Showing posts with label STEPHEN WASSIRA. Show all posts
Showing posts with label STEPHEN WASSIRA. Show all posts

30 May 2013

Magufuli amkana Sitta, asema hana ubia naye urais 2015


Siku chache baada ya Waziri wa Afrika Mashariki Samuel Sitta kumhusisha Dk John Magufuli na kundi la urais la mwaka 2015, Waziri huyo wa Ujenzi, ameibuka na kupinga kauli hiyo, akisisitiza hafikirii kuwania nafasi hiyo.
Waziri Sitta alinukuliwa na gazeti hili juzi akieleza kuwa wakati ukifika, yeye na rafiki zake Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Waziri wa Ujenzi, Dk Magufuli na Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe, watachagua mmoja wao watakayeona anafaa kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa 2015. Alisema hayo juzi kwenye Kongamano la Mawasiliano katika Nyanja za Digitali la wanafunzi wa Idara ya Uhusiano na Masoko, Chuo Kikuu cha St. Augustine (SAUT), Mwanza.
Kabla ya hapo alikuwa amewataja rafiki zake hao wakati wa hafla ya kuchangia Kanisa Katoliki, Josephine Bakita, Parokia ya Igoma, Mwanza, Jumapili iliyopita.
Alisema hatagombea tena ubunge mwaka 2015, baada ya kuwa katika ulingo wa siasa kwa miaka 35 na badala yake ataangalia namna nyingine ya kuwatumikia wananchi huku akigusia mchakato wa kuwania urais ambao alieleza anamwachia Mungu.
“Kwa ubunge nimekwishawaeleza inatosha, sitagombea tena kwani miaka 35 inatosha, … lakini hatima yangu ni nini siwezi kujua lakini nina afya nzuri na mmoja wa wanasiasa wakongwe, wenye afya nzuri, mnaona ninavyopendeza... kwa urais namwachia Mungu tutaona,” alisema Sitta.
Kauli ya Magufuli
Akizungumza na gazeti hili nje ya ukumbi wa Bunge jana, Dk Magufuli alisema haelewi msingi wa kauli ya waziri mwenzake huyo, kwani hajui chochote katika mtandao wa urais alioutaja.
Magufuli alisisitiza kusema hana kundi, hakuwahi kuzungumza wala kuhudhuria vikao vya kundi lolote, na kwamba kundi lake ni CCM na Mwenyekiti wake ni Jakaya Kikwete.
“Sina kundi. Sijawahi kuwa na kundi na sitarajii kuwa na kundi lolote. Ninachojua kundi langu ni CCM na kiongozi wake ni mwenyekiti wake, Rais Kikwete,” alisema Dk Magufuli.
Hata hivyo, Dk Magufuli pia alipuuza taarifa kuwa alichangia harambee hiyo akisema, “Si kweli, Mwanza sijatoa hata senti na hata siku ilipofanyika hafla hiyo, nilikuwa Dar es Salaam katika mkutano na makandarasi.” Licha ya kutajwa kuwa miongoni mwa vinara wa urais 2015, Magufuli alieleza kuwa hakuwahi kuzungumza na Sitta suala hilo linalohusu makundi ya urais mwaka 2015.
CHANZO: Mwananchi
WAKATI HAYO YAKITOKEA, JANA PIA ILIKUWA SIKU CHUNGU  KWA SITTA,KAMA INAVYOONYESHA HABARI HII HAPA CHINI
Wassira amvaa Sitta
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Mahusiano na Uratibu, Stephen Wassira, amemtaka waziri wa ushirikiano wa Afrika Mashariki Samwel Sitta, aweke wazi njia anazotumia kupambana na ufisadi nchini ambazo mawaziri wengine wa serikali ya CCM hawawezi kuzitumia.

Wakati Wassira akitaka ufafanuzi huo, Waziri wa Katiba na Sheria Mathias Chikawe kwa upande wake alikataa kuzungumzia mbinu anazotumia Samwel Sitta kwa kile alichoeleza kuwa hawezi kuongelea masuala ya serikali na mtu asiyemjua.

Wassira na Chikawe walitoa kauli hiyo jana wakati gazeti hili lilipotaka maoni yao juu ya kauli ya Sitta iliyonukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari akisema kuwa katika serikali nzima ni mawaziri wanne waliojipambanua kupambana na ufasadi na kutetea wanyonge.

Wassira alisema kwa sasa hawezi kuchangia jambo lolote juu ya kauli hiyo ya Sitta kwa kuwa hajaliona katika vyombo vya habari au kumsikia waziri huyo akisema hadharani.

Alisema kama kauli hiyo imetolewa na Sitta ni vema angefafanua mbinu anazotumia ili wengine waige.
“Mimi siwezi kuzungumzia hayo; mmeyasema nyie pia ingekuwa ni vema kama angeulizwa Sitta mwenyewe na atueleze mbinu zake tuone na wengine wanafanya nini,” alisema Wassira.

Alipoulizwa kama majina yaliyotajwa ni miongoni mwa makundi yanayodaiwa kujipanga ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), kwa ajili ya urais wa 2015; Wassira alisisitiza jambo hilo aulizwe Sitta.

Kwa upande wake Waziri wa Katiba na Sheria Mathias Chikawe, alipopigiwa simu kwa ajili ya ufafanuzi wa kauli hiyo, alikataa kuzungumzia jambo lolote kwa madai kuwa alishajeruhiwa kwa kutoa habari kwa njia ya simu.

“Sitaki na sizungumzi mambo ya serikali na mtu nisiyemjua tena katika simu…siku moja alinipigia mtu akasema anatoka Daily News nilipompa habari akaandika anavyojua na ikaniletea matatizo, kwanza kwa sasa niko Arusha,” alisema Chikawe na kukata simu.

Juzi wakati Waziri Sitta, akishiriki harambee ya kuchangia ujenzi wa Kanisa la Mtakatifu Joseph katika Parokia ya Igoma jijini Mwanza, aliwataka Watanzania kujihadhari na watu wasio waadilifu katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwaka 2015.

Alisema watuhumiwa wa kashfa ya ufisadi wa kampuni ya kufua umeme ya Richmond na Dowans ni hatari na hawastahili kuungwa mkono katika uongozi.

Alisema kutokana na hali hiyo ya ufisadi yeye pamoja na mawaziri wengine watatu wako pamoja katika fikra za kupambana na vitendo vya kifisadi, uonevu na mikataba tata.

Aliwataja mawaziri hao kuwa ni Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe, pamoja na Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli.


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.