Showing posts with label TABORA BOYS. Show all posts
Showing posts with label TABORA BOYS. Show all posts

19 Jul 2012


Wanafunzi wa Sekondari ya Wavulana Tabora wakiwa katika mafunzo ya kivita katika mapori ya Uchama,wilayani Nzega.Picha kwa hisani ya Tabora School Facebook Group

Naikumbuka Tabora Boys,Najivunia Uzalendo Wangu
NIANZE makala hii kwa kurejea barua-pepe niliyotumiwa na mmoja wa wasomaji wa gazeti hili. Msomaji huyo ambaye kwa bahati mbaya au makusudi hakuambatanisha jina lake alieleza kuwa aliguswa sana na makala yangu katika toleo lililopita iliyobeba kichwa cha habari “Ni Vigumu Kuiamini Serikali kwa Dkt Ulimboka.”
Na kuguswa kwa msomaji huyo ni kwa namna mbili; kwa upande mmoja alidai amevutiwa sana na changamoto niliyoitoa kwa Idara ya Usalama wa Taifa, ambayo kwa maelezo yake, anaiona kama taasisi pekee anayoitumainia kuiokoa Tanzania yetu inayoelekea kusikoeleweka.
Lakini kwa upande mwingine, msomaji huyo alionyesha wasiwasi wake kuhusu anachokiona kama uwezekano wa walioudhiwa na makala hiyo (na nyinginezo zinazowazungumzia) kutafuta namna ya kuninyamazisha.
Msomaji huyo aliniusia kuwa japo anatambua kuwa pengine ninachoandika kuhusu yasiyopendeza huko nyumbani kinatokana na uchungu tu kwa taifa langu lakini akanikumbusha yaliyowahi kutokea huko nyuma kwa wengi waliojaribu kukemea maovu katika jamii yetu.
Akanikumbusha kuhusu kiongozi aliyemuita ‘mtoto wa kweli wa Tanzania’ yaani aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Sokoine, ambaye kwa mujibu wa msomaji huyo, anaamini alifupishiwa maisha kutokana na kuingilia maslahi ya mafisadi wa zama hizo.
Kadhalika, aligusia kilichomkumba mmoja wa waandishi bora kabisa wa habari za uchunguzi Marehemu Stan Katabalo. Akadai, kilichompeleka kuzimu mwandishi huyo hakina tofauti na shambulio la kinyama la kumwagiwa tindikali mwandishi mwingine, Said Kubenea.
Pia akaniusia kuwa (namnukuu) “Kama kosa la Dk. (Steven) Ulimboka lilikuwa kutimiza tu wajibu wake kama kiongozi wa jumuiya ya madaktari na matokeo yake ametishia kutekwa na kuteswa, vipi wewe unayediriki kuikosoa taasisi nyeti kama Idara ya Usalama wa Taifa?”
Katika kuhitimisha, msomaji huyo aliniusia kwamba kwa maneno haya (namnukuu), “Kwa vile wewe upo huko Ulaya ambapo shida zake si kama huku kwetu, basi mie ninakushauri usijitafutie matatizo. Hii nchi yetu mtuachie sie wenyewe tuliokwishazoea mgawo wa umeme usioisha licha ya ahadi za kila kukicha, rasilimali zetu kutoroshwa kana kwamba tumezichoka, na mabilioni yetu kuletwa huko Ulaya kwenu kwenye akaunti za mafisadi huku wakituacha tunataabika na uchumi unaozidi kudidimia.”
Kwa hakika nimeguswa mno na barua-pepe hiyo ya msomaji huyu. Japo hakutaja jina lake lakini ninamshukuru kwa yote aliyoandika. Na kikubwa zaidi, angalau anatambua kwa nini 'ninajiingiza matatizoni' kwa kuzungumzia yale ambayo katika mazingira ya kawaida hayapaswi kuzungumzwa.
Ni kweli, nina uchungu na nchi yangu, na kama hilo ni ‘kosa’ litakaloweza kunigharimu huko mbeleni, basi na iwe hivyo. Naomba niweke rekodi vizuri: ninaposema nina uchungu kwa nchi yangu simaanishi kuwa mie ndiye mwenye uchungu (au mapenzi zaidi) kwa nchi yangu zaidi ya watu wengine. Hapana. Ninaamini huo ni wajibu wa asili wa kila Mtanzania mzalendo.
Lakini pengine ni vema nikieleza kwa nini ninaguswa sana na mwenendo wa mambo huko nyumbani, ukiachilia mbali Utanzania wangu. Pengine ni baadhi ya mazingira niliyopitia hadi kufika hapa nilipo. Kwa mfano, mwaka 1990 nilichaguliwa kujiunga na Shule ya Sekondari ya Wavulana ya Tabora (Tabora Boys High School). Shule hii yenye historia ya kipekee kwa nchi yetu imetoa mchango mkubwa sana wa ‘kuzalisha’ viongozi wa nchi yetu.
Wakati ninajiunga na shule hiyo ilikuwa na mchepuo wa kijeshi. Kama kuna faida kubwa niliyoipata kwa kuwa mwanafunzi hapo ni hiyo ‘bahati’ ya kuwa ‘nusu-mwanafunzi, nusu-mwanajeshi.’
Bahati nyingine niliyoipata nikiwa mwanafunzi shuleni hapo ni kuchaguliwa kuwa kiranja mkuu. Kwa vile shule ilikuwa ni ya mchepuo wa kijeshi, wadhifa wa kiranja mkuu ulikuwa ukijulikana kama Kamanda Mkuu wa Wanafunzi (kwa kimombo Students’ Chief Commander). Hadi leo, baadhi ya wanafunzi niliokuwa ninasoma nao wanaendelea kuniita ‘Chief.’
Kufupisha maelezo, mchepuo huo wa kijeshi sio tu ulitupatia wanafunzi ukakamavu na nidhamu ya hali ya juu bali pia ulitujaza uzalendo kwa nchi yetu kwa kiwango kikubwa. Huku tukiwa na sare zetu za ‘kijeshi’ (zilikuwa kombati za khaki kama za jeshi la mgambo), maafande wa Jeshi la Wananchi (JWTZ) waliokuwa wakiendesha ‘kitengo cha jeshi’ shuleni hapo walitupatia mwamko wa hali ya juu kuhusu kuitumikia na kuilinda nchi yetu.
Kabla ya kuanza masomo tulipewa kile kilichoitwa “karibu shuleni” iliyojumuisha kwata za kijeshi na hatua nyingine wanazopitia ‘makuruta’ wanapoingia kambini kwa mara ya kwanza. Ilipofika mwisho wa mwaka, wanafunzi wa kidato cha tatu na cha tano tulipelekwa msituni kwa mafunzo ya vita kwa vitendo.
Baada ya kutoka hapo nilijiunga na Jeshi la Kujenga Taifa ambapo kwa wakati huo ilikuwa ni lazima (kwa mujibu wa sheria). Kwa bahati nzuri, muda mfupi tu baada ya kujiunga na JKT nilichaguliwa kuingia kwenye kundi lililotarajiwa kutoa marubani na mainjinia wa ndege za jeshi.
Tukapelekwa kambi ya JWTZ Kunduchi (RTS). Tulipofika hapo, tukapewa jina la ‘wazalendo,’ yaani watu tuliojitolea kwa ajili ya nchi yetu. Well, sikufanikiwa kuwa rubani au injinia lakini ‘tuzo’ hiyo ya kuitwa mzalendo ilikuwa shani kubwa kwa kila mmoja wetu.
Miaka machache baadaye nilijiunga na taasisi moja ambayo sio tu ili kujiunga ilipaswa kuwa na uzalendo wa hali ya juu lakini pia ilinijaza ‘dozi zaidi’ za kuipenda na kuitumikia nchi yangu kwa nguvu zote.
Kama ilivyo kwa taaluma kama ualimu ambapo pindi ukiwa mwalimu unabaki kuwa na maadili ya kiualimu hadi uzeeni, mafunzo na uzoefu wa kazi niliopata kutoka katika taasisi hiyo unanifanya niendelee kuwa na wajibu ule ule: kutimukia nchi yangu kwa nguvu zote.
Sipendi kuandika makala inayonizungumzia mie, kwani lengo la safu hii ni kuzungumzia masuala muhimu yanayohusu nchi yetu. Lakini Nimelazimika kuandika haya ili kuondoa dhana potofu kuwa labda nina chuki na taasisi fulani au ‘kwa mujibu wa wahusika’ ninafanya uchochezi.
Kuna suala moja la msingi ambalo walafi wanaotafuna rasilimali zetu na mafisadi kwa ujumla wanajitahidi kulipuuza. Tanzania ni yetu sote, na kwa namna moja au nyingine sote ni kitu kimoja. Sasa fisadi anapokwapua fedha zilizopaswa kuleta maendeleo kwa nchi yetu anapaswa kutambua kuwa katika mlolongo wa wahanga wa ufisadi huo ni mtu au watu wanaohusiana naye.
Ni muhimu tufike mahala turuhusu maoni yanayokinzana na matendo au mtizamo wetu. Mara kadhaa tumeshuhudia wazalendo wanaojaribu kuwakumbusha watawala wetu wajibu wao wakiishia kuitwa majina mabaya na wengine kuhujumiwa. Mifano ni mingi lakini si vibaya kupigia mstari kauli za mtu kama Mzee Hans Kitine, Mkurugenzi wa zamani wa Idara ya Usalama wa Taifa, ambaye mara kadhaa amekuwa mstari wa mbele kujaribu kushauri kuhusu mwenendo wa CCM, serikali na taifa kwa ujumla. Lakini kila anayefuatilia vema matukio ya huko nyumbani, mzee huyo aliyelitumikia taifa kwa uadilifu (akiwa Mkurugenzi wa TISS, kabla ya kuingia kwenye siasa) ni mmoja wa wahanga wa fitna dhidi yake. Kosa lake kubwa ni kukemea maovu na kushauri njia mwafaka za kulinusuru taifa letu.
Sawa, kama alivyoandika msomaji aliyenitumia barua-pepe, sisi wengine tupo mbali na nyumbani, na ni kweli kuwa hatuguswi moja kwa moja na adha mbalimbali zinazoendelea huko. Lakini, uwepo wetu huku nje sio tu hautupunguzii Utanzania wetu bali pia ifahamike kuwa baadhi yetu tuna ndugu, jamaa na marafiki ambao ni wahanga wa kila siku wa mwenendo mbovu wa mambo huko nyumbani. Haihitaji busara kumaizi kuwa huwezi kuwa na raha ughaibuni huku watu wako wa karibu huko nyumbani ‘wanapigika.’
Kwa wanaodhani kuwa dawa na kudhibiti ‘kelele kama zetu’ ni ‘kutushughulikia sisi wapiga kelele’ ni vema wakatambua kuwa huwezi kuua wazo sahihi. Kama ambavyo vifo vya akina Katabalo havijazuia uzalendo wa kuwasemea walalahoi wasio na wasemaji (rejea timua-timua huko bungeni kwa baadhi ya wabunge wanaowasilisha vilio vya wapiga kura wao) ndivyo ambavyo baadhi yetu tutaendelea kukemea maovu yanayotishia kuipeleka Tanzania yetu kwenye korongo lenye kina kirefu.
Nimalizie makala hii kwa fundisho hili la historia: japo wabaguzi wa rangi walimuua Martin Luther King, Jr (mpigania haki za Weusi huko Marekani) lakini leo taifa hilo lina Rais Mweusi (Barack Obama). Na japo makaburu waliweza kumfunga Nelson Mandela kwa miaka kadhaa, leo hii Afrika Kusini ipo chini ya utawala wa weusi walio wengi.
Kutekwa na mateso kama vilivyomkumba Dk. Ulimboka, na matukio ya kihuni kwa watu kama Kubenea, na ‘sumu’ inayomwagwa kwa wazalendo kama Mzee Kitine, kamwe haviwezi kutuzui sisi wenye uchungu na nchi yetu kuendelea kukemea maovu na kudai kile Waingereza wanaita ‘value for money’ yaani ubora unaotokana na fedha (ya mlipakodi wa Tanzania).
Na kwa msomaji aliyenisihi niwe makini, licha ya kumshukuru ningependa kumhakikishia kuwa sijakurupuka katika harakati hizi za kuwasemea walalahoi. Mwanafalsafa wa Kichina wa sanaa ya vita (Art of War) Sun Tzu anaasa; “If you know the enemy and know yourself you need not fear the results of a hundred battles.”
Mungu Ibariki Tanzania (na umwangamizie kila fisadi na yule anayemlinda).

26 Nov 2010


Kwa mara nyingine,shule ya Sekondari ya Wavulana ya Tabora (Tabora Boys')imezalisha kiongozi mwingine baada ya Mheshimiwa Mahadhi Juma Mahadhi (pichani kulia anayehojiwa) kuteuliwa kuwa Naibu Waziri Wizara ya Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa.Mahadhi pia alishinda ubunge wa jimbo la Muyuni kwa tiketi ya CCM huko Zanzibar.

Ushindi wako wa kiti cha ubunge na kuteuliwa kuwa Naibu Waziri ni sifa kubwa kwako na kwa Tabora Boys kwa ujumla,a inadumisha rekodi ya shule hiyo kama kitalu cha kuzalisha viongozi wa baadaye wa taifa.

Hongera sana,Mheshimiwa Naibu Waziri.

2 Mar 2008

MTANZANIA UGHAIBUNI

Sakata la mkataba wa Kampuni ya Richmond linaelekea kuchukua mwelekeo mpya kila kukicha. Ni rahisi kutafsiri kwamba suala hili lisipopatiwa ufumbuzi wa kudumu linaweza kuwa na madhara makubwa kwa nchi na kwa chama tawala, CCM.

Tangu ripoti ya “Tume ya Mwakyembe” ilipowekwa hadharani katika kikao kilichopita cha Bunge la Jamhuri ya Muungano, kumejitokeza kauli kadhaa za utatanishi ambazo japo zinaweza kuwa ni za kawaida tu, tafsiri ya ndani inaashiria matatizo makubwa huko tuendako.

Naomba niwe muwazi zaidi katika makala hii, na ningependa kutamka bayana kwamba sina nia ya kumshushia heshima yeyote nitakayemtaja. Lengo kuu la makala hii ni kuikumbusha kila pande inayoguswa na sakata hilo kutambua kwamba taifa letu ni muhimu zaidi kuliko maslahi ya mtu mmoja.

Naikumbuka sana siku taifa lilipotangaziwa kifo cha Baba wa Taifa.Watanzania wengi walitokwa na machozi sio tu kwa vile hawangemwona tena Mwalimu bali pia ni ile hali ya kutokuwa na uhakika taifa letu lingekuwaje bila Nyerere.Naamini kwamba laiti Mwalimu angekuwepo, baadhi ya upuuzi kama huo wa mkataba wa Richmond wala usingetokea, lakini ndio hivyo tena, hatuko naye duniani.

Wanaoilaumu “Tume ya Mwakyembe” kuwa imewaonea wanasahau kwamba tume hiyo haikuundwa baada ya Mwakyembe na wenzake kutuma maombi ya kuwa kwenye tume hiyo.Inashangaza wanaolalamika sasa kwamba ripoti ya tume hiyo ilikuwa na ajenda za kumalizana kisiasa,ilhali hawakuipinga wakati inaundwa na pale ilipokuwa ikitimiza majukumu yake.Ina maana ajenda hizo za kisiasa zilianza baada ya akina Mwakyembe kuwa wajumbe wa tume au zilikuwapo kabla.Kama zilikuwapo kabla,kwanini basi waliotajwa kuhusika na kuliingiza taifa katika hasara kubwa kwa mkataba huo wa kizembe hawakulalamika?

Na iwapo ajenda hizo zilianza baada baada ya wajumbe hao kuingia kwenye tume,kwanini basi watajwa walikimbilia kujiuzulu (huku wengine wakigoma waziwazi kujiuzulu kwa kuendelea kung’ang’ania madaraka) badala ya kudai haki itendeke?Ni rahisi kuhitimisha kuwa kelele zinazoendelea hivi sasa ni za mfa maji.

Nakumbuka kwenye miaka ya tisini nilipokuwa mwanafunzi wa sekondari ya wavulana ya Tabora (Tabora Boys) tulibahatika kutembelewa na Komandoo Salmin Amour.Nayakumbuka baadhi ya maneno yake ambayo kimsingi yalikuwa na lengo la kutupa changamoto ya mafanikio ya kielimu na hatimaye kufanikiwa maishani (japo sio kila mara kufanikiwa kielimu ni tiketi ya moja kwa moja ya kufanikiwa kimaisha).Alitueleza kwamba madaraka ni mazuri na kutupa mifano ya namna yeye kama rais alivyokuwa na wasaidizi kibao wa kuhakikisha kila kitu kinakwenda vema.

Nilikubaliana na Komando wakati huo,na nakubaliana nae sasa,kwamba madaraka ni mazuri na matamu,na ndio maana tunashuhudia hizi kelele zinazoendelea kutoka kwa waliokumbwa na zahma ya kisiasa baada ya skandali ya mkataba wa kampeni ya Richmond.Hakuna dhambi kwa madaraka kuwa matamu kwani hata njia ya kuyafikia sio nyepesi.Inahitaji jitihada na juhudi za kutosha kufikia hatua ya kuongoza watu wenye akili timamu.Na inatarajiwa kwamba mtu akishapata bahati ya kuwa kiongozi atatambua kwamba wengi,kama sio wote,wa aliokuwa akiwaongoza ni watu wenye akili timamu,uwezo wa kufanya maamuzi na wanaostahili heshima.

Waziri Mkuu aliyepita,Edward Lowassa,ameendelea kuonyesha kwamba japo aliamua kubwaga manyanga kwa hiari yake,alifanya hivyo huku roho ikimuuma.Nasema hivyo kwa sababu kauli zake za hivi karibuni zinaashiria wazi kwamba bado ana kinyongo kikubwa na matokeo ya uchunguzi wa “Tume ya Mwakyembe.”

Lowassa anaamini kwamba atarejea tena kwenye ulingo wa juu wa kisiasa kama Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi ambaye alipokuwa Waziri alilazimika kujiuzulu kutokana na skandali iliyoikumba Wizara yake.Tofauti ya msingi kati ya Mwinyi na Lowassa ni ukweli kwamba wakati Mwinyi alijiuzulu kutokana na tukio lililotokea mbali kabisa na mahala alipokuwa akifanyia kazi (lilitokea Shinyanga wakati ofisi ya Mwinyi ilikuwa Dar es Salaam),Lowassa alijikuta akikumbwa na shutuma kuhusu mkataba huo kwa vile katika hatua flani ulipita machoni mwake na akaamua “kusikiliza maamuzi ya wataalamu.”

Uongozi ni pamoja na kuwa na maamuzi ya haraka na yanayoangalia athari zinazoweza kujitokeza mbeleni iwapo yatafanyika maamuzi potofu.Haiyumkiniki kwamba Waziri Mkuu mzima anaweza kusikiliza ushauri mbovu na kuafikiana nao pasipo kujiridhisha iwapo ushauri huo ni wa manufaa kwa taifa.Hilo pekee linamvua sifa ya uongozi mtu yeyote aliye katika nafasi ya juu kitaifa.

Hivi kama mkataba wa Richmond ungekuwa na madhara ya moja kwa moja kwa familia ya Lowassa,kiongozi huyo angeendelea kusikiliza ushauri asio na uhakika na matokeo yake au angetaka kujiridhisha kwamba kilichokuwa kikifanyika hakingekuwa na madhara kwa familia yake?

Tukimweka kando Lowassa kwa muda,tumeshuhudia vituko vingine kutoka kwa Mkurugenzi wa TIC Emmanuel Ole Naiko ambaye anadai kuna dalili za “mauaji ya halaiki” dhidi ya watu wenye asili ya wilaya ya Monduli.Hizi ni hoja mufilisi ambazo kama zitaachwa bila kudhibitiwa zinaweza kuliingiza taifa kwenye matatizo yasiyo na msingi.


Hivi Ole Naiko amefanya utafiti wa kutosha kiasi gani kuthibitisha kwamba kuna mpango wa “ethnic cleansing” dhidi ya watu wa Monduli?Kwa hakika serikali inapswa kumhoji kwa undani mtu huyu mwenye heshima kubwa ndani na nje ya nchi kutokana na matamshi hayo ambayo yanaweza kabisa kuathiri hata utendaji wa ofisi yake (hakuna mwekezaji aliye tayari kuwekeza kwenye nchi inayoelekea kwenye “ethnic cleansing.”)

Kuna tetesi kwamba upo mkakati mkubwa wa “kujibu mashambulizi” dhidi ya ripoti ya “Tume ya Mwakyembe.” CCM imekuwa ikituaminisha kila siku kwamba vikao nje ya chama ni majungu,sasa basi inapaswa kuhakikisha kwamba wote wenye kudhani hawakutendewa haki wawasilishe malalamiko yao kwa ngazi hsuika katika chama hicho au hata bungeni.

Kama taarifa tunazozisoma katika vyanzo mbalimbali kwamba kuna mgawanyiko mkubwa ndani ya CCM kutokana na skandali la Richmond zina ukweli, basi ni muhimu kwa uongozi wa juu wa chama hicho kuachana na itifaki zake za kawaida za kuwasifia hata wanaostahili kukemewa na badala yake kuwawekwa “kiti moto” waeleze malalamiko yao mbele ya vikao halali badala ya kuendeleza mbinu za chini chini ambazo zinaweza kabisa kuathiri hali ya usalama wa nchi yetu.

Tusirejee makosa yaliyojitokeza katika mkataba wa Richmond ambapo baadhi ya watu walitahadharisha mapema kuhusu uhalali wa kampuni hiyo lakini wakapuuzwa.Kuna watu wanataka urais kwa kutimia njia yoyote ile hata kama kwa kufanya hivyo wanahatarisha uhai wa chama.

Lakini wakati tunawalaumu wanaolalamika kwamba wameonewa na “Tume ya Mwakyembe” tunapaswa pia kujiuliza kama hawapati jeuri hiyo kutokana na uzembe unaendelea wa kutowachukulia hatua wahusika.Pengine jeuri waliyonayo inatokana na ukweli kwamba wanaamini kuwa hakuna mwenye jeuri ya kuwachukulia hatua hasa ikizingatiwa kuwa baadhi yao wameishia kupongezwa kwa “ushujaa wao” badala ya kushutumiwa kwa hasara waliyoisababisha kwa taifa.

Nadhani anachopaswa kufanya Lowassa,Ole Naiko na wengine wote waliohusishwa na mkataba wa Richmond ni kutafuta msaada wa kisheria kuona haki inatendeka upande wao iwapo wanaamini kuwa hawakutendewa haki,badala ya kuendeleza hizi porojo ambazo kwa hakika zinaweza kuua kabisa ndoto zao za kurejea kwenye ulingo wa juu wa siasa za nchi yetu.Mahakama zipo,vikao vya chama vipo,sasa kwanini kelele za kuonewa zisipelekwe huko?TANZANIA NI MUHIMU ZAIDI KULIKO MASLAHI YA MTU BINAFSI.

BAADA YA KUMALIZA KUSOMA MAKALA HII,UNAWEZA KUANGALIA VITUKO VYA SIASA ZA URUSI AMBAVYO VIMEZAA TERM MPYA YA NANO PRESIDENT (as in iPod Nano).BONYEZA HAPA

HALAFU KWA WALE AKINA DADA "WENYE ULIMI MZITO",CLIP IFUATAYO INAWEZA KUWA YA MSAADA WA INA FLANI



Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.