Showing posts with label SIASA TANZANIA. Show all posts
Showing posts with label SIASA TANZANIA. Show all posts

18 Feb 2018


Nianze makala hii kwa kutoa salamu zangu za pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu Daniel John, ambaye hadi alipouawa kinyama alikuwa Katibu wa Chadema kata ya Hananasifu, na pia kwa familia, ndugu,jamaa na marafiki wa marehemu Acqulina Akwilin (samahani kama nimekosea jina).

Kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa na Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe, mwili wa marehemu Daniel uliokotwa kwenye ufukwe wa Coco jijini Dar es Salaam ukiwa na majeraha. Alieleza kuwa awali marehemu alichukuliwa na Land Rover nyeupe na watu waliohifanya askari polisi, lakini tangu wakati huo Polisi hawakuwa na taarifa zozote za kiuchunguzi, na hata jitihada za kupatikana mwili huo zilifanywa na Chadema wenyewe.




Kwa upande wa marehemu Acquilina, kifo chake kilisababishwa na kasumba hatari inayozidi kuzoeleka kwa watumishi wa vyombo vya dola kufanya mzaha katika matumizi ya silaha za moto, ambapo katika tukio husika, polisi waliokuwa wakizuwia maandamano ya wafuasi wa Chadema, walitumia risasi za moto,na moja kati ya risasi hizo ilipelekea kifo cha binto huyo, ambaye hadi mauti yanamfika alikuwa mwanafunzi katika Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) akisomea shahada ya ununuzi na ugavi.
Ni muhimu kutambua kuwa vifo vyote hivi viwili vingeweza kuepukika laiti utu na ubinadamu wetu ungewekwa mbele ya chuki za kisiasa. Huhitaji kuwa mjuzi wa uchunguzi wa mauaji kufahamu kuwa vifo hivyo ni matokeo ya chuki, hujuma, uonevu na kila aina ya baya dhidi ya chama kikuu cha upinzani, Chadema, kuhusiana na kampeni za uchaguzi mdogo katika jimbo la Kinondoni, ambalo kama ilivyo kwa jimbo la Siha, ni "piga ua" kwa CCM ishinde. Yaani chama hicho tawala kilitarajiwa kutumia kila mbinu kuhakikisha inashinda katika majimbo hayo mawili.

Lakini kabda sijaingia kwa undani katika mada hii - ambayo lazima nikiri kwamba inanipa wakati mgumu sana kuiandika kwa sababu nimebanwa na mchanganyiko wa majonzi na hasira, sambamba na hofu ya kuona taifa langu likisukumwa kuelekea kwenye upotevu wa amani na mshikamano wetu – naomba kuweka wazi masuala matatu ya msingi kunihusu mie mwandishi wa mwakala hii.

Kwanza, mimi licha ya kuwa na makazi nje ya Tanzania kwa takriban miaka 15 sasa bado no Mtanzania. Utanzania wangu ni haki nilioirithi kutoka kwa wazazi wangu, na itabaki hivyo milele. Naeleza hili kwa sababu kuwa wabaguzi wanaopenda kutuhukumu Watanzania tunaoishi huku ughaibuni, na kutaka tuonekane kama Utanzania wetu sio kamili. Kwa mantiki hiyo, kama Mtanzania, nina kila haki ya kutoa maoni yangu kuhusu mustakabali wa taifa letu, hususan katika nyakati hizi ambapo kuna dalili za wanaotaka kulipeleka kubaya taifa letu.

Pili, mwaka 2015 nilishiriki kikamilifu katika kampeni zilizomwingiza madarakani Rais John Magufuli. Kwa upande mmoja nililazimika kumkampenia Magufuli kwa vile nilikuwa nina "sababu binafsi" dhidi ya aliyekuwa mpinzani wake mkuu, mgombea urais wa tiketi ya UKAWA, Edward Lowassa. Wanasema "adui ya adui yako ni rafiki yako."Kwa upande mwingine, nililipwa kutoa huduma ya ushauri wa kitaalamu (usadi, yaani consultancy kwa kimombo) hususan kwenye mitandao ya kijamii. Natanabaisha hili ili asije akakurupuka mtu na kusema "ah ulishiriki kutupigia kampeni kwa vile tulikupa pesa."

Tatu, huko nyuma nilikuwa mtumishi wa Idara ya Usalama wa Taifa. Na kabla ya kuanza utumishi katika taaluma hiyo muhimu na nyeti, nilikula kiapo kwa nchi yangu, kiapo ambacho nitaishi nacho hadi ninaingia kaburini. Kiapo hicho sio cha kukitumikia chama flani au viongozi wake bali Tanzania yetu. Nchi ni muhimu  kuliko vyama vya siasa au wanasiasa.

Mtu aliyepikwa na kuiva kwenye taaluma ya uafisa usalama wa taifa, katika nchi yoyote ile, anapaswa kubaki kuwa mtiifu kwa nchi yake bila kujali yupo ndani au nje ya ajira ya taasisi inayohusika na usalama wa taifa wa nchi husika.

Wanasema hata nje ya ajira rasmi, kila mtu aliyewahi kuwa afisa usalama wa taifa anaendeshwa na "sense of public duty born in their previous lives" yaani wajibu kwa umma uliozaliwa katika maisha yao huko nyuma. Jasusi mmoja mstaafu anaeleza “...I have obligations, professional obligations. If there’s a national security emergency or possible national security issue, I should report it."


Kwahiyo, hata kama "maafisa wenzangu wa zamani" wataamua kukaa kimya kwa sababu moja au nyingine – wengi wanahofia usalama wa maisha yao – sie wengine hatuwezi kukaa kimya, hasa kwa vile baadhi yetu tumeshalipa gharama kubwa kwa kelele zetu. Kukaa kimya ni sawa na kuafiki uhuni unaoendelea ambao ni tishio kwa usalama wa taifa.

Lakini licha ya wajibu huo unaotokana na utumishi wetu kwa nchi huko nyuma, Rais Magufuli amefanikiwa kuvifunga mdomo vyombo vya habari kiasi kwamba haviwezi kusema lolote kuhusu "mabaya" yake, na amefanikiwa kuvijengea nidhamu ya uoga vyombo hivyo vya habari kiasi kwamba habari pekee zenye umuhimu kwao ni za kumtukuza na kumpamba "mungu-mtu" huyo. Kwahiyo na sie tuliopikwa na kuiva kuhusu ujasiri, kujitoa mhanga na kutokuwa waoga tukiufyata na kukaa kimya - ilhali media zetu ndio zishapigwa kufuli - hali itazidi kuwa mbaya.


Baada ya kuweka wazi nafasi yangu, sasa tuangalie kwa kina kinachoendelea huko nyumbani hasa kuhusiana na uchaguzi mdogo kwenye jimbo la Kinondoni na Siha na kuuawa kwa Daudi na Acquiline.

Ni muhimu kutambua kwamba ukandamizaji dhidi ya vyama vya upinzani sio kitu kilichoanza chini ya utawala wa Magufuli bali hali hiyo imedumu mfululzo tangu kuanzishwa kwa mfumo wa siasa za vyama vingi mwaka 1992. Labda kilicho tofauti kwa zama hizi ni "ujasiri" wa Magufuli kutoficha chuki yake dhidi ya vyama vya upinzani. Yaani angalau akina Mwinyi,Mkapa na Kikwete walikuwa "wanauma na kupuliza." Kwamba angalau walikuwa na "mshipa wa aibu" na walijitahidi japo kutowaonea Wapinzani waziwazi.

Kwa wanaojua "yanayojiri nyuma ya pazia" watakwambia kuwa hujuma dhidi ya vyama vya upinzani ni miongoni mwa vipaumbele vikubwa kwa CCM na serikali zake, na hiyo imepelekea kujengeka "symbiotic relationship" kati ya chama hicho tawala na taasisi za dola, ambapo kila mmoja anategemea uhai wa mwenzie.

Lakini kama kuna kitu kinachokera zaidi kuhusu hujuma dhidi ya demokrasia ni pale CCM na taasisi zake hasa za dola wanapoweka mbele maslahi yao mbele ya utu na uhai wa Watanzania. Na hili halijaanza jana au katika kampeni za chaguzi ndogo katika majimbo ya Kinondoni na Siha.

Uchaguzi mkuu wa kwanza wa vyama vingi mwaka 1995 ulihusisha matukio mengi tu ambayo kwa makusudi hayapo kwenye kumbukumbu za wazi (japo yamehifadhiwa mahala flani).

Lakini kama wanavyosema "amekula asali sasa anachonga mzinga," baada ya hujuma za kimyakimya za mwaka 1995 kuzaa matunda, CCM na taasisi zake ikanogewa, na matokeo yake ni kwamba uchaguzi mkuu uliofuata, mwaka 2000 uliweka doa kubwa kwa historia ya Tanzania yetu ambapo kwa mara ya kwanza nchi yetu ilizalisha wakimbizi kufuatia unyama uliofanyika huko Zanzibar na kupelekea vifo kadhaa (idadi halisi ya vifo haijawahi kuwekwa hadharani japo "wenyewe" walisema zaidi ya watu 19 ndio waliokufa kwenye machafuko hayo. Wasichosema pia ni idadi ya watu waliobakwa, kuteswa na kuwekwa kizuizini.

Kwamba hujuma hizo za CCM dhidi ya demokrasia zilipelekea vifo na majeruhi ni kitu kibaya kabisa. Lakini kitu kingine kibaya ni ukweli kwamba hakuna mtu hata mmoja aliyechukuliwa hata kutokana na unyAma waliofanyiwa Wazanzibari hao.

Kwa namna ya kipekee, CCM ikawa kama imepewa ruhusa ya kutumia vyombo vyake vya dola kufanya lolote itakalo ili ifanikishe hujuma zake dhidi ya Wapinzani na demokrasia kwa ujumla, kisha iibuke na ushindi.

Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 ulikuwa na "uchafu kupindukia." Kundi lililofahamika kama "mtandao" lilijipenyeza katika kila sekta, kuanzia kwenye vyombo vya habari, taasisi za dola hadi kwenye taasisi za dini. Yayumkinika kabisa kuhitimisha kwamba yaliyojiri wakati "mtandao unafanya jitihada za kumwingiza mtu wao Ikulu" ni mabaya zaidi ya haya tunayoshuhudia sasa tangu Magufuli aingie madarakani.

Kwanini basi hayo yaliyojiri kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 hayajulikani? Jibu ni kwamba, wakati mbinu iliyotumika mwaka 1995 na 2000 ilitegemea zaidi vyombo vya dola, uchaguzi wa mwaka 2005 na 2010 ulitegemea zaidi nguvu ya fedha, nyingi zikiwa fedha haramu. Na sehemu ya fedha hiyo ilitumika "kununua ukimya" wa wanahabari wengi tu. 

Lakini si fedha tu bali pia kuna hujuma mbalimbali – nyingine chafu na za kuchefua – zilizotawala safari za ushindi wa chama tawala kwenye chaguzi hizo.


Image result for lowassa kikwete 2005

Labda tofauti nyingine kuhusu mwaka 2005 na 2010 ni ukweli kwamba wakati chaguzi hizo zilihusisha "kikundi binafsi" yaani hicho cha wanamtandao ambacho hakikuwa taasisi ya serikali au chama.

Lakini muda wote huo, CCM ilikuwa kama imepwa ruhusa na Watanzania kuendeleza hujuma zake dhidi ya Wapinzani na demokrasia kwa ujumla. Hakujawahi na utashi miongoni mwa Watanzania kutaka kukabiliana kwa dhati za uhuni/uhalifu wa kisiasa. Na kwa bahati mbaya, kwa vile vipaumbele vya Watanzania wengi ni kwenye "ubuyu" na "kubeti/mkeka" basi habari mbaya ni uwezekano wa CCM kuendelea kufanya itakavyo kwa muda mrefu sana.

Sio kama kwa kubashiri kuwa unyanyasaji wa CCM utaendelea muda mrefu sana ninamaanisha kuwa nimekata tamaa. Hapana. Ninakuwa mkweli tu. Tatizo ni zaidi ya CCM na uhuni wake. Watanzania wenyewe ni sehemu ya mfumo unaowezesha CCM kufanya uhuni/uhalifu huo.

Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 ulihusisha pia matuki kadhaa yaliyojiri "nyuma ya pazia." Na ukitaka kufahamu kuwa Tanzania yetu haijawahi kuhangaishwa na mauaji ya kisiasa – kuanzia yale ya mwaka 2001 huko Zanzibar hadi haya ya Daudi wa Hananasifu na dada Acquilina – ni kifo cha Mchungaji Christopher Mtikila.


Kwahiyo, na ninaandika haya kwa uchungu mkubwa uliochanganyika na hasira, kuuawa kwa Daudi na Acquilina kutaishia kuwa moja tu ya matuko yaliyowahi kutokea katika Tanzania yetu. Tutawasikia wanasiasa wetu wa vyama vya upinzani wakiongea kwa hisia kubwa. Tutashuhudia pia wanafiki wengi tu miongoni mwa wasanii wetu nao wakijifanya kuguswa na vifo hivyo, lakini wakiwa makini kuepuka kumuudhi "Bashite na baba yake" au kuitibua CCM. Tutashuhudia pia kundi la wanafiki hatari ndani ya CCM wakijifanya kuumizwa na mauaji hayo, na kutaka uchunguzi ufanyike, ilhali nao ni kondoo waliojivika ngozi ya mbwa mwitu.



Kama ambavyo "mauaji mengine ya kisiasa" yalivyoruhusiwa kupita kimyakimya, ndivyo unyama huu uliofanywa dhidi ya Daudi na Acquilina utakavyoruhusiwa uishe kimyakimya.

Kwa upande mmoja tusitarajie Rais Magufuli awajibike – sio kwa yeye binafsi kujiuzulu kwa sababu hilo litakuwa kutarajia zaidi ya muujiza – kwa kumtimua Waziri husika na watendaji katika jeshi la polisi. Kwa upande mwingine, hakuna wa kumshinikiza Rais Magufuli achukue hatua stahili dhidi ya wahusika.

Na nisingependa kuuma maneno hapa. Yeye Magufuli mwenyewe ni chanzo muhimu cha siasa hizi za uhasama zinazoendelea kuitafuna Tanzania yetu. Huyu ni mtu ambaye wala hapati shida kuonyesha chuki zake za waziwazi dhidi ya Wapinzani, Upinzani na demokrasia kwa ujumla.


Kama ilivyo kwa madikteta wengine duniani, Magufuli amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kutumia ajenda yake ya ufisadi kama kisingizio cha kusigina haki za binadamu nchini Tanzania, na kubinya kila fursa ya haki za kidemokrasia na uhuru wa habari. Kama nilivyoeleza awali, amefanikiwa kuviziba midomo vyombo vya habari na ndio maana hata habari za kusikitisha kuhusu mauaji ya Daudi na Acquiline hazijaripotiwa vya kutosha.

Kwa kuviziba midomo vyombo vya habari Magufuli amefanikiwa kuzuwia "habari asizozipenda" na ndio maana hadi muda huu ni Watanzania wachache tu wanaofahamu kilichojiri huko MKIRU katika kilichoitwa "operesheni dhidi ya ugaidi." Kuna siku yaliyojiri huko – na ambayo yamechangia "kupotea" kwa mwandishi wa gazeti la Mwananchi Azory Gwanda – yatajulikana hadharani. Haijalishi itachukua miaka mingapi.


Lakini "yaliyojiri MKIRU" ni uthibitisho mwingine wa hicho nilichoeleza hapo juu kuwa Watanzania wenyewe ndio wanaopaswa kubeba lawama nyingi katika kasumba ya CCM kutojali uhai katika harakati zake za kukandamiza demokrasia. Kwamba kama yaliyojiri MKIRU yameachwa yaishe kienyeji, kwanini tutegemee hali tofauti kwa vifo vya Daudi na Acquiline?

Kama ndugu zetu wa Chadema (na kila mpenda haki) "wamekubali yaishe" kuhusu kifo cha Kamanda Mashaka, "kupotea" kwa kada Ben Saanane (hata zile kampeni za #BringBackBenAlive zimejifia kifo cha asili), na hawasumbuliwi na serikali ya Magufuli kupuuzia jaribio la mauaji dhidi ya Tundu Lissu, kwanini tutarajie jipya katika mauaji yaliyofanywa dhidi ya Daudi na Acquiline?

Yaani Mnadhimu Mkuu wa upinzani anamwagiwa risasi hadharani wakati mkutano wa bunge unaendelea huko Dodoma, na tunaambiwa kuwa tukio hilo lilitokea katika eneo lenye ulinzi mkubwa na lenye CCTV, kwanini basi wanaosumbuliwa na tukio hilo wasitafute njia stahili za japo kuifanya serikali ione aibu na kufanya japo "uchunguzi wa kizushi"?

Kuhusu hujuma "za kawaida" za uchaguzi, kama kila aina ya uhuni uliofanywa na CCM kwenye chaguzi ndogo za madiwani katika kata 43 uliofanyika Novemba mwaka jana uliruhusiwa upite "kimya kimya" – kwa maana kwamba hakuna hatua zozote zilizochukuliwa dhidi ya uhuni huo – kwanini basi chaguzi hizi ndogo katika jimbo la Siha na Kinondoni zilitarajiwa kuwa tofauti?

Na katika hili, inapaswa wana-Chadema wajiulize kuhusu busara za viongozi wao kuamua kushiriki katika chaguzi hizo ndogo Siha na Kinondoni ilhali mazingira yaliyokuwepo yalikuwa yaleyale yaliyopelekea chama hicho kususia chaguzi nyingine ndogo tatu katika majimbo ya Longido, Singida Kaskazini na Songea Mjini uliofanyika mwezi uliopita.

Hadi wakati ninaandika makala hii, tayari Tume ya Uachaguzi ilikuwa imeshamtangaza mgombea wa CCM jimbo la Siha, Godwin Mollel kuwa mshindi kwa tofauti kubwa tu ya kura dhidi ya mgombea wa Chadema. Hata kama CCM wameiba kura, ukubwa wa tofauti kati ya kura za mgombea wao na huyo wa Chadema zinaashiria kuwa chama hicho kikuu cha upinzani kilipitisha mgombea fyongo.


Na kama ilivyotarajiwa mgombea wa CCM jimbo la Kinondoni, Maulid Mtulia, naye ametangazwa mshindi.


Mie mtumishi wako nilishabashiri mapema tu kuwa chama hicho tawala kingeshinda majimbo hayo, "iwe isiwe."

Ushindi kwa wagombea hao wa CCM ulipaswa kupatikana kwa gharama yoyote kwa sababu laiti wangeshindwa, kinachoelezwa kama "mkakati wa Magufuli kuua upinzani kwa kununua wabunge na madiwani wa Upinzani"  kingemfanya achekwe hata huko kwenye chama chake.

Na kwa vile hadi sasa wabunge na madiwani waliohama upinzani na kujiunga na CCM wamefanikiwa kurudi madarakani baada ya chama hicho tawala kuwapa fursa ya kuwa wagombea wake kwenye chaguzi ndogo, na kuwasaidia kwa hali na mali washinde, tutarajie wabunge na madiwani wengin zaidi kuhama vyama vya upinzani na kujiunga na CCM. Kisa? "Dili hilo linalipa," kwa CCM na kwa wanasiasa hao wanaohama.

Na unadhani mbunge au diwani "mwenye moyo mwepesi" akiona jinsi chama chake "kilivyochukulia poa" yaliyowasibu akina marehemu Mashaka na Daudi, na yaliyowasibu Ben Saanane na Lissu, kwanini iwe ngumu kwake kushawishika kuhama?

Ningetamani sana kuhitimisha makala hii kwa kushauri nini kifanyike lakini itakuwa kupoteza muda wangu na muda wako msomaji. Ni vigumu mno kuwashauri watu waliokubali kwamba mgao wa umeme ni stahili yao kwa zaidi ya miaka kumi sasa, na ambao kila mara umeme unaporudi wanashangilia kana kwamba wamepewa upendeleo flani.

Kama Watanzania wameshindwa kuilazimisha Tanesko iache mgao wa umeme, wataweza kweli kuilazimisha CCM iache hujuma dhidi ya vyama vya upinzani na demokrasia kwa ujumla? Ndio maana bila utu wala aibu, chama hicho tawala kinapata ujasiri wa kukifanyia mzaha kifo cha Acquiline ambapo kwa kudai polisi (haohao waliomuua binti huyo) wachukue hatua dhidi ya Mbowe. Utterly disgusting!


Na kama mauaji mbalimbali ya kisiasa huko nyuma yameachwa yapite na kusahaulika, kwanini tutarajie miujiza kwenye mauaji haya ya sasa dhidi ya wapendwa wetu Daudi na Acquline?

Na ukweli mchungu ni kwamba Magufuli ataendelea kuwapelekesha Watanzania atakavyo ka sababu si watangulizi wake -Mwinyi, Mkapa na Kikwete – wenye jeuri ya kumwambia "Ee bwana ee, huku unakoipeleka nchi siko." Hawawezi kwa sababu nao ni kama "mateka." Madhambi waliyofanya kwenye tawala zao yanawafanya wahofie hatma yao pindi wakimkosoa "mungu-mtu" aliyepo madarakani.

Na wakati wastaafu au watumishi wa zamani wa Idara za Usalama wa Taifa kwenye nchi kama Marekani wamekuwa mstari wa mbele kukemea kila tendo linalotishia usalama wa nchi hiyo – kwa mfano 'ndoa' kati ya Rais Donald Trump na Russia – wastaafu wetu sie hawana jeuri ya kufungua mdomo sio tu kwa vile wanahofia kuathiri posho na marupurupu yao bali kwa vile nao ni mateka wa "madudu" waliyofanya walipokuwa madarakani. Ukiwa mchafu unajinyima uhuru wa kukemea uchafu.


Basi niishie hapa kwa kurejea tena salamu zangu za pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu Daudi na Acquiline. Ni vigumu kuwaambia maneno yanayotosha kuwaliwaza lakini la muhimu ni kuendelea kuzikumbuka roho za marehemu hao, hasa katika kipindi hiki cha Kwaresma ambapo sisi Wakristu tunaadhimisha mateso ya Bwana Yesu Kristo. Pumziko la Milele awape Bwana, na Mwanga wa Milele awaangazie, wapumzike kwa amani. Amen


25 Jan 2012


Rais Kikwete amefungua milango

Rais Kikwete msibani kwa Marehemu Mbunge Regia
Rais Kikwete msibani kwa Marehemu Mbunge Regia
KWA mara ya pili ndani ya takriban kipindi cha wiki moja, Tanzania imepoteza wabunge wawili. Kabla majonzi hayajatuisha kutokana na kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalumu kupitia CHADEMA, Regia Mtema, taifa likapatwa na msiba mwingine wa Mbunge wa Arumeru Mashariki kwa tiketi ya CCM, Jeremiah Sumari.
Kila kifo kinaacha pengo lakini kifo cha kiongozi (awe wa familia kama mzazi au wa jamii) kinaacha pengo linalowagusa na kuwaathiri wengi. Japokuwa yayumkinika kuhisi kuwa katika zama hizi za siasa za kuendekeza maslahi kuna wanaofurahi vifo vya viongozi kwa vile vitatoa nafasi ya wao kugombea, ukweli unabaki kuwa ni vigumu kupata mrithi atakayelingana kwa kila kitu na marehemu (hasa katika utekelezaji wa majukumu).
Kama nilivyoandika katika makala ya wiki iliyopita kuhusu kifo cha Regia, njia bora ya kumuenzi marehemu Sumari ni kudumisha mema yote aliyofanya wakati wa uhai wake. Kwa wanaofikiria kumrithi nafasi yake (na kwa atakayeteuliwa kumrithi nafasi ya Marehemu Regia) changamoto kubwa itakuwa kwenye kuwaenzi viongozi hao kwa kuwajibika ipasavyo. Japo utendaji kazi bora wa kiongozi anayerithi madaraka kutoka kwa kiongozi marehemu hauwezi kurejesha uhai, kwa kiasi fulani unasaidia kupunguza machungu ya wananchi walioathiriwa na pengo lililotokana na kifo husika.
Katika mila na desturi za kiafrika, shughuli ya msiba inatawaliwa na majonzi na kwa kiasi kikubwa ni kumbukumbu kwa kila aliyehai kuwa sote “tulitoka kwenye udongo na tutarejea kwenye udongo.” Misiba inapaswa kutukumbusha kuwa sote ni wasafiri na kila nafsi ya mmoja wetu itaonja mauti.
Moja ya matukio yaliyotawala msiba wa Regia ni habari kwamba Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willbroad Slaa, alikwepa kusalimiana na Rais Jakaya Kikwete. Habari hiyo ilichukua uzito mkubwa kiasi cha kukaribia kufunika tukio la huzuni lililowakutanisha viongozi hao huko Ifakara.
Kwa sababu anazozijua mwenyewe, jamaa mmoja aliamua kusambaza waraka katika blogu kadhaa ndani na nje ya nchi kukemea kitendo hicho cha Dk.  Slaa. Mtu huyo ambaye hakufanya jitihada za kuficha itikadi yake ya siasa, akaenda mbali zaidi na kudai kuwa kilichosababisha Katibu Mkuu huyo wa CHADEMA kutosalimiana na Rais ni amri iliyotolewa na mwenza wa Dk. Slaa (Josephine).
Pengine kwa kuelewa kuwa kukalia kimya jambo hilo kungeibua maneno zaidi, hatimaye Dk. Slaa alieleza kilichomfanya ashindwe kusalimiana na Rais Kikwete. Kwa wanaojua protokali, mtu hakurupuki tu na kwenda kusalimiana na kiongozi mkuu wa nchi hasa ikizingatiwa kuwa kumkaribia kiongozi huyo (hata kama ni kwa nia nzuri) kunawafanya walinzi wake watafsiri kama tishio la usalama kwake.
Kadhalika, Dk. Slaa alieleza bayana kuwa kilichompeleka Ifakara ni kumzika Regia na si vinginevyo. Kwa lugha nyingine, alimaanisha kuwa isingehitaji kutokea kifo cha mbunge au kiongozi wa chama ndipo “mahasimu wawili” (kama ‘wazushi’ wa habari hiyo walivyojaribu kutuaminisha) wakutane na kupeana mikono.
Lakini kama kuwasuta wanaokuza matukio madogo, siku chache baadaye vyombo vya habari vilitawaliwa na picha inayomwonyesha Rais Kikwete na Dk. Slaa wakipeana mikono baada ya mazungumzo kati ya Rais na viongozi wa CHADEMA yaliyofanyika Ikulu ya Magogoni, Dar es Salaam.
Sijui waliozusha kuwa Josephine alimkataza Dk. Slaa wanasemaje kuhusu hilo. Labda watazusha kuwa alimtoroka mwenza wake kama sio kuzusha kuwa kiongozi huyo wa CHADEMA aliamua kuambatana na viongozi wenzie Ikulu ili kujisafisha kutokana na tukio la Ifakara.
Inasikitisha kuona mambo ya msingi yakigubikwa na porojo zisizo na mashiko. Binafsi, moja ya mambo ya msingi yaliyonigusa na kunipa matumaini mapya ni jinsi Rais Kikwete na takriban uongozi wake mzima (serikalini na huko CCM) walivyoweza kuweka kando tofauti za kiitikadi na kumzika Regia kama kiongozi wa Watanzania na si mbunge wa CHADEMA pekee.
Mara kadhaa nimekuwa nikishutumiwa kwa kumkosoa au kumlaumu Rais Kikwete. Lakini siku zote nimejitahidi kusisitiza kuwa lawama hizo na kukosoa hakumaanishi chuki au husuda bali ni kwa minajili ya ustawi wa taifa letu.
Natambua kuna uwezekano wa baadhi ya wasomaji kuhisi nimefikia hatua ya kumpongeza Rais Kikwete kwa vile tukio husika linaihusu CHADEMA (ambayo nimekuwa nikituhumiwa kuipendelea na baadhi ya watu, huku wengine wakidai mimi ni mwanachama wa chama hicho.)
Yeyote aliyesoma salamu za rambirambi zilizotolewa na Rais Kikwete kwenda kwa familia ya marehemu Regia na CHADEMA hatoshindwa kubaini kuwa zilikuwa zimetoka moyoni kwa dhati. Hakukuwa na hata chembe ya tofauti za kiitikadi bali hisia za kibinadamu pindi zinapopatikana habari za kifo.
Naomba nisisitize kuwa tukio hilo sio pekee au la kwanza kwa Rais Kikwete kuonyesha kile wanachokiita Waingereza ‘human side’ (ubinadamu wake, kwa tafsiri isiyo rasmi). Mara nyingi mkuu huyo wa nchi ameonyesha kuguswa kwa dhati kila anapokuwa kwenye matukio ya huzuni.
Japo wakati mwingine huishia kulaumiwa kuwa ‘haisaidii kuonyesha uchungu ilhali janga husika lingeweza kuzuilika’ (kwa mfano kwenye matukio ya milipuko ya mabomu huko Mbagala na Gongo la Mboto), hiyo haindoi ukweli kuwa ameguswa na matukio hayo.
Lakini pamoja na pongezi hizi kwa Kikwete na CCM kwa ujumla pengine ni muhimu kukumbushana kuwa kama tunaweza kushikamana wakati wa misiba kwa nini basi iwe vigumu kufanya hivyo nyakati nyingine?
Kwa lugha nyingine, kwa nini tusubiri hadi kiongozi wa chama cha upinzani afariki ndipo tuonyeshe kuwa tofauti za kiitikadi haziondoi ukweli kuwa sote ni Watanzania tunaoweza kutofautiana kimtizamo au kiitikadi pasipo umuhimu wa ‘kuong’oana’ macho.
Japo Kikwete si mahiri katika kuendekeza siasa za uhasama (aidha kwa vile si muumini wa dhana hiyo au anatumia wasaidizi wake kukwepa lawama zinazoweza kuelekezwa kwake), kiujumla chama anachoongoza, yaani CCM, kimekuwa kikifanya jitihada kubwa kuuaminisha umma kuwa vyama vya upinzani ni mithili ya mikusanyiko ya maharamia wasioitakia mema nchi yetu.
Ukisikiliza hotuba za baadhi ya viongozi wa CCM wanapovizungumzia vyama vya upinzani unaweza kabisa kutamani kwenda Idara ya Uhamiaji kuhoji iwapo viongozi hao wa upinzani ni raia halisi wa nchi hii. Hivi haiwezekani kukosoana pasipo kupandikiza chuki ya uadui miongoni mwetu?
Katika tafiti za kitaaluma, kuna hatua ambapo mtafiti huwezi kubashiri matokeo ya utafiti husika kwa kuzingatia dhana alizotengeneza (hypothesis). Japo makala hii si sehemu ya utafiti lakini ningependa kutengeneza dhana kuu mbili zinazoweza kubashiri matokeo fulani.
Ya kwanza, kwa vile Rais Kikwete na CCM wameweza kututhibitishia kuwa tofauti zao za kiitikadi na CHADEMA si za kiadui, na ndio maana wameshiriki kikamilifu katika msiba wa marehemu Regia, Tanzania inaingia kwenye zama mpya za siasa za upendo na kukosoana kistaarabu.
Ya pili, kwa vile siku chache baada ya msiba wa mbunge wa CHADEMA, Rais Kikwete aliwaalika viongozi wa CHADEMA kufanya majadiliano nao, tunaanza kushuhudia ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya Rais (na pengine CCM kwa ujumla) katika uongozi wa nchi.
Matokeo yanayotarajiwa ni kwamba badala ya muda mwingi wa ujenzi wa taifa letu kutumika kunyoosheana vidole, kuitana majina ya ajabu ajabu na upuuzi mwingine, sasa tunaweza kuona uongozi wa nchi ukifanya kazi bega kwa bega kwa lengo la kuikomboa Tanzania yetu kutoka katika lindi la umasikini (licha ya rasilimali lukuki tulizojaliwa) na kuunganisha nguvu kukabiliana na kundi la maharamia walioigeuza nchi yetu kuwa ‘shamba la bibi’ kwa ufisadi.
Unaweza kudhani labda aya tatu za hapo juu nimeziandika nikiwa ndotoni. La hasha. Kila nililoandika linawezekana kwani sababu (ya kushirikiana) ipo, na uwezo wa kufanya hivyo upo (kama ilivyothibitika katika tukio hilo la msiba wa marehemu Regia), ila kinachokosekana ni nia tu.
Ni matarajio ya safu hii kuwa Rais Kikwete (ambaye naamini anasoma makala hizi au anasimuliwa na wasaidizi wake) hatorudi nyuma katika kufungua sura mpya ya siasa za maelewano na ushirikiano kwa manufaa na ustawi wa Tanzania yetu. Penye nia pana njia.


2 Apr 2010

Jana ilikuwa Siku ya Wajinga Duniani.Binafsi niliiadhimisha kwa matendo mawili.Kwanza niliweka 'breaking news ya kizushi' kuwa Baba Mtakatifu Benedikti wa 16 ametangaza kujiuzulu kufuatia skandali ya ngono na ulawiti inayolikabili Kanisa Katoliki.Pili,kwenye ukurasa wangu wa Facebook niweka tahadhari kuwa 'pranks' kama kuwapigia simu polisi na kudai wewe ni gaidi wa kujilipua bomu la kujitoa mhanga (suicide bomber)zinaweza kumwingiza mtu matatani hata kama zilikuwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Wajinga.Vitendo au kauli za utani katika Siku ya Wajinga zina mipaka yake. Nimekutana na habari katika gazeti la Mwananchi kuwa Kamati ya Bunge ya Miundombinu imetoa ushauri wa kununuliwa ndege nyingine ya rais kwa madai kuwa zilizopo zimechoka.Naamini kuwa kauli hiyo ilikuwa sio serious bali ni sehemu tu ya maadhimisho ya Siku ya Wajinga Duniani.Kama kauli ya Mwenyekiti wa Kamati hiyo,Mohammed Missanga ilikuwa ya dhati basi yayumkinika kusema kwamba baadhi ya wanasiasa wetu wana upeo finyu kupindukia linapokuja suala la vipaumbele vyetu kama taifa.

Of course,rais kama mheshimiwa hawezi kusafiri kwa miguu au kwa punda,japo wengi wa anaowatawala ni masikini wa kutupwa ambao hawawezi kumudu hata gharama ya mlo wa siku.Lakini pamoja na uheshimiwa huo wa rais,na umuhimu wa yeye kusafiri kwa ndege yake maalum,wazo la kumnunulia ndege mpya ni mufilisi na linalopaswa kukemewa kwa nguvu zote.Kama hoja ni uzamani wa ndege zilizopo basi kuna haja gani ya kupuuzia malalamiko ya wafanyakazi wa serikali wanaotoshia kugoma kwa madai ya mishahara kiduchu?Maana nao pia mishahara yao ni ya zamani kama zilivyo ndege za rais.

Missanga na Kamati yake wanapendekeza pia kununuliwa helikopta zitakazowezesha viongozi kufika maeneo yanayokumbwa na majanga.Hivi la muhimu ni kufika kwa viongozi katika maeneo hayo au first responders (eg zimamoto)?Kwanini kipaumbele kisiwe katika kuboresha vitendea kazi vya first responders badala ya nyenzo za usafiri wa viongozi?Kwahiyo kiongozi akishafika eneo la janga atasaidia kuokoa maisha ya wahanga wa janga husika?Au Missanga na wenzake anajaribu kutueleza kuwa mara nyingi hakuna jambo linalofanyika hadi kiongozi afike mahala husika?Kama ni hivyo,la muhimu si ndege au helikopta mpya bali uongozi na usimamizi mzuri wa nguvu kazi,sambamba na kukomesha tabia ya kusubiri maagizo ya rais au viongozi wengine wakuu katika kuutumikia umma.

Na kichekesho cha mwaka,na kilichonifanya niamini kuwa kauli ya Missanga na wenzie ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Wajinga,ni ukweli kuwa ndege za rais zimetumika kwa asilimia 37 tu hadi kufikia mwezi Machi mwaka huu.Kwa lugha sahihi,ndege hizo zimetumika chini ya nusu ya mahitaji yake.Je hiyo si sababu tosha kuonyesha kuwa ndege hazina umuhimu na ndio maana zinatumika 'kwa bahati mbaya'?

Leo ni Ijumaa Kuu.Kwa Wakristo,hii ni siku ambapo mkombozi wetu Yesu Kristo alitoa maisha yake msalabani kuwakomboa wanadamu.Japo natambua kuwa uongozi wa kisiasa ni tofauti na wa kidini lakini mfano wa Bwana Yesu kutoa maisha yake kwa ajili ya wanadamu unapaswa kuigwa na viongozi wetu kwa maana ya kujitoa mhanga kwa ajili ya wanaowaongoza.Na mhanga ninaozungumzia hapa sio wa kujitoa maisha kama alivyofanya Bwana Yesu bali kuangalia kuwatumikia wananchi kwa uadilifu na ufanisi.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.