Showing posts with label UKIMWI. Show all posts
Showing posts with label UKIMWI. Show all posts

6 Mar 2014

 
Wanasayansi wanadai kuwa wamefanikiwa kuwadunga waathirika 12 wa Ukimwi viini vya kinga ambavyo vina uwezo wa kuzuwia virusi vya ugonjwa huo. Watafiti wanadai kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuelekea kwenye matibabu kamili ya Ukimwi, ugonjwa unaomlazimu mwathirika kutumia vidonge vya kupunguza makali kwa muda wote wa uhai wake.

"Hii inaimarisha imani yetu kwamba viini vya aina ya T (T cells) vilivyorekebishwa ni ufunguo muhimu katika kuondoa haja ya mwathirika wa Ukimwi kuhitaji dawa kwa muda wote wa uhai wake..." alieleza Dkt Carl H. June, Profesa wa Richard W. Vague katika tiba za kinga katika Idara Tiba na Matibabu na Dawa za Maabara , Shule ya Madawa ya Penn's Perelman huko Philadelphia nchini Marekani.

Watafiti walitumia teknolojia inayojulikana kama "zinc finger nuclease" (ZFN)- waliyoielezea kama 'mkasi wa kimolekyuli kurekebisha viini vya T katika mfumo wa kinga mwilini ili kuiga kuongezeka kwa CCR-5-delta-32, viini vinayofahamika kwa kuwafanya baadhi ya watu wasipate Ukimwi.

Soma habari kamili HAPA (na usisite kuwasiliana nami iwapo utahitaji tasfiri)

20 Jul 2011



Majaribio yameanza ya kinga inayotokana na mimea kutumika kama kinga dhidi ya virusi vinavyosababisha upungufu wa kinga ya mwili (UKIMWI).Kinga hiyo inatengenezwa kwa kutumia majani ya tumbaku iliyozalishwa maabara,ikitarajiwa kuwa ufanisi wake utapunguza gharama ya dawa za kurefusha maisha ya waathirika wa ugonjwa huo,na kwa muda mrefu kupata tiba ya kudumu ya ugonjwa huo.

Vidonge vilivyotengenzwa kutokana na mimea vinafanyiwa majaribio kwa kundi la wanawake hapa Uingereza,hasa kuangalia ufanisi wake.Watengenezaji wa vidonge hivyo wanategemea vitasaidia kupatikana kwa kinga dhidi ya maambukizo ya virusi vinavyosababisha ukimwi lakini mafanikio makubwa yanatarajiwa kwenye ukweli kwamba molekyuli zinazotarajiwa kuwa na ufanisi ni nafuu zaidi kwa minajili ya gharama.

Majaribio hayo katika miili ya binadamu yameidhinishwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Madawa na Huduma za Afya ya hapa Uingereza,na inafanyika huko Guildford katika taasisi ya utafiti wa afya ya Chuo Kikuu cha Surrey.

"Pharma-Plant" ni mradi ulioanzishwa miaka saba iliyopita ukiwa na lengo la kutumia mimea iliyozalishwa maabara kupunguza gharama ya uzalishaji wa vidonge kwa ajili ya tiba mbalimbali.Wanasayansi wanadhamiria kutengenza madawa yenye ufanisi lakini kwa gharama nafuu,na kuzisaidia nchi masikini duniani.

Habari hii imetafsiriwa kutoka katika gazeti la Guardian.Kwa habari kamili soma HAPA

26 Mar 2011

Habari na picha hii zimetumwa na mdau wa Mbeya yetu,nami naiwasilisha kama ilivyo...with no comment!



Mganga mwingine wa tiba za magonjwa Sugu aliyefahamika kwa jina la Jafar Welino(17) mkazi wa mtaa wa Mianzini Kitongoji cha Mabatini jijini Mbeya ameibuka na kutoa tiba kwa mamia ya wakazi wa jiji la Mbeya na viotongoji vyake.



Umati wa watu ulionekana katika nyumba anayoishi kijana huyo wakisubiri kupatiwa tiba hiyo huku wakiwa na vikombe vyao mikononi. Baadhi ya wananchi waliofika eneo hilo walidai kuwa wamefika hapo kutokana na taarifa za kuwa kijana huyo anatibu magonjwa Sugu bure kama vile ambavyo anatibu Mchungaji mstaafu wa Loliondo Mzee Ambilikile Mwasapila.



Akizungumza kwa niaba ya kijana huyo mama mkubwa wa mganga huyo aliyejitambulisha kwa jina la Edina Sanga alisema kuwa kijana huyo alianza tiba hiyo wiki mbili zilizopita ambapo kabla ya kuanza kutibu alimueleza mama yake huyo kuwa alitokewa na mama yake mzazi a,mbaye kwa sasa ni marehemu akimuelekeza kurithi mikoba yake.



Bi.Sanga alisema kuwa mama yake kijana huyo ambaye kwa sasa ni marehemu alikuwa ni mtu mwenye maruhani ambapo kwa kutumia maruhani hayo alikuwa akitoa tiba kwa wakazi mbalimbali mjini Mbeya.Alisema kijana huyo ambaye wamezaliwa mapacha na dada yake aliyemtambulisha kwa jina la Hadija Welino kwamba yeye anasoma kidato cha Nne katika shule ya sekondari Itende.

Hata hivyo Bi.Sanga alisema kuwa kijana huyo aliitwa katika ofisi ya Ofisa Mtendaji ili kutoa maelezo ya namna ambavyo anaendesha tiba hiyo na kuwa hata hivyo anaendelea kutoa tiba kwa watu kwa kunywa vikombe viwili kwa muda wa siku mbili. Alisema kuwa dawa hiyo aliifuata katika kijiji cha Iyula kilichopo wilayani Mbozi na kuwa mara alipofika alianza kuichemsha na kuwagawia wananchi wanaosumbuliwa na maradhi sugu. Aidha umati wa watu walikuwa wamejipanga katika mistari kusubiri tiba hiyo ambapo


Mwenyekiti wa mtaa wa Mianzini Bi.Elizabethy Mwakabungu aliweka utaratibu wa wananchi kupata tiba ikiwa ni pamoja na kuchangia fedha kidogo kwa ajili ya kununulia kuni za kuchemshia dawa hiyo.Akizungumza na umati wa watu waliokuja kujipatia tiba hiyo Mwenyekiti huyo wa mtaa alisema kuwa kila ambaye atapata kikombe kimoja cha dawa anatakiwa kupata kikombe cha pili siku inayofuata.



‘’Mganga katuagiza kuwa kila anayekunywa kikombe kimoja anatakiwa kunywa kikombe cha pili siku inayofuata…yeyote atakayekunywa hatakiwi kunywa pombe kwa muda wa siku saba,’’alisema Bi. Mwakabungu


Wakipata kikombe

maelekezo ya kufika eneo hilo

Pamoja tunaendeleza kupashana Habari


HABARI NA PICHA: Mbeya Yetu

18 Mar 2011


Mwaka huu mbona mambo!!!Baada ya stori inayokamata chati kwa sasa-ya "Babu" anayedaiwa kuwa na uwezo wa kutibu maradhi kadhaa ikiwa pamoja na ukimwi (na Watanzania wamesahau kabisa habari za akina Adawi na Dowans yake)-sasa ameibuka "Babu" mwingine huko Rombo.

Hebu soma kwanza mkasa huu

Rombo kama Loliondo 
Thursday, 17 March 2011 20:25

Daniel Mjema, Moshi

Ni siku za mwisho? Hili ndilo swali lililoanza kuumiza vichwa vya watu baada ya kijana mmoja kuibuka wilayani Rombo, mkoani Kilimanjaro na kudai ameoteshwa dawa ya ajabu na Bikira Maria inayotibu magonjwa sugu ukiwamo Ukimwi.Kama ilivyo kwa mchungaji mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Ambikile Mwasapile wa Loliondo ambaye amejizolea umaarufu mkubwa ndani na nje ya nchi, kijana huyo naye amekuwa akitoa tiba kwa sh500.

Kwa imani ya waumini wa Kanisa Katoliki Duniani, Bikira Maria ni mama wa Yesu ambaye anaaminiwa na waumini wa Kanisa hilo na hata katika sala jina lake ndilo linalotumika zaidi huku wakiamini kuwa Yesu ni mtoto wa Mungu.Habari za uhakika kutoka eneo la Customs katika mji mdogo wa Tarakea, mpakani mwa Kenya na Tanzania, zilimtaja kijana huyo ambaye sasa anajiita Nabii, kuwa ni Hilary James Kitwai (28), kutoka wilayani Babati.

Akizungumza na Mwananchi kwa njia ya simu kutoka Tarakea, Kitwai alisisitiza kuwa dawa hiyo ameoteshwa na Bikira Maria na Yesu na kwamba inatibu Ukimwi, Saratani, Kisukari, Shinikizo la Damu, Figo, Pumu na maradhi ya maumivu.

"Walinitokea kwenye ndoto wakanionyesha huo mti na waliniambia kwa sasa tuko wawili tu Tanzania, lakini huyo mwenzangu simfahamu. Mimi natoza Sh500 lakini katika hiyo pesa yangu na familia yangu ni Sh300 tu,"alidai.

Kitwai ambaye amekuwa gumzo katika mji wa Tarakea, alisema anakabiliwa na changamoto kubwa katika kuwahudumia wenye mahitaji kwa kuwa hana msaada na kuomba serikali imsaidie kumpatia wahudumu.

Kwa mujibu wa vyanzo vya habari kutoka wilayani Rombo, tayari vyombo vya ulinzi na usalama vimemzuia kwa muda, kijana huyo kutoa tiba inayofanana na ya mchungaji Mwasapile na kuitisha sampuli za mizizi anayoitumia.

Kijana huyo ambaye ni fundi baiskeli kwa miaka mingi katika eneo hilo, aliibuka Jumatatu wiki hii na kuanza kutoa tiba kwa kutumia kikombe na tayari watu takribani 100 kutoka Kenya na Tanzania wamekunywa dawa yake.

"Anadai kuwa ameoteshwa na Bikira Maria na alielekezwa huo mti ambao una utomvu na kuanzia juzi (Jumatatu),watu kama 100 hivi walishakunywa dawa hiyo ambayo wenyeji wanadai mti wake ni sumu,"kilidai chanzo chetu.Ofisa Mtendaji wa Kata ya Tarakea, Motamburu, Kimario, alilithibitishia Mwananchi kuwapo kwa kijana huyo.

Kimario alisema yeye binafsi, Ofisa Afya na Ofisa Usalama wa Taifa, walifika nyumbani kwa kijana huyo juzi na kumfanyia mahojiano."Tulimhoji akasema alitokewa na Bikira Maria na Yesu ambao walimwonyesha mti huo ambao upo katika Mto Tarakea na walimwambia yupo mmoja tayari anayetibu maradhi sugu na kwamba yeye atakuwa wa pili,"alisema mtendaji.

Kwa mujibu wa mtendaji huyo, kijana huyo aliwaeleza kuwa baada ya Babu wa Loliondo na Yeye, bado atatokea mtu wa tatu ambaye naye ataoteshwa dawa za kutibu maradhi hayo na baada ya hapo Yesu mwenyewe atakuja duniani.

"Tulimuuliza kama ameshatoa dawa hiyo kwa watu mbalimbali akasema alianza kutoa Jumapili na watu kama 20 hivi walikunywa na alitupa vipande vya miti viwili vya dawa hiyo na tumevikabidhi kwa uongozi wa juu,"alisema Kimario.

Kwa mujibu wa Kimario aliyekuwa akimkariri kijana huyo, alisema 'nabii' huyo ameamua kutoendelea kutoa tiba hiyo hadi hapo serikali itakaporidhia na kwamba kwa sasa anamuomba Mungu ampe maono zaidi juu ya dawa hiyo.

Wananchi walioongea na Mwananchi baada ya kuzagaa kwa taarifa hizo, wameitahadharisha serikali kuwa makini na watu wanaojiita ni manabii vinginevyo wananchi wanaweza kukumbwa na maafa ya kunywa sumu bila kujua.

Wananchi hao wameitaka Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) kuwajibika kikamilifu kwa kuzuia matumizi ya dawa ambazo hazijathibitishwa kutokuwa na madhara.Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Rombo, Anthony Tesha ambaye pamoja na kukiri kusikia habari hizo lakini alisema anaviachia vyombo husika kufuatilia jambo hilo.

CHANZO: Mwananchi

Ngoja nikalale mie...huenda nami nitaoteshwa tiba ya ufisadi....hahaha!!!

7 Mar 2011


Kwa siku kadhaa sasa kumekuwa na taarifa kuwa Mchungaji mmoja mstaafu huko Monduli,mkoani Arusha anatoa tiba ya Ukimwi kwa gharama nafuu ya shilingi 500.Inaelezwa kuwa maelfu kwa maelfu ya watu wamekuwa wakimiminika kwa Mchungaji huyo Ambilikile Mwasakile kujipatia tiba ya gonjwa hilo hatari .

Japo kwa kiasi kikubwa ugonjwa wa Ukimwi unadhibitika kwa sasa kutokana na uvumbuzi wa dawa zenye ufanisi zaidi katika kudhibiti athari za ugonjwa huo,tiba rasmi haijapatikana.Hata hivyo,ukweli huu haumaanishi kuwa tiba ya Mchungaji Mwasakile ni feki kwa vile hadi sasa hakuna mtu au taasisi iliyopinga madai yake.

Pia,huwezi kuwashangaa maelfu ya watu wanaofurika kwa Mchungaji huyo kusaka tiba.Kama malaria tu inawafanya watu wakimbilie mahospitalini,sembuse waathirika wa Ukimwi!

Lakini kama kichwa cha habari kinavyohoji,ukimya wa Wizara ya Afya na serikali kwa ujumla kuhusu madai hayo unaweza kuzua zahma kama ile ya upatu maarufu wa DECI.Katika sakata hilo la "kupanda mbegu",watumishi kadhaa wa Mungu walifanikiwa kuhamasisha maelfu kwa maelfu ya Watanzania "kupanda mbegu" zao kwa matarajio ya kuvuna mamilioni.Sote tunajua kilichofuata.

Serikali ilikuwa ikifahamu uwepo wa DECI lakini haikuchukua hatua stahili (kuruhusu au kuharamisha) hadi pale ilipozinduka na kupiga marufuku upatu huo,hatua iliyowaacha wananchi lukuki wakiwa wamepoteza fedha zao "za ngama".

Sasa japo katika suala hili la tiba ya ukimwi,malipo ni shilingi 500 tu,unyeti wa suala hilo na faida au athari zake unalazimisha serikali kutoa kauli rasmi.Tunafahamu ombwe kubwa la uongozi linaloikabili serikali yetu lakini si kwa kiwango cha kushindwa kusema lolote kuhusu suala hili "dogo" japo linaloweza kuwa na athari kubwa kwa jamii.

Hivi kwa mfano tiba ya Mchungaji huyo ni feki,je hiyo haitoathiri watu wanaoweza kusitisha matibabu ya dawa za kudhibiti virusi vya Ukimwi (ARVs?Serikali yoyote yenye kujali watu wake inapaswa kutoa kauli ya mwongozo kwa wananchi wake kuhusu ukweli au uongo wa madai hayo ya kupatikana kwa tiba ya ukimwi.

Japo kujaribu kuhalalisha au kupinga madai hayo si kazi nyepesi,mazingira yafuatayo yanaweza kutoa mwanga japo kidogo:

Kwanza,katika imani za kidini,kuna uwezekano kwa binadamu kujaliwa karama za kufanya miujiza.Nadhani baadhi ya wasomaji wanafahamu kazi za watu kama Father Nkwera na yule mama wa Mikocheni (anadhani alikuwa anaitwa Esther kama sikosei).Kadhalika,wengi wetu tumesikia miujiza ya Sheikh Shariff.

Pili,kuna watu wanaoaminika kuwa na uwezo wa kutibu maradhi mbalimbali kwa kutumia tiba za asili.Katika ukoo wetu,kuna ndugu yangu mmoja ambaye amekuwa akitoa tiba za asili katika eneo la Kiberege huko Morogoro.Kila nilipokuwa namtembelea nilikuwa nashuhudia namna anavyotibu watu wenye matatizo mbalimbali,ya kiafya na kimaisha.Hata hivyo,hapo kwenye "zahanati" yake kuna tangazo kuwa yeye hana uwezo wa kutibu ukimwi.

Tatu,ni rahisi kuzusha jambo na likaaminika miongoni mwa wengi.Na kama jambo lenyewe ni habari njema basi si ajabu "waaminifu" wa awali wakasambaza habari hizo "njema" na kupelekea tetesi zisizo na ukweli kupata uaminifu.Waingereza wana msemo kwamba uongo usipokemea unaishia kupata hadhi ya kuwa ukweli.Sasa ikitokea kuwa madai ya Mchungaji huyo si ya kweli,lakini hakuna anayekanusha,basi madai hayo yanaweza kuchukua hadhi ya "ukweli".

Kinachonipa wasiwasi ni kauli ya Mchungaji Mwasakile kuwa alianza kutoa matibabu hayo mwezi Agosti mwaka jana baada ya kuoteshwa na Mungu.Kwa maana hiyo,kuna watu kadhaa ambao wanaweza kuwa mashuhuda wa ufanisi wa dawa anazotoa kwa wagonjwa wake.Kwanini habari hizo hazikufahamika hadi majuzi,inabaki kuwa muujiza kama habari yenyewe ya tiba.

Pengine unaweza kusema si rahisi mtu kutapeli kwa kutoza shilingi 500 tu.Lakini ukifanya hesabu za chap chap utagundua kuwa laiti wagonjwa 2000 tu wakilipa kiwango hicho,Mchungaji atakuwa ametengeneza shilingi milioni moja.Na kwa mujibu wa taarifa za idadi ya watu wanaoelekea kwa Mchungaji huyo,yawezekana ameshachuma shilingi milioni kadhaa hadi sasa.


Ni mapema mno kubaishiri lolote kuhusu madai hayo.Kwa upande mmoja tiba kwa nguvu za kiroho au dawa asilia inawezekana,japo sina hakika kama ukimwi nao unatibika kwa njia hizo.Lakini,again,katika Mungu yote yanawezekana.

Serikali inaweza kuwasaidia Watanzania kwa kutoa tamko rahisi kuhusu madai hayo.Na licha ya ombwe la uongozi linaloikabili serikali yetu,suala hili linaweza kuwa rahisi zaidi hasa kwa vile taarifa zinaeleza kuwa vigogo kadhaa wameonekana wakielekea kwa Mchungaji huyo kwenda kujipatia tiba.Hawa wanaweza kuwa mashuhuda wazuri katika suala hilo.


Wakati jamii inasubiri uthibitisho wa madai ya Mchungaji huyo ni vema kubaki na msimamo rasmi wa kitabibu kuwa ukimwi hauna tiba.Na kwa waliokwishapewa "tiba" ya Mchungaji huyo,ni muhimu kwao kufanya vipimo vya kitaalamu kuthibitisha kama kweli wamepona.Na kama wakipona basi iwe fundisho kwao badala ya "kurejesha libeneke kwa kasi mpya,nguvu mpya na ari mpya"

Picha zote kwa hisani ya Michuzi

Kwa habari na picha zaidi soma hapa kwa Miss Jestina

20 Jul 2007

Asalam aleykum,

Juzi nilipata barua-pepe kutoka kwa rafiki yangu mmoja aliyeko huko nyumbani.Huyu jamaa alikuwa akinilaumu “kirafiki” kwamba inaelekea nimeanza kuishiwa pointi za kuandika ndio maana takriban nusu ya makala yangu iliyopita ilikuwa ina habari “nyepesi nyepesi.”Sikukasirika kwani siku zote nathamini sana ushauri wenye lengo la kujenga au kuleta maendeleo.Nilimjibu kwamba nina pointi lukuki za kuandika,lakini kuna wakati inabidi “tupunguze kasi ya maisha” kwa kuangalia habari za vituko mbalimbali hususan vinavyojiri huku Ughaibuni.Pia nilimhakikishia kuwa “nyepesi nyepesi” hizo sio “fiksi” bali ni habari zinazohusu matukio ya kweli,ila tu yanachekesha kwa namna moja au nyingine.Kicheko ni afya.

“Nyepesi” za wiki hii ni pamoja na taarifa kwamba “wanene” 7 ndani ya baraza jipya la mawaziri la Gordon Brown (mrithi wa Tony Blair) wamekiri katika nyakati tofauti kuwa walishawahi kutumia “widi” (kwa wale ambao lugha ya mtaani ni mgogoro, “widi” ni bangi au marijuana).Siku kadhaa zilizopita,kiongozi wa chama cha wahafidhina (Conservative Party) David Cameron naye alijikuta kwenye wakati mgumu baada ya kupatikana nyeti kuwa alikuwa akivuta bangi katika siku za ujana wake.Cameron amekataa kuendelea na mjadala wa suala hilo akisema kuwa kila binadamu anaweza kufanya makosa hususan akiwa kijana.Alitaka wanaomshupalia wamhukumu kwa utendaji wake wa kazi wa sasa na sio mambo aliyofanya nyma.Kali zaidi ya zote ni pale Katibu wa Ofisi ya Mambo ya Ndani (Home Office-yaani ni sawa na Wizara ya Mambo ya Ndani huko nyumbani),Jacqui Smith,na waziri mmoja katika ofisi hiyo (hapa katibu wa wizara ni mkubwa kicheo kuliko waziri),Tony McNulty,walipotangaza hadharani kuwa nao walishawahi kuvuta bangi huko nyuma.Na “ushuhuda” huo umekuja wakati mwanamama huyo (Smith) akitangaza mpango wa serikali kuangalia upya uamuzi wa awali wa serikali ya Blair wa kushusha daraja (declassifying) la bangi.Habari kwamba viongozi hao wawili (ambao pamoja na majukumu mengine wana dhamana ya kudhibiti mihadarati) waliowahi kuwa wavuta bangi zimezua mjadala kama kweli wanapaswa kuendelea na nyadhifa zao.Pengine kinachowasaidia ni ukweli kwamba kuna wanasiasa wengine (wakiwamo mawaziri vivuli wa upinzani) ambao nao wameweka bayana kuwa walishawahi kuvuta bangi walipokuwa vijana.Uwazi na ukweli au vituko vya siasa?


Kuna habari nyingine ya majonzi lakini kwa namna flani inaweza inachekesha.Mwanamke aliyekuwa na uzito mkubwa kuliko wote hapa Uingereza,Nazima Hussein,amefariki na kuwaacha wanandugu wakiwa na wakati mgumu baada ya kubambikwa ushuru wa pauni 4,000 (zaidi ya shilingi milioni 8) kutoka kwa manispaa huko Southall,London.Ushuru huo ulitokana na gharama za kuuhudumia mwili wa marehemu ambao ulihitaji watumishi wa kikosi cha zima moto (firemen) 13 kuutoa mwili huo (uliokuwa na unene wa futi 3) kutoka katika flati aliyokuwa akaishi.Na walipoufikisha mochwari huko Uxbridge ilizuka kasheshe nyingine kwani hakuna toroli la kubebea maiti lililomtosha marehemu na pia mafriji yote ya kuhifadhia maiti hayakuweza kumudu ukubwa wa mwili wa marehemu huyo.Marehemu Nazima alifariki akiwa na uzito wa kilo 349 .Habari njema ni kwamba baada ya watu wa Manispaa “kusomeshwa” walikubali kupunguza gharama hadi pauni 3,000 (zaidi ya shilingi milioni 6).Ukiskia msiba mzito ndio huo.

Turejee nyumbani.Siku chache taifa limepewa changamoto ya kutosha kutoka kwa JK kuhusu suala la “kupima ngoma” (ukimwi).Na kwa mujibu wa taarifa za magazeti mbalimbali ya huko nyumbani watu kadhaa wameitikia wito wa Rais kwa kwenda kwenye vituo vya afya kupima ukimwi.Kwa mtizamo wangu,hamasa aliyotoa JK inaweza kuwa na matokeo makubwa sana kwani kwa upande mmoja inaweza kuwasaidia wale waliokuwa hawajui kama wameathirika kuanza kuchukua tahadhari ambazo zitawasaidia kuishi maisha marefu zaidi.Pia kwa wale ambao vipimo vitaonyesha hawajaathirika wanaweza kuachana kabisa na matendo ya ngono zisizo salama,na hata kumrejea Mola wao.Kadhalika,kwa wale watakaokutwa wana virusi vya ukimwi na wakati huohuo wana familia zinazowategemea wanaweza kupata nafasi mwafaka ya kuandaa “future” za familia zao.Jingine ni kwamba kampeni hiyo inaweza kuwafumbua macho wale vichwa sugu na viwembe wanaopenda kujidanganya kuwa ukimwi ni ajali kazini,na eti ajali haina kinga.

Waziri wa Afya amelielezea Bunge kuwa kuna mpango wa kuwapima ukimwi wale wote wanaofika hospitali kwa matibabu.Wazo hilo ni zuri sana lakini linahitaji tahadhari ya namna flani.Wapo wanaosema kuwa ukimwi ni sawa na maradhi mengine yasiyo na tiba kama kansa au kisukari.Hapana,ukimwi ni tofauti sana hasa kwenye namna jamii yetu inavyowaangalia walioathirika na ukimwi (unyanyapaa).Nadhani wapo watakaokubaliana nami kwamba baadhi ya watumishi wa taasisi za afya wana tabia ya kukiuka maadili ya taaluma yao kwa kutoa siri kuhusu afya za wagonjwa.Naamini baadhi ya wasomaji wameshawahi kunong’onezwa na dokta au nesi flani kuwa “yule nanihii anao (ukimwi).” Sasa kama Wizara ya Afya itatekeleza dhamira yake ya kutaka watu wote wanaofika hospitali wapime ukimwi inapaswa pia kuboresha mambo kadhaa ikiwa pamoja na kuhakikisha kuna washauri nasaha wa kutosha watakaoweza kuwasaidia hao watakaobainika kuwa “wanao.” Naamini pia kuwa kuna sheria inayowabana watumishi wa afya kutoa “siri” ya ugonjwa wa mtu,na katika mpango huu wa Wizara ni muhimu sheria hiyo ikaimarishwa zaidi kwani bila kufanya hivyo si ajabu watu wanaweza kukwepa kwenda hospitali sio kwa kuhofia kupimwa na kukutwa wanao bali kwa kuwaogopa hao wauguzi wasioweza kuhifadhi siri za wagonjwa.Pia Wizara inapaswa kuweka bayana iwapo mpango huo wa kumpima kila mgonjwa utakuwa ni suala la hiari au la lazima.Kwa hapa,wagonjwa wanahamasishwa kupima ukimwi lakini hawalazimishwi.Pasipo kuweka misingi mizuri,nia nzuri ya Wizara ya Afya inaweza kuleta mkorogano usio wa lazima,maana si ajabu tukasikia flani kanyimwa nafasi ya kuonana na daktari kwa vile tu kukataa kupima ukimwi.Ifahamike kuwa suala la kupima au kutopima ni haki ya mtu binafsi.

Pia nimesoma habari iliyonisikitisha husu kilio cha Kamisheni ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kwamba imekuwa ikipata ushirikiano hafifu kutoka kwa waajiri katika suala la kuhakiki vyeti vya taaluma za waajiriwa.Unajua utandawazi umeleta mambo mengi sana ikiwa ni pamoja na fursa ya mtu kujipatia taaluma bila kutia mguu chuoni.Vipo vyuo kadhaa duniani vinavyotoa kozi kwa njia ya mtandao,lakini tatizo ambalo limekuwa likizisumbua hata nchi za Magharibi ni lile la baadhi ya vyuo vya kitapeli ambavyo vinaweza kukupatia cheti cha Udaktari wa Falsafa kwa wiki moja.Ukiona mfumuko wa madokta (sio wale wa hospitali) usikimbilie kufikira kuwa pengine siku hizi PhD zimekuwa rahisi.Ukweli ni kwamba PhD feki zimetapakaa sana kutokana na vyuo feki (japo vingine vimeandikishwa kisheria) ambavyo wanachojali wao ni fedha tu ya huyo anayehitaji PhD ya chapchap.Inatuuma sana sie wengine ambao tunazeekea maktaba kutafuta huo udokta “wa kwelikweli” huku wenzetu “wanasomea baa au kwenye nyumba ndogo zao” na wanaamka asubuhi na “hangover” wakiwa madaktari wa falsafa.Nadhani falsafa pekee waliyonayo “vilaza” hawa ni kuhusu waganga gani wa kienyeji wanasaidia mtu kula rushwa na aendelee kuonekana mwadilifu au namna ya kutogonganisha magari kati ya mama watoto na nyumba ndogo.

Ukweli mchungu ni kwamba TCU ina wakati mgumu kufanikiwa katika azma yake hiyo njema,kwani wengi wetu tunajua kuwa baadhi ya waajiri nao wana elimu za kutilia mashaka.Pia nadhani kuna mapungufu ya kisheria kuhusu matumizi ya vyeti feki,kwani nakumbuka jeshi la polisi halikuchukua hatua yoyote lilipobaini kuwa mbunge mmoja hakuwa mkweli kuhusu elimu yake ya sekondari.Sasa kama ufeki wa vyeti vya sekondari “sio big deal” kwa polisi je hao wenye PhD feki wataweza kuguswa?Enewei,tuna vita kadhaa tunazopenda zianze dakika hii:dhidi ya wala rushwa,majambazi,wabadhirifu,wauza unga,nk.Pengine siku moja itatangazwa vita ya kitaifa dhidi ya vyeti na taaluma feki.Yote yanawezekana.

Alamsiki


18 Jun 2006

KULIKONI UGHAIBUNI

Habarini za huko nyumbani.Hapa shwari.

Mada yangu ya leo najua dhahiri itawakera wateule wachache wa aina flani.Lakini kabla ya kuwapa somo ngoja tuongelee suala la imani na dini hapa napoishi.Nilipofika hapa kwa mara ya kwanza nilionyeshwa majengo kadhaa ambayo hapo awali yalikuwa makanisa lakini sasa yamegeuzwa kuwa kumbi za disko na klabu za usiku.Na hao walioyageuza makanisa hayo kuwa sehemu za starehe wala hawakujishughulisha kubadili mwonekano wake bali wameyaacha yatoe ushuhuda kuwa huko nyuma yalikuwa sehemu za ibada.Nilipofanya udadisi kwa wenyeji niliambiwa kuwa makanisa hayo yaliuzwa baada ya kuwa matupu kutokana na ukosefu wa waumini.Wengi wa waumini wa makanisa ya mji huu naoishi ni aidha wageni (waliotoka nje ya nchi hii kama mimi) au vikongwe.Na si ajabu kukuta kanisa lenye uwezo wa kuchukua watu 500 likiwa na waumini 50 tu.

Binafsi sina majibu ya moja kwa moja kuwa tatizo la hawa wenzetu ni nini.Ila nachofahamu ni kwamba kuna watu kadhaa ambao wanajitambulisha kuwa hawana dini,au hawaamini kuwa kuna Mungu.Pengine labda kwa vile wengine wamezaliwa na kukuta maisha ni mteremko basi hawaoni umuhimu wa kuamini kuwa kuna Mungu.Hata hivyo,imani ni suala la mtu binafsi hivyo pengine si mwafaka kuhoji kwa nini flani anaamini au haamini kuwepo au kutokuwepo kwa Mungu.Japo mie ni muumini wa aina flani huwa sisiti kuwasifu wale wasio waumini lakini hawaoni aibu kuelezea msimamo wao wa kidini.Kwa lugha nyingine watu hao sio wanafiki,wanaelezea bayana kile wanachokiamini au kutokiamini.

Kuna tatizo la msingi huko nyumbani japokuwa natambua dhahiri kwamba watu wengi hawapendi kujadili mambo ya dini.Tatizo hilo ni UNAFIKI.Hivi ndugu zanguni,kama imani unayoifuata na kujidai nayo inakukataza kuvuta sigara si bora usivute tu kuliko kuwachanganya watu?Baadhi ya viongozi wetu wa dini wamekuwa mstari wa mbele sana kuwakemea wale ambao wanakwenda kinyume na imani zao,lakini wakati huohuo viongozi hao wanashirki kwenye maovu wanayoyakemea.Ndio tunatambua kuwa mara nyingi viongozi wetu wa dini wana wafadhili wao nje ya nchi,lakini hicho sio kigezo cha wao kuishi maisha tofauti kabisa na wafuasi wao.Utakuta katika kijiji flani ambacho kimegubikwa kabisa na umasikini,kiongozi flani wa dini anaishi kama yuko peponi vile.Na bila huruma,huku akitumia kisingizio cha maandiko matakatifu,anawashurutisha waumini wake kujipigapiga kuongeza sadaka wanazotoa.Pengine ni ule msemo kuwa alie nacho atazidi kuongezewa na yule asie nacho atanyang’anywa hata kile kidogo alichonacho.

Kinachokera zaidi ni hili ni suala la baadhi ya viongozi wa madhehebu flani kuwa na watoto mtaani huku sheria za madhehebu yao haziwaruhusu kufanya hivyo.Hivi unapomzalisha mwanamke ambae huwezi kumuoa kwa vile majukumu uliyonayo yanakukataza kufanya hivyo si ni sawa tu na kumharibia maisha huyo mwanamke uliezaa nae.Tatizo hili ni sugu sana hususan maeneo ya vijijini.Kinachosikitisha ni ukweli kwamba waumini wanafahamu kuwa kiongozi flani wa dini anaishi kinyume na maadili lakini hawachukui hatua yoyote zaidi ya kulalamika chinichini.Mimi binafsi nina mifano hai ya baadhi ya viongozi wa madhehebu yangu ambao wana watoto lukuki mitaani.Baadhi yao wanatoa huduma kwa wazazi wa watoto hao lakini wengine wamewatelekeza tu.Hawa watu ni wanafiki ambao hawastahili kuachwa wanaendeleza uhuni kwa kisngizio kuwa daraja walilofikia haliwezi kutenguliwa.Mitume wetu waliishi maisha ya uadilifu ambayo yalishabihiana kwa asilimia mia moja na kile walichokuwa wakikihubiri.Na sio kwenye uzinzi tu,bali hata kwenye dili za kibiashara.Wapo wanaopokea kitu kidogo ili,kwa mfano,mtu akiagiza gari lake kutoka nje apunguziwe ushuru kwa vile linaonekana limeagizwa na taasisi ya kidini.Huu ni ukwepaji wa kodi ambao joho la utumishi wa Mungu halipaswi kuwa ngao ya kuzuia mhusika kuchukuliwa hatua za kisheria.

Hivi majanga kama ukimwi yataondoka vipi iwapo baadhi ya wale wanaopaswa kukemea vitendo vya ngono kwa vile vinavunja amri ya Mungu nao ni washiriki wa vitendo hivyo?Ndio,maandiko yanataka tufuate yale yanayosemwa na sio matendo ya msemaji lakini katika hali halisi mzazi anayeendekeza ulabu hawezi kueleweka pale anapomkemea mwanae anaefuata mkumbo wake.

Tafadhalini jamani,naomba mhubiri kile mnachokiamini na kukifuata ili kuwasaidia kuwafikisha peponi hao naowahubiria.Na hilo si ndio jukumu lenu?

Alamsiki

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.