Showing posts with label ULAYA. Show all posts
Showing posts with label ULAYA. Show all posts

22 Aug 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Kombe la Dunia mwaka 2006.Wenyewe wanaiita shughuli hii “the biggest show on earth.” (yaani mashindano makubwa kabisa duniani).Inaweza kuwa kweli.Kombe la dunia linawaunganisha mamilioni kwa mamilioni ya watu katika takriban kila pembe ya sayari hii.Wapo wale wanaofuatilia timu zao za taifa zikitafuta nafasi katika vitabu vya historia ya soka,wengine tukiwamo Watanzania tunafuatilia michuano hiyo kwa vile wengi wetu tunapenda soka japokuwa kwa sababu zinazoweza kuchukua mwaka mzima kuzitaja hatujui lini nasi tutakuwa washiriki.

Kuna mjadala mdogo japo muhimu unaoendelea huku Ughaibuni na pengine hata kwingineko kuhusu kama ni kweli michuano hii na michezo kwa ujumla inaleta umoja na sio mpasuko miongoni mwa timu au nchi shiriki na mashabiki ulimwenguni kote.Pengine hakuna sehemu nzuri zaidi ya kuanzia mjadala huu kama hapa Uingereza.Pengine ni vema kuielezea Uingereza kwa kutumia majina wanayotumia wenyewe.United Kingdom ni muungano wa “nchi” nne:England,Scotland,Wales na Northern Ireland. Great Britain ni hizo tatu za mwanzo ukitoa Northern Ireland (ambayo kijiografia haiko katika ardhi moja na hizo tatu).Kwa hiyo kuna wakati utasikia nchi hii ikiitwa The United Kingdom of Great Britain and Northern Ireland.Kwa kawaida,katika mashindano mbalimbali Uingereza huwakilishwa na timu za taifa au klabu kutoka “nchi” hizo nne kama vile ilivyo kwa timu za Taifa za Bara na Zanzibar zinavyoiwakilisha Tanzania.

Katika mchakato wa kutafuta nafasi ya kushiriki katika Kombe la Dunia ni England pekee iliyofanikiwa na kuziacha Wales, Scotland na Northern Ireland kubaki watazamaji tu.Hapo ndipo shughuli inapoanza.Kwanza Waziri Mkuu (First Minister) wa Scotland Jack McConnell aliweka msimamo wake wazi kwamba hatashabikia England,ambayo kwa hapa Scotland inajulikana kwa jina la kiutani kama Auld Enemy (Adui wa zamani) na badala yake angeshabikia Trinidad and Tobago-au kwa kifupi T&T.Na si yeye pekee mwenye mtizamo huo.Asilimia kubwa ya Waskotishi walishabikia T&T ilipopambana na England.Wapo waliotoa kisingizio kwamba ushabiki wao ulitokana na ukweli kwamba kuna mchezaji wa T&T mwenye ubini Scotland (anaitwa Jason Scotland,anayechezea timu ya daraja la kwanza ya St Johnstone) lakini wengine hawakuwa hata na haja ya kutoa visngizio bali kusema ukweli kwamba ushindi kwa England ni karaha kwao.Kama kuna sehemu zaidi ya nchini T&T ambako jezi za timu yake ya taifa ziliuzika sana basi si kwingine bali Scotland.
Kuna hii kitu inayoitwa “bendera ya Mtakatifu Joji” (St George flag).Nadhani kwa wale wanaofuatilia mechi za England watakuwa wameona bendera hiyo nyeupe yenye msalaba mwekundu.Bendera hiyo ina historia ndefu ambayo pengine hapa si mahala pake,lakini lililo wazi ni kwamba inahusishwa kwa kiwango flani na hisia za ubaguzi wa rangi (racism).Hata baadhi ya taasisi zimekuwa na wasiwasi pale watumishi wake wanapopeperusha bendera hizo.Kwa mfano,hivi karibuni supamaketi kubwa iitwayo Tesco ilipiga marufuku madereva waliokuwa wanaleta mizigo kwenye supamaketi hiyo huku wakipeperusha bendera ya Mtakatifu Joji,japo baadaye uamuzi huo ulibatilishwa.Pia mamlaka ya viwanja vya ndege (BAA) ilipiga marufuku kupeperusha bendera hiyo kwenye majengo yanayofanyiwa ukarabati Terminal 5 Heathrow Airport.Mkanganyo zaidi kuhusu bendera hii umeongezwa na ukweli kwamba BNP,chama cha siasa chenye mtizamo wa kibaguzi,kimekuwa kikiitumia bendera hiyo katika harakati zake dhidi ya wahamiaji na wageni.Watetezi wa bendera hiyo wanasema inawaonyesha uzalendo na sio alama ya ubaguzi.

Tofauti na huko nyumbani ambako hadi hivi karibuni kitendo kutundika bendera ya Taifa dirishani kingeweza kukupeleka Segerea (jela) huku kwa wenzetu bendera ni miongoni mwa alama za kujivunia utaifa/uzalendo wao.Hata hivyo,wapo wanaotumia utaifa kama kifuniko (cover) cha dhamira zao za kibaguzi.Mara nyingi vikundi vinavyoendekeza siasa za kibaguzi vimekuwa vikitumia sana bendera za mataifa yao kujitambulisha (kama ilivyo kwa BNP).Utaifa uliopindukia ni mithili ya ulafi:kula sio kitendo kinachoudhi lakini kula kupita kiasi (ulafi) unaudhi kwa vile unaweza kuwaathiri watu wengine,kwa mfano kuwalaza na njaa.Wachambuzi wa soka la Hispania walikuwa na wasiwasi iwapo timu yao ingefanya vizuri kwenye Kombe la Dunia kutokana na ukweli kwamba Waspanishi wengi wanajali zaidi timu zinazotoka katika miji yao (kwa mfano Real Madrid,Barcelona au Valencia) kuliko timu ya taifa.Hapo tatizo ni zaidi ya utaifa bali asili ya mtu anakotoka katika taifa.

Na pengine ni kwa vile waandaaji wa Kombe la Dunia wanafanya kila jitihada kupambana na wakora wa soka ndio maana inapunguza na vitendo visivyopendeza machoni wa watu kwa mfano kutoa sauti kama za nyani kuwakashifu watu weusi.Matukio ya ubaguzi katika soka yamekuwa ni tatizo linalowagusa watu wengi.Hali ni mbaya sana huko Ulaya Mashariki ambapo kwa mfano baadhi ya timu za hapa zenye wachezaji weusi huwa zinatahadharishwa mapema kabla ya kwenda huko kuwa zitegemee wachezaji hao weusi kunyanyaswa na mashabiki wabaguzi.Soka la Hispania katika siku za karibuni limegubikwa mno na kelele za kibaguzi dhidi ya wachezaji weusi.Italia pia inasifika kwa hilo kama ilivyo kwa Ujerumani yenyewe.Hata hapa Uingereza kuna hisia kwamba miongoni mwa sababu zinazoifanya timu kama Chelsea “kuchukiwa” ni kwa vile mmiliki Roman Abramovich si Mwingereza, kocha Jose Maurinho ni Mreno na wachezaji wengi ni kutoka nje ya Uingereza.

Kwa kumalizia,ngoja niwachekeshe kidogo.Hapa kuna kundi la akina mama wanaojiita “Wajane wa Kombe la Dunia.”Hawa ni wale wanaoyaona mashindano haya kama adhabu kwa vile waume zao wakereketwa wa soka huwasahau kwa muda wake zao na akili yote kuelekezwa kwenye michuano hiyo.Huenda hata huko nyumbani kuna “wajane” pia.Si unajua tena wapo wanaotumia kisingizio cha kwenda “kucheki boli” kupata wasaa wa kuzungukia nyumba ndogo…huo ni utani tu.

Alamsiki

17 Apr 2006

KULIKONI UGHAIBUNI

Habarini za huko nyumbani.Naamini mambo yanakwenda vema.Hapa napo ni shwari tu japokuwa viama vyetu vya kawaida bado vinaendelea.Pengine utashtuka kusikia neno “viama” (umoja-kiama,wingi-viama).Ngoja niende moja kwa moja kwenye pointi.

Fikra nilizokuwa nazo wakati niko huko nyumbani,na ambazo nilikuwa nashea na jamaa zangu kibao,ni kwamba maisha ya Ughaibuni ni kama ya peponi:ardhi ya maziwa na asali,kama vitabu vya dini vinavyosema.Tabu ya kwanza niliyokutana nayo ni lugha.Si kwamba mie ni maimuna ambae lugha ya “kwa mama” haipandi.La hasha,lugha hiyo inapanda ki-sawasawa.Tatizo ni kwamba wakati nakuja hapa nilishazowea kuongea Kiswahili changu chenye lafidhi ya ki-Ndamba (ndio,mimi ni Mndamba kutoka Ifakara.Awije mlongo…).Uzuri wa Daresalama nilipokuwa naishi ni kwamba wewe ongea Kiswahili cha aina yoyote,lakini una hakika watu watakuelewa na mtasikilizana bila matatizo.Hapa “kwa mama” unaweza kwenda sehemu na ukawa unaongea kiingereza chenye lafidhi ya ulikotoka na watu wakaishia kukukodolea macho tu.Hawakuelewi unaongea nini.Unakwenda sehemu,unahitaji huduma fulani.Unamuuliza mhudumu hapo,anaonekana kutoelewa unachoongea.Anabaki kukuomba “sorry can you say that again?” (samahani,unaweza kurudia ulichokisema?).Basi hapo inabidi useme neno mojamoja tena taratibu ili muelewane.

Lakini tatizo la pili ni lile la kujisahau na kujikuta unaingiza maneno ya Kiswahili kwenye lugha yao,hasa pale mtu anapoonekana aidha hataki kukuelewa au ni mgumu wa kuelewa.Hebu fikiri,unakwenda dukani,unamwambia muuza duka “nipatie maji ya kunywa ya Kilimanjaro”,yeye anakuuliza “unasemaje anko?”,unarudia tena,na yeye anarudia kukuuliza unasemaje!Ikifika mara ya tatu kuna hatari ukataka kujaribu kumwelewesha muuzaji huyo kwa lugha ya kwenu.

Kama mawasiliano ni tatizo sugu basi kufanya shopping ni tatizo zaidi.Hili ni tatizo ambalo binafsi nakutana nalo takribani kila napoingia kwenye duka au supamaketi.Sijui tatizo ni hisia kwamba Mtanzania kama mimi sina uwezo wa kununua kitu dukani au vipi!Ile kuingia tu kwenye duka au supamaketi utakuta mlinzi anaanza kukuandama nyuma yako.Hofu ni kwamba labda utakwapua kitu na kuondoka nacho bila kulipa.Kichekesho ni kwamba wakati walinzi wa duka wanahangaika na wewe mtu mweusi,mateja ya kizungu yanatumia mwanya huo kukwapua vitu na kuchomoka navyo bila kulipa.Ndio,Ulaya kuna mateja kibao kama ilivyo huko kwetu.Ipo siku nitakupatia stori hiyo ya mateja wa Ulaya kwa kirefu.Mara nyingi utakuta hao wadokozi wanavizia mtu mweusi aingie dukani nao wakafanye vitu vyao kwa vile wanajua akili za walinzi zitakuwa kwako.

Kwenye mabasi nako wakati mwingine ni adha tupu.Utamkuta mtoto wa kizungu anakushangaa utadhani ameona muujiza flani.Kibaya zaidi ni pale mtoto huyo anapodiriki kumuuliza mama yake kama wewe ni mtu au sana mu.Si mchezo manake.Unaweza kutaka kurusha ngumi lakini ukikumbuka kilichokupeka Ughaibuni huko inabidi umezee tu.Watoto wengine waliolelewa ovyo huweza kudiriki kukugusa ngozi kisha kuangalia mikono yao kama imebakia na rangi nyeusi kwani kwao mtu lazima awe mweupe!

Haya wengi wenu mnaweza kuwa hamyajui si kwa sababu hayaripotiwi na BBC au Skynews bali ni kwa vile wengi wetu tulioko huku tukirudi nyumbani tunapenda kutoa stori nzuuri kuonyesha kuwa huku ni kuku kwa mirija tu,ardhi ya maziwa na asali,na kuficha viama tunavyokumbana navyo kila siku.

Hiyo ndio Ughaibuni,ndugu zanguni.Hata hivyo,naomba nisisitize kwamba viama hivyo havipo kila mji.Ile miji yenye wageni wengi au tuseme watu weusi wengi,kuna unafuu kidogo,japokuwa huko nako kuna viama kama vya umbeya,kusutana na hata kuagiziana mafundi (waganga wa kienyeji) kufanyiziana.Ukibisha kwamba watu wanaagiza wataalam kutoka huko nyumbani kuja kurekebisha mambo yao au kufanyiza kwa njia za asili basi nenda pale Buguruni kwa mwinjilisti flani ambae huja huku mara kwa mara kuhubiri neno la Bwana na kutoa pepo.Huyo ameshasikia maungamo na ushuhuda kadhaa wa hao waagizaji mafundi kutoka huko nyumbani.

Hadi wiki ijayo,Alamasiki

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.