Showing posts with label Vita Dhidi ya Madawa ya Kulevya. Show all posts
Showing posts with label Vita Dhidi ya Madawa ya Kulevya. Show all posts

9 Feb 2017

MWEZI Machi mwaka jana, watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Nottingham cha hapa Uingereza walichapisha matokeo ya utafiti wao kuhusu kushamiri kwa tabia ya uvunjaji wa sheria. Katika matokeo hayo ya utafiti uliochunguza nchi 159, Watanzania tuliibuka vinara kwa kuwa watu wanafiki kupita kiasi, tukifuatiwa na watu wa Morocco.
Na mifano ya unafiki wetu ipo mingi tu, sisi ni miongoni mwa wapinzani wakubwa wa suala la ushoga. Lakini ukitaka kufahamu unafiki wetu katika suala hilo, nenda kwenye mtandao wa kijamii wa Instagram, shuhudia lundo la mashoga wa Kitanzania waliojitundika huko, wakifanya vitu vichafu kabisa, huku wakiwa na “followers” hadi laki kadhaa, hao si tu ni Watanzania wenzetu bali ni miongoni mwa sisi ‘wapinga ushoga.’ Unafiki wa daraja la kwanza.
Na sababu kuu tunayoitumia kupinga ushoga ni imani zetu za kidini. Na kwa hakika tumeshika dini kweli, hasa kwa kuangalia jinsi nyumba za ibada zinavyojaa. Lakini kuthibitisha unafiki wetu, ucha-Mungu huo sio tu umeshindwa kudhibiti kushamiri kwa ushoga (na usagaji) bali pia kutuzuia tusishiriki kwenye maovu katika jamii.
Kwa taarifa tu, kwa mujibu wa utafiti uliofanywa miaka michache iliyopita na taasisi ya Pew ya Marekani, Watanzania tunaongoza duniani kwa kuamini ushirikina. Na kwa mujibu wa taarifa ninazozipokea kutoka huko nyumbani, ushirikina umeshamiri mno kiasi kwamba sasa ni kama sehemu ya kawaida ya maisha ya Watanzania.
Wacha-Mungu lakini tumebobea kwenye ufisadi, rushwa, ujangili na biashara ya dawa za kulevya. Na asilimia kubwa ya kipato haramu kinachotokana na uhalifu huo kinachangia kushamiri kwa “michepuko” na “nyumba ndogo.”
Mfano wa karibuni kabisa kuhusu unafiki wetu ni katika mshikemshike unaoendelea hivi sasa huko nyumbani (Tanzania) ambao watu kadhaa maarufu aidha wametakiwa kuripoti polisi au ‘kuhifadhiwa’ na polisi wakichunguzwa kuhusiana na biashara ya dawa za kulevya. Hali hiyo inatokana na tangazo rasmi la Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, ‘kujitoa mhanga’ kukabiliana na biashara hiyo haramu.
Lakini licha ya kuwepo kwa lundo la lawama mfululizo kwa serikali kuwa imekuwa ‘ikiwalea’ watu wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya, tangazo la Makonda limesababisha kuibuka kwa lawama lukuki dhidi yake, huku wengine wakidai anatafuta ‘kiki (sifa) za kisiasa’ na wengine kudai amekurupuka kwa kutaja majina ya watu maarufu, na wengine wakimlaumu kwa kukamata ‘vidagaa’ na kuacha ‘mapapa.’
Kwa watu hao, na wapo wengi kweli, Makonda atashindwa kama alivyoshindwa kwenye amri zake nyingine. Sawa, rekodi ya Mkuu wa Mkoa huyo katika ufanisi wa maagizo yake sio ya kupendeza. Hata hivyo, kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania, kiongozi sio tu ametangaza vita dhidi ya biashara ya dawa za kulevya bali pia ametaja baadhi ya majina ya wahusika, na kuwafikisha polisi. Hili ni tukio la kihistoria.
Lakini ‘wapinzani’ wa RC Makonda sio wananchi wa kawaida tu. Kuna ‘wapinzani wa asili,’ mbunge wa Chadema, Tundu Lissu, ambaye aliandika ujumbe mtandaoni, “kuwataja vidagaa na kuwaacha nyangumi/papa si ajabu ni moja kati ya mambo ya ovyo ya awamu ya tano.” Huyu ni mnafiki wa mchana kweupe. Sasa kama anawajua hao nyangumi/papa si awataje?
Kilichonisikitisha zaidi ya vyote ni kauli za Waziri Nape Nnauye alipozungumza na waandishi wa habari huko Dodoma. Pamoja na mambo mengine, Waziri Nape alidai kuwa, “ …watumiaji ni wengi lakini wanaoonekana zaidi ni wale wenye majina makubwa,” (sijui kwa mujibu wa utafiti gani); “Kama wizara tunaunga mkono juhudi za kupambana na dawa za kulevya, tatizo ni namna ya kushughulika na wahusika ikiwemo busara” (sijui alitaka tatizo lishughulikiwe kwa namna gani – na kwa nini hakuongoza kwa mfano kwa kutumia namna hiyo – na sijui busara ipi iliyokosekana katika utekelezaji wa agizo la Makonda); “Tunaunga jitihada za mapambano lakini ni vizuri lifanywe katika namna ya kulinda haki ya mtuhumiwa ili heshima yake isipotee” (haelezi hiyo ‘namna ya kulinda haki ya mtuhumiwa ili heshima yake isipotee’ ni kitu cha aina gani)
Nilimshutumu vikali Waziri Nape kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter (nilim-tweet yeye mwenyewe), na kumweleza bayana kuwa alihitaji kutumia busara badala ya kukurupuka kutetea wasanii wanaotuhumiwa kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya. Kadhalika, kama mtendaji wa serikali, alikuwa na nafasi nzuri kuzungumza na watendaji wenzake wa serikali faragha badala ya kuongea suala hilo hadharani. Kadhalika, kuonekana anahofu zaidi kuhusu “brand” (thamani/hadhi ya msanii, kwa tafsiri isiyo rasmi) badala ya athari kubwa zinazosababishwa na biashara ya dawa za kulevya sio busara hata kidogo.
Nihitimishe makala hii kwa kutoa wito kwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba naye ajitokeze hadharani kuongelea suala hili maana amekuwa kimya mno. Awali, naibu wake alipohojiwa na wanahabari alikuwa mkali na alitoa kauli zisizopendeza. Ili vita hii ifanikiwe ni lazima serikali iwe kitu kimoja na viongozi na wananchi kwa ujumla waache unafiki, na wampe ushirikiano RC Makonda na Jeshi la Polisi.
Tanzania bila dawa za kulevya inawezekana

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.