Showing posts with label URAIS 2015. Show all posts
Showing posts with label URAIS 2015. Show all posts

31 Oct 2014

Makala hii ilipaswa kuchapishwa katika jarida la Raia Mwema toleo la Oktoba 22, 2014 lakini kwa sababu wanazozijua wahusika pekee haikuchapishwa. Nomba kukupa fursa ya kuisoma katika uhalisi wake.

Duru za siasa za Uingereza zimevamiwa na mwanasiasa hatari lakini mahiri kwa ushawishi, ndivyo wanavyoeleza baadhi ya wachambuzi wa siasa nchini hapa kufuatia kuibuka kwa kasi kwa Nigel Farage na chama chake ‘cha kibaguzi’ cha United Kingdom Independence Party (UKIP).

Pamoja na kauli zake za kukera na pengine za ubaguzi wa waziwazi, Farage ana kipaji muhimu kwa mwanasiasa: kutumia mapungufu  ya vyama vikuu – Conservatives, Labour na Liberal Democrats – kuwavuta wananchi wakiunge mkono chama chake. Na anafanikiwa kwa kiasi kikubwa, hasa baada ya chama hicho kushinda kiti cha ubunge katika uchaguzi mdogo wa jimbo la uchaguzi la Clacton huko England.

Matokeo hayo yamekipatia chama hicho mbunge wa kwanza, Douglas Carswell, ambaye alihama kutoka Conservatives hivi karibuni. Taratibu duru za kisiasa nchini hapa zinaanza kuiona UKIP kama chama makini licha ya sera zake zenye mwelekeo wa ubaguzi.

Ajenda kuu ya UKIP ni kuitaka Uingereza ijiondoe kwenye Umoja wa nchi za Ulaya (European Union). Kadhalika, chama hicho kinapinga vikali ujio wa wageni nchini hapa, huku kikidai kuwa serikali ya chama tawala (Conservatives) inayoshirikiana na Liberal Democrats, imeshindwa kama ilivyokuwa kwa serikali iliyotangulia ya Labour kutatua tatizo hilo.

Suala la uhamiaji ni moja ya turufu muhimu kila unapojiri uchaguzi katika nchi hii, na UKIP wanaitumia ajenda hiyo kwa ufanisi mkubwa. Hata hivyo, baadhi ya wachambuzi wanatahadharisha kuwa Farage ni mtu hatari kwa sababu ya mrengo wake mkali wa kulia ambao unakaribiana na ule wa chama cha wazi cha kibaguzi cha British National Party. Baadhi ya wachambuzi wanaiona UKIP kama mchanganyiko wa Conservatives na BNP, lakini wanatambua kuwa mvuto wake unachangiwa na kuongea yale yanayowagusa wapiga kura wengi.

Laiti UKIP ikiendelea kufanya vema, na dalili zipo za kutosha, kuna uwezekano wa chama hicho kuweza kuunda serikali ya umoja na Conservatives baada ya uchaguzi mkuu ujao. Laiti hilo likitokea, ni wazi kuwa Uingereza itakuwa taifa tofauti kwa kiasi kikubwa na hilo tulilonalo hivi sasa.

Lengo la makala hii sio kumzungumzia Farage au chama chake cha UKIP bali kuangalia haja ya kuwa na ‘akina Nigel Farage wa siasa za Tanzania.’ Hapo simaanishi kuwa na wanasiasa wenye sera za kibaguzi bali wenye kutambua matatizo yanayoikabili Tanzania yetu na sio tu kuyatumia kupata sapoti bali kuyatafutia ufumbuzi. Kwa sasa hatuna mwanasiasa wa aina hiyo.

Sijui hadi muda huu ni Watanzania wangapi wanatambua kuwa tuna chini ya mwaka mmoja kabla ya kufanyika kwa uchaguzi mkuu hapo mwakani. Sintofahamu ya Bunge la Katiba na hatimaye kupatikana kwa Katiba pendekezwa kumewachanganya wananchi vya kutosha. Na katika kukoroga mambo zaidi, yayumkinika kuhitimisha kuwa ni Watanzania wachache tu wanaofahamu iwapo kutakuwa na kura ya maoni ya kupitisha au kukataa Katiba pendekezwa. Tayari Tume ya Taifa ya Uchaguzi imeshatamka kuwa haiwezi kuharakisha kura hiyo, japo Rais Jakaya Kikwete ameendelea kuwahakikishia Watanzania kuwa Katiba mpya itapatikana hivi karibuni.

Tupate Katiba mpya au la, mwaka mmoja kutoka sasa tutamchagua mrithi wa Rais Kikwete, awe ni kutoka CCM au chama kingine. Mazingira yalivyo hadi sasa hayatoi mwelekeo wa nani anayeweza kushika wadhifa huo muhimu kwa Tanzania yetu. Binafsi, ninaamini kuwa mrithi wa Kikwete atakuwa ‘mtu wake wa karibu,’ chaguo lake ambalo kwa mbinu za wazi na zisizo wazi atapigiwa upatu hadi kushika wadhifa huo.

Sababu ya Kikwete kuuhitaji ‘mtu wake’ ipo wazi. Vipindi vyake viwili vya utawala vimetawaliwa na mlolongo wa kashfa mbalimbali za ufisadi. Pasipo kuwa na mtu ‘wa kuaminika,’ si ajabu tukashuhudia yaliyomkumba Rais wa zamani za Zambia Frederick Chiluba. Na hata kama haistahili kwa Rais aliye madarakani kumwandama mrithi wake, mantiki ya kawaida tu inatosha kueleza kuwa hakuna mtu anayetaka kustaafu huku hajui hatma yake itakuwa vipi. Moja ya kanuni isiyo rasmi ya siasa ni hii: “kamwe usimkabidhi madaraka adui yako. Atakuangamiza hata kabla hajaizowea ofisi uliyomkabidhi.” Ni wazi Kikwete analitambua hilo.

Mengi yanaongelewa kuhusu ‘watu wa karibu na Kikwete’ lakini ni vigumu kujua ukweli. Kama kuna mwanasiasa ambaye amefanikiwa sana kuonekana kama mrithi asiye rasmi wa Kikwete ni Edward Lowassa. Lakini taarifa zinakanganya kuhusu mahusiano ya wanasiasa hao ambao walikuwa marafiki wakubwa. Kuna wanaodai urafiki wao umevurugika, lakini uzoefu wa kisiasa waonyeshe kuwa hakuna maadui (au marafiki) wa kudumu katika siasa. Kwa vile Lowassa (Akishirikiana na mwanasiasa mwingine Rostam Aziz) alimsaidia sana Kikwete kuingia madarakani, yawezekana ‘deni’ hilo likapelekea Kikwete kumsaidia Lowassa kuwa mrithi wake, hasa endapo (Lowassa) atamhakikishia Kikwete ‘usalama wake’ baada ya kustaafu.

Kuna wanaosema Bernard Membe, mwanasiasa mwingine aliye karibu na Kikwete ni miongoni mwa wanaoweza kupewa nafasi hiyo. Nilishawahi kuongelea vikwazo dhidi ya Membe lakini kwa vile ni vigumu kwa nchi ya Kiafrika kupata Rais kinyume na matakwa ya Idara ya Usalama wa Taifa ya nchi husika, na kwa vile Membe ni shushushu mstaafu, basi hakuna lisilowezekana iwapo atapata sapoti ya kutosha kutoka kwa ‘mashushushu wenzake.’

Lipo suala la Zanzibar ambalo kwa akina sie tunaochimbachimba mambo tunaona ni kama bomu la wakati (time bomb) linalosubiri kulipuka kuhusiana na hatma ya Muungano. Sahau kuhusu Katiba pendekezwa, hatma ya Muungano itategemea uwezo wa aliyepo madarakani kulazimisha matakwa ya watawala. Na kwa minajili hiyo, naona uwezekano wa Dkt Ali Shein kupigiwa chapuo amrithi Kikwete. Na kwa vile Shein amekuwa Makamu wa Rais wa Kikwete kwa miaka 10, si vigumu kumpatia ‘bosi wake wa zamani’ uhakika wa ustaafu wake.

Kuhusu Waziri Mkuu Mizengo Pinda, binafsi ninashindwa kuelewa malengo yake kuhusu kuwania urais. Labda yawezekana ni kile kinachoitwa ‘Plan B’ yaani iwapo kila ‘mrithi mtarajiwa wa Kikwete’ akishindikana, basi Pinda anakuwa ‘mchezaji wa akiba’ wa kuokoa jahazi. Katika mazingira ya kawaida, ni miujiza tu ndiyo inayoweza kumwingiza Pinda Ikulu. Sababu ni nyingi, nitaziongelea katika makala zijazo. Hata hivyo, kama alivyo Membe, Pinda ni shushushu mstaafu, na hilo laweza kuwa turufu kwake.

Wakati takriban yote niliyoyaongelea hapo juu ni ya kufikirika zaidi kwa maana hayajiri waziwazi, mwanasiasa pekee ambaye tangu aitangaze nia yake ya kutaka urais hapo mwakani ameendelea kuwaaminisha Watanzania kuwa yupo ‘serious’ ni January Makamba. Ninaomba kukiri kwamba awali nilipomsikia January akitangaza nia hiyo nilidhani anatania. Siku kadhaa baadaye, kwa kutumia mitandao ya kijamii hasa Twitter, mwanasiasa huyo kijana amejitanabaisha kama mtu anayetaka kwa dhati kuliongoza taifa hili.

Hivi ninavyoandika makala hii, January ameanzisha utaratibu wa maswali na majibu (question and answer session) huko Twitter kwa kutumia ‘hashtag’ #askJanuary yaani ‘Muulize January.’ Japo ninatambua kuwa ni vigumu kuhitimisha ‘mafanikio’ ya mwanasiasa kwa kuangalia ‘anavyojichanganya na watu’ katika mtandao wa kijamii, hasa kwa kuzingatia ukweli kwamba bado Watanzania wengi si watumiaji wa mitandao ya jamii, January amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kujenga sio tu kuaminika kuwa yupo ‘serious’ katika dhamira yake ya kutaka urais mwakani lakini pia amejiweka karibu na watu wengi wanaotumia mitandao hiyo ya kijamii.

Sasa kama Rais ajaye atatokana na kutambulika kwake kwa angalau baadhi ya wapiga kura, basi hadi muda huu January anaongoza katika hilo- pasi haja ya kufanya opinion poll. Alitangaza anataka urais, ameendelea kuwaaminisha wananchi kuwa anataka urais, anaendelea kueleza atafanya nini akiwa Rais, na kwa sie tunaoamini kuwa mitandao ya kijamii ni moja ya nyenzo muhimu kufikisha ujumbe kwa wananchi (angalau huku nchi za Magharibi), basi lolote linawezekana kwa mwanasiasa huyo kijana.

Nihitimishe makala hii kwa kuahidi kuendelea na uchambuzi huu wa wagombea urais ambapo katika moja ya makala zijazo nitazungumzia ‘muungano wa UKAWA kumsimamisha mgombea mmoja’ nikielemea zaidi kwenye vikwazo kutoka kwa ‘nguvu za giza’, sambamba na kuwachambua wanasiasa wengine wanaotajwatajwa. Kwa mfano, kuna anayedhani Ridhiwani Kikwete anaweza kuingia katika mbio za kurithi nafasi inayoshikiliwa na baba yake hivi sasa?

Mwisho kabisa, kama tahadhari, uchambuzi wangu unaelemea zaidi katika kile tunachoita’ hali halisi mtaani,’ kufuatilia matokeo kadri yanavyojiri, upepo wa kisiasa unavyovuma, na ninajitahidi kuepuka kutumia uelewa wangu wa stadi za siasa au taaluma nyinginezo kuniongoza katika uchambuzi huu.  Kwa kifupi, ninaongozwa na hali halisi.

MUNGU IBARIKI TANZANIA

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com  


28 Nov 2013


MAKALA hii ni mwendelezo wa ile iliyochapishwa katika toleo lililopita la gazeti hili, iliyobeba kichwa cha habari ‘Nani kinara wa CCM urais 2015?’
Lakini kabla sijaingia kiundani, nadhani ni vema nikarejea nilichoandika katika makala iliyopita kuhusu kukua kwa uwezekano wa CCM kubaki madarakani baada ya Uchaguzi Mkuu ujao. Wiki iliyopita ilishuhudia chama kikuu cha upinzani cha CHADEMA, kikiingia katika mtafaruku mkubwa ambao licha ya kutishia uhai wake unazidi ‘kupapalia’ mazingira mwafaka ya ushindi kwa CCM.
Awali, CHADEMA ilitangaza kuwavua madaraka viongozi wake waandamizi watatu, Zitto Kabwe, Dk. Kitila Mkumbo na Samson Mwigamba na kuwapa siku 14 kujieleza kwa nini wasivuliwe uanachama baada ya kupatikana kwa nyaraka inayodaiwa kulenga kukihujumu chama hicho.
Jumapili iliyopita, Zitto na Kitila waliitisha mkutano na waandishi wa habari ambao kimsingi haikusaidia japo kupunguza moto unaozidi ‘kuunguza nyumba ya CHADEMA.’ Kwa kifupi, wanasiasa hao wawili walipinga vikali shutuma zilizoelekezwa kwao na kuhalalisha kile kilichotafsiriwa na uongozi wa chama hicho kama hujuma, huku wao wakibainisha kama matumizi ya demokrasia kwa minajili ya kuiboresha CHADEMA.
Pasi haja ya kuingia kwa undani katika sokomoko hilo, ni wazi kwamba uamuzi wa kuwavua madaraka viongozi hao na msimamo uliotolewa na ‘wahanga’ hao unaendeleza mapambano ya madaraka ndani ya CHADEMA. Kubaki au kuondoka kwa akina Zitto hakuwezi kukirejesha chama hicho katika mahala kilipokuwa. Kibaya zaidi, japo hakuna tathmini yoyote iliyokwishafanywa kuhusu athari za mgogoro huo, ni wazi Watanzania wengi wameanza kupoteza matumaini kwa chama hicho kilichotarajiwa sio tu kutoa upinzani mkubwa kwa CCM bali pia hata kuweza kuingia Ikulu mwaka 2015.
Nihitimishe suala hili la CHADEMA kwa kutanabaisha kuwa japo inafahamika kuwa lolote linawezekana katika siasa, ukweli kwamba tumebakiwa na takriban mwaka na ushee tu kabla ya Uchaguzi Mkuu ujao, sambamba na ukweli kuwa hakuna dalili ya mgogoro huo wa CHADEMA kumalizika hivi karibuni, itakuwa vigumu mno kwa chama hicho kujipanga upya na vyema, kuweza kutoa ushindani wa maana katika Uchaguzi Mkuu ujao. Nitaijadili kwa kirefu hatma ya CHADEMA katika makala zijazo.
Tukiendelea na mada ya urais kwa tiketi ya CCM, niliahidi kuwa wiki hii nitajadili ‘odds’ (uwezekano wa kufanikiwa au la) zinazowakabili wanasiasa wawili ambao tathmini yangu inawaona kama ndio vinara katika mbio za kumpata mrithi wa Rais Jakaya Kikwete kupitia CCM, yaani Edward Lowassa na Bernard Membe.
Pengine hadi siku chache zilizopita, kikwazo kikubwa kwa wote wawili kingeweza kuwa uwezekano wa CCM kubwagwa na CHADEMA katika Uchaguzi Mkuu ujao. Lakini kwa kuzingatia mwenendo ulivyo katika chama hicho kikuu cha upinzani, yayumkinika kuhitimisha kuwa kikwazo hicho ni kama kimekufa kifo cha asili.
Kwa upande wa Lowassa, doa kubwa linaloonekana kuendelea ‘kuchafua’ jina na wasifu wake ni tuhuma za ufisadi wa Richmond. Bila kujali kuwa uamuzi wake wa kujiuzulu uwaziri mkuu kufuatia kashfa hiyo ni ‘kutolewa kafara’ au ‘alivuna alichopanda,’ tafsiri ya haraka kwa wananchi wengi wa kawaida inabaki kuwa ‘ni vigumu kumtenganisha mwanasiasa huyo na moja ya matatizo makubwa kabisa yanayoikabili nchi yetu, yaani ufisadi.’
Ukweli kwamba Tanzania yetu sio tu ni moja ya nchi masikini sana bali pia inazidi kuwa masikini huku ufisadi ukizidi kushamiri, umesababisha kujengeka kwa hisia (pengine zisizopendeza) kuwa kila mwenye uwezo wa kifedha ni fisadi. Hisia hizo hazimsaidii Lowassa ambaye kwa siku za hivi karibuni amekuwa mstari wa mbele katika harambee za kuchangisha mamilioni ya fedha hususan kwenye taasisi za dini. Badala ya ukarimu wake kumjenga kama kiongozi anayejali, kuna wanaotafsiri jitihada zake hizo kama ‘rushwa’ ya kutaka urais mwaka 2015.
Kadhalika, kuna hisia hasi kuwa hata hizo fedha anazotoa kusaidia miradi mbalimbali ‘ni chafu’ kwa maana ya hisia kuwa huenda ni zile zilizotokana na tuhuma za ufisadi. Kibaya zaidi, kutofahamika chanzo cha kinachotajwa kama utajiri mkubwa wa mwanasiasa huyo kunaimarisha hisia hizo za ufisadi.
Vile vile, na hili linawagusa wote-Lowassa na Membe- ukweli kwamba wanasiasa hao wanatajwa kama sehemu muhimu ya ‘mtandao’ uliomwingiza madarakani Rais Kikwete mwaka 2005, unaleta hisia za ‘mvinyo mpya kwenye chupa ya zamani’ (kwa wasiofahamu, thamani ya mvinyo inaelemea sana kwenye ‘ukale’ wake na si upya wake)
Sasa, kama tukiafikiana kuwa mtizamo wa Watanzania wengi ni kuwa utawala wa Kikwete (ambao uliingizwa madarakani na ‘mtandao’ uliowashirikisha Lowassa na Membe) umetawaliwa zaidi na tuhuma za ufisadi huku hali ya maisha ya Mtanzania ikizidi kuwa ngumu, kwa nini basi watu hao wapewe fursa ya kuboronga mambo zaidi?
Faraja kubwa kwa Lowassa (na hata Membe kwa ‘uhusika wake katika mtandao) kuhusu tuhuma za ufisadi ni ukweli mchungu kuwa Watanzania ni wepesi kusahau ‘mabaya.’ Wanasiasa wetu wengi wanafahamu kuhusu udhaifu huo ambao kwa kiasi kikubwa umewasaidia wengi kuendelea kuwapo madarakani licha ya ‘madudu’ yao.
Iwapo ‘kete ya fedha’ niliyobainisha katika makala iliyopita kuwa inamsaidia sana Lowassa itaendelea kutumika, basi kuna uwezekano mkubwa wa mwendelezo wa ‘who cares?’ (nani anajali?) ambapo mahitaji ya muda mfupi kama vile sukari, khanga, mchele na mengine kama hayo yatafunika mahitaji ya muda mrefu kama vile kuondokana na umasikini sambamba, kupambana na ufisadi, na hatma ya taifa letu kwa ujumla.
Kwa upande wa Membe, kikwazo kikubwa kwake ni kutokuwa maarufu ndani na nje ya CCM. Na ukubwa wa kikwazo hicho unatokana na ukweli kwamba ‘mpinzani’ wake, yaani Lowassa, ni mwanasiasa maarufu kuliko wote ndani ya CCM hivi sasa (bila kujali umaarufu huo ni stahili au la). ‘Wajuzi wa mambo’ wanaeleza kuwa inahisiwa Lowassa anaungwa mkono na zaidi ya asilimia 75 ya viongozi wa chama wenye uwezo wa kufanya uamuzi, huku wengi wao wakiwa watu waliofanyiwa fadhila zilizosababisha wawepo madarakani hivi sasa.
Tegemeo pekee kwa Membe dhidi ya Lowassa ni lile nililogusia katika makala iliyopita; nafasi ya Idara ya Usalama wa Taifa katika kumpata mgombea urais ajaye (ndani ya CCM). Kama kuna kitu chochote kinachoweza kumzuia Lowassa kuingia Ikulu, na pengine kumsaidia Membe kupata fursa hiyo, ni pale Idara hiyo itakapoamua ‘kumbeba mwenzao’ (Membe ni shushushu mstaafu). Na hilo si gumu kama inavyoweza kudhaniwa. Moja ya maeneo ambayo mashushushu wetu wanayomudu sana ni hujuma (sabotage) na uzandiki (subversion).
Ni hivi, kwa vile tayari kuna hisia za ‘uchafu’ kuhusu Lowassa (yaani tuhuma za ufisadi) basi haitokuwa vigumu kwa mashushushu kuzikuza na kuziendeleza katika namna ya kile kinachofahamika kama character assassination. Lakini kwa vile Lowassa bado yupo katika ‘himaya’ ya Idara ya Usalama wa Taifa (kama waziri mkuu wa zamani, anapatiwa huduma za ulinzi na Idara hiyo) ni rahisi kwa mashushushu kuibua mengi (ya kweli au hata ya kutunga) dhidi yake, iwapo wataona haja ya kufanya hivyo.
Kwa hiyo, kwa kifupi, kufanikiwa kwa Membe kutategemea kukwama kwa Lowassa. Na pengine katika hatua hii, ni vema nikitanabaisha waziwazi kuwa mwana-CCM anayeongoza katika kinyang’anyiro hicho ni Lowassa akifuatiwa kwa karibu kiasi na Membe.
Nihitimishe makala hii kwa kueleza kuwa mada hii ni endelevu, kwa maana ya kuwa nitaendelea na uchambuzi na mjadala huu kadri tunavyoelekea Uchaguzi Mkuu ujao. Hata hivyo, ninapenda kurejea tena mtizamo wangu kuwa CCM kurejea tena madarakani mwaka 2015 ni janga kwa Watanzania. Chama hicho tawala sio tu kimeishiwa na kila mbinu ya kuongoza nchi lakini pia hakipo kwa ajili ya maslahi ya Watanzania. Na kama uchambuzi huu ulivyoonyesha kuwa uwezekano mkubwa wa aidha Lowassa au Membe kuwa mgombea kwa tiketi ya chama hicho ni kwa aidha fedha au ‘sanaa za giza’, yeyote kati yao atakapopata urais hatokuwa tofauti na utawala uliopo madarakani hivi sasa ambao nao ulitumia mbinu ya ‘mtandao.’
Kwa bahati mbaya au makusudi, watu tuliodhani wangeweza kutusaidia kuiondoa CCM madarakani, yaani CHADEMA, wanaonekana kuwa ‘bize’ kupigana ngwala kugombea madaraka ndani ya chama chao. Sasa kama zoezi dogo tu la kupata uongozi wa chama linasababisha ‘watiane vidole machoni’ kwenye uongozi wa nchi itakuwaje? Ni ukweli mchungu lakini usioepukika na hivyo ni vema kujiandaa kisaikolojia kuendelea kuwa chini ya utawala wa CCM (ninatamani kuwa na suluhisho mbadala lakini sijalipata hadi muda huu)

Soma zaidi kuhusu:

- See more at: http://raiamwema.co.tz/nani-kinara-wa-ccm-urais-wa-2015-ii#sthash.RAQui2j5.dpuf

24 Nov 2013


KAMA nilivyoahidi katika makala yangu ndani ya toleo lililopita la gazeti hili maridhawa, wiki hii nitafanya uchambuzi kuhusu kinyang’anyiro cha kumpata mgombea urais kwa tiketi ya CCM katika Uchaguzi Mkuu ujao, mwaka 2015.
Kwa wanaofuatilia safu hii, niliwahi kugusia mada hii katika toleo la Oktoba 26, 2011 ikibeba kichwa cha habari “Mizengwe na mitego ya mgombea urais kutoka CCM.” Mengi yametokea kati ya wakati huo na sasa, na kwa vile Uchaguzi Mkuu unazidi kujongea, nimeona ni muhimu kurejea tena mada hii.
Pengine msomaji unaweza kubaini mabadiliko kidogo katika mtizamo wangu kuhusu uwezekano wa CCM kung’oka madarakani 2015. Ninaomba kukiri kwamba chokochoko zisizo na msingi zinazoendelea ndani ya chama kikuu cha upinzani (na tegemeo la wengi kuiondoa CCM madarakani, CHADEMA, zinanifanya nikubaliane na ukweli mchungu kuwa fursa za chama tawala kushinda tena katika uchaguzi mkuu ujao zinazidi kuongezeka.
Na moja ya mambo ya kusikitisha zaidi kuhusu CHADEMA ni kuibuka kwa kundi la ‘wahuni wa kisiasa’ waliojipachika joho la uanaharakati. Kwa wababaishaji hao, kuanza kukubalika kwa chama hicho kumetoa fursa kwao kufahamika kwa namna moja au nyingine. Ni tatizo lilelile sugu katika jamii yetu la kusaka umaarufu hata kwa mambo ya kipuuzi, Waingereza wanasema ‘famous for nothing.
Sasa ‘wahuni’ hawa wamebinafsisha ajenda ya CHADEMA kupambana na ufisadi na kujipa hakimiliki kuwa wao pekee ndio wenye uelewa na mbinu za kukiwezesha chama hicho kufanikisha ajenda hiyo. Pasi kujali madhara ya uhuni wao kwa hatma ya chama hicho, wamejikuta wakitumiwa na maadui wa CHADEMA kwa njia isiyo ya moja kwa moja - kwa ‘remote control.’
Lakini kuashiria kuwa chama hicho kina wakati mgumu japo uongozi wake wa juu unaendeleza porojo za “njama za CCM na Usalama wa Taifa,” imefika mahala Mwenyekiti wa chama hicho ngazi ya mkoa anabandika tuhuma nzito dhidi ya Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Zitto Kabwe, kwenye blogu yake. Hivi pamoja na madudu ya CCM unatarajia ‘utoto’ wa aina hiyo?
Tuelekee huko CCM sasa. Kwanza ninaomba kuweka bayana kuwa uchambuzi huu umeelemea katika uelewa wangu wa siasa za huko nyumbani, maongezi yangu na watu walio karibu na siasa hizo, na taarifa mbalimbali katika vyombo vya habari (vya ‘asili’ na vya ‘kisasa’)
Kwa mtizamo wangu, hadi muda huu wanasiasa wawili wanaoongoza katika kinyang’anyiro cha kumpata mrithi wa Rais Jakaya Kikwete hapo 2015 ni aliyekuwa Waziri Mkuu Edward Lowassa na Waziri wa Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa, Bernard Membe.
Kwa ‘pembeni’ kidogo kuna Waziri Mkuu wa zamani Frederick Sumaye na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki Samuel Sitta. Kimsingi, majina mengine yanayosikika kama William Ngeleja, John Magufuli na wengineo ni ya ‘kuchangamsha gumzo’ zaidi kuliko kuwa na uzito wowote wa maana.
Pengine baadhi ya wasomaji wangetamani nisiandike hivi lakini kimsingi hauepukiki, kama mazingira yatabaki kama yalivyo muda huu (constant) ni vigumu kwa mwanasiasa yeyote yule ndani na nje ya CCM kumzuia Lowassa kuwa rais mwaka 2015. Ninaomba nikiri kuwa ninatamani isiwe hivyo (kwa sababu binafsi ninaamini kuwa hafai kuwa Rais) lakini ukweli una tabia moja: kuuchukia hakuufanyi uwe uongo.
Turufu kubwa ya Lowassa ni uwezo wake mkubwa wa kifedha japo mwenyewe amekuwa akikanusha na kudai kuwa mamilioni anayoyamwaga katika harambee mbalimbali ni michango ya rafiki zake (hajawahi kuwataja wala kutueleza vyanzo vya utajiri wao).
Inaelezwa pia kuwa mwanasiasa huyo amejijenga mno ndani ya CCM kiasi cha kuwa sahihi kuhitimisha kuwa ana nguvu zaidi ya Mwenyekiti wa Taifa, Kikwete.
Sasa, huhitaji japo kozi ya muda mfupi ya siasa za nchi yetu kufahamu kuwa katika zama hizi fedha ndio nyenzo muhimu zaidi ya kumwezesha mwanasiasa kushinda uchaguzi kuliko kitu chochote kile. Mpigakura mwenye njaa hana habari na sera ya chama bali anachofikiria ni pishi ya mchele, doti ya khanga au kilo ya sukari.
Kwa upande wa Membe, turufu zake muhimu zaidi ni tatu. Kwanza, nafasi yake kama Waziri wa Nje inamweka karibu sana na Rais Kikwete kwani wanasafiri pamoja takriban katika kila ziara ya Rais nje ya nchi. Huhitaji kuwa mdadisi kufahamu kuwa watu wanaosafiri pamoja kwa miaka 10 mfululizo wana ukaribu kiasi gani.
Pili, kuna taarifa zisizo rasmi kuwa Membe anaungwa mkono na familia ya Kikwete. Katika moja ya mahojiano, mmoja wa watoto wa Kikwete, Ridhiwani, alikiri bayana kuwa anadhani Membe anaweza na anafaa kuwa Rais. Siasa za kifamilia zinaweza kubadilika lakini kwa angalau kwa sasa hali ipo hivyo.
Tatu, na kwangu hii ndio turufu muhimu zaidi, Membe ni ‘shushushu mstaafu.’ Pengine ni vigumu kuelezea kwa undani umuhimu wa kigezo hiki, lakini kwa kifupi, ni vigumu sana kwa mwanasiasa kuingia Ikulu pasi kuungwa mkono na Idara ya Usalama wa Taifa ya nchi husika (angalau katika ‘demokrasia changa’). Mashushushu, kama watumishi wengine wa vyombo vya dola, wana tabia moja ya kumuunga mkono ‘mwenzao.’
Lakini sambamba na hilo ni kile kinachofahamika kama ‘sanaa za giza’ (dark arts), yaani kwa lugha ya kawaida, zile mbinu zinazosababisha kura kuyeyuka katika mazingira ya ajabu. Tukiamini kuwa mashushushu watamuunga mkono Membe, kwa nini basi wasiende mbali zaidi kuhakikisha kuwa anashinda kwa ‘gharama yoyote’ (na ‘gharama’ hapa si lazima iwe fedha)?
Kwa hiyo licha ya uwezo mkubwa wa kifedha wa Lowassa (tukiweka kando kukanusha kwake kuwa yeye si tajiri), Membe anaweza kumshinda kwa mbinu (ambazo kwa mtizamo wangu zinaweza kuhusisha watumishi wa sasa na wa zamani wa Idara ya Usalama wa Taifa)
Kuhusu Sitta, nafsi yangu inanituma kuamini kuwa haitokuwa jambo la kushangaza endapo miezi michache kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2015 tukakutana na kichwa cha habari kama hiki “Sitta: Lowassa ni chaguo la Mungu.” Kwa nini nina hisi hivyo? Binafsi ninamwona kama mwanasiasa asiyeaminika, anayeendeshwa na siasa za kusaka umaarufu na hata ‘rahisi kutulizwa.’ Kwa kifupi, Sitta anaendeshwa zaidi na imani (kuwa anaweza kuwa rais) kuliko uhalisia.
Kwa Sumaye, japo pengine ni mapema mno ‘kumpuuza,’ nafasi pekee ya yeye kuwa rais ni nje ya CCM. Tatizo kubwa kwa mwanasiasa huyu ni kwamba lugha anayoongea haieleweki ndani ya chama hicho. Naam, amejitokeza kuwa msemaji wa wanyonge na mkemeaji mkubwa wa ufisadi lakini sote tunafahamu kuwa hiyo sio sera ya CCM (angalau kwa vitendo na si kauli za majukwaani).
Nafasi hairuhusu kuangalia ‘odds’ dhidi ya Lowassa na Membe (ninataraji kufanya hivyo katika matoleo yajayo), lakini muda mfupi kabla ya kuandaa makala hii nilishiriki katika mjadala mzito kuhusu hatma ya Tanzania yetu hususan jinsi ya kuzuia uwezekano wa kumpata Rais atakayetokana na rushwa. Pia tulijadili tatizo la rushwa na namna ya kulimaliza.
Kwa bahati nzuri, mjadala huo uliofanyika katika mtandao wa kijamii wa Twitter ulimvutia mwanasiasa kijana na Mbunge wa Tanzania kwenye Bunge la Afrika Mashariki, Abdullah Mwinyi. Kwa kifupi, alitueleza kiini cha tatizo la rushwa, na nini kinaweza kufanyika kupambana na tatizo hilo sugu. Bila kuingia undani kuhusu mjadala huo, ulipofikia tamati takriban kila mshiriki alikiri kuwa “kumbe CCM bado ina hazina zaidi ya hayo majina tunayoyasikia kila siku.”
Je, wanasiasa kama Abdullah, mtoto wa Rais wa Awamu ya Pili Mzee Ali Hassan Mwinyi wanaweza kuwa chaguo mbadala (alternative choice) hasa ikizingatiwa kuwa hawana ‘mawaa’ kama ya Lowassa au Membe (nitayajadili mbeleni)?
Nihitimishe makala yangu kwa kusisitiza jambo moja: japo kwa jinsi hali ilivyo ni muhimu kujiandaa kisaikolojia kuiona CCM ikiendelea kuwa madarakani baada ya Uchaguzi Mkuu ujao, bado kuna umuhimu mkubwa kwa chama hicho kikongwe kupumzishwa kwani kimeshindwa kazi.
Si Lowassa, Membe, Sitta au Sumaye anayeweza kuibadili CCM irejee misingi aliyoasisi Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere. Tegemeo dogo katika chama hicho ni damu mpya kama za akina Abdulla Mwinyi, japo pengine ni mapema mno kuhitimisha hilo.
ITAENDELEA...


- See more at: http://raiamwema.co.tz/nani-kinara-wa-ccm-urais-wa-2015#sthash.fO09a0nd.dpuf

30 May 2013

Magufuli amkana Sitta, asema hana ubia naye urais 2015


Siku chache baada ya Waziri wa Afrika Mashariki Samuel Sitta kumhusisha Dk John Magufuli na kundi la urais la mwaka 2015, Waziri huyo wa Ujenzi, ameibuka na kupinga kauli hiyo, akisisitiza hafikirii kuwania nafasi hiyo.
Waziri Sitta alinukuliwa na gazeti hili juzi akieleza kuwa wakati ukifika, yeye na rafiki zake Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Waziri wa Ujenzi, Dk Magufuli na Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe, watachagua mmoja wao watakayeona anafaa kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa 2015. Alisema hayo juzi kwenye Kongamano la Mawasiliano katika Nyanja za Digitali la wanafunzi wa Idara ya Uhusiano na Masoko, Chuo Kikuu cha St. Augustine (SAUT), Mwanza.
Kabla ya hapo alikuwa amewataja rafiki zake hao wakati wa hafla ya kuchangia Kanisa Katoliki, Josephine Bakita, Parokia ya Igoma, Mwanza, Jumapili iliyopita.
Alisema hatagombea tena ubunge mwaka 2015, baada ya kuwa katika ulingo wa siasa kwa miaka 35 na badala yake ataangalia namna nyingine ya kuwatumikia wananchi huku akigusia mchakato wa kuwania urais ambao alieleza anamwachia Mungu.
“Kwa ubunge nimekwishawaeleza inatosha, sitagombea tena kwani miaka 35 inatosha, … lakini hatima yangu ni nini siwezi kujua lakini nina afya nzuri na mmoja wa wanasiasa wakongwe, wenye afya nzuri, mnaona ninavyopendeza... kwa urais namwachia Mungu tutaona,” alisema Sitta.
Kauli ya Magufuli
Akizungumza na gazeti hili nje ya ukumbi wa Bunge jana, Dk Magufuli alisema haelewi msingi wa kauli ya waziri mwenzake huyo, kwani hajui chochote katika mtandao wa urais alioutaja.
Magufuli alisisitiza kusema hana kundi, hakuwahi kuzungumza wala kuhudhuria vikao vya kundi lolote, na kwamba kundi lake ni CCM na Mwenyekiti wake ni Jakaya Kikwete.
“Sina kundi. Sijawahi kuwa na kundi na sitarajii kuwa na kundi lolote. Ninachojua kundi langu ni CCM na kiongozi wake ni mwenyekiti wake, Rais Kikwete,” alisema Dk Magufuli.
Hata hivyo, Dk Magufuli pia alipuuza taarifa kuwa alichangia harambee hiyo akisema, “Si kweli, Mwanza sijatoa hata senti na hata siku ilipofanyika hafla hiyo, nilikuwa Dar es Salaam katika mkutano na makandarasi.” Licha ya kutajwa kuwa miongoni mwa vinara wa urais 2015, Magufuli alieleza kuwa hakuwahi kuzungumza na Sitta suala hilo linalohusu makundi ya urais mwaka 2015.
CHANZO: Mwananchi
WAKATI HAYO YAKITOKEA, JANA PIA ILIKUWA SIKU CHUNGU  KWA SITTA,KAMA INAVYOONYESHA HABARI HII HAPA CHINI
Wassira amvaa Sitta
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Mahusiano na Uratibu, Stephen Wassira, amemtaka waziri wa ushirikiano wa Afrika Mashariki Samwel Sitta, aweke wazi njia anazotumia kupambana na ufisadi nchini ambazo mawaziri wengine wa serikali ya CCM hawawezi kuzitumia.

Wakati Wassira akitaka ufafanuzi huo, Waziri wa Katiba na Sheria Mathias Chikawe kwa upande wake alikataa kuzungumzia mbinu anazotumia Samwel Sitta kwa kile alichoeleza kuwa hawezi kuongelea masuala ya serikali na mtu asiyemjua.

Wassira na Chikawe walitoa kauli hiyo jana wakati gazeti hili lilipotaka maoni yao juu ya kauli ya Sitta iliyonukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari akisema kuwa katika serikali nzima ni mawaziri wanne waliojipambanua kupambana na ufasadi na kutetea wanyonge.

Wassira alisema kwa sasa hawezi kuchangia jambo lolote juu ya kauli hiyo ya Sitta kwa kuwa hajaliona katika vyombo vya habari au kumsikia waziri huyo akisema hadharani.

Alisema kama kauli hiyo imetolewa na Sitta ni vema angefafanua mbinu anazotumia ili wengine waige.
“Mimi siwezi kuzungumzia hayo; mmeyasema nyie pia ingekuwa ni vema kama angeulizwa Sitta mwenyewe na atueleze mbinu zake tuone na wengine wanafanya nini,” alisema Wassira.

Alipoulizwa kama majina yaliyotajwa ni miongoni mwa makundi yanayodaiwa kujipanga ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), kwa ajili ya urais wa 2015; Wassira alisisitiza jambo hilo aulizwe Sitta.

Kwa upande wake Waziri wa Katiba na Sheria Mathias Chikawe, alipopigiwa simu kwa ajili ya ufafanuzi wa kauli hiyo, alikataa kuzungumzia jambo lolote kwa madai kuwa alishajeruhiwa kwa kutoa habari kwa njia ya simu.

“Sitaki na sizungumzi mambo ya serikali na mtu nisiyemjua tena katika simu…siku moja alinipigia mtu akasema anatoka Daily News nilipompa habari akaandika anavyojua na ikaniletea matatizo, kwanza kwa sasa niko Arusha,” alisema Chikawe na kukata simu.

Juzi wakati Waziri Sitta, akishiriki harambee ya kuchangia ujenzi wa Kanisa la Mtakatifu Joseph katika Parokia ya Igoma jijini Mwanza, aliwataka Watanzania kujihadhari na watu wasio waadilifu katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwaka 2015.

Alisema watuhumiwa wa kashfa ya ufisadi wa kampuni ya kufua umeme ya Richmond na Dowans ni hatari na hawastahili kuungwa mkono katika uongozi.

Alisema kutokana na hali hiyo ya ufisadi yeye pamoja na mawaziri wengine watatu wako pamoja katika fikra za kupambana na vitendo vya kifisadi, uonevu na mikataba tata.

Aliwataja mawaziri hao kuwa ni Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe, pamoja na Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli.


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.