Showing posts with label VITA BARIDI. Show all posts
Showing posts with label VITA BARIDI. Show all posts

22 Aug 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum,

Kabla sijaenda kwenye mada yangu ya leo ngoja nielezee kichekesho kimoja nilichokisoma kwenye mtandao kuhusu maandalizi ya timu ya Moro United katika majukumu ya kitaifa yanayowakabili.Kiongozi mmoja wa timu hiyo alinukuliwa akisema kwamba timu hiyo imeamua kufuta safari ya kwenda nchini Ufaransa kwa vile wamekosa nafasi ya sehemu ya kufikia “kutokana na hoteli nyingi kujaa kipindi hiki cha summer…”Hiki ni kichekesho kwa sababu Ufaransa ni nchi na sio kijiji au mtaa wenye hoteli moja au mbili.Kilichonisikitisha ni ukweli kwamba mwandishi aliyeripoti habari hiyo hakufanya jitihada yoyote ya kumuuliza kiongozi huyo ni hoteli zipi na katika miji gani ya Ufaransa ambazo timu hiyo ilipanga kufikia,na hapo ingekuwa rahisi kwa mwandishi huyo kuhakiki hoja hiyo kwenye tovuti ya hoteli au sehemu zilizotajwa.Tunaambiwa kuwa badala ya Ufaransa sasa timu hiyo itakwenda Italia,kana kwamba huko Italia sasa ni majira ya baridi au hakuna watalii waoweza kujaza hoteli “kama ilivyokuwa huko Ufaransa.”

Enewei,tuachane na ubabaishaji huo.Majuzi nilipata barua pepe kutoka kwa rafiki yangu mmoja anayesoma siasa kama mimi japo yeye eneo lake la utafiti ni Kusini Mashariki mwa bara la Asia na mimi eneo langu ni Afrika.Katika barua hiyo,niliombwa kutoa mawazo yangu kuhusu kile ambacho rafiki yangu alikiita kukua kwa kasi kwa interests za China katika bara la Afrika.Tangu Januari mwaka huu viongozi wa juu wa nchi hiyo wameshatembelea nchi 15 za Afrika.Wakati Waziri Mkuu Wen Jiabao ametembelea Misri,Ghana,Congo,Angola,Afrika Kusini,Uganda na Tanzania,Rais Hu Jintao ametembelea Morocco,Nigeria na Kenya,huku Waziri wa Mambo ya Nje Li Zhaoxing amezuru Libya,Senegal,Cape Verde,Mali,Liberia na Nigeria.Wafuatiliaji wa siasa za kimataifa wa nchi za Magharibi wanaonekana kuwa na kihoro kwa namna mambo yanavyoonekana kwenda vyema kwa China na marafiki zake wa Afrika.Eti wanadai kuwa tofauti na mapatna wakuu wa biashara wa Bara la Afrika,yaani Marekani na Uingereza,China haijali sana kuhusu masuala ya haki za binadamu na ndio maana baadhi ya misaada ya nchi hiyo imekwenda kwa nchi ambazo rekodi zake katika haki za binadamu sio za kuuridisha sana.Kwa mujibu wa tovuti ya Council for Foreign Relations, China iliipatia Sudan ndege za kivita aina ya Shenyang na silaha vyote vikiwa na thamani ya dola zaidi ya milioni 100,na kati ya 1998 na 2000 ilitoa misaada ya silaha zenye thamani ya dola bilioni 1 kwa Ethiopia na Eritrea wakati nchi hizo zikiwa kwenye vita.Lakini pia wachambuzi hao wanadai kuwa katika kupata mikataba minono China haijali sana wale wanaoomba “teni pasenti” kusaini mikataba yenye utata,na ziadi ni suala la kutumia wataalamu wake badala ya wazawa kwenye nchi inazoshirikiana nazo.

Hata hivyo,pamoja na “longolongo” hizo ukweli unabaki kwamba mchango wa China kwa Afrika ni wa manufaa kwa bara hilo lenye mlolongo wa matatizo.Kwa mfano,mwaka jana uchumi wa Afrika ulikuwa kwa asilimia 5.2 ambayo ni rekodi ya juu kabisa,na miongoni mwa sababu muhimu ni mchango wa China kwenye uchumi wa bara hilo.Pia China ilifuta madeni kwa Afrika yanayofikia takribani dola bilioni 10,mwaka juzi ilichangia askari 1500 kwenye majeshi ya kulinda amani ya Umoja wa Mataifa barani Afrika,na ujenzi wa miundombinu unaofanywa na nchi hiyo ni wa gharama nafuu na unazingatia muda.

Jambo jingine la hivi karibuni ambalo limegusa hisia za duru za kisiasa za nchi za Magharibi ni kikao cha 7 cha Umoja wa Afrika (AU) ambapo Rais wa Iran,Mahmoud Ahmadinejad,na mwenzie wa Venezuela,Hugo Chavez,walihudhuria.Viongozi hao wawili wanaonekana kama “miiba mikali” kwa Marekani na washirika wake.Nchi zote hizo mbili zinajivunia “silaha” zake yaani mafuta,na kwa namna flani Marekani na marafiki zake wanaishia kulalamika tu bila kuchukua hatua yoyote dhidi ya nchi hizo pengine kwa kuhofia madhara kwenye suala nyeti la “wese” (mafuta).

Mara nyingi Afrika inavuta zaidi hisia za siasa za kimataifa kwenye majanga-kama vita,ukimwi,nk-pale inapoonekana kuwa bara hilo linaweza kukumbatiwa na wale wanaoonekana (kwa Marekani na wenzie) kuwa ni nguvu tishio.China ina uchumi unaokuwa kwa kasi ya kutisha,yaani ile shaa kama wanavyosema watoto wa mjini,na ukichanganya na watu wake zaidi ya bilioni moja,wachumi wa nchi za Magharibi wanaiangalia nchi hiyo kwa makini sana.

Enzi za Vita Baridi,washiriki wakuu-nchi za Magharibi chini ya Marekani,na za Mashariki zikiongozwa na Urusi-walipigana vikumbo ndani ya Afrika ili kuliweka mikononi bara hilo.Mbinu chafu sana zilitumika katika kutekeleza azma hiyo ikiwa ni pamoja na mauaji ya wanasiasa kama Patrice Lumumba,na sapoti kwa wanaharamu kama Jonas Savimbi na UNITA yake.Yayumkinika kusema kwamba bara la Afrika halikupata nafasi ya kupumua baada ya mapambano dhidi ya ukoloni kwani mara baada ya uhuru likajikuta limewekwa mtu kati kwenye mapambano kati ya ubepari na ukomunisti.

Ni matarajio yetu kwamba iwapo hao wanaowashwa na kukua kwa mahusiano kati ya China na Afrika wataamua kufanya lolote basi haitokuwa kuligeuza bara letu kuwa uwanja wa mapambano ya kiitikadi.Kwa kuwa hali kwa sasa iko shwari,acha tufaidi ukarimu wa wajukuu wa Mwenyekiti Mao na mwenzie Zhou Enlai (fasheni za zamani zinarudi,je suti za chwenlai nazo zitarudi?).

Alamsiki

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.