Showing posts with label UANDISHI WA HABARI TANZANIA. Show all posts
Showing posts with label UANDISHI WA HABARI TANZANIA. Show all posts

11 Feb 2012


Uongo una tabia moja kuu: usipokanushwa huweza kujenga hadhi ya kuonekana ukweli.Ni kwa sababu hiyo,mara nyingi siruhusu kitu kisicho na ukweli kiachwe kuishi na hatimaye kionekane ni cha kweli.

Nilipoingia kwenye ukurasa wangu wa Twitter hapo jana nilikumbana na tweets za waungwana wawili, Bwana @semkae na Ndugu @chiume, ambapo pasipo kuingia kiundani kunukuu kila walicho-tweet,waliniona kiojakwa mambo mawili: kwanza, "kuingizwa mkenge" kunukuu tweets za Rais Jakaya Kikwete kwenye makala yangu katika toleo lililopita la jarida la Raia Mwema,na pili,kuandika "nilifanya maongezi yasiyo rasmi na Rais Kikwete."

Nianze na hilo la pili.Tofauti na ilivyokuwa nyakati za Zama za Mawe ambapo njia pekee ya mawasiliano ilikuwa kukutana uso kwa uso,maendeleo ya teknolojia sasa yanawezesha mawasiliano kwa njia mbalimbali kama vile barua-pepe,SMS,mitandao ya jamii,nk.Kwa watu wenye mawazo ya kale,ukisema NIMEONGEA NA FLANI basi kwao lazima iwe aidha maongezi hayo ni ya barua kupitia posta,uso kwa uso au (kidogo) SMS au e-mail.Kwa mtizamo wa watu hao,ukijadiliana na mtu huko Facebook au Twitter basi huna haki ya kusema MMEONGEA.Kwao maongezi ni lazima ufumbue mdomo na maneno yatoke mdomoni kama si maandishi kwenye barua,nk.

Chanzo cha nukuu husika ni swali nililomuuliza Rais kuhusiana na mkanganyiko uliojitokeza kuhusiana na suala la posho za wabunge.Nilijibiwa na mheshimiwa,na kwa vile makala yangu katika toleo lililopita la Raia Mwema ilikuwa inazungumzia suala hilo basi sikuona ubaya wa kunukuu majibu hayo ya Rais Kikwete (pasipo kupunguza au kuongeza neno).Na kwa kuondoa utata,nikaandika "nilifanya MAZUNGUMZO YASIYO RASMI na Rais kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter kwa kumuuliza...."

Sikuandika hivyo kwa minajili ya kutaka sifa kuwa "eeh nimeongea na Rais..." bali kama muumini wa kuthibitisha hoja kwa mifano hai ilikuwa muhimu kuambatanisha nukuu hizo.

Lakini pengine kuwafumbua macho waungwana hawa kuelewa kuwa katika zama tunazoishi hata tweet ya kiongozi inaweza kuchukuliwa kama tamko lake rasmi,angalia taarifa ifuatayo ya Shirika la Utangazaji la Kenya ambalo (kama nilivyofanya mie) walinukuu tweet ya Rais Kikwete

Kama KBC walinukuu tweet ya Kikwete na haikuwa tatizo kwa @semkae na @chiume kwanini basi matumizi yangu ya nukuu ya aina hiyohiyo iwe tatizo?

Twende kwenye hoja ya kwanza kwamba handle ya @jmkikwete sio ya Rais Jakaya Kikwete.Awali ilidaiwa kuwa inatumiwa na timu yake ya mitandao ya kijamii lakini kadri mjadala ulivyoendelea ikadaiwa kuwa hiyo handle ya @jmkikwete ni feki,huku wengine wakiita ni mzimu.

Hoja baada ya hoja.Hivi kweli pamoja na madudu mbalimbali yanayoendelea huko nyumbani,inawezekana kweli mtu mmoja akakurupuka na kujiita Jakaya Kikwete,Rais wa Nne wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania,na asichukuliwe hatua?


Lakini hata tukikutana na hoja kama "ah kama wameshindwa kuwakamata majambazi wa Kagoda wataweza kumkamata huyu anayejifanya Rais Kikwete huko Twitter?" bado kuna hoja nyingine kadhaa zinazoweka nguvu kwenye ukweli kuwa @jmkikwete ni Rais mwenyewe.

Hebu bonyeza LINK HII na utapelekwa kwenye ukurasa wa Social Good Summit iliyofanyika jijini New York Marekani kuanzia tarehe 19 hadi 22 Septemba mwaka jana.Kwenye ukurasa huo,ukishuka hadi profile ya mtoa mada (speaker) wa 31 utakutana na picha na wasifu mfupi wa Rais Kikwete.Chini ya maelezo hayo kuna link ya akaunti yake ya Twitter.Guess what?Ni hiyohiyo @jmkikwete ambayo @semkae na @chiume wanadai ni feki.

Kila mtoa mada ameweka link ya social media profile zake.Sasa kwanini Rais Kikwete atumie profile ya mtu hewa?Halafu habari husika imewekwa kwenye tovuti ya Mashable ambayo kwa anayefuatilia teknolojia na social media atakuwa anaelewa fika hadhi yake mtandaoni.Au nao waliingizwa "choo cha kike" (kunukuu kebehi ya @chiume)?


Ukienda kwenye ukurasa husika  na hatimaye kwenda kwenye wasifu wa Kikwete,ukibonyeza 'kindege cha Twitter' utapelekwa @jmkikwete.Hiyo ina maana gani?Tuwaachie @semkae na @chiume watueleze

Lakini hata kama hiyo si hoja ya msingi,ukienda kwenye ukurasa wa profile @jmkikwete ambayo hadi sasa ina followers 11336 (yani watu wote hawa nao wameingizwa "choo cha kike"?) utakuta watu na taasisi zenye heshima waki/zikimufata @jmkikwete.Kuanzia CCM hadi Chadema,Mbowe hadi  Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu Salva Rweyemamu na Ubalozi wa Uingereza huko nyumbani.Lakini kubwa zaidi ni familia ya Kikwete mwenyewe,yaani mkewe Mama Salma na wanae Ridhiwani na Miraji.Yaani hata familia ya Kikwette nayo inamfuata @jmkikwete 'feki'!!!!?????

Na MAKALA HII kutoka Rwanda inatanabaisha kuwa Rais Kikwete ni miongoni mwa viongozi wachache wa Afrika-pamoja na marais Paul Kagame na Jacob Zuma-ambao wapo Twitter.Je @semkae na @chiume wanaweza kutwambia kama @jmkikwete sio Rais Kikwete then anatumia handle gani?

Talking of Zuma,waungwana hao walidai kuwa kinachowafanya waamini kuwa @jmkikwete si Rais Kikwete ni kwa vile akaunti hiyo haijawa verified.Wanasema hayo ilhali wao wenyewe akaunti zao haziko verified lakini tunaamini tunao-interact nao ni wao halisi.Na kama suala ni verification,mbona hata Rais Zuma naye akaunti yake ya Twitter (@therealjz) sio verified?Au naye ni mzimu?Hoja mfu hazina uhai mrefu kabla ya kurejea tena kaburini.
La mwisho,na ambalo nisngependa kuingia kwa undani ni vyanzo vyangu binafsi.Kila mmoja wetu ana past yake.Kwa sababu za kimaadili,huwa sipendi kuzungumzia past yangu.Ninachoweza kuandika hapa ni kwamba kupitia past hiyo nimeweza kuthibitisha mambo mbalimbali kabla siyaandika kwenye makala zangu.Na licha ya past hiyo,hakuna kitu ninachoepuka kwa nguvu zote kama kupotosha wasomaji wa jarida lenye heshima kubwa huko nyumbani la Raia Mwema.Mara nyingi ninalazimika kuwapigia simu angalau watu wawili hadi watatu kabla sijaandika makala ili kuhakikisha kuwa ninachoandika ni sahihi.Na watu hao ninaowauliza ni vyanzo vya uhakika kabisa.Lakini kwa mtu mbishi anaweza kudai huo pia ni uzushi...au kwa kunukuu nkauli ya Bwana @semkae, ni MISREPRESENTATION tu.

Nakuachia msomaji ufikie hitimisho mwenyewe.

13 Sept 2009



Na Mwandishi Wetu
KUNA kila dalili kwamba Rais Jakaya Kikwete ameamua kuwakana marafiki zake wa karibu baada ya kuueleza umma kuwa, hana urafiki wala udugu katika vita vya kupambana na ufisadi nchini.

Akizungumza na taifa kwa staili mpya ya kuwasiliana moja kwa moja na wananchi Alhamisi wiki hii, Kikwete alionya kuwa katika masuala ya rushwa, hasa ya Richmond na Kagoda, hana udugu wala urafiki.

“Mimi niseme kwamba, katika mapambano ya rushwa hakuna udugu wala urafiki, na suala la kuamua nani ashtakiwe au nani asishtakiwe halipo katika mamlaka yangu, hilo ni la Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP),” alifafanua Rais Kikwete.

“DPP akiridhika kwamba, mtu fulani ana la kujibu mahakamani wanastahiki kumfikisha mahakamani bila ya ushauri kutoka , kwa sababu katika vita hii hakuna rafiki wala ndugu."

Rais Kikwete alikuwa akijibu swali la msikilizaji aliyejitambulisha kwa jina la Joseph Machumu, aliyetaka kujua kwamba kashfa za Richmond na Kagoda zinachelewa kushughulikiwa kutokana na Rais Kikwete kuwa na urafiki na watu wanaotuhumiwa kuhusika.

Kauli hiyo ya Rais Kikwete iliibua maswali miongoni mwa wachunguzi wa mambo ya kisiasa, wakihoji kama ni kweli ameamua kwa dhati kuwatosa marafiki zake wa karibu waliohusishwa na Richmond au ililenga tu kufurahisha wananchi.

Kamati ya Bunge iliyokuwa ikichunguza kashfa ya Richmond ilimhusisha katika kashfa hiyo aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa na Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz na watumishi wengine wa serikali.

Wengine waliotajwa kuhusika katika kashfa hiyo ni aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi, aliyekuwa Waziri wa Afrika Mashariki, Ibrahim Msabaha na watendaji wengine wa serikali, wakiwamo wanaoteuliwa na rais.

Baadhi ya watendaji hao ni Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Edward Hosea, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Johnson Mwanyika, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Athur Mwakapugi na wengineo.

Lowassa, Karamagi na Msabaha walijiuzulu mara tu baada ya kamati hiyo iliyoongozwa na Mbunge wa Kyela, Dk Harrison Mwakyembe kuwasilisha bungeni ripoti yake, Februari mwaka jana.

Miongoni mwa waathirika hao wa kashfa ya Richmond, ni Lowassa na Rostam pakee ambao Rais Kikwete aliwahi kukiri kuwa ni rafiki zake wakati akichukua fomu za kuwania uteuzi wa CCM kugombea urais mwaka 2005 mjini Dodoma.

Kikwete aliwataja maswahiba wake hao baada ya kuulizwa swali kwamba, alikuwa anajiamini nini hadi akateua baraza la mawaziri kabla ya kuteuliwa kugombea, jambo alilolipinga akifafanua kuwa akina Lowassa na Rostam walikuwa wanatajwa kwa kuwa ni marafiki zake na yeye kama mgombea hakuwa anazuiliwa kuwa na marafiki.

Baada ya uteuzi huo kumpitisha yeye na baadaye kunyakua urais, alimteua Lowassa kuwa Waziri Mkuu na Rostam akawa Mweka Hazina wa CCM na wawili hao walishiriki kwa kiwango kikubwa katika kampeni zilizomweka Rais Kikwete madarakani.

Lakini mara kwa mara Rais Kikwete amekuwa akieleza bayana kuwa hana ubia kwenye urais wake, isipokuwa Makamu wake, Dk Ali Mohamed Shein aliyekuwa mgombea wake mwenza.

Vilevile kitendo cha Rais Kikwete kukubali kupokea barua ya kujiuzulu kwa Lowassa kutoka kwenye nafasi hiyo ya juu, na kuondolewa kwa Rostam katika uweka hazina wa CCM kunawafanya baadhi ya watu waamini kuwa kweli Rais Kikwete hakuwa na ubia naye na kukubali maneno yake kuwa, kwenye suala la Richmond na kashfa nyingine za ufisadi hana urafiki wala udugu.

Pamoja na ufafanuzi huo wa Rais Kikwete suala la Richmond limekuwa ni tete tangu kuibuka kwake, huku likiwa limewagawa wabunge katika mapande mawili, moja likiwatetea washirika wa kampuni hiyo na jingine lenye nguvu likitaka watoswe kabisa.

Pia mgongano huo umehamia kwenye vikao vya CCM ambapo pande hizo zimeendelea kukamiana huku lile la watetezi wa Richmond likiwa na nguvu kuliko jingine linalotaka watoswe kwenye chama

Kutokana na mpambano uliopo kwenye suala hilo limekuwa likiibuka kila kukicha na ndio maana wasikilizaji waliamua kutumia nafasi hiyo adimu kumuuliza rais wao.

Akifafanua zaidi kuhusu suala hilo, Rais Kikwete alisema kampuni hiyo iliteuliwa na Tanesco katika mchakato wao. "Mimi nilipoambiwa nilisema kwamba, ni jambo zuri kumpata mwekezaji huyo."

Lakini Rais alikiri kwamba, ripoti za uchunguzi wa Richmond zinaonyesha kulikuwa na uzembe katika mchakato wa kuipata kampuni hiyo ya kufua umeme kwa sababu mchakato ulifanyika bila ya kamati kuthibitisha uwezo wa kampuni.

“Ingefanya utafiti wa kutosha, ikiwa ni pamoja na kutembelea ofisi za kampuni hiyo ili kujua uwezo wao na kurudisha ripoti kwa waziri na baadaye kwa waziri mkuu, lakini hilo halikufanyika. Yangefanyika haya matatizo yote yangeepukika,” alisema.

Alisema ukiachia mawaziri waliowajibika kwa kujiuzulu, maofisa wa chini waliofanya mchakato huo kushughulikiwa kwake hakujaridhisha.

“Tunapenda kuona kwamba, maofisa hawa washughulikiwe na mambo haya bado yanaendelea, katika vikao vijavyo tutapata taarifa nzuri kwa sababu hawa ndio tuliotegemea watuepushe na hasara hii, hivyo walistahili wachukuliwe hatua zinazostahili,” alisisitiza.

CHANZO: Mwananchi

TATIZO LA WENGI WA WAANDISHI WETU WA HABARI NI UVIVU WA KUCHAMBUA HABARI,SAMBAMBA NA KUJIKOMBA/KUJIPENDEKEZA KWA WATAWALA.UCHAMBUZI WENYE MANUFAA UNAPASWA KWENDA BEYOND RHETORICS NA KUNUKUU.UZEMBE WA KUSOMA "KATI YA MISTARI" UNASABABISHA UCHAMBUZI MWINGI KUWA RIPOTI YA KILICHOSEMWA NA FLANI.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.