zaidi ya wapiga kura.

Kwa mujibu wa takwimu zisizo rasmi, CCM ina takriban wanachama milioni 8 ilhali wapinzani wana wanachama takriban milioni 5. Kwa makadirio, takriban Watanzania milioni 25 walijiandikisha kupiga kura katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015. Kwahiyo, milioni 8 wa CCM jumlisha milioni 5 wa upinzani jumla inakuwa milioni 13. Ukichukua milioni 25 kutoa miloni 13 unabakiwa na milioni 12. Kwa makadirio, hawa ni "wapigakura wasio na vyama." Na kimahesabu, hata nusu tu ya kundi hili likielemea upande mmoja, upande huo unaweza kabisa kushinda uchaguzi husika. Of course, hapo tunaweka kando hujuma za kawaida za kuibeba CCM kwenye takriban kila uchaguzi mkuu.

Nimalizie kwa kukumbusha kuwa uchambuzi huu sio exact science. Umeelemea kwenye uelewa wa kutosha wa mchambuzi kuhusu siasa za Tanzania.

Kadhalika, uchambuzi huu ni endelevu. Utafanyiwa marejeo mara kwa mra kila kutakapokuwa na umuhimu wa kufanya hivyo


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.